Mwanakijiji,
Nafurahishwa sana na michango yako. Sijawahi hata siku moja kukuandikia au kukujibu makala yako yoyote. Mimi ni mmoja wa watu tunaovutiwa sana na michango yako. Na huwa nasoma michango yako yote.
Leo naandika kwa kuwa umenistua.......nimehisi kama unataka kuweka mpira kwapani na kutundika njumu. Nafahamu kuwa kuna wakati unafikia hatua ya kukata tamaa kwa kuona kuwa pamoja na mawazo yako mazuri pengine nguvu na ushawishi wako una kikomo. Nikukumbushe tu kuwa 'mwale mdogo wa mshumaa hufukuza giza'. Hivyo, usikate tamaa kwa kuwa kila siku bila kujua unatengeneza shujaa mmoja ama unagusa sikio na moyo mmoja wa mtu mpya.
Nikirudi kwenye hoja yako ya hitaji la chama kipya. maoni yangu ni hatuhitaji chama kipya. Kwa maoni yangu, Sera za CCM ni sera za kitaifa. Ni za kitaifa si kwa sababu ya umahiri wa viongozi wa sasa, ila ni kwa sababu ni Chama kilichoundwa kwa mtazamo wa kuwa Chama cha Umma, chenye agenda ya Umma (Mass Party). Isitoshe, CCM imekuwa madarakani kwa miaka 49 ya uhuru wetu ( Nikijumlisha na TANU) na hivyo kuwa sehemu ya utamaduni wetu. Kama kuanguka kwa CCM ndio kungezaa vyama vingi mwaka 1992, basi hoja yako ingekuwa na mantiki, tungehitaji chama Kipya. Lakini kwa kuwa CCM imeendelea kuwepo katika mfumo wa vyama vingi, utakuta kuwa vinavyoitwa vyama vya upinzani si kitu zaidi ya kuwa mchepuo wa CCM kisera au kivuli cha Chama fulani kutoka nje.
Vyama vyetu vya upinzani ni 'reactionary'. Vimezaliwa kutokana na kuwepo CCM si kutokana na vuguvugu la mabadiliko ya mfumo lililotokana na umbwe wa falsafa, itikadi au sera. Ndiyo maana utakuta kwa kiasi kikubwa vimekuwa vikiishi kwa kuibomoa na kuikandia CCM tu. Nafasi ya mawazo mbadala ni finyu. Tatizo lao kubwa ni kutoridhika tu kwa namna ambavyo sera na itikadi ya asili ya CCM isivyoshughulikiwa ipasavyo. Sio kosa la wapinzani ama mapungufu yao, ila ndio mazingira yanavyowalazimu.
Hivyo, leo hii, hata ungeanzisha Chama kipya, sitarajii kuwa kitakuja na itikadi ama sera tofauti na zilizopo. Na kwa kiasi kikubwa, ili Watanzania wakuelewe, lazima utagusa yale maeneo ambayo watanzania wanayathamini. Utaongelea amani, mshikamano, usawa wa binadamu, utu na kujitegemea. Hii ndio misingi ya utamauni wa siasa (political culture) ya Tanzania. Na hii iko katika CCM. Narudia tena, si kwa kuwa CCM ni werevu sana, isipokuwa tu, historia imeipa CCM tunu na dhima hiyo. Ahadi za Mwana Tanu na baadae mwana CCM zimeendelea kuhodhiwa na CCM, baadhi ya misingi na falsafa za kiuongozi zilizokuwapo kwenye Azimio la Arusha zimeendelea kuhodhiwa na CCM. Hivyo, Tanzania kwa kiasi kikubwa ni CCM. Ndio maana Baba wa Taifa aliwahi kusema kuwa " Bila CCM madhubuti nchi yetu itayumba". Ni imani yangu kuwa, masuala haya ya Ahadi za mwana TANU, Azimio la Arusha na hususan maadili ya uongozi vingekuwa kwenye Katiba ili viwe mali ya wote na si CCM pekee. Tanzania ni muhimu zaidi kuliko CCM. CCM yaweza kuondoka siku moja....lakini taifa linapaswa kuendelea kuwepo.
Kwa mantiki hiyo, niungane na waliotangulia kusema kuwa tatizo tulilokuwa nalo katika uwanja wa siasa leo hii ni ukosefu ama udhaifu wa uongozi ambao unazaa wanasiasa hovyo. Tukipata viongozi wazuri, vyama vilivyopo na sera zilizopo zatosha. Hata ukiangalia CCJ na ujio wake, ukisoma kile wanachokisimamia utagundua kuwa si kipya bali ni kile ambacho CCM wameacha kukisimamia na kukisemea ilihali kipo katika sera na miongozo yake. Katika nchi maskini kama zetu, siasa ni maji, chakula, elimu, afya na miundombinu. Hizo ni agenda za kitaifa. Wananchi wetu wanahitaji matumaini ya maisha yao na vizazi vyao. Hakuna Chama kitakachokuja na agenda mbali na hizi na kikubalike.
Changamoto iliyo mbele yetu ni kupata uongozi huo. Nadiriki kusema kuwa tatizo tulilokuwa nalo leo katika vyama tulivyokuwapo ni kuwa vyama vya upinzani vingali vikiongozwa na viongozi wa kizazi cha kwanza cha mageuzi (1st generation of opposition leaders). Viongozi wa Kizazi cha Kwanza cha mageuzi ( Mrema, Lipumba, Seif, Mtikila, Mbatia na Cheyo) ambao kuwa kwao upinzani kulikuwa ni aidha kuchukizwa au kuenguliwa katika mfumo wa CCM wangali ni viongozi hadi leo. Nakiri kuwa walifanya kazi nzuri sana lakini utume wao umefika kikomo. Wafuate nyayo za Mtei, Makani , Chipaka, Marando na wengine waliostaafu.
Kizazi cha Pili cha Mageuzi (Mbowe, Slaa, Ruhuza, Lwakatare, Lissu) ni kizazi cha pili cha mageuzi. Nacho kinakaribia kukamilisha utume wake ambao ulikuwa ni kuchepuka kutoka kwenye siasa za kupandikiza chuki na kuamia kwenye siasa za kujenga hoja, kutoa fikra mbadala, kuhubiri utaifa na kuongelea agenda za kitaifa (mfano rasilimali za nchi) na hasa kupata busara ya kutumia BUNGE kama chombo cha mabadiliko kuliko majukwaa ya kutupiana lawama na kupaka matope CCM. Kizazo hiki kimeleta mapinduzi katika upinzani ya kifikra na kiutendaji.Sasa tunapata mawazo mbadala juu ya mfumo wa kuendesha nchi mfano "Sera ya Majimbo". Kizazi hiki bado kina jukumu kubwa la kuandaa kizazi cha tatu cha makada na wapinzani wa kitaifa (humu wako wakina Mdee, Mnyika, Zitto na wengineo).
Hakika tunakwenda vizuri kama taifa. Yafaa tuvute subira. Suluhisho si kuing'oa CCM madarakani. Tena ni kosa kubwa kutaka kuing'oa CCM ghafla. CCM ni zaidi ya chama katika Tanzania. Ni taasisi kubwa, ni imani, ni historia, ni utamaduni na zindiko la nchi hii. Imeishi nasi kwa miaka 49 (including ya TANU) na haiwezekani ikaondolewa ghafla na nchi hii ikabaki salama. Ni heri ife taratibu na kansa yake yenyewe wakati upinzani ukikomaa na kupata mbadala wake. Tuongozwe zaidi ya dira ya Tanzania kwanza. Tuisaidie CCM kwa kuiboresha, tuipe upinzani wa kuisaidia kama inavyofanyika katika BUNGE hili la 2005-2010. Vyama vilivyoleta Uhuru vina mapungufu yake lakini si sumu......Botswana inaongozwa na Chama kikombozi na tawala na uchumi wake unakwenda vizuri na nchi inatawalika na imetulia.
Nimalizie tu kwa kusema kuwa, sishawishiki kuwa tunahitaji Chama chochote kipya kwa sasa.
Tanzania itajengwa na wenye moyo! Tanzania, Tanzania..... nakupenda kwa moyo wote!