Stori ya kusisimua - Taxi

Stori ya kusisimua - Taxi

Taxi - (76)

Joyce alimtazama mumewe kwa huzuni na uso wenye kutia huruma, alitingisha kichwa chake kwa masikitiko, kiganja chake cha kushoto kikiwa kimeshikilia paji lake la uso.

“Nilidhani yameisha, mume wangu!” Joyce alisema kwa huzuni.

“Hayawezi kwisha kirahisi rahisi hivyo,” Sammy alisema huku akigeuza shingo yake kumtazama Joyce.

Muda huo huo simu ya Joyce ikaanza kuita. Joyce alishituka sana ila alijikaza na kuuma meno. Aliitazama ile simu kisha akamtazama Sammy kwa wasiwasi. Wakatazamana.

Sammy alinyoosha mkono wake na kuichukua ile simu, akaitazama kwa makini na kuona namba ngeni isiyo na jina. Alimtazama Joyce kwa macho makali. Joyce alionekana kuwa na hofu na kujikunyata pale alipokaa.

“Pokea simu yako,” Sammy alisema kwa sauti iliyoashiria hasira huku akimpa Joyce ile simu.

Joyce alikataa kuipokea ile simu kutoka kwa mumewe. Alikuwa anatetemeka kwa hofu.

“Kwa nini unakataa kupokea, kwani unajua ni ya nani anapiga?” Sammy aliuliza kwa ukali huku akiendelea kunyoosha mkono wake kumpa simu Joyce.

“Wala sihitaji kumjua mpigaji,” Joyce alisema huku akinyanyua mabega yake juu kama ishara ya kutotaka kuipokea. Ile simu ikakatika.

Kabla Sammy hajasema chochote wakasikia sauti ya mtu akigonga geti huku akiita “Mama Pendo!” ilikuwa ni sauti ya jirani yao, Bibi Stumai. Joyce alibaki kajikunyata kwa hofu huku akimtumbulia macho mumewe.

“Nenda kamsikilize shoga yako huko nje,” Sammy alisema huku akijiegemeza kwenye sofa.

Joyce alivuta pumzi ndefu na kuzishusha taratibu, akajizoazoa kutoka pale kwenye sofa na kuelelekea nje.

* * * * *

Gari aina ya Toyota Hilux double cabin la rangi ya bluu lililokuwa na namba bandia lilikuwa limeegeshwa kwenye mtaa mmoja mtulivu katika eneo la Tabata Mawenzi. Ndani ya gari hilo kulikuwa na wanaume wawili, Spoiler na Dulla Mcomoro waliokuwa makini sana kuitazama nyumba moja ya kifahari iliyozungushiwa ukuta mrefu wenye uzio wa umeme. Mbele ya ukuta wa ile nyumba kulikuwa na geti kubwa jeusi.

Ukuta wa nyumba ile haukumruhusu mtu aliyeko nje kuona chochote kilichomo ndani ya nyumba hiyo kutokana na urefu wake. Kilichoonekana ukiwa nje ya ile nyumba ilikuwa miti miwili mikubwa ya kivuli na paa la kijani la nyumba ile. Ilikuwa ni sehemu tulivu sana lakini pia ya kifahari.

Spoiler na Dulla Mcomoro walikuwa wanafuatilia kujua kila aliyeingia au kutoka ndani ya nyumba ile. Spoiler alikuwa ametulia tuli akiwa makini sana kana kwamba alikuwa ameambiwa kungetokea kitu cha ajabu muda wowote.

Zilikuwa zimeshapita takriban dakika ishirini tangu wafike eneo lile baada ya kubaini kuwa aliyenunua gari aina ya Cadillac DeVille aliishi katika nyumba ile, kwa mujibu wa nyaraka walizozichukua katika duka la kuuza vipuri vya magari la Jonas Odilo, lililopo mtaa wa Lindi eneo la Shaurimoyo.

Hawakuwa na papara, waliamua kubaki ndani ya gari ili kufanya uchunguzi kabla hawajashuka na kwenda katika nyumba ile. Hadi muda ule hawakuwa wamemuona mtu yeyote kuingia au kutoka ndani ya nyumba ile, hali ilikuwa ya ukimya mno. Wakaanza kupatwa na wasiwasi iwapo nyumba ile iliishi watu.

Wakiwa bado wanafuatilia kila kinachotokea katika eneo lile mara wakaliona garo dogo aina ya Toyota Lexus RX jeusi likifika katika nyumba ile, likapiga honi na baada ya sekunde kadhaa lile geti kubwa likafunguliwa, gari likaingia ndani.

Ilichukua takriban dakika tano tu geti likafunguliwa na lile gari likatoka na kuingia barabarani, likaondoka. Spoiler akamtaka Dulla Mcomoro asogeze gari.

Dulla Mcomoro alilisogeza gari na kusimama mbele ya lile geti kubwa. Wakashuka haraka na kubonyeza kengele iliyokuwa kando ya geti, sekunde chache baadaye mlango wa lile geti ukafunguliwa, mlinzi mmoja wa Kimasai akatoa kichwa kuchungulia na kuwaona.

“Habari zenu?” yule mlinzi aliwasalimia huku akiwaangalia kwa macho ya kuwasaili.

“Nzuri. Habari za hapa?” Spoiler alimjibu yule mlinzi huku akimtazama kwa makini. Wakati huo Dulla Mcomoro alikuwa anachungulia kwenye uwazi wa ule mlango wa geti kutazama ndani.

“Sijui niwasaidie nini?” yule mlinzi aliwauliza huku akiwakazia macho, alionekana kuwa makini zaidi na kazi yake.

“Sisi ni wageni wa Dk. Mloka,” Spoiler alisema kwa kujiamini zaidi na kumfanya yule mlinzi amkazie macho kwa mshangao.

“Dk. Mloka!” yule mlinzi aliuliza kwa mshangao mkubwa, “Kwani Mloka yupi mnamtaka?” akaongeza huku akiwaangalia kwa udadisi, bado mshangao uliendelea kujionesha usoni kwake.

Spoiler na Dulla Mcomoro wakaangaliana na macho yao kuzungumza, kengele ya tahadhari ikalia kichwani kwa Spoiler, akashusha pumzi na kumtazama tena yule mlinzi.

“Kwani hapa siyo nyumbani kwa Dk. Mloka?” Spoiler aliuliza huku naye akijifanya kuonesha mshangao.

“Hii ni nyumba ya Dk. Mloka lakini mbona yeye amefariki dunia miaka miwili iliyopita!” yule mlinzi alisema huku akiwa bado anawatazama kwa makini.

“Kwa hiyo hapa anaishi nani kwa sasa?” Spoiler akamwahi kabla hajafanya chochote.

“Anaishi mkewe, Dk. Marina na watoto wake.”

“Hivi sasa kuna nani ndani?” Spoiler aliuliza huku akijaribu kuchungulia ndani kupitia upenyo mdogo ulio wazi wa mlango wa lile geti.

“Kwani ninyi mnamtaka nani hasa?” yule mlinzi akawauliza baada ya kufikiria kwa kitambo huku akionesha wasiwasi.

“Basi tunaomba tuonane na mama, mke wa Dk. Mloka, maana sisi ni jamaa zake marehemu Dk. Mloka,” Spoiler alisema huku akisogea karibu na yule mlinzi.

“Jamaa zake Dk. Mloka halafu hamjui kama alishakufa! Itabidi msubiri hapa ili nikaulize ndani kwanza, maana siwafahamu na wala sikutaarifiwa kama kuna wageni wa aina yenu watakuja hapa leo!” yule mlinzi alisema huku akijiandaa kuufunga ule mlango wa geti.

Mambo yanazidi kunoga, mlinzi ameonesha kuwashtukia kina Spoiler. Je, watafanikiwa kuingia ndani na kupata taarifa kuhusu mmiliki wa sasa wa gari wanalolitafuta? Vipi kuhusu Sammy na mkewe Joyce, moto utapoa? Na Tunu je, ana mission gani iliyomleta Dar es Salaam? Winifrida atakuja na jipya lipi? Endelea kufuatilia stori hii ya kusisimua ili kuujua mwisho wake...
Mlinzi kawazidi akili
 
Taxi - (91)

ILIPOISHIA

Winifrida akashikwa na kitete na kushindwa kuongea, hofu ilikuwa imemtawala na donge la fadhaa kumkaba kooni. Alimeza funda kubwa la mate kwa nguvu mithili ya mtu anayejaribu kukisukuma kipande cha mfupa kilichokwama kooni. Alitamani sana kupiga yowe lakini sauti yake ikamsaliti. Akajiuliza kwa nini apige yowe? Akili ilimhoji na kumtia ganzi.

Akajikuta akishindwa kabisa kuongea japo alimsikia Sammy akiendelea kuita upande wa pili wa simu. Alishindwa, si kwa sababu ya hofu ya kusikiwa, bali alijiuliza kuwa endapo Sammy angemuuliza simu ile aliitoa wapi angemjibu nini kwani hakuna yeyote aliyejua kama anamiliki simu. Akaikata.

Alianza kujilaumu kwa kutokuzungumza na Sammy, kwani ni hatari zaidi kumwacha Sammy arejee nyumbani na kukutana na wale watu hatari kuliko yeye kutafuta majibu ya wapi ameitoa ile simu. Majuto yalipita haraka kichwani mwake, yalipita kwa kasi mno kiasi cha kumwita Mungu na asimweleze alilotaka amfanyie.

Mara akapata wazo la kupiga tena simu. Lakini kwa wahaka aliokuwa nao, asingeweza kuzungumza na Sammy kwa kuchelea kusikiwa na wale watu. Alishusha pumzi huku akijaribu kusikiliza kwa makini akihofia kuingia kwenye mtego kwa kudhani mmoja wa watu wale, ambao hakujua idadi yao, angeweza kuwa amejificha mle chumbani kumsubiri. Alijitahidi kuangaza macho yake sehemu alizoweza kuzifikia lakini hakuona kitu cha kutilia shaka.

ENDELEA...

Kisha akapata wazo jingine. Sasa alikata shauri, liwalo na lilwe lakini asingeweza kuendelea kujikunyata pale juu ilhali alikuwa na uwezo wa kunusuru ile hali. Aliazimia kupiga simu, kuwapigia polisi kwa kutumia ile namba yao ya dharura na kuwaleleza kilichokuwa kinaendelea kwenye nyumba yao.

* * * * *

Sammy aliendelea kuendesha gari lake katika barabara ya Uhuru kwa mwendo wa kasi akiyapita magari mengine. Sasa alikuwa anazivuka taa za kuongozea magari barabarani za Buguruni Shell na kuingia barabara ya Mnyamani, mara akaonekana kugutuka na kuwauliza wale watu aliokuwa amewapa msaada wa usafiri bila kugeuka wala kuwatazama. “Kwani mnashukia wapi? Mimi napitia barabara ya Mnayamani.”

Kimya!

Sammy akashangaa na kugeuza shingo yake kuwatazama. Akapigwa na butwaa na kushtuka sana. Akanywea. Yule mwanamume mrefu aliyepanda hewani kisawasawa na mwenye mwili ulioshiba alikuwa amemnyooshea bastola huku akiwa makini sana.

Uso wa Bob Chopa, yule mwanamume mfupi kiumbo lakini mkakamavu na mwenye sura ya unyenyekevu ulikuwa umepambwa na tabasamu la kifedhuli.

“Sasa sikiliza, utafuata maelekezo yangu,” yule mwanamume mrefu mwenye mwili ulioshiba alisema kwa ukali.

Sammy alionekana kubabaika sana. Alishusha pumzi za ndani kwa ndani na kubana midomo yake, hakujua afanye nini.

“Ni nini mnakitaka toka kwangu?” Sammy aliuliza kwa sauti tulivu huku akipunguza mwendo wa gari kuwakwepa wapiti njia.

“Hatuna shida ya kukudhuru wala kuchukua gari lako ila kuna kitu tunakihitaji ndani ya hili gari, tukikipata tutakuacha uende zako,” yule mwanamume mrefu mwenye mwili ulioshiba alimwambia Sammy.

“Na msipokipata?” Sammy aliuliza huku akipata shaka, hakuiamini ile kauli ya yule mwanamume mrefu mwenye mwili ulioshiba.

“Tutajua cha kufanya…”

“Kwani kitu gani mnachokihitaji kwangu?” Sammy aliuliza huku akimtupia jicho la wizi yule mwanamume mrefu mwenye mwili ulioshiba.

“Utajua baadaye, kwa sasa endesha gari hadi nitakapokwambia usimame,” yule mwanamume mrefu mwenye mwili ulioshiba alimwambia na Sammy pasipo kubisha aliendesha gari lake pasipo kuhoji. Muda huo akili yake ilikuwa inafanya kazi haraka ili kujinusuru toka katika mikono ile ya watekaji.

Yule mwanamume mrefu mwenye mwili ulioshiba aliikoki bastola yake na kuisogeza katika kichwa cha Sammy. Sammy alibana pumzi baada ya kuuhisi ubaridi wa bomba la bastola. Aliuma meno yake akionekana kuzuia donge la hasira lililoanza kumchonyota kooni. Waliivuka reli ya kuelekea Ubungo na hapo Sammy akataka kugeuza shingo yake kuwatazama.

“Endesha na usigeuze shingo yako kutazama nyuma,” yule mwanamume mrefu mwenye mwili ulioshiba alimwambia Sammy kwa ukali.

Muda wote Bob Chopa alikuwa ameketi katika siti yake akiwa mtulivu mno, alikuwa anatabasamu kama ambaye hakuhusika na lile tukio. Alikuwa anashuhudia kila hatua, jinsi ambavyo yule mwenzake mrefu mwenye mwili ulioshiba alivyokuwa makini kuhakikisha Sammy hafanyi jambo lolote ambalo lingeweza kuwagharimu.

Maara simu yake ikaanza kuita, Bob Chopa aliitazama kwa makini na kupokea mara moja baada ya kuliona jina la mpigaji. “Hallo, boss,” alisema mara baada ya kuiweka sikioni.

“Vipi, Bob, mmefikia wapi?” sauti upande wa pili wa simu ilisikika ikiongea kwa wasiwasi.

“Bado, hatujafika eneo sahihi,” Bob Chopa alijibu na kushusha pumzi.

“Kuweni makini, nadhani kuna mtu anawafuatilia, pia hakikisheni huyo bwana haumii nitamhitaji baadaye kwa matumizi ya nyumbani, tumeelewana?”

“Sawa, boss,” Bob Chopa alisema huku akiachia kicheko hafifu, alikwisha fahamu nini maana yake. Akakata simu huku akimwangalia Sammy kwa makini na kusema. “Kazi kwelikweli!”

“Vipi, kamanda?” yule mwenzake mrefu mwenye mwili ulioshiba alimuuliza Bob Chopa kwa shauku.

“Disko limeingiliwa na Mmasai,” Bob Chopa alijibu huku akiendelea kutabasamu. “Ila usijali, nitacheza naye muziki wowote anaoutaka,” akaongeza huku akiendelea kutabasamu.

“Ongeza mwendo!” yule mwanamume mrefu mwenye mwili ulioshiba alimwambia Sammy baada ya kuona mwendo wa gari umepungua, wakati huo walikuwa wanavuka eneo la Kidarajani.

Simu ya Sammy ikaanza kuita. Sammy akashtuka na kuitupia jicho katika hali ya kukata tamaa kwa kuwa alijua asingeweza kuipokea bila kuruhusiwa na wale watu. Simu yake ilikuwa imewekwa kwenye dashboard. Ilikuwa ni simu kutoka kwa Joyce aliyetaka kujua alikuwa amefika wapi.

Yule mwanamume mrefu mwenye mwili ulioshiba aliitupia jicho la haraka ile simu kisha akayarudisha macho yake kumtazama Sammy kwa makini. Aliamua kuihamisha bastola yake toka kwenye kichwa cha Sammy na kuigandamiza kwenye mbavu zake. Hofu ilizidi kumsonga Sammy. Akaitupia tena jicho simu yake iliyoendelea kuita. Akaanza kuomba Mungu utokee muujiza.

Mara wakaliona gari moja likija kasi nyuma yao, lilikuwa ni gari aina ya Nissan Patrol la rangi nyeusi.Sammy akashusha pumzi za ahueni huku akiendelea kuomba Mungu. Bob Chopa alitoa bastola yake kutoka mafichoni na kujiweka tayari kwa lolote, macho yake aliyakaza kuliangalia kwa makini lile gari lililokuwa linawasogelea.

Wakati huo walikuwa wanalivuka soko la Vingunguti Kwa Simba. Lile gari aina ya Nissan Patrol jeusi likawafikia na kuanza kuwapita huku dereva wake akipiga honi kuonesha kuwa alikuwa na haraka. Wote walilitupia macho na kuyaona maandishi makubwa ya ‘POLISI’ ubavuni. Moyo wa Sammy ukapiga kite. Pah!

Bob Chopa akawa makini kuangalia ndani ya lile gari. Kulikuwa na maofisa wawili wa polisi. Sammy akataka kujaribu bahati yake, akaongeza mwendo ili kwenda sambasamba na lile gari la Polisi huku akigeuza shingo yake kuwatazama wale maofisa wa polisi kwa jicho la kuomba msaada.

Inaendelea...

CC the_legend Norshad bobefu zoefu Pablo PAKAYA Ibney blackstarline Bryece Tater Bigjahman moneytalk marybaby nipo2 ram kisukari Smart911 Madame S carbamazepine Astelia culture gal Prisoner of hope Mine eyes kuku mweus Thad hearly Shunie moneytalk Tumosa Mine eyes Kudo swahiba92 ludist Toyota escudo Clkey macson3 boga la kiangazi LEGE Smart911 Richard irakunda skfull popie Krizy Beat hearly nipo2 MWINDAJI HARAMU kakhulu Katavi Norami mbududa iron2012 popie Bughy Harry Mlenge Kacheda mjasiliamali Laki Si Pesa cocochanel kinusikwetu big jambo mludego Shupavu Kacheda mjasiliamali Mweweso Songa Heri esiankiki mnadhimu mkuu wa jf red apple
 
Taxi - (92)

Ofisa wa Polisi aliyekuwa ameketi upande wa kushoto aligeuza shingo yake kumtazama Sammy kwa macho ya kuuliza. Sammy akajaribu kuonesha hofu usoni kwake ili wale maofisa wa polisi waweze kubaini kuwa alihitaji msaada. Yule mwanamume mrefu mwenye mwili ulioshiba aligundua ujanja wa Sammy, akazidi kuigandamiza bastola yake kwenye mbavu za Sammy.

“Usijaribu kufanya jambo lolote la kijinga. Utajutia uamuzi huo,” yule mwanamume mrefu mwenye mwili ulioshiba alimtahadharisha Sammy kwa sauti ya chini. Kisha akachungulia nje kumtazama yule ofisa wa Polisi na kuachia tabasamu huku akimfanyia ishara ya dole gumba.

Yule ofisa wa polisi naye alionesha ishara ya dole gumba kwa yule mwanamume mrefu mwenye mwili ulioshiba. Sammy hakuwa na ujanja tena, alitulia na kuendesha gari ilhali hofu ikizidi kumtambaa mwilini. Lile gari la Polisi likaongeza mwendo na kuwaacha.

Sammy akashusha pumzi huku akiwa amekata tamaa. Kisha akaonekana kupata wazo, lakini kabla hajafanya chochote simu yake ikaanza kuita tena. Sasa Bob Chopa alinyoosha mkono wake na kuichukua kisha akaitazama kwa makini na kuliona jila “My Wife’ likijitokeza kwenye kioo cha simu. Akaikata na kuizima kabisa.

Wakati huo gari lilikuwa limefika Vingunguti kwenye makutano ya barabara za Barakuda, iliyoelekea Fida na iliyokuwa inakwenda kutokea barabara ya Nyerere. Yule mwanamume mrefu mwenye mwili ulioshiba akamuamru Sammy akunje kuelekea barabara ya Barakuda kupitia machinjioni.

* * * * *

Baada ya Sammy kutoka na hapo hapo Bob Chopa na mwenzake nao wakaondoka haraka kuelekea nje, Tunu alianza kupata hisia tofauti zilizoanza kuumbika kichwani mwake, moyo wake ulipiga kite kwa nguvu, hata hivyo aliendelea kutulia kwenye kiti chake.

Muda huo huo alimwona yule mrembo aliyekuwa ameketi kwenye meza iliyokuwa jirani na mlango wa kuelekea maliwato akiwa na wasiwasi huku akimtupia jicho la wizi Tunu. Tunu alianza kumtazama kwa udadisi huku akijaribu kukumbuka ni wapi na lini alimwona maana sura yake haikuwa ngeni sana kwake.

“Sijui nimemuona wapi huyu mdada?” Tunu alinong’ona kama bwege na
wakati huo zile kumbukumbu chache zilizosalia kichwani mwake kuhusu yule mrembo ziliyeyuka kabisa na kumwacha katika mduwao wa kizembe.

Yule mrembo alinyanyua mkono wake kuitazama saa yake ya mkononi na kisha akageuka na kutazama katika ule mlango wa kutokea mle ukumbini huku akionekana mwenye haraka na wasiwasi. Aliponyanyuka kutaka kuondoka, Tunu naye akanyanyuka. Yule mrembo akaonekana kusita kidogo na kumtupia Tunu jicho la wizi. Macho yao yakagongana.

Muda huo kulikuwa na watu waliokuwa wakiendelea kuingia mle ukumbini na vilevile walikuwepo wengine walioonekana kuondoka. Ulipita muda mfupi yule mrembo akijifanya kutazamatazama huku na kule mle ndani kama aliyekuwa akimtafuta mtu na alipoona kuwa kila mtu alikuwa akiendelea na hamsini zake alielekea maliwato ya wanawake.

Tunu alihisi kuwa huo ulikuwa ujanja tu wa yule mrembo ili kumhadaa kabla hajatoroka, naye akaamua kuelekea kule kule maliwato ya wanawake lakini akiwa na tahadhari kichwani. Alisimama kwa muda pale katika mlango wa kuingilia, baada ya kuhakikisha hali ni shwari akaingia akiwa na nia ya kumbana yule mrembo amweleze ukweli, yeye ni nani na alikuwepo pale kufanya nini.

Alipoingia alijikuta ametokea kwenye ukumbi mpana na msafi wa maliwato uliokuwa na masinki kadhaa ya kunawia mikono. Tunu aliyazungusha macho yake kutazama eneo lile na kuiona milango saba ya.vyumba vya maliwato. Akasubiri pale huku akiwa makini. Aliwaona wanawake wakitoka na wengine kuingia lakini yule mrembo hakumwona.

Alipochunguza vizuri akagundua kioo cha dirisha moja kilikuwa kimevunjwa. Yule msichana mrembo alikwishatoweka. Tunu hakutaka kusubiri, alitoka mbio na kuelekea ukumbini kisha akaufuata mlango mkubwa wa kutokea nje. Alishuka ngazi haraka haraka akiwa hataki kumpoteza yule mrembo. Alipotoka tu nje akagundua kuwa usiku ulikuwa umeshamiri.

Kulikuwa na giza zito lililoashiria kuwa mvua ilikuwa mbioni kunyesha tena hata hivyo kwa msaada wa taa za ule mgahawa na zile za barabarani zilizokuwa kando ya barabara kwenye nguzo ndefu, giza lile zito liligeuka mchana kwa baadhi ya sehemu.

Tunu alishangaa kutomuona yule msichana pale nje, akaamua kutoka kabisa katika eneo lile na kuvuka barabara, akaelekea upande wa pili uliotazamana na ule mgahawa, ambako kulikuwa na teksi kadhaa zimeegeshwa. Akumuona yule mrembo akiwa anatembea kwa mwendo wa haraka kama mwanamtindo aliyekuwa jukwaani katika mashindano ya urembo.

Wakati akitembea yule mrembo alikuwa anageuka kutazama nyuma mara kwa mara akionekana kuwa na wasiwasi. Muda huo alikuwa anaongea na simu. Tunu hakutaka kupoteza muda, akavuka tena ile barabara haraka na kuanza kumfuatilia kwa nyuma lakini katika namna ambayo alikuwa na uhakika kuwa asingeweza kushtukiwa.

Tunu alikuwa akijua namna ya kutembea haraka na alikuwa mwangalifu sana katika nyendo zake. Yule mrembo alikuwa takriban mita thelathini mbele yake, umbali uliomfanya Tunu aweze kujificha haraka kila yule mrembo alipokuwa akijiandaa kugeuka nyuma.

Yule mrembo alipofika mwisho wa barabara ya mtaa ule akaingia upande wa kulia akiifuata barabara nyingine ya lami iliyokuwa inakwenda kutokea barabara ya Uhuru ikikatisha katikati ya mtaa wenye migahawa na maduka kadhaa ya vyakula. Mara akasimama kwenye kioski kimoja cha vinywaji na kugeuka tena nyuma akitazama katika namna ya kujiridhisha kuwa hakukuwa na mtu yeyote aliyekuwa akimfuatilia nyuma yake. muda wote alikuwa anaongea na simu.

Inaendelea...
 
Taxi - (93)

Aliporidhika kuwa hakukuwa na mtu nyuma yake akavuka barabara upande wa pili na wakati akifanya hivyo kuna gari dogo aina ya Toyota Verossa jeusi likatokea na kuufuata ule uelekeo wa yule mrembo. Lilisimama hatua chache pembeni na hapo yule mrembo akafungua mlango wa nyuma na kuingia ndani. Gari likaondoka kwa kasi. Lilikuwa tukio ambalo Tunu hakulitarajia.

* * * * *

Gari la Sammy lilikuwa likiyavuka machinjio ya Vingunguti katika barabara ile ya kuelekea Barakuda na kuanza kuteremsha kwenye mteremko mkali wa bonde la Mto Msimbazi, yule mwanamume mrefu mwenye mwili ulioshiba akamtaka Sammy kuifuata njia nyembamba ya vumbi iliyoingia kushoto kabla hawajalivuka daraja la Mto Msimbazi. Sammy akatii, sasa wakawa wanaelekea eneo yalipo makaburi ya Vingunguti kando ya Mto Msimbazi.

Eneo lile lilikuwa kimya kabisa na mwanga eneo lile ulikuwa hafifu uliotoka kwenye taa za nyumba zilizokuwa ng’ambo ya Mto Msimbazi, mbali kidogo na eneo lile. Kiujumla eneo lile lilitisha mno kwa ukimya uliotawala. Yule mwanamume mrefu mwenye mwili ulioshiba akamwelekeza Sammy eneo la kusimama.

Sammy hakubisha, alikanyaga breki na kulisimamisha gari lake eneo lile huku akimtupia jicho yule mwanamume mrefu mwenye mwili ulioshiba kwa wasiwasi kidogo. Bastola yake ilikuwa bado imegusa mbavu zake.

“Zima injini, fungua mlango utoke nje na uinue mikono yako juu,” yule mwanamume mrefu mwenye mwili ulioshiba aliamrisha.

Sammy alifanya kama alivyoelezwa, alizima injini ya gari lake, akachomoa ufunguo wa gari na kuushika mkononi. Lakini kabla hajafungua mlango Bob Chopa alishuka haraka na kuufuata mlango wa dereva, akashika kitasa na kuufungua huku akimtazama Sammy kwa makini kama simba jike anayewinda nyati.

Sammy alishuka na kutaka kuanza kuleta utata. Bob Chopa aliishika vyema bastola yake akiielekeza kwa Sammy, tayari kwa lolote. Wakati huo huo yule mwanamume mrefu mwenye mwili ulioshiba alikuwa ameshashuka toka garini na kusimama akiielekeza bastola yake kwenye kichwa cha Sammy.

Sammy akagwaya. Alishusha pumzi huku akinyoosha mikono yake juu kama ishara ya kusalimu amri. Akaamuriwa kukaa chini akiwa ameweka mikono yake kichwani.

“Kamanda, hatuna muda wa kupoteza, pekua gari chapchap tusepe. Huyu fala niachie mimi,” Bob Chopa alimwambia yule mwanamume mrefu mwenye mwili ulioshiba.

Yule mwanamume mrefu mwenye mwili ulioshiba aliingia ndani ya gari, akavuta siti ya mbele ya abiria upande wa kushoto na kuinama. Akaangalia chini ya kile kiti. Patupu! Akamfuata Sammy aliyekuwa amedhibitiwa na Bob Chopa. “Umeiweka wapi?” alimuuliza Sammy huku akimkazia macho.

“Nini?” Sammy alimuuliza huku akimtazama kwa mshangao. Hakuelewa walichokuwa wanakitaka toka kwake.

“Kadi! Umeiweka wapi?” yule mwanamume mrefu mwenye mwili ulioshiba akamuuliza kwa msisitizo.

“Kadi gani?” Sammy aliuliza huku akiendelea kushangaa.

Memory card, umeiweka wapi?”

“Sijakuelewa, memory card ipi?” Sammy alizidi kushangaa.

Yule mwanamume mrefu mwenye mwili ulioshiba alimtazama Sammy kwa kitambo kifupi pasipo kumjibu, kisha alirudi ndani ya gari na kuanza kufanya upekuzi wa haraka haraka kila mahali lakini akiwa makini. “Sioni kitu, huyu fala anajua alipoiweka!” alisema akionekana kukata tamaa.

Bob Chopa akiwa bado ameshika bastola yake kwa umakini alitoa simu yake ya mkononi na kubofya namba kadhaa, akaweka kwenye sikio lake na kusikiliza kidogo wakati ile simu ikiita. Muda mfupi baadaye simu ilipokelewa na upande wa pili.

“Bosi, hatujapata kitu…” Bob Chopa alisema huku akimkazia macho Sammy. Akasikiliza kwa kitambo kidogo na kubetua kichwa chake huku akitabasamu. “Okay! Nimekuelewa.” akakata simu.

“Hili gari umeanza kulimiliki lini?” Bob Chopa alimuuliza Sammy huku akiendelea kutabasamu lakini akiwa amemkazia macho.

“Kwani vipi?” Sammy aliuliza kwa mshangao huku naye akimkazia macho Bob Chopa.

“Jibu swali langu,” Bob Chopa alisema kwa ukali kidogo.

Sammy alibaki kimya akimtazama Bob Chopa kwa hasira, akili yake ilikuwa inajaribu kufanya kazi haraka haraka akijaribu kupanga namna ya kujinasua toka mikononi mwa wale watu.

“Umeanza kulimiliki lini hili gari?” Bob Chopa alirudia tena swali lake huku akimkazia macho Sammy.

“Sijui,” Sammy alijibu kwa mkato huku ghadhabu zikianza kumpanda. Donge la hasira lilikuwa limemkaba kooni na kumfanya aanze kupumua kwa shida. Aliona watu wale walikuwa wanamchelewesha kufika nyumbani kwake kuyaokoa maisha ya mtoto wake Pendo. Hakujua mtoto wake alikuwa na hali gani muda huo.

“Naona sasa anaanza kuwa jeuri,” alisema yule mwanamume mrefu mwenye mwili ulioshiba na kumsogelea Sammy. Kufumba na kufumbua Sammy akawa amewekwa mtu kati na wale watu walioonekana kudhamiria kumuua. Walizishika vyema bastola zao na kumuelekea Sammy.

Sammy alitweta, ujanja wowote ule ambao angejaribu kuufanya mbele ya silaha zile ungeweza kumgharimu maisha yake kwa kuchakazwa vibaya kwa risasi jambo ambalo hakuwa tayari litokee. Hata hivyo, hakutaka kufa kibudu, aliamua kupambana. Alisimama akiwa tayari kwa lolote, aliamini kuwa hawakujua kama walikuwa wanacheza na mtu hatari ambaye hakutakiwa kufanyiwa mchezo.

Kitu alichokuwa anamshukuru Mungu mpaka wakati huo ni kumpa uwezo wa kufikiri na kufanya uamuzi sahihi na wa haraka. Ingawa hajawahi kukumbana na misukosuko mikubwa kama hiyo lakini kila alipojikuta katika sehemu hatari ambayo si rahisi kwa mtu wa kawaida kujiokoa aliweza kutumia uwezo wake wa kufikiri na kuamua kwa haraka ili kujiokoa.

Wakati wakiwa wanaangaliana kwa ghadhabu Sammy akashangaa kumwona Bob Chopa akiachia tabasamu kisha akashusha chini bastola yake.

“Tuondoke, tutatafuta namna nyingine ya kuipata,” Bob Chopa alimweleza yule mwanamume mrefu mwenye mwili ulioshiba. Na hapo wakaanza kuondoka toka eneo lile wakimwacha Sammy katika mshangao.

Alisimama pale pale akiwatazama kwa makini akiwa haamini kama kweli waliamua kuondoka, alidhani ule ulikuwa mtego wao ili wapate kumdhuru lakini akashangaa kuwaona wakizidi kuyoyoma na kupotelea kizani, wala hakujua walikoelekea. Watu hawa ni akina nani? Walikuwa wanataka nini? Na nani aliyewatuma? Sammy alijiuliza bila kupata majibu.

Mambo yanazidi kunoga, usikose kuifuatilia stori hii ya kusisimua...
 
Naam! Naona umekaa mkao wa kula, natamani sana nitupie japo episode mbili lakini nipo chimbo na sina access ya stori yangu hadi nitoke hapa...
Umeitikia.. kilainiii...

Subiri..Legend aje...

Watu wa Darisalama..shkamoo...yaani kupata mke kwa riwaya tu?

Dah@!

Bishop upo?

Twende kazi nijipoze machungu ya dunia hii mbaya!..
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom