Taxi - (97)
“Sasa nataka uyajibu vizuri maswali yangu na usilete hila yoyote kwani nakuhakikishia kuwa mimi si Lisa yule uliyekuwa ukimfahamu. Kwa sasa hakuna kiumbe yeyote msumbufu anayeweza kuingia anga zangu akaniponyoka,” Lisa alimwonya Tunu huku akiachia tabasamu la dharau.
* * * * *
Gari aina ya
Cadillac DeVille lilifunga breki mita therathini kabla halijaifika nyumba ya Sammy baada ya kusimamishwa na askari mmoja aliyekuwa amebebelea bunduki na kifua chake kikiwa kimekingwa na vazi maalumu linalozuia risasi. Kulikuwa na kundi la watu waliokuwa wamejazana eneo lile wakiwa na nyuso za huzuni.
Wakati huo aliwaona askari wengine wawili ambao pia walivaa mavazi ya kuzuia risasi na kubebelea bunduki waliokuwa wanaweka utepe maalumu wa njano katika eneo lile kuashiria hali ya hatari. Walikuwa wanapashana habari na watu wengine ambao hawakuwepo eneo lile kwa vifaa maalumu vya kisasa vya mawasiliano. Wale askari wenye silaha walikuwa wanajitahidi kuwazuia watu wasisogee katika eneo lile huku nyuso zao zikionesha wazi kuwa walikuwa tayari kwa lolote, tayari kuua, tayari kufa.
Sammy alishikwa na bumbuwazi, aliteremka toka kwenye gari lake na kusimama akiwatazama wale askari kwa makini, alipouona ule utepe wa njano ukizingushwa katika eneo la nyumba yake moyo wake ukapiga kite, ukaanza kwenda mbio isivyo kawaida na mwili ukaishiwa na nguvu.
“Kuna nini?” Sammy aliwauliza wale askari wenye silaha kwa wasiwasi huku akili yake ikikataa kuamini kama kulikuwa na tatizo nyumbani kwake. Askari yule alikuwa anakagua eneo lile huku akiwasiliana na watu ambao hawakuwepo eneo lile.
“Majambazi,” yule askari alimjibu kwa kifupi huku akiendelea kukagua eneo lile.
“Wako wapi?”
“Wametoroka na pikipiki.”
Kauli ile ikamfanya Sammy amkumbuke yule mtu aliyekuwa anaendesha pikipiki kwa mwendo wa kasi ya ajabu kama mwendawazimu na kuingia upande wake akitaka kumgonga, akashusha pumzi.
“Kwa hiyo kumetokea nini huko ndani?” Sammy alizidi kuuliza huku wasiwasi ukimtawala.
“Kwani wewe ni nani unayeniuliza maswali ya kipolisi?” yule askari alimuuliza Sammy huku akimkazia macho.
“Mimi ndiye mwenye nyumba hii, nilipigiwa simu nirudi haraka kuna tatizo,” Sammy akasema huku akianza kukereka.
“Basi ndiyo kama ulivyosikia,” yule askari akamwambia Sammy.
“Kusikia nini! Unajua hadi sasa sielewi kilichotokea?”
“Ni kwamba majambazi walivamia nyumba hii, hatujajua bado walichokuwa wakikitaka ila kuna mwanamke, sijui kama ni mkeo amepigwa risasi...” askari mmoja alimwambia Sammy.
Moyo wa Sammy ukapiga kite kwa nguvu kama aliyepigwa konde zito kichwani bila kutarajia. Hakusubiri tena kuambiwa, alichomoka na kukimbilia ndani kama mtu aliyepagawa. Askari mmoja akataka kumzuia lakini alishachelewa kwani Sammy alishafika getini na kuzama ndani. Pale sebuleni alimkuta Joyce akiwa sakafuni amelalia dimbwi la damu huku akikoroma kwa maumivu. Upesi Sammy alimkimbilia na kutaka kumnyanyua bila kujali damu.
“Mama Pendo! Mama Pendo!” Sammy aliita huku akimgeuza Joyce. Wale askari walimshika Sammy na kumzuia. Sammy akaanza kuleta purukshani huku akipiga kelele kama aliyepandwa na wazimu kichwani lakini wale askari walidhibiti kisawasawa.
“Mama Pendo!
Please don’t die!" Sammy aliita na Joyce akafungua macho lakini hakuweza kusema chochote. Mwili wake haukuwa na nguvu kwani alipoteza damu nyingi.
“Mama Pendo, tafadhali usituache, bado tunakuhitaji. Siwezi kuishi bila wewe, Mama Pendo!” Sammy alisema kwa uchungu huku akimtazama Joyce kwa huzuni, machozi yalikuwa yanamtoka. “Ee Mungu baba, nakuomba usimchukue mke wangu,” Sammy aliomba kimyakimya huku akishusha pumzi za kukata tamaa,
Alitupa macho yake kando na kuwaona Winifrida na Pendo wakiwa wamesimama wanalia kwa uchungu. Sammy aliwasogelea, akambeba Pendo huku akiwakumbatia wote kwa uchungu. Hakika lile tukio la kupigwa risasi Joyce lilikuwa pigo kubwa kwao wote, ni kama pigo la kisu lililopenya mwilini na kujeruhi mioyo yao.
Akiwa bado amewakumbatia Pendo na Winifrida, Sammy aliwashuhudia watu wawili waliovalia makoti marefu meupe na glavu nyeupe mikononi wakiingia haraka mle ndani wakiwa wamebeba machela, wakambeba Joyce na kumlaza kwenye ile machela kisha wakatoka naye na kupeleka katika gari la wagonjwa lililokuwa limeegeshwa nje.
Sammy hakutaka kubakia pale, aliwakabidhi Winifrida na Pendo kwa wale askari aliowakuta mle ndani kisha akatoka kumfuata Joyce kule kwenye gari.
* * * * *
“Nilihisi tu kuwa mtafanya makosa… nilijua tu,
we are fucked up!” sauti ya Mr. Oduya ilisikika kwenye simu, ikapenya katika ngoma ya sikio la Spoiler hadi kwenye ubongo wake na kumfanya asisimkwe mwili kwa hofu.
“Lisa aliponipigia simu kunieleza kuwa Sammy yupo na Tunu nikajua kila kitu kimeharibika...” Mr. Oduya alisema kwa sauti yenye mtetemo na kuendelea, “Mbaya zaidi, Sammy aliondoka na watu wawili ambao kwa vyovyote walipandikizwa na Tunu ili kumlinda ndiyo maana hakufika nyumbani. Sijui huyu Tunu ametokea wapi baada ya miaka yote hii na ilikuwaje mkashindwa kubaini kuhusu uwepo wake?”
Kwa mara ya kwanza katika harakati za namna ile Spoiler alianza kuhisi hofu ikimtambaa mwilini mwake.
“Sasa, hakuna haja ya Sammy kukamatwa na kupelekwa kule Kinondoni, ninachotaka ni kifo tu, afe tu basi! Tena siyo yeye tu, nataka Tunu naye afe, halafu niletewe vichwa vyao hapa!” Mr. Oduya alisema kwa ghadhabu.
“Nitakuongezea watu, sijui umenielewa!” Mr. Oduya alipaza sauti kwa ukubwa kiasi cha kumfanya Spoiler aisogeze simu yake mbali na sikio kwa kuhofia kuleta madhara kwenye ngoma ya sikio.
“Nimeelewa!” Spoiler alisema na kushusha pumzi.
Spoiler alikuwa amesimama katika eneo la makaburi ya Vingunguti yaliyopo katika bonde la Mto Msimbazi baada ya kutoka nyumbani kwa Sammy eneo la Tabata Chang’ombe. Eneo lile la makaburi ya Vingunguti lilikuwa moja ya maeneo yaliyotisha sana kutokana na sifa yake ya kuwa eneo hifadhi la wahalifu waliokuwa wakivizia wapita njia ili kuwakaba na kuwaibia mali zao.
Spoiler alifika eneo lile baada ya purukshani nyingi barabarani, laiti kama asingekuwa mzoefu wa harakati kama zile angekamatwa au angeuawa. Nguo zake zilikuwa zimetapakaa damu. Aliutazama mwili wa Dulla Mcomoro ambao haukuwa na uhai jinsi ulivyolala kifudifudi juu ya pikipiki. Alitamani kuutupa pale makaburini lakini aliogopa ingeweza kuwaletea shida baadaye kwa kuwa Dulla alikuwa anafahamika kuwa na ukaribu na Mr. Oduya.
Mambo ni 

usikose kufuatilia simulizi hii ya kusisimua...