Nimekakumbuka kale ka nyimbo kanakoimba alosto alosto
Taxi - (84)
ILIPOISHIA
“Hivi, yule bwana anayeendesha lile gari la kizamani aina ya Cadillac DeVille atarudi kweli, maana nilikuwa nahitaji huduma yake lakini nashangaa hadi sasa sijamwona!” Tunu alimuuliza yule mhudumu huku akipitisha ulimi wake kulamba midomo yake.
“Sina uhakika, kwani huna namba yake ya simu umpigie?” yule mhudumu aliuliza huku akiyatupa macho yake kutazama kwenye meza aliyoketi mzungu na wanawake wawili wa kibantu waliokuwa wakimwita.
“Ningekuwa nayo wala nisingehangaika kukuuliza,” Tunu aliuliza ma kuminya midomo yake.
“Basi endelea kusubiri, maana subira yavuta heri,” yule mhudumu alisema na kuanza kupiga hatua kwenda kwenye ile meza alikoitwa. Tunu alishusha pumzi na kujiegemeza kwenye kiti chake na kuyatupa tena macho yake kwa yule mwanadada aliyeketi peke yake ambaye hakulijua jina lake.
Alimwona akiinamisha kichwa chake kama aliyeona kitu katika bilauri yake ya bia, alitazama ndani ya ile bilauri kwa kitambo kisha aliinua uso wake taratibu kwa madaha kana kwamba alikuwa anaigiza filamu, mara macho yao yakakutana. Kwa dakika nzima macho yao yalitulia yakitizamana kama ambao walikuwa wakisomana fikra zao, kisha yule mwanadada aliyahamisha macho yake na kutazama kando.
SASA ENDELEA...
Muda huo huo simu yake ya mkononi ikaanza kuita, ilikuwa ni simu ghali ya kisasa aina ya
Samsung Galaxy Fold. Yule msichana aliitazama kwa kitambo akionekana kama aliyekuwa akijishauri iwapo aipokee au aipotezee, akabana taya zake na kuipokea kisha akaipeleka moja kwa moja sikioni.
Alionekana kuwa mtulivu sana alipokuwa akiongea na simu, muda wote alipokuwa akiongea alikuwa akimtupia Tunu jicho la wizi na baada ya mazungumzo ya takriban dakika mbili alikata simu na kushusha pumzi za ndani kwa ndani.
Sasa alionekana kuanza kukosa uvumilivu, aliitazama tena saa yake na kukunja sura yake kisha akachukua chupa ya bia iliyokuwa juu ya meza na kumimina bia katika bilauri, bilauri ilijaa na bia kuanza kumwagika juu ya meza hali akiwa hana habari, alikuwa amezama kwenye lindo la mawazo.
Aliposhtuka bia ile ilikuwa imemlowesha kwenye sketi yake, akashtuka na kuruka huku akijaribu kuyaepuka macho ya watu yaliyokuwa yakimtazama kwa mshangao, alichukua tishu na kujifuta huku akisonya. Muda huo huo mhudumu alifika kwenye meza yake na kufuta meza huku akimpa pole.
Baada ya mhudumu kuondoka yule msichana alinyanyua bilauri yake na kuigida bia yote iliyokuwemo katika bilauri hiyo kisha akaikita ile bilauri juu ya meza na kunyanyuka, huku akimtazama Tunu kwa jicho la wizi akachukua simu yake na kuelekea maliwato.
Tunu alikuwa ametulia tuli akinywa mvinyo wake taratibu huku akijifanya kutoona kilichokuwa kikiendelea kwa yule msichana, alihisi kuwepo kwa jambo lisilo la kawaida na kujikuta akitamani kufuatilia ili ajue lakini hakufanya hivyo kwa kuhofia kuchanganya mambo, kwani hakuwepo pale kwa jambo jingine lolote isipokuwa lile lililompeleka hapo.
* * * * *
Saa tatu na ushee usiku, Joyce alikuwa kasimama barazani akionekana kutokuwa katika hali nzuri japo alijitahidi kuwa mtulivu sana. Alikuwa amevaa vazi la kulalia, kiunoni kajifunga khanga na kiganja cha mkono wake wa kushoto kakitumbukiza ndani ya khanga kwa mbele. Mkono wa kulia ulikuwa ameshika simu yake akiigongagonga kwenye shavu lake la kulia. Alionekana yuko mbali sana kimawazo.
Mtoto wake Pendo hakuwa amelala hadi muda huo, alikuwa amesimama kando yake akiwa ameng'ang'ania khanga ya mama yake. Joyce hakuonekana kumjali bali akili yake ilikuwa mbali, nje kabisa ya mahala pale aliposimama.
Joyce aliitazama ile simu aliyoishika, akashusha pumzi na kutafuta namba ya Sammy, akabofya ili kupiga lakini ghafla akaonekana kughairi na kuikata. Muda huo huo akasikia mvumo wa gari lililokuwa likisogea eneo lile. Joyce akatega vyema sikio lake kwa makini akijaribu kubaini sauti ya mvumo ule.
Gari lilipofika usawa wa nyumba yao likaongeza mwendo na kupitiliza na kumfanya Joyce aume meno yake kisha akayaachia, aliganda pale pale asijue la kufanya. Mara mvumo mwingine wa gari ukasikika tena ukisogea eneo lile na kupita. Joyce aliuma tena meno yake huku machozi yakimlengalenga.
Alishusha pumzi na kumtupia jicho Pendo aliyekuwa bado kamng’ang’ania khanga yake huku akimwangalia usoni kwa udadisi bila kusema jambo. Joyce alimtazama Pendo na kushtuka, akaufunika uso wake kwa khanga kujifuta machozi. Kisha aligeuka na kuingia sebuleni.
Hapo sebuleni alisimama karibu na kabati la vyombo. Pendo naye alimfuata kila aendako, pia alisimama huku akiendelea kumwangalia mama yake usoni kwa udadisi. Alikwisha hisi kuwepo kwa jambo lisilo la kawaida lakini hakuthubutu kuuliza.
Joyce alionekana kuzidiwa na mawazo, bila kufikiri akipiga ngumi ukutani kwa nguvu na kumshtua sana Pendo aliyemtazama mama yake kwa hofu. Joyce alishindwa kuvumilia, alichuchumaa pale alipokuwa amesimama, akajiegemeza na ukuta na kuanza kulia kimya kimya kwa uchungu huku uso akiwa kaufutika kwenye khanga aliyojifunga. Pendo alisogea pambeni kwa hofu.
Muda huo huo Winifrida alitokea sebuleni akiwa na uso wa mshangao, hofu na udadisi. Aliangaza macho yake na kumwona Joyce akiwa kajikunyata ukutani huku akilia kilo cha kwikwi. Winifrida alimtazama kwa wasiwasi na macho yake yakahamia kumtazama Pendo ambaye alikuwa amesimama kando akiwa ameduwaa, alikuwa anamshangaa mama yake huku machozi yakimlengalenga machoni.
Winifrida alifyatuka haraka toka pale alipokuwa amesimama na kumfuata Pendo, alimshika na kumnyanyua kisha akaelekea naye chumbani huku akimtuliza na kumwacha Joyce bado kajikunyata akilia kwa uchungu.
* * * * *
Tunu aliitazama saa yake kwa mara ya mia moja, dakika nyingine therathini na tano zilikuwa zimepita, zaidi ya muda aliokuwa ameukadiria. Alishusha pumzi za ndani kwa ndani na kunyanyua bilauri iliyokuwa na mvinyo, akapiga funda kubwa na kuunywa mvinyo wote uliokuwemo.
Uso wake ulionesha wasiwasi, alishusha pumzi na kumtupia jicho yule mwanadada aliyekuwa ameketi peke yake akinywa bia taratibu, akamwona sasa akiwa ameketi na mtu mwingine, mwanamume ambaye kwa mtazamo tu alionekana kunuka fedha. Uso wake ulikuwa umetulia akionekana hana wasiwasi na anacho kila kitu ambacho angeweza kukihitaji duniani.
Tunu hakutaka kuendelea kukaa hapo huku akiwa hajui mtu aliyekuwa akimsubiri angefika saa ngapi, alitaka kunyanyuka lakini akasita baada ya kumwona mwanamume mmoja mrefu na mweupe mithili ya chotara wa kizungu akiingia ndani ya ukumbi. Mwanamume huyo mwenye sura ya tabasamu muda wote alikuwa anatembea kwa madaha huku akizungusha macho yake kutazama watu walioketi mle ukumbini. Mkononi alikuwa ameshika funguo za gari lake akizungusha kwenye kidole chake cha shahada.
Inaendelea...
CC
the_legend Norshad bobefu zoefu Pablo PAKAYA Ibney blackstarline Bryece Tater Bigjahman moneytalk marybaby nipo2 ram kisukari Smart911 Madame S carbamazepine Astelia culture gal Prisoner of hope Mine eyes kuku mweus Thad hearly Shunie moneytalk Tumosa Mine eyes Kudo swahiba92 ludist Toyota escudo Clkey macson3 boga la kiangazi LEGE Smart911 Richard irakunda skfull popie Krizy Beat hearly nipo2 MWINDAJI HARAMU kakhulu Katavi Norami mbududa iron2012 popie Bughy Harry Mlenge Kacheda mjasiliamali Laki Si Pesa cocochanel kinusikwetu big jambo mludego Shupavu Kacheda mjasiliamali Mweweso Songa Heri esiankiki mnadhimu mkuu wa jf red apple