Stori ya kusisimua - Taxi

I see...mambo ni moto, naona tunu anakuja kukamilisha misheni baada ya kuona gari ya Sammy, sasa ile memory card sijui itakuwaje, halafu mshtuko atakaokutana nao Dr Odinya baada ya kugundua gari ni LA Sammy sijui utakuwaje??
 
Taxi - (74)

ILIPOISHIA

“Kaondoka?” Maximilian alimuuliza yule mhudumu wa kiume.

“Eeh! Ila kakasirika huyo! Amesema mtakutana mahakamani,” yule mhudumu alisema, kisha akamgeukia Tunu, “Anti, nikusaidie?”

Tunu aliyekuwa akimtazama Maximilian alishusha pumzi za ndani kwa ndani na kugeuza shingo yake kumtazama yule mhudumu mara moja.

“Nilitaka kumuulizia huyu kaka, bahati nzuri nimemuona,” Tunu alimwambia yule mhudumu kwa sauti tulivu na kumkabili Maximillian, “Samahani, kaka’angu!”

Maximilian aligeuza shingo yake kumtazama Tunu kwa makini. Tunu aliachia tabasamu pana la kirafiki huku akimsogelea. Maximilian naye alijikuta akiachia tabasamu, huku akionekana kuvutiwa na Tunu. Walitazama kwa sekunde chache kila mmoja akiwa kimya. Macho yao yaliongea mengi kuliko ambavyo wangeweza kuongea kwa mdomo.

SASA ENDELEA...

“Enhe, nikusaidie!” hatmaye Maximilian alimudu kumuuliza Tunu.

Tunu alishusha pumzi za ndani kwa ndani na kuonekana kama aliyekuwa akitafuta neno la kuongea.

“Jana usiku katika kipindi chako nimeliona gari aina ya Cadillac DeVille nikawa very interested…” Tunu alianza kujieleza, akasita na kuzungusha macho yake kuwaangalia watu waliokuwa wameketi kwenye eneo la kusubiria pale mapokezi. Wale wahudumu wa mapokezi na Maximillian wakatazamana, kisha wakamtazama Tunu kwa makini.

“Nahitaji kuonana na mmiliki wa gari hilo, sijui utanisaidiaje kaka’angu!” Tunu alisema huku akishusha pumzi. Maximilian alishusha pumzi na kulamba midomo yake.

“Mmh… hata sijui nisemeje, sina namba zake na hadi sasa tuna ugomvi. Alikuwepo hapa na ameondoka dakika chache tu zilizopita, nadhani mmepishana hapo nje,” Maximilian alisema huku akiegemeza kiwiko cha mkono wake juu ya meza ya mapokezi.

Tunu alishika kiuno chake na kukunja sura yake akionekana kuwaza kidogo. Kisha alimtazama Maximilian, “Hakuna sehemu yoyote unayoijua labda naweza kumpata?”

Maximilian alifikiria kidogo akionekana kujishauri, kisha alivuta pumzi ndefu na kuzishusha taratibu.

“Nenda pale kwenye mgahawa wa kisasa wa Elli’s, Ilala Sharif Shamba, mara nyingi huwa anakuwepo pale kwa rafiki yake. ila usimwambie kama mimi ndiye nimekuonesha,” Maximilian alimwambia Tunu.

“Usijali, kaka’angu. Nashukuru sana, nikiwa na chochote nitarudi tena kwako,” Tunu alisema na kuanza kupiga hatua taratibu kuondoka eneo lile huku macho ya Maximillian na wale wahudumu wa mapokezi yakimsindikiza hadi alipotoka nje ya jengo.

Alifika kwenye maegesho ya magari ya lile jengo la kituo cha televisheni ya Mzizima na kuingia ndani ya gari, alimkuta Victor akiwa amejiegemeza kwenye siti yake akiwa anasinzia.

“Twen’zetu. Naomba nipeleke Sinza nikapumzike,” Tunu alisema huku akifunga mkanda wa siti yake.

“Umempata uliyekuja kumtafuta?” Victor aliuliza kwa shauku huku akimkazia macho Tunu.

“Sijampata, nitamfuatilia tena baadaye!” Tunu alijibu kwa kifupi kisha akajiegemeza kwenye siti yake na kufumba macho.

Victor hakuongeza neno jingine, aliwasha gari na kuliondoa taratibu, akaingia barabara ya Lumumba na kwenda mbele alikokutana na barabara ya Morogoro, akakunja kuingia kushoto akiifuata barabara ile ya Morogoro. Ilikuwa ni safari ya kuelekea Sinza.

* * * * *

Saa tano ya asubuhi Joyce alikuwa ameketi kwenye sofa sebuleni kwake akitazama runinga, hata hivyo macho yake yalitazama runinga lakini akili yake haikuwa kwenye runinga, alikuwa mbali sana kimawazo, japo alionekana mtulivu sana.

Siku ile hakujisikia kutoka kwenda sehemu yoyote, alitaka kubaki ndani akipumzika baada ya kile kilichotokea kati yake na mumewe usiku wa siku iliyotangulia. Alishusha pumzi na kujilaza juu ya sofa.

Siku ile ilionekana kuwa ndefu sana kwa Joyce kuliko kawaida, hadi wakati huo alikuwa hajatia kitu chochote tumboni na hakuwa akihisi njaa, alikuwa peke yake nyumbani baada ya Sammy kutoka kwenda kazini kwake na watoto kwenda shule. Alijihisi mpweke sana.

Katika upweke ule alijikuta akizama kwenye tafakari, alikumbuka jinsi alivyokutana na Sammy kwa mara ya kwanza, walivyoanza uhusiano wao hadi walipofunga ndoa.

Alikumbuka kuwa alikutana na Sammy kwa mara ya kwanza miaka minane iliyokuwa imepita akiwa safarini kutoka Tanga akielekea jijini Dar es Salaam kuanza kazi ya ukatibu muhtasi baada ya kumaliza masomo yake ya uhazili katika Chuo Cha Uhazili tabora.

Ni siku hiyo hiyo Sammy alikuwa anatoka kutembelea vivutio vya mapango ya Amboni yaliyopo umbali wa kilomita 8 kutoka jijini Tanga katika barabara kuu inayoelekea Mombasa.

Ilikuwa saa kumi na mbili na dakika tano alfajiri ya siku ya safari yake ilimkuta akiwa bafuni anaoga na alitakiwa kuondoka saa kumi na mbili na nusu. Huaminika kuwa wanawake huchukua muda mrefu sana katika kujiandaa, kuanzia kuoga, kujipodoa na hata kuvaa nguo. Joyce alimaliza kuoga katika muda usiozidi dakika kumi, kisha alitoka haraka, akaingia chumbani mwake.

Kwa mara ya tatu, aliitupia jicho la wasiwasi saa yake ya mkononi iliyokuwa juu ya meza ya vipodozi, akajifuta maji haraka haraka. Zilikuwa zimebaki kama dakika tano tu tu kabla ya muda wa basi kupita uliokuwa umeandikwa kwenye tiketi yake, basi hilo lilikuwa likitokea jijini Tanga.

Kwa kawaida kutoka nyumbani kwao hadi kituo cha basi ingemchukua zaidi ya dakika arobaini na tano kama angetembea kwa miguu, lakini ilimchukua dakika tatu tu kufika kituo cha basi. Dereva wa pikipiki iliyomchukua kumpeleka hapo kituoni alikuwa ni kama nusu kichaa kutokana na mwendo wake wa kasi.

Joyce hakuamini kwamba angeweza kuwahi na kujiunga na wasafiri wenzake katika kituo cha basi kabla ya basi la Tahmeed halijapita.

Alipofika kituoni alitafuta sehemu nzuri akasimama. Siku ile alikuwa amevaa gauni zuri la kitenge cha wax lililokuwa limeshonwa na kudariziwa kwa nyuzi za dhahabu na kuushika mwili wake huku likilichora vyema umbo lake maridhawa na kichwani alikuwa amevaa kilemba kikubwa.

Kama ilivyokuwa imeandikwa, ndani ya dakika mbili tu basi la Tahmeed likawafikia na kusimama kituoni, Joyce akajiunga na wasafiri wengine kupanda ndani ya lile basi. Wakati akiingia kondakta wa lile basi alijikuta amebabaishwa sana na uzuri wa Joyce kiasi cha kusahau hata majukumu yake.

Kondakta alijikuta akipiga mluzi mdogo wa mshangao uliowafanya baadhi ya abiria walioketi jirani na mlango kumtazama kwa mshangao kabla ya macho yao kuhamia kwa Joyce. Si wanawake wala wanaume, wote walijikuta wakimkodolea macho Joyce huku wakiyasanifu mengi ya huba mbele ya hua aliyejitanashati kikweli kweli mbele ya macho yao!

Inaendelea...

CC the_legend Norshad bobefu zoefu Pablo PAKAYA Ibney blackstarline Bryece Tater Bigjahman moneytalk marybaby nipo2 ram kisukari Smart911 Madame S carbamazepine Astelia culture gal Prisoner of hope Mine eyes kuku mweus Thad hearly Shunie moneytalk Tumosa Mine eyes Kudo swahiba92 ludist Toyota escudo Clkey macson3 boga la kiangazi LEGE Smart911 Richard irakunda skfull popie Krizy Beat hearly nipo2 MWINDAJI HARAMU kakhulu Katavi Norami mbududa iron2012 popie Bughy Harry Mlenge Kacheda mjasiliamali Laki Si Pesa cocochanel kinusikwetu big jambo mludego Shupavu Kacheda mjasiliamali Mweweso Songa Heri esiankiki mnadhimu mkuu wa jf
 
Taxi - (75)

Joyce alikuwa amebeba begi lake la safari lenye magurudumu lililokuwa na ukubwa wa wastani mkono wake wa kulia. Akiwa na uhakika kuwa macho yote yalikuwa yakimtazama, alijifanya hajui kilichokuwa kinaendelea, akapiga hatua taratibu huku akiangaza macho yake kuangalia namba za siti.

Alikuwa akiitafuta siti namba ishirini na nne. Aliiona na kuanza kukukuruka kuweka vizuri begi lake kwenye sehemu maalumu ya kuwekea mizigo iliyokuwa sehemu ya juu ndani ya lile basi.

Kumbe muda wote macho ya kijana mmoja mtanashati aliyekuwa ameketi dirishani katika siti namba ishirini na tano yalikuwa kazini yakimkagua Joyce tangu miguu iliyosimamia vidole hadi kwenye mikono iliyokuwa inasokomeza begi kwenye eneo maalumu la juu la kuwekea mizigo. Kijana huyo aliitwa Samuel Kombona au Sammy kwa kifupi.

Joyce alipomaliza kuuweka vizuri mzigo wake aliketi, muda huo dereva wa basi alikuwa ameshaliondoa gari huku wakiwaacha wasindikizaji wao wakipunga mikono yao.

“Habari yako, kaka!” Joyce alimsalimia Sammy huku akiyakwepesha macho yake baada ya kugundua kuwa abiria huyo alikuwa anamtazama usoni kwa makini.

“Nzuri tu, za utokako?” Sammy aliitikia na kumpiga swali papo hapo huku akimkazia macho usoni kwa tabasamu.

“Nzuri,” Joyce alijibu kwa ufupi na kutoa simu kubwa ya kisasa aina ya ‘Samsung’, akawasha data na kufungua mtandao wa facebook kisha akaanza kuperuzi, hali iliyoonesha kuwa hakutaka kumpa nafasi Sammy kuendelea kumsaili.

“Umpendaye hajambo?” Sammy alimtupia swali la uchokozi licha ya kumwona akiwa bize na simu yake lakini Joyce akajifanya hajamsikia na kubaki kimya akiendelea kuperuzi kwenye simu yake.

Wakati akiperuzi kuna wakati alijikuta akicheka na wakati mwingine alisonya. Baadhi ya abiria walikuwa wakigeuza shingo zao kumtazama ingawa hakuna aliyejua anacheka au kusonya nini!

“Na mimi natamani nicheke kidogo,” Sammy alishindwa kuvumilia, hivyo akajikuta akimsemesha kwa sauti tulivu ya chini.

Joyce aligeza shingo yake na kumtazama mara moja bila kusema neno, kisha akayaondosha macho yake kwa Sammy na kuyarudisha kwenye simu yake. Kitendo kile kikamfanya Sammy aanze kujilaumu kwa kuwa alianza kuonekana kuwa anajipendekeza na pengine ndiyo maana Joyce aliamua kumdharau.

“Samahani kama nimekuwa msumbufu kwako,” Sammy alimwambia Joyce na kujiegemeza kwenye siti yake.

Joyce hakunijibu bali alimtupia jicho la wizi huku akiachia tabasamu la aibu. Sammy hakutaka makuu, akachukua kitabu cha hadithi chenye jina la The Devil in Love kilichoandikwa na Barbara Cartland na kukifungua, akaanza kusoma ingawa akili yake ilikuwa kwa Joyce.

Kitendo kile kilimfanya Joyce apate nafasi nzuri ya kumsaili Sammy, alimtazama kwa makini kuanzia usoni hadi unyayoni na kushtuka kidogo japo alijaribu kuuficha mshtuko wake. Aligundua kuwa hakuwa amemchanganyia vizuri macho kwa kuwa alimchukulia Sammy kama mmoja wa vijana wahuni wasiopenda kupitwa na kila kilichofichwa ndani ya sketi.

Wakati Joyce akiendelea kumtazama Sammy katika namna ya kumsaili, Sammy aligeuza shingo yake kumtazama Joyce na mara macho yao yakagongana, wakajikuta wote wawili wakiachia tabasamu. Kwa hakika tabasamu la Sammy lilifanikiwa kuziteka hisia za Joyce kwani Joyce alijikuta akipumbazika na utanashati wa Sammy.

“Naitwa Sammy… Samuel Kambona,” Sammy alijitambulisha huku akimtazama Joyce kwa utulivu. Uso wake uliendelea kupambwa na tabasamu la kirafiki.

Joyce alisita kidogo na kumtazama Sammy huku tabasamu maridhawa la aibu likiendelea kuchomoza usoni mwake na kuusuuza mtima wa Sammy.

“Nafurahi kukufahamu,” Joyce alisema kisha akampiga swali la papo kwa papo, “Ulisema unataka kucheka?”

Swali lile lilimshtua Sammy kwani hakuwa amekumbuka kuwa alikuwa amemwambia kuwa na yeye alitamani acheke wakati Joyce alipokuwa akiperuzi simu huku wakati fulani akionekana kucheka.

“Hapana nilikuwa nakutania,” alisema huku akiachia kicheko hafifu.

“Ooh, kumbe!” Joyce alisema huku naye akiangua kicheko hafifu. “Naitwa Joyce…” aliongeza huku akionekana kuanza kuchangamka zaidi.

Kuanzia hapo stori kati yao zikakolea, na huo ndiyo ukawa mwanzo wa kufahamiana kwao, walipofika Dar es Salaam mapenzi yakachipua na miezi michache baadaye posa ikapelekwa…

_____

Mlio wa simu ya mkononi iliyoanza kuita ulimshtua sana Joyce na kumzindua kutoka kwenye lindi la mawazo, alinyoosha mkono wake kuichukua huku akiinua kichwa na kutazama kwa makini, moyo wake ukapasuka pah! Jasho jepesi likaanza kumtoka mwilini. Ilikuwa ni simu kutoka kwa Dynamo Plus.

Huku mwili wake ukimtetemeka kwa hasira aliikodolea ile simu kama aliyekuwa akilitazama bomu ambalo lilibakiza sekunde chache tu kabla halijalipuka, akakunja sura yake na kushusha pumzi huku akiendelea kuitazama ile simu bila kuipokea hadi ikakatika.

Simu ilianza kuita tena, Joyce aliiangalia tu pasipo kuipokea, aliiacha ikaita hadi ikakatika. Dakika moja baadaye ujumbe mfupi wa maneno ukaingia. Ulikuwa unasomeka: “Mbona hupokei simu, unapoteza bahati mtoto.”

Joyce alisonya na kuufuta ujumbe ule, wakati akitaka kuizima simu akasikia sauti ya muungurumo wa gari lililosimama nje mbele ya geti kubwa la nyumba yao, kisha akasikia honi za gari kumwashiria afungue geti. Aliitupia simu juu ya sofa na kukimbilia nje. Akachungulia getini na kuliona gari la Sammy.

Alionekana kushtuka kidogo baada ya kuliona gari la Sammy nyumbani kwani haikuwa tabia ya Sammy kurudi nyumbani muda ule. Hata hivyo hakutaka kuonesha mshtuko wake, akafungua geti huku akiachia tabasamu lililochanganyika na hofu.

Alimkodolea Sammy macho aliyeshuka kutoka kwenye gari na kutazama saa yake ya mkononi. Taratibu akaanza kupiga hatu kuelekea ndani. Joyce alifuata nyuma taratibu. Wakaketi sebuleni.

“Nilidhani ungekwenda kusaini mkataba!” Sammy alimwambia Joyce huku akimtulizia macho Joyce.

Joyce alimtazama mumewe kwa mshangao akiwa kakunja uso wake. Muda huo Sammy alikuwa hamtazami bali anatazama kwenye dari.

“Sikuelewi!” Joyce alisema huku akimkazia macho Sammy, ni wazi alikuwa amekerwa na kauli ya Sammy.

“Asiyemwelewa mwenzake ni wewe au mimi?”

Inaendelea...
 
Taxi - (76)

Joyce alimtazama mumewe kwa huzuni na uso wenye kutia huruma, alitingisha kichwa chake kwa masikitiko, kiganja chake cha kushoto kikiwa kimeshikilia paji lake la uso.

“Nilidhani yameisha, mume wangu!” Joyce alisema kwa huzuni.

“Hayawezi kwisha kirahisi rahisi hivyo,” Sammy alisema huku akigeuza shingo yake kumtazama Joyce.

Muda huo huo simu ya Joyce ikaanza kuita. Joyce alishituka sana ila alijikaza na kuuma meno. Aliitazama ile simu kisha akamtazama Sammy kwa wasiwasi. Wakatazamana.

Sammy alinyoosha mkono wake na kuichukua ile simu, akaitazama kwa makini na kuona namba ngeni isiyo na jina. Alimtazama Joyce kwa macho makali. Joyce alionekana kuwa na hofu na kujikunyata pale alipokaa.

“Pokea simu yako,” Sammy alisema kwa sauti iliyoashiria hasira huku akimpa Joyce ile simu.

Joyce alikataa kuipokea ile simu kutoka kwa mumewe. Alikuwa anatetemeka kwa hofu.

“Kwa nini unakataa kupokea, kwani unajua ni ya nani anapiga?” Sammy aliuliza kwa ukali huku akiendelea kunyoosha mkono wake kumpa simu Joyce.

“Wala sihitaji kumjua mpigaji,” Joyce alisema huku akinyanyua mabega yake juu kama ishara ya kutotaka kuipokea. Ile simu ikakatika.

Kabla Sammy hajasema chochote wakasikia sauti ya mtu akigonga geti huku akiita “Mama Pendo!” ilikuwa ni sauti ya jirani yao, Bibi Stumai. Joyce alibaki kajikunyata kwa hofu huku akimtumbulia macho mumewe.

“Nenda kamsikilize shoga yako huko nje,” Sammy alisema huku akijiegemeza kwenye sofa.

Joyce alivuta pumzi ndefu na kuzishusha taratibu, akajizoazoa kutoka pale kwenye sofa na kuelelekea nje.

* * * * *

Gari aina ya Toyota Hilux double cabin la rangi ya bluu lililokuwa na namba bandia lilikuwa limeegeshwa kwenye mtaa mmoja mtulivu katika eneo la Tabata Mawenzi. Ndani ya gari hilo kulikuwa na wanaume wawili, Spoiler na Dulla Mcomoro waliokuwa makini sana kuitazama nyumba moja ya kifahari iliyozungushiwa ukuta mrefu wenye uzio wa umeme. Mbele ya ukuta wa ile nyumba kulikuwa na geti kubwa jeusi.

Ukuta wa nyumba ile haukumruhusu mtu aliyeko nje kuona chochote kilichomo ndani ya nyumba hiyo kutokana na urefu wake. Kilichoonekana ukiwa nje ya ile nyumba ilikuwa miti miwili mikubwa ya kivuli na paa la kijani la nyumba ile. Ilikuwa ni sehemu tulivu sana lakini pia ya kifahari.

Spoiler na Dulla Mcomoro walikuwa wanafuatilia kujua kila aliyeingia au kutoka ndani ya nyumba ile. Spoiler alikuwa ametulia tuli akiwa makini sana kana kwamba alikuwa ameambiwa kungetokea kitu cha ajabu muda wowote.

Zilikuwa zimeshapita takriban dakika ishirini tangu wafike eneo lile baada ya kubaini kuwa aliyenunua gari aina ya Cadillac DeVille aliishi katika nyumba ile, kwa mujibu wa nyaraka walizozichukua katika duka la kuuza vipuri vya magari la Jonas Odilo, lililopo mtaa wa Lindi eneo la Shaurimoyo.

Hawakuwa na papara, waliamua kubaki ndani ya gari ili kufanya uchunguzi kabla hawajashuka na kwenda katika nyumba ile. Hadi muda ule hawakuwa wamemuona mtu yeyote kuingia au kutoka ndani ya nyumba ile, hali ilikuwa ya ukimya mno. Wakaanza kupatwa na wasiwasi iwapo nyumba ile iliishi watu.

Wakiwa bado wanafuatilia kila kinachotokea katika eneo lile mara wakaliona garo dogo aina ya Toyota Lexus RX jeusi likifika katika nyumba ile, likapiga honi na baada ya sekunde kadhaa lile geti kubwa likafunguliwa, gari likaingia ndani.

Ilichukua takriban dakika tano tu geti likafunguliwa na lile gari likatoka na kuingia barabarani, likaondoka. Spoiler akamtaka Dulla Mcomoro asogeze gari.

Dulla Mcomoro alilisogeza gari na kusimama mbele ya lile geti kubwa. Wakashuka haraka na kubonyeza kengele iliyokuwa kando ya geti, sekunde chache baadaye mlango wa lile geti ukafunguliwa, mlinzi mmoja wa Kimasai akatoa kichwa kuchungulia na kuwaona.

“Habari zenu?” yule mlinzi aliwasalimia huku akiwaangalia kwa macho ya kuwasaili.

“Nzuri. Habari za hapa?” Spoiler alimjibu yule mlinzi huku akimtazama kwa makini. Wakati huo Dulla Mcomoro alikuwa anachungulia kwenye uwazi wa ule mlango wa geti kutazama ndani.

“Sijui niwasaidie nini?” yule mlinzi aliwauliza huku akiwakazia macho, alionekana kuwa makini zaidi na kazi yake.

“Sisi ni wageni wa Dk. Mloka,” Spoiler alisema kwa kujiamini zaidi na kumfanya yule mlinzi amkazie macho kwa mshangao.

“Dk. Mloka!” yule mlinzi aliuliza kwa mshangao mkubwa, “Kwani Mloka yupi mnamtaka?” akaongeza huku akiwaangalia kwa udadisi, bado mshangao uliendelea kujionesha usoni kwake.

Spoiler na Dulla Mcomoro wakaangaliana na macho yao kuzungumza, kengele ya tahadhari ikalia kichwani kwa Spoiler, akashusha pumzi na kumtazama tena yule mlinzi.

“Kwani hapa siyo nyumbani kwa Dk. Mloka?” Spoiler aliuliza huku naye akijifanya kuonesha mshangao.

“Hii ni nyumba ya Dk. Mloka lakini mbona yeye amefariki dunia miaka miwili iliyopita!” yule mlinzi alisema huku akiwa bado anawatazama kwa makini.

“Kwa hiyo hapa anaishi nani kwa sasa?” Spoiler akamwahi kabla hajafanya chochote.

“Anaishi mkewe, Dk. Marina na watoto wake.”

“Hivi sasa kuna nani ndani?” Spoiler aliuliza huku akijaribu kuchungulia ndani kupitia upenyo mdogo ulio wazi wa mlango wa lile geti.

“Kwani ninyi mnamtaka nani hasa?” yule mlinzi akawauliza baada ya kufikiria kwa kitambo huku akionesha wasiwasi.

“Basi tunaomba tuonane na mama, mke wa Dk. Mloka, maana sisi ni jamaa zake marehemu Dk. Mloka,” Spoiler alisema huku akisogea karibu na yule mlinzi.

“Jamaa zake Dk. Mloka halafu hamjui kama alishakufa! Itabidi msubiri hapa ili nikaulize ndani kwanza, maana siwafahamu na wala sikutaarifiwa kama kuna wageni wa aina yenu watakuja hapa leo!” yule mlinzi alisema huku akijiandaa kuufunga ule mlango wa geti.

Mambo yanazidi kunoga, mlinzi ameonesha kuwashtukia kina Spoiler. Je, watafanikiwa kuingia ndani na kupata taarifa kuhusu mmiliki wa sasa wa gari wanalolitafuta? Vipi kuhusu Sammy na mkewe Joyce, moto utapoa? Na Tunu je, ana mission gani iliyomleta Dar es Salaam? Winifrida atakuja na jipya lipi? Endelea kufuatilia stori hii ya kusisimua ili kuujua mwisho wake...
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom