Uhusiano kati ya China na Afrika wavutia vyuo maarufu duniani kuanzisha utafiti wa ushirikiano kati ya China na Afrika

ldleo

JF-Expert Member
Jan 9, 2010
1,010
1,036
myhc_319951.jpg


Kwa muda mrefu utafiti wa kitaaluma kuhusu Afrika halikuwa ni jambo linalofikirika kwa watafiti wengi, kwani utafiti kuhusu bara la Afrika ulikuwa na wigo mdogo na matokeo yake kitaaluma hayakuwa makubwa, na hivyo utengaji wa fedha zinazohusu masomo au utafiti unaohusiana na bara la Afrika ulikuwa finyu hata kutokuwepo kabisa.

Kimsingi hali hii bado haijabadilika sana, lakini katika kipindi cha miaka 10 iliyopita kumekuwa na ongezeko la masomo yanayohusu utafiti kuhusu Afrika.

Elimu katika nchi za magharibi imewaaminisha watu kuwa Afrika ni sehemu iliyojaa dhiki, migogoro na changamoto nyingi, na sio sehemu inayostahili ufuatiliaji mkubwa zaidi ya maliasili zake kama vile madini na mafuta, au vivutio vya utalii kama vile fukwe na mbuga za wanyama.

Hii ndio picha waliyoondoka nayo wakoloni, na ndio picha iliyobaki kwa watu wengi wa magharibi kuhusu Afrika. Kwa hiyo waliokuwa wanasoma kuhusu Afrika ni wale waliotaka kujua jiografia yake, anthoropolia na kidogo siasa zake, ndio maana vyuo vingi vya nchi za magharibi havikuwa na kozi zinazohusu nchi za Afrika.

Katika muongo mmoja uliopita kumekuwa na wimbi jipya la ongezeko la utafiti kuhusu Afrika. Kwa sasa nchini Marekani Chuo Kikuu cha Brown-Rhode Island, Chuo Kikuu cha California, Chuo Kikuu cha Yale na Chuo Kikuu cha Columbia, na nchini Uingereza Chuo Kikuu cha London (SOAS) vinatajwa kuwa ni vyuo vyenye masomo ya utafiti wa kina kuhusu Afrika na mambo ya Afrika.

Sio kama tu vyuo vikuu hivi vimekuwa vikipata wanafunzi kutoka katika nchi hizo, bali pia vimekuwa na wanafunzi kutoka nchi mbalimbali duniani.

Kumekuwa pia na idara maalum katika vyuo vikuu mbalimbali ambavyo, vimeanzisha utafiti maalum, au kozi maalum kuhusu uhusiano kati ya China na nchi za Afrika. Ni nini kimesukuma vyuo na taasisi mbalimbali za utafiti kuanza kuweka mkazo kwenye masomo kuhusu Afrika?

Ukweli ni kwamba kilichosukuma ongezeko la wataalamu wa magharibi kutaka kujua zaidi Afrika kuna nini, ni kutambua kuwa picha iliyojengwa na vyombo vya habari vya nchi za magharibi si sahihi.

Kwanza katika kipindi hicho cha muongo mmoja, hali ya uchumi wa nchi za Afrika ilishangaza wataalamu wa uchumi, na katika ya nchi 10 zilizokuwa na ongezeko la kasi la uchumi duniani, nyingi zilikuwa ni nchi za Afrika.

Pili ni kuwa ushirikiano wa karibu kati ya China na Afrika umezitia wasiwasi nchi kubwa za magharibi. China ni nchi pekee kubwa duniani yenye mtazamo tofauti na nchi za magharibi kuhusu Afrika, na kupitia ushirikiano na nchi za Afrika makampuni ya China yaliyoko barani Afrika yameweza kupata faida kutokana na uwekezaji wake, na pia yameweza kubadilisha sura ya Afrika hasa kwenye upande wa miundo mbinu.

Katika kipindi hicho pia nchi kubwa za magharibi ambazo kwa muda wa miongo saba zilizoweka pembezoni nchi za Afrika, zilianza kutambua polepole kuwa bara la Afrika ni bara lenye umuhimu mkubwa kimkakti na kwenye siasa za kijiografia.

Ukaribu wa kisiasa kati ya China na nchi za Afrika ambao msingi wake ni ukaribu wa ushirikiano wa kiuchumi, umefanya pande hizi mbili kuwa na sauti moja kwenye jukwaa la kimataifa.

Ile hali ya nchi za magharibi kuzilazimisha nchi za Afrika kufuata maoni yake inaendelea kufifia, na ndoto ya jinamizi ilitokea pale wakati nchi za Afrika ziliamua kuwa na maoni yake huru kuhusu mgogoro kati ya Russia na Ukraine.

Ukweli ni kwamba uhusiano kati ya China na Afrika umekuwa na matokeo mazuri kwa nchi za Afrika, na umeweza kubadilisha sura ya nchi za Afrika kwa watu wa magharibi.

Kulipuuza bara la Afrika kwa muda mrefu kumekuwa na matokeo mabaya kwa nchi za magharibi, na kuzifanya sasa zianze kufanya juhudi kwenye sekta ya elimu, diplomasia na hata uchumi ili kurudisha mvuto wake kwa nchi za Afrika. Ni jambo la kukaribisha, lakini kinachosubiriwa ni nini kitakacholetwa na hamasa hii mpya.
 
Back
Top Bottom