Taxi - (88)
ILIPOISHIA
Sammy alimchukua Tunu hadi kwenye nyumba aliyokuwa amepanga eneo la Makumbusho, Kijitonyama. Siku hiyo Tunu alikuwa amevaa blauzi na kaptula ya kitenge. Kaptula ile iliishia juu ya magoti yake na kuifichua minofu ya miguu na mapaja yake yaliyonona.
“Nimekuja mara moja tu kukusalimia, sitakaa muda mrefu,” Tunu alisema huku akiitazama saa yake ya mkononi mara tu walipoingia ndani. Hata hivyo, Tunu alikuwa akimtazama Sammy kwa macho ya wizi, macho yake yalikuwa yamelegea kama aliyekuwa amekula kungu, sura yake ilionekana wazi kumsubiri Sammy afanye kitu.
Sammy aligundua kuwa Tunu alikuwa amekolea ingawa haikuwa rahisi kwake kukubali moja kwa moja, akamshika mkono. Hakuleta pingamizi lolote, kwani alionekana kutojiweza na uso wake aliuinamisha chini kwa aibu. Alimvutia kifuani kwake akamkumbatia. Tunu alijigandamiza kwenye mwili wa Sammy na kutulia huku akihema kwa nguvu.
Sammy hakuendelea kusubiri, alimbeba hadi kitandani, akamwangusha kama mzigo. Tunu pumzi zilimpaa! Kilichofuata baada ya hapo kilimfanya ahisi kuchanganyikiwa. Alijikuta akiwa taabani huku akiyashuhudia maumivu ya kupendeza yaliyokuwa yakimuua taratibu kama mgonjwa taabani. Yote yaliyotendeka kwenye mwili wake hakuwahi kuyaona ndotoni au hata kuyafikiria.
ENDELEA...
Hakujimudu na wala hakuweza kuvumilia, alitapatapa kama samaki anayekaangwa hai, akaanza kulia. Kilikuwa kilio cha faraja kilichotokana na adhabu aliyojitakia mwenyewe ambayo wala hakuijutia. Alilia na machozi yakamtoka, sauti ikamkauka. Ilikuwa ni siku ya aina yake kwake, siku ambayo kamwe isingepotea katika fikra zake.
Mechi ilipoisha Tunu hakuweza hata kumtazama Sammy machoni, alikuwa anatweta kama aliyemaliza mbio ndefu za kilomita arobaini na mbili baada ya kuvunja rekodi ya dunia. Aliyafuta machozi yake kwa kiganja cha mkono na kushusha pumzi ndefu.
“Pole mpenzi, pole sana…” Sammy alimpa pole Tunu huku akicheka kimoyomoyo, kilikuwa kicheko cha ushindi.
“Mmh, hakyamungu ungeniua,” Tunu alisema kwa sauti legevu ya chini huku akipiga miayo.
“Usijali, mpenzi wangu, utazoea tu. Hata hivyo, umenifurahisha sana, you’re a real gift to me. Kuanzia leo sitakuita Tunu bali wewe ni Gift…”
Tunu aliitazama saa yake na kushtuka, ilikuwa imeshatimu saa mbili na nusu usiku, akaamua kuaga na kuondoka, alikuwa hoi. Sammy alimsindikiza hadi kituo cha daladala, wakapeana mabusu motomoto ya kuagana kisha akampandisha daladala la kuelekea Sinza huku wakiahidiana kukutana baada ya siku tatu, lakini tangu siku hiyo Sammy hakuweza kumtia tena machoni Tunu! Bahati mbaya hakuwa akijua Tunu aliishi Sinza ipi, maana Sinza ni kubwa ati!
Sammy alikuwa kama mwehu, alizunguka mji mzima kumtafuta Tunu, alifika kila pembe ya Sinza na viunga vyake, aliuliza watu aliodhani wangeweza kuwa na taarifa za Tunu, lakini hakuna alichoambulia ambacho kingeweza kumsaidia kujua alipo. Alimfuata Grace, dada wa Elli ambaye alisoma darasa moja Tunu, lakini pia hakupata habari zake.
Kutokuonekana kwa Tunu katika maisha ya Sammy kulimwathiri sana kisaikolojia na hata kuathiri utendaji wake wa kazi za kila siku. Alijikuta akiwa na mwili wa mgonjwa akisubiri kifo ili arudi mavumbini, ubongo upo hospitali na nafsi kwa Mungu. Tabibu pekee wa kuutibu ugonjwa wake alikuwa mmoja tu, Gift!
Alimuwaza yeye tu muda wote. Mbele ya uzuri wa kiumbe aliyemwita Gift, Sammy alijiona kama limbukeni wa mapenzi. Gift alikuwa amemwachia shimo kubwa sana moyoni liitwalo mapenzi. Shimo ambalo hakukuwa na mtu mwingine wa kuliziba isipokuwa yeye tu. Kwa miaka miwili Sammy hakujiweza, kutwa kucha alimwaza Gift tu! Alishangaa, iweje mrembo yule apotee ghafla katika kipindi ambacho alimhitaji mno?
Katika kipindi cha miaka miwili tangu kutoweka kwa Tunu, Sammy alishindwa kabisa kumwondoa moyoni mwake, mawazo kuhusu Gift yalimpitia kila siku na kila alipolikumbuka jina lake moyo wake ulimwenda mbio kama mtu aliyekuwa na ugonjwa wa wasiwasi. Alijiuliza iwapo hali ile ilikuwa ni matokeo ya kumpenda sana Gift, ingekuwaje pindi angesikia kuwa ameolewa na mwanamume mwingine?
Yako wapi yale macho yake mazuri yenye mvuto wa ajabu yaliyomtia utumwani? Hivi iliwezekanaje kwa msichana kama Gift, aliyeamini ni zawadi yake kutoka kwa Mungu, kutoweka ghafla na kumwacha yeye katika kipindi kama kile? Kuachwa si kioja, laiti angelipewa nafasi ya miaka kadhaa kusema na roho yake pengine angeweza kuwa na uamuzi mzuri zaidi, ingawa ni ajabu sana kwa donda ndugu kupona!
Baada ya miaka miwili ya maisha ya mateso, Sammy alijiambia kuwa ilikuwa imetosha, huo sasa ulikuwa ni wakati mwafaka wa yeye kuanza maisha mapya kwani hakuweza kuendelea kumsubiri mtu ambaye hakujua yupo wapi, kama ni mzima au amekufa. Ni katika kipindi hicho ambacho Sammy alikutana na Joyce wakati akitoka Tanga kutembelea mapango ya Amboni. Kipindi ambacho Joyce alikuja kwenye maisha yake kama malaika mwokozi aliyeshushwa kumwondolea machungu ya kukimbiwa na Gift. Yote yaliyokuja kutokea baadaye yamebaki kuwa historia…
“Sammy!” sauti nyororo ya Tunu ilimzindua Sammy kutoka kwenye lindi la mawazo. Sammy alimtazama Tunu akamwona akiwa anamtazama kwa utulivu huku akitabasamu.
“Gift!” Sammy alimudu kusema huku akishusha pumzi za ndani kwa ndani. “Ninahitaji kujua ukweli na tafadhali naomba usiniongopee. Niambie ukweli hata kama ukweli huo utaniumiza sana,” Sammy alimwambia Tunu huku akimtazama usoni kwa makini.
“Unataka kujua nini, Sammy?” Tunu aliuliza huku akiwa makini kusikiliza alichotaka kuambiwa.
“Kwa nini ulinikimbia? How could you do this to me? ” Sammy aliuliza huku akimtazama Tunu kwa uchungu mkubwa. “Maybe I was not important to you at all,” aliongeza kabla Tunu hajasema neno.
Kwa sekunde chache Tunu alibaki kimya akimtumbulia macho Sammy akiwa hajui niseme nini, hakuweza kabisa kumjibu bali alibaki kimya huku akimtazama kwa makini. Kila alipotaka kujieleza alihisi kukosa ujasiri.
“Kwa nini ukaamua kutupa jongoo na mti wake! Tunu I need to know the truth,” Sammy alisema huku akiwa ameyatuliza macho yake kwenye uso wa Tunu.
“I’m so sorry…” Tunu alisema kwa sauti ya chini.
“Sorry? Baada ya miaka yote hii ya kunipa mateso leo unaniambia kirahisi rahisi tu, eti I’m so Sorry! Sorry for what? I’m disappointed, very disappointed,” Sammy alishindwa kuvumilia akaanza kuzungumza kwa sauti kubwa na kuwafanya watu wengine wageuze shingo zao kuwatazama kwa mshangao.
“Enough! Can you please stop blaming me?” Tunu naye alikuja juu na kusema kwa sauti ya ukali huku akikunja sura yake.
Kwa kitambo fulani hali ya mahali pale ilikuwa tete, walibaki kimya wakiwa wanaangaliana kama majogoo yaliyotaka kupigana. Tunu alishusha pumzi za ndani kwa ndani.
Inaendelea...