Madame S
JF-Expert Member
- Mar 4, 2015
- 17,177
- 34,444
- Thread starter
- #121
NYEMO CHILONGANI.Aiseeeee
Madame asantee
UTAJIRI WENYE UCHUNGU.
Sehemu ya Kumi na Sita.
Mpaka dakika kumi baadaye, Bwana James na mkewe walifika katika floo hiyo, kila mmoja alionekana kuchoka mno. Hawakuwa peke yao bali walikuwa na watu wengine ambao wote hao walibaki wakiwaangalia kwa mshangao, hawakujua ni kitu gani kilikuwa kikiendelea.
“Watoto wangu...” alisema Bwana James, akawasogelea na kuwakumbatia wote.
****
Dylan alikuwa na ndoto kubwa za kuwa mchezaji mkubwa wa mpira wa kikapu, ila ndoto zake zote zikafa kwa sababu baba yake alitaka asimamie biashara zake kwani kwa jinsi zilivyokuwa, kama angemuachia Catherine, asingeweza kabisa.
Hilo kwake wala halikuwa tatizo, akaanza kusimamia biashara hizo kama alivyoambiwa. Dylan yule kijana aliyekulia kwenye umasikini mkubwa, leo hii hakuwa masikini, alikuwa tajiri aliyekuwa akiogelea katika dimbwi la fedha za baba yake.
Hakuwa mtu wa starehe, hakuwa mtu wa kupenda wanawake kutokana na hali yake kiafya ilivyokuwa. Siku zikaendelea kukatika kama kawaida huku utajiri huo wa baba yake ukizidi kuongezeka kwani usimamizi aliokuwa akiufanya ulikuwa mkubwa na uliojaa umakini.
Kutokana na kuwa kijana mdogo, wanawake wengi walimpapatikia, kila alipopita alionekana kuwa kawaida, hakuwa mtu wa kujikweza, sifa, hayo yalikuwa mambo yaliyomfanya kupata marafiki wengi kila siku.
“Habari yako....” ilisikika sauti ya msichana mmoja, alikuwa ameingia kwenye lifti kupanda juu katika jengo la Kampuni ya Ericom aliyokuwa akimili baba yake nchini Marekani.
Dylan akageuka nyuma kwani mara alipoingia ndani ya lifti hiyo, hakuwa amemuona msichana huyo kutokana na macho yake kuwa kwenye karatasi alizokuwa amezishika. Ndani ya lifti walikuwa wawili tu.
“Salama tu, habari yako binti?” alimsalimia.
“Salama kabisa. Umependeza...” alisema msichana huyo.
“Asante sana.”
Dylan hakutaka kuzungumza neno jingine lolote, alibaki kimya huku macho yake akiyarudisha katika karatasi ile. Alionekana kuwa makini sana na hakutaka kusubiri mpaka afike ofisini kwake kwani kila siku aliokuwa mtu wa kuwa bize tu.
“Naitwa Katty....” alisema msichana huyo huku tabasamu likiwa usoni mwake.
“Nashukuru kukufahamu...”
“Nashukuru pia Dylan...”
Lifti ilipofika katika ghorofa ya saba, Dylan akateremka na kumuacha msichana yule ndani ya lifti ile huku watu wengine wakiwa wamekwishaingia. Akaondoka na kwenda ofisini kwake, kitu cha kwanza kabisa akahitaji ripoti kamili juu ya viporo vyote alivyoviacha jana yake, hivyo akaletewa.
Aliendelea kukaa ofisini, hakuwa mtu wa kutoka, aliwaamini wafanyakazi wake kwamba walikuwa watendaji na hawakuwa watu wa kumuangusha. Walifanya kazi vizuri na kwa kujitoa sana.
Wakati amemaliza kazi zake majira ya saa nane mchana, akachukua begi lake lililokuwa na laptop, akaliweka begani kwa ajili ya kutoka huku akiwa amekwishampigia simu dereva kwa ajili ya kuligeuza gari lake. Wakati anaingiza mkono mfukoni mwake, akahisi kuna kitu, alipoangalia vizuri, mkono wake ukakutana na kikaratasi, akakitoa na kuanza kukiangalia, kwani kumbukumbu zake zilimwambia kwamba kwa siku hiyo hakuwahi hata kukiingiza kikaratasi chochote mfukoni mwake.
‘Maybe, I am in love, see you soon, it’s me, Katty Perrishian...’ (Labda, nipo kwenye penzi zito, nitakuona hivi karibuni, ni mimi, Katty Perrishian...) yalisomeka maneno yaliyokuwa kwenye kikaratasi kile.
Moyo wa Dylan ukapiga paa! Akahisi kwamba aliingiziwa kikaratasi kile na yule msichana wakati wapo ndani ya ile lifti. Akashusha pumzi nzito.
****
Dylan hakumfahamu msichana huyo, hakujua alikuwa nani na alihitaji nini kutoka kwake. Moyo wake ukawa na presha kubwa, hakumkumbuka hata sura yake kwani walipokutana kwenye lifti hakuonekana kujali sana kuhusu yeye, alikuwa na mambo yake hivyo ilikuwa vigumu mno kuikumbuka sura yake.
Hakutaka kujali sana, akarudi nyumbani kwake na kutulia. Alikuwa kwenye hali ya kawaida tu, akafungulia televisheni na kuanza kuangalia mchezo wa kikapu uliokuwa ukiendelea kati ya Chicago Bulls na La Lakers. Hakutaka kumtilia maanani msichana huyo, aliamua kwa moyo mmoja kufanya mambo yake kwani alikumbuka vizuri kwamba hakuwa salama kiafya na hilo tatizo hakutaka lijulikane na mtu yeyote yule.
Ulipofika muda wa kulala, akajikuta akianza kukikumbuka kile kikaratasi kilichoandikwa ule ujumbe aliopewa. Ulikuwa ujumbe mfupi lakini wenye kusisimua sana. Kwa kipindi hicho, hakutaka kuwa na msichana yeyote yule, mawazo yake yalikuwa kwenye kazi tu. Alipoona ameshindwa kabisa kujikontroo, akachukua simu yake na kumtumia ujumbe wa maneno mdogo wake, Catherine.
“Kama utakuwa na nafasi kesho, naomba nikuone,” aliandika uumbe huo kwenye simu yake na kumtumia Catherine.
“Kuna nini?”
“Hakuna kitu cha kutisha, naomba nikuone kwanza...’
“Sawa...”
Usingizi haukumpata, alikuwa kwenye mawazo tele, alijaribu kuuvuta kwa kbimbilika huku na kule lakini hakulala mpaka ilipofika majira ya saa sita usiku ndipo akalala usingizi mzito.
Asubuhi alipoamka, kitu cha kwanza kilichokuja kichwani mwake kilikuwa ni juu ya yule msichana, bado alikisumbua kichwa chake japo kuukumbuka uso wake lakini hilo halikuwezekana.
Akaelekea bafuni, akaoga na kisha kujiandaa kwa ajili ya kuonana na Catherine kabla ya kwenda ofisini kwake. Jambo kama hilo, hasa kuhusu msichana hakutaka liwe peke yake, alimzoea Catherine, alikuwa ndugu yake na rafiki yake wa karibu ambaye mara kwa mara alikuwa naye na kushauriana mambo mbalimbali kuhusu maisha.
“Huyo msichana ni nani?” aliuliza Catherine.
“Simfahamu kabisa...”
“Na haujawahi kumuona kabla?”
“Ndiyo! Na hata pale nipomuona, sikumtilia maanani..” alijibu Dylan.
Catherine ndiye alikuwa mshauri wake lakini mpaka muda huo hakujua ni kwa namna gani alitakiwa kumshauri Dylan ambaye alionekana kutamani sana kuambiwa neno lolote lile kuhusu msichana huyo.
Hiyo ilikuwa siku ya pili, alitegemea kumuona msichana huyo siku hiyo lakini palikuwa patupu. Katika hali ya kushangaza kabisa, mawazo yakaanza kumsumba, hakuwa na furaha, muda wote alikuwa kimya ndani ya ofisi yake akimfikiria msichana huyo.
Ukimya huo haukuishia siku hiyo tu, ilikatika wiki ya kwanza, msichana huyo hakutokea, wiki ya pili ikakatika lakini bado msichana huyo hakuweza kutokea kitu kilichompa maswali mengi kwani naye kwa kipindi hicho alitamani sana kumuona msichana huyo.
Wiki ya tatu ilipoingia huku mawazo juu ya msichana huyo yakiwa yamepungua kichwani mwake ndipo sekretari wake alipompigia simu na kumwambia kwamba kulikuwa na mzigo wake na ulikuwa umeletwa na msichana fulani ambaye hakujitambulisha.
“Mzigo wa nini?” aliuliza kwenye simu.
“Maua...”
“Maua?”
“Ndiyo bosi! Nikuletee?” aliuliza sekratari.
“Niletee...”
Ndani ya sekunde kadhaa, msichana huyo akaufungua mlango na kuingia ndani, moja kwa moja akaenda katika meza aliyokuwepo bosi wake kisha kumpa maua yale.
Ndani ya sekunde kadhaa, msichana huyo akaufungua mlango na kuingia ndani, moja kwa moja akaenda katika meza aliyokuwepo bosi wake kisha kumpa maua yale.
Dylan akayachukua, kitu cha kwanza kabisa ilikuwa ni kuyanusa, yalinukia vizuri, harufu yake ilimvutia mno. Yalikuwa maua ya kila rangi, yaliyopendeza machoni mwake.
“Nashukuru,” alimwambia mfanyakazi wake na kutoka.
Alibaki akiyaangalia, kila wakati moyo wake ulihisi kitu fulani hivi ambacho wala hakupata wakati mgumu kutambua kilikuwa kitu gani, yalikuwa ni mapenzi ya dhati.
Hakutaka kabisa kitu hicho kitokee, aliufahamu moyo wake, aliifahamu afya yake ambayo ndiyo ilikuwa sababu kubwa ya kuwakataa wanawake waliokuwa wakimfuatilia, kitu ambacho kilimpa maswali ni juu ya huyu msichana ambaye wala hakumkumbuka sura, alikuwa amempenda tu kutokana na vitu alivyokuwa amemfanyia.
Maua yale yalikuja kama yalivyokuja, hakukuwa na kitu kingine kama watu wengine wanavyofanya kwamba kuna jina, namba ya simu na hata mahali yalipotoka.
Siku hiyo kazi hazikufanyika, kila wakati macho yake yalikuwa kwenye maua yale ambapo muda wa kutoka ulipofika, akayachukua, akayaingiza ndani ya gari na kisha kuondoka zake kuelekea nyumbani.
Huo ndiyo ukawa mwanzo, hakuishia kupokea maua, aliendelea kupokea zawadi mbalimbali za kimapenzi ambazo zilimchanganya. Alipagawa, hakujua Katty alikuwa wapi na alihofia nini kurudi tena katika jengo lile kwa ajili ya kumuoa.
Katika siku ambayo aliletewa boksi lililokuwa na nguo za kiume ndiyo siku ambayo alichanganyikiwa zaidi baada ya kuona anuani iliyomuenyesha kwamba mzigo huo ulitumwa kutoka nje ya nchi, tena Ulaya nchini Ufaransa.
“Duh! Hayupo Marekani tena?” alijiuliza.
Ndani ya boksi hilo kulikuwa na cd ambayo aliichukua na kuiweka kwenye kompyuta yake na kuanza kuitazama. Picha alizozikuta humo zikamfariji, akamuona msichana mwenyewe, alikuwa msichana mrembo mno na kila picha iliyokuwa ikionekana ilibeba ujumbe mzito ulioandikwa kwa lugha mbili, yaani Kiingereza na Kiitaliano.
“Te amo,” (Nakupenda) lilikuwa neno pekee la Kiitaliano ambalo alilielewa.
Uso wake ukawa kwenye tabasamu pana, moyo wake ukajisikia faraja kubwa, mapenzi yakaongezeka zaidi, kiu ya kumuona msichana huyo ikamshika zaidi.
Huo ulikuwa mwezi wa kwanza, hakukuwa na kitu alichokuwa akikitamani kama kuonana na msichana huyo. Mwezi wa pili ulipoingia, akatumiwa zawadi ya gari ambayo ilipelekwa mpaka ofisini kwake.
Japokuwa alikuwa bilionea lakini zawadi ile ya gari ambayo alipelekewa ilikuwa bab’ kubwa kwake. Hakuamini kama msichana huyo angeweza kumletea gari ya thamani kama hilo.
Akatokea kulipenda kutokana na jinsi lilivyokuwa ila pamoja na hayo yote, akalipenda zaidi kwa kuwa lilikuwa ni zawadi kutoka kwa msichana aliyehisi kwamba alikuwa na mapenzi mazito juu yake.
Pale lilipoegeshwa, kila mtu alikuwa akilishangaa, lilikuwa zuri, aina ya Porsche lenye gharama kubwa na lilikuwa la kisasa zaidi. Wengi wakahisi kwamba bosi wao Dylan ndiye alikuwa amelinunua, wengi wakampongeza pasipo kujua kwamba lile lililetwa kama zawadi kutoka kwa msichana ambaye hakuwahi kumuona uso kwa uso zaidi ya mara moja.
Miezi ikakatika, mwaka wa kwanza ukapita, bado aliendelea kupokea zawadi tu, kulikuwa na jina, ila hakukuwa na anuani yoyote, akabaki akiwa amechanganyikiwa tu. Alitamani hata kuisikia sauti yake.
Je, nini kitaendelea?
Tukutane Alhamisi hapahapa
