Utajiri wa damu

Utajiri wa damu

UTAJIRI WA DAMU-21-


Yule askari wa kike alinichukuwa na kunipeleka mahabusu ambako alinifungia lakini kila kitu kilichokuwa kinatokea nje nikawa nakisikia.
“Huyu jamani siyo mbwa, huyu ni binadamu amefanyiwa mambo ya kishirikina na kugeuzwa mtu,” nilimsikia mtu mmoja akisema.
“Ni kweli kabisa afande. Ni lazima huyu mzee Mitimingi na binti yake Chepriska wanalijua hili.”
“Chepriska yupi tena huyo?”
“Si kale kabinti kadogo ulikokaona kanaingizwa mahabusu sasa hivi!”
Moyo ulinipiga paa kwa kuona kuwa wanaozungumza hapo nje wananihusisha na mbwa mtu wakati kiukweli sikujua chochote. Niligundua kuwa wanaozungumza ni askari kwa sababu nilimsikia mmoja akimuita mwenzake afande nikajua kwamba ni lazima watanihoji na kuniadhibu ili niwaambie ukweli kuhusu mbwa mtu huyo ambaye hakika wataniua kama wangenilazimisha niwape habari kwa kuwa sikujua kitu.
Baada ya muda nilisikia mngurumo wa gari nikajua kuwa hilo ni gari la polisi aina ya ‘defenda’ kwa sababu nilisikia askari wakiamuru watu kushuka.
“Shuka mmoja mmoja na kila anayeshuka achuchumae na mkae kwa mstari.”
“Mzee Mitimingi pia chuchumaa nyuma ya huyo mganga wako.”
Maelezo hayo yalinifanya nijue kuwa safari ya mzee Mitimingi na askari makachero kwenda kumsaka mganga wa kienyeji imefanikiwa kwa kumnasa sangoma huyo.
Haukupita muda nilisikia askari wakiwaelekeza waliowaleta kuingia katika ofisi ya wapelelezi.
“Kila anayeingia ndani akae chini.” Ilikuwa ni amri ya askari wa kiume na alisema kwa sauti kali ya juu kuonesha kuwa ilikuwa ni amri.
Chumba cha mahojiano cha askari wa upelelezi kilikuwa siyo mbali sana na mahabusu ya wanawake kwa hiyo kama pana ukimya kiliwezesha anayefungiwa humo kusikia kila kitu.
“Wewe mzee unaitwa nani?”
“Naitwa Antonia Mpepechere.”
“Kabila lako na umri wako.”
“Mmakonde. Nina miaka 65.”
“Kazi yako ipi?”
“Mganga wa kienyeji.”
“Huyu mzee Mitimingi anasema kuwa wewe ni mganga wake, je taarifa hiyo ni kweli au siyo kweli?”
“Taarifa hiyo ni kweli kabisa.”
“Umewahi kumpelekea huyu mzee kiganja cha mtu?”
“Ndiyo.”
“Ulikipata wapi?”
“Nilikipata barabarani, njia kuu ya kuelekea Morogoro.”
“Ulikipataje?”
“Mara baada ya ajali moja ya basi kutokea sijui ni lini, lakini iliua sana, nilikiokota kiganja cha mkono, nikakichukua kwa kuona kuwa kitanifaa kwa kazi yangu.”
“Kazi gani mzee, hukujua kuwa unatenda kosa la jinai?”
“Sikuona kama ni kosa, niliona kitanifaa siku zijazo lakini siku ileile akaja huyu mzee kutaka dawa ya utajiri nikamuagiza atafute kiganja cha mtu akasema hiyo kazi hataiweza, basi nikampa kile nilichokiokota ajalini kwa kulipia. Sikwenda popote kumkata mtu hata ukihoji watu wa kijiji hiki, hakuna ambaye amekatwa kiganja.”
Nilijua kuwa huyo anayejitetea ni yule mganga wa kienyeji wa mzee Mitimingi lakini nikamuona hana akili ya kujitetea kwa sababu kuwa na kiganja tena cha binadamu ni kosa la jinai. Ni bora kingekuwa kiganja ya nyani japokuwa hilo pia angebanwa na watu wa Tanapa.
“Lakini mzee hujui kuwa kiganja cha mtu ni haramu kuwa nacho?”
Kimyaa.
“Sasa tuachane na kiganja, tuambie kuhusu ngozi ya chui ambayo ulimpelekea mzee Mitimingi, ni kweli kwamba wewe ndiye ulimpelekea?”
“Ndiyo.”
“Ulipata wapi ngozi ile?”
“Nililetewa na watu.”
“Tunajua kuwa uliletewa na watu, tunachota utufahamishe watu hao ni akina nani?”
“Siwajui. Mimi walikuja nyumbani kwangu na kuniambia kuwa wana ngozi ya chui, nikainunua, sijui walitokea wapi na hivi sasa nimeingiwa na wazo kuwa inawezekana ndiyo walioleta taarifa kwenu. Kwa maana kuwa inawezekana wamenizunguka.”
“Sasa tuambie kuhusu huyu mbwa mtu. Je, ni wewe ambaye umemgeuza mtu na kuwa katika hali ile?”
“Mimi sijamgeuza isipokuwa mzee Mitimingi nilimpa dawa yenye masharti sasa kwa vyovyote inawezekana yeye hakufuata masharti ndiyo maana yamemkuta ya kumkuta.”
“Lakini unajua wewe mzee una matatizo sana, huoni kuwa kumgeuza mtu mbwa ni kosa? Licha ya kuwa ni kosa hujui kuwa huo ni unyama?”
“Kwa kweli mimi sijamgeuza huyo mtu isipokuwa masharti yamemfanya awe vile?”
“Kwani masharti hayo ni ya nani? Siyo wewe uliyeyaweka?”
Kimyaa.
“Unatakiwa umrejeshee ubinadamu wake. Utaweza kumgeuza?”
“Mhhhh ina…ina…ina….” yule mganga alishikwa na kigugumizi na kushindwa kuzungumza, akawa anameza mate huku jasho likimtoka.

Je, ataweza kumgeuza mbwa mtu huyo au atashindwa? Fuatilia Alkhamisi ijayo........
 
UTAJIRI WA DAMU-22-

ILIPOISHIA
"Lakini unajua wewe mzee una matatizo sana, huoni kuwa kumgeuza mtu mbwa ni kosa? Licha ya kuwa ni kosa hujui kuwa huo ni unyama?"
"Kwa kweli mimi sijamgeuza huyo mtu isipokuwa masharti yamemfanya awe vile?"
"Kwani masharti hayo ni ya nani? Siyo wewe uliyeyaweka?"
Kimyaa.
"Unatakiwa umrejeshee ubinadamu wake. Utaweza kumgeuza?"
"Mhhhh ina ina ina" Mganga alishikwa na kigugumizi na kushindwa kuzungumza, akawa anameza mate huku jasho likimtoka.
Songa Nayo...


Baada ya mahojiano ya muda mrefu mzee yule mganga wa kienyeji alilazimishwa na polisi kumrudishia ubinadamu wake mbwa mtu yule.
"Itabidi mniachie ili nikaifanye kazi hiyo nyumbani kwenye banda langu la uganga."
"Ukweli ni kwamba hutaachiwa isipokuwa utapelekwa kwako na polisi na utakuwa huru kufanya uganga wako,"alisema afisa wa polisi.
"Sawa nakubali. Baada ya hapo je?" alihoji mganga huyo huku akiwa anatoka jasho.
"Kitakachofuata utafahamishwa, elewa kwamba sasa hivi upo chini ya dola."
"Lakini itabidi na mzee Mitimingi tufuatane," akasema.
"Kwa nini? Kwani yeye ndiye aliyemgeuza mtu yule kuwa mbwa?"
"Yeye hakumgeuza lakini ndiye aliyekiuka masharti ya uganga."
"Sawa. Tutamfungulia na mtafuatana naye, kuna lingine?"
"Lipo." Akaitikia mganga yule haraka huku akimuangalia yule askari aliyekuwa akimhoji.
"Lipi hilo mzee?"
"Gharama."
"Gharama za nini?"
"Gharama za kumrejeshea umbile la kibinadamu. Kuna vitu vitahitajika, nani atalipa?"
"Sisi hayo hatuyajui, tunachotaka mtu huyu uliyemgeuza mbwa anakuwa binadamu."
"Sawa, sijakataa sasa nani atalipia gharama ya vitu vya kuchanganya ili awe binadamu?"
"Kwani kunahitajika nini na nini?"
"Vipo vitu vingi kama vile mkia wa kondoo, pembe za ng'ombe mbili, mtungi mkubwa mmoja, kitambaa chekundu mita sita, mbwa mzima mmoja, vibuyu vitatu, mchanga wa baharini au maji ya bahari na kadhalika."
Baada ya kutaja masharti hayo yule askari alimuangalia kisha kutikisa kichwa.
"Ina maana hivyo vyote ni lazima vipatikane? Fanya shotikati."
"Hakuna shotikati katika mambo haya ya uganga. Leteni vitu , turejeshe ubinadamu wake."
"Ukipewa fedha utaweza kuvitafuta vitu hivyo?"
"Penye fedha hakuna lisilowezekana."
"Kama shilingi ngapi kwa vifaa vyote hivyo?"
"Shilingi laki nne."
"Sawa."
Baada ya mahojiano hayo askari yule aliamuru mzee Mitimingi aletwe pale ofisini kwake na baada ya dakika chache alikuwa tayari amesimama mbele ya afande huyo.
"Mzee Mitimingi hapa una msala. Ni lazima mtu huyu uliyemgeuza mbwa ajirudie hali yake na kuwa mwanadamu."
Mzee Mitimingi hakujibu chochote akawa anatetemeka.
***
Mbele ya nyumba ya mganga huyo Mtaa wa Mtandi kulikuwa kumejaa watu wengi waliokuwa na shauku ya kuona kwa macho yao mbwa mtu akigeuzwa na kuwa binadamu.
Kulikuwa na polisi wa kumwaga ambao walikuwa na bunduki za rasharasha pamoja na mabomu ya machozi pia kulikuwa na askari kanzu pamoja na mbwa wa polisi wote hao walikuwepo kulinda usalama wa mganga kwa sababu haijajulikana huyu aliyegeuzwa mbwa ni nani.
Mbwa wa polisi walibweka sana baada ya kumuona mbwa mtu akishushwa katika gari la polisi aina ya difenda.
Bila shaka walikuwa wakimshangaa mwenzao kwa jinsi alivyokuwa anafanana na binadamu hasa macho, pua na mdomo.
Lakini cha kushangaza zaidi mbwa mtu huyo aliwasononesha watu wengi kwa jinsi alivyokuwa akitiririkwa na machozi kama binadamu na mkia wake akiwa ameufyata.
Lakini mzee Mitimingi alipokuwa anashushwa na watu kujua kuwa ndiye aliyesababisha hayo yote alianza kuzomewa na umati uliofurika nje ya nyumba hiyo ya sangoma.
"Mchawi huyoooo, Mchawi huyooo, utajiri wake kumbe ni wa damuu, chawi hilooo," yalikuwa ni maneno ya baadhi ya watu waliokuwa wakimzomea.
Baada ya muda uliwashwa moto katika jiko moja kubwa la mkaa na ukawekwa mkia wa kondoo ambao ulisaidia kukoleza moto na kuwa mkubwa.
Watu waliokuwa wanazomea walikaa kimya ili kushuhudia kitakachotokea na baada ya dakika chache wakamuona mganga wa kienyeji akitoka katika banda la uganga huku akiwa amevaa lile tambaa la rangi nyekundu tupu na mkononi alikuwa ameshika usinga.
Alikwenda moja kwa moja kwenye moto na kutoa kipande cha mkia wa kondoo uliokuwa unababuka. Aliuweka kwenye chungu cheusi na kukatakata vipande kisha akamuendea mbwa mtu na kumlisha mkia huo huku akisema maneno ambayo wengi tulikuwa hatuyaelewi maana yake.
"N-dyeke mwilha, nthathueke ntu (Kula mkia ugeuka kuwa mtu)" ni maneno ambayo alikuwa akiimba mzee huyo.

Je, atafanikiwa kumgeuza mbwa mtu huyo binadamu? Fuatilia Jumatano.
 
UTAJIRI WA DAMU-23-

Umati wa watu uliminyana kila mmoja akitaka kuona kitakachotokea kwa mbwa mtu ambaye alikuwa akila mkia wa kondoo huku akilia.

Alikuwa akitiririkwa na machozi kama binadamu hasa ikizingatiwa kuwa macho yake yalifanana kabisa na ya binadaamu.

Kutokana na watu kumzunguka mbwa mtu huyo, polisi iliwabidi wafanye kazi ya ziada kuwatawanya na baadaye sangoma akaamua kumchukua na kumuingiza katika chumba chake cha uganga.
Watu hawakuridhika na uamuzi huo kwani walikimbilia dirishani kuchungulia ili waone kinachoendelea ndani, hata hivyo, waligonga mwamba baada ya sangoma kufunga madirisha yote, ndani nilikuwepo mimi Chepriscar, mzee Mitimingi, mbwa mtu na wasaidizi wa mganga.
Haukupita muda mrefu yalianza kusikika manyanga yakipingwa huku nyimbo zikiimbwa na sangoma pamoja na wasaidizi wake. Polisi na watu wengine walikaa nje na kushuhudia moshi wa ubani ukitoka kupitia kwenye nyufa za madirisha.
Baada ya dakika thelathini mganga huku akiwa amejifunika kitambaa cha rangi nyekundu alitoka nje ya ile nyumba na kuanza kutangaza:
“Ndugu zangu, kazi imekamilika, mbwa mtu amegeuka binadamu na baada ya dakika chache nitamtoa nje mumuone,”
“Mtoe sasa hivi,” “Mtoeeeee,” “Mtoeeeeeee”, zilikuwa ni kelele za watu waliokuwa wameongezeka baada ya habari hiyo kusambaa mji mzima.
“Ndugu zangu, tuache apumzike na anapewa dawa ili akili zake ziwe sawasawa….. Msiwe na shaka atatoka na mtamuona,” alizidi kuwasihi, niliogopa nikawa na hofu kuwa wanaweza kuvamia na kuingia ndani kwa nguvu.
Baadaye aliingia ndani na baada ya nusu saa alitoka mmoja wa wasaidizi wake na kumchukua mkuu wa wale polisi wakaingia ndani, alipoingia aliniangalia kama vile alitaka kusema na dakika kumi baadaye walitoka sangoma, kamanda na mtu anayetajwa kuwa aligeuzwa mbwa.
Umati ulishangaa huku wengine wakipiga kelele ambazo hazikuwa zikieleweka walitaka nini kwani wapo waliokuwa wakisema; “Azungumzeeee,” wengine wakawa wanasema; “Mpeni kipaza sauti.”
Hii ni kutokana na mkuu wa polisi kutumia kipaza sauti cha kiganjani mara kwa mara alipotaka kuwaambia jambo.
***
Tulikuwa tukishushwa kituo cha polisi kutoka kwenye gari ‘difenda’ ambalo lilikuwa na askari wenye silaha, watu walikuwa wengi kituoni kushuhudia tukio hilo japokuwa walikuwa wakisogezwa mbali na askari.
Alianza kushuka sangoma, akafuatia mzee Mitimingi kisha mbwa mtu ambaye sasa alikuwa binadamu na alivikwa kile kitambaa cha rangi nyekundu na shati alilopewa na sangoma, nikamalizia mimi.
“Wewe Chepriska, mfuate huyo kamanda wa kike akupeleke mahabusu ya wanawake,” alisema yule mkuu wa polisi.
**
Ilikuwa ni Jumatatu, saa mbili asubuhu nilishitukia yule askari wa kike akifungua geti la chuma la chumba cha mahabusu.
“Cheprisca jiandae, tunawapeleka mahakamani,” alisema.
“Kwa kosa gani?” nilimuuliza.
“Utajua hukohuko,” aliniambia huku akitoa pingu kwenye mkanda wake.
Nilifungwa pingu hiyo na kupelekwa nje ambako niliingizwa kwenye difenda. Baada ya dakika chache waliingizwa mzee Mitimingi na yule sangoma, lakini yule mbwa mtu ambaye sasa ni binadamu sikumuona, nadhani aliachiwa.
Baadhi ya ndugu zangu walikuwepo na ndugu wa Sangoma pia walijaa tele pale. Dada yangu mmoja aliniambia nisiwe na wasiwasi kwa sababu wamenitafutia Wakili Mabere Marando ambaye nitamkuta mahakamani.
Nilifarijika sana kusikia hivyo lakini nikajua pia kuwa kwa upande wa mzee Mitimingi alitafutiwa wakili aitwaye Dk. Ngali Maita. Ni sangoma tu ambaye sikusikia ndugu zake wakimfahamisha kuwa atakutana na wakili wake huko kortini.



Itaendelea Jumamosi ijayo
 
UTAJIRI WA DAMU - 24-

Nilifarijika sana kusikia hivyo lakini nikajua pia kuwa kwa upande wa mzee Mitimingi alitafutiwa wakili aitwaye Dk. Ngali Maita. Ni sangoma tu ambaye sikusikia ndugu zake wakimfahamisha kuwa atakutana na wakili wake huko kortini.
SONGA NAYO..


Tulifikishwa katika Mahakama ya Mtandi mapema sana na kweli mimi nilimkuta Marando ambaye alinichukua nikiwa chini ya ulinzi hadi kwenye chumba kimoja cha mawakili mahakamani hapo.
“Wewe ndiye Chepriska bila shaka,” alisema.
“Ndiyo.”
“ Kwa kuwa sijakusikiliza. Hapa leo kila utakachoulizwa utakataa na sisi tutaomba kesi kuahirishwa, baada ya hapo tutajua la kufanya,” aliniambia Marando.
Baadaye tuliingia katika mahakama ya wazi ambayo ilikuwa imefurika watu waliotaka kujua nini kitatokea. Mle mahakamani niliona watu wengi wakiwa na Gazeti la Uwazi ambalo lilikuwa lina picha zetu ukurasa wa mbele huku mbwa mtu akiwa ndiye picha kubwa.
“Kooooooooooorti,” zilikuwana kelele za askari wakati hakimu anaingia mahakamani.
Tulisomewa mashtaka ya kumgeuza mtu kuwa mbwa na kukutwa na kiganja cha mtu na ngozi ya chui. Wote tulikataa. Kesi iliahirishwa mpaka baada ya wiki mbili, tuliwekewa dhamana.
**
Siku ya kesi ilifika shahidi wa kwanza upande wa Jamhuri alikuwa yule mtu aliyegeuzwa kuwa mbwa. Alipanda kizimbani kutoa ushahidi wake nasi watatu, sangoma, mzee Mitimingi na mimi Chepriska tulikuwa katika kizimba cha washtakiwa.
Mwendesha mashtaka Zombi Kwale ndiye aliyekuwa akimuongoza kutoa ushahidi wake.
“Ieleze mahakama, unaitwa nani na dini yako ni ipi na una umri gani?” aliuza mwendesha mashtaka.
“Naitwa Mavata Mpwanyera. Nina miaka 28, Mmakua na Mkristo.”
“Iambie mahakama wale washtakiwa unawafahamu?”
Mavata mbwa mtu: Namfahamu, mzee Mitimingi na sangoma yaani mganga ambaye anaitwa Ntimwi.
Wakili Kwale: Ieleze mahakama, unawafahamuje?
Mavata mbwa mtu: Namfahamu mzee Mitimingi kwa sababu ndiye aliyenigeuza kuwa mbwa mtu na mganga Ntimwi alikuwa akinipa dawa kupeleka kwa huyo mzee.
Wakili Kwale: Ilikuwaje mpaka akakugeuza mbwa mtu?
Mavata mbwa mtu: “Alikuwa ananituma mara kwa mara kwa mganga Ntimwi na nikawa nampelekea. Siku hiyo nilikwenda kwa sangoma Ntimwi akanipa dawa na kunieleza kwamba jinsi ya kutumia amemuelekeza kwa njia ya simu. Nilipofika kwake baada ya kumpa dawa aliniambia nikae kwa muda mle ndani. Baadaye alileta chai tukanywa. Chai ile ilinishangaza kwa sababu chini yake nilikuta kuna vijiti kama kumi na mbili.”
Wakili Kwale: Baada ya kuona hivyo vijiti, nini kiliendelea?
Mavata mbwa mtu: Nilimuuliza mzee Mitimingi, kwa nini hii chai ina miti kumi na mbili?
“Alianza kunifokea kwamba siyo kazi yangu kujua, akasema kwa kuwa nimevunja miiko, sasa nitakiona cha moto. Pale pale nikaanza kuhisi mwili kufa ganzi na kuona ngozi yangu ikianza kubadilika na kuwa kama ya mbwa. Nilianza kulia huku nikiishiwa nguvu na haraka haraka akachukua kitambaa na kunifunga mdomo.”
Wakili Kwale: Baada ya kukufunga mdomo, ilikuwaje? Hakukuwa na mtu mwingine ndani ya nyumba hiyo?
Mavata mbwa mtu: “Hakukuwa na mtu na tangu nimfahamu huyu mzee Mitimingi sijawahi kumuona mtu pale isipokuwa mlinzi tu.
Wakili Kwale: Baada ya hapo ilikuwaje?
Mavata mbwa mtu:Niliendelea kubadilika na kuota mkia, nililia sana kwa sababu sikuwa na la kufanya baadaye nikaona mikono na miguu inanyauka na kugeuka kama ya mbwa, ndani ya dakika kumi nikawa mbwa.
Wasikilizaji: Looooooohhhhh…. mkatili jamani….
Askari polisi: Jamani, hapa ni mahakamani, utulivu unatakiwa, ohoooo.
Wakili Kwale: Baada ya kugeuka mbwa, ulikuwa ukijitambua?
Mavata mbwa mtu: Ndiyo nilikuwa najitambua, akili za kibinadamu hazikuniondoka na ndiyo maana nilikuwa nikilia sana. Baadaye alichukua mnyororo na kunifunga shingoni akawa ananiburuza kunipeleka kwenye banda uani.
Wakili Kwale: Wakati anakupeleka kwenye banda kulikuwa na mtu yeyote anaona?
Mavata mbwa mtu: Ndiyo, alimuita mlinzi akamuambi kuwa amemleta mbwa na itakuwa marufuku kwake kwenda kumpa chakula au kumfungulia kibandani. Nililia sana kwa kujua kuwa sasa nitakufa kwa njaa.


Je, nini kiliendelea? Fuatailia simulizi hii ya kuhuzunisha wiki ijayo.
 
UTAJIRI WA DAMU -25-


ILIPOISHIA
Wakili Kwale: Wakati anakupeleka kwenye banda kulikuwa na mtu yeyote anaona?
Mavata mbwa mtu: Ndiyo, alimuita mlinzi akamuambi kuwa amemleta mbwa na itakuwa marufuku kwake kwenda kumpa chakula au kumfungulia kibandani. Nililia sana kwa kujua kuwa sasa nitakufa kwa njaa.
Je, nini kiliendelea? SONGA NAYO...


Baada ya Wakili Kwale kumuongoza yule mtu aliyegeuzwa mbwa aitwaye Mavata. Hakimu Makoteni alisema: "Sasa ni zamu ya Wakili Mabere Marando anayemtetea Cheprisca kumuuliza maswali anayedaiwa kugeuzwa mbwa."
Nilianza kutetemeka baada ya hakimu kumruhusu wakili wangu kuuliza maswali lakini aliniambia kuwa niondoe shaka kabisa katika shauri hili hasa baada ya kumsimulia jinsi nilivyoingizwa katika kesi hii. Alisimama akaweka vema joho lake la kiwakili.
Marando: Mavata umesema uligeuzwa mbwa, Je, wakati unageuzwa huyu (akanyoosha mkono kunielekea mimi), alikuwepo?
Mavata mbwa mtu: Huyu hakuwepo.
Marando: Je, wakati unakwenda kwa mzee Mitimingi uliwahi kukutana na Chepriska?
Mavata mbwa mtu: Hapana.
Marando: Unamjua au kufahamiana kabla ya kukamatwa na polisi?
Mavata mbwa mtu: Hapana.
Marando: That's all my load (Ni hayo tu mtukufu).
Hakimu Makoteni alimpa nafasi wakili wa mzee Mitimingi, Dk. Ngali kama atakuwa na la kuhoji.
Dk. Ngali: Wewe Mavata umesema uligeuzwa mbwa mtu na mzee Mitimingi, utaihakikishia vipi mahakama?
Mavata mbwa mtu: Mimi siwezi kuihakikishia mahakama kwa sababu nilikuwa mbwa, hiyo kazi wataifanya polisi.
Dk. Ngali: Baada ya kugeuzwa mbwa unasema ulikuwa ukijitambua, kweli au si kweli?
Mavata mbwa mtu: Kweli.
Dk. Ngali: Mahakama itakuamini vipi?
Mavata mbwa mtu: Nitaweza kuhadithia kila kitu hasa siku ambayo polisi walifika pale na kuniona kwa mara ya kwanza na mahakama ikitaka itawaita hao polisi na kuwauliza, naamini maelezo yangu yatafanana na yao na mahakama itagundua kuwa nilikuwa na akili zangu.
Dk. Ngali: Siku hiyo walipofika polisi katika banda hilo ilikuwaje?
Mavata mbwa mtu: Nililia sana, nikasikia askari mmoja akisema bila shaka huyo mbwa hana chakula au kuna kitu kipo bandani kwake. Walipofika bandani walishangaa kumuona mbwa ambaye ana sura kama binadamu. Wakati huo mimi nilikuwa nalia na machozi yalikuwa yakinichuruzika kama binadamu.
Wote waliokuwepo pale walipigwa na butwaa na wakasema huyu siyo mbwa ni mtu na wakati huo mzee Mitimingi alikuwa akitetemeka kama aliyekuwa na homa kali. Mzee Mitimingi na wote waliokuwepo pale wakaondoka huku polisi wakimuagiza mlinzi ahakikishe ananipa chakula kwa sababu bosi wake kuanzia hapo alikuwa chini ya ulinzi wa polisi.
Dk. Ngali: Ikawaje ukachukuliwa na polisi?
Mavata mbwa mtu: Siku ya pili niliona polisi wakiingia uani na kuja katika banda na kunichukua. Polisi mmoja akawa ananiambia nisiogope kwa sababu wamekuja kwa kuwa wana imani kuwa mimi ni mtu niliyegeuzwa mbwa, wakanihakikishia kuwa aliyefanya unyama huo watamgundua na ubinadamu wangu utarudishwa.
Wakati Mavata anahojiwa na mawakili na kujieleza akina mama fulani niliwaona wakilia kwani mara kwa mara walikuwa wakifuta machozi. Nilihisi kwamba inawezekana wale ni ndugu zake.
Dk. Ngali: Ulipofikishwa polisi mambo yalikuwaje?
Mavata mbwa mtu: Nilifarijika sana kumuona mzee Mitimingi akiwa ameshikiliwa huku akiwa na binti yule (akanyoosha mkono kuelekeza kwenye kizimba tulichokuwa tumeketi, moyo ukanifanya paa).
Mavata alichukua kitambaa mfukoni na kufuta machozi kisha akaendelea kusimulia.
Mavata mbwa mtu: Pale ndipo nilipomuona kwa mara ya kwanza mtu aliyempa dawa mzee Mitimingi zilizonigeuza kuwa mbwa.
Dk, Ngali: Ulimjuaje?
Mavata mbwa mtu: Polisi walikuwa wakimshurutisha anirejeshee ubinadamu wangu.
Dk. Ngali: Ni hayo tu mheshimiwa hakimu.
Hakimu aliandika mahojiano hayo kwenye jalada lake kisha akasema kwa kuwa serikali imeshaleta mashitaka ya wote kimaandishi na mawakili na nakala yake sasa ni zamu ya Cheprisca yaani mimi kuhojiwa na wakili wangu.
Wakili Marando alisimama na kuniangalia. Alisogea nilipokuwa nimesimama huku akiwa na kalamu mkononi. Nilihisi kutetemeka lakini nilipiga moyo konde na nilifarijika na maneno yake tulipokuwa faragha kwamba nisiwe na wasiwasi.

Itaendelea Jumapili.....
 
Back
Top Bottom