Tulichomfanya yule mchawi hatakuja kusahau kamwe

UMUGHAKA

JF-Expert Member
Sep 1, 2021
2,157
10,718
Nisikuchoshe na usinichoshe, tusichoshane.

Miaka ya fulani baada ya kumaliza shule ya sekondari,niliamua kwenda kumsalimia Ba'mdogo aliyekuwa mkuu wa shule fulani ya sekondari hapo kwenye hicho kijijini.

Wana kijiji walikuwa wakimpa heshima kubwa Ba'mdogo kwasababu wanafunzi wote waliosoma kwenye ile shule walifaulu kuendelea na elimu ya Sekondari ya upili(Advance),japo shule ile ilikuwa ya kata na kwa mwaka ule nilienda mimi ilikuwa imefaulisha kwa awamu ya kwanza,yaani toka hiyo shule ianzishwe wanafunzi waliokuwa wamefika kidato cha ilikuwa tayari ni mara moja,hivyo nilipofika mimi wale nilowakuta ndo walikuwa wa awamu ya pili.

Sasa kwa mwaka ule wa kwanza wanafunzi wa kidato cha nne walimaliza 12 na wote walifaulu kuendelea Advance tena walienda kwenye shule za vipaji maalumu ikiwemo Ilboru.Sasa wanakijiji kiukweli walimpenda sana Dingi mdogo kwa kujitolea kuwaleta waalimu wa ziada ambao kile kijiji kilikuwa kinawalipa.

Nilipofika nilikuta pale kwa Ba'mdogo kila siku iendayo kwa Mungu ilikuwa inakuja Galoni ya maziwa fresh lita 5, kile kijiji kilikuwa na wafugaji wengi sana wa mifugo ya kila aina! Yaani kumuona mwanakijiji anamiliki ng'ombe elfu 10 ilikuwa kitu cha kawaida,sasa mbali na maziwa, kila Jumapili alikuwa analetewa kuku jogoo mmoja na mwanakijiji.

Ba'mdogo aliwahi kuniambia waliwahi kukaa kikao na wana kijiji wakakubali kila kaya kuwa wanakamua maziwa kulingana na zamu walizokuwa wamewekeana kwa ajili ya mwalimu mkuu ikiwemo kitoweo hicho cha kuku.

Nilipofika mara ya kwanza kwa sababu ya uroho na ulafi, nilikuwa nakunywa yale maziwa kwa wingi kana kwamba kesho hayatokuja mengine,yaani kila niliposikia kiu ya maji mimi nilitwanga maziwa, baadae sasa baada ya kuzoea ilifika sehemu tukawa tunayaangalia na tunaishia kuyamwaga tu maana hakukuwa na wakumpa.

Pale kwa Ba'mdogo baada ya mimi kufika,ni kama nilifanya wapumue maana kazi za hapa na pale nilikuwa nikizifanya mimi, ilikuwa ikifika ijumaa dingi mdogo alikuwa akiondoka kuelekea mjini kwa familia yake na ikifika jumapili jioni alikuwa akilejea.

Sasa kwa wakati huo dingi mdogo alikuwa akiishi na bwana mdogo mmoja alikuwa wa rafiki yake ambaye baada ya kufeli shule mahali fulani alimpatia namba na jina akawa amerudia pale kidato cha pili,hivyo nilipofika mimi tukawa watu watatu.

Japo kulikuwa ni kijijini lakini kulikuwa na maisha fulani ya amani sana,kulikuwa na Lambo kubwa ambalo wanakijiji walikuwa wakijipatia maji ya mahitaji yao hapo. Kwa upande wa umeme ulikuwa bado haujafika na wana kijiji walitumia Solar na Majenereta.

Ilipokuwa ikifika wikiendi nilikuwa ninashuka senta kwa ajili ya kuangalia mpira,wakati huo nilikuwa shabiki wa kutupwa wa Arsenal, ingawaje hivi leo sina mahaba kama hapo zamani kwasababu timu haieleweki nini inafanya. Yaani ilikuwa ni bora nilale na njaa kuliko kwenda kuitazama timu yangu pendwa ya Arsenal.

Kwenye ule ukumbi jamaa alikuwa anatumia jenereta na malipo ilikuwa Tsh 100 kwa wakati ule, sasa lile jenereta lilikuwa likiwashwa wakati wa mechi inapoanza tu ili kuokoa mafuta, yale mambo ya kuangalia uchambuzi wa kina Thomas Mlambo na Robert Marawa yalikuwa hayapo.

Sasa nilikuwaga nikimaliza shughuli zangu hapo nyumbani ikifika saa nane mchana,huyoooo naondoka zangu na kurudi mpaka gemu nihakikishe zimeisha ndo narudi nyumbani. Yule jamaa aliyekuwa hapo nyumbani hakuwa mpenzi wa mpira ila alikuwa mpenzi wa papuchi, yaani alikuwa anatembeza stiki si kwa wanafunzi wenzie tu, hadi wanakijiji.

Kutoka hapo nyumbani hadi ufike senta ilikuwa kilomita 3, kwenda na kurudi inakubidi utembee kilomita sita. Kiukweli kile kijiji hakikuwa na ujambazi wala vibaka, shida ya pale ilikuwa Uchawi!

Aiseeee sijawahi kuona asikwambie mtu.


-/-/-/-/-/-/-/-/-/-/-/-/-/-/-/-/-/-/-



SEHEMU YA - 2


Sasa siku moja nakumbuka ilikuwa kati kati ya wiki nadhani kati ya J4 au J5, siku hiyo kulikuwa kuna mashindano ya Uefa champions ambapo timu yangu pendwa ilikuwa ikicheza na Chelsea.

Nilijiandaa mapema kabisa ilipofika mida ya saa 1 usiku nikamwambia Dingi mdogo anipe ruhusa na bila ajizi akaniruhusu kwenda kutazama kabumbu, japo alinisisitiza nisiende maana wakati wa kurudi ingekuwa shida lakini mwanaume sikutaka kuelewa hata kidogo. Baada ya kuona nimekuwa mbishi na mpira uko kwenye damu aliamua kuniruhusu huku akisema "Uwe makini maana huu mji siyo huko ulikotoka, huu mji una wenyewe".

Basi nikamuomba yule jamaa tuondoke nae jamaa akagoma akasema yeye anajisomea,sikutaka kuchelewa ikabidi niondoke zangu. Plani yangu ilikuwa ni kwamba niondoke hiyo saa 1 ili kufika kwenye ngoma 2 niwe nimefika nikapige soga na kubadilishana mawazo na mashabiki wengine pale kwenye banda huku tukisubiri mpira uanze.

Sasa kwenye ile njia ya kwenda hapo senta ulikuwa ukifika katikati ya senta na mahali ninapoishi kulikuwa na miti miwili mikubwa mno ya miembe ambayo sikuwahi kuona ikitoa miembe kwa miaka 2 niliyokaa hapo kijijini.Ile miembe ilikuwa pembeni ya ile njia,yaani ile barabara ilikuwa ikipita katikati ya ile miembe miwili mikubwa.

Kwa kuwa siku hiyo ndiyo ilikuwa mara yangu kwanza kupita hapo usiku nilikuwa naona kawaida tu na wala sikuogopa chochote.

Baada ya kufika kwenye banda la mpira ilibidi nisubiri hadi luninga itakapowashwa,ulipofika muda jenereta liliwashwa na tukaingia ndani kwa ajili ya kutazama mpira,kama nilivyosema mechi ilikuwa kati ya Arsenal na chelsea na ilikuwa ligi ya mabingwa hiyo ilikuwa mwaka 2004. Arsenal tulipigwa Goli 2-1 tukiwa kwenye uwanja wetu wa nyumbani Highbury,nakumbuka Goli letu lilifungwa na Jose Antonio Reyes huku yale ya Chelsea yalifungwa na Frank lampard na mchezaji mwingine ambaye nishamsahau!

Basi bana baada ya mechi kumalizika hiyo mida ya saa tano usiku kila mmoja akatawanyika kwenda alikotoka na mimi nikashika njia yangu kurudi nilikotoka,Japo ile mechi tulipoteza lakini furaha yangu mimi ilikuwaga kuwaona Arsenal tu hata ifungwe vipi nilikuwa napata amani ya moyo.

Sasa ile njia niliyotokea mimi nilijikuta nipo pekee yangu kwasababu kule nilipokuwa nina kaa ilikuwa ni njia maalumu ya kwenda shule na nyumba za walimu,hivyo hakukuwa na mwana kijiji aliyekuwa akielekea kule,basi nikaanza kutembea kuelekea nyumbani!

Kila nilipopiga hatua ndivyo ukimya ulivyokuwa kuwa ukitawala,kulikuwa na giza la kitakatifu kwa usiku huo,zilikuwa ni sauti za wadudu wale waliao usiku tu ndizo zilisikika.Nilipotembea sana ndipo sasa kwa mbali baada ya kuikaribia ile miembe kama umbali wa mita 500 nikaona ikiwaka moto mkubwa sana. Ilibidi nisimame kwanza nitazame vizuri uenda nilikuwa sijaona vizuri.

Kweli bana!,ilikuwa ni ile miembe ikiwaka moto, sasa nikawa najiuliza ni nani alikuwa amewasha ule moto?,basi nikajipa moyo nikaendelea kupiga hatua nikiamini uenda kulikuwa kuna watu wikuwa wameichoma kwa bahati mbaya,sasa ajabu kadiri nilivyokuwa nikisogea ndipo moto nao unapungua!,kiukweli nilibaki kushangaa sana na wakati huo akili yangu haiwazi mawazo ya kijinga kuhusu wachawi!

Basi baada ya kufikia kabisa ile miembe sikuona moto wala moshi,sasa nilipofika katikati ya ile miembe,nilihisi kama watu wanacheka kwa nguvu mno huku mwili wangu ukisismka sana!,yaani hadi nilihisi vinyweleo vimesimama, nilichofanya niliinama nikakamata ndala nilizokuwa nimevaa nikatoka nduki kama mwendawazimu, sasa baada ya kufika mbele kabisa ilibidi nisimame nipumzike maana nilikuwa nahema kama mbwa mlafi!,Niligeuka tena kuitazama ile miembe kwa mbali nikashangaa kuona tena ikiwaka moto,kiukweli ilibidi niondoke hilo eneo kwa haraka sana.

Namshukuru Mungu nilifika nyumbani usiku huo ikiwa inakaribia saa 7 usiku,nilimgongea yule dogo ambaye kwa wakati huo alikuwa yuko macho bado akiendelea kupiga buku.Baada ya kunifungulia mlango alishangaa nikihema kwa nguvu kama nilikuwa nafukuzwa.

Jamaa "vipi mbona unahema sana"

Mimi " Nilikuwa nakimbia niwahi kufika"

Jamaa " Mpira umeisha?"

Mimi " Umeisha ila tumepigwa"

Sasa baada ya maswali na majibu kadhaa hapo ndani ikabidi nimuulize yule jamaa maswali kadhaa!.

Mimi " Hivi ulishawahi kutembea usiku huku"

Jamaa "Hapana,mwisho wangu ni saa 12 tu inapaswa niwe ndani,siunamjua tena ticha alivyo mkora!"

Mimi " wakati narudi nimepita pale kwenye miembe nimekuta inawakata moto"

Jamaa "Ile miembe ya kule chini?"

Mimi " Eenh ile ya pale chini"

Jamaa " Ina maana imechomwa moto?"

Mimi " Hapana,yaani wakati naikaribia ilikuwa inawaka moto,ila baada ya kuifikia nikakuta hakuna moto wowote na nikasikia pipo zinacheka kishenzi"

Baada ya kumsimulia jamaa akaanza kucheka sana huku akiniambia "Kijana naona unachezea kifo"

Jamaa" Ile njia haifai hata kidogo sema tu nilishindwa kukwambia,siku nyingine ukiwa unaenda mpirani uwe unapitia ile njia ya kule lamboni"

Sasa jamaa njia aliyoniambia ni njia ndefu mno ya kuzunguka,lakini ile ya kwenye miembe ni fupi.

Jamaa " Hapa mbona sisi tumepata taabu sana,usione sasa hivi kumetulia ukadhani tulikuwa salama"

Mimi " Kumetulia kivipi?"

Jamaa " Kuna siku nimerudi kutoka shule kuja kupika nikakuta mavi ya mtu kwenye dumu la unga"

Jamaa akaendelea " Tumefanyiwa vituko mno hadi ikabidi Ticha akaitisha kikao cha wazazi na wana kijiji na akatishia kuondoka huku ndipo angalau mambo yakapungua,huku ni hatari sana kijana kuwa muangalifu utapotea"

Baada ya jamaa kunipa maelezo hayo kidogo niliogopa sana na shida ikawa nitaangalia wapi mpira?




-/-/-/-/-/-/-/-/-/-/-/-/-/-/-/-/-/-





SEHEMU YA - 3


Baada ya kuambiwa yale maneno na yule jamaa kiukweli ilibidi niwe na tahadhari ingawa mpaka wakati huo sikutaka kabisa kuamini mambo ya kishirikina.

Sasa nakumbuka Jumamosi moja kama kawaida niliamka na shughuli za hapo nyumbani zilichukua nafasi ikiwemo kwenda lamboni kuchota maji na kuleta hapo nyumbani.

Headmaster ambaye alikuwa ba'mdogo wangu yeye ijumaa tu alikuwa ameshaondoka kuelekea mjini kuiona familia yake, kama nilivyowaambia ya kwamba, kila ilipofika Ijumaa ya kila wiki alikuwa akiondoka na kurejea jumapili jioni kwa ajili ya mambo ya shule!

Sasa siku hiyo kulikuwa kuna mechi kati ya Arsenal na Blackburn ambayo ilikuwa inachezwa saa 12 jioni, lakini pia kulikuwa na mechi nyingine!,kama kawaida ilipofika saa 11 jioni nilimwambia jamaa tuondoke tukacheki gemu akagoma akadai ataenda kusoma baadae kwao na demu wake! Basi nikachukua zangu tochi au taa ya sola kwa ajili ya kumulika njiani pindi nitakaporudi maana ingekuwa usiku.

Kipindi kile kulikuwa na vile vitaa vya sola ambavyo ulikuwa unaviweka juani vinapata chaji halafu usiku vinamulika kama taa ya umeme, vilikuwa na mwanga sana!,sasa hapo nyumbani vilikuwepo 2,moja alikuwa anaitumia Headmaster chumbani kwake na nyingine alikuwa anaitumia jamaa kule kwenye chumba alichokuwa akilala.

Ile nyumba ilikuwa na chumba na sebule pamoja na stoo,lakini kwa nje pia kulikuwa na chumba kimoja ambacho pembeni yake kulikuwa na jiko ambalo humo humo ilikuwa stoo. Kulikuwa na milango miwili mikubwa, mmoja ulikuwa wa mbele ambao mara zote ulikuwa ukifungwa lakini pia kulikuwa na mlango wa nje ambao ulikuwa umeshikamanishwa na ukuta wa fensi,huu mlango ndiyo ulitumika mara zote kutoka na kuingia!

Sasa wakati naondoka nilimwambia jamaa anipe kile kitaa chake niende nacho halafu yeye angetumia kile cha Headmaster.

Niliondoka zangu kuelekea kucheki boli kama kawaida,ijapokuwa jamaa alinionya kuhusu ile njia sikutaka kabisa kuacha kwasababu ilikuwa fupi kuliko ile aliyokuwa amenielekeza ya kupitia lamboni ambayo ilikuwa ya mzunguko!.Wakati huo mvua ilikuwa imemaliza kunyesha kama siku mbili zilizopita,hivyo bado ardhi ilikuwa na unyevunyevu wa kutosha!

Nilifanikiwa kufika lakini nilikuta tayari mechi imekwisha kuanza. Sasa baada ya kutazama mechi ya Arsenal ambayo tulishinda 2-0,nilitazama na mechi nyingine. Mpaka namaliza kutazama mechi ilikuwa yapata saa 3 usiku,nikaamua sasa ni wakati wa kurudi nyumbani.

Kabla sijaondoka niliwaza nipite njia ipi kati ya zile mbili,lakini nilifikiria ile njia ya lamboni ilivyo ya mzunguko ingenichukua muda mrefu kufika,nikaona nirudi na ileile niliyoizoea,nikajifariji kwa kuwa nilikuwa na taa ya sola hivyo kisingeharibika kitu!

Basi bana nikaanza mdogo mdogo kupiga kwato huku nikimulika mulika kwa madaha njia nzima,nina tochi tena!,utaniambia nini!.Sasa kadri nilivyokuwa nikisogea ndivyo utulivu na ukimya ulivyo tawala,kama kawaida nikawa nimeikaribia ile miembe miwili ambayo kila nikifika hapo moyo wangu unashituka sana,sasa safari hii sikuona moto wala nini, nikasonga kuikaribia ile miembe,sasa nilipofika katikati ya ile miembe mikubwa nikahisi kuna mtu nyuma yangu na nikageuka ghafla lakini sikuona mtu, nikahisi yalikuwa mawenge tu ya kitete,kiukweli nilikuwa nasisimkwa na nywele sana kila nikifika hilo eneo!.

Sasa ili kujiamini na kutoa uoga,niliamua kunyanyua kile kitaa na kuanza kumulika juu ya ile miembe angalau nione kuna nini ili nipite kwa amanj, nilipomulika sikuona chochote, sasa ile nashusha tochi chini ghafla nikajikuta nimejikwaa kwenye kitu ambacho sikukiona hapo awali, kiukweli nilianguka pale chini na ile taa ikawa imeanguka kwa mbele na kuzimika, ndala moja pia ikawa imechomoka mguuni nikawa nimebakiwa na moja, sasa nikawa najiuliza nini kile ambacho kimefanya nimejikwaa mpaka nimeanguka, niliamka kwenda kuchukua kile kitochi nikawa nakiwasha nimulike kutafuta ndala yangu ili nivae niondoke lakini kinagoma kuwaka,sasa ikabidi nianze kukipiga piga nikadhani uenda kilipata hitilafu!

Nimekipiga piga sana hatimaye kikawa kinawaka na kuzima, kinakaa muda kinawaka halafu kinazima, nikaendelea kukipiga tena sasa kikawaka kama ilivyokuwa mwanzo, ikabidi nianze kumulika kuitafuta ndala yangu itakuwa imehangukia wapi!,sasa ile namulika kwa nyuma nikaona mtu amelala akiwa uchi wa mnyama!,daaah nikashituka sana na nikataka kukimbia lakini nikajikaza na kuanza kuita kwa nguvu "wewe ni nani?" Niliita sana lakini mtu yule alikuwa hasemi wala hatikisiki,nikagundua uenda ndiye aliyefanya nikadondoka ingawa wakati najikwaa nilihisi kitu kama jiwe na maeneo yale hakukuwa na mawe!.

Sasa akili yangu ikadhani uenda yule mtu alikuwa mlevi ambaye alikuwa amekunywa pombe zikamzidi akawa amelala pale chini,nilisahau kutafuta ile ndala akili yangu ikaamia kwa yule jamaa,nilimsogelea na kuanza kumtikisa kwa mguu huku nikisema " wewe....wewe....wewe" lakini hakuamka,nilipomulika vizuri nikagundua ile ilikuwa maiti na hakuwa mlevi kama nilivyodhani.

Hakuna siku ambayo sitakuja kuisahau kama ile siku na ndipo nikaamini kuna wachawi!,sikumbuki nilifikaje nyumbani mpaka wakati huo maana nilipopata kumbukumbu nilijikuta nipo kwenye mlango wa nyumbani nikiwa ninahema balaa! Kibaya zaidi pale nyumbani nilikuta jamaa hayupo na mlango wa kuingia ndani ukiwa umefungwa kwa nje na kofuli,niliamua kukaa chini kwanza ili kutuliza presha nikawa najiuliza kile nilichokiona kilikuwa kweli au uenda nilikuwa naota? Baada ya kutulia kwa dakika kadhaa, kujiangalia chini nilikuwa peku na kile kitochi nacho sina mkononi!.

Sasa nikawa nimekaa pale nje kwa uoga mwingi,kwakuwa jamaa aliniambia angeenda kwao demu wake kusoma nikaondoka kuelekea kwao yule demu wake ili nikachukue funguo nirudi kulala,wakati naenda nilipitia njia ya lamboni lakini sikutaka kabisa kutembea ilibidi nikimbie maana ilikuwa usiku wa saa 4 kuitafuta saa 5, kiukweli nilikuwa nikifika kwenye vichaka nilikuwa napita kwa spidi kali mno kama ngiri!

Nilipofika kwa na yule demu wake jamaa nikaona mbwa wanaanza kubweka kwa sana!,sasa ile boma yao ilikuwa imezungukwa na miti na katikati kulikuwa na zizi kubwa la ng'ombe,nyumba aliyokuwa akilala yule binti na mdogo wake ilikuwa kwa pembeni ambako ilinibidi kufanya kazi ya kuzunguka ili kuwakwepa wale mbwa!

Nilipofika kwa nyuma nilichungulia kwenye upenyo wa kidirisha nikaona kuna mwanga,basi angalau moyo wangu ukatulia nikajua walikuwa wakijisomea.Nilianza kugonga nikimuita jamaa ili asikie aje anipe funguo za nyumba,sasa wakati nagonga na kumuita jamaa yule demu wake aliuliza "we nani?"

Mimi " Mimi Umughaka"

Demu " oooh,ngoja nije"

Basi yule demu akafungua nyumba akaniambia "Zunguka huku mbele".

Kwakuwa alikuwa ametoka nje,sikuwa tena na mashaka kuhusu wale mbwa.

Mimi " Mambo Debo"

Deborah "Poa umughaka"

Deborah "vipi mbona usiku?"

Mimi " Mwambie ema aniletee funguo"

Deborah "Kwani hayupo nyumbani?,na wewe kwani ulikuwa wapi?"

Mimi " Mimi natoka senta kuangalia mpira,wakati naondoka aliniambia angekuja huku kwa ajili ya kujisomea"

Baada ya yale maelezo yule demu akaniambia wala huyo jamaa aliyeitwa emmanuel hakwenda kwake,sasa akaniambia huenda alienda kwa rafiki yake mmoja alikuwa akiitwa maganga.

Mimi "Duuu sijui nitafanyaje na mlango amefunga"

Deborah " Kwani kwao maganga hupafahamu?"

Mimi " mimi napajua hapa kwenu tu Debo,kwao marafiki zake sipajui!"

Debo "Nisubiri nivae nije nikupeleke".

Mimi "Kama ni mbali tusiende ni bora nikarudi ili nisije kupishana nae njiani"

Debo " Yule mimi naijua akili yake,unadhani anarudi muda huu,utakaa nje mpaka uchoke,wewe subiri nije nikupeleke"

Basi baada ya Deborah baada ya kujiandaa alitoka ndani na taa ya chemri tukandoka kuelekea kwa huyo Maganga ambaye ni rafiki yake na jamaa ambapo Deborah aliyekuwa demu wa jamaa alidhani uenda angekuwa hapo!

Tulipofika hapo kwao Maganga tulianza kumgongea,cha ajabu jamaa akatoka akionyesha kabisa alikuwa amelala!.

Maganga " Mambo vipi"

Deborah " Poa,Ema yuko wapi?"

Maganga "Alipita hapa mida fulani akaniambia anaenda kupiga buku kwao Jackson"

Deborah "Jackson yupi?"

Maganga "Jackson Mashida"

Maganga "Kwani kuna nini?"

Deborah "Aah ameondoka na funguo za nyumba,sasa ndugu yake alikuwa anazihitaji!"

Maganga " Nendeni kwao Jack mtamkuta"

Basi tuliondoka tena nikifuatana na binti Jasiri Deborah,ingawa ilikuwa saa 5 ya usiku lakini Deborah hakuonyesha kabisa kujali hilo,nadhani kwakuwa wao walikuwa wamezaliwa vijijini na kukulia huko haikuwa taabu kwao!.

Haikupita muda tukawa tumefika kwa huyo dogo tuliyeelekezwa kwao.
Tulipofika Deborah aligonga mlango na hatimaye mlango ulifunguliwa!.

Jamaa "Oooh Debo mambo"

Debo "Poa,vipi"

Debo " Ema yuko wapi?"

Jamaa akaanza kuita "Oyaa ema,njoo unaitwa huku"

Sasa kile kinyumba kilikuwa na chumba na sebule halafu juu kimeezekwa kwa nyasi,mimi wakati huo nilikuwa nimesimama kwa mbali kidogo,Deborah yeye alikuwa pale mlangoni.
Jamaa haikuchukua muda akawa ametoka nje.

Aliponiona akaanza kusema " Aaah kaka,nilijisahau nikaondoka na funguo,ila ningewahi kurudi"

Sasa anasema angewahi kurudi wakati muda huo ni saa 5 ya usiku!,nilimtazama kwa jazba lakini ilibidi nikaushe,sikutaka kunyesha kuchukizwa!

Sasa kumbe wakati ameenda kuchukua funguo ndani si ikasikika sauti ya binti,nadhani kuna kitu alikuwa akimuiliza na jamaa akimjibu.

Kumbe wakati huyo Jackson yeye akipiga buku hapo sebuleni,ema yeye alikuwa akivinjari na kibinti fulani kule chumbani!.

Aliponiletea funguo ndipo Deborah akaanza kumuuliza " Ema huyo ni nani?"

Jamaa akawa anajifanya kama hajasikia "Unasema?"

Baada ya kukabidhiwa funguo nilikuwa namsubiria Debo tuondoke lakini binti wa watu akaanza kuwaka,akaiweka ile taa chini akasukuma mlango akazama mpaka ndani!,baada ya muda akatoka amemkwida binti fulani ambaye alikuwa yupo na chupi tu!,ngumi na makonde ya kike yakaanza kurindima hapo na matusi juu!.





-/-/-/-/-/-/-/-/-/-/-/-/-/-/-/-/-/-/-




SEHEMU YA - 4.


Ngumi na makonde yaliendelea pale huku matusi mazito mazito yakichukua nafasi,kiukweli yule Deborah alikuwa na nguvu sana,alikaweka chini kale kabinti akawa anakasukumia ngumi za kike zisizo kuwa na idadi,sasa yule Ema yeye alipoingia ndani hakutoka nje,ilibidi mimi na huyo jamaa aliyeitwa Jackson tuingilie kati ule ugomvi kuachanisha!.

Deborah alikuwa amechukia sana huku akimporomoshea matusi yule mshikaji wake Ema ambaye hakutaka kabisa kutoka nje!.

Mimi " Debo nisikilize,hebu achana na haya mambo ya ugomvi tuondoke,ni usiku sana sasa hivi"

Debo " Hapana umughaka wewe nenda mimi niache"

Kiukweli alikuwa amejaa sumu sana kwa wakati huo!.
Baada ya kuona lile timbwili haliwezi kuisha muda huo,nilimvuta yule jamaa ambaye aliitwa Jackson nikamwambia amchukue huyo dada aliyekuwa akipigwa ampeleke kwao vinginevyo mambo yangekuwa makubwa.

Mimi "Jack hebu sikia,wewe mchukue huyo demu umpeleke kwao ili hawa wabaki wawili wazungumze yataisha"

Jackson "Unajua huyu demu jamaa amekuja nae hapa sijui kamtoa wapi mi ndo mara ya kwanza namuona na wala si mwanafunzi wa skuli"

Mimi "Hebu mwambie Ema namuita"

Nilitaka kusovu ile ishu ili isiendelee kutupigia kelele pale nimchukue binti wa watu Deborah turudi tulipotoka.

Jackson "Jamaa anasema wewe sepa"

Mimi " Anasema nisepe,nisepe wapi?,umemwambia namuita?"

Jackson "Nimemwambia lakini kasema wewe ndiye umemleta huyu demu wake kumfanyia fujo"

Baada ya jamaa kuniambia vile nikaona kumbe yule Ema ni mjinga wa hali ya juu,mimi kikichonipeleka pale ni funguo na wala si mambo ya kijinga kama alivyodhani,sasa hakutaka kabisa kutoka nje kuja kuongea na mimi aliamua kukatalia ndani.
Sasa nikamwambia Jack amchukue yule binti amtoe waende pembeni ya nyumba wajifanye amempeleka ili iwe rahisi kwa Deborah kutoka pale,kweli!,baada ya muda kupita Deborah alipunguza hasira na nikamwambia tuondoke akawa amekubali lakini wakati tunaondoka alikuwa akimtukana sana Ema matusi ya nguoni!.

Tuliondoka sasa kuishika njia ya kuelekea nyumbani huku nikiamini baada ya sisi kuondoka Jack na yule demu wangerudi maana nilimwambia ajidai anamsindikiza ili kwa debora iwe rahisi kuondoka!.

Deborah "Huyu mjinga atanitambua mimi ni nani,we ngoja uje uone!"

Mimi "Huyo ni mshikaji wako debo msamehe tu,ameteleza"

Deborah "Wewe umekuja juzi tu,huyu mjinga huijui akili yake,mara kibao tu nishamfumania,kuna siku nimemfuma akiwa na rafiki yangu"

Basi ikabidi nifunge bakuli langu ili niendelee kumsikiliza Debo akifunguka kwa hasira.

Deborah "Ema ni mshenzi sana,wewe hujamjua vizuri!,yaani safari hii labda ahame shule lakini vinginevyo atanijua mimi ni nani!"

Basi pamoja na kumtaka amsamehe Ema lakini ilionekana kama natwanga maji kwenye kinu!,baada ya mwendo mrefu nilimfikisha kwao na mimi ikabidi nielekee nyumbani usiku huo.Kiukweli lilikuwa giza totoro na sikuwa na tochi na nilikuwa peku!.
Nilipofika nyumbani,nilichota maji kwenye pipa nikaingia bafuni kuoga,baada ya kuoga niliingia jikoni kuangalia jamaa kama alikuwa amepika lakini nikakuta chakula kimeisha,inavyoonekana alikuwa amepika chakula kinachomtosha yeye mwenyewe akala akamaliza,sasa sikutaka kumtupia lawama maana siku zote mtembezi hula miguu yake!.Ilibidi kwa usiku ule nilale na njaa.

Asubuhi kulipo pambazuka,niliwahi kuamka mida ya saa 12 nikasema niende kule kwenye ile miembe miwili nikatafute kile kitochi kabla watu hawajaanza kupita ile njia wasije kuokota kile kitaa halafu nisiwe na majibu ya kumpa Ba'mdogo!.

Niliondoka hiyo asubuhi kwa kukimbia mdogo mdogo mpaka lile eneo la tukio,nilipofika pale cha kwanza kabla ya yote nilitazama kama bado ile maiti ipo au la!,kitu cha ajabu ule mwili haukuwepo lile eneo!,nilibaki najiuliza ni nani aliuweka pale hiyo usiku lakini nikakosa majibu,mpaka wakati huo nilikuwa siamini kabisa ishu za uchawi!,sema nilikuwaga naogopa kutokana na kusimuliwa kuhusu lile eneo.
Basi nikaanza kutafuta ile tochi bila mafanikio,nilicho ambulia kupata ni zile ndala zangu tu!.Niliwaza ningemwambia nini mzee atakaporudi maana ni lazima angeiulizia ile tochi!.

Baada ya kuitafuta kwa muda na kuikosa ilibidi niondoke kurejea nyumbani,nilipofika nyumbani cha kwanza ilikuwa ni kuingia jikoni na kukoroga uji maana nilikuwa nina njaa ya kufa mtu!.Mpaka wakati huo yule jamaa alikuwa bado hajarudi nyumbani.
Nilipomaliza kunywa uji nikakusanya nguo zangu na kuelekea lamboni kwa ajili ya kufua!.
Nilimaliza kufua mida ya saa 4 asubuhi,sasa wakati naondoka zangu kurudi nyumbani nikamuona demu mmoja alikuwa anafua nguo upande wa wanawake,kiukweli alikuwa na mtungi wa maana ila sura ilikuwa ya baba yake(mbovu).Sikuweza kumfuata maana kule kulikuwa na akina mama wengine wakifua hivyo nikaogopa kwenda,nikasema kama nikimuona siku nyingine ingebidi niimbe nae ili awe poozeo langu hapo kijijini!.

Basi nilipofika nyumbani nikamkuta mshikaji keshafika,sasa ajabu ni kwamba nilipo mpa hai jamaa akanikaushia.

Mimi "Mbona nakupa hai unauchuna?,nini shida?"

Ema "Achana na mimi wewe jamaa,kwani lazima niitikie?"

Kiukweli yale majibu yaliniskitisha sana na nikajiuliza ni kipi ambacho nilimkosea,kama ni jana usiku mimi nilienda kwa ajili ya kufuata ufunguo,na nilikuwa najitahidi sana kumtetea kwa demu wake lakini jamaa alidhani mimi ndiye chanzo cha yote!.
Basi na mimi sikutaka kujikomba kwake ilibidi nikaushe,nilipanga kumsimulia mkasa niliokutana nao usiku lakini kwasababu hakutaka maongezi na mimi ilibidi nikaushe!.

Ilipofika mida ya jioni mzee alirejea kutoka mjini kama kawaida!.
Usiku huo jamaa alianza kutafuta kile kitaa kwa ajili ya matumizi lakini hakutaka kuniuliza maana alikataa kuongea na mimi,sasa na mimi nikawa namchora tu!,yaani alisahau kabisa kama jana yake tu alikuwa amenipa wakati naenda kutazama mpira!.
Sasa nadhani uzalendo ulimshinda akaniuliza.

Ema " Hivi ile tochi iko wapi mbona siioni?"

Mimi "Umetafuta kila sehemu umeikosa?"

Ema "Haionekani"

Mimi " Sijui sasa itakuwa wapi"

Namshukuru Mungu jamaa hakukumbuka kabisa kama jana yake tu alikuwa amenipa halafu yeye akabaki na ile ya Headmaster.

Sasa kwakuwa jamaa alikuwa amezira,hakutaka kabisa stori na mimi na ulipofika muda wa kulala alichukua godoro lilikuwa limechomekwa juu ya mbao za dari akatandika chini akalala,mimi nikalala kitandani kama kawaida!.

Ile shule ilikuwa na madarasa manne pamoja na ofisi ya mkuu wa shule na ofisi ya walimu wengine,yaani kuanzia form 1 hadi form 4 kulikuwa na darasa moja moja,shule nzima ilikuwa na walimu wanne pekee ukiongeza na Headmaster.
Walimu wawili walikuwa wameajiriwa na serikali na walimu wengine wawili walikuwa wanalipwa na kijiji,sasa walimu wote hao wao walikuwa wanakaa kule senta,hapo shuleni tulikuwa tunakaa sisi maana kulikuwa na nyumba moja tu ya Headmaster.

Sasa nakumbuka baada ya kupita wiki kadhaa ndani ya mwezi huo wa 3 mwaka 2004,siku hiyo mimi baada ya kumaliza kula nikaenda zangu kulala,jamaa yeye akabaki sebuleni akiwa anasoma,sasa ilipofika mida ya saa 5 naye akawa amekuja kulala,kama kawaida yake hakutaka kabisa kulala na mimi pale kitandani akawa anatandika chini analala.

Sasa usiku mkubwa nikashitushwa na kelele zikiwa zinaita "Mamaaaaa.......Mamaaaaaaa........Mamaaaaaaa".

Hizo kelele zikawa zinaita kule madarasani,sasa nikaamka kutazama chini kwenye godoro jamaa sikumuona nikajua uenda atakuwa sebuleni anasoma.
Haukupita muda ba'mdogo nae akawa ameamka na kutoka nje kuja kutuita.

Ba'mdogo "Mnazisikia hizo kelele kama mimi navyosikia?"

Mimi "Ndiyo baba na mimi nimeamka kwasababu ya hizo kelele"

Ba'mdogo "Hebu mwambie Ema anipe hilo panga"

Mimi "Ema hayupo"

Ba'mdogo " Hayupo?,ameenda wapi?"

Mimi "Nimeamka sijamkuta baba"

Ba'mdogo "Ina maana jana hakulala hapa"

Mimi"Alilala baba,sema niliposhituka sijamkuta"

Sasa wakati naendelea kumjibu headmaster zile kelele zikaanza tena

"Mamamaaa.....Mamamaaaaa.....mamamaaaaaa"

Sasa safari hii tulisikia sauti ilikuwa ya Ema na ilisika kile madarasani!,hatukujua ametoka vipi nje maana milango ilikuwa imefungwa na makomeo!




-/-/-/-/-/-/-/-/-/-/-/-/-/-/-/-/-/-/-



SEHEMU YA - 5



Ba'mdogo " Hebu ingia humo stoonj niletee panga"

Basi nikachukua tochi nikaingia stoo nikatoka na panga.

Ba'mdogo " Shika hizi gambuti(Gun boot/Rain boot) uvae"

Ba'mdogo "Hakikisha unakaa nyuma yangu"

Mimi "Sawa baba"

Basi Ba'mdogo akafungua mlango tukatoka nje kuelekea kule kwenye vyumba vya madarasa ambako sauti ilikuwa ikitokea.Mpaka wakati huo hatukuwa na shaka kabisa kwamba ile sauti iliyokuwa ikisikika ilikuwa ni sauti y Ema.

Kiukweli mimi nilibaki kushangaa sana kwasababu sikufahamu jamaa alitokaje nje na milango yote ilikuwa imefungwa kwa ndani,pili,nakimbuka jamaa mara mwisho alipomaliza kusoma aliingia ndani akafunga mlango na kuingia kulala.Nilibaki najiuliza sana maswali yasiyokuwa na majibu.
Basi tukawa tunatembea kwa kunyata kuelekea lile darasa ambalo Ema alikuwa akilia akihitaji msaada!.Ba'mdogo alikuwa ameshika tochi mkono wa kushoto na kulia kukiwa na Panga huku mimi nikiwa nyuma yake.Tulipofika pale kwenye Darasa ambalo kelele zilisikika mara gafla kukawa kimya ajabu.

Ba'mdogo akaanza kuita "Ema.."

Aliendelea kuita "Ema unanisikia?"

Pamoja na kuita lakini kulikuwa ukimya wa ajabu.
Basi baba alivua koti alilokuwa amevaa akaniambia nimshikie.

Kwa ukakamavu akasonga mpaka kwenye mlango wa darasa,alipofika mlangoni akaniambia nimsogelee,wakati huo mimi macho yangu yalikuwa hayatulii kwa hofu,nilikuwa nageuka kila muda kuangalia nyuma isije ikawa kuna mtu nyuma yetu.Nilikuwa najisemea endapo mambo ya kiharibika ningetoka nduki kurudi nyumbani nikamuacha dingi mdogo akipambana.
Basi ba'mdogo akausukuma ule mlango kwa panga,hakuingia ndani bali aliishia pale mlangoni akawa anachungulia kwa tahadhari kubwa.Baada ya kumulika mle ndani ya darasa kwa umakini ndipo tukamuona mtu amening'inizwa kwenye mbao za kenchi kichwa chini miguu juu huku akiwa uchi kama alivyozaliwa.

Ba'mdogo aliendelea kumulika pande zote za lile darasa ili kuona kama kuna watu,sasa wakati huo bado tunachungulia kwa uoga na tahadhari kubwa,basi aliingia ndani akaniambia na mimi niingie.

Alipo mulika kwa makini ni kweli alikuwa Ema na safari hii ni kama alikuwa haelewi chochote,sasa baba akawa anaita " Ema....Emaaa".
Aliita sana lakini mtu aitiki wala hatikisiki,ndipo akaniambia "Hebu nipe hilo koti".Baada ya kumpa koti lake,alisogea mpaka pale katikati ya chumba akaanza kumpiga na lile koti huku akiita "Ema......wewe Ema".

Ghafla jamaa alishituka tena akaanza kupiga kelele kama mwanzo,ndipo tukatoka nduki mle darasani baada ya ule mshituko na zile kelele!.
Baada ya dingi mdogo kutoka nduki ndipo nikasema kumbe hatari haina baba mdogo wala baba mkubwa!.Ukimya ulitawala kwa muda ndipo sasa tulirudi tena pale mlangoni.

Ba'mdogo akaanza kuita tena "Emaa..."

Alipoita kama mara tatu jamaa akazitambu a sauti.

Ba'mdogo "Emaaa".

Ema "Eenh"

Ba'mdogo "Ni mimi mwalimu Wambura"

Baada ya jamaa kusikia ni Headmaster alikuwa akimuita akaanza tena kulia huku akiomba msaada.

Ema "Nisaidie mwalimu naumia"

Ema "Nisaidie nakufaaa....nisaidie nakufaaa"

Ba'mdogo "Sawa nyamaza nimekusikia"

Basi baba mdogo alisogeza dawati akapata balansi akapanda juu ya dawati akazikata kamba zilizokuwa zimemfunga jamaa miguu.Baada ya kukata zile kamba jamaa alianguka mzima mzima chini huku akipelekea na baba kukosa balansi naye akawa ameanguka chini.
Nilisogea mpaka pale kwa Ba'mdogo na kumsaidia kumnyanyua jamaa aliyekuwa yuko hoi bin taabani.

Sasa baada ya kummulika mgongoni alikuwa na alama za kutosha za fimbo ambazo zifanya jamaa kuvimba mgongo.

Ba'mdogo aliniambia tumnyanyue tumpeleke nyumbani,mpaka wakati huo jamaa alikuwa uchi kama alivyozaliwa na hatukujua nguo alizokuwa amevuliwa zilikuwa zimewekwa wapi!.Muda huo ilikuwa yapata saa 8 usiku.

Baada ya kumfikisha nyumbani akiwa hoi,baba aliniambia nitoe lile godoro alilokuwa analalia na kulipeleka pale sebuleni ili akalale kule.Sasa wakati nikiwa nimelitandika lile godoro na kumlaza Ema ambaye alikuwa anaugulia maumivu ya stiki za mgongoni ambazo hatukujua ni nani alikuwa akimuadhibu,mara ghafla tukaanza kusikia mbuzi analia kule jikoni ambako pia ilikuwa stoo.
Mara ya kwanza nilidhani uenda nitakuwa nimesikia vibaya lakini alipolia mara ya pili ndipo Ba'mdogo nae akawa amesikia.

Ba'mdogo "Huyo siyo mbuzi analia"

Mimi "Nami pia nimesikia baba"

Basi wakati tukiwa tunashangaana,yule mbuzi akalia tena.

"Meeeeeee.......meeeeee"

"Huyo mbuzi anayelia ni wa nani?" Lilikuwa ni swali la Ba'mdogo.

Mimi "Mimi sifahamu Baba"

Ba'mdogo "Sasa kama ufahamu ametokea wapi?"

Mimi "mimi hata sijamuona na niliingia kuchukua panga muda si mrefu,lakini baba kungekuwa na mbuzi wakati napika ningemuona"

Baba mdogo alipigwa na butwaa sana!,basi akaniambia "Hebu muangalie huyu".

Basi mimi nikabaki pale sebuleni namuangalia Ema,yeye akatoka kwenda jikoni ambako mbuzi alikuwa akilia.




-/-/-/-/-/-/-/-/-/-/-/-/-/-/-/-/-/-/-




SEHEMU YA - 6.


Haukupita muda ba'mdogo akawa amerudi ndani na kusema amejaribu kutazama kila pembe ya lile jiko hakuona mbuzi.Sasa tukawa tunajiuliza yule mbuzi alikuwa akilia mle ndani ya jiko au alikuwa akililia nje?,mashaka na hofu viliendelea kutawala sana.

"Naona hawa wajinga wanataka tena kurudia mambo yao" Alisema ba'mdogo.

"Hizi dalili siyo nzuri kabisa za kuendelea kuishi hapa,haya mambo yalinitesa sana kipindi fulani ila yalikoma,naona sasa yanaanza kurudi" Aliendelea kusema.

Tulikaa macho kiasi kwamba mpaka kukapambazuka mida ya saa 11 alfajiri.Sasa Ema nae akawa anajigeuza geuza akiugulia maumivu ya kipigo alichokuwa amepokea usiku.Ilipofika mida ya saa 1 asubuhi headmaster alielekea shuleni akisema angewahi kuja ili aelekee kwa mwenyekiti wa kijiji kutoa taarifa uenda ingesaidia kama mwanzo.
Mimi niliendelea na shughuli zangu za kawaida hapo nyumbani,sasa wakati nikiwa nje jamaa akawa ametoka anachechemea akaenda kukaa kwenye jiwe akawa anaota jua!.
Nilimsalimia lakini aliitikia kama vile hataki,sasa nikawa namdodosa ajaribu kunieleza usiku ilikuwaje mpaka kufikia kuning'inizwa kwenye makenji ya darasa,Jamaa alikuwa anasonya tu!,niliendelea kumsihi ajaribu kunieleza lakini akaendelea kukaa kimya!.

Baada ya kuona ana kiburi nilimuacha nikaendelea na mambo yangu.Ilipofika mida ya saa 5 headmaster alirudi pale nyumbani akiwa na wazee wawili ambao sikuwafahamu.
Sasa akaniita akaniambia "Hebu mwambia huyo aje hapa"

Nikatoka nje nikaenda kumuita jamaa aliyekuwa amejianika juani kama kibambala.Baada ya jamaa kuingia ndani ikabidi na mimi sasa nisogee karibu ili nisikie umbeya maana nilivyojaribu kumwambia aligoma kuniambia.

"Dogo mwenye ndo huyu hapa mwenyekiti" alisema ba'mdogo.

Aliendelea "yaani jana hatujalala kabisa"

Mwenyekiti "Eti wewe!,hebu tuambie ni nini kilikupata"

Ema "Mi sijui chochote,nilishituka nikaona nimefungwa juu ya mbao huku nikipigwa"

Mwenyekiti "Waliokuwa wanakupiga uliwaona?"

Ema "Hapana"

Ba'mdogo "Yaani ni hatari mwenyekiti,nadhani nilikueleza haya mambo ya kiendelea mi nitaondoka"

Mwenyekiti "Sasa mwalimu Wambura utaondoka halafu watoto wetu nani atawafundisha!?"

Ba'mdogo "Siwezi kuendelea kukaa hapa wakati unaona kabisa huu ni ushirikina"

Mwenyekiti "Sasa rafiki wakati wanakupiga hawakusema chochote?"

Ema "Mi wakati wananichapa nilikuwa nasikia wanacheka na nilikuwa napigwa na watu wawili,maana alipokuwa ananipiga huyu na mwingine pia ananipiga"

Mwenyekiti "Hebu toa shati nione"

Ema alivua shati alilokuwa amevaa akamgeuzia mgongo yule mwenyekiti.Ema hakuwa na majeraha lakini mgongo ulikuwa umeumuka kama andazi.

Mwenyekiti "Mwalimu hebu tuteremke na huyu kijana senta akapate dawa pale kwa Malimi"

Basi baada ya maongezi yalichokuwa takribani nusu saa waliondoka wote kuelekea huko Senta.Siku hiyo ilikuwa ngumu sana na sikutaka kabisa kuzurura hovyo,ilipofika mida ya saa 10 alasiri nilichukua zangu dumu nikaelekea lamboni kuchota maji ya kuoga.Usiku wa siku hiyo jamaa hakulala kabisa,japo alikuwa akijifanya mbishi lakini ilibidi arudi kitandani kulala maana aliona angeendelea kulala chini yangemkuta kama ya usiku ulokuwa umepita.

Sasa hali ya mambo ikawa shwari kwa siku kadhaa na yale mauzauza hatukuyaona.

Nakumbuka siku moja mida ya saa 11 jioni headmaster akiwa amerudi nyumbani,alinituma niende Senta nikanunue betri za redio,sasa wakati naondoka sikutaka kabisa kupita njia ya ile miembe kwasababu nilianza kuingiwa na hofu,ilinibidi nizungukie njia ya kwenye lambo japo ilikuwa ya mzunguko lakini ilikuwa salama kabisa.Sasa wakati nikiwa napita kando kando mwa lambo nikama nilimuona yule binti aliyekuwa na Ema pale kwa rafiki yake Jackson ule usiku wa varangati la yeye na Deborah.
Wakati namtazama alikuwa anachuma yale majani marefu huwa yanaota kando kando mwa maji yanayotumikaga kutengenezea majanvi.
Sasa wakati navuta taswira huku nikigeuka nyuma kumtazama ili nimpe hai!,ghafla sikumuona,nikashituka ikabidi nisimame nitazame vizuri,kweli hakuwepo.Sasa ile nageuka zangu mbele niendelee na safari ya kuelekea senta nikakutana naye uso kwa uso akiwa amejitwisha yale majani kichwani!,kiukweli niliogopa sana na nikajikuta nimepiga kelele "Mamaaaaaaa".

Ili kuondoa aibu ya kiume,nikajifanya "Umenishitua".

Yule binti akaanza kucheka huku akiniambia "kumbe na wewe shemeji yangu ni muoga hivo eeenh".

Mimi "vipi lakini"

Yeye "freshi"

Mimi "Huonekani"

Yeye "Mi nipo,ndugu yako hajambo?"

Mimi "Yeye mzima"

Yeye "Wapi mbona upo spidi?"

Mimi "Naelekea senta mara moja"

Yeye " sawa shemeji tutaonana,ngoja niwahi nyumbani kupika"

Niliondoka nikiwa namtazama yule binti lakini sikummaliza hata kidogo,nilijiuliza maswali mengi sana ambayo kiukweli sikupata majibu.
Basi nilifika Senta nikachukua nilichokuwa nimekifuata na kurudi zangu nyumbani.

Nilipofika nyumbani baada ya kukabidhi zile betri kwa Headmaster nilirudi kule kwenye chumba chetu,sasa safari hii jamaa akaanza kuongea na mimi kwa furaha sana,sikujua ile furaha alikuwa ameitoa wapi maana kwa siku kadhaa alikuwa ameninunia kama mwanamke.

Ema "Baadae nataka unisindikize kwa debo kaka"

Mimi "Kuna nini?"

Ema "Tulipo onana shule aliniambia niende kwao baadae"

Mimi "Mlishayamaliza?"

Ema "Tuliyaongea yakaisha kaka"

Mimi "Sasa baadae ya saa ngapi?"

Ema "Tusubiri kwanza headmaster akilala tuondoke"

Mimi "Haitakuwa noma?"

Ema "Hapana,huwa akiingia kulala ni mpaka asubuhi"

Mimi "Sawa nitakusindikiza".

Kweli,baada ya kupata msosi wa usiku,tuliingia ndani kwenye chumba chetu na headmaster alifunga mlango wa sebuleni akaingia chumbani kwake.

Sasa ilipofika mida ya saa 3 ikabidi jamaa anaimbie tusepe.Kule kijijini kutembea usiku ilikuwa ni kitu cha kawaida sana,kulikuwa hakuna majambazi wala vibaka,changamoto ya kule ilikuwa hayo mambo ya kishirikina.
Tukiwa njiani tuelekea kwao debo,nikamwambia jamaa nilikutana na demu wake alikuwa anamsalimia.

Mimi "Hivi huwa mnasoma nae?"

Ema "Kale kademu nilionana nako pale mashineni siku moja nikienda kusaga"

Mimi "Ooh sawa,nikajua labda ni kanafunzi"

Ema "Halafu siku ile nilikaambia kaondoke kakawa kanang'ang'ania kulala kaka"

Mimi "Kwahiyo baada sisi kuondoka ulilala nako mpaka asubuhi?"

Ema " Niliamua kulala nako kaka,yaani huwezi amini siku ile Deborah nilikuwa namuona kama mavi pamoja na uzuri wake wote"

Mimi "Inaonekana kalikupa vitu ambavyo debo hajawahi kukupa"

Baada ya kumwambia hivyo jamaa akaanza kucheka sana huku akiniambia "Hamna kaka ni kawaida tu"

Mimi " Huwa anakaa wapi?"

Ema "Anakaa kule Masairo"

Sasa baada ya jamaa kuniambia hiyo sehemu inayoitwa masairo na nikipiga umbali niliomkuta yule binti pale lamboni nilibaki nimechoka,hiyo Masairo aliyoniambia jamaa kutoka tu hapo senta mpaka hapo masairo si chini ya kilometa 7,sasa vuta picha kutoka pale lamboni ambapo ilikuwa jirani na shule mpaka huko masairo,kiukweli ilikua ni mbali mno kikawaida tena kwa mtoto wa kike ndipo nikabaki najiuliza maswali yasiyokuwa na idadi.

Sikutaka kumwambia jamaa kile nilichokuwa nimekiona pale lamboni wakati ule,ilibidi nikaushe ili niendelee kujifanya bwege stori zinoge.



-/-/-/-/-/-/-/-/-/-/-/-/-/-/-/-/-/-/-




SEHEMU YA - 7.


Tulitembea kwa muda kidogo hatimaye tukawa tumefika kwao Deborah,sasa tulipofika mbwa walianza kubweka sana,kwakuwa jamaa alikuwa akifahamika pale,aliwapigia wale mbwa mruzi hatimaye wakawa wanamfuata wakitikisa mikia.

Tulisonga mpaka kwenye kile kinyumba alichokuwa anakaa debora na mdogo wake,sasa kwa muda ule alikuwa debora mwenyewe na yule mdogo wake nadhani alilala nyumba kubwa.Ema alianza kugonga mlango hatimaye binti wa watu alifungua!.

Ema "Ulikuwa umelala?"

Debo "mmh" aliitikia huku akipiga miayo.

Basi nilimwambia Deborah aniletee kiti mie nikae kwa nje kama wao walikuwa na mazungumzo marefu,Debo akanitaka niingie tu ndani!.Basi niliingia ndani hatimaye taa ya chemri ikawashwa,sasa kwakuwa hakukuwa na mazungumzo yeyote ya maana,mimi ilibidi nijiongeze nitoke nje ili jamaa achakate papuchi.

Nilitoka nje nikakaa kwa muda kama saa nzima.Walipotoka ili kupotezea nikajifanya kama najipigisha mruzi wa uongo na kweli ili kupotezea.Nilimuona jamaa ni mshamba sana kwasababu hawezi kunitembeza usiku wote huo kisa tu yeye anakwenda kuchakata papuchi kwa demu wake,nilichukia sana lakini ikabidi nivunge tu.Mimi nilidhani wanakwenda kuzungumza vitu vya maana ambavyo ilinipasa niwepo ili nitoe ushauri kumbe ilikuwa ni uchakataji wa papuchi.

Basi bana hatukumaliza muda debo akawa anatusindikiza,sasa tulipotoka nje ya fensi ya miti ya boma lao ilibidi nimgusie kuhusu yule binti ambaye nilimuona lamboni akiwa anafua.Sasa baada ya kuwa nimempa specifications za namna yule binti alivyo,debo alicheka sana.

Debo "Jamani shem,mwanamke gani yule sasa"

Ema akadakia "Kwani ni nani?"

Debo "Si yule Mwise!"

Ema "Wewe umejuaje ni Mwise?"

Debo "Sasa ni nani Pale shuleni mwenye matako makubwa kama siyo Mwise?"

Basi kwa namna nilivyomuelezea Debora namna yule binti alivyo alikuwa ameshamfahamu kabisa.Sasa mimi kiukweli yule binti nilitokea kumtamani sana kulingana na umbo lake namna lilivyokuwa,kiukweli sura ilikuwa ya baba yake(mbaya) lakini umbo lilikuwa la mama yake(zuri),Kuhusu sura kwangu haikuwa tatizo,mimi nilichotaka ni kuchakata papuchi tu!.

Debo "Shem yule hata hakufai,hata hamuendani!"

Mimi "Shem mbona yupo freshi tu!"

Debo "Yaani ulivyo smati hivyo utembee na yule binti?,hapana kwa kweli"

Debo "Wewe usijali shem mimi nitakupa rafiki yangu,ni mzuri kweli nahisi utampenda"

Basi kiukweli yale maneno ya Debo ni kama yalitaka kunikata stimu lakini moyoni bado tamanio langu ni kuwa na mtoto Mwise matako makubwa maana ndivyo vitu nilivyokuwa nikivipenda kwa miaka hiyo!.Kweli,baada ya yale mazungumzo tuliondoka kurejea nyumbani kama kawaida,hiyo ilikuwa yapata saa 5 usiku.

Sasa kuna siku mwanakijiji mmoja alileta Jogoo mkubwa pale nyumbani,kama nilivyosena hapo awali ya kwamba,pale kwa Headmaster wakati ule kila siku alikuwa analetewa kidumu cha maziwa fresh cha lita tano na kila wikiendi alikuwa akiletewa kuku na wanakijiji tofauti tofauti,hii ilikuwa ni kama bonasi ya Mwalimu mkuu kwasababu ile shule ilikuwa ikifanya vizuri kimasomo.Sasa wikiendi hiyo headmaster hakwenda mjini kama kawaida yake,nilimchinja yule Kuku na hatimaye mchana tukawa tume mla tukabakiza mboga ya usiku.

Baadae mida ya mchana saa 8 ba'mdogo akasema anashuka senta na baadae angerudi na mama mdogo kwasababu walikuwa wanatokea mjini kuja hapo kijijini,hivyo akasema angekaa huko mpaka mida atakayompokea mke wake waje nae.Pale kijijini kulikuwaga na gari aina ya Hiace ambayo ilikuwa ikitoka mjini inalala hapo na kesho yake inaondoka,hivyo kama ulikuwa unakwenda mjini na hiyo gari ikikuacha basi inakubidi uhairishe safari.

Ba'mdogo "Hiyo mboga muiche kwa ajili ya wageni,nyie chambueni dagaa ambazo mtalia ugali usiku"

Mimi "Sawa baba"

Basi bana huo mchana nikaingia zangu kupumzika,Ema yeye alikuwa ameenda madarasani huko kusoma na wanafunzi wenzie.Ilipofika saa kumi na moja nikaanza kutengeneza dagaa kwa ajili ya kitoweo cha usiku.
Ilipofika saa 12 niliwasha jiko ili sasa nipashe yule kuku tuliyemla mchana halafu baada ya hapo nipike wale dagaa.

Nimeenda kuchukua sufuria ile ili niweke kwenye jiko nakuta ni nyepesi mno,kufungua mfuniko na kutazama ndani nakuta mboga hamna,ilikuwa ni mifupa tu inanikodorea macho!,yaani hata mchuzi ulikuwa umelambwa wote!.Nilishituka sana na nikajiuliza hiyo mboga ni nani atakuwa amekula?
Nilitoka nje ili niende pale darasani kumshitua Ema kumuuliza yawezekana yeye ndiye aliyekula ile mboga ili headmaster atakaporudi aweze kujibu.
Sasa wakati nakwenda kule madarasani nikamuona na yeye akiwa anakuja.

Mimi "Ndo mnatoka?"

Ema "eeenh ndo tumemaliza pindi"

Mimi "Yule kuku ulimla wewe?"

Ema "Kuku?,kuku yupi?"

Mimi "Si ile mboga tuliyokula mchana"

Ema "Kwani imekuwaje?"

Mimi "Aiseee twende ukajionee mwenyewe".

Basi tulipofika ndani moja kwa moja jikoni.

Ema "Daaaah sa nani kala?"

Mimi "mimi sijui,nimelala mchana nikaamka ili niipashe ndo kama unavyoona".

Mimi "Na dingi alisema anakuja na mama mdogo,sasa sijui itakuaje maana alisema kuku tuache kwa ajili ya mgeni na sisi tupike dagaa"

Tuliendelea kutazamana pale tusijue cha kufanya.Nilimwambia Ema tutamwambia dingi kilichotokea lakini Ema ni kama alisita sana.

Ema "Wewe headmaster humjui vizuri,usione anakuchekea hapa ukamfanyia utani,niulize mimi"

Mimi "Yule ni baba yangu mdogo na nina mfahamu vema,sasa kama hatujala sisi tufanyeje?

Ema "Yule hawezi kuamini kaka"

Ema "Sikiliza,mimi ngoja nikimbie kwao Debo nimwambie anikamatie kuku tuje kuchinja,vinginevyo itakuwa hatari"

Mimi "Mbona kama muda umeenda sana,na wao nadhani wanaweza kuwahi kurudi"

Ema "Headmaster namjua,hawezi kurudi saa hizi,hapo mpaka ngoma tatu ndo unamuona hapa na mkewe"

Basi jamaa ilibidi aondoke anakimbia kwenda kwa demu wake kufata kuku wakuja ku-replace.Kiukweli ile hali haikuwa ya kawaida kabisa,pamoja na vile vitisho lakini wanaume bado tuliendelea kukomaa!.Ilipofika mida ya saa moja usiku nilikuwa nikismubiri jamaa lakini sikuona,sasa baada ya kupika wale dagaa na jamaa alikuwa haonekani,niliona nikimbie nimfuate,nilisema yawezekana alipofika kwa demu wake uchakataji ukaanza akasahau mambo ya kuku.

Nikafunga mlango nikaondoka zangu,nimetembea sana bila kukutana na jamaa njiani,nilikuwa nimekasirika sana na hakuna siku niliyomuona jamaa ni mpumbavu kama siku hiyo,sasa nimefika kwao Deborah nakuta jamaa amekaa kwenye kiti tena amekunja kabisa nne.

Mimi " Sasa ema umefika tena umekaa?"

Ema " Hapana kaka sijakaa kama unavyodhani,Deborah amesema anampika kabisa ili tukifika sisi ni kusonga ugali tu kaka"

Basi ikabidi nikae tusubiri huyo kukua aive,kiukweli nilikuwa nimechukia sana kwa namna jamaa ambavyo alikuwa hachukulii vitu serious!.
Sasa tumekaa pale mpaka mida ya saa tatu usiku ndipo kuku akawa ameiva,nilikuwa nawaza tukimkuta dingi kafika tutamueleza tulikuwa wapi!.

Baada ya Deborah kutukabidhi yule kuku kwenye hotpot tukaanza mwendo wa kutembea haraka kuwahi nyumbani,sasa cha ajabu tulitembea sana lakini tukawa hatufiki,Aisee kiukweli wasukuma nawanyooshea mikono.

Yaani fikiria tunatembea lakini kila tukiangalia hatufiki,sasa nikamwambia jamaa "hebu tusimame kwanza".

Mimi "Isije kuwa hii njia tumeichanganya Ema".

Ema " Kaka njia ndiyo hii".

Mimi "Mbona sasa tumetumia muda mrefu sana?"

Jamaa akaniambia "twende nzetu tutafika kaka,najua una kimuhe muhe cha dingi yako".

Jamaa alikuwa anafanya masihara lakini kiukweli tulipiga sana makitaimu.

Sasa wakati tunatembea hatuna hili wala lile,tukasikia sauti nyuma yetu ikiita "Emaaa mpenziiii".

Aiseee sitakuja kuisahau ile siku,kila mtu alipita chocho lake na tulikutana nyumbani asubuhi.




-/-/-/-/-/-/-/-/-/-/-/-/-/-/-/-/-/-/-




SEHEMU YA - 8.


Niliruka nikaingia kwenye shamba la mahindi ambayo bado yalikuwa madogo kiukweli nilikimbia sana na sikufahamu nilikuwa naelekea wapi!.Nilifika sehemu ambapo kulikuwa na kimlima ikabidi nisimame nishike magoti huku nikiwa nahema kama mbwa!.Sasa akili iliporudi nikaanza kujiuliza hivi nilichokuwa nina kimbia ni nini?,kwanini nikimbie kama labda nimeua mtu?,lakini pia aliyefanya na mimi kukimbia alikuwa Ema baada ya kushituka akaanza kukimbia ndipo na mimi kuitafuta njia yangu!.
Basi nikaanza kuteremka kurudi nilikotoka,nilitembea kwenye yale mashamba usiku ule bahati nzuri hakukuwa na giza kubwa ambalo lingezuia mimi kutazama vizuri!,nilijaribu kuitafuta njia ya kuelekea nyumbani lakini sikuweza kuifahamu maana nilikuwa nimekimbia umbali mrefu!.Sasa wakati natembea ili kulitafuta barabara kuu ambalo pengine lingenipa muongozo wa kuelekea nyumbani,mara ghafla nikasikia watu zaidi ya mmoja wakiwa wanakuja wanazungumza,ikabidi nilale chini ili wasinione maana ilikuwa usiku pengine kuhisi mimi ni mwizi!.Wale watu walipita walikuwa wakizungunza mambo yao tu kwa lugha ya kisukuma,nilipoona wamefika mbele na mimi sasa nikaanza kuwafuata kwa nyuma nikisi uenda ile njia ingenirudisha mpaka mahali ambapo nilikuwa napatambua ili iwe rahisi kufika nyumbani.

Sasa niliendelea kutembea lakini nikawa naona kabisa naelekea kwenye mazingira ambayo sikuwahi kufika,ikabidi nisimame huku hofu ikitanda,kumbuka mida hiyo ilikuwa yapata saa 4 kuelekea saa 5 usiku.Ikabidi nirudi tena na ile njia,nimetembea sana na hofu ilipokuwa ikizidi nikaanza kukimbia huku napiga mruzi wa uoga ili kujipa matumaini hata kama kuna kitu kibaya basi kiogope.

Ile njia ilinipeleka mpaka kwenye uwanja mmoja ambao ulikuwa ukifanyika mnada kila tarehe 15 ya kila mwezi,nilipofika hapo niliweza sasa angalau kupata picha uelekeo wa nyumbani.Sasa nikatembea ili niende kukamata njia ya uelekeo wa kule lamboni ambako kungenipeleka moja kwa moja hadi nyumbani.
Sasa wakati natembea nikasikia sauti ya kike ikiimba nyimbo kwa lugha ya kisukuma,nilipogeuka kwa mbali kidogo nikaona huyo mtu akawa anakuja uelekeo niliokuwa nikielekea mimi,sikuwa na hofu nilijua ni mpita njia kama mimi.Sasa wakati natembea na yule mtu naye anakuja kwa kasi,alipofika karibu yangu ndipo kumtazama vizuri alikuwa yule binti demu ya Ema,akajifanya kama hajaniona!.

Sasa moyoni nikawa najiuliza,kwanini kila mara mimi hukutana huyu binti?,na mazingira ninayokutana nae siyo mazingira rafiki hata kidogo.
Akanipita na kiukweli sifahamu kama hakuniona au aliniona ila akaamua kuuchuna!.

Mimi "Shem!" Niliita kwa nguvu.

Akasimama akageuka.

Binti "Aah shem,kumbe ni wewe"

Mimi "Unaenda wapi usiku wote huu?".

Binti "We acha tu,mama aliniagiza mahali ndiyo narudi"

Mimi "unawezaje kutembea usiku hivi tena uogopi?"

Binti "Nikuulize wewe maana sisi huku vijijini tulishazoea"

Kale kabinti siyo kwamba kalikuwa kabaya sana,La hasha!,kiukweli kama huna hili wala lile kalifaa kuzugia kwa hapo bushi.

Binti "Mbona upo mwenyewe,mwenzio yuko wapi?"

Mimi "Yuko nyumbani"

Binti "Na huku unatoka wapi?"

Mimi "Kuna mgeni natoka kumsindikiza ndo narudi nyumbani"

Baada ya kukadanganya hivyo mara ghafla kakaanza kucheka sana na kile kicheko hakika kilikuwa cha dharau,na kiukweli sikuelewa maana yake nini.

Binti "mmmh sawa bana utamsalimia mwenzio"

Mimi "Mbona lakini unacheka?"

Binti "Nacheka kwasababu nakuhurumia wewe mwenyewe unawezaje kutembea usiku huu hapa kijijini tena ukiwa mgeni!"

Sasa baada ya kusema maneno yale mara ghafla tamaa ya ngono ikanijia usiku ule na kichwani nikawaza kwakuwa tulikuwa wawili tu yale maeneo ndipo ilikuwa nafasi ya kukadanganya ili kanipatie papuchi nipunguze ugwadu wa muda mrefu.

Mimi "lakini unajua mwenzio huwaga Nakupenda"

Binti "Jamani wewe sini shemeji yangu lakini!"

Mimi "Sawa!,lakini kwani nani atajua!?"

Binti "utaniweza lakini?"

Mimi "nitakuweza,wewe nipe tu japo kidogo hakuna atakayejua"

Yule binti tena akaanza kucheka vilevile kwa dharau ya hali ya juu na sikuelewa lile cheko kwa wakati ule lakini kwa baadae nilikuja kufahamu ni kwanini alikuwa akicheka vile.
Basi nikakasogelea nikaanza kukashika pale huku mimi wakati huo abdala kichwa wazi ametuna kama kijiti!.

Binti "Kwanini tusiende nyumbani kwetu"

Mimi " kwenu ni mbali,wewe tufanye tu hapa kidogo halafu kila mtu aondoke kwao"

Binti "Aliyekwambia kwetu mbali ni nani?"

Mimi "Kwenu sini kule masairo?"

Binti "Jamani,sasa hapo Masairo kwani ni mbali?".

Sasa wakati yeye anasema si mbali,kumbuka pale tulipokuwa nikipiga umbali wa kutoka hapo mpaka kwao,si chini ya kilometa 4 lakini binti anakwambia si mbali.Basi kwakuwa nilikuwa nina hamu ya kuchakata papuchi ikabidi niwe bwege nimkubalie binti tuelekee kwao.
Basi tulitembea na jambo la kushangaza safari tulitembea kidogo tukawa tumefika hapo kwao,nilibaki najiuliza maswali kibao kichwani lakini sikuwa na majibu.

Nikawa najiuliza,kwanini leo hapo Kjijini Masairo pamekuwa karibu kiasi hicho?,au kwasababu nilikuwa nina ugwadu kiasi kwamba sikuona ni mbali?,sasa akili yangu ni kwamba nifike nichakate papuchi na ikiwezekana niondoke nirudi nyumbani hata kama ikiwa ni usiku wa manane,cha msingi nisilale nje tu!.
Sasa tulipofika hapo kwao na binti mara moja akawa amenipeleka kwenye kinyumba cha nyasi ambacho ndani kulikuwa na giza ila chini kulikuwa na godoro limetandikwa.

Binti "Kaa humu unisubiri niende kwa mama kwanza"

Sasa pale nje kulikuwa na moto ambao ulikuwa una fifia fifia ikionyesha yawezekana kulikuwa na watu wakiota muda si mrefu!.
Sikutakaa kabisa kukaa na nikawa tayari kutoka nduki endapo ningehisi hatari,nikasogea kwenye mlango nikawa nachungulia!.
Yule binti akaelekea mpaka kwenye nyumba iliyokuwa imeezekwa kwa nyasi lakini ilikuwa kubwa kiasi,kwa muonekano ni kama ilikuwa chumba na sebule.Alipofika akaanza kugonga mlango huku akiongea kwa lugha ya kisukuma.

Basi alifungua mlango mwanamke mmoja ambaye bila shaka alikuwa mama yake kwa mujibu wa maelekezo yake!.Wakaanza kuongea kwa kisukuma ambapo sikujua walikuwa wanaongea nini!.Ghafla baada ya maongezi ya yale maongezi yule mama akawa anakuja kule kwenye kile kinyumba nilichokuwamo,sasa ikabidi nitoke pale mlangoni nikarudi kukaa kwenye godoro chini nione nini kilikuwa kinaendelea.Alipofika akaanza kugonga mlango.

Mimi "Karibu"

Mama "Hujambo Umughaka?"

Ooooh!,nikawaza huyu mama jina langu kalijulia wapi?,hata huyo binti yake tu hakuwahi kulifahamu jina langu zaidi ya kuniita shemeji.Sikutaka kuonyesha nimeshangazwa lakini akili kukichwa zikaanza kuchaji ghafla!.

Mimi "Sijambo mama"

Mama "Mwalimu mkuu yeye mzima?"

Mimi "Yeye mzima kabisa"

Mama "Sawa,karibu mwanangu"

Baada ya ile salamu akaondoka zake kuelekea kwake na binti yake alikuja akafunga mlango,kiukweli nilikuwa nina hamu na papuchi lakini ghafla hamu ikawa inakata.Nilijiuliza maswali mengi mno.

Inawezekanaje huyo mama akalijua jina langu?,au uenda alikuwa akifahamiana na ba'mdogo sasa akamtajia jina langu?,lakini bado nilikataa!,inawezekanaje mama ambaye ndiyo ameniona mara moja tu akanichangamkia kiasi kile?,Je ni ulikuwa ni utaratibu wa kabila la kisukuma kuruhusu mabinti zao kuchakatwa ovyo bila mama kuonyesha kuchukizwa?.Mimi nilidhani uenda binti angegombezwa na mama yake mimi kwenda pale lakini mama ndiye alionekana kufurahia ugeni wangu!.

Basi sikuwa na hiyana ikabidi uchakataji wa papuchi uchukue nafasi kwa usiku ule,sasa kuna wakati tukiwa tunavuta pumzi baada ya mizagamuano ya muda mrefu,binti akawa anaanzisha stori ambazo zilikuwa zinazidi kunichanganya!.

Binti "Unajua mama yangu anakupendaga sana wewe".

Daaah!,kiukweli ile sentensi ya anakupendaga sana wewe ndiyo ikazidi kunichanganya.

Mimi "Kwani mama yako amewahi kuniona wapi?"

Binti "wewe unajiona hapa kijijini kama mgeni wakati unafahamika sana tu"

Binti "wewe si kuna siku ulimsaidia mama kubeba kuni kuleta nyumbani,au umesahau"

Mimi "Hapana,siyo mimi labda mama yako atakuwa amenifananisha"

Binti "Mama yangu huwa asahau"

Sasa nikawa navuta picha ni lini nimemsaidia huyo mama kubeba kuni lakini nikawa sikumbuki kabisa,lakini binti akawa anakomaa kwamba ni mimi.

Lakini kuna muda nikasema huenda ikawa kweli,lakini ni siku ipi?,mbona mimi siikumbuki hiyo siku?,na jina langu huyo mama alilijuaje?,Kiukweli maswali hayakuisha ila kwakuwa papuchi ndilo kusudio la mimi kwenda pale,nikasema liwalo na liwe!.




-/-/-/-/-/-/-/-/-/-/-/-/-/-/-/-/-/-




SEHEMU YA - 9.


Basi mizagamuano ilipamba moto kiukweli hadi nikasahau kurejea nyumbani nikajikuta nimepitiwa na usingizi.Nimekuja kushituka ni saa 1 asubuhi sikumuona yule binti kwenye godoro.Nikakurupuka kuamka nikavaa zangu nguo na kutoka nje.

Sasa ile nimetoka nje na endelea kushangaa shangaa kumuangalia yule binti, nikamuona akiwa anakuja amejitwisha ndoo ya maji kichwani.Alipofika nikamsaidia kumtua.

Binti "Mbona mapema?"

Mimi "mapema tena!,mimi naondoka!"

Binti "Subiri basi nimebandika michembe ule ndiyo uende"

Basi kwakuwa nilikuwa nina njaa sikula tangia nilipokula kule nyumbani mchana wa ile siku tuliyokula kuku,sikuwa na namna ikabidi nisubiri michembe iive nipakuliwe nile,kiukweli nilikuwa nina njaa sana!.Aliingia ndani akawa amenitolea kiti nimekaa zangu pale nje huku nikiendelea kuyaangalia mazingira ya pale kwao.

Kiukweli pale kwao miji ya majarani ilikuwa mbali sana na kilichokuwa kimezunguka nyumba ni mashamba ya mahindi na mihogo.

Mimi "Mama yuko wapi?"

Binti "Ameenda shambani"

Basi baada ya kuniambia mama yake amekwenda shambani nilikaa kwa kujiachia nikapata amani sasa.Sikuona mtu mwingine pale kwao tofauti na yule binti pamoja na mama yake,sasa sikuweza kufahamu kwa haraka haraka wanaishi wao wawili tu au kuna watu wengine,sikutaka kabisa kupeleleza peleleza.
Ile michembe ilipoiva alinipakulia pamoja na uji uliokuwa umejazwa maziwa ya kutosha,ingawa uji haukuwa na sukari lakini ulikuwa mtamu.

Alitandika jamvi chini akaweka chakula kile tukaanza kula.Sasa wakati tunakula kiukweli nilikuwa nikimtazama yule binti na mambo aliyonipa usiku vilikuwa haviendani, binti alikuwa wa umri mdogo tu kama miaka 17 lakini alikuwa na mambo yaliyowazidi wakubwa wengi tu!.,Japo hakuwa mnene lakini alikuwa na umbo la wastani,kiukweli sura ilimbeba sana.

Mimi kwa wakati huo nilichojua ni kupunguza tu ugwadu,hizo habari nyingine za sijui matako makubwa mimi kwa wakati huo sikutaka kuzisikia,cha msingi nilikuwa nimepunguza ugwadu basi mambo mengine yangefahamika mbele kwa mbele.Sasa wakati tunakula akawa ananiambia.

Binti "Usije kabisa ukamwambia Ema"

Mimi "Hapana siwezi kusema chochote,mimi siyo mjinga"

Binti "Unajua Ema aliniambia atanioa"

Mimi "Kweli eeeh".

Binti "Kweli kabisa"

Mimi "Kama ndivyo atakuoa wala usijali".

Sasa kwa akili ya yule ndugu yangu hayo maneno ya kumuoa binti wa watu nilijua kabisa ni uongo na asingeweza kumuoa zaidi ya kumpotezea muda tu!.

Binti "Unajua yule Deborah ningemfanya kitu kibaya sana,sema tu mama yake anafahamiana na mama na ni marafiki tangu zamani,lakini isingekuwa hivyo angenitambua!"

Sasa nilikuwa naangalia binti aliyekuwa anasema angemfanya Deborah kitu kibaya nabaki namshangaa tu kwasababu ukiwapima yeye na Deborah hata hawaendani kimuonekano na kimabavu,Deborah alikuwa na nguvu kumshinda!.

Basi baada ya kula nikashiba ikabidi nimwambie anionyeshe njia ya kuelekea senta ili mimi niende zangu nyumbani.

Alinisindikiza huku akiendelea kunisisitiza nisije kumwambia mpenzi wake jambo tulilokuwa tumefanya.Mimi nikamhakikishia sitoweza kumwambia.

Nilitembea zangu kuitafuta senta ili niwahi nyumbani.Nilifika nyumbani mida ya saa 4 asubuhi moja kwa moja nikaingia ndani kupitia mlango wa uani!.Sikutaka kupoteza muda nikaingia jikoni nikachukua dumu la maji ili nielekee lamboni kuchota maji nije kuoga.
Sasa nadhani wakati nafungua mlango maza mdogo akawa amesikia hivyo akatoka kuja kuangalia ni nani aliyekuwa akifungua mlango.

Mimi "Oooh mama,shikamoo!"

Maza "Marhaba,vipi?"

Mimi "poa,za mjini?"

Maza "Nzuri"

Maza "Sijakuona,ulikuwa umelala nini?"

Mimi "Hapana kuna mahali nilienda mara moja ndo narudi"

Maza "Aaah sawa,kuna uji humo kwenye chupa utakunywa"

Mimi "Sawa mama".

Baada ya salamu na mazungumzo alirudi ndani.Sasa wakati nashuka zangu lamboni nikawa najiuliza jana ilikuwaje?,Je yeye na headmaster walielewa jambo hivyo kaamua kuuchuna au hakuna walichoelewa?,sikutaka mambo yawe mengi,niliamini jamaa angekuwa shule na angetoka ningemuuliza ishu za jana zilienda vipi.

Basi baada ya kuoga nikachukua ule uji nikapiga vikombe viwili,japo nilikuwa nimeshiba lakini nikanywa tu kwa kujilazimisha!.Niliingia kulala na nilishitushwa na jamaa akinishika miguu akiniamsha kwa kunitingisha!.

Nilipoamka baada ya jamaa kuniona tukajikuta tunaanza kucheka!.

Ema "Mwanangu jana ulipotelea wapi?"

Mimi "Wewe acha tu!,sinilikimbia nikajikuta hata njia ya kurudi home nimeisahau!".

Ema "Sasa ulilala wapi?

Mimi " Kuna mahali nilifika nikakuta jamaa wamekoka moto ikabidi nijumuike nao"

Sasa nilimdanganya ili maswali yasiwe mengi,ingawaje na yeye alishindwa kuelewa ya kwamba ule niliyomwambia ulikuaa uongo kabisa kwasababu kwa miezi ile ilikuwa miezi ya palizi na mvua zilikuwa zikinyesha.Jamaa yeye alikuwa akicheka tu bila mpango.

Mimi "Wewe ulilala home?"

Ema "mwanangu mimi nilikimbia na lile hotpot japo nilifika nyumbani nimeloana na michuzi lakini sikujali"

Mimi "Ulikuta dingi ameshafika?"

Ema "Alikuwa bado hajaja,mimi nilikwambia huyu namfahamu vizuri,tena akiwa na mke wake ndiyo kabisaa!"

Ema "Walikuja wakagonga nikaamka kuwafungulia,hata chakula chenyewe hawakula".

Baada ya jamaa kunieleza vile angalau sasa moyo wangu ukatulia.

Ema "Lakini ile sauti nilisikia ilikuwa kama ya Monica!"

Mimi "Monica!,Monica yupi tena?"

Ema "Si kile kidemu changu cha kule Masairo!"

Mimi "oooh sawa"

Mimi "Sasa kama ilikuaa sauti ya demu wako mbona tulikimbia?"

Ema "Mi nilishituka tu nikajikuta nakimbia"

Mimi "Lakini una uhakika alikuwa Monica?"

Ema "Kaka ile sauti niya kwake kabisa,na siunakumbuka aliniita Mpenzi?"

Mimi "Sasa alikuwa anatoka wapi muda ule?"

Ema "Yawezekana alikuwa akitufuatilia,unajua kale nako ni kajanja kajanja sana"

Basi nilianza kuvuta picha na kuunganisha,sasa nikawa najiuliza yule binti ni binti wa namna gani?,Kama mpaka muda ule wa saa 3 usiku hakuwa kwao nilibaki nashangaa,ukiacha hivyo ule muda niliyokutana nae kule kwenye uwanja wa mnadani ilikuwa usiku mnene lakini hata hawazi,niliendelea sana kupata mashaka kuhusu binti Monica.

Basi kuna siku headmaster akawa ametuambia isije ikatokea kufika saa 12 jioni mtu akakosa hapo nyumbani,alisema yaani ikifika saa 12 na ukawa hujarudi nyumbani basi utafute pa kwenda!.Kwa upande wangu nilijisikia vibaya kwasababu sasa zile mechi za Arsenal zilizokuwa zikichezwa usiku ningekuwa nazikosa!,kiukweli niliumia sana.

Sasa siku moja nakumbuka Maza mdogo akawa amenituma mafuta ya kupaka kule senta ambayo ni losheni,sasa akawa ameniandikia jina la ile losheni akanipatia na hela nikaondoka zangu!.,Sasa nilipofika nikakuta yale mafuta yapo ya aina 2,muuzaji akawa ameniuliza ni yapi kati ya hayo ninahitaji?,ikabidi nimuulize ambayo kina mama wanapendelea sana kati ya hayo mawili ni yapi?,yule mama akasema kina mama wengi wanapendelea yaliyokuwa na harufu ya cocoa,basi nikamwambia anipatie hayo hayo yenye harufu ya cocoa!.
Niliporudi nyumbani Maza akawaka sana,kwamba ni mafuta gani yale nimemletea,nikajaribu kumwambia kwamba niliyakuta yapo ya aina mbili na yeye hakuniambia nichukue yapi niache yapi.

Maza "Chukua ya kopo la maziwa bhana"

Maza "Ushakuwa mtu mzima hebu uwe unajiongeza"

Kiukweli nilikasirika sana na kwakuwa alikuwa Maza mdogo ikabidi niuchune,kiukweli sema alijikuta tu amekuwa Maza mdogo basi heshima ilibidi ichukue mkondo wake lakini kwa upande wa umri hakuwa mkubwa wala nini!.

Maza "Hebu rudi ukanichukulie yale mengine".

Basi ikabidi niwe mpole nirudishe tena midenge yangu kule senta,yeye alikuwa afahamu kwamba senta palikuwa mbali,kwenda na kurudi si chini ya kilometa 6,sasa nilipoenda mara mbili maana yake nikajikuta natembea zaidi ya kilometa 12.Nilichukia sana lakini sasa ningefanyaje?,ilibdi nienda nikayafuate tu!.

Sasa wakati narudi ilikuwa mida ya 10 jioni.Nikamgongea mlango nikampa mafuta yake lakini nikiwa nimechukia sana!.

Maza "Siku nyingine nikiwa nakuagiza uwe unaniletea haya siyo yale uliyorudisha"

Mimi "Sawa mama haina shida"

Basi yeye kwa akili yake alidhani mpaka hayo mafuta yaishe mimi ningeendelea kuwa hapo,kwa maisha aliyoanza kuyaonyesha kwa siku chache hizo tu,yalionyesha tungekuja kukwazana sana.

Sasa nikaingia zangu kupumzika kitandani kwasababu nilikuwa nimechoka halafu jua lilikuwa kali.Nikiwa nimejiegesha kuutafuta usingizi kwa mbali,mara ghafla nikasikia sauti ya Maza mdogo akipika kelele!.

Sasa ile nafungua mlango nakuta anakomaa kufungua mlango wa bafuni yeye akiwa kwa ndani,ndipo nikasogea kwenda kumsaidia,sasa ile nimefika mlangoni nataka kuusukuma maana alikuwa akiomba msaada na mimi nikadhani uenda aliingiliwa na nyoka bafuni lakini kumbe yeye alikuwa naya kwake.

Maza "Yaani umughaka kabisa umekuja kunishika matako mimi!"

Maza akaendelea "Wewe niwa kunishika matako mimi nakuuliza?"

Nilibaki nimepigwa na butwa nikawa hata kuongea siwezi nabaki kujing'ata ng'ata tu kwa mshangao.

Mimi "Mimi mbona nilikuwa nimelala!"

Maza "Wewe ngoja baba yako arudi"

Mimi "Mama mimi nimekuja kukusaidia baada ya kusikia kelele"

Maza "Peleka huko utahira wako mbwa wewe"

Maza "Yaani wewe ni wakuja kunishika mimi matako?"

Basi baada ya kusema maneno yale kwa ukali akawa ameingia ndani.Sasa nikabaki najiuliza maswali yasiyokuwa na majibu,Je ni kweli ameshikwa matako?,na kama ameshikwa matako ni nani kamshika?,ina maana hakuona kama mlango alikuwa amelock kwa ndani na mimi ningengiaje bafuni?,Au uenda ni style tu za kunifukuza pale ki-aina?.

Uenda aliona kama tunammalizia mumewe chakula au yale maziwa aliyokuwa akiletewa kila siku!.Kiukweli moyo wangu uliuma sana.

Kumbuka mpaka mida hiyo nipo tu mimi na yeye hapo nyumbani,Ema na Headmaster wako shuleni,swali nililokuwa nalo kichwani ni nani ataniamini?



-/-/-/-/-/-/-/-/-/-/-/-/-/-/-/-/-/-/-





SEHEMU YA - 11


Safari mpya ya maisha ilianza rasmi pale nyumbani baada ya Maza mdogo kuja,kabla hajaja kutoka mjini tuliishi kwa kujiachia kama vile tupo mamtoni na tulikula na kunywa tutakavyo,lakini sasa yale maisha ya mwanzo yakatoweka,kula nyama ya kuku tena ilikuwa muujiza uliohitaji Mungu mwenyewe kuingilia kati!,kuku wale wa wikiendi walikuwa wakisafirishwa kupelekwa mjini na sisi hapo nyumbani kula Kayabo wa chukuchuku bila viungo,ilifikia sehemu ukila mboga iliyoungwa kwa mafuta na nyanya unamshukuru Mungu kwa muujiza wa kipekee!.
Kuku alipopikwa mimi na Ema vyetu ilikuwa ni miguu,shingo na kichwa na tunyama twa kuzugia kama tuwili hivi,nyama nyingine yote iliyobaki ilimuhusu Maza mdogo na mumewe!.

Tabia ile japo haikuwa nzuri lakini mumewe hakuwahi kuikemea,yeye alitulia tuli kana kwamba mkewe alichokuwa akitenda kilikuwa sawa.Sasa tulidhani siku si nyingi angeondoka lakini kumbe tulikuwa tunajidanganya!.Hatukufahamu kumbe kilichomleta hapo kijijini ilikuwa ni kuweka kambi kwa ajili ya biashara ya ushonaji wa nguo!.Pale senta kwa wakati ule hakukuwa na fundi cherehani,sasa nadhani mumewe alimwambia aichangamkie ile fursa iliyokuwa na hela za kutosha kwa kipindi kile hapo kijijini!.

Basi baada ya yule mzee Masumbuko kukataa ile miwa pamoja na mapapai alinikabidhi,nilimuomba anichumie majani ya mgomba ili nifungie ile miwa nipate urahisi kuibeba,yale mapapai aliniwekea kwenye kigunia cha chumvi chumvi(salfeti).Sasa nikanyanyua mzigo wa miwa nikajitwisha kisha nikamwambia yale mapapai aniwekee juu ya mzigo wa miwa ili nitandike kwato kuitafuta senta.

Ule mzigo haukuwa wa kitoto hata kidogo,lakini sikuwa na wakumdekea!,niliogopa endapo nikiutua ili nipumzike ni nani tena angenitwisha?,hivyo nilikomaa nao hivyo hivyo.Ingawaje Senta palikuwa mbali sikutaka kabisa kupumzika njiani,kuna muda nilikuwa nahisi shingo inauma lakini nilijikaza kisabauni kama mtoto wa kiume niliyetokea jamii ya Kikurya!.

Baada ya safari ndefu hatimaye nikafika senta.Sasa nilitafuta sehemu ambayo ni nzuri na yenye kivuli ili niweke ile miwa na mapapai nianze kuuza.Basi nilisogea kwenye mti mmoja ambao hakuwa mkubwa sana kisha nikaisimamisha ile miwa kwenye ule mti na yale mapapai nikayotoa kwenye ile salfeti nikayapanga yakawa tayari kwa kuuzwa!.

Nilipata taabu sana kuuza zile bidhaa kwasababu aliyesema nikauze hakuniambia niuzeje au alitaka faida ya kiasi gani!,nilichokuwa nakumbuka ni yeye kuununua ule mzigo kwa bei ya shilingi elfu 3.
Sasa ilibidi mimi mwenyewe nijiongeze kwenye namna ya uuzaji ili utoe hela ya watu na faida ipatikane.Nilianza kuuza ule mzigo hiyo mida ya saa 4 asubuhi lakini hakukuwa na wateja waliojitokeza kununua.Ilipofika mida ya saa 5 asubuhi,alikuja jamaa mmoja akiwa amefunga mzigo kwenye baiskeli na kuweka kambi lile eneo nililokuwepo.

Jamaa "Aisee mambo vipi?"

Mimi "Mambo poa"

Jamaa "Mbona umenivamia kwenye eneo langu?"

Mimi "Eneo lipi?"

Jamaa "Hapo ulipoweka mapapai ni eneo langu ambalo huwa naweka biashara yangu"

Mimi "Sikujua kaka,ngoja niondoe"

Jamaa "Hapana usiondoe,wewe sogeza kidogo kule kushoto ili na mimi nikipate kivuli"

Basi nikaamua kuyasogeza mapapai kushoto ya ule mti ambao nilikuwa nimesimamisha miwa.Yule jamaa alikuwa mstaarabu sana,japo kweli nilikuwa nimevamia eneo lake lakini hakutaka kunifukuza pale,alichoniambia ni kwamba nisogeze ili kila mmoja afaidi kivuli cha ule mti!.
Jamaa alifungua ule mzigo kwenye baiskeli kisha akatandika kavelo(turubai) ndipo akaanza kutoa kwenye boksi viatu aina ya kata mbuga(sendeu).Sasa kumbe jamaa ile ndiyo ilikuwa biashara yake pale siku zote ya uuzaji wa kata mbuga!.

Kiukweli baada ya jamaa kufika sikujiona tena mnyonge kwakuwa nilikuwa na mtu wa kupiga nays stori.

Muda ulipozidi kusonga na wateja wa miwa nao walianza kuja,sasa ishu ikawa ni kisu cha kukatia pingiri za miwa ningekitoa wapi!.Kuna kiduka kimoja ambacho kwa nyuma kulikuwa kuna nyumba,nikajongea mpaka pale nikaomba waniazime panga au kisu kwa ajili ya kukatia miwa halafu ningewarudishia!,yule aliyekuwa akiuza kwenye kile kiduka alikuwa mama mmoja ambaye alimuagiza mwanaye aniletee panga ila akasema nikimaliza nirudishe.

Kiukweli miwa niliuza sana ila mapapi hakuna aliyenunua hata moja.Sasa ilipofika mida ya saa 8 mchana nilikuwa nahisi njaa kishenzi na sikujua ningekula nini kwa wakati huo!,sikuwa na namna zaidi ya kukata pingiri tatu za muwa na kuanza kutafuna ili kupoza njaa!.Ilipofika mida ya saa 10 alasiri nilihesabu hela niliyokuwa nayo mfukoni ilikuwa jumla elfu 2600/=,Hiyo ilikuwa ya miwa pekee,papai hakuna lililonunuliwa mpaka muda huo.

Sasa nikiwa naendelea kuuza zile bidhaa pale,kwa mbali nikamuona Ba'mdogo akiwa anakuja pale senta,sasa kwakua alinicheki akiwa mbali hakupata taabu kunitafuta,hata hivyo ile senta haikuwa kubwa kiasi hicho mpaka nishindwe kuonekana.Alipofika niliona kama ananihurumia lakini hakutaka kuonyesha ile hali alijifanya kuvunga.

Ba'mdogo "biashara inaenda?"

Mimi "Ndiyo baba inaenda ila mapapai hayajanunuliwa"

Ba'mdogo "Ningejua ukaja na miwa tu,watu wa huku si walaji wa mapapai,wanapenda miwa"

Sikutaka kumjibu nikawa nimekaa kimya namtazama.

Ba'mdogo "mpaka sasa umeuza shilingi ngapi?"

Mimi "Nimeuza elfu mbili na mia sita baba".

Ba'mdogo "Sawa nipe hiyo hela"

Basi nikatoa ile hela mfukoni nikampatia akawa ameondoka kuelekea kwenye maduka yaliyokuwa upande wangu wa kulia.Hakukaa sana kule akawa amerejea nilipokuwepo.

Ba'mdogo "Yule mama anamuona?"

Akawa anionyesha kwa kidole uelekeo alipokuwa mwanamke mmoja aliyekuwa amekaa kwenye matofali ya kuchoma.

Mimi "Ndiyo baba namuona"

Ba'mdogo "Ikifika jioni hayo mapapai hujauza,nenda umpelekee yule mama,nimemwambia tayari"

Mimi "sawa"

Baada ya maelekezo yale yeye akawa ameondoka na mimi kubaki pale.

Ilipofika mida ya saa 12 jioni,kweli nilimpelekea yule mama yale mamapai baada ya kudoda kutwa nzima pale chini!.

Miwa nayo ikawa imebaki miwili,sasa nikaona nimuombe yule mama aliyeniazima kisu ile miwa niilaze pale kwake ningekuja kuifuata asubuhi,yule mama hakuwa na tatizo alikubali!.

Sasa nikaanza kuwaza wakati wa kurudi nyumbani nipite njia ipi,je nipite ile ya mzunguko wa lamboni au nipite ileile fupi iliyokuwa katikati ya ile miembe mikubwa!.Wakati huo mfukoni nilikuwa nina shilingi 700.Basi nikaone ni heri nipite ile fupi ili niwahi kufika nyumbani.
Nilimuaga yule jamaa tuliyekuwa tukiuza wote hapo nikamwambia tungeonana kesho yake,jamaa nae akawa ameniambia naye angeondoka muda si mrefu.

Nikaanza kupiga kwato mdogo mdogo kurudi nyumbani.Wakati natembea kiukweli nilikuwa nina mawazo mengi sana,ukizingatia nilikuwa sijala chochote zaidi ya kutafuna vipande kadhaa vya muwa!.Niliona kabisa mambo endapo yangenishinda ningerudi nyumbani!.Wakati huo giza nalo lilikuwa halichezi mbali maana ilikuwa mida ya saa 1 usiku.

Sasa wakati natembea huwaga nina kawaida ya kuangalia chini kama kondoo,huwa naangalia mbele,kushoto na kulia kwa muda mfupi sana lakini muda mwingi huwa natazama chini!,sijajua ni kwanini uenda ndivyo nilivyozaliwa na kurithi kwa mzee wangu!.
Sasa wakati nakwenda sikumuona mtu nyuma yangu wala mbele yangu akiwa anakuja,nilishitukia tu ghafla naitwa jina langu na mzee ambaye nilikuwa napata taabu kumkumbuka.

Mzee "Hujambo Umughaka"

Nikashituka sana!,nikabaki nashangaa ametokea wapi yule mzee mtu mzima!,nikadhani uenda muda ambao nilikuwa natembea huku nikitazama chini sikumuona.

Mimi "Sijambo,shikamoo"

Mzee "Marhaba,vipi mwalimu yupo?"

Mimi "Eenh yupo"

Mzee "sawa utamsalimia"

Mimi "Sawa,nimwambie nani vile!"

Mzee "we mwambie Makono anamsalimia"

Mimi "Sawa"

Yule mzee nilianza kuvuta taswira nimewahi kumuona wapi lakini nikawa sikumbuki vizuri!.Alikuwa mtu mzima mwenye miaka kama 50 -60 hivi!.

Sasa wakati natembea zangu nikawa nageuka nyuma ila cha ajabu yule mzee sikumuona!,nikabaki nashangaa kwasababu lile eneo pembe zoni hakukuwa na njia ya mchepuko,pia kulikuwa na katani za kutosha ambazo kama ungejifanya kuchepuka basi zingekuchoma na ile miba yake mpaka uchanganyikiwe na kile kibarabara kilikuwa kimenyooka moja kwa moja.Tulikuwa tumetoka kuzungumza kwa sekunde kadhaa tu lakini cha ajabu kugeuka nyuma sikumuona tena!,Kuhusu jina langu sikuwaza sana nikawa nasema huenda Ba'mdogo aliwahi kumwambia mimi ni kijana wake na jina langu ni umughaka.

Basi namshukuru Mungu siku hiyo niletembea kwa amani kabisa hakukuwa na viroja wala vituko nilivyokutana navyo pale kwenye miembe.Nilifika nyumbani mida ya saa 2 usiku.Sasa wakati usiku tukiwa tunakula Ba'mdogo akawa ameniambia hela niliyokuwa nayo nihakikishe asubuhi naelekea kwa mzee masumbuko kufata miwa mingine ili nikauze kwa kuwa hiyo ndiyo iliyokuwa kazi yangu.

Tulipokuwa tukiendelea kula nikamwambia Ba'mdogo alikuwa anasalimiwa na yule mzee niliyekutana naye muda si mrefu.

Ba'mdogo "Makono?,makono ndiyo nani?"

Mimi "mimi sijui baba,yeye ameniambia nikwambie hivyo utamfahamu"

Ba'mdogo "Uenda atakuwa mzee mwalukala huyo,yule ndiye huwa anamajina mengi ya utani"

Basi mimi sikutaka makuu,nilipomaliza kula nilielekea zangu kulala kwakuwa nilikuwa nimechoka,Ema yeye alipoingia ndani akaanza kupiga buku kama kawaida.
Sasa picha ya yule mzee ikaanza kunijia vizuri na nikakumbuka ni yule mzee ambaye alikuja na mwenyekiti pale nyumbani siku ile ambayo Ema alikuwa ametoka kukung'utwa viboko darasani na watu wasiofahamika.Yule mwenyekiti wakati anakuja na headmaster pale nyumbani kumohoji Ema alikuwa na huyo mzee,ndipo nikawa nimemkumbuka vizuri.

Basi asubuhi mida ya saa 1,niliwahi kuamka lakini sikumuona Ema,nikasema uenda aliwahi mapema kwenda shuleni wakati mimi nikiwa nimelala.Nilipomaliza kupiga mswaki wakati navaa viatu ili niende nikamsalimie Maza mdogo na mumewe ili niondoke zangu,mara nikaanza kusikia sauti za wanafunzi huko shuleni wakipiga kelele kwa nguvu.




-/-/-/-/-/-/-/-/-/-/-/-/-/-/-/-/-/-/-




SEHEMU YA - 12.


Zile kelele za wanafunzi hazikunishitua sana kwakuwa nilidhani uenda ingekuwa mambo ya kiuanafunzi tu huko shuleni.

Niliingia ndani kumsalimia Ba'mdogo na mkewe halafu mimi niondoke zangu nikachukue miwa ili nielekee kuuza.Sasa nilimsalimia Ba'mdogo lakini hakuwa akijibu,nilidhani uenda angekuwa amewahi shuleni,nilimsalimia pia Maza mdogo lakini nae hakujibu chochote,sasa nikasema Maza mdogo yeye nikimsalimiaga huwa kama kawaida yake anauchuna!.Niliamua kuondoka zangu niwahi kwa mzee Masumbuko.
Sasa nilipotoka nje kukiwa kumeshamiri mapambazuko,niliendelea kusikia wanafunzi wakipiga kelele kwa mshangao huku wengine wakicheka na kuzungumza kisukuma!,kwakuwa njia ile iliyokuwa ikipita lamboni kuelekea kwa mzee Masumbuko ilikuwa ikipita nyuma ya madarasa ya shule!,ikabidi nisimame kuwaangalia na kuwatazama wale wanafunzi kilichokuwa kinawafanya wapige kelele na kuendelea kucheka huku wengine wakiteta kwa lugha ya kisukuma.

Basi kwakuwa walikuwa wanachungulia darasani ikabidi na mimi nisogee kuchungulia kuona walichokuwa wanashangaa,sasa ile nimefika kuchungulia nikamuona Ema na mama mdogo wakiwa wamelala kwenye sakafu wakiwa wamejifunika shuka jeupe,yaani walivyokuwa wamelala ni kama mtu na mkewe.
Nilihamaki na kushangaa sana,ikabidi nizunguke haraka kuingia darasani nione nini kilikuwa kinaendelea!.Sasa mpaka wakati huo hakukua na mwalimu hata mmoja pale shuleni,wanafunzi nao walikuwa wachache huku wengi wakiwa wanaongezeka kuja shuleni.Nilipoingia ndani ya darasa ambapo niliwakuta wanafunzi wengine wakishangaa,sikutaka kuuliza maana ile ilikuwa ni aibu ya karne.

Nilianza kumwamsha Ema kwa kumshitua na kumpiga piga mabega hatimaye akashituka,aliposhituka akaanza kupiga miayo na kujinyoosha kana kwamba ni mtu aliyekuwa na hangover ya pombe,baada ya kushituka na kujitambua alikuta wanafunzi wengi wakicheka na wengine wakiwa wanashangaa;mara ghafla Maza mdogo naye akawa ameshituka ghafla mpaka kupelekea sehemu ya kifua chake kubaki wazi na maziwa kuonekana mbele ya wanafunzi,alibaki anahamaki kama mwendawazimu!.
Kwakuwa walikuwa wamejifunika shuka moja na wote wakiwa uchi,nilimaambia dogo mmoja avue sweta limsitiri Ema ili akimbie nyumbani,ndivyo ilivyokuwa.

Nilimpa lile sweta Ema nikamwambia asimame alivae liwe kama sketi ili atoke aende nyumbani,ingawaje aliposimama alikuwa uchi na wanafunzi walishuhudia kila kitu!,mama mdogo yeye alikuwa akivuta lile shuka ili kujisitiri na ndipo nilimnyanyua na kuondoka naye huku akiendelea kushangaa amefikaje hapo na nini kilikuwa kinaendelea.Wanafunzi waliokuwepo mpaka wakati huo wengi walikuwa wakicheka na wengine kushangaa ni kitu gani kile!.

Sasa tulipofika nyumbani Maza mdogo alikuwa akiniuliza ni nini kimetokea na kwanini wamejikuta wakiwa uchi pale darasani.Mimi sikuwa na majibu zaidi ya kushangaa.Kumbe wakati huo tunajadili pale headmaster alikuwa amelala chumbani,sikufahamu wakati namsalimia alikuwa akinisikia ama la!.

Ba'mdogo "Hebu niwekee maji ya kuoga"

Alikuwa akimwambia mkewe lakini mkewe akawa anamshangaa headmaster.

Maza "Ina maana ba'Mary kinachoendelea wewe hukijui?"

Ba'mdogo "Kuna nini?"

Maza "Nimefikaje shuleni tena nikiwa uchi mbele ya wanafunzi?"

Ba'mdogo "Shuleni uchi,uchi kivipi?"

Ba'mdogo "wewe siumetoka muda si mrefu kuniamsha ukaniambia nachelewa shuleni,sasa umetoka saa ngapi kwenda shule ukiwa uchi?"

Baada ya kauli ile ya Ba'mdogo nikajisemea ndo yale yale ya Ema ya siku ile kuning'inizwa juu ya kenji.Baba mdogo ni kama alikuwa aelewi chochote kabisa na muda huo yeye alikuwa anadai Maza mdogo alikuwa ndani amelala.

Maza "Mungu wangu hiki ni nini?"

Basi hakutaka kupoteza muda akawa ameingia ndani!,basi Headmaster nilijaribu kumuelezea lile tukio lilivyokuwa lakini ni mtu ambaye ilionekana kama hakubaliani nalo,yeye akakomaa kwamba mkewe alikuwa chumbani na ndiye aliyemuamsha awahi shuleni.
Siku hiyo ikawa gumzo hapo kijijini na shuleni pia,talk of the town ikawa hiyo stori ya mke wa mwalimu!,Mazungumzo ya wengi walisema uenda mke wa mwalimu walikuwa na mahusiano na Ema na siku hiyo baada ya mizagamuano ya muda mrefu walichoka wakapitiwa na usingizi,wengi waliamini hivyo japo mimi niliamini lile tukio halikuwa la kawaida!.

Siku hiyo sikuondoka kuelekea kufata miwa ikabidi nitulie nyumbani,sasa nilijaribu kumuuliza Ema uenda alikuwa amifahamu jambo lolote!.

Ema "Yaani sielewi hata nilifikaje pale"

Mimi "Ina maana hukujua kama umelala na Maza mdogo?"

Ema "Mimi nimeshituka tu naona wanafunzi kaka,sielewi kiukweli nilifikaje pale"

Kiukweli hali ile haikuwa nzuri lakini nilibaki kucheka kama mazuri vile lakini hali ilikuwa inatisha sana,japo halikuwa jambo jema,lakini kimoyo moyo nilikuwa nasema angalau sasa Maza mdogo atapunguza mdomo wake!.

Headmaster baada ya kwenda shule muda haukupita alirudi nyumbani,sasa akawa anajaribu kumuuliza mke wake kama lile jambo ni kweli!,basi kumbe kuna wanafunzi shuleni pia walikuwa wamemueleza vilevile kama ambavyo nilimueleza,sasa akaamua kuwarudisha wanafunzi wote nyumbani na kikaitishwa kikao cha kijiji siku hiyo hiyo.Sikutaka kukosa kwenye kile kikao kwasababu nilikuwa mmoja wa mashuhuda na wanafunzi kadhaa!.

Kikao kile kilizungumza mambo mengi mno,kila mwanakijiji alikuwa akizingumza jambo lake.Wapo ambao walikuwa wanasema hizo tabia za kijinga zikome mara moja na wapo wengine waliokuwa hawakubalini na lile jambo.
Sasa yule mzee ambaye nilikutana naye ile jioni wakati natoka kuuza miwa akaniambia nimsalimie mwalimu,yeye pia alikuwa ni mmoja wa watu waliofika kwenye kile kikao na hakukubaliana na lile jambo.

Mzee "Kwanini kila siku ni nyie tu na siyo kwa watu wengine?"

Mzee "Hapo naanza kupata mashaka kidogo"

Mzee aliendelea "Juzi ilikuwa kwa kijana wako na tukaja mpaka kwako mwalimu,leo tena mambo ni yaleyale,ili jambo lingekuwa kwa watu wengine hapo kungekuwa na walakini,kila siku mambo haya yawapate nyie tu?,sisi tutaamini vipi mwalimu?,kama hutaki kuendelea na shule basi bwana na uache lakini hatuwezi kila siku hatuwezi kuwa tunazungumzia mambo yale yale yanayotokea kwa mtu yuleyule"

Mzee "Ingekuwa uchawi hata sisi ungetupata pia,sasa yawezekana mkeo na huyo kijana anayekaa kwako ni wapenzi!"

Sasa hili suala la Ema na Maza mdogo kuwa wapenzi naona wanakijiji wengi walilishupalia kama kweli vile!.

Akasimama mwana kijiji mwengine akasema "Hiki kituko hakijawahi kutokea kwenye hiki kijiji,na mimi sikubaliani na kwamba eti ni uchawi,haiwezekani kabisa!,huyo dogo na mkeo watakuwa wapenzi na uenda mkeo alitoka ndani akakuacha umelala wao wakaja kufanya yao na wakapitiwa na usingizi,hivyo mwalimu nikuombe umchunguze mkeo!"

Watu wengi waliunga mkono ile kauli ya mzee na huyo jamaa.

Headmaster alishindwa aseme nini mbele ya ile kadamnasi,sasa mwenyekiti wa kile kijiji ambaye pia alikuwa mwenyekiti wa kile kikao alisema kile kijiji hapo mwanzo ni kweli kulikuwaga na habari za washirikina,lakini baada ya kuitisha vikao kadhaa yale mambo yakapotea.

Mwenyekiti " Mimi niseme tu kwamba,yawezekana haya mambo yakawa yamerudi,mimi pia nikiongozi wa kimila na kama haya mambo yamejirudia ningefahamu mapema sana,sasa nadhani Mwalimu unakumbuka tukio la kijana wako,na nilikwambia pia tusiendelee kudhani ni ushirikina kumbe kijana wako ndiye mkorofi amewachokoza wenzie wakaamua kumuadhibu kwa style ile,hivyo nikuombe umchunguze na kijana wako pia".

Basi kile kikao baada ya kuchukua masaa kadhaa kikawa kimemalizika lakini jibu lilikuwa ni kwamba Ema yawezekana alikuwa na mahusiano na mke wa mwalimu.Tulitawanyika pale na kila mtu kwenda kuendelea na shughuli zake.

Headmaster hakutaka kabisa kuamini ya kwamba siku hiyo Ema alilala na Mkewe kwenye darasa,alichoamini yeye ni kwamba siku hiyo mkewe alikuwa chumbani wamelala wote,yaani ni kama mtu ambaye alikuwa amepofushwa!

Kiukweli lile tukio lilikuwa ni gumzo sana hasa ukienda hadi senta huko na nadhani pia kwa upande wa Maza mdogo ni tukio ambalo hatokuja kulisahau kwenye maisha yake.Baada ya siku kusonga lile tukio likawa kama linafifia.

Sasa Maza mdogo akawa naye ameanza kushona cherehani pale senta,alikuwa akitoka asubuhi anarejea jioni,muda ambao mimi nilikuwa nikimaliza shughuli ya kuuza miwa inabidi nimshubiri na yeye amalize tuongozane kurejea nyumbani.

Sasa nakumbuka siku moja nimeamka asubuhi mida ya saa 12 ili niwahi kusudi kuepuka jam ile ya asubuhi bafuni,nimeoga nimemaliza nikavaa kama kawaida ili niende sasa kusalimia kule ndani halafu niondoke zangu mdogo mdogo kuchukua miwa.
Nilifungua mlango wa pale sebuleni ili kuingia ndani niwasalimie Headmaster na mkewe,sasa ile nimengia ndani hapo sebuleni,aiseee nilishuhudia mzigo mkubwa wa mavi ambayo kikawaida kama ungeyapima kwenye sufuria,basi yangeweza kufikia kilo 3,mavi yale yalikuwa yamenyewa juu ya meza na ilionekana aliyekuwa ameyanya alikuwa amekula ugali wa mtama,kwasababu kile tunachokula ndiyo tunachokinya!,Sasa harufu ilikuwa kali sana na kiukweli nilishindwa kuelewa waliwezaje kulala ndani kukiwa na harufu kali kiasi kile,baada kushuhudia ule mzigo nikarudishia mlango kwenda kumshitua Ema ili aje ajionee!.




-/-/-/-/-/-/-/-/-/-/-/-/-/-/-/-/-/-




SEHEMU YA - 13


Jamaa alipokuja akafungua mlango na kutazama aliondoka ghafla ameshika pua kutokana na ile harufu namna ilivyo kuwa ya kutisha.

Ema "Nani Kanya hayo mavi?"

Mimi "Sijui"

Mimi "Nimeamka kuja kusalimia ndiyo nakutana na hii hali"

Ema "Headmaster bado amelala?"

Mimi "Bado sijajua,hebu ngoja niwagongee"

Nilienda kujaribu kugonga ule mlango lakini ulifunguka wenyewe kuashiria ulikuwa wazi,basi nikaanza kuita lakini hakukuwa na mtu mle chumbani aliyeitikia!,niliamua kusukuma ule mlango na kuchungulia chumbani kwa Headmaster lakini hakukuwa na mtu!.

Basi nilitoka nikamwambia Ema Headmaster na Mkewe hawapo chumbani.

Ema "Mmmh huu mji aisee mimi utanishinda"

Mimi "kwanini?"

Ema "Hivi unadhani hii hali niya kawaida?,hivi siunakumbuka nilikwambia kuna siku nimekuta mavi kwenye lile debe la unga!"

Ema "Haya mambo si yakawaida,mimi shule ikifungwa sidhani kama nitarudi huku tena"

Mimi "Dingi atakuwa ameenda wapi?"

Ema "Inaonekana wameamka mapema kuna mahali watakuwa wameenda,na nadhani haya mavi niya muda huu tu,Headmaster angekuwa ameyaona najua angetuamsha!".

Basi nilimwambia Ema tuibebe ile meza na kuitoa nje ili kuifanyia usafi,niliingia stooni nikachua jembe nikawa nakokota yale mavi kutoka mezani na kuangukia chini,baada ya kuisha juu ya meza,nilienda kuzoa michanga na kuyafukia yale ya pale chini na kuanza kuyazoa na kwenda kuyatupa huko nje!.Baada ya kuiosha ile meza ikabidi niianike juani ili ipigwe na jua la kutosha!.

Nilipomaliza na kufanya ndani usafi niliondoka zangu kuelekea kwa mzee masumbuko kwa ajili kufata miwa.Sasa siku hiyo sikuona kile kibanda cha Maza mdogo kikifunguliwa,nilihisi uenda aliamua asije tu kwa kuchoka kwasababu kama kweli walitoka yawezekana akawa alichoka.Ile jioni baada ya kumaliza biashara yangu ya uuzaji miwa nikaamua kurudi zangu nyumbani kama kawaida.

Nimefika nyumbani mida ya saa 2 usiku nikakuta hapo uwani yupo mzee mmoja ambaye alikuwa amekaa kwenye stuli,nilimsalimia na kuingia zangu chumbani kwetu.Sasa muda kidogo nikasikia sauti ya Headmaster ikisema "umesharudi?"

Mimi "Ndiyo baba,shikamoo"

Ba'mdogo "Nani umughaka?"

Mimi "Ndiyo baba ni mimi"

Ba'mdogo "aah mi nilidhani ni huyo mpumbavu,nimemwagiza muda sasa sijui linafanya nini huko"

Ba'mdogo "Hebu nenda ukamuangalie huyo mjinga kwa mzee masalu,ukimkuta umwambie achume kabisa na fimbo aje nazo"

Mimi "Sawa baba"

Ba'mdogo "Kimbia bhana na muwahi hapa".

Basi nikatoka nduki kuelekea kwa mzee mmoja aliyekuwa na ng'ombe wa kutosha hapo kijijini akifahamika kama mzee masalu,sikuwahi kufika kwa huyo mzee ila kwasababu ya umaarufu wake pale kijijini nilikuwa nikimfahamu na kwake pia palikuwa pakifahamika.Nilifanikiwa kufika kwa huyo mzee hiyo mida ya saa 2 kuelekea saa 3 usiku.

Nilipofika nilikuta bado watu wako nje wakipiga soga,nilisogea kwa mtu mmoja ambaye ni mwanamke nikamsalimia na kujitambulisha ya kwamba nilikuwa nimeagizwa na mwalimu Wambura.Basi nikawa nimemuomba aniitie mzee masalu ili niweze kumuulizia kuhusu Ema.

Yule mama aliniambia "Hebu Nenda kwenye lile zizi kule utamkuta huko anakagua mbuzi"

Basi nikazunguka nyuma ya nyumba kuliko kuwa na zizi la mbuzi,nilimkuta mzee akiwa na vijana kama 3 wakiendelea kusavei kwenye lile zizi huku wakiongea kisukuma,nilimsalimia mzee na ndipo nikajitambulisha kwake.

Mzee Masalu " Ooh yule kijana wa mwalimu wambura mbona nimempa na ameondoka muda mrefu"

Mzee masalu "Uenda mtakuwa mmepishana,ametoka hapa muda si mrefu"

Mimi "Sawa mzee mimi naondoka"

Mzee Masalu "Sawa msalimie mwalimu".

Basi sikutaka kupoteza muda nikatoka nduki kurudi nyumbani kumpelekea taarifa Headmaster.Nilipofika nyumbani nilimkuta Ema naye akiwa amefika lakini inaonekana Headmaster alikuwa amemgombeza sana maana alikuwa amevimba kama chura!.

Sasa kumbe jamaa alikuwa ameagizwa damu ya ng'ombe,na yule mzee niliyemkuta pale nyumbani wakati mimi natoka senta kuuza miwa alikuwa mganga,hivyo alikuja kwa ajili ya kufanya zindiko pale nyumbani.Wakati wa asubuhi kumbe Headmaster na mkewe walidamka kwenda kijiji kingine kwa ajili ya kumleta huyo mtaalamu na kiboko ya wachawi kama alivyojinasibu!.

Tulitakiwa kila mtu kuvua shati na kupigwa chale kichwani,mgongoni na kwenye mbavu!,basi lile zoezi lilipokamilika kuna dawa huyo mganga akawa ameichimbia katikati ya nyumba na kututaka kila mmoja kukaa kwa matako huku tukiangalia mashariki na kisha kutamka maneno aliyokuwa akituelekeza!.
Baada ya kumaliza kufanya vimbwanga vyake akawa ameaga ya kwamba aondoke na sisi tukae kwa amani huku tukisubiri kuona matokeo!.

Sasa usiku wakati tukiwa tumelala Ema akawa ananiambia.

Ema "mwanangu unajua nilipita kwa Deborah"

Mimi "Muda gani?"

Ema "Si wakati Headmaster ameniagiza"

Mimi "Kumbe ndiyo maana tumepishana"

Ema "Headmaster naye mnoko tu!"

Mimi "Kwanini?"

Ema "Mwanangu amenitukana kishenzi?"

Mimi "Ni-kupiga kimya tu,sasa utafanyaje"

Ema "Mwanangu halafu debo aneniambia yule mtoto ameeleweka"

Mimi "Nani,Mwise au?"

Ema "Si alikwambia atakupa rafiki yake!."

Mimi "Daaah mi nikajua Mwise"

Ema "Mwanangu yule sura mbaya kakuroga nini!,mbona unampenda hivyo"

Mimi "we acha tu!"

Ema "Halafu lile mbona jepesi tu,wewe subiri kesho shule"

Basi tulilala siku hiyo na hakukuwa na mauzauza hata kidogo.Kutokana na yale mauzauza pale nyumbani ilifika sehemu tukayaona niya kawaida kabisa!.

Kulipopambazuka kama kawaida niliamka nikajiandaa na kwenda kuwasalimia Headmaster na mkewe kisha nikaondoka zangu kwenye kibarua cha uuzaji wa miwa.

Sasa siku hiyo ilipofika mida ya saa 10 jioni nilimuona Ema akiwa anakuja na yule binti mwenye shepu iliyokuwa ikiichanganya nafsi yangu akifahamika kwa jina la Mwise,baada ya kuwaona kwa mbali nilianza kuufuta mdomo wangu ambao ulikuwa umetapakaa uchafu wa miwa na ndipo nikakaa sawa sawa kumkabili Mwise!.

Ema "Ooya demu wako huyu hapa bhana nimemleta akusaidie kuuza miwa".

Ema alivyokuwa mpumbavu alikuwa ananiambia halafu anacheka!,daah nilisikia uchungu wa aibu lakini ningefanya nini?,basi baada ya jamaa kumfikisha yule demu pale aliondoka akaelekea kibandani kwa Maza mdogo ili sisi tuendelee na mazungumzo.
Kiukweli yule binti nilikuwa nampenda ingawaje alionekana sura haivutii.

Sasa nikawa najiuma uma pale hata cha kumwambia nikakosa,nashukuru yeye alikuwa mcheshi na akawa amenianza!.

Mwise "Hivi wewe ndiye unakaaga pale kwa Headmaster eeeh"

Mimi "Yeah ni mimi,yule ni baba yangu mdogo"

Mwise "oooh,kumbeee"

Mwise "Mmh niambie sasa maana nataka kuwahi nyumbani"

Mimi "kwani Ema hajakwambia?"

Mwise "Huyo mjinga amenitoa nyumbani hata hajaniambia chochote"

Mimi "Lini utapata muda nina maongezi na wewe"

Mwise "jamani muda wenyewe ndiyo huu,wewe niambie tu"

Mimi "Unaitwa nani?"

Mwise "Ina maana Ema hajakwambia jina langu?"

Mimi "Ema hajaniambia"

Mwise "Naitwa Mwise"

Mimi "ooh Mwise,unajua mimi nakupenda"

Mwise "ndo hicho tu ulitaka kuniambia?"

Mimi "Yes,ndi hicho tu"

Mwise "Sawa mimi naondoka"

Basi yule binti akaondoka huku nikiendelea kumtazama anavyotingisha dunia kwa msambwanda wake aliyotunukiwa.Nilijiona mjinga na domo zege kwa kumbwelambwela kwa mwanamke niliyekuwa nikimtamani kwa muda mrefu!.

Haukupita muda Ema naye akawa amekuja pale huku akitaka kujua nini kimeendelea,niliamua kumdanganya Ema kwamba binti kakubali na ameniahidi tungeonana siku si nyingi kumbe haikuwa hivyo!.Basi tuliendelea kupiga stori hapo kijiweni na ilipofika mida ya saa 12 nilifunga mzigo nikapeleka kwa yule mama aliyekuwa akinihifadhia na mimi kuondoka na Ema kuelekea nyumbani.

Basi wakati tukiwa tunatembea kuelekea nyumbani huku tukipiga stori za hapa na pale,ghafla kwa mbele nikamuona yule binti Monica demu wa Ema akija akiwa na mabinti wenzie wawili!.

Mimi "Demu wako huyo anakuja"

Ema "Mkaushie,mi sikataki wala nini!"

Basi tulipowafikia yule binti akatusalimu,Ema aliuchuna lakini mimi nilimuitikia.Sasa Ema yeye akawa anaendelea na safari bila kujali,mimi nikaona isiwe kesi ngoja niongee nae.

Monica "Huyo mwenzako mbona asalamii"

Mimi "Mi sijui bhana"

Mimi "Unatoka wapi?"

Monica "Natoka kwa mama mdogo naelekea nyumbani"

Monica "Huyo ndugu yako tangu awe na huyo debora wake kiburi kimemjaa,ngoja tutaona"

Basi sikutaka kusema kitu ikabidi ninyamaze.

Monica "Njoo basi nyumbani leo"

Mimi "Itakuwa ngumu Monica"

Monica "Kwanini?"

Mimi "Sitoweza kutoka,wewe siunajua itakuwa usiku na nalala na Ema,nitaaga naenda wapi?"

Monica "Mimi nakupenda sana na wewe ndiye mama yangu anakufahamu ,usijali nakuja kukufata"

Mimi "Sasa ukija itakuwaje?"

Monica "Hilo niachie mimi,kwanza leo nyumbani kuna ngoma za mwana lemi,nakufata"

Mimi "Unajua inabidi iwe siri isifahamike"

Monica "Hata wakijua wewe ni mtu wangu,hakuna wakunitisha"

Monica "Naenda lakini narudi,hivyo kajiandae".

Basi niliondoka nikawa namkimbilia Ema ambaye alikuwa amefika mbali.

Ema "Huyo mjinga anakwambia nini!"

Mimi "Nilikuwa tu namtuliza ili asijisikie vibaya"

Ema "Mimi sikataki ila kenyewe kutwa kunitafuta tu"

Basi kwakuwa hakujua nilikuwa namtafuna,sikutaka kabisa na mimi kumwambia chochote.

Ingawaje kale kabinti hakakuwa na ndundu(msambwanda)kama wa mwise,mimi nilikuwa ninapooza njaa tu!,sikutaka mambo mengi.

Sasa ilipofika mida ya saa 3 usiku,niliskia sauti ya Monica ikiniita nje,niliamka kujifanya najinyoosha na nilipomtazama Ema nilikuta amelala isivyo kawaida.




-/-/-/-/-/-/-/-/-/-/-/-/-/-/-/-/-/-/-




SEHEMU YA - 14.


Niliamka taratibu nikajifanya kumshitua jamaa ili nione kama alikuwa akisikia,nilitaka kama angenisikia basi nimwambie naelekea chooni!,sasa kwakuwa alikuwa amelala usingizi wa pono,niliamka nikafungua mlango taratibu kisha nikairudishia!.Nilifungua mlango wa nje taratibu nikatoka nikakuta yule binti Monica akiwa nje ananisubiri!.

Monica "Yaani muda huu mlikuwa mmelala?"

Mimi "Kwani saa ngapi sasa?"

Monica "Bado mapema sana"

Sasa muda huo ninazungumza naye ilikuwa yapata mida ya saa 5 usiku,sikuwa na saa lakini kwa makadirio sisi tuliingia kulala mida ya saa 3 usiku na baada ya yeye kuja ilikuwa imepita muda kidogo!.
Sasa kwakuwa nilikuwa tayari nishakuwa na hamu na papuchi,sikutaka kabisa kuwaza umbali tutakao tembea kwenda kwao,cha msingi ni mimi kufika na kumcharaza stiki za kutosha na kurudi mapema nyumbani.Kwakuwa mpaka muda huo hapo kijijini sikuwa kabisa na demu mwingine wa kuzugia ilibidi niwe mpole tu kwa yule binti ili angalau niwe napooza njaa ya mashine!.

Basi tulianza kutembea kwa haraka huku nikiwa nimemshika kiuno kana kwamba atanitoroka!.

Monica "Mimi nakupenda sana wewe umughaka,yaani sasa hivi najikuta tu nakupenda"

Mimi "Lakini Moni mimi na wewe tunaiba tu,Ema akijua najua tutakosana"

Monica "Wewe achana nae huyo,mbona yeye anatembea na Deborah"

Monica "Huyo mjinga nitamkomesha aliniambia atanioa kumbe alitaka kupata anachokitaka kwangu halafu aniletee dharau,hanijui vizuri binti Makoye".

Aliendelea kusema "Nilikwambia leo nyumbani kuna ngoma za mwana lemi,ndo maana nimekuja kukuchukua"

Mimi "Ngoma za mwana lemi ndiyo ngoma gani?"

Monica "Wewe twende tu utaona"

Monica "Tukifika nyumbani utafanya kila nitakachokuambia lakini,sawa?"

Mimi "Sawa"

Sasa mwanaume nikadhani ile kuniambia nitafanya kila atakachosema ilikuwa ni kumbadili kila style wakati wa mizaguamuano,moyoni nilifurahi sana na nikawa nina shauku ya kufika nyumbani kwao haraka ili nikaikung'ute papuchi mpaka ichakae!.

Mimi "Mama yako yupo?"

Monica "Yupo ila atakuwa bize kwenye ngoma".

Basi tulitembea kwa dakika kadhaa tu tukawa tumekaribia nyumbani kwao,nilipata mshangao sana kwakuwa haikuwa kawaida kwasababu nyumbani kwao ilikuwa mbali sana!,sasa nikawa najiuliza au kwasababu ni usiku na hakuna kashikashi njiani ndo maana tumefika mapema?,niliwaza pia siku ile nilivyokutana na Monica pale kwenye viwanja vya mnada na namna tulivyokwenda kwao haikuchukua muda mrefu,nilidhani uenda kwasababu ilikuwa usiku hivyo kujikuta unatembea kwa haraka kwasababu hakuna jua wala nini!.

Sikuwa kabisa na mawazo uenda yule binti anaweza kufanya namna yeyote kwasababu hakuwahi kunionyesha jambo lolote baya nala kutisha mpaka nimtilie shaka,isipokuwa ni ile siku moja tu ambayo nilimuona pale lamboni akichuma yale majani ya kutengeneza majamvi ndipo kama nilishangaa namna alivyotokea mbele yangu ghafla!.Basi nikajipa moyo kwasababu alikuwa ananipenda hata kama angekuwa ni mbaya asingenifanyia ubaya mimi.
Kabla ya kwenda kuingia ndani,aliniambia nimsubiri kwanza anarudi.Aliondoka akaenda akazunguka nyuma ya nyumba yao ambako kulikuwa na shamba la mihogo akaingia ndani!.Nilimsubiri pale kwa takribani dakika 5 hivi akawa amekuja na kimfuko cha rambo kilichokuwa kimefungwa ambacho sikufahamu ndani kulikuwa na nini!.

Monica "Chuchumaa chini"

Basi nikachuchuma chini,akakifungua kila kimfuko kisha akatoa vijifuko vingi vingi vilivyokuwa vimefungwa kwa kukazwa sana!.Sikumuuliza chochote nikawa nabaki kumuangalia anataka kufanya jambo gani.

Sasa kwakuwa lilikuwa giza totoro,sikuweza kuona mle ndani ya tule tujifuko tudogo tudogo kulikuwa na kitu gani.

Monica "Kama nilivyokwambia leo hapa nyumbani kuna ngoma,nataka nikupake hii dawa ili wakati wa ngoma usije kuonekana na wacheza ngoma wanaweza kukufanya kitu kibaya na mimi nitaadhibiwa"

Basi akilini mwangu nikasema uenda alitaka kabla ya mizagamuano tukacheze ngoma ya kisukuma iliyoitwa "Mwana lemi" kama alivyokuwa ameniambia hapo awali.

Basi alianza kunipaka ile dawa usoni,miguuni na mikononi na kuna nyingine akawa amenipa ili niirambe.Baada ya lile zoezi akaniambia tuondoke twende ndani!.Safari hii wakati tunaelekea kwenye kile kinyumba cha nyasi alichokuwa akilala Monica tulizunguka kwa nyuma ambako ilibidi kukanyaga matuta ya mihogo na kuingia ndani,ile siku ya kwanza kulala hapo nakumbuka tulipitia moja kwa moja mbele ya nyumba,ila safari hii imekuwa tofauti!.

Nilipofika ndani Monica aliniambia nikae kwa kutulia na kila atakachukuwa akiniambia basi nifanye.Alinisogelea karibu akanivua nguo zote nikabaki mtupu,alipomaliza alianza na yeye kuvua nguo zote,kwakuwa mle ndani kulikuwa na giza totoro hakuna aliyemuona mwenzie kiufasaha,sasa sikujua kama yeye alikuwa akiniona ama la!,alianza kunipaka dawa ambayo sikuitambua mwili mzima na alipomaliza alinipatia mkononi na mimi akasema nimpake,sasa wakati nampaka kufika kiunoni nikakuta amevaa shanga!,nilishangaa sana siku hiyo kumuona ana shanga kiunoni kwasababu siku ile ya kwanza hakuwa na shanga kabisa!.
Basi nikaendelea kumpaka ile dawa kuzunguka mwili mzima,wakati huo abdala kichwa wazi alikuwa amesimama akionyesha kuwa na kiu ya maji ya mdimu!.

Baada ya kumaliza lile zoezi,Monica akawa amenitaka nikae kwenye godoro.

Monica "Umughaka mimi nakupenda sana na nia yangu ni kukusaidia"

Mimi "Kunisaidia na nini Moni?"

Monica "Wewe unadhani uko salama?,hivi huwa hujiulizi kwanini wewe hayakukuti?"

Mimi "Ma nini ambayo hayanikuti"

Monica "Yaani wewe nae umezidi utahira,pamoja na kukueleza tu hujiongezi!"

Aliendelea "Subiri utajionea ila naomba usije kupiga kelele,sawa?"

Mimi "Sawa"

Basi wakati tukiwa mle ndani tukiongea,ghafla nikaona miale ya moto ikitokea nje,ilionekana kuna moto ulikuwa umewashwa,Sasa Monica akanifanyia ishara ya kwamba nifunge domo langu na nisishituke!.Baada ya muda nikaanza kusikia ngoma zinapigwa kwa nguvu huku sauti za kina mama na wanaume wakiwa wanaimba kwa kisukuma.

Zile ngoma zikaanza kukolea huku nikisikia vishindo vya watu kama wakiruka na kucheza!.Sasa baada muda kupita kidogo,Monica akanifanyia ishara ya kwamba nisimame nimsogelee alipokuwa,niliposogea ndipo akaniambia nichungulie kwenye upenyo wa ule mlango wa bati!.Sasa kile kinyumba kilivyokuwa kimejengwa kilikuwa cha mviringo kama simtank(nadhani waliokulia vijijini watakuwa wanazifahamu nyumba hizo),sasa kutokana na kile kinyumba kilivyokuwa kimejengwa,mlango wa kile kinyumba hata kama ungefungwaje,kwa juu kulikuwa na uwazi mkubwa uliowezesha kuchungulia nje na kuona kwa uzuri!.

Basi nikachungulia nje nikaona moto mkubwa mno ukiwa umewashwa pale mbele ya nyumba yao Monica,pia nikawaona watu wake kwa waume wakiwa uchi kama walivyozaliwa(uchi wa mnyama)wakicheza kwa kuzunguka mduara,mpiga ngoma alikuwa mwanaume ambaye yeye alikuwa pembeni kabisa,sasa wakati wakiwa wanazunguka ule mduara huku wakiimba ngoma,nikamuona mama yake Monica naye akiwa mmoja wao,nilipoendelea kutazama vizuri nikamuona na yule mzee ambaye nimewahi kukutana naye jioni wakati natoka Senta akanisalimia kisha akaniambia nimsalimie headmaster,nilipomuuliza jina akaniambia anaitwa Makono.

Pia ni huyu huyu mzee wakati wa kikao pale shuleni baada ya lile sakata la Ema na Maza kukutwa wamelala darasani ndiye aliyekuwa akichangia na akisema mambo ya ushirikina hayakuwepo hapo Kjijini.

Nikabaki nimekodoa macho na nikawa kimya kabisa,sasa baada ya zile ngoma kupigwa kwa sana na wao kuuzunguka ule moto,ghafla kuna mzee akapiga kelele kwa kisukuma akisema "Bhebheeeeeeee",kisha mpiga ngoma akaacha kupiga ile ngoma na watu wote wakasimama.




-/-/-/-/-/-/-/-/-/-/-/-/-/-/-/-/-/-





SEHEMU YA - 15.


Kila mcheza ngoma alisimama ghafla na kumtizama yule mzee ambaye ilionekana kabisa alikuwa kiongozi wao.Baada ya hapo alinyoosha mkono juu akiwa ameshika usinga(mkia wa mnyama)ambao sikuweza kufahamu ulikuwa wa mnyama pori au mnyama wa kufugwa!.

Alipoteremsha mkono chini niliona watu wote wameweka mikono mbele kuonyesha unyenyekevu huku vichwa vikitazama chini.Sasa yule mzee alianza kuongea kwa sauti kubwa mno!.

Mzee alisema "Ng'wana Charles"

Aliendelea "Ng'wana ndekeja"

Baada ya kusema hivyo nikaona ananyoosha usinga kuwapa ishara hao aliowaita wasogee mbele,sasa nikaona wazee wawili wamesogea mbele huku wakiwa wameinamisha nyuso chini na mikono imewekwa mbele kuashiria unyenyekevu wa hali ya juu!.

Mzee akasema "Ng'wenagi umnho ng'wenuyo aha"

Basi wale wazee waliondoka na kuingia kwenye ile nyumba ya mama yake Monica,hawakuchukua muda wakawa wametoka ndani huku wakiwa wamembeba mtu ambaye sikumuona kwa haraka,sasa baada ya kumfikisha yule mtu na kumbwaga pale kando ya ule moto ndipo nikamuona vizuri nikawa nimemtambua!,alikuwa ni mzee ambaye alijinasibu ni mganga aliyekuja pale nyumbani kuweka zindiko na kutupiga chale za kutosha!.

Basi yule mzee ambaye ilionekana ndiye mkubwa pale akawa toa amri tena ya kuanza kupiga ngoma na kucheza!,sasa wakati wanacheza kwa kuzunguka ule moto,akajitokeza mama mmoja ambaye alikuwa amejifunga shanga kiunoni na kiremba cheusi kichwani huku mkononi akiwa ameshika kisu!,sasa akamsogelea yule mzee ambaye alikuwa akishanga shangaa kama tahira pale chini,yule mama akafika akamkamata kichwa akaanza kumyoa nywele!.

Wakati mambo yote hayo yanaendelea,mimi na Monica tupo tunachungulia kwenye ule upenyo wa mlango na Monica alinizuia kabisa kutopiga kelele!.

Sasa baada ya lile tukio la kumnyoa yule mzee nywele kukamilika,yule mama alichukua zile nywele akaziweka kwenye kitu kama sahani halafu akamkabidhi yule ambaye alionekana ni kiongozi,sasa wakati anamkabidhi kama kawaida uso uliinama chini kuashiria unyenyekevu!.Baada ya hapo yule mama akaanza kumvua yule mzee nguo zake zote!,alipomaliza aliinama chini kwenye akachukua vitu ambavyo sikuvifahamu akaanza kumpaka yule mzee!.Baada ya kumaliza lile tukio la kumpaka yule mzee vitu visisvyo julikana,akaondoka kinyume nyume kurudi kwenye mstari kuuungana na wenzie kuendelea kucheza ngoma.

Sasa haukupita muda yule mzee tena akatoa ishara ile ngoma ikasitishwa!,baada ya hapo ilikuwa kitendo cha kufumba na kufumbua wakawa wametoweka pale kwenye lile eneo na ghafla kukawa na giza kuu!,nilitaka kufahamu kiliendelea nini na hivyo ikabidi nimuulize Monica.

Mimi "Mbona hawaonekani?"

Monica "Unataka nikupeleke walipoelekea?"

Mimi "Hapana"

Monica "Nakupenda wewe sana ndiyo maana nimekuleta ujionee mwenyewe"

Monica "Mimi nitakulinda wala usiogope"

Aliendelea kusema "Wameelekea kwenye sherehe za kula nyama"

Monica "Ile miembe miwili mikubwa ya kwenye ile njia ambayo tumekutana si unaikumbuka?"

Mimi "Ndiyo"

Monica "Ndo wako hapo"

Mimi "Sasa hapa wameondokaje?"

Monica "wewe bado mdogo ukikuwa utaacha kuuliza uliza maswali"

Sasa nilikuwa nashangaa binti anayeniambia mimi mdogo nabaki kumshangaa kwasababu ulikuwa ukiniangalia mimi na yeye utajua kabisa yeye ndiye mdogo!.

Monica "Halafu wewe una mizimu mikali sana ndiyo maana nataka uwe mume wangu"

Mimi "Mizimu mikali?,mizimu mikali kivipi?"

Monica "Umekuwa ukiwasumbua sana wanapokuwa wakila nyama zao"

Nikashituka sana nikabaki nashangaa mle ndani ambako mpaka muda huo kulikuwa na giza totoro!.

Monica "Unakumbuka siku unapita pale kwenye miembe usiku uliona nini?"

Mimi "Nakumbuka kuna siku nilikuwa natoka senta kuangalia mpira nikaona moto unawaka kwenye ile miembe"

Monica "Achana na mambo ya moto,wewe hukuwahi kuona mtu pale?"

Aisee,sasa nikawa najiuliza huyu binti matukio yote hayo yeye alionaje?,kiukweli nilianza kuingia uoga ila akawa ananisihi ya kwamba nisiogope na yeye yupo kwa ajili ya kunisaidia!.

Monica "Yule mtu uliyemuona siku ile aliliwa nyama,sasa wewe umekuwa ukiwasumbua kupita ile njia kwasababu hakuna mtu anayepita ile njia usiku kama ule".

Aliendelea kusema "Kwa ujasiri ulionao waliona wakujaribu kuona kama unawaona na ndiyo maana walikutega na kukutisha na ulivyotishika na kukimbia wakaona kumbe huna lolote"

Mimi "Sasa nawatesaje?"

Monica "Pale kwenu ni wewe ndiye ambaye huwezekaniki na sijui kwanini,wewe unanyota nzuri mno"

Mimi "Yule mganga amefanya kosa gani"

Monica "Yule ni mjeuri,anaenda kuliwa nyama".

Akaendelea kusema "Kuna siku mama yangu alienda kusenya kuni na mlikutana njiani ukamsaidia zile kuni,hivyo mama yangu akakupenda sana"

Mimi "Mbona sikumbuki siku ambayo nimebeba kuni za mama yako?"

Monica "Wewe bado mtoto mdogo nimekwambia acha maswali utaelewa tu".

Kiukweli nilikuwa ninawaza na kujiuliza sana lakini nakosa majibu!,ndipo sasa nikajua uenda matukio mengi pale nyumbani yalikuwa yanasababishwa na hilo kosi hatari lilikuwa likicheza ngoma,sikutaka kumwambia mama yake ni mchawi ingawa nilimshuhudia kwa macho yangu,nilidhani uenda ningemwambia kuhusu mama yake angenibadirikia mle ndani na nikaipata freshi,sikutaka kabisa kutengeneza matatizo!.

Baada ya maongezi ya muda mrefu mizagamuano ikachukua nafasi!,sasa nikawa nimemwambia Monica inapaswa baada ya mizagamuano ikifika saa 10 usiku anisindikize kurudi nyumbani ili asije akajua mtu yeyote kwamba nilitoka usiku.

Monica "Nalekotogwa natokoreka"

Mimi "Ndiyo nini?"

Monica "Wewe naye,utajifunza lini kisukuma!"

Monica "Nakwambia nakupenda na sitokuacha"

Basi sikutaka kumjibu na mimi akili yangu haikuwa kwake kabisa,kilichokuwa kinanipeleka kwake ni kumpatia maji ya uzima wa milele abdala kichwa wazi ili asihangaike na kiu.
Basi baada ya kasi ya mizagamuano ni kama Monica alipitiwa na usingizi,mimi sikuweza kabisa kupata usingizi kwasababu ya kile nilichokuwa nimetoka kukishuhudia pale!.

Sasa baada ya muda kupita nikiwa natafakari huku usingizi ukianza kunipitia,ghafla nikasikia kishindo kikubwa nyuma ya ile nyumba tulimolala!,sasa nikajaribu kupeleka mkono ili nimpapase Monica ashituke ili na yeye asikie lakini hakukuwa na mtu kwenye godoro!.

Nilikurupuka nikaanza kupiga kelele za uoga kama mwehu!




-/-/-/-/-/-/-/-/-/-/-/-/-/-/-/-/-/-/-





SEHEMU YA - 16.

Nilifungua ule mlango ulokuwa umefungwa kwa komeo nikatoka nje na kuanza kukimbia kama mwendawazimu.Niliingia kwenye shamba la jirani na hapo kwao Monica lililokuwa na mahindi madogo saizi ya magoti kisha nikalala chini!.Nilishindwa kuelewa mpaka muda huo binti Monica atakuwa yupo wapi maana mlango haukufunguliwa na yeye ndani hakuwepo!.Sasa nilinyamaza kimya ili kuona ni kitu gani kilikuwa kinaendelea.

Baada ya kama dakika 20 hivi,nikawa nasikia sauti ya Monica ikiniita kuashiria kunitafuta,mimi niliendelea kukaa kimya huku nikichukua tahadhari na nilidhani uenda asiwe Monica nikaingia chaka!.Kwa mbali niliona ule mlango wa ile nyumba unagunguliwa mtu akaingia ndani kisha akatoka tena akawa anaita.Baada ya kujiridhisha kwamba alikuwa Monica ndiye aliyeniita,niliamua kusimama na kujipangusa mchanga uliokuwa umenijaa kwenye tumbo na magoti na hii ilikuwa ni baada ya mimi kulala chini!,mpaka wakati huo nilikuwa kama nilivyozaliwa maana nilipokurupuka sikukumbuka hata nguo nimeziweka sehemu gani!

Monica "Uko wapi?"

Monica alijifanya kuniuliza niko wapi kana kwamba alikuwa hanioni,ila nilichoamini mimi ni kwamba alikuwa akiniona tu vizuri!.Niliondoka kuelekea ule uelekeo alokuwa amesimama Monica.

Monica "ulikuwa wapi?"

Mimi "Nilikuwa pale"

Monica "Sasa huku nje umefata nini!?"

Mimi "Wewe ulienda wapi?"

Monica "Mimi mbona nilikuwepo?"

Mimi "Ulikuwepo wakati nimekutafuta sikuoni!?"

Monica "Kuna mjinga mmoja nilikuwa namshikisha adabu"

Mimi "Mjinga gani?"

Monica "Hukusikia napigana na mtu"

Mimi "Mimi sijasikia,nilichosikia ni kishindo kikubwa nyuma huko nageuka nakuangalia na wewe hauonekani,ndiyo nikatoka kukimbia"

Monica "Nilikwambia umughaka nitakulinda usiku na mchana,kuna mjinga alikuja kutaka kunijaribu,nimepambana nae alitaka kunishinda nikamuita mama"

Mimi "Kwahiyo mama yupo ndani!"

Monica "Mama amemchukua amempeleka wakamtengeneze vizuri!"

Basi baada ya kuniambia maneno yale ilibidi tuingie ndani,kiukweli nilikuwa nina hofu sana na nilijilaumu kwanini nimeingia kwenye mahusiano na yule binti,kibaya zaidi siku zilivyokuwa zikienda ndivyo na mimi nilikuwa siambiliki wa kuelezeka kwa yule binti!,ilifikia pointi ambayo nisipokuwa nikimuona nilikuwa ninapata mawazo sana.
Mida hiyo ilikuwa yapata saa 9 usiku na tangia hapo sikupata usingizi tena,ilipofika mida ya saa 10 kuelekea saa 11 ambapo niliona kabisa kama kuna miale ya mapambazuko,nilimwambia anisindikize kurudi nyumbani.

Monica "Mbona unawahi hivyo?"

Mimi "Nadhani unamjua Ema alivyo muongo,na najua kama aliamka kwenda chooni akakuta sipo sijui itakuwaje,lazima tu amwambie Ba'mdogo"

Monica "Yule hawezi kuamka mpaka wewe ufike"

Mimi "Wewe yule humjui vizuri!"

Monica "Basi tufanye kidogo halafu ndiyo uende"

Kiukweli sikuwa kabisa na hamu tena ya mizagamuano ila kwakuwa alitaka sikuwa na namna,ikabidi tulianzishe tena!.Fimbo ziliendelea mpaka sasa nikawa nasikia majogoo yanawika huko nje kuashiria kumepambazuka!.Nilivaa zangu nguo na yeye pia akavaa na safari ya kunisindikiza kwetu ikachukua nafasi.Monica hakutaka kabisa kuniacha njiani,alihakikisha mpaka naingia ndani ndipo na yeye anarudi kwao.

Ilikuwa ni kama kuonekana kwao ni mbali lakini nilipokuwa nikitembea na yeye sikuwahi kuona wala kuhisi umbali wowote,hebu fikiria umbali wa zaidi ya kilometa 6 lakini ndani ya dakika kama 10 mnajikuta shafika!,haya yalikuwa ni maajabu ya binti wa kisukuma Monica.Basi baada ya kuhakikisha nimefungua mlango na kuingia ndani na yeye aliondoka kurudi kwao.
Nilisukuma mlango nikaingia ndani nikakuta Ema bado amelala,sasa sikufahamu aliamka wakati mimi sipo ama la!.Kwakuwa kulikuwa kumepambazuka sikutaka kujiegesha maana niliona ningepitiwa na usingizi,nilijifanya namuamsha jamaa ili nione!.sasa baada ya kumpiga piga na mkono,jamaa alishituka sana!.

Mimi "nimekushitua?"

Ema "Maanangu nilikuwa naota"

Mimi "Ooh,jana ulichoka sana nini!"

Ema "Yaani sijawahi kulala usingizi mtamu kama wa leo"

Mimi "Kumekucha kijana jiandae uende skonga"

Ema "Leo sidhani kama nitaenda"

Mimi "Shida nini?"

Ema "Nahisi kuchoka tu"

Sasa jamaa alikuwa ananieleza huku akiendelea kupiga miayo ya kufa mtu!.Nilipoendelea endelea kumdodosa ndipo nikagundua tangu ule usiku nilipotola hakuwa ameamka hata kidogo!.

Basi kulipopambazuka zaidi nilielekea lamboni kuchota maji ya kuoga na kurejea nyumbani,basi baada ya kumaliza kila kitu niliingia ndani kumsalimia Headmaster na mkewe na kisha mimi kuelekea kwa mzee masumbuko kuchukua miwa ya kwenda kuuza.Sasa wakati unatoka hapo kwa mzee masumbuko ili uikamate njia ya kuelekea Senta,kulikuwa kama na makutano ya njia,njia moja ndiyo njia ambayo ilikuwa inatoka kwenye uwanja unapofanyikia mnada na ukipandisha nayo inakupeleka moja kwa moja kwa kina Monica kule Masairo,njia nyingine ni njia ambayo ilikuwa inakupeleka mpaka lamboni ambako unatokea mpaka shuleni,na njia nyingine ndiyo njia ambayo nilikuwa naipita mimi kuelekea senta kila ninapotoka kuchukua miwa!.

Sasa wakati naikamata njia ambayo ilinipaswa kupita kwa mbele kuna kina mama walikuwa wakija wakiwa wawili,mmoja wapo nikama nilimuona kwenye zile ngoma pale kwao Monica ule usiku!,sasa walizungumza kisukuma halafu wakawa wananitazama sana,nikama walikuwa wananiteta!,waliponipita nilihisi kabisa wanaendelea kunitazama,sasa nilipofika kwa mbele nikautua ule mzigo wa miwa nikajifanya kama naufunga kwa kukaza,nikawaangalia kwa kuibia ndipo nikaona wananitazama na nikama wakawa wanazungumza kwa kubishana!,walipoona nawaangalia wakaondoka huku wakionekana kama kunishangaa!.

Sasa nikabaki namuangalia yule mama ambaye nilimuona ule usiku nikabaki kushangaa tu,kiukweli ukikutana naye hivi kwa mara moja na ukiambiwa mambo anayoyafanya huwezi kabisa kuamini!.Nilijitwisha zangu zigo la miwa na kuondoka huku nikishindwa kuelewa kwanini wale kina mama walikuwa wakiniangalia kwa makini sana!.

Siku hiyo biashara ya miwa ilikuwa mbaya sana,kiukweli tangu asubuhi hadi jioni niliuza pingili tatu tu za muwa,basi kwakuwa nilijua biashara siku zote haifanani sikutaka kujipa presha kabisa,nilipanga Headmaster akiniuliza nitamaambia ukweli ya kwamba biashara imekuwa ndivyo sivyo,basi ilipofika jioni nilienda kupeleka miwa kwa yule mama aliyekuwa akinifadhia na mimi kuondoka kueleke nyumbani,wakati wote nilikuwaga naondoka hapo senta mida ya saa 12 jioni na kufika nyumbani mida ya saa 1 kuelekea saa 2.

Sasa nilipotembea kwa umbali mrefu,huku nikiwa naendelea kuitafakari siku,mara ghafla mbele yangu akatokea yule mzee Makono ambaye pia alikuwa mmoja aa wale watu waliokuwa wakicheza ngoma ule usiku,nilishangaa sana kwasababu eneo nililokutana nae,ndilo aneo ambalo siku ile nilikutana nae na akanitaka nikamsalimie Headmaster,safari hii nilishituka sana mpaka akashangaa!.

Mzee makono "Unishituka nini wewe!"

Mimi "Mzee shikamoo"

Mzee makono "Kwahiyo hujashituka jana leo ujifanye kushituka!"

Kiukweli nilishangaa sana na ghafla uoga mkuu ukaniingia,nilishindwa hata kukimbia nikabaki nimepigwa na bumbuwazi,sasa nilibaki kushangaa kwasababu iliwezekana vipi jana kuniona na wakati Monica aliniambia sababu ya yeye kunipaka ile dawa ni kusudi nisionekane na wacheza ngoma kama adui na wahisi mimi ni mmoja wao!,pili nikajiuliza yeye mzee makono alinionaje?,Sasa wakati naendelea kutafakari nisijue cha kufanya,akaendelea kuniambia kwamba

Mzee makono "wewe na kale kakondefu mmeshirikiana kunitesea mwanangu!,si ndiyo?"

Akaendelea "Nataka leo unitambue mimi ni nani!"

Sikutaka kabisa kumjibu yule mzee nikawa nimebaki kimya kwa bumbuwazi,basi baada ya kuniambia maneno hayo akasonya kwa kufyonza kisha akaondoka!,kiukweli ongea ya yule mzee alionekana kabisa amechukizwa sana na alikuwa na hasira mno!.
Sikufahamu kwa haraka haraka ni kitu gani kilikuwa kimemkasirisha na ni nani aliyekuwa amemtesa mwanaye!.

Basi kutokana na uoga niliyokuwa nao,nikaanza kukimbia ili kuwahi nyumbani,safari hii nilipofika pale kwenye miembe nilipita kwa spidi kali mno kama kipanga na sikutaka hata kugeuka nyuma!.

Sasa nilipofika karibu na nyumbani nilimkuta Monica akiwa amesimama anaongea na Ema.

Ema "Haya huyo hapo ongea nae"

Baada ya kusema hivyo Ema akawa anaelekea ndani!.

Mimi "Kwani kuna nin?"

Monica "Tuondoke hapa"

Mimi "Nakupenda umughaka,nakuomba tuondoke,utajua huko huko"

Basi Monica akanishika Mkono tukaongozana kuelekea nisipopafahamu.Mpaka muda huo hata ndani sikufika kabisa.

Mimi "Tunaenda wapi?"

Monica "Nilikwambia nitakulinda kwa gharama yeyote,huyo mjinga anajifanya
mjanja muache".



-/-/-/-/-/-/-/-/-/-/-/-/-/-/-/-/-/-/-




SEHEMU YA - 17.


Wakati tunaondoka Monica alikuwa amechukia sana na haikuwa kawaida yake,niliwaza sana itakuwaje maana niliona Ema ameondoka kwa hasira kuelekea nyumbani baada ya mimi kufika pale!.Basi nilikuwa mpole huku binti wa watu akiniongoza kuelekea nisikokufahamu.

Mimi "Tunaelekea wapi?"

Monica "Wewe twende acha hayo maswali yako".

Mimi "Lakini si tunawahi kurudi?"

Baada ya kuona maswali yamekuwa mengi,Monica alisimama akawa ananisukuma sukuma kwa mkono akiniambia "Hivi lini utafunguka hayo macho yako?,hivi wewe unajiona upo kawaida?"

Monica "Huku nimekuja kwa ajili yako,kama unataka hurudi kwenu wewe rudi lakini kitakachokukuta utajua mwenyewe!"

Mimi "kwani kuna nini Moni?"

Monica "Yaani unataka kuwa tahira kama huyo ndugu yako"

Aliendelea "Nishakwambia kila kitu tangu jana kwamba nitakulinda usiku na mchana lakini unajitoa ufahamu!"

Monica "Kama unanipenda na unaniamini twende,lakini kama huniamini rudi kwenu,njia hiyooo nyeupe".

Monica alikuwa mkali sana baada ya kuona kama namchosha kwa maswali ambayo yeye aliamini kabisa majibu yake uenda nikawa nayafahamu,sikuwa na namna ikabidi nijifanye kondoo niongozane nae kusikofahamika.

Mimi "Mbona jamaa alikuwa amekasirika?"

Monica "Achana nae mjinga yule,itakula kwake"

Monica "Mimi leo nimemueleza ukweli kwamba wewe ni mpenzi wangu"

Mimi " Siulisema lakini iwe siri Moni?"

Monica "Nimefika pale kwa mambo mengine kabisa,sasa yeye akaanza kuleta mambo yake ya niache kumsumbua,mimi nikamwambia sijaja hapa kwa sababu hiyo,kilichonileta sicho unachofikiria,na kama ni mapenzi kwasasa mpenzi wangu ni umughaka siyo wewe"

Aliendelea "Basi ndiyo kama ulivyotukuta,alipokuona akasema niongee na wewe na kwa hasira akaondoka,sasa mimi ulitaka nifanyeje?".

Mimi "Ninavyo mjua yule,hatutaongea mwaka mzima".

Monica "Nimekwambia achana nae,utakipata".

Basi tulitembea kwa muda mrefu kidogo huku tukiendelea kupiga stori za hapa na pale,yule binti Monica kiukweli mpaka wakati huo nilikuwa nampenda sana toka ndani ya moyo wangu!,na alikuwaga jasiri sana asiyeogopa chochote!.Sasa kwakuwa alikuwa amenihakikishia ulinzi kama mpenzi wake,sikuwa na hofu kama angeweza kunifanyia jambo lolote!.

Baada ya safari ya dakika kadhaa,tuliiacha njia na kuingia kwenye shamba moja kubwa la mihogo,tulitembea mle kwenye lile shamba kwa takribani dakika 2 tukawa tumefika kwenye mji mmoja ambao ulikuwa umezungukwa na mashamba ya mihogo,sasa baada ya kufika pale ghafla nikawaona wanawake watatu ambao kwa haraka haraka sikuweza kuwatambua kwakuwa walikuwa kwa mbali kidogo!.Monica aliniambia nisubiri hapo pembeni na yeye akawa amewafuata wale kinamama na kuanza kuzungumza nao kisukuma.

Sasa ghafla nikaona wale kina mama wananikimbilia na walipofika wakawa wamenishika kwa kunitaka nifanye haraka nisogee walipokuwepo wao.Basi wakamwambia Monica kwa kisukuma kwamba aingie ndani na alete jamvi ili nikalie.Sasa wale kina mama nikawa nimewatambua baada ya kuwa nimewaona kwa karibu,mmoja alikuwa mama yake Monica,na wale wawili walikuwa wale kina mama ambao nilionana nao njiani wakati natoka kuchukua miwa kwa mzee masumbuko ile Asubuhi,kumbuka hao wote akiwamo na mama yake Monica walikuwa ni miongoni mwa watu waliokuwa wakicheza ngoma ule usiku pale kwao Monica.

Sikuelewa kwa nini Monica alinipeleka pale na sikufahamu ni kitu gani kilikuwa kikiendelea!.Baada ya lile jamvi kuletwa na kuwekwa chini,mama yake Monica akaniambia nisimame na nivue nguo zangu zote nibaki kama nilivyozaliwa!.Basi ikabidi nifanye kama alivyoniambia.

Sasa baada ya kumaliza kuvua nguo,akaniambia nikae pale katikati ya jamvi;Mama mmoja kati ya wale niliokutana nao ile asubuhi nikaona anachukua maji kwenye chungu akawa anakunywa kwa kupiga fundo kisha ananitemea,alinitemea yale maji mwili mzima mpaka yalipomalizika kwenye kile chungu!.Baada ya hilo zoezi la kutemewa maji walinizunguka wote wale kina mama akiwemo mama Monica wakaanza kunipaka vitu ambavyo sikuelewa ilikuwa ni kitu gani,harufu yake haikuwa nzuri kiukweli na nilibaki kushangaa tu!.

Waliendelea kunipaka kwa haraka na walipomaliza,mama mmoja akaniambia nisimame.Sasa baada ya kusimama yule,yule yule mama ambaye ndiye alikuwa akinitemea yale maji,niliona mkononi ameshika kitu kama usinga wa mnyama na akaanza kuchovya ule usinga kwenye chungu kiingine kilichokuwa pembeni akawa kama ananichapa na ule usinga uliojaa yale maji aliyokuwa akichovya kwenye kile chungu.
Wakati anaendelea kunitandika na ule usinga alikuwa akinuia kwa kisukuma.

Sasa baada ya lile zoezi la kuchapwa na usinga,mama yake Monica alimwambia binti yake aingie ndani awashe kibatari alete,baada ya kuletwa kile kibatari kukawa angalau na mwanga pale nje,sasa mama yake Monica akanisogeza kwa pembeni kulipokuwa na jiwe lilikuwa lichongwa kama kigoda akaniambia nikae.(Lile jiwe nadhani ni yale mawe ambayo huwa wanasagia nafaka kama mtama,udaga, na ulezi,lilikuwa ni jiwe fulani ambalo lilikuwa limekaa kama bakuri).

Basi baada ya kukaa hapo akaanza kunichanja kwa kisu kilichokuwa kikali mithili ya wembe,amenipiga chale za kutosha karibia mwili mzima.Baada ya kumaliza lile zoezi nikatakiwa nikae kwanza uchi ili niendelee kukauka kisha ndipo nikatakiwa kuvaa nguo.Sasa baada ya kuwa nimemaliza kuvaa nguo ndipo mama yake na Monica na wale kina mama wakaanza kuzungumza na mimi,kile kitendo kilikuwa ni kitendo cha haraka sana ambacho hakikuchukua hata saa nzima!.

Mama Monica "Mkwe wangu hujambo mwanangu"

Mimi "Sijambo mama,shikamoo"

Mama Monica "Maraba mwanangu"

Mama Monica "Baba huu ulimwengu una watu wabaya sana,lazima tukulinde mwanangu".

Basi mimi nikawa nimetulia tu sikusema jambo lolote,mama yake Monica akaanza kuongea na mwanaye kisukuma na nadhani alimwambia aniambie kilichokuwa kinaendelea!.

Monica "Umughaka dhumuni la mimi kukuleta huku kama nilivyokwambia ni kukulinda mpenzi wangu,sitaki baya lolote likukute kwasababu nakupenda na wewe ndiye mama yangu anataka unioe!"

Aliendelea "Unakumbuka kile kishindo cha jana kilichofanya mpaka ukakimbia?"

Mimi "Ndiyo,nakumbuka!"

Monica "Basi yule mtu alikuwa ametumwa na baba yake ili waje kukuchukua,ndipo nikamuwahi kupambana nae kabla hajaleta madhara,sasa aliponizidi nguvu nilimuita mama yangu akaja kunisaidia na akawa ameondoka naye"

Aliendelea "Sasa lile jambo limeleta shida kwa huyo mshirika mwenzao na mama na kuna vita inaendelea"

Kiukweli nilikuwa nimekodoa macho huku nikiendelea kusikiliza kinaga ubaga ile stori ya Monica ambayo nilikuwa hata siifahamu.

Monica "Kuna mzee mmoja ambaye naye jana alikuwa akicheza ngoma na hutoweza kumfahamu,sasa yule mzee kumbe wakati wakiwa kule miembeni alimuagiza mwanaye aje akuchukue akupeleke kwake wakakufanyie michezo yao".

Aliendelea kusema "Sasa baada ya yule mzee kuona mwanaye amedhibitiwa alikasirika sana na mama anasema walikaa kikao wakamtaka atoe sadaka kwa kufanya lile jambo kwa mshirika mwenzie".

Monica "Sasa yule mzee alisema kwa wenzie kwamba anataka aisambaratishe nyumba ya mwalimu na lazima awapeleke mbele ya kamati iliyomuagiza sadaka nyinyi nyoote ingawaje alitumwa mtu mmoja tu kama fidia"

Sasa baada ya kusema yale maneno nilishituka sana na ndipo akili yangu ikafunguka kwa haraka sana!,kwa haraka nikamuwaza uenda atakuwa ni mzee makono kwasababu ndiye niliyekutana naye akawa amenipa vitisho vingi kuhusu tulichomfanyia mwanaye!,pia nikajua uenda atakuwa ndiye maana usiku nae alikuwa miongoni mwa wacheza ngoma pale kwao Monica!.

Mimi "Kuna mzee mmoja anaitwa Makono,je mama mnamfahamu?"

Baada ya kuuliza vile lile swali wakashituka sana na mama yake Monica akaniambia "Unamjua mzee Makono?"

Mimi "Ndiyo mama"

Mama yake Monica "Ndiyo huyo huyo anataka kukutoa sadaka mwanangu,sitakubali!"

Basi wakaanza kuzungumza kwa kisukuma huku wakionekana kusikitika!.

Mimi "wakati natoka senta nimekutana naye jioni akanitisha sana kuhusu mwanae"

Mama Monica "Ndiyo maana tumekuleta hapa maanangu tukutengeneze vizuri,huyo makono ni mtoto mdogo sana kwetu,nitamshughulikia".

Basi kwakuwa hali haikuwa nzuri siku hiyo kutokana na Makono na genge lake kupanga kwenda kufanya uhalifu wa kichawi pale nyumbani,mama yake Monica na wale kina mama wakaniambia leo sipaswi kabisa kukanyaga pale nyumbani na nitalala hapo kwa hao kina mama mpaka asubuhi!.

Mimi "Je sitaonekana"

Mama Monica "Baba hapa ni kiboko,hakuna wa kukanyaga hapa"

Aliendelea "Tumekupika na hakuna wa kukusogelea na hata wakija hakuna wa kukuona,ondoa shaka mwanangu"

Mama Monica "Huyu huyu makono tuliyemfundisha kazi anataka kuniulia mwanangu na mkwe wangu?,atanijua mimi ni nani,nitamuaibisha mpaka atajuta"



-/-/-/-/-/-/-/-/-/-/-/-/-/-/-/-/-/-



SEHEMU YA - 19.


Kiukweli nilikuwa nimechukia sana namna nilivyodharirishwa pale shuleni mbele ya wanafunzi!,sikutaka kuonekana mkorofi na mkaidi,nilifanya kila nilichoambiwa ili mambo mengine yapite!,niliona angalau Ba'mdogo aniadhibu kuliko taarifa za kulala nje ningemfikia baba yangu hakika angeniua kwa kipigo na shule angeweza kuacha kunisomesha nikawa mchunga ng'ombe!.Japo nilifanya kosa la kulala nje bila taarifa lakini nilidhani ile adhabu ya kudharirishwa haikufaa hata kidogo na ilijaa uonevu mkubwa!.

Basi nilianza kutembea kutoka hapo Senta kuelekea nyumbani huku kile kichwa cha cherehani nikiwa nimejitwisha kichwani,kiukweli nilichukia sana lakini niliamua kujikaza mtoto wa kiumwe,niliamini hayo ni mambo ya kawaida tu na yangepita!.Kile kichwa cha cherehani hakikuwa chepesi kama nilivyodhani na ilipelekea nikawa nafika sehemu najitua kichwani nashikiria kwa mikono miwili lakini bado haikusaidia,kwahiyo nilichokifanya ilikuwa nakiweka begani angalau nikawa naona kuna unafuu!

Nilifika nyumbani nikiwa nimechoka sana na kwakweli kuanzia siku hiyo,mimi na Ema tulikuwa kama Paka na Panya,sikutaka kabisa jamaa aniambie chochote wala kunisogelea kwasababu nilimuona ni mnafiki!,mara kibao tu yeye nilikuwa nikimtunzia siri zake lakini jamaa yeye za kwangu hakutaka kabisa kuziweka moyoni.Kitendo cha kumwambia Ba'mdogo nilikuwa natembea na binti Monica tena mbele ya wanafunzi kilifanya nikamchukia sana jamaa!,na nilichoamua ni kwamba kama mbwai na iwe mbwai!.

Haikupita muda Maza mdogo naye akawa ametoka senta,kama kawaida yeye alikuwa akitoka senta alikuwa anaingia kuoga na kusubiri kula,wa kupika sana sana nilikuwaga mimi maana Ema nae alikuwa anajifanya kusoma kila alipokuwa akitoka shule,sasa nilikuwaga najiongeza tu kuingia jikoni kupika ili kuepuka matusi ya Ba'mdogo.
Siku hiyo nilikuwa nimechoka sana na nilikuwa nanuka jasho kwasababu ya zile kazi kuanzia asubuhi hadi ile usiku lakini sikuweza kuyasogelea maji kwasababu niliambiwa na Monica na akanionya nisiguse maji!.

Siku hiyo nililala kwa uchovu sana,namshukuru Mungu palipo pambazuka niliamka nikajiandaa kuondoka zangu senta,sasa nilichofanya nikupiga mswaki tu na kubadili nguo,sikutaka kabisa hata kunawa uso,nilipomaliza niliingia ndani kuwasalimia Headmaster na mkewe!.

Maza mdogo "Wewe unaenda halafu hicho kichwa cha cherehani nani atakipeleka?"

Nikawa kimya kwa muda huku nikiwa natafakari nini cha kujibu!.

Headmaster "Kwani kichwa cha cherehani sikuhizi unakileta nyumbani?"

Maza mdogo "Juzi sinilikwambia wanasema yule mama Mayala aliwahi kuibiwa kichwa cha cherehani pale kibandani kwake,unadhani chanzo cha Mama Mayala kuacha kushona ni nini?"

Headmaster "Sasa kwanini usiwe unamuomba mama Rebecca unakiacha pale nyumbani kwake kuliko kupata kazi ya kukileta huku!".

Maza mdogo "Ngoja nitajaribu kuongea nae!".

Headmaster "Wewe nenda uwahi kwenye shughuli zako bhana!"

Maza mdogo "Sasa nani atanisaidia kukipeleka senta"

Headmaster "Utakamata hapo mwananfunzi akusaidie"

Sasa mimi sikutaka kabisa kuonekana uenda nilichukia kukibeba kile kichwa,niliamua kujikaza na kumwambia ningekifata baada ya kupeleka miwa senta.

Mimi "Haina shida mama ngoja nikachukue miwa nipeleke senta halafu narudi kukichukua".

Maza mdogo "Sawa,uwahi sasa"

Sasa nilidhani uenda Headmaster alivyokuwa amemshauri ya kwamba angekamata pale shuleni mwanafunzi amsaidie kubeba kile kichwa na kukipeleka Senta angekubaliana nae lakini haikuwa hivyo,kitendo cha kuniambia niwahi kurudi kukibeba ilionyesha kabisa alifurahishwa na mimi kwenda senta na kurudi kukibeba!.Basi sikuwa na hiyana mtoto wa kiume nikaondoka zangu kuelekea kwenye mashamba ya mzee Masumbuko kwa ajili kufata miwa kama kawaida,ingawaje miwa iliyokuwepo haikuisha ila niliona ni heri nikakusanya ikawa mingi ili inipunguzie safari ya kila siku kuamka asubuhi na mapema kisa kuwahi miwa!.

Nilipofikisha ile miwa pale senta niliibwaga chini nikaondoka zangu kurejea nyumbani kwa kukimbia ili kuwahi kurudi!,sasa kuna sehemu nilifika nikamuona dogo mmoja akiwa kwa mbele kabeba kile kichwa cha cherehani huku Maza mdogo akiwa nyuma yake,nilipowafikia nilimwambia dogo anipe kile kichwa nimsaidie na yeye arudi shule!.

Nilijifanya kuchangamka na kutabasamu kiunafiki lakini kiuweli nilikuwa nimechukia sana,nikawa najiuliza kama alikuwa anajua angempatia mwanafunzi amsaidie kubeba kwanini alitaka nirudi tena?,kama kawaida yangu sikutaka maneno na mtu nikaamua kufunga bakuli langu ili mwanaharamu apite.Wakati huo kiukweli nilikuwa nimeanza kupoteza nuru ya muonekano wangu kwasababu ya kushinda kule senta wakati mwingine sili kabisa mchana na chakula nilikuwa nakutana nacho usiku tu!,mara nyingi nikiwa pale senta nilikuwa nashindia sana miwa!.

Tulifanikiwa kufika senta na nikakipeleka kile kichwa kwenye kibanda alichokuwa akishonea na mimi kwenda mpaka kwa yule mama ambaye nilikuwa nikilaza ile miwa,niliichukua nikaenda kuinganisha na ile niliyokuwa nimekuja nayo na kuanza kuuza!.Namshukuru Mungu siku hiyo niliuza sana ile miwa,japo haikuisha lakini mpaka kufika mida ya saa 10 alasiri ikawa imepungua kwa kiasi kikubwa!
Sasa nikiwa naendelea kuuza miwa yangu pale,kwa mbali nikamuona yule binti Mwise akiwa na binti mmoja wakiwa wamevaa sketi za shule na tisheti za kawaida wakiwa wanakuja hapo senta, sikufahamu kilichokuwa kimewaleta uenda walifata mahitaji kama watu wengine!.

Yule binti kiukweli ndiye alikuwa binti wa kwanza kwa hapo kijijini kuumiza na kuutesa moyo wangu,nilikuwa nampenda na kumtamani sana kutokana na shepu yake nzuri!,ila baada ya kuanza kutembea na Monica kiukweli upendo na matamanio yangu kwake yakaanza kupungua kwa kasi ya ajabu!.Walipofika karibu waliingia kwenye duka moja wakanunua kilichowaleta kisha wakatoka wakawa wanaelekea kwenye vibanda na maduka ya mbele ambako huko pia ndiko mama mdogo anakofanyia shughuli zake,sasa baada ya kugeuka na kutazama uelekeo niliokuwepo mimi,nikampiga mkono kwa ishara ya kwamba aje!.

Mwise "Narudi!"

Kwakuwa aliniambia anarudi nikasema ngoja nisubiri.Safari hii sikutaka kabisa kuwa na kimuhe muhe kwasababu sikuweza kujificha na ile biashara yangu na yeye alifahamu kabisa nilikuwa muuza miwa!,niliamini kama ni kumpata basi ningempata tu na kama ni kumkosa basi ningemkosa vilevile!.

Haukupita muda wakawa wanarudi na huyo mwenzie,sasa alipofika pale kwenye eneo langu la biashara akaanza kama kuonyesha nyodo na dharau.

Mwise "Nionjeshe muwa rafiki yangu!"

Mimi "Kwahiyo mimi leo nimekuwa rafiki yako?"

Mwise "Jamani!,kwani kuna ubaya wewe kuwa rafiki yangu?"

Basi nikamkatia pingili mbili za muwa yeye pamoja na mwenzie!,basi wakawa wanazungumza na huyo rafiki yake maneno ya kisukuma huku wakicheka kwa kicheko cha kichini chini!,kiukweli walikuwa wanikiteta kwa kisukuma na ishu kubwa walikuwa wakizungumzia zile stiki nilizokuwa nimelambwa na Headmaster mbele ya wanafunzi!,wao walidhani siwaelewi lakini hata kama sikuelewa kisukuma vizuri mtu alikuwa akiteta inafahamika kabisa!.

Walipomaliza kukwangua kwangua miwa kwa kisu akawa ameniambia wanaondoka kuwahi kurudi nyumbani,nikawa nimemuomba anivumilie angalau kwa dakika mbili nizungumze nae!,sasa yule mwenzake akawa amemwambia atamkuta mbele!.

Mwise "Sasa na wewe unaniacha nyanoko"

Mwenzie "Utanikuta mbele bhana"

Mwise "Mmh!,niambie mi nina haraka"

Mwise "Kwahiyo Mwise Ombi langu vipi lakini?"

Mwise "Ombi gani tena jamani"

Mimi "Kwani mara ya mwisho mimi na wewe tuliongea nini?".

Mwise "Siulianimbia unanipenda,nashukuru kwa kunipenda"

Mimi "Usinifanyie hivyo Mwise"

Mwise "Wewe si unaye mwanamke wako"

Mimi "Mwanamke gani tena jamani!?"

Mwise "Wewe ema kaniambia habari zako nyingi tu!,kumbe ulikuwa tu unataka unilale uniache"

Mimi "Daaah!,hebu achana na mambo ya Ema Mwise,Ema anashida kubwa na wewe yule unamfahamu akili yake".

Mwise "Mimi nachelewa bhana,kesho!"

Basi yule binti alianza kukimbia kumfuata mwenzie aliyekuwa akimsubiria.Niliamini kabisa kwa kilichotekea pale shule ukichanganya na uongo wa Ema,haikuwa rahisi mimi kumpata tena yule binti.Niliamua kujipa moyo ya kwamba mademu mabaya siku zote ndiyo yanayoringa lakini kuna muda bado nilikuwa nikifikiria kiuno cha yule binti na kuwaza kinavyo chakatwa na wanaume wengine,kiukweli nilikuwa naumia sana!.

Sikuwa na namna ilibidi niwe tu mpole ili maisha yasonge!.

Baada ya kukamilisha siku ya uuzaji wa miwa niliamua kurudi nyumbani na namshukuru Mungu safari hii sikurudi na kichwa cha cherehani kwasababu maza mdogo alipata pa kukiweka hapo senta.

Sasa nilifika nyumbani mida ya saa 1 usiku,nilielekea lamboni ile usiku kuchota maji ili nije nioge kwasababu nilikuwa sijaoga tangu jana yake!,sasa nilipotoka bafuni kuoga,nikawa nimeingia ndani kwa ajili ya kupaka mafuta!,sasa wakati napaka mafuta nikasikia kuna mtu ananipiga piga mgongoni kwa mkono akiashiria nigeuke!,sasa ile nimegeuka nikawa nimekutana na Monica uso kwa uso!.

Kiukweli nilishituka sana ila akanifanyia ishara ya kidole mdomoni akinitaka nisipige kelele wala kuongea!.

Mimi "Monica kuna nini mbona huko humu"

Monica "Vaa nguo tuondoke"

Mimi "Tuondoke twende wapi tena!?"

Monica "wewe vaa twende"

Mimi "Tunarudi lakini?,maana mwenzio jana jana nimepigwa kwasababu yako"

Monica "Hatuendi mbali tutakuwa nje hapo"

Basi baada ya kuvaa nguo,Monica akawa amenishika mkono na ghafla tukawa nje ya nyumba kwa pembeni kidogo.

Monica "Tusogee pale kwenye lile jiwe!"

Baada ya kufika pale kwenye lile jiwe akanitaka tukae pale na kuna watu tuwasubiri walikuwa wanakuja!.



-/-/-/-/-/-/-/-/-/-/-/-/-/-/-/-/-/-



SEHEMU YA - 20.


Basi wakati tukiwa tumekaa pale kwenye lile jiwe,ghafla wakawa wametokea wale kina mama wawili ambao juzi yake tu nilitoka kwao kupigwa chale!.Walifika pale kwa ghafla sana na wakanitaka nisimame!.Baada ya kusimama, mama mmoja wapo akaniambia nivue nguo ili nipakwe dawa,sikutaka kabisa kupoteza muda nikaanza kuvua nguo na wakaanza kunipaka dawa kwa haraka sana!.Walipomaliza wakawa wamekaa kimya kwa muda kidogo.

Mimi "Kwani kuna nini?"

Monica "Shiiiiiiiiiiii,nyamaza"

Monica alinifanyia ishara ya kidole mdomoni kwamba ninyamaze na aliniambia kwa sauti ndogo sana.Sasa baada ya muda kidogo kupita mama mmoja akamwambia Monica kwa kisukuma aniambie kila kitu!.

Monica "Mpenzi wangu umughaka,unaniamini?"

Mimi "Ndiyo,nakuamini"

Monica "Sasa hawa mama zangu wadogo siunawakumbuka?"

Mimi "Ndiyo,Hawa si ndiyo wale wa juzi?"

Monica "kumbe una kumbukumbu,sasa ni hivi!,mama yangu kawatuma kuja kukusaidia maana kuna kikao kilikuwa kinaendelea kwa yule mzee mshenzi(Makono)na washirika wenzie ya kwamba leo unapaswa ufe!"

Mimi "Kwanini nife Monica!?".

Kiukweli nikaanza kupaniki na amani ikaanza kunitoweka!.

Monica "Yule mzee nilikueleza alipewa adhabu ya kutoa kafara kwasababu alivunja mashariti ya kumtuma yule mwanaye pale nyumbani kwetu akifahamu kabisa mama yangu ni mmoja wapo,sasa hasira zake amehamishia kwangu na kwako,hivyo ndiyo maana nilikwambia nitakulinda usiku na mchana mpenzi wangu!"

Mimi "Kwahiyo tutakaa hapa mpaka asubuhi hawezi kutuona?"

Monica "Hapa tunamsubiri mama afike kwanza atupe maelekezo"

Mimi "Sawa"

Tulikaa pale kwenye yale mawe mimi na Monica wakati huo wale kina mama wakiwa wamesimama!.Haukupita muda ghafla mama yake Monica akawa amefika pale tulipokuwepo.Monica alisimama akamuinamia mama yake kwa heshima na unyenyekevu ikiwemo pia wale kina mama.

Mama Monica "Mwanangu hujambo?"

Mimi "Sijambo mama,shikamoo"

Mama Monica "Marhaba mkwe wangu"

Mama Monica "Sasa hebu shika hii"

Alinipatia kitu kama kibuyu kidogo sana ambacho sikuelewa ndani kulikuwa na kitu gani!.

Mama Monica "Nenda ndani utakiweka pembeni ya mlango chumbani unapolala,sawa?"

Mimi "Sawa mama"

Mama Monica "Ukishaweka hurudi hapa,fanya haraka".

Niliondoka kuelekea ndani ambako nilipofika sikumkuta mtu nje!,basi niliingia ndani nikakiweka kile kibuyu kisha nikatoka nje!,sasa nadhani baada ya kuurudishia ule mlango Headmaster alisikia.

Headmaster "Wewe leo huli?"

Mimi "Nakuja kula baba"

Maza mdogo "Njoo uchukue hili bakuli ukaongeze mboga umughaka"

Basi niliamua kwenda sebuleni na nikawakuta wakiwa wanakula!.Nilichukua lile bakuli nikaingia jikoni kupakua mboga kisha nikarudi sebuleni kula haraka ili niondoke niende kwa mama yake Monica aliyekuwa ameniambia niwahi kurudi!.

Maza mdogo "Uliondoka saa ngapi leo!,nimewahi kufunga ili tuongozane sikukuona"

Mimi "Mimi niliwahi mama baada ya kuona giza limeanza"

Headmaster "Kwani ulikuwa wapi?,mbona mwenzio anasema hukuwepo?"

Mimi "Nilikuwa hapo nje baba"

Headmaster "Mbona tumekuita na hukuitika?"

Mimi sikutaka kujibu kitu nikaamua kukaa kimya ili kuepeusha mambo mengi!.

Headmaster "Biashara inakwendaje?"

Mimi "Leo angalau kidogo nimeuza uza"

Kiukweli wakati huo nilikuwa naona kama wananichelewesha kuondoka kwenda nje,baada ya kupiga matonge kadhaa ya ugali nikaamka nikasema nimeshiba!.

Headmaster "Leo ulikula wapi bhana"

Mimi "Sijala sehemu baba nahisi kushiba".

Headmaster "Hivi mchana huwa unakula wapi?"

Mimi "Huwa nashindia miwa tu pale kijiweni".

Headmaster "Aya bhana"

Niliamka nikanawa kisha nikatoka nje kujifanya kama najikoholesha pale kisha nikafungua mlango na kutoka nje ya nyumba.Nilitembea kwa haraka kuelekea nilipokuwa nimewaacha kina Monica,nilipofika nilimkuta Monica akiwa peke yake,wale kina mama pamoja na mama yake Monica sikuwaona.

Monica "Ila wewe nae kuna muda unakera sana"

Mimi "Sasa nakera nini Moni!".

Monica "Mama alikwambia uende uwahi kurudi wewe umefika ukaamua kukaa!"

Mimi "Haikuwa rahisi Moni kama unavyodhani"

Monica "Hebu tuachane na hayo,shika hii hapa ulambe na hii uweke mfukoni."

Monica alinipatia kitu kama unga ulokuwa mweusi kama mkaa nikalamba kisha akanipatia kitu kilichokuwa kimefungwa kwa kitambaa kidogo cheusi akanitaka niweke mfukoni.

Mimi "Mama anarudi?"

Monica "Arudi huku kufanya nini?,wao ndiyo wameondoka hivyo!".

Monica "Naomba unisikilize kwa makini umughaka"

Aliendelea "Utakachokiona leo usipige kelele na ikawe siri yako,mimi nipo na wewe na nikizidiwa nitamuita mama atatusaidia"

Mimi "Sawa"

Monica "Twende"

Basi tuliondoka kuelekea ndani ya nyumba yetu nikiwa nimeongozana na Monica,sasa nilipofungua geti kuingia ndani ghafla sikumuona,nikabaki kushangaa tu na kujiuliza atakuwa ameleekea wapi kusiko julikana,sasa kwakuwa nilifahamu alikuwa na uwezo mkubwa niliamini ametoka mara moja na angerudi!.Nilipoingia hapo uwani nilimkuta Ema anafua soksi zake za shule na kufuta futa viatu vyake!,kwakuwa sikuwa na stori nae nikaingia zangu ndani!.

Nilipoingia tu chumbani Ghafla nikamuona Monica akiwa amesimama kwenye ile kona ambayo niliweka kile kibuyu!,alinifanyia ishara ya kunyamaza!.Sasa jamaa alipomaliza shughuli zake aliingia ndani akaanza kusoma,mimi niliamua kujilaza kitandani wakati huo namuona Monica huku Ema yeye akiwa haoni kitu chochote!.Sasa baada ya kupiga buku kwa dakika kama ishirini niliona anarudisha madaftari kwenye mfuko kisha akazima ile taa akapanda kitandani kuja kulala!.

Baada ya jamaa kulala,Monica alinisogelea kitandani akanishika mkono akanisogeza kwenye ile pembe aliyokuwepo yeye akanitaka nikae kimya!.

Tulisimama kwa muda mrefu kidogo ndipo nikasikia kuna vishindo hapo uani kama miguu ya watu!,na kwa vishindo vile yaelekea walikuwa watu zaidi ya wawili.Monica akaniambia nitulie tuli kwani hakuna ambaye angetufanya chochote.Kiukweli nilikuwa nina jiamini kupita maelezo kwa wakati huo!.

Haukupita muda nikaona mlango unasukumwa,waliingia watu wanaume wawili waliokuwa uchi ambao sikuwa nikiwafahamu,basi Monica akanitaka nitulie kabisa!,wale jamaa wakaenda mpaka pale kitandani wakawa kama wanashangaa!,basi mmoja akatoka nje,haukupita muda akawa ameingia na mzee mmoja ambae nilimfahamu alikuwa yule mzee makono!.

Yule mzee alisogea mpaka pale kitandani kisha nikaona anaangalia kwa kushangaa na yeye pia!.

Jamaa "Ndiye huyu?"

Makono " Siye huyu"

Makono "Mchukueni huyu tuondoke"

Basi nikaona wale jamaa wanamuamsha Ema akaamka,Ema aliamka akiwa kama mlevi aliyepoteza kumbukumbu kabisa!.Walimtoa nje Ema na ndipo Monica akaniambia tutoke nje na nihakikishe kile kibuyu kidogo alichonipatia mama yake nakibeba!,basi tulipotoka nje tukakutana na grupu la watu wengine kama watano akiwemo Headmaster ambao walikuwa kama wamewelewa pombe na hawakuelewa kitu chochote!.

Wale jamaa wawili mmoja alikaa mbele na mwingine nyuma huku wa mbele akitoa ishara kwamba waondoke,sasa yule wa nyuma alikuwa akiwapiga wale watu akiwemo Headmaster na walisimama wakatoka nje!.Sikumuona tena mzee makono hapo nje kwa wakati huo na sikufahamu alikuwa amekwenda wapi!.

Monica "Twende"

Mimi "Tunaenda wapi?"

Monica "wewe twende"

Basi tukaanza kuwafatilia wale watu wakiwa wanapelekwa kusiko julikana!.



-/-/-/-/-/-/-/-/-/-/-/-/-/-/-/-/-/-




SEHEMU YA - 21.


Safari ikazidi kusonga kuelekea kusiko julikana.Ilikuwa muda wa usiku sana na giza lilikuwepo kiasi,kiasi fulani kulikuwa na nuru ya mbala mwezi.Tulitembea tukiwafuata wale watu ambao mpaka wakati huo hawakufahamu kama tulikuwa nyuma yao!.
Sasa kuna mahali walifika yule wa mbele akampatia mwenzie aliyekuwa nyuma ishara ya kwamba inapaswa wasimame,waliposimama pale kwa muda ndipo kuna watu wengine ambao nilipowahesabu walikuwa ishirini,sasa ukijumlisha na wale wa lile kundi la kwanza ambao walikuwa wa tano akiwemo Headmaster pamoja na Ema,jumla yao ilifanya kundi lote la watu kuwa ishirini na tano.Basi ndipo nikamuona yule mzee Makono akiwa kwa mblele akiongoza jahazi huku akiendelea kuimba nyimba za kisukuma na wenzie kuitikia.

Baada ya safari ya muda mrefu ndipo sasa tukafika kulipokuwa na mashamba yaliyokuwa yamepandwa mtama,ule ulikuwa mtama kwasababu nilikuwa ninafahamu namna mahindi yalivyo na mtama ulivyo hata ukiwa bado haujakomaa,kwahiyo sikuwa na shaka kabisa kwamba lile lilikuwa shamba la mtama kwasababu pia lilikuwa shaghala baghala,tofauti na mahindi yanayopandwa kwa kuacha nafasi na kwa mstari!.Walipofika hapo mzee makono alipiga mruzi kama vile anachunga ng'ombe.
Basi wale jamaa waliokuwa wakimsaidia ile kazi walikimbia kuelekea mbele ambapo walianza kuwapanga wale watu na kuwapa majembe,majembe yale hayakuwa kama haya ambayo sisi tunalimia kawaida,yale yalikuwa kwa mbele yamechongoka kama Mundu!.Baada ya kukabidhiwa yale majembe kila mtu alikuwa akipewa ishara na kuanza kulima kwa spidi kali mno!.

Hakuna jambo ambalo mpaka leo siwezi kusahau kama lile la watu kulimishwa kichawi huku nikiwa nashuhudia kwa macho yangu,miaka ya nyuma kwa stori za vijiweni nilidhani yawezekana ikawa tu stori watu wanajitungia lakini baada ya kushudia mimi mwenyewe ndipo nikaamini kwa hakika uchawi upo na unafanya kazi kubwa mno!.Kwa spidi ile waliyokuwa wanatumia wale watu kiukweli haikuwa ya kawaida!.Niliendelea kumtazama Headmaster na Ema wanavyohenyeshwa kuna muda huruma iliniingia sana lakini sikuwa na nmna!.

Kutokana na ule udharirishaji wa Ba'mdogo mbele ya wanafunzi niliona kabisa anachokipata ndicho anachokistahili,ningeweza kumwambia Monica amwambie mama yao awasaidie lakini niliona ngoja wapitie shubiri,kwa upande wa Ema sikuwa kabisa na huruma nae na nilitaka amenyeke kishenzi maana alikuwa na mdomo mrefu sana!.

Monica "Huyo ndugu yako juzi nilimwambia akajifanya mjanja,ngoja wamfundishe adabu"

Mimi niliendelea kutulia na kujionea mwenyewe huku moyoni nikifurahia kupendwa na Monica maana isingekuwa hivyo na mimi uenda ningekuwa ni miongoni mwa wahenyeshwaji!.Wale watu walipalilia lile shamba bila kupumzika hata kidogo!.

Mimi "Hivi hawachoki?"

Monica "Unataka ukajaribu?"

Mimi "Hapana,mi nimeuliza tu!"

Monica "Hapo hakuna kuchoka,utaenda kuchoka huko kwako lakini hapo hauchoki"

Basi tuliendelea kutazama lile shuruba walilopata wale watu na kiukweli hakukuwa na huruma hata punje!.

Baada ya muda mrefu kupita,ndipo nikasikia tena mruzi unapigwa kwa nguvu!,alikuwa ni yuleyule mzee makono akatoa ishara ya kwamba wamemaliza lile eneo na kilichofuata ni kuhamia eneo jingine ili kazi ya kulima iendelee!.Lile zoezi lilimaliza kukiwa kunakaribia mapambazuko kabisa!.

Monica "Tuondoke"

Mimi "Nyumbani?"

Monica "Nikurudishe kwenu niwahi kwenda kulala".

Mimi "Wamemaliza"

Monica "Pakishapambazuka kama hivi hakuna ujanja,watawarudisha tu"

Basi tukaondoka lile eneo mpaka nyumbani,tulipofika nyumbani Monica hakutaka kuondoka na akanitaka kile kibuyu nilichokuwa nimekishika nikiweke pale pembezoni ya mlango kama ilivyokuwa mwanzo na akanitaka nisimame nae pale ukutani mpaka Ema na Ba'mdogo watakaporejeshwa!.

Basi haukupita muda kuna jamaa aliingia na Ema mpaka ndani akawa amemlaza pale kitandani!,sasa ile jamaa anataka kutoka ni kama alikuwa na mashaka sana akaanza kuangaza chumba kizima lakini hakuona chochote!,ndipo akawa ametoka nje!.Sasa wakati Monica anataka kutoka pale tulipokuwa akanibana tena na kunitaka nitulie kimya kabisa!,mara ghafla aliingia mle chumbani mzee makono na yule jamaa aliyemlaza Ema pale kitandani!,walijaribu kuangaza chumba kizima lakini mzee makono nikaona ni kama alikuwa na mashaka!,basi wakazungumza na yule jamaa kisukuma kisha wakawa wametoka nje!.Kiukweli niliingiwa uoga na hofu kubwa mno!.

Mimi "Hawajatuona kweli?"

Monica "Hivi unamjua mama yangu au unamsikia?"

Aliendelea "Mama ndiye mkubwa hata huyo mzee haoni ndani,mama hajawahi kushindwa!"

Monica "Hivi Umughaka huwa huniamini ninapokwambia nitakulinda?,wala hakuna anayeweza kutuona hapo,hao ni wadogo sana mbele ya mama"

Baada ya kunihakikishia hivyo kiukweli sasa moyo wangu ulipata amani!.

Monica "Mimi naondoka,nikuombe usimuamshe huyo ndugu yako mpaka atakapoamka mwenyewe"

Aliendelea "Jioni nitakuja kukuchukua,Bibi yangu aliyemzaa mama anakuja na mama alisema nije kukuchukua nikakutambulishe".

Mimi "Sawa"

Baada ya kuniambia hivyo akawa ametoweka,nilimuitikia kishingo upande nilakini moyoni sikutaka kabisa kwenda kwao maana niliogopa viboko na adhabu ya Ba'mdogo,sikuwa na namna ilibidi niwe mtumwa wa penzi la Monica,ingawaje kuna muda niliona kabisa ananipenda na ndiyo maana mimi sikupata taabu na shuruba za wachawi pale kijijini,zile feva zilifanya nikampenda sana Monica!.

Baada ya Monica kuondoka na kile kibuyu ndipo nilivua zile nguo nilizokuwa nimevaa nikaavaa nguo nyingine na kupanda kitandani!,sasa nilipopanda kitandani ndipo kumuangalia Ema miguuni nikakuta bado anatope la shambani!,sasa sikufahamu ndiyo ulikuwa utaratibu wao au walijisahau kuwaosha au waliwaacha vile kwa kusudi la kuwakomoa,nilipanga lile swali ningeonana na Monica nimuulize!.Muda huo ilikuwa saa 11 alfajiri,sikuweza kabisa kulala niliamua kushuka kwenye kitanda na kwenda kukaa kwenye kiti.
Siku hiyo sikuwa na haraka kabisa ya kwenda kufata miwa nilitaka Ema aamke nione ataniambia nini!.Sasa ilipofika saa 12 asubuhi jamaa bado alikuwa amelala huku akiendelea kujigeuza geuza kitandani akichafua shuka na yale matope!.

Nilichukua mswaki nikaanza kusukutua na kunawa uso hapo kando ya bafu!,sasa wakati nikiwa ndani nilimsikia Maza mdogo akiita "Emaaaa....." wewe Emaaaaa".

Baada ya kuona aliyekuwa anamuita haitikii akaanza kuniita "Umughaka!"

Mimi "Naaam"

Basi nikaenda nikafungua mlango wa sebuleni ambao mara zote ulikuwaga unarudishiwa tu kwakuwa haukuwa na komeo!.

Mimi "Mama shikamoo"

Maza mdogo "Marhaba"

Aliendelea "Hebu ingia"

Mimi "Wapi mama,huko?"

Maza mdogo "Ndiyo,njoo"

Basi nikausogelea mlango nikagonga ndipo mama mdogo akaja kunifungulia!.

Maza mdogo "Hebu muangalie baba yako mdogo"

Basi nilipomtazama dingi mdogo miguuni pia alikuwa na tope la kufa mtu!.

Mimi "Amelitolea wapi?"

Maza mdogo "Mi sijui kwakweli,hii nyumba mbona kila siku maajabu hayaishi!".

Mimi " Kwani Ba'mdogo hakutoka kweli?"

Maza mdogo "Huyu usiku kucha nimelala nae hapa,atoke usiku aende wapi?"

Niliamua kukausha na sikutaka kabisa kufungua domo langu na kumueleza mtu jambo lolote!.,Pengine ningewaambia kwa makusudi mema tu lakini nikaogopa wasije kunituhumu na mimi ni mshirikina!.

Maza mdogo "Baba Mary......wewe baba mary"

Maza mdogo "Amka basi"

Ba'mdogo aliendelea kujigeuza kana kwamba yuko kwenye godoro la sita kwa sita kumbe kigodoro chenyewe kilikuwa kidogo tu cha kusukimia maisha pale kijijini!.
Basi mimi ilibidi nitoke nje ili niwache wao humo ndani wakiendelea kuamshana!.Sasa nilipoingia chumbani kwetu nilikuta Ema akiwa ameshaamka na miguuni hakuwa na tope,inaonekana wakati mimi nikiwa kule chumbani kwa Headmaster yeye baada ya kuamka alienda kunawa,hata lile shuka lililokuwa limechafuka alikuwa amelitoa na ametandika shuka jingine!.

Sasa nikasubiri aongee jambo lolote lakini jamaa akapiga kimya,pengine alidhani uenda sifahamu chochote,kimoyo moyo niliona kabisa hata ile adhabu aliyokuwa amepewa ilikuwa ndogo kutokana na namna alivyokuwa na kiburi!.

Haukupita muda ba'mdogo naye akawa ameamka kutoka chumbani kwake akawa ametoka nje!.

Ba'mdogo "We Umughaka"

Mimi "Ndiyo ba'mdogo"

Nilitoka nje kuona alichokuwa ameniitia.

Ba'mdogo "Huyo yuko wapi?"

Mimi "Yupo chumbani Baba"

Mimi "Ema"

Ema "Eeenh"

Mimi "Njoo unaitwa"

Ba'mdogo "Hivi na nyie mmefanywa hivi kama mimi?"

Wakati Ba'mdogo anazungumza alikuwa akizuonyesha miguu yake iliyokuwa imejaa matope.

Mimi "Hapana baba mimi kwangu sijaona"

Ema "Hata mi kwangu sijaona"

Hapo ndipo nikajua Ema anaweza asiwe na akili timamu,yaani alidhani mimi sijamuona miguuni akiwa na matope!,sasa nilishindwa kuelewa kwanini alikuwa akificha,hiyo yote ni kwamba alidhani mimi nitamcheka na kwenda kumtangaza!,kiukweli nilibaki namshangaa!.Sasa nikawa najiuliza lile shuka atalifuaje?,nilibaki kumshangaa tu kiukweli!.

Ba'mdogo "Haya mambo hapa kijijini yameshakuwa ya kawaida na tukijaribu kuyasema hatueleweki"

Aliendelea "Yule mzee nae akaja hapa nikampatia mpaka hela lakini hamna alichokifanya"

Sikutaka kabisa kusema jambo lolote,mzee aliyekuwa akimsema ni yule ambaye wakati wa kuchezwa ngoma pale kwao Monica alishapewa adhabu na kuliwa kabisa!.

Ba'mdogo "Nataka nifanye tukio kubwa hapa kijijini kwa hawa washenzi ndipo niondoke"

Ba'mdogo "wao si wanajifanya wajanja!,ngoja uone"

Basi baada ya tafakari na kushangaana pale kila mtu aliendelea na mambo yake,mimi kama kawaida sikutaka kupoteza muda nilielekea kuchukua miwa.




-/-/-/-/-/-/-/-/-/-/-/-/-/-/-/-/-/-





SEHEMU YA - 22.


Baada ya kufika senta niliendelea na biashara yangu ya uuzaji wa miwa kama kawaida!,sasa ilipofika jioni muda ambao wanafunzi walikuwa wametoka shule,nilimuona Mwise siku hiyo tena akiwa na marafiki zake wakiwa wanakuja hapo senta,safari hii sikutaka kabisa mazoea na mtoto wa mtu,niliamua kuuchuna na sikuwa na shobo nae kabisa!.Sasa yeye alidhani uenda ningemuita ila mwanaune niliamua kula buyu la hatari!,alikuwa anajiangalisha kwangu lakini kila nikimcheki kwa jicho la kuibia najifanya kupiga stori na jamaa yangu aliyekuwa akiuza kata mbuga.

Walipo maliza kufanya kilichokuwa kimewapeleka hapo senta waliondoka huku mimi nikijifanya niko bize kipiga stori na jamaa lakini kiukweli moyo wangu ulikuwa unauma sana!.Siku hiyo mama mdogo hakuka kabisa hapo senta na sikufahamu sababu ni nini!.

Ilipofika jioni mida ya saa 12 nilirudisha ile miwa iliyokuwa imebaki kwa yule mama na mimi kuianza safari ya kurejea nyumbani.Nilifika nyumbani mida ya saa 1 usiku kuelekea saa 2,niliingia jikoni nikachukua dumu la maji nikaondoka zangu kuelekea lamboni kuchota maji ili nije kuoga nijiweke safi kwasababu Monica alikuwa ameniambia angekuja kunichukua!.

Sasa wakati napandisha nyumbani nikakutana na Ema akiwa bado amevaa nguo za shule akiwa na Deborah,mimi napandisha na wao wakiteremsha!.

Deborah "Mambo umughaka"

Mimi "Poa,vp?"

Deborah "poa!,aya baadae!"

Nilipata mashaka kidogo kwasababu haikuwaga tabia ya Deborah nikionana nae kuacha kupiga stori na mimi,sikuumiza kichwa sana maana niliamini mpumbavu Ema atakuwa amenikandia sana kwa demu wake!,kwasababu hata wakati Deborah ananisalimia jamaa alikuwa anajitembeza taratibu huku akinikaushia!.Basi nilibeba zangu dumu nikanyoosha zangu nyumbani!.
Nilipomaliza kuoga niliingia jikoni fasta kupika ili atakapokuja Monica akute nikiwa nimemaliza kila kitu!.Kama nilivyosema hapo awali ya kwamba,kule kwenye kile kijiji kutembea usiku haikuwa shida,shida ilikuwa ni wachawi tu,lakini mambo ya wezi na majambazi hayakuwepo kabisa,kuna matukio machache sana yaliwahi kufanyika kule senta yaliyohusu wezi lakini yalikuwa yakuhesabika na hayakujirudia tena!.

Nilipomaliza kupika nilichukua sinia nikafunika ugali nikauweka mezani,kisha nikachukua mabakuli ya mboga nikapakua mboga kisha nazo nikapeleka sebuleni,sasa niliendelea kuona ndani kwa Headmaster kuko kimya hata mwanga wa taa au tochi haukuonekana!.Nilisogea karibu nikaanza kugonga ule mlango kuwakaribisha kwa ajili ya chakula lakini nikaona kimya!,nilipoangalia vizuri mlangoni nikakuta kuna kofuli,basi niliamini watakuwa wametoka.

Basi nilichukua sahani nikakata ugali wa kunitosha size yangu nikaanza kula!.Nimekula mpaka namaliza si Ba'mdogo wala Maza mdogo aliyerudi,nikakumbuka uenda kwa kuwa ilikuwa ijumaa labda watakuwa wameondoka kwenda mjini,lakini isingekuwa rahisi kwasababu niliondoka kwenda senta nikawaacha hapo nyumbani,halafu pia ile Hiace ya kuelekea mjini ilikuwaga inaondoka saa 12 asubuhi,niliamini uenda watakuwa wametoka tu na walikuwepo hayo mazingira ya kijijini.Kilicho fanya pia kujiuliza uenda wakawa wameenda mbali ni kitendo cha Ema na mpenzi wake Deborah kujiachia usiku ule bila presha!.Nilirudishia ule mlango wa sebuleni nikarudi zangu chumbani kwetu!.

Mpaka inafika mida ya saa 3 sikumuona Ema na nikajua kabisa headmaster na mkewe watakuwa wameenda mbali.Mpaka muda huo sikumuona Monica hivyo nikaamua kujilaza huku nikiwa namsikilizia.

Haukupita muda nikasikia mlango wa nje unagongwa!,nilienda kuufungua ndipo nilikuta alikuwa Monica!.

Mimi "Karibu"

Monica "Ulikuwa umelala mpenzi wangu?"

Mimi "Nimekusubiri sana"

Monica "Nilikuwa napika,nisamehe"

Mimi "Sikunyingine usiwe unagonga bhana utaniletea shida!"

Monica "Unadhani mimi mjinga?"

Aliendelea "Nimejua hawapo ndiyo maana nimegonga"

Mimi "Umejuaje?"

Monica "Twende nyumbani tunachelewa"

Basi niliingia ndani nikavaa viatu nikatoka zangu,nilifunga ule mlango wa chumbani kwetu na komeo lakini sikuweka kufuli!.Ule wa nje nilirudishia tu tukaondoka zetu na Monica.Mara ya kwanza kutembea na Monica ilikuwa ni kutuliza tu uwendawazimu wa abdala kichwa wazi lakini sikumpenda kabisa,sasa kadri siku zilivyokuwa zikienda ndivyo ulikuwa uniambii kitu kwa yule binti wa kisukuma na kiukweli kuna wakati nilikuwa naona ni kwanini nilichelewa kumfahamu maana alikuwa akinijali sana,licha ya kwamba papuchi ilikuwa ni moja ya sababu ya kumpenda lakini sura yake nzuri pia ilinivutia zaidi,alichokuwa amekosa yule binti wa kisukuma ni matako makubwa tu ambayo ndiyo ulikuwa ugonjwa wangu wakati huo,lakini kwingine kote alikuwa amekamilika binti wa watu wala nisimseme vibaya!.

Mimi "Umeambia ulijua hawapo,umejuaje"

Monica "Nishakwambia mpenzi wangu usiwe unauliza uliza maswali,utaelewa tu siku moja"

Aliendelea "Nimemuona ndugu yako wakati nakuja akiwa na mpenzi wake"

Mimi "Umekutana nao?"

Monica "Kuna mahali nimewaona wanaongozana"

Mimi "Nadhani tupite pale kwao Deborah ili nikamuulize kama headmaster ametoka anarudi au harudi maana muda umeenda"

Monica "Ningekwambia lakini unaweza usiniamini,twende ukamuulize!".

Basi tulichepuka na kuacha ile njia kubwa na tukashika njia ya kuelekea kwao Deborah,basi tulipofika Monica alisimama kwa mbali kidogo hakutaka kuongozana na mimi!.

Monica "Nenda utanikuta nakusuniri hapa"

Nilipofika kwenye boma la ile nyumba kwa mbali nikaona taa ikiwa inawaka kwenye kile kinyumba alichokuwa akilala Deborah na nikaelewa watakuwa bado macho!.Basi nilipofika nikasikia watu wakiongea kwa sauti za chini lakini cha ajabu niligonga sana ule mlango bila mtu kutoka wala kuitikia!.Sikutaka kupoteza muda niliondoka zangu kimya kimya kama mtu aliyetengwa na wazazi wake,nilikuwa najiuliza maswali mengi sana nikawa nakosa majibu!.Nilifahamu kabisa Ema atakuwa amemlisha sumu mbaya Deborah kwasababu haikuwa kawaida ya Deborah kunidharau kiasi kile.

Monica "Umemkuta"

Mimi "Nimewasikia kabisa wanaongea lakini wamekataa kuniitikia"

Monica "Huyo ndugu yako anakiburi sana,wewe subiri ajifanye mjanja"

Aliendelea "Baba yako na mama yako mdogo kuna mahali wameenda na wangekuwa wanajua wanajisumbua wangebaki wakatulia"

Mimi "Kwani unajua walipoenda?"

Monica "Tuondoke tunachelewa"

Basi tulitembea kwa haraka kuelekea kwao Monica,jambo lilikuwa ni lilelile la kufika mapema ingawa palikuwa mbali.Sasa nilipofika niliwakuta watu kadhaa wakiwa pale nje wakiwa wamekaa wakipiga stori huku wakiwa wameshaa taa ikiwa juu ya jamvi.

Mama Monica "Karibu mwanangu"

Mimi "Shikamoo mama"

Mama Monica "Marhaba mwanangu,karibu"

Mama yake Monica alinyanyuka kwenye kiti alichokuwa amekaa akawa amenikabidhi nikalie.Basi haukupita muda nikaona Monica anebeba kimeza kidogo anakileta mahali nilipokuwa nimekaa!.Baada ya kuileta ile meza na kuiweka vizuri akawa ameingia ndani ndipo akaja na vyungu akawa ameviweka chini ya meza,alirudi tena akaja na mabakuli akaanza kupakua mboga,kisha akaendea ugali wa udaga na kuukarisha juu ya meza,alinikaribisha kwa kupiga magoti hadi chini!.

Mwanaume nikaanza kula,kumbe nilikuwa nimeachiwa bata ambaye alipikwa kwa ajili ya bibi yake aliyekuwa amekuja kuwatembelea,kwakweli nilikula sana japo nilikuwa nimeshiba maana nilimisi sana nyama ya bata!.Baada ya kumaliza kula mama yake Monica alianza kuongea kisukuma na yule mwanamke mzee ambaye nilifahamu kabisa ni bibi yake Monica kwasababu alikuwa amekwisha kunitonya!.

Mama Monica "Mwanangu,huyu ni mama yangu"

Mimi "Ooh sawa"

Baada ya kuongea na mimi kisha akawa anaongea na bibi yake Monica!.

Monica "Bibi hajui kiswahili ndiyo maana unaona mama anaongea nae kilugha"

Basi tuliendelea kupiga stori za hapa na pale na Monica, sasa muda ulivyozidi kwenda bibi yake Monica akasimana akawa ameingia ndani,nadhani aliingia kulala!.Baada ya kuingia ndani,mama yake Monica alisogeza kiti mahali nilipokuwa nimekaa na Monica.

Mama Monica "Mwanangu kwanza nikupe Pole kwa uliyayaona jana"

Mimi "Aaah mama wala usijali"

Mama Monica "Sasa mwanangu nisikilize kwa makini"

Aliendelea "Niliwahi kukwambia haya yote nayafanya kwa ajili ya binti yangu,nakuomba usije kumuacha mwenzako"

Mimi "Siwezi kumuacha mama"

Mama Monica "Sawa"

Aliendelea "Sasa ila mwalimu anachokifanya si jambo jema,angetulia ningemsaidia"

Mimi "Amefanya nini mama?"

Mama Monica "Maalimu anaenda kwa waganga akitaka kufahamu wanaomuaharibu"

Aliendelea "Mmmmh ngoja tumuone"

Mimi "Mama kwanini usimsaidie tu ba mdogo?"

Mama Monica "Yule mwalimu aliwahi kunitukana mwanangu,wewe hujui tu!,na hata niliposikia unaishi kwa mwalimu nilikujaribu ukanibebea kuni zangu,nilipoona wewe ni kijana mzuri na mwanangu kukupenda nikaona nikusaidie wewe!"

Aliponiambia ya kwamba nimewahi kumbebea kuni nilishituka sana lakini sikutaka kuonyesha!,niliendelea kujipa moyo nikiamini kwasasa hawezi kunifanyia jambo baya kwasababu nilikuwa kwenye mahusiano na binti yake,nilifahamu kabisa ile familia niya kishirikina lakini kwakuwa walikuwa wakinilinda sikuwa na namna!.

Mama Monica "Hata huko walipoenda wameenda kupoteza muda tu mwanangu"

Mimi "Kwani wameenda kwa mganga"

Monica "Wewe nilikwambia nikikuambia hutoniamini,ngoja mama akueleze sasa"

Mama Monica "kwani hujui mwanangu?"

Mimi "Nimetoka senta sijakuta mtu nyumbani mama"

Mama Monica "Hawawezi kukwambia mwanangu"

Aliendelea "Sasa kesho kuna vitu nitakupatia uende navyo nyumbani na nitakuja mwenyewe baadae kukuelekeza namna ya kufanya!"

Mama Monica "Kwakuwa hata hivyo yule mbwa anataka kuniulia nyinyi wanangu nitamshikisha adabu halafu baada ya hapo nitapandishwa cheo"




-/-/-/-/-/-/-/-/-/-/-/-/-/-/-/-/-/-




SEHEMU YA - 23.


Baada ya mazungumzo ya muda mrefu pale nje,mama yake Monica alituaga akawa ameingia ndani kwa ajili ya kulala,basi na sisi hatukutaka kupoteza muda kabisa tukawa tumeingia ndani ya kwa ajili ya kulala.Ilipofika asubuhi niliamaka mapema nikawa nimemwambia Monica inapaswa nielekee nyumbani!,siku hiyo nakumbuka ilikuwa jumamosi.

Monica "Subiri basi mama aamke kwanza"

Basi Monica alinipatia maji nikanawa uso kisha nikarudi ndani kusubiri hadi mama yake aamke maana alikuwa ameniambia usiku ya kwamba angenipatia kitu ambacho ningeenda nacho nyumbani ili kitusaidie!.
Ilipofika mida ya saa 1 asubuhi mama yake Monica alikuwa ameshaamka na alikuja kugonga mle ndani nilimo lala ili atusalimie,wakati huo nilikuwepo mimi peke yangu na Monica alikuwa yupo jikoni akiandaa uji kwa ajili ya mlo wa asubuhi!.

Mama Monica "Hujambo baba"

Mimi "Sijambo mama,shikamoo!"

Mama Monica "Marhaba,baba yangu"

Aliendelea "Mbona mapema yote hii,unawahi wapi?"

Mimi "Nilitaka kuwahi nyumbani mama nikaendelee na shughuli zangu,siunajua tena ninapaswa kuelekea senta"

Mama Monica "Ni kweli baba"

Aliendelea "Basi njoo umsalimie bibi yako"

Basi nilitoka mle chumbani nikaelekea mpaka nje ya mlango wa ile nyumba aliyokuwa amelala bibi yake Monica!.Kwakuwa kisukuma changu kilikuwa cha salamu tu na kuombea maji ilibidi mama yake Monica niwe naongea halafu na yeye anamtafusiria bibi maana alikuwa hakijui kiswahili hata tone!.

Baada ya salamu na mazungumzo mafupi,mama yake Monica akawa amenitolea kiti nje akanitaka nikae nisubiri uje uive ninywe wakati ambao yeye ananiandalia mitishamba na dawa aliyokuwa ameniambia angenipatia.Kiukweli niseme tu ukweli,mama yake Monica alitokea kunipenda sana na kuna muda nilikuwa nikifika pale kwa Monica najihisi niko kwenye dunia nyingine,mara kwanza nilikuwa naogopaga sana,lakini baada ya kuhakikishiwa usalama wangu,kwakweli sikuwa naogopa tena!.Yule mama alikuwa yuko radhi afanye jambo lolote ili mimi na mwanaye tusalimike!.

Basi haukupita muda Monica akawa ameivisha uji na maboga akatenga kwenye jamvi!,nilishuka kutoka kwenye kiti na kukaa kwenye jamvi kwa ajili ya kupata brekifasti!,kama ambavyo nilisema hapo awali,ile familia haikuwa na hela ila ilikuwa na uchawi wa kutosha!,kunywa uji usiyokuwa na sukari halikuwa jambo la mjadala na kiukweli japo sikuwahi kunywa uji wa sukari hapo kwa Monica lakini uji ulikuwaga mtamu sana kwasababu walikuwa wakiweka maziwa!,hivyo kuufanya kuwa mtamu sana!.Nilipomaliza kupata ile brekifasti,mama yake Monica aliniita ndani ya nyumba kubwa kule alikokuwa amelala bibi yake Monica.

Mama Monica "Mwanangu nisikilize kwa makini!"

Aliendelea "Najua wewe na mwanangu mtakwenda kuniletea mjukuu hivi karibuni,hivyo wewe ni mtu muhimu sana kwasasa katika familia hii"

Mama Monica "Najua Mwalimu Wambura ni Mkurya wa Musoma huko na ndiyo maana ni mjeuri,ila wewe nimekupenda kwakuwa unanisikiliza sana mwanangu,nakuomba usije ukachukua roho ya mwalimu Wambura!"

Aliendelea "Naamini hautanitesea mwanangu pekee Monica"

Mama Monica "Baba yake alikufa angali bado mdogo,hivyo nimemlea kwa matatizo makubwa mno!"

Aliendelea "Tulihamia huku baada ya kufukuzwa huko Ilungu-Magu,na hii yote ni kwasababu ya baba yake Monica"

Mama Monica "Haya yote unayoyaona tumerithishwa na huyu bibi yako unayemuona ningali binti mdogo"

Aliendelea "Kwakuwa baba yake Monica alitaka kuniulia mwanangu wa pekee kwenye michezo yao,ndipo huyu bibi yako tukasaidiana kummaliza kabla hajafanya jambo baya".

Aliendelea kusema "Baada ya mambo kuharibika ndipo tukahamia hapa,kutoka huko Ilungu".

Aliendelea kusema "Hivyo nikuombe mwanangu,hata nikifa leo,nakuomba umtunze mwenzio kwa gharama kubwa maana aliniambia anakupenda sana".

Aliendelea kusema "Mwanangu hajasoma,lakini ni mwerevu na anajua mambo mengi,hivyo na wewe nakuomba umpende!.

Kiukweli siku hiyo mama yake Monica aliamua kunipasulia ukweli kuhusu mwananye na familia yake kwa ujumla, ndipo nikaona kabisa nilikuwa nimethaminiwa kwa kiasi kikubwa na ile familia.

Mimi "Mimi nampenda sana Monica mama na sitaki kumpoteza na yote uliyoongea nimekusikia!".

Mama Monica "Sawa nisubiri nakuja".

Mama yake Monica aliingia chumbani akawa anazungumza na bibi yake Monica kisukuma.Sasa wakati nikiwa nasubiri mama atoke chumbani,ndipo Monica naye akawa ameingia ndani!.Haukupita muda mama yake Monica alitoka ndani akiwa amebeba furushi la mfuko wa rambo la blue!.
Alianza kuufungua ule mfuko kisha kutoa vitu ambavyo sikuvielewa.

Mama Monica "Kamata hii"

Aliendelea "Hiyo niliyokupa ukifika pale nyumbani kwenu,nenda kule nyuma lilipo dirisha la chumba cha Mwalimu na uhakikishe unachimbia chini usawa wa dirisha!".

Mimi "Sawa mama"

Aliendelea "Kamata na hii"

Alisema " Hii naomba umwambie mwalimu aogee yeye na mkewe,halafu wakimaliza kuoga wajipake hii hapa".

Aliendelea kusema "Wewe na mwenzio pia mfanye hivyo hivyo,baadae nitakuja mimi mwenyewe na nitakupatia maelekezo namna ya kufanya"

Mama Monica "Nataka kumsaidia mwalimu ili aepukane na hii fedheha ya yule mpumbavu na wenzie"

Aliendelea "Mwalimu amewahi kunitusi na tulikuwa hatusalimiani,ila inapaswa akushukuru sana wewe".

Mimi "Mwalimu hatakataa nikimwambia?"

Mama Monica "Wewe mwambie,akikataa shauri yake"

Aliendelea "Kama anataka kuondoa fedheha na kumuahibisha mbaya wake mwambie atumie,akikataa usimlazimishe muache".

Mimi "Nashukuru sana mama"

Mama Monica "Andaeni sherehe kesho mtafurahi na itakuwa fedheha hapa kijijini"

Basi baada ya mama yake Monica kunikabidhi zile dawa nikawa nimeaga na kuondoka kurudi nyumbani.Muda huo ilikuwa yapata saa 3 asubuhi.

Baada ya kutembea kwa muda namshukuru Mungu nikawa nimefika nyumbani salama,nilipofika mida hiyo bado sikumkuta mtu yeyote pale nyumbani!.Basi niliingia stoo nikachukua jembe nikazunguka kule nyuma ya nyumba ambako kulikuwa na dirisha la chumba alichokuwa analala Ba'mdogo.Nilichimba haraka haraka na kufukia ile dawa kama ambavyo mama yake Monica alikuwa amenielekeza.
Nilipomaliza nilirudisha jembe stoo kama kawaida,nilichukua dumu la maji nikaelekea lamboni kuchota maji ili nije nikaoge ile dawa ambayo alinipatia maelekezo na kututaka wote tuoge kama tunataka kuwa salama ikiwemo Headmaster na mkewe!.Basi baada ya kumaliza kuoga nilianza zoezi la kuosha vyombo na kumwaga ule ugali nikiyokuwa nimeupika jana na ukakosa walaji!.

Baada ya ile kazi iliyochukua muda wangu mwingi,niliingia ndani kulala!.Nilishituka nikiwa naamshwa na Ema mida ya Saa 7 mchana,wakati huu jamaa alikuwa akijechekelesha chekelesha na nikajua kutakuwa na kitu lazima kwasababu haikuwa kawaida yake,mara nyingi alikuwaga akiharibu mahali basi alikuwa akinichangamkia sana kwakuwa mimi nilikuwa mtetezi wake!.

Mimi "Vipi".

Ema "Mwanangu si Headmaster amenifuma nampiga Deborah mate"

Mimi "Amekufuma wapi"

Ema "Situlikuwa tumesimama pale karibu na ule muale".

Mimi "Sasa amewaona vipi"

Ema "Yaani mwanangu na mimi sifahamu,nimeshituka namuona huyu hapa"

Mimi "Amekwambia nini"

Ema "Ametuchora tu,hajaniambia chochote"

Nilijua tu atakuwa ameharibu mahali na ndiyo maana akajifanya kuja kwangu na kuanza kujichekesha!,kimoyo moyo nilimuhurumia maana nilijua fika stiki atakazokutana nazo si za kitoto!.

Sasa ilipofika mida ya saa 9 alasiri nilitoka zangu ndani na kwenda kumsalimia Headmaster ambaye alikuwa amesharudi,lakini haikuwa kawaida yake nilivyomuona,kiukweli alio alionekana kama mtu aliyekata tamaa na kuchoka kwingi,sasa sikufahamu huko alipokuwa ameenda kilikuwa kimemkuta nini!.

Headmaster "Hivi mwalimu Dani huwa unafahamu anapokaa"

Mimi "Hapana,sijawahi kufika kwake"

Headmaster "Hebu mwambie huyo mjinga aje nimuagize"

Basi nilitoka kwenda kumuita Ema.

Headmaster "Wewe mwalimu Dani siunapafahamu anapokaa?"

Ema "Eeenh,napajua"

Headmaster "Nenda ukimkuta umwambie akupatie mzigo wangu,na uwahi kurudi".

Basi baada ya Ema kuondoka,nilimwambia baba nilikuwa nina mazungumzo nae yeye pamoja na mama.

Headmaster "Kwani huwezi kuniambia mimi mpaka awepo mama yako mdogo?"

Mimi "Ni vizuri akiwepo na mama baba"

Headmaster "Sawa,nilimuacha kwa mama Salome,ngoja tumsubiri arudi".

Nilitaka awepo Maza mdogo maana nilifahamu ningemwambia Headmaster angeweza kukataa,ila Maza mdogo akiwepo isingekuwa rahisi yeye kukataa!.



-/-/-/-/-/-/-/-/-/-/-/-/-/-/-/-/-/-



SEHEMU YA - 24.


Baada ya Maza mdogo kurudi,ulikuwa ukiwaangalia yeye na Headmaster ilionekana kuhuzunika sana na sikuelewa sababu ilikuwa ni nini!,nimewazoea mara zote tukiwa pale sebuleni eidha tukila chakula au tukiwa tumekaa,mara zote mazungumzo yenye utani na ucheshi mwingi huwa yakishika kasi,safari hii imekuwa tofauti kabisa!.

Headmaster "Ulisema ulikuwa na jambo la kutuambia,ni jambo gani hilo bhana"

Mimi " Ni jambo la kawaida tu Baba"

Mimi "Baba mimi nina rafiki yangu wa kike anaitwa Monica,na niseme tu ukweli baba ile siku uliyoniadhibu ni kweli nili lala kwao".

Mimi "Sasa nimeamua Kuwaita ili niwashirikishe jambo"

Mimi " Yule binti kiukweli kwao ni wataalamu wakusaidia watu na wameshawasaidia watu wengi,sasa huwa nikienda kwao kumsalimia ananielezaga mambo mengi kuhusu hii nyumba tunayoishi".

Sasa niliamua mambo mengine kukoleza chumvi ili mradi tu waniamini na wakubali hatua za haraka zifanyike!.

Mimi " Jana nilipotoka senta nilikutana nae njiani akawa amesema nimsindikize hadi kwao,sasa nilipofika kwao mama yake akaanza kuniambia kuna mtu amewahi kuja hapa nyumbani kufanya zindiko,sasa lile zindiko lilifeli kwasababu yule mtu aliuawa kichawi"

Sasa baada ya kusema hiyo sentensi,nikaona Headmaster na mkewe wanaangaliana kwa mshangao!.

Mimi "Yule mama aliniambia adui wa hii nyumba ni mzee makono!".

Headmaster "Hivi huyo mzee makono ndiye nani?"

Mimi "Kama unakumbuka baba nimewahi kukwambia nilikutana nae akaniambia anakusalimia na akajitambulisha kwamba anaitwa makono"

Headmaster "Sawa nakumbuka lakini najaribu kuvuta picha ni mzee gani huyo"

Mimi "Unakumbuka ile siku Ema amening'inizwa darasani?"

Headmaster "Mmh!"

Mimi "Sasa siulikuja na wazee wawili kama unakumbuka,yeye ni yule mwemamba mrefu"

Headmaster "aaaaaaah!,hivi kumbe ndiyo anajiita makono!"

Maza mdogo "Ni nani?"

Headmaster "Si yule mzee lameki"

Headmaster "Sawa,sasa hapa ndipo naanza kupata picha!"

Aliendelea "Basi hilo jina litakuwa la kisukuma au la kwao huko,kama ni yule mzee jina lake ni Lameki"

Aliendelea "Na alikuwa rafiki yangu sana lakini siku za karibuni naona ananikwepa sana".

Headmaster "Sisi bhana tumekuelewa na labda kwa niaba ya mama yako mdogo nikuombe radhi kwasababu kuna mahali tulienda na tukaambiwa mambo mengi sana,hata suala wewe kumchungulia mama yako akiwa anaoga haikuwa kweli,tumeambiwa ni mtu mmoja ambaye anazo nguvu za kutosha tu,na kwa maelezo yako sasa angalau nduyo napata mwanga".

Aliendelea "Kumbe matukio yote yanayofanyika hapa ndani kuna watu ndiyo wanatufanyia hiyo michezo na tumeambiwa anayeongoza genge ni mwanaume mwenye nguvu haswa,sasa namna ya kukabiliana nae ndiyo changamoto,ingawaje kuna dawa tumepewa ndo tunataka kuzijaribu tuone!"

Alisema "Je mama yake huyo binti anapatikana wapi?"

Mimi "Wao wanaishi kule masairo"

Headmaster "Aisee mnazurura,hadi Masairo ushafika!"

Aliendelea "Huyo mama yukoje?"

Basi baada ya kumuelezea namna mama yake Monica alivyo,mzee alishangaa sana!.

Headmaster "Siyo mke wa mzee Kulola kweli?,maana kwa unavyoniambia ni kama yeye"

Aliendelea "Yaani yule mchawi ndiyo unasema anasaidia watu?,wale inasemekana walifukuzwa huko vijijini kwasababu ya uchawi!"

Baada ya kuniambia hivyo nikaona kabisa bila kujitetea nitaharibu mambo!.

Mimi "Hata mimi mara ya kwanza baba nilikuwa nasikia watu wanasema hivyo,lakini nilivyombananisha yule binti alikataa na hata pia nikaongea na mama yake akaniambia walikuwa wanasingiziwa tu,hakukuwa na ushahidi dhidi yao"

Headmaster "Mimi na yule mama hatupatani na yeye analijua hilo,kuna kipindi nilimtukana sana"

Mimi "Lakini baba asingekuwa mtu mwema asingeniambia haya yote"

Maza mdogo "Ila kweli,kama ni mchawi unadhani angesema hivyo?"

Mimi "Kuna dawa alinipatia jana akawa amesema tuitumie na kama ukikubali mimi nitamuita aje atusaidie ili kumnasa mtu anayetusumbua"

Headmaster "Hiyo dawa iko wapi?"

Basi niliondoka kwenda ndani kuchukua ile dawa na kuileta!.

Headmaster "Ndiyo hii?"

Mimi "Ndiyo baba"

Maza mdogo "Matumizi yake yakoje?"

Mimi "Hii tunaogea watu wote mama"

Maza mdogo "Baada ya hapo"

Mimi "Nitaenda kumuita mama yake Monica aje atuelekeze cha kufanya"

Headmaster "Shida tukitumia dawa zote hatutajua ni nani ametusaidia"

Aliendelea "Sawa,ngoja tumuone huyo mama,kama amekwambia yote hayo inawezekana akawa mkweli "

Kwakuwa nilifahamu ikifika usiku mama yake Monica angekuja kama alivyokuwa ameniahidi,sikuwa na presha na niliwaambia ningemfata kumbe mimi nilikuwa ninaujua ukweli.

Headmaster "Hivi huyo mjinga bado hajarudi tu"

Mimi "Bado sijamuona"

Headmaster "Ngoja licheze na dunia,sikuhizi badala ya kusoma limeanza kuhangaika na wanawake!"

Aliendelea "Mabinti wa hii shule niwa kuhangaika nao?,ngoja acheze na hiki kijiji kama hatujamuacha hapa".

Baada ya maelekezo ya namna ya kutumia ile dawa,namshukuru Mungu walikubali na walioga!,sasa kitu kilichokuwa kinasubiriwa ni mama yake Monica kuja,niliwaambia ikifika jioni nitaenda kumuita,lengo langu lilikuwa ni kusubiri mpaka atakapokuja mwenyewe maana nilichoka kutembea mpaka Masairo ambako kulikuwa mbali!.
Headmaster alihuzunika sana kusikia ya kwamba aliyekuwa akitufanyia uhuni pale nyumbani alikuwa huyo mzee aliyejiita makono ilihali jina lake ni Lameki.Nakumbuka Headmaster alisema akipatikana huyo basi angejuta kuzaliwa!.

Ilipofika mida ya saa 11 jioni,niliwaaga nikasema naelekea kwao Monica kumchukua mama yake!,sasa kwa muda ule niliona nitembee kwa kukimbia ili niwahi kufika maana palikuwa mbali!.Baada ya safari ya muda mrefu kidogo nilifanikiwa kufika kwao Monica.

Nilimkuta bibi yake Monica akiwa amelala kwenye jamvi kwa nje!,nilipiga hodi yule bibi akaitikia kisukuma,sasa kasheshe ilikuwa ni kuongea nae kumuuliza Monica na mama yake wako wapi kwasababu sikuwakuta!,nilipojaribu kumuuliza kwa kiswahili,yeye alinijibu kwa kisukuma,niliamua kusimama kando ya nyumba ili kuvuta muda angalau nikiamini wangekuja maana walikuwa wamemuacha bibi peke yake.
Baada ya muda kwenda ikiwa inakaribia saa 1 usiku,nilimuona Monica akiwa anakuja akiwa amebeba gunia kichwani na jembe mkononi!,alipofika nilienda kumtua ule mzigo ndipo nikakuta alikuwa amebeba mihogo mibichi.

Mimi "Mlienda shambani?"

Monica "Eeeh!,umekuja muda mrefu?"

Mimi "Nimekuja muda ndiyo"

Mimi "Mama yuko wapi?"

Monica "Anakuja,nimuacha hapo nyuma"

Mimi "Sasa hii mihogo mtamenya saa ngapi?"

Monica "Hii itamenywa kesho,nani wakumenya sasa hivi nimechoka"

Mimi "Sawa,kesho nikipata nafasi nitakuja kuwasaidia kumenya".

Ile mihogo ilikuwa ni ile michungu(rumala) iliyokuwa inavundikwa ikishamenywa kwa ajili ya kutengenezea unga wa muhogo(Udaga).

Basi haukupita muda mama yake Monica naye akawa amekuja na yeye akiwa na mzigo wa mihogo kichwani.

Mimi "Mama shikamoo"

Mama Monica "Marhaba mwanangu"

Aliendelea "Umefika zamani?"

Mimi "Ndiyo mama,nimefika muda tu"

Mama Monica "Tusamehe mwanangu,tulienda kuchimba mihogo tumtengenezee bibi yako unga wa kuondoka nao"

Mimi "Sawa mama haina shida"

Mimi "Sidhani kama nitakaa sana,maana nimetumwa ba Ba'mdogo "

Mama Monica "Mwalimu anasemaje?"

Mimi "Mama niliwaeleza jambo uliloniambia na wamekubali"

Mama Monica "Kweli?"

Mimi "Kweli mama"

Mama Monica "Basi wewe nenda ukawaambie nakuja,ngoja nijiandae nikawachukue wenzangu tunakuja"

Sikutaka kupoteza muda nilitoka nduki kurudi nyumbani kwasababu ilikuwa tayari ni usiku!.Nilifika nyumbani mida ya saa 2 usiku nikamueleza headmaster na mkewe na wao wakawa wanawasubiri!.
Kila mtu hapo nyumbani alikuwa amekwisha kuoga ile dawa na hata Ema ambaye nae pia wakati naondoka sikkumuacha ila alipo rudi alipewa maelekezo namna ya kuoga ile dawa!.

Sasa wakati usiku tukiwa tunakula,nilisikia mlango wa nje unagongwa,Ema alienda kufungua ule mlango na alikuja kuniita akisema naitwa!.Basi nilinyanyuka kuelekea nye ndipo nikamuona mama yake Monica akiwa na wale wanawake wawili,safari hii walikuja wakiwa wamevaa nguo za kawaida na wametanda Khanga!.

Mimi "Karibu mama"

Mama Monica "Haya tushafika,hao wapo?"

Mimi "Wapo mama,ingieni ndani?"

Basi waliingia mpaka uani wakawa wamesimama,mimi niliingia ndani kumwambia headmaster.

Mimi "Amekuja baba"

Headmaster "wewe msukuma njoo tule bhana"

Mama Monica "Nyie endeleeni sisi tumekula"

Headmaster "Toa viti hapo nje"

Basi nikatoa viti vya idadi ya wale kina mama nikapeleka!.

Tulivyomaliza kula,headmaster alitoka nje na mkewe ili kumsikiliza mama yake Monica!.

Headmaster "Mmh!,we msukuma lete maneno"

Mama Monica "Mimi nipo mkurya"

Mazungumzo ya kutaniana kati ya headmaster na mama yake Monica yalipokwisha maliza,sasa usiriasi ulichukua nafasi!.

Headmaster "Huyu kijana wangu amenifikishia yote uliyomwambia,na sisi tumeyapokea kwa mikono miwili"

Aliendelea "Hebu nisaidie maana nimeshahangaika sana na sijui nitakulipa nini nikifanikiwa"

Aliendelea "Hayo yaliyopita tuachane nayo,mimi na wewe tuanzie hapa sasa!"

Mama Monica "Tusipoteze muda,nileteeni karai na maji"

Nilichua karai nikasogezea mama yake Monica.

Alisimama akafungua mfuko uliyokuwa na makorokoro mengi yasiyoeleweka,alichukua unga akawa amemwaga ndani ya yale maji kwenye karai,baada ya hapo alizungumza kisukuma na mmoja ya wale kina mama ndipo mmoja wapo akawa amebeba lile karai na kutoka nje,haukupita muda akawa amerudi yale maji ndani ya karai yakiwa yameisha!.

Mama Monica "Leo wabaya wako wapo kwenye kikao mwalimu,hivyo wakiishatoka tu lazima waje hapa,wakifika hapa ndipo wataipata freshi"

Aliendelea "Sasa nawapatia hii kitu kila mmoja ahakikishe analala nayo kwa kuishikiria na usije ukaiachia"

Alitukabidhi watu wote kitu kikiwa kimeshonwa na kitamba kigumu mno,mimi sikupata shaka kuelewa kwamba ile ilikuwa ni irizi!.

Mama Monica "Hizi hapa mtapakaa kila mtu usoni kabla ya kulala"

Aliendelea "Mwalimu shika hii"

Headmaster alipewa kibuyu kidogo kama kile ambacho nilipewa mimi siku ile.

Mama Monica "Hiki kibuyu hakikisha unakiweka nyuma ya kona ya mlango"

Headmaster "Sawa"

Mama Monica "Mwanangu shika hii"

Na mimi pia alinikabidhi kile kibuyu kidogo na akanitaka nikiweke nyuma ya mlango kwenye kona.

Mimi na ndugu zangu hawa tutakuwa mazingira ya karibu,hivyo msiwaze!.

Headmaster "Kwahiyo hapa ushamaliza?"

Mama Monica "Kila kitu tayari"

Aliendelea "Msije mkapiga kelele kwa mtakachokiona,mkipiga kelele tu ,mtakuwa mmeharibu kila kitu!"

Mama Monica "Kama kuna mtu anajua hatokuwa mvumilivu aseme kabisa"

Baada ya hilo swali na wote kumuhakikishia tutakuwa wavumilivu ndipo aliendelea akasema.

Mama Monica "Mwalimu utakachokishuhudia wewe simama na chukua kibuyu nilichokupatia na ukifungue kikae wazi"

Aliendelea "Ukishakifungua tu,huyo mbaya wako atajuta kuitembelea hii nyumba"

Baada ya muda mama yake Monica na wale kina mama waliaga kuondoka,Headmaster na mkewe walitoka kuwasindikiza.



-/-/-/-/-/-/-/-/-/-/-/-/-/-/-/-/-/-




SEHEMU YA - 25.


Baada ya Headmaster kutoka kuwasindikiza wageni,tuliamua kukaa kikao cha kifamilia na kuzungumza mambo kadhaa yaliyotuweka sawa.Sasa kila mtu alielekea chumbani kulala,baba mdogo na mkewe waliingia chumbani kwao,mimi na Ema pia tuliingia chumbani kwetu kulala.

Siku hiyo mle chumbani hakuna aliyepata usingizi kabisa,kabla ya kulala nakumbuka tulipakaa usoni dawa aliyokuwa ametupatia mama yake Monica,pia tukashikiria na zile hirizi mkononi kama alivyokuwa ameagiza tufanye!.Kadri muda ulivyokuwa ukisonga tuliona kimya,mimi nilianza kupitiwa na usingizi maana nilikuwa nimechoka sana!,kumbe wakati mimi napitiwa na usingizi,Ema yeye alikuwa macho kabisa na jamaa alikuwa na shauku ya kuona ni kitu gani kingetokea!.

Sasa ilipofika mida ya saa 8 usiku,nilishitushwa na Ema akiniamsha!.

Ema "Umesikia hicho kishindo?".

Mimi "Hapana,kishindo cha kitu gani?"

Ema "Kutakuwa na kitu nadhani!"

Ema alikuwa akiniambia kwa sauti ndogo kabisa na yenye uoga ndani yake!.

Mimi "Nyamaza"

Niliamka kitandani nikaenda kuwasha taa,nilifahamu kabisa kile kishindo Ema alichosikia hakikuwa cha kawaida na uenda wale jamaa wakawa wamekuja kama kawaida yao,kiukweli mimi kwa upande wangu sikuwa kabisa na hofu kwasababu kwa siku chache nilikuwa nimeshazoea yale mazingira ya kuwaona wachwawi laivu!.Nilimwambia na kumbusha Ema ya kwamba chochote atakachokiona asipige kelele wala kushituka!.

Haukupita muda,mara ghafla wakaonekana watu watatu wakiwa wamesimama mle chumbani huki wakiwa uchi kama walivyozaliwa,watu wale safari hii walikuja wawili wanaume na mmoja akiwa mwanamke!.Niliwaangalia kwa kuibia kama vile sielewi chochote!,Ema alikuwa akitetemeka sana na nilimpatia ishara ya kwamba atulie kabisa!.Basi nadhani yule mwanamke alihisi jambo maana niliona anamsogelea Ema akawa kama anamtisha aone kama amemuona,sasa alipoendelea kumtisha Ema nikaona anaweza kupiga kelele,nikaanza kumpigisha Ema stori ili kupotezea ile hali!.

Mimi "Mwanangu wewe piga kimya kabisa wala usimfanye chochote yule demu"

Ema "Yule demu mwanangu anazingua kinoma"

Mimi "Halafu Headmaster alisema ukamuamshe aandae yale masomo"

Ema "Halafu kweli umenikumbusha,ngoja nikamuamshe!"

Sasa wakati tunaongea yule mwanamke alirudi kwa wenzie na wakaendelea kushangaa shangaa,tulichokifanya na Ema pale kwa ule muda mfupi ni hakika walidhani hatuwaoni kumbe lengo lilikuwa ni kumuondolea Ema uoga na kuwapoteza maboya!.
Ema aliamka akatoka kwenda kumgongea Headmaster chumbani kwake ili aje ajionee!,sasa wakati Ema ameondoka,nilianza kujipigisha mruzi wa uongo na kweli ili kuikabili ile hali kwasababu ilikuwa inatisha si kitoto!..

Headmaster "Umughaka tacho omahe"

Baba alipotoka nje aliniita kwa kilugha nikawa nimetoka nje,sasa alianza kutueleza ya kwamba tusishituke na tuendelee kuwa watulivu,alitwambia Ema achukue madaftari tuelekee wote sebuleni ili iwe rahisi kuwakabili,mimi nilimwambia wao wakae sebuleni na mimi nirudi chumbani kukaa karibu na kibuyu kwa kazi maalumu!.
Basi wale watu wakawa wamepotea ghafla mle chumbani!,nilitoka nje kwenda kumwambia Headmaster.

Headmaster "Ngoja tusubiri,yawezekana wakawa wameshituka"

Mimi "Lazima warudi"

Headmaster "Halafu mbona yule mzee hayupo?"

Mimi "Uenda leo kawaagiza hawa"

Wakati tukiwa tunaendelea kuongea pale,Maza mdogo akamwambia Headmaster kwa kikurya kwamba,wale watu wako kule chumbani kwake na anawaona,Headmaster akamwambia atulie na asipige kelele!.Sasa tukiwa tunaendelea kuongea pale sebuleni huku Headmaster akijifanya kumpigisha Ema pindi,tukasikia kishindo kikubwa tena pale uani!.

Haukupita muda akawa ametokea yule mzee makono akiwa na usinga mkononi huku akiwa uchi kama wenzie!,akaja mpaka pale sebuleni huku tukiendelea kumpimia tu!,aliendelea kuangaza huku na huko na hatimaye akawa ameingia mle chumbani kwa Headmaster.Basi baada ya kuingia chumba cha Headmaster,Headmaster aliinuka kwa ghadhabu huku akisema "Lero n'uramanye uwe tombanyoko" (Leo utanitambua).

Sasa Headmaster alipoingia chumbani alijifanya kuongea na mkewe huku wakiwatazama,sasa nadhani mzee makono aliwaambia wale watu waende wakawalete watu wa kwenda kulima ili wakifika watuunganishe na sisi tuondoke!,wale watu watatu walitoweka wakamuacha mzee makono mle chumbani akitaka kufanya mambo yake ili amchukue Headmaster kama kawaida aje atuunganishe na sisi tuelekee kwenye kilimo cha usiku kisichokuwa na tija!.

Wale watu walipotoweka tu na mzee makono kubaki mwenyewe,Headmaster alichukua kile kibuyu alichopewa na mama yake Monica akakifungua,alipokifungua tu!,yule mzee akaanza kucheza kwa kuzunguka mle chumbani kama mwendawazimu!.Headmaster alituita tukaingia kumtazama,yaani kuna muda nilianza kumuonea huruma maana alikuwa kama amepagawa kwa kushikwa ugoni.

Kadiri muda ulivyokuwa ukienda,wale watu waliotumwa na mzee makono hawakurudi kabisa na nadhani watakuwa walishituka mapema!.Ile hali ilifanya maza mdogo kutoka kule chumbani akabaki mzee makono akizunguka chumba kizima kama mwendawazimu.Usiku huko hakuna mtu aliyepata usingizi kabisa,tumekuja kushangaa imefika saa 11 alfajiri bila kujua!.
Sasa ilipofika saa 12 asubuhi,Mama yake Monica alikuja akiwa na wale kina mama,alihuzunika sana kwanini tuliamua kuwaachia wale watu watatu wakaondoka!.

Mama Monica "Mwalimu nilikwambia,nadhani sasa unaniamini"

Headmaster "Sikuzote Msukuma nakuamini,si leo tu!".

Mama Monica "Kwanini mmewaachia wale washenzi?"

Headmaster "Wameondoka wenyewe"

Mama Monica "Nilikwambia wakifika tu,ungefungua kibuyu"

Headmaster "Nilipoingia chumbani kufungua kibuyu wakawa wameondoka akabaki mzee lameki"

Mama Monica "watasimuliana,hakuna kilichoharibika"

Aliendelea "Haya sema,unataka tumfanye nini huyu mzee"

Headmaster "Nadhani kama kuna uwezo muondolee uwezo wake asije akaponyoka halafu mengine utaniachia mimi"

Mama Monica "Huyu ameshakwisha,hapa hawezi kukuponyoka kamwe"

Aliendelea "Mimi namshughurikia halafu nakuachia wewe utajua cha kumfanya".

Basi mama yake Monica alimsogelea yule mzee akachukua ule usinga kisha akamvua shanga alizokuwa amejivika kuanzia begani kuteremkia kiunoni!,baada ya hapo kuna dawa alimpatia Headmaster akamwambia kukishapambazuka vizuri atampaka ile dawa na kisha atamuondoa mle ndani!.Mama yake Monica na wale kina mama waliondoka wakawa wamemuacha mzee makono humo ndani akizinguka kama mwehu!.

Kulipopambazuka,Headmaster alielekea kwa mwenyekiti wa kijiji na kutaka yowe ipigwe karibia kijiji kizima ili wananzengo wahalifiwe ya kwamba kulikuwa kuna tukio kubwa la kushangaza!,Basi yowe ilipigwa na watu wakawa wanakuja pale nyumbani huku wengine mikoni wakiwa wameshika mapanga na mafimbo!.Haukupita muda mrefu watu wakawa wamejazana pale nyumbani huku wengine wakichungulia dirishani wakishangaa lile tukio!.

Ilipofika mida ya saa 3 Asubuhi baada ya watu kujazana pale nyumbani,Headmaster alifanya kama alivyoambiwa afanye na mama yake Monica,baada ya kupakwa dawa yule mzee alikurupuka akawa anashangaa sana!,alikuwa akizunguka kitafuta usinga wake lakini hakuuona,ndipo Headmaster aliamrishwa na wananzengo ya kwamba amtoe yule mzee nje ya nyumba ili akapambane na viboko vilivyokosa huruma!.

Yule mwenyekiti aliamuru yule mzee avishwe nguo hadi kwenye ofisi ya serikali ya kijiji lakini wananzengo wakagoma,walisema inapaswa atembezwe kijiji kizima huku akila mboko na inapaswa siku hiyo hiyo ahame kijiji!.

Basi nakumbuka Headmaster alimuagiza Ema akalete viboko ili aanze nae mle ndani kwasababu alikuwa akimtafuta sana,viboko vilipoletwa kiukweli yule mzee alichezea kiasi kwamba sikutaka hata kuangalia,viboko vilipozidi aliamua kutoka ndani spidi akikimbilia nje,kufika nje wananzengo wakamdaka nako wakaanza kumsulubisha!.
Alitembezwa kijiji kizima huku akiwa uchi kama alivyozaliwa,kiukweli lilikuwa ni tukio la aibu mno!,sasa walipomfikisha kwake wananzengo hawakutaka mjadala,walimwambia avae nguo kisha atoke,alipotoka waliwasha moto nyumba yake na kila kitu kiliteketea kwa moto!.

Baada ya pale alirudishwa serikali ya kijiji na kutakiwa apotee kwenye kile kijiji ndani ya masaa 2!,hakutakiwa kubaki pale na wananzengo walimwambia watamuua endapo angebaki kwa siku hiyo!.

Lile tukio lilivuta hisia kubwa sana pale kijijini na kiukweli lilimpatia Headmaster ujiko na heshima sana ingawaje mimi ndiye niliyepambana sana mpaka kufikia ile hali.Headmaster aliogopeka sana tangu siku ile lile tukio litokee na hakukuwahi tena kuwa na mambo ya ajabu pale nyumbani.

Headmaster kwa baadae alihama ile shule na kuhamia huko Biharamulo ambako amejenga na anaishi hadi leo,mimi niliondoka na kurudi nyumbani kisha kuelekea shuleni Advance!.

Ema yupo hapo Shinyanga anauza duka la vipuri vya magari,amejenga na anaishi hapo hapo shinyanga.

Monica kuna wakati niliambiwa yupo Mwanza ila sijajua ni Mwanza sehemu gani!,kuna mtu nilikutana nae wa pale kijijini akawa ameniambia hivyo,kwasababu baada ya mimi kuondoka pale kijijini sikurudi tena hivyo tukawa tumepotezana na mpenzi wangu huyo!.

Mimi kwasasa nipo Dar es salaam napambana na maisha ya kukimbizana!,nina kiboda boda changu japo kimekwisha lakini tunapambana na maisha!.




MWISHO.
 
Mimi nilimvumilia nikajua hajui kukadiria. Nilimvumilia tena shule ya kata kuwa na wanafunzi 12 tu, tena wanafaulu wote kwenda vipaji.

Ila kwenye mpira kulipia 100, umeme wa jenereta tena kingamuzi kulipiwa na ni enzi hizi za after shule ya kata. Nikaona huyu kenge hana akili kabisa
 
Mimi nilimvumilia nikajua hajui kukadiria. Nilimvumilia tena shule ya kata kuwa na wanafunzi 12 tu, tena wanafaulu wote kwenda vipaji.
Ila kwenye mpira kulipia 100, umeme wa jenereta tena kingamuzi kulipiwa na ni enzi hizi za after shule ya kata. Nikaona huyu kenge hana akili kabisa
Wewe ndiye huna akili, unadhani thamani ya Tsh 100 kwa sasa ni sawa na mwaka 2005 kurudi nyuma?
 
Back
Top Bottom