UTAJIRI WA DAMU-19-
"Mzee Mitimingi hapa umeletwa mbele yangu kwa sababu ya vitu viwili, kiganja cha mkono na ngozi za chui, basi. Unaelewa hili?"
"Naelewa." Akajibu.
"Bila kukutwa na vitu hivyo wala usingehojiwa hapa. Je, kile kiganja ni cha nani?" alihoji mtu yule ambaye ni askari wa upelelezi.
Mzee Mitimingi alipata kigugumizi cha kujibu swali akawa anang'aang'aa macho tu.
SASA TIRIRIKA NAYO..
Ndani ya chumba kile cha mahojiano kulikuwa na baridi kali kutokana na kuwa na kiyoyozi, lakini nadhani iliongezeka mwilini mwangu kutokana na woga wa kesi inayotukabili.
Nilikuwa najiuliza kwamba inawezekana kabisa tukaunganishwa na kesi ya mauaji ikiwa kama kuna maiti iliwahi kuokotwa ikiwa haina kiganja.
Naamini kabisa kuwa woga wangu wa kuhojiwa na polisi haukumzidi mzee Mitimingi ambaye alikuwa akitetemeka waziwazi.
Licha ya mwili wake kutetemeka lakini pia meno yake niliyasikia yakigongana na nikahisi kwamba anaweza kuanguka kwa presha.
Yule askari aliyeletwa atuhoji alikuwa akitembeatembea katika chumba kile kana kwamba hakuwa na kazi ya kufanya.
Baadaye alirudia kumuuliza mzee Mitimingi swali lilelile.
"Kile kiganja ni cha nani?"
Mzee Mitimingi hakujibu akawa anazidi kutetemeka. Nilishitukia akizabwa kibao cha shavuni.
"Mzee sema, nitakuumiza na sitaki kabisa kupoteza wakati hapa. Niambie kile kiganja ni cha nani?"
"Mimi nililetewa tu mheshimiwa."
Baada ya jibu hilo alikula konzi ya nguvu kichwani, akawa anamwagika jasho.
"Sitaki majibu nusunusu, sema aliyekuletea."
"Nililetewa na mganga wa kienyeji."
"Mzee nadhani unataka kuleta mchezo. Huyo mganga hana jina siyo?"
"Anaitwa Mwapacha."
"Anaishi wapi au mtaa gani?"
"Anaishi Mtaa wa Kamchape, jirani na grosari."
"Alikuambia kiganja kile ni cha kazi gani?"
"Alisema kitanifanya niwe tajiri sana."
"Je, tangu akuletee kiganja hicho umetajirika."
"Sikutajirika kwa ajili ya kiganja nilikuwa nimeshakuwa tajiri ila alisema utajiri utaongezeka mara dufu."
"Uliongezeka?"
"Ahh wapi!!"
"Alikuambia sababu za wewe kutotajirika zaidi?"
"Alisema angenipa sababu hivi karibuni."
"Kiganja kile ni cha nani?"
"Sijui, kwa sababu aliniambia nimtafutie kiganja nikasema hiyo kazi sitaweza, akasema ataifanya yeye."
"Je, vipi kuhusu ngozi ya chui?"
"Hii nililetewa na mwindaji mmoja anayeishi Mtandi."
"Mtandi?"
"Ndiyo, Kijiji cha Mtandi."
"Nakifahamu."
"Unafanya biashara haramu ya ngozi za chui wewe mzee?"
"Hapana, sifanyi."
"Sasa wewe ngozi ya chui kuwa ndani ya nyumba yako maana yake ni nini""
"Hapana, hii ngozi siyo yangu…"
"Siyo yako wakati imekutwa ndani ya nyumba yako? Au kuna mtu aliiweka, kama yupo, nitajie."
"Mle ndani niliiweka mimi…"
"Ndiyo maana nikasema umekutwa na ngozi ya chui maana hata wahenga walisema anayekutwa na ngozi ndiye mwizi wa ng'ombe, hujawahi kusikia msemo huo mzee Mitimingi?"
"Nimewahi."
"Basi hili ni lako. Au unamjua huyo mtu aliyekuletea anakaa wapi."
"Ni yule yule mganga wa kienyeji aliyeniletea kiganja cha mtu."
"Khaa! Huyu mtu ana matatizo kweli, kakuletea kiganja, akaleta na ngozi ya chui, hii nayo alisema ni ya kazi gani?"
"Alisema zote hizo zinahusiana na uganga wake wa kunizidishia utajiri."
"Jamani duniani kuna mambo, mzee utajiri wote ulionao unakubali kuwa na vitu vya ajabu nyumbani kwako, tena siyo vya ajabu bali ni vya hatari kwa maisha yako."
"Kweli kijana wangu, nimekosea sana. Mnisamehe."
"Hili siyo jambo dogo tena, hukusoma kwenye gazeti la Uwazi?"
"Sijasoma."
Yule askari alitoa gazeti na kumuonesha mzee Mitimingi. Kichwa cha habari kilikuwa kikisomeka kwa wino uliokolea, ‘Tajiri akamatwa na kiganja, ngozi ya chui na nywele za watoto.'
"Mzee habari ikishatoka kwenye gazeti kama hivi ni sawa na moto wa petroli, kuuzima ni kazi nzito,"alisema yule askari aliyekuwa akihoji.
"Sasa niambie zile nywele ambazo tulizikuta ndani ni za nani?"
"Mwenye nywele simjui, nazo nililetewa."
"Uliletewa na yule yule mganga?"
"Hapana, alileta ni Che … Che…"
"Unababaika nini?"
Nilianza kutetemeka kwa kuona kuwa akinitaja basi nitakuwa nimekwisha.
Kwa kuwa nilikuwa nipo jirani na mzee huyo nilisogeza mguu wangu na kumkanyaga, kumkataza asinitaje.
Aliniangalia huku akibubujikwa na machozi.
Je, Mzee Mitimingi atamtaja Chempriska kuwa ndiye aliyemletea nywele hizo? Fuatilia Jumatano ijayo.