Hii ni historia fupi ya uwindaji wa simba..
Simba ni wanyama wenye nguvu ambao mara zote huwinda kwa makundi na kumkazania windo walilochagua. Hata hivyo hawajulikani sana kwa stamina yao, kwa mfano, moyo wa simba jike unajumisha tu asilimia 0.57 ya uzito wa mwili wake (wa dume ni asilimia 0.45 ya uzito wa mwili wake), wakati ule wa fisi ni karibu asilimia moja ya uzito wake. Hivyo basi, japokuwa simba anaweza kufikia mwendokasi wa km 81 kwa saa, wanaweza kufanya hivyo kwa mwendo mfupi tu na inawapasa kuwa karibu na mawindo kabla ya kuanza shambulio. Hutumia mwanya wa kupunguza uoni; kwa kufanya uwindaji sana nyakati za usiku. Humnyatia adui mpaka pale wamekaribia kwa walau mita 30 au pungufu. Kisha kukaribia huchagua mnyama aliye karibu. Shambulio huwa fupi na la nguvu; hujaribu kumkamata kwa kumkurupusha kwa kasi na kisha kumrukia. Mnyama huyo daima huuawa kwa kunyongwa. Mara kadhaa pia huweza kuuawa kwa kuzibwa mdomo na pua zake kwa taya za simba. Wanyama wadogo huuawa tu kwa kupigwa ngwala kwa mguu wa simba.
Kitoweo cha simba hujumuisha wanyama wengi wakubwa, hasa wildebeest, nyati, impala, pundamilia, na warthogs kwa Afrika na nilgai, wild boar na aina kadhaa za tandala huko India. Spishi nyingine huwindwa kutokana na upatikanaji wao.
Simba wakiwa wanawinda katika kundi kubwa wana uwezo hata wa kuangusha wanyama wakubwa lakini mara nyingi huwa hawashambulii wanyama wakubwa sana kama vile twiga kwa kuhofia kujeruhiwa pia.
Simba pia wana uwezo wa kushambulia wanyama wanaofugwa na binadamu; kwa mfano huko India ng’ombe wengi huwa chakula cha simba. Simba pia wanaweza kula wanyama wenzao wanaokula nyama kama vile chui, duma, fisi na mbwa mwitu. Pia wakati mwingine hula mizoga ya wanyama wengine waliouawa kwa majanga au na wanyama wengine, na huangalia sana mahali wapozungukazunguka tai, wakijua fika mahali walipo patakuwa na mizoga. Simba anaweza kula mpaka kg 30 kwa mlo mmoja; na kama hawezi kula windo lake lote, hupumzika kwa saa kadhaa na kisha kuendelea tena. Wakati wa mchana na joto kali, kundi la simba hukaa kivulini na dume mmoja au wawili kubakia kama walinzi. Simba jike anahitaji walau kg 5 za nyama kwa siku wakati dume ni kg 7.
Kwa sababu simba huwinda kwenye sehemu wazi, ambapo wanaonekana kwa urahisi na adui zake, uwindaji wa ushirikiano ndio husaidia na kufanikiwa, hasa kwa wanyama wakubwa. Ushirikiano huu husaidia pia kulinda mawindo yao kwa urahisi dhidi ya wanyama wengine, kama vile fisi, ambao mara moja hujua mzoga ulipo kwa kuangalia mahali ambapo tai wanaruka. Uwindaji mkubwa hufanywa na simba jike; simba dume waliopo kwenye kundi hawashiriki kwenye uwindaji mpaka tu pale wanapohitaji kuwinda wanyama wakubwa kama vile twiga au nyati. Wakati wa kuwinda kila simba jike ana nafasi ya kuwinda na kumpata mnyama, aidha kwa kunyatia kwenye na kisha kushambulia au kusogea umbali kidogo karibu na katikati mwa kundi na kumkamata mnyama huyo amwindaye kutoka kwa simba wengine.
Simba wadogo huonesha tabia ya kunyatia wanyama wakiwa na miezi mitatu tu, ingawa hawashiriki kwenye uwindaji mpaka wawe na umri wa mwaka mmoja. Huanza rasmi kuwinda wakiwa na umri wa miaka miwili.