Stori ya kusisimua - Taxi

Stori ya kusisimua - Taxi

Taxi - (94)

ILIPOISHIA

Kufumba na kufumbua Sammy akawa amewekwa mtu kati na wale watu walioonekana kudhamiria kumuua. Walizishika vyema bastola zao na kumuelekea Sammy.

Sammy alitweta, ujanja wowote ule ambao angejaribu kuufanya mbele ya silaha zile ungeweza kumgharimu maisha yake kwa kuchakazwa vibaya kwa risasi jambo ambalo hakuwa tayari litokee. Hata hivyo, hakutaka kufa kibudu, alidhamiria kupambana. Alisimama akiwa tayari kwa lolote, aliamini kuwa hawakujua kama walikuwa wanacheza na mtu hatari ambaye hakutakiwa kufanyiwa mchezo.

Kitu alichokuwa anamshukuru Mungu mpaka wakati huo ni kumpa uwezo wa kufikiri na kufanya uamuzi sahihi na wa haraka. Ingawa hajawahi kukumbana na misukosuko mikubwa kama hiyo lakini kila alipojikuta katika sehemu hatari ambayo si rahisi kwa mtu wa kawaida kujiokoa aliweza kutumia uwezo wake wa kufikiri na kuamua kwa haraka ili kujiokoa.

Wakati wakiwa wanaangaliana kwa ghadhabu Sammy akashangaa kumwona Bob Chopa akiachia tabasamu kisha akashusha chini bastola yake.

“Tuondoke, tutatafuta namna nyingine ya kuipata,” Bob Chopa alimweleza yule mwanamume mrefu mwenye mwili ulioshiba. Na hapo wakaanza kuondoka toka eneo lile wakimwacha Sammy katika mshangao.

Alisimama pale pale akiwatazama kwa makini akiwa haamini kama kweli waliamua kuondoka, alidhani ule ulikuwa mtego wao ili wapate kumdhuru lakini akashangaa kuwaona wakizidi kuyoyoma na kupotelea kizani, wala hakujua walikoelekea. Watu hawa ni akina nani? Walikuwa wanataka nini? Na nani aliyewatuma? Sammy alijiuliza bila kupata majibu.

ENDELEA...

Kitu kimoja tu alichokifahamu kwa wakati huo ni kwamba, eneo lile alilokuwa amesimama usiku huo halikuwa eneo salama hata kidogo, hivyo hakutakiwa kuendelea kuwepo pale. Bila kujali kama ule ulikuwa mtego au lah aliingia ndani ya gari lake na kuwasha injini kisha akaligeuza na kuondoka kwa kasi.

* * * * *

Ilikuwa inaelekea kutimia saa tano kamili usiku, gari dogo aina ya Land-Rover 110 jeupe la POLISI lilikuwa linaendeshwa kwa mwendo wa kasi mno kuelekea mtaa mmoja katika eneo la Tabata Chang’ombe, ndani ya gari lile mbele kulikuwa na askari wawili, mmoja akiwa ndiye dereva wa gari. Nyuma ya gari lile kulikuwa na askari sita waliokuwa wamebebelea bunduki na vifua vyao vimekingwa na mavazi maalumu yanayozuia risasi ‘bullet proof’. Askari hao walikuwa na sura ya kazi.

Jinsi walivyosimama nyuma ya gari lile ilionesha wazi kuwa mambo hayakuwa shwari kabisa huko walikokuwa wanaelekea.

Gari lile liliingia katika mtaa anaoishi Sammy na kupunguza mwendo baada ya kuikaribia nyumba ya Sammy, kitendo kile kikawafanya polisi watatu waruke kutoka nyuma ya lile gari katika mtindo wa kivita na kujiviringisha barabarani kama maninja kwa namna ya kuonesha kuwa kulikuwa na jambo la hatari, kisha kila mmoja akashika uelekeo wake kuizingira nyumba ile.

Mmoja alikwenda kujibanza mwanzo wa ukuta wa nyumba ya Sammy upande wa kushoto. Mwingine akakimbilia mbele ya geti kubwa la ile nyumba na kujibanza, na yule wa tatu alikwenda kujibanza kwenye kona ya ule ukuta iliyokuwa upande wa kulia. Lile gari Land-Rover 110 likaongeza mwendo na lilipofika mwisho wa mtaa ule likakata kona na kuuzunguka ule mtaa kwenda kutokea mtaa wa nyuma yake.

Kwenye ule mtaa wa nyuma lilipunguza tena mwendo na kuwaruhusu wale askari watatu waliobakia kule nyuma waruke na kujiviringisha barabarani kama maninja. Kisha lile gari Land-Rover 110 halikusimama badala yake likaongeza kasi mbele ya na kwenda kutokea tena katika mtaa lilioingilia, kisha likasimama mwisho kabisa wa ule mtaa.

Wale askari walioruka kutoka kwenye lile gari Land-Rover 110 kule mtaa wa nyuma wakaanza kuusogelea kwa tahadhari ukuta wa ile nyumba ya Sammy huku wakiwa wamezishika vyema bunduki zao mikononi. Watu wawili watatu katika mtaa ule wakaanza kujitokeza wakishangaa, wasijue kilichokuwa kinaendelea.

Dulla na Spoiler ambao walikuwa bado wanawashikilia mateka Joyce na Pendo waliisikia sauti ya gari lile nje ya nyumba lilipopita na kupunguza mwendo kisha vikafuatia vishindo vya watu walioruka. Haraka Dulla akajongea dirishani na kuchungulia nje lakini kwa sababu nyumba ilikuwa imezungukwa na ukuta hakuweza kuona mtu. Akayatega vizuri masikio yake kusikiliza kwa makini, akasikia sauti hafifu za vishindo vya watu waliokuwa wanakimbia sambamba na ukuta ulioizunguka ile nyumba.

Alishtuka sana na kumpa ishara Spoiler kuwa kulikuwa na watu nje ya nyumba kisha akatoka haraka akipitia mlango wa jikoni na kujibanza kwenye kibaraza kidogo cha upande wa jiko, akasubiri kwa dakika moja huku akiwa makini sana kuangalia eneo lote la ule uwa wa nyumba. Mara akawaona wanaume watatu walioshika bunduki na vifua vyao vimekingwa na bullet proof wakipanda ukuta haraka na kurukia ndani ya uwa bila vishindo. Dulla akashtuka sana na kurudi haraka ndani. “Askari!” alimwambia Spoiler kwa sauti ya chini huku akimwonesha vidole vitatu akimaanisha wapo watatu.

“Mafala hawa! Siwezi kukubali kukamatwa kijingajinga na hawa mabwege,” Spoiler alisema kwa hasira huku akielekea dirishani kuchungulia. Kabla hajafanikiwa kuchungulia dirishani kikatokea kitendo cha ghafla ambacho wote hawakukitegemea. Joyce alinyanyua stuli akampiga nayo Spoiler kichwani. Spoiler alianguka sakafuni huku damu zikianza kumtoka kichwani.

Wakati huo huo Joyce alimnyakua Pendo aliyekuwa amewekwa juu ya sofa na kuanza kukimbilia kule jikoni ilia toke nje lakini Dulla aliachia risasi mbili zilizompata mgongoni. Joyce akipiga yowe kubwa la maumivu na kudondoka sakafuni. Pendo aliangukia kando na kugugumia kwa maumivu. Hakuweza kutoa sauti kwa kuwa alikuwa bado amebandikwa gundi maalumu ya karatasi mdomoni.

Spoiler alinyanyuka haraka akiwa ameghadhabika sana, akatazama upande wa kushoto kwake na kulia akiwa makini, kisha akampa ishara fulani Dulla ambaye alikuwa ameshika bastola tayari kwa lolote. Kitendo bila kuchelewa, wakagawana njia, huyu akaelekea mlango wa jikoni akimruka Joyce na mwingine akaelekea mlango wa barazani.

Spoiler alielekea mlango wa barazani na kuufungua mlengo kwa tahadhari, akawaona askari wawili wakijongea kuelekea pale mlangoni kwa tahadhari, akabana pumzi na kukimbilia kwenda kuichukua ile stuli kisha akazima umeme kwenye swichi kubwa. Eneo lote la nyumba ile likawa kiza, kitendo ambacho wale askari hawakuwa wamekitegemea.

Kufumba na kufumbua Spoiler aliirusha ile stuli katikati ya wale askari wawili ambao walishtuka na kujaribu kuikwepa. Hiyo ilikuwa nafasi ambayo Spoiler alikuwa anaitarajia itokee. Alichomoka kama umeme wakati wale askari walipokuwa katika harakati za kuikwepa ile stuli na kukimbilia upande wa nyuma, akarukia juu ya ukuta wa uwa na kujirusha huku akitua salama nje. Aliusikia mvumo wa risasi zilizomkosakosa.

Alipotua chini aliangaza macho yake pande zote na hakuona mtu yeyote anayemfuatilia, akaanza kukimbia akiambaa na ule ukuta kuelekea kule walipokuwa wameacha pikipiki yao lakini akiwa na tahadhar kubwa, kisu chake kakishika mkononi tayari kwa lolote. Mara akaisikia milio ya risasi zikirindima kule ndani na muda huo huo akamshuhudia Dulla akirukia juu ya ukuta huku akijibu mashambulizi kwa kurusha risasi. Mara akapiga kelele na kuanguka chini baada ya kupigwa risasi kadhaa mgongoni.

Spoiler alishtuka sana na kugeuka nyuma yake, akamwona Dulla akiwa anagugumia kwa maumivu, mita chache tu toka pale alipokuwa amesimama, akamfuata na kumbeba kisha akakimbia naye na kumpandisha kwenye pikipiki akimlaza kifudifudi. Aliiwasha ile pikipiki na kuondoka kwa mwendo wa kasi huku akikoswakoswa na risasi. Mita therathini tu mbele yake akakutana na gari aina ya Cadillac DeVille la Sammy lililokuwa likija katika mwendo wa kasi na kuonekana likiingia upande wake.

Inaendelea...

CC the_legend Norshad bobefu zoefu Pablo PAKAYA Ibney blackstarline Bryece Tater Bigjahman moneytalk marybaby nipo2 ram kisukari Smart911 Madame S carbamazepine Astelia culture gal Prisoner of hope Mine eyes kuku mweus Thad hearly Shunie moneytalk Tumosa Mine eyes Kudo swahiba92 ludist Toyota escudo Clkey macson3 boga la kiangazi LEGE Smart911 Richard irakunda skfull popie Krizy Beat hearly nipo2 MWINDAJI HARAMU kakhulu Katavi Norami mbududa iron2012 popie Bughy Harry Mlenge Kacheda mjasiliamali Laki Si Pesa cocochanel kinusikwetu big jambo mludego Shupavu Kacheda mjasiliamali Mweweso Songa Heri esiankiki mnadhimu mkuu wa jf red apple
 
Taxi - (95)

Sammy aliiona ile pikipiki akakanyaga breki kwa nguvu, gari lake likasota na kuyumba na wakati huo huo ile pikipiki ile ilionekana kuserereka huku ikiyumba kulikwepa lile gari kisha Spoiler akaiweka sawa.

Shit!” Spoiler alisema kwa hasira baada ya kugundua kuwa lilikuwa gari aina ya Cadillac DeVille na dereva wake ni Sammy, hata hivyo, hakuthubutu kusimama kwa kuhofia kukamatwa, aliongeza mwendo na pikipiki ikatokomea kizani huku watu wakishangaa.

* * * * *

Baada ya gari dogo aina ya Toyota Verossa jeusi kumchukua yule mrembo na kuondoka kwa kasi, Tunu hakutaka kukata tamaa mapema, alitoka mbio kukimbilia yalipo maegesho ya taxi mwisho wa mtaa ule. Dreva mmoja mjanja alikuwa amemwona Tunu tangu alipokuwa mbali akikimbilia kule, akawasha gari lake na kumfuata.

Alipomfikia alisimama na kumfungulia mlango wa mbele, “Twende zetu, sister!” yule dereva wa taxi alisema huku akimkazia macho Tunu.

“Una petroli ya kutosha?” Tunu alimuuliza yule dereva wa taxi kwa wasiwasi.

“Kwani unakwenda mbali, sister?”

“Itategemea,” Tunu alijibu huku akiingia ndani ya gari na kuketi. “Nataka ulifuate lile gari aina ya Toyota Verossa la rangi nyeusi lililoondoka maeneo haya muda mfupi uliopita.”

Yule dereva alielewa na muda uleule akayaacha yale maegesho ya teksi na kuingia barabarani akiufuata ule uelekeo wa lile gari Toyota Verossa jeusi.

“Ila naomba kuwa mwangalifu sana, wasijue kuwa wanafuatwa,” Tunu alimwonya yule dereva wakati ile taxi ikiingia katika barabara ya Uhuru kwa mwendo wa kasi.

Yule dereva wa teksi alionekana mjanja na mwerevu anayeitambua vyema kazi yake, alibetua kichwa chake kuonesha kuwa alimwelewa Tunu. Alikuwa kijana tu aliyekadiriwa kutozidi umri wa miaka therathini, alivaa suruali ya jeans rangi ya bluu na fulani nyekundu.

Katika muda ule wa usiku barabara ya Uhuru ilikuwa na msongamano wa magari, ikamlazimu yule dereva wa taxi atumie mbinu ya ziada kwa kupita pembeni hadi alipofika kwenye daraja la Malapa, jirani na kituo cha mafuta cha Lake Oil.

Alipenyapenya na kuvuka eneo la Malapa Hostel kisha akaiacha barabara ya Uhuru na kuingia upande wa kulia akiifuata barabara ya vumbi iliyopita nyuma ya makaburi ya Malapa.

“Una uhakika hawawezi kutupoteza?” Tunu aliuliza huku akionesha wasiwasi baada ya kuona dereva akipita njia nyingine.

“Sister, kwani shida yako si kulipata lile gari Toyota Verossa jeusi?” yule dereva alimuuliza Tunu, lakini akaendelea pasipo kusubiri jibu, “Toa wasiwasi, ninaijua vizuri kazi yangu.” alisema huku akiwa makini barabarani, taxi likakatiza mitaani kiasi cha kumchanganya kabisa Tunu.

Baada ya mwendo fulani wakatokea katika barabara ya Uhuru, katikia mtaa ambao ulikuwa ukitumika kama kituo cha daladala za kuelekea Muhimbili. Mara wakaliona lile gari Toyota Verossa jeusi likiwa mbele yao usawa wa ukuta wa Shule ya Msingi Hekima, eneo la Buguruni.

Muda ul ule askari wa usalama barabarani wakaanza kuyaruhusu magari yaliyopo katika barabara ya Uhuru kuvuka eneo la taa za barabarani za Buguruni. Dereva wa ile taxi aliyopanda Tunu alijitahidi kupenyapenya kwa kuyachomekea magari mawili matatu yaliyokuwa mbele yake na kujikuta akiwa nyuma ya lile gari Toyota Verossa.

Walipozivuka taa za kuongozea magari barabarani lile gari Toyota Verossa lilielekea barabara ya Mnyamani. Taxi nalo likaelekea barabara ileile ya Mnyamani wakilifuata lile gari Toyota Verossa. Hata hivyo, yule dereva wa taxi alikuwa mjanja, aliyaacha magari mawili yakawa katikati yao na lile gari Toyota Verossa.

Safari iliendelea hadi walipofika eneo la Vingunguti katika makutano ya barabara za Barakuda, Fida na ile inayokwenda kutokea barabara ya Nyerere, lile gari Toyota Verossa likanyoosha kuifuata barabara ya lami iliyokuwa inaelekea Fida. Yule dereva wa taxi naye akaifuata barabara ile akiwa nyuma huku gari moja likimtenganisha na lile Toyota Verossa.

Barabara ile haikuwa na msongamano, hivyo mwendo wao uliongezeka kidogo, wakakatiza katikati ya makazi ya watu wakikutana na kona kadhaa na hatimaye wakaanza kupita katika eneo la viwanda. Lile gari Toyota Verossa lilipofika mwisho wa barabara ile ya lami likakunja kona na kuingia kulia likiifuata barabara ya vumbi iliyoelekea eneo la Karakata.

Likaanza kushusha mteremko katika barabara ile ya vumbi likipita katikati ya makazi ya watu yenye nyumba mchanganyiko, za kawaida na za kisasa na baada ya mwendo wa dakika tano lile gari likakomea mbele ya nyumba moja kubwa ya kisasa iliyojitenga, ikiwa na uwanja mkubwa kwa mbele. Ilikuwa ni nyumba tulivu sana na mahala pa kifahari.

Ile taxi aliyopanda Tunu ilikuwa kwa mbali nayo ilikunja na kuelekea upande ule ikiifuata barabara ya vumbi na kwenda kusimama kwenye uwanja mpana wa mchanga uliokuwa mbele ya baa moja iliyokuwa inapiga muziki laini muda huo huku watu wakionekana kuburudika. Baa hiyo ilikuwa umbali wa mita mia moja toka pale ilipokuwa ile nyumba.

Tunu akamtaka dereva wake azime injini ya gari, yule dereva alikuwa mwepesi kuelewa, akafanya kama alivyoagizwa. Kisha Tunu akamuuliza kuhusu kiasi cha fedha alichokuwa anadai kama malipo ya umbali wa kutoka Ilala alikokodiwa hadi pale.

Yule dereva akamwambia kiasi cha fedha na bila kupoteza muda Tunu alimlipa na kumzidishia ili kujenga uaminifu kwa yule dereva. Yule dereva alizipokea zile fedha huku akishukuru sana. Tunu alitulia mle garini kwa muda akijaribu kulichunguza eneo lile kwa makini na mara akamwona yule mrembo akifungua mlango na kushuka toka kwenye lile gari Toyota Verossa, akaliendea geti la mbele la ile nyumba na kutoa ufungo, akafungua na kuzama ndani ya ile nyumba huku geti likifungwa haraka.

Muda huo huo lile gari Toyota Verossa likaonekana kugeuza na kuondoka likirudi lilikotoka na kuwapita kwa kasi, kisha likatokomea kizani. Tunu aliiangalia ile nyumba kwa shauku, akageuza shingo yake kumwangalia yule dereva wa taxi na kumwahidi kuwa angerudi baada ya dakika therathini ila endapo asingetokea katika muda huo basi angekuwa huru kuondoka zake.

Akiwa katikati ya udadisi na shauku alishuka toka ndani ya ile taxi, na kuanza kupiga hatua taratibu na kwa tahadhari kuelekea kwenye ile nyumba huku moyo wake ukienda mbio sana, hakuweza kuhisi nini ambacho kingemtokea mbele yake, hata hivyo, hilo halikumzuia kuendelea na harakati zake.

“Liwalo na liwe,’ Tunu aliwaza huku akizidi kujongea kwenye ile nyumba.

Sasa mambo ni 🔥🔥🔥 kwelikweli! Kama ni gari ndiyo limeshakata breki likiwa linateremsha mteremko mkali wa Kitonga. Ili kujua kitakachoendelea usikose kufuatilia simulizi hii ya kusisimua ya 'Taxi'...
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom