Bishop Hiluka
JF-Expert Member
- Aug 12, 2011
- 7,147
- 14,711
- Thread starter
- #221
Taxi - (61)
Winifrida alinawa mikono huku akiendelea kumtazama Sammy kwa kuvizia vizia, kila mmoja alijipakulia chakula kwa kadiri ya tumbo lake, Winifrida alikuwa akimtazama Sammy kwa jicho la wizi wakati akijipakulia chakula.
Sammy alijipakulia wali wa kumtosha kwenye sahani, akawekea mchuzi wa kuku na kumwagia maharage kwa wingi, kisha aliweka mboga za majani nyingi na kujisogezea huku akiketi kitako. Alionekana kupoa sana jambo lililomshangaza kila mtu isipokuwa Winifrida, kwani yeye alifahamu ukweli kwa nini Sammy alikuwa amepoa sana siku ile.
Joyce alikuwa akimtupia Sammy jicho la wizi wakati akisogeza poti la chakula, akampakulia Pendo kidogo na kumwekea mchuzi mzito wa kuku na maharage kisha akampa na kuanza kujipakulia chakula chake mwenyewe, alipomaliza alianza kula taratibu.
Winifrida naye alijipakulia chakula huku Sammy akimtazama kwa makini, hakusema kitu lakini alionekana kuwa na donge moyoni. Alitamani kumwambia Joyce ni wapi alimkuta Winifrida akiwa na mwanamume lakini alihofu siri yake ingefichuka.
Pendo alimtazama baba yake kwa udadisi, Sammy naye alishusha macho yake kumtazama Pendo akiwa mtulivu sana. Akachota chakula na kuanza kula.
Siku hiyo meza ya chakula ilitanda ukimya mzito wakati wote wa chakula, hakuna aliyeongea na kilichokuwa kikisikika muda ule kilikuwa ni mgongano wa vijiko na vyombo vingine vya mezani, wakati wakila.
* * * * *
Saa sita na nusu usiku Winifrida, mtoto wa kike mchache wa miaka lakini mwingi wa maneno, alikuwa ameketi kitandani chumbani kwake, akiwa amejiegemeza kwenye ukuta akiwaza. Usiku huo ulikuwa mrefu kwake kuliko kawaida na usingizi ulikuwa adimu.
Rohoni mwake mlikuwa na shauku kubwa. Alipomaliza kula usiku ule aliingia chumbani kwake akapanda juu ya kitanda chake, si kulala bali kuendelea na fikra zake zisizokuwa na mwisho kuhusu Jackson. Kijana mtanashati na mcheshi sana.
Alishusha pumzi za ndani kwa ndani na kugeuza shingo yake kumtazama Pendo aliyekuwa katika sayari ya mbali muda ule akikoroma, alikuwa akivuta pumzi taratibu na kuzishusha.
“Hmm, utoto raha sana! Unakuwa huru na huna stress, hufikirii maisha wala mapenzi kama ilivyo kwa wakubwa,” Winifrida aliwaza.
Alizungusha macho yake kukitazama kile chumba chao kwa makini kana kwamba alikuwa akikiona kwa mara ya kwanza, akafumba macho yake, mawazo yalizidi kumsonga usiku huo, aliwaza vitu vingi: alifikiria masomo, maisha, mapenzi. Alimwaza Jackson, kijana aliyetokea kumpenda sana. Alitamani usiku ule angekuwa na Jackson mle chumbani, wakiwa wao wawili tu. Lakini hakukuwako!
Kilichokuwa pamoja naye usiku ule, ukimwacha Pendo aliyelala fofofo kitandani, ni mito miwili mikubwa, alifumbua macho yake na kuutazama mto mmoja, akauvuta kisha aliubana kifuani kwake na kuubusu.
“Jackson,” Winifrida aliuita ule mto huku akiyafumba macho yake, “Nakupenda sana mpenzi wangu. Tafadhali niambie kama nawe wanipenda kwa dhati.”
Kisha alitegesha sikio lake kwenye ule mto akifanya kama anayesikiliza, kwa mbali katika sikio lake la mawazo alimsikia Jackson wa ndotoni akimjibu, “Winnie, mpenzi wangu, ni wewe peke yako ninayekupenda hapa duniani. Nakupenda na nitaendelea kukupenda hadi mwisho wa maisha yangu…”
Winifrida alihisi mapigo ya moyo wake yakiongezeka maradufu na joto lake likizidi kupanda. Akaubusu tena ule mto kama aliyepatwa na wazimu. Hakuamini kama yote yale alikuwa anafanya na ule mto, wala Jackson hakuwako.
Aliendelea kuubusu ule mto mpaka aliporudiwa na fahamu. Akaona haya, japo Pendo alikuwa amelala na hapakuwa na mtu mwingine aliyeuona upumbavu wake. Aliusukuma ule mto pembeni, akaridhika kuwa alikuwa na Jackson muda ule.
“Lo, Jackson! Laiti ningekuwa na uwezo ningehama naye hapa duniani, nikajifiche naye pahala pa peke yetu, sina hofu ya pute wala vijicho, ni mimi na yeye tu, kutwa kucha,” Winifrida aliwaza na kushusha pumzi.
Akakumbuka alivyokutana na Jackson mara ya kwanza, ilikuwa mwaka uliokuwa umetangulia, miezi sita tu iliyokuwa imepita, wakati huo Winifrida akiwa kidato cha tatu na Jackson akiwa kidato cha nne. Ilikuwa ni katika mashindano ya ujirani mwema yaliyofanyikia Shule ya Sekondari ya Azania na kuzikutanisha shule kongwe za jijini Dar es Salaam.
Siku ile wanafunzi wa Zanaki walipanda jukwaani kuonesha mchezo wa kuigiza ulioitwa ‘Hadi Lini!’ na yeye Winifrida alicheza nafasi ya mhusika mkuu. Ulikuwa mchezo uliomwelezea mwanamke jasiri aliyepambana kunusuru ndoa yake pale mumewe aliyempenda alipoamua kumsahau na kumpenda mwanamke mwingine, baada ya kufanikiwa.
Winifrida alicheza nafasi ya mke mtii kwa ndoa yake ambaye mume wake alipata penzi jipya. Alicheza nafasi hiyo kwa uthabiti na kuuvaa uhalisia wa kweli, hasa pale aliposimamia kile alichokiamini na kuwafanya nusu ya watazamaji wasisimkwe na kupiga kelele za shangwe.
Walipomaliza tu onesho lao Jackson alimfuata alipokuwa amesimama na wenzake na kumpongeza. Winifrida alibinya mikono yake kwa shauku, raha iliyoje kupongezwa na kijana kama Jackson. Ni yeye Winifrida aliyetamani kumpongeza kwanza Jackson kwa onesho lake lililomsisimua kila mtu ukumbini. Ni Jackson aliyepanda jukwaani kabla yao.
Jackson alikuwa amejaaliwa sauti tamu na kipaji cha kuimba na alipokuwa jukwaani kila mtu alipagawa! Winifrida alihisi damu ikimchemka, roho ikamlipuka, miguu ikamcheza na moyo kumpapatika.
Kwa kweli Jackson alijaaliwa sauti nzuri na alijua hasa kuburudisha mashabiki awapo jukwaani, ndiyo maana haikuwashangaza wengi kuona wimbo wake wa ‘Nadhiri Yangu’ aliokuwa ameuachia kipindi hicho ukifanya vizuri sana kwenye vituo mbalimbali vya redio na runinga kuliko hata nyimbo za wakongwe.
Inaendelea...
Winifrida alinawa mikono huku akiendelea kumtazama Sammy kwa kuvizia vizia, kila mmoja alijipakulia chakula kwa kadiri ya tumbo lake, Winifrida alikuwa akimtazama Sammy kwa jicho la wizi wakati akijipakulia chakula.
Sammy alijipakulia wali wa kumtosha kwenye sahani, akawekea mchuzi wa kuku na kumwagia maharage kwa wingi, kisha aliweka mboga za majani nyingi na kujisogezea huku akiketi kitako. Alionekana kupoa sana jambo lililomshangaza kila mtu isipokuwa Winifrida, kwani yeye alifahamu ukweli kwa nini Sammy alikuwa amepoa sana siku ile.
Joyce alikuwa akimtupia Sammy jicho la wizi wakati akisogeza poti la chakula, akampakulia Pendo kidogo na kumwekea mchuzi mzito wa kuku na maharage kisha akampa na kuanza kujipakulia chakula chake mwenyewe, alipomaliza alianza kula taratibu.
Winifrida naye alijipakulia chakula huku Sammy akimtazama kwa makini, hakusema kitu lakini alionekana kuwa na donge moyoni. Alitamani kumwambia Joyce ni wapi alimkuta Winifrida akiwa na mwanamume lakini alihofu siri yake ingefichuka.
Pendo alimtazama baba yake kwa udadisi, Sammy naye alishusha macho yake kumtazama Pendo akiwa mtulivu sana. Akachota chakula na kuanza kula.
Siku hiyo meza ya chakula ilitanda ukimya mzito wakati wote wa chakula, hakuna aliyeongea na kilichokuwa kikisikika muda ule kilikuwa ni mgongano wa vijiko na vyombo vingine vya mezani, wakati wakila.
* * * * *
Saa sita na nusu usiku Winifrida, mtoto wa kike mchache wa miaka lakini mwingi wa maneno, alikuwa ameketi kitandani chumbani kwake, akiwa amejiegemeza kwenye ukuta akiwaza. Usiku huo ulikuwa mrefu kwake kuliko kawaida na usingizi ulikuwa adimu.
Rohoni mwake mlikuwa na shauku kubwa. Alipomaliza kula usiku ule aliingia chumbani kwake akapanda juu ya kitanda chake, si kulala bali kuendelea na fikra zake zisizokuwa na mwisho kuhusu Jackson. Kijana mtanashati na mcheshi sana.
Alishusha pumzi za ndani kwa ndani na kugeuza shingo yake kumtazama Pendo aliyekuwa katika sayari ya mbali muda ule akikoroma, alikuwa akivuta pumzi taratibu na kuzishusha.
“Hmm, utoto raha sana! Unakuwa huru na huna stress, hufikirii maisha wala mapenzi kama ilivyo kwa wakubwa,” Winifrida aliwaza.
Alizungusha macho yake kukitazama kile chumba chao kwa makini kana kwamba alikuwa akikiona kwa mara ya kwanza, akafumba macho yake, mawazo yalizidi kumsonga usiku huo, aliwaza vitu vingi: alifikiria masomo, maisha, mapenzi. Alimwaza Jackson, kijana aliyetokea kumpenda sana. Alitamani usiku ule angekuwa na Jackson mle chumbani, wakiwa wao wawili tu. Lakini hakukuwako!
Kilichokuwa pamoja naye usiku ule, ukimwacha Pendo aliyelala fofofo kitandani, ni mito miwili mikubwa, alifumbua macho yake na kuutazama mto mmoja, akauvuta kisha aliubana kifuani kwake na kuubusu.
“Jackson,” Winifrida aliuita ule mto huku akiyafumba macho yake, “Nakupenda sana mpenzi wangu. Tafadhali niambie kama nawe wanipenda kwa dhati.”
Kisha alitegesha sikio lake kwenye ule mto akifanya kama anayesikiliza, kwa mbali katika sikio lake la mawazo alimsikia Jackson wa ndotoni akimjibu, “Winnie, mpenzi wangu, ni wewe peke yako ninayekupenda hapa duniani. Nakupenda na nitaendelea kukupenda hadi mwisho wa maisha yangu…”
Winifrida alihisi mapigo ya moyo wake yakiongezeka maradufu na joto lake likizidi kupanda. Akaubusu tena ule mto kama aliyepatwa na wazimu. Hakuamini kama yote yale alikuwa anafanya na ule mto, wala Jackson hakuwako.
Aliendelea kuubusu ule mto mpaka aliporudiwa na fahamu. Akaona haya, japo Pendo alikuwa amelala na hapakuwa na mtu mwingine aliyeuona upumbavu wake. Aliusukuma ule mto pembeni, akaridhika kuwa alikuwa na Jackson muda ule.
“Lo, Jackson! Laiti ningekuwa na uwezo ningehama naye hapa duniani, nikajifiche naye pahala pa peke yetu, sina hofu ya pute wala vijicho, ni mimi na yeye tu, kutwa kucha,” Winifrida aliwaza na kushusha pumzi.
Akakumbuka alivyokutana na Jackson mara ya kwanza, ilikuwa mwaka uliokuwa umetangulia, miezi sita tu iliyokuwa imepita, wakati huo Winifrida akiwa kidato cha tatu na Jackson akiwa kidato cha nne. Ilikuwa ni katika mashindano ya ujirani mwema yaliyofanyikia Shule ya Sekondari ya Azania na kuzikutanisha shule kongwe za jijini Dar es Salaam.
Siku ile wanafunzi wa Zanaki walipanda jukwaani kuonesha mchezo wa kuigiza ulioitwa ‘Hadi Lini!’ na yeye Winifrida alicheza nafasi ya mhusika mkuu. Ulikuwa mchezo uliomwelezea mwanamke jasiri aliyepambana kunusuru ndoa yake pale mumewe aliyempenda alipoamua kumsahau na kumpenda mwanamke mwingine, baada ya kufanikiwa.
Winifrida alicheza nafasi ya mke mtii kwa ndoa yake ambaye mume wake alipata penzi jipya. Alicheza nafasi hiyo kwa uthabiti na kuuvaa uhalisia wa kweli, hasa pale aliposimamia kile alichokiamini na kuwafanya nusu ya watazamaji wasisimkwe na kupiga kelele za shangwe.
Walipomaliza tu onesho lao Jackson alimfuata alipokuwa amesimama na wenzake na kumpongeza. Winifrida alibinya mikono yake kwa shauku, raha iliyoje kupongezwa na kijana kama Jackson. Ni yeye Winifrida aliyetamani kumpongeza kwanza Jackson kwa onesho lake lililomsisimua kila mtu ukumbini. Ni Jackson aliyepanda jukwaani kabla yao.
Jackson alikuwa amejaaliwa sauti tamu na kipaji cha kuimba na alipokuwa jukwaani kila mtu alipagawa! Winifrida alihisi damu ikimchemka, roho ikamlipuka, miguu ikamcheza na moyo kumpapatika.
Kwa kweli Jackson alijaaliwa sauti nzuri na alijua hasa kuburudisha mashabiki awapo jukwaani, ndiyo maana haikuwashangaza wengi kuona wimbo wake wa ‘Nadhiri Yangu’ aliokuwa ameuachia kipindi hicho ukifanya vizuri sana kwenye vituo mbalimbali vya redio na runinga kuliko hata nyimbo za wakongwe.
Inaendelea...
