NYEMO CHILONGANI.
UTAJIRI WENYE UCHUNGU.
Sehemu ya Kumi na Tano.
Kila mmoja alibaki kimya ndani ya chumba kile na ni Bwana James peke yake ndiye aliyekuwa akizungumza. Kila mmoja alimshangaa, kitendo chake cha kumkumbatia Dylan huku akisema kwamba kijana huyo alikuwa mtoto wake, walimshangaa.
Hawakutaka kuzungumza lolote lile, walihisi kwamba kulikuwa na kitu kilichokuwa kikiendelea hivyo kusubiri ni kitu gani kingetokea baada ya hapo. Bwaja James aliendelea kumkumbatia kwa fuara mpaka baada ya dakika tano, akamuachia huku machozi yakimbubujika mashavuni mwake.
“What is going on?” (Nini kinaendelea?) aliuliza bi Leticia.
“He is my son,” (Ni kijana wangu) alijibu.
“Your son?” (Kijana wako?)
“Yes!”
Kila mmoja alishangaa, maneno aliyoongea yaliwachanganya, ilikuwaje mtu huyo aseme kwamba huyo alikuwa kijana wake na wakati hawakuwa hata ndugu? Hapo ndipo Bwana James alipoanza kuhadithia kila kitu kilichotokea siku ya nyuma, kipindi kile tsunami ilipotokea mpaka mpenzi wake kufariki dunia na yeye kumuweka mtoto katika friji.
“Sikuwa na jinsi, sikuwa tayari kumuona mtoto wangu akifariki hivyo nilichokifanya ni kuchukua friji na kumuingiza ndani,” alisema Bwana James na kuendelea.
Alisimulia kila kitu mpaka namna alivyonusurika na mwisho wa siku kukutana na msichana Catherine na hivyo kuanza uhusiano wa kimapenzi na mwisho wa siku kumuoa na kupata mtoto aliyempa jina la Catherine ambalo lilikuwa ni kama kumuenzi mpenzi wake wa zamani.
“Wewe ni baba yangu?” aliuliza Dylan huku akionekana kutokuamini.
“Ndiyo! Wewe ni mtoto wangu wa kwanza...nilijua nimekupoteza na nisingekuona tena,” alisema Bwana James.
Moyo wake ulijawa na furaha tele, hakuamini kwamba mara baada ya miaka mingi kupita tena huku akiwa amemtelekeza mtoto wake katika friji hatimaye siku hiyo angeonana naye.
Huo ndiyo ulikuwa mwanzo, Dylan alifanyiwa matibabu na kisha kuruhusiwa kuondoka huku akitakiwa kunywa dawa alizopewa kwa ajili ya afya yake. Hilo halikuwa tatizo, hivyo wakaanza safari ya kurudi nchini Marekani.
Muda wote Bi Leticia alikuwa kimya, moyo wake ulimuuma, alihakikisha kwamba Dylan hajui chochote kile kwa kuwa aliogopa kumpoteza katika maisha yale lakini mwisho wa siku kijana huyo akajua kama yeye hakuwa mama yake, tena katika hali ambayo hata yeye mwenyewe hakuitegemea.
Safari ya kurudi nchini Marekani iliendelea kama kawaida, safari nzima Bwana James alionekana kuwa mwenye furaha tele, alikuwa karibu na Dylan na muda wote alikuwa akimwangalia, moyo wake ulijisikia faraja kubwa.
Mbali na hilo, pia kulikuwa na kitu kilichomtatiza sana kuhusu binti yake, Catherine ambaye alimuahidi kwamba angefanikisha kijana huyo anakuwa mpenzi wake kwa gharama zozote zile.
“Sijui itakuwaje?” alijisema pasipo kujua kama alisikika.
“Kuhusu nini?”
“Catherine, ananiumiza sana kichwa..” alijibu.
“Mwambie ukweli....nadhani kila kitu kimetokea kwa makusudi ya Mungu,” alisema Dylan.
Njiani, Catherine alikuwa askisumbua, kila wakati alikuwa akimpigia simu baba yake, alitaka kujua ni kitu gani kilikuwa kikiendelea, alitaka kufahamu kama mzee huyo alifanikiwa au la.
“Niambie baba...” alisema Catherine.
“Usiwe na presha, tunakuja...” alijibu.
“Umefanikiwa? Niambie ukweli, unaniweka kwenye mshtuko mkubwa...”
“Usijali, nitakuja na utajua kila kitu...” alisema Bwana James.
Walichukua saa ishirini na mbili ndipo wakaanza kuingia nchini Marekani. Kila mmoja alikuwa amechoka. Baada ya kufika katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa JFK jijini New York, wakateremka na kuelekea nje ambapo huko wakakuingia ndani ya magari yao na kuondoka kuelekea nyumbani.
“Dylan...ninamshukuru Mungu hatimaye nimekutana nawe, nilikufikiria kwa kipindi kirefu sana,” alisema Bwana James kwa sauti ya chini huku akionekana kuwa mwenye furaha tele.
Hawakuchukua muda mwingi wakafika nyumbani hapo ambapo gari likaingizwa ndani ya eneo la jumba hilo kubwa. Dylan alibaki akiliangalia jumba hilo tu, hakuamini kile alichokiona, hakuamini kama ingetokea siku ambayo angeweza kuingia katika jumba kubwa kama lilivyokuwa hilo.
Gari lilipoingizwa ndani, wakateremka na kuingia ndani. Kitu cha kwanza kabisa alichokifanya Bwana James ni kumuita mkewe na mtoto wake, Catherine. Kwa jinsi uso wake ulivyoonekana tu, tabasamu pana wakajua kwamba tayari Dylan alimazana na mzee huyo na hatimaye alikubali kumuoa.
Kitu cha kwanza kabiisa alichokifanya Catherine ni kumsogelea Dylan na kisha kumkumbatia kwa nguvu kama kawaida yake. Tabasamu aliloonyesha baba yake lilimpa uhakika kwamba kila kitu kilikuwa kama kilivyotakiwa kuwa.
“Naomba unioe Dylan, ninaumia jinsi unavyonikataa!” alisema Catherine kwa sauti ndogo, nyororo ya kumtoa nyoka pangoni.
Dylan hakujibu kitu, alibaki akimwangalia msichana huyo. Bwana Dylan alisimama pembeni, alifuatilia kila kitu kilichokuwa kikiendelea. Japokuwa alijua kwamba binti yake angeumia sana mara baada ya kumwambia kwamba Dylan alikuwa ndugu yake lakini hakutaka kujali, ilikuwa ni lazima amwambie ili kuepusha mambo mengine.
“Catherine...” aliita Bwana James huku uso wake ukiwa kwenye tabasamu pana.
“Abeee...”
“Kaa kochini kwanza...” alisema Bwana James huku tabasamu likiendelea kuonekana usoni mwake.
Wote wakakaa kochini. Catherine hakutaka kukaa mbali na Dylan, alikaa pembeni yake huku akiwa na shauku ya kutaka kusikia baba yake angesema nini juu ya kile alichokuwa amemwambia.
“Baba zungumza.....nini kinaendelea?” alijikuta akisema kwa sauti ya chini. Moyo wake ulikuwa na hamu kubwa wa kusikia kile alichotaka kuzungumza baba yake.
Kila mmoja alikuwa na hamu ya kumsikiliza Bwana James alitaka kuzungumza nini kuhusu Dylan. Wote walikuwa na uhakika kwamba mvulana huyo alikubali kuwa naye kwa sababu hata uso wa Bwana James ulionyesha matumaini makubwa baada ya tabasamu kubwa kuonekana usoni mwake.
Kitu cha kwanza kabisa alichokifanya Bwana James kilikuwa ni utambulisho kwa Bi Leticia ambaye alikuwa pembeni kabisa. Hilo walilifahamu kwamba mwanamke yule waliyekuja naye alikuwa mzazi wa Dylan, wao walichotaka kufahamu ni juu ya Dylan, alikubali kuwa naye, au alikataa.
“Baba, unazunguka sana, tuambie nini kinaendelea,” alisema Catherine huku akionekana kuwa na hamu ya kusikia kile alichotaka kusikia.
“Hakuna ndoa...” alijibu Bwana Dylan kwa kifupi.
“Unasemaje baba?”
“Hakuna ndoa...hakuna tena!” alisema mzee huyo.
Hapohapo Catherine akayahamishia macho yake kwa Dylan, hasira za waziwazi zikaonekana machoni mwake, kile alichozungumza baba yake kilimuumiza moyoni mwake na hakutegemea kusikia kitu kama hicho.
“Kwa nini? Kwa nini unanikataa Dylan, kwa nini hunipendi Dylan?” aliuliza Catherine huku akimkunja shati Dylan ambaye hakuzungumza kitu chochote kile.
Catherine aliumia mno, hakuamini kuona kile alichokisikia kutoka kwa baba yake, japokuwa Bwana James alitaka kufafanua nini kilitokea lakini Catherine akasimama kutoka pale alipokuwa, akatoka nje na kuanza kukimbia mitaani.
Kila mmoja akashtuka, hawakutaka kubaki mahali hapo, walijua jinsi msichana huyo alivyompenda Dylan, kwa kukosa penzi alikuwa tayari kufanya kitu chochote kile hata kujidhuru.
Wakatoka nje na kuanza kumkimbiza, alikimbia kwa kasi, mtaa mzima ulikuwa kimya na ni yeye tu ndiye aliyekuwa akionekana barabarani. Walikuwa nyuma, walimkimbiza huku wakimuita lakini msichana huyo hakutaka kusimama.
Alipokimbilia ilikuwa ni kwenye jengo kubwa la Motorola lilikokuwa hapohapo New York ambapo halikuwa mbali na mtaa wao ulipokuwa, jengo hilo lilikuwa refu na kulikuwa na floo zaidi ya mia moja.
Japokuwa kulikuwa na walinzi getini na walimuona wakati akija kwa kasi kule walipokuwa, msichana huyo hakusimama, alikimbia, alipofika pale getini akapita kama upepo, alipoingia ndani ya jengo hilo, kitu cha kwanza akaanza kupanda kwenda juu kwa kutumia ngazi.
“Anakwenda wapi?” aliuliza Bwana James huku akionekana kuwa na wasiwasi.
“Anakwenda kujirusha ghorofani,” alijibu Dylan.
Kwa kuwa alikuwa mtu wa mazoezi, akaongeza kasi zaidi, akaingia ndani ya jengo lile na kuanza kupandisha juu huku akimuita Catherine. Alikuwa makini, kila floo aliyofika, alikuwa akiangalia kama msichana yule alikuwa mahali hapo.
Aliendelea kupandisha juu zaidi, alipofika katika floo ya ishirini, akamuona Catherine akiwa amesimama pembezoni mwa ukuta huku akijiandaa kujirusha.
“Catherine...usijirushe, tafadhari usijirushe...” alisema Dylan huku akihema kwa nguvu.
“Utanioa?” aliuliza Catherine huku akiwa anajiandaa kuruka.
“Catherine....”
“Niambie utanioa?” aliendelea kuuliza.
“Catherine, wewe ni ndugu yangu, nitakuoa vipi? Tangu lini mtu akamuoa dada yake?” aliuliza Dylan huku akimwangalia Dylan usoni.
“Nani ndugu yako?”
“Wewe...wewe ni ndugu yangu wa damu, baba yako ni baba yangu pia, zamani alizaa na mwanamke aitwaye Catherine, alipotezana naye kwenye balaa la tsunami, jina lake ndiyo akakupa wewe kama kumbukumbu...Catherine, tunachangia baba, siwezi kukuoa...” alisema Dylan huku akimsogelea Catherine pale alipokuwa.
Catherine hakuamini kile alichokisikia, moyo wake ukapigwa ganzi na akabaki akimwangalia Dylan tu, moyo wake ulichanganyikiwa, alipomwangalia kijana huyo alionekana kufanana kabisa na baba yake, hakuwa na wasiwasi kwamba yule alikuwa ndugu yake.
“Wewe ni ndugu yangu?” aliuliza Catherine, hakuonekana kuamini hata kidogo.
“Ndiyo! Catherine, sikuwa nikilifahamu hili, baba hakuwa akilifahamu pia, yule mwanamke ambaye kila siku nilijua kwamba ni mama yangu ndiye aliyesema ukweli, niliokotwa baada ya mama kufa, akanilea mpaka muda huu,” alisema Dylan, tayari alimfikia Catherine, alichokifanya ni kumvuta na kumkumbatia.
Sauti kubwa ya kilio cha Catherine ikaanza kusikika mahali hapo, aliumia kile alichokisikia, moyo wake ulikosa furaha. Akajuta kuuruhusu moyo wake kumpenda mwanaume ambaye ukweli wa mambo ulieleza kwamba alikuwa ndugu yake wa damu.
Mpaka dakika kumi baadaye, Bwana James na mkewe walifika katika floo hiyo, kila mmoja alionekana kuchoka mno. Hawakuwa peke yao bali walikuwa na watu wengine ambao wote hao walibaki wakiwaangalia kwa mshangao, hawakujua ni kitu gani kilikuwa kikiendelea.
“Watoto wangu...” alisema Bwana James, akawasogelea na kuwakumbatia wote.
Je, nini kitaendelea?