Stori ya kusisimua - Taxi

Stori ya kusisimua - Taxi

Taxi - (61)

Winifrida alinawa mikono huku akiendelea kumtazama Sammy kwa kuvizia vizia, kila mmoja alijipakulia chakula kwa kadiri ya tumbo lake, Winifrida alikuwa akimtazama Sammy kwa jicho la wizi wakati akijipakulia chakula.

Sammy alijipakulia wali wa kumtosha kwenye sahani, akawekea mchuzi wa kuku na kumwagia maharage kwa wingi, kisha aliweka mboga za majani nyingi na kujisogezea huku akiketi kitako. Alionekana kupoa sana jambo lililomshangaza kila mtu isipokuwa Winifrida, kwani yeye alifahamu ukweli kwa nini Sammy alikuwa amepoa sana siku ile.

Joyce alikuwa akimtupia Sammy jicho la wizi wakati akisogeza poti la chakula, akampakulia Pendo kidogo na kumwekea mchuzi mzito wa kuku na maharage kisha akampa na kuanza kujipakulia chakula chake mwenyewe, alipomaliza alianza kula taratibu.

Winifrida naye alijipakulia chakula huku Sammy akimtazama kwa makini, hakusema kitu lakini alionekana kuwa na donge moyoni. Alitamani kumwambia Joyce ni wapi alimkuta Winifrida akiwa na mwanamume lakini alihofu siri yake ingefichuka.

Pendo alimtazama baba yake kwa udadisi, Sammy naye alishusha macho yake kumtazama Pendo akiwa mtulivu sana. Akachota chakula na kuanza kula.

Siku hiyo meza ya chakula ilitanda ukimya mzito wakati wote wa chakula, hakuna aliyeongea na kilichokuwa kikisikika muda ule kilikuwa ni mgongano wa vijiko na vyombo vingine vya mezani, wakati wakila.

* * * * *

Saa sita na nusu usiku Winifrida, mtoto wa kike mchache wa miaka lakini mwingi wa maneno, alikuwa ameketi kitandani chumbani kwake, akiwa amejiegemeza kwenye ukuta akiwaza. Usiku huo ulikuwa mrefu kwake kuliko kawaida na usingizi ulikuwa adimu.

Rohoni mwake mlikuwa na shauku kubwa. Alipomaliza kula usiku ule aliingia chumbani kwake akapanda juu ya kitanda chake, si kulala bali kuendelea na fikra zake zisizokuwa na mwisho kuhusu Jackson. Kijana mtanashati na mcheshi sana.

Alishusha pumzi za ndani kwa ndani na kugeuza shingo yake kumtazama Pendo aliyekuwa katika sayari ya mbali muda ule akikoroma, alikuwa akivuta pumzi taratibu na kuzishusha.

“Hmm, utoto raha sana! Unakuwa huru na huna stress, hufikirii maisha wala mapenzi kama ilivyo kwa wakubwa,” Winifrida aliwaza.

Alizungusha macho yake kukitazama kile chumba chao kwa makini kana kwamba alikuwa akikiona kwa mara ya kwanza, akafumba macho yake, mawazo yalizidi kumsonga usiku huo, aliwaza vitu vingi: alifikiria masomo, maisha, mapenzi. Alimwaza Jackson, kijana aliyetokea kumpenda sana. Alitamani usiku ule angekuwa na Jackson mle chumbani, wakiwa wao wawili tu. Lakini hakukuwako!

Kilichokuwa pamoja naye usiku ule, ukimwacha Pendo aliyelala fofofo kitandani, ni mito miwili mikubwa, alifumbua macho yake na kuutazama mto mmoja, akauvuta kisha aliubana kifuani kwake na kuubusu.

“Jackson,” Winifrida aliuita ule mto huku akiyafumba macho yake, “Nakupenda sana mpenzi wangu. Tafadhali niambie kama nawe wanipenda kwa dhati.”

Kisha alitegesha sikio lake kwenye ule mto akifanya kama anayesikiliza, kwa mbali katika sikio lake la mawazo alimsikia Jackson wa ndotoni akimjibu, “Winnie, mpenzi wangu, ni wewe peke yako ninayekupenda hapa duniani. Nakupenda na nitaendelea kukupenda hadi mwisho wa maisha yangu…”

Winifrida alihisi mapigo ya moyo wake yakiongezeka maradufu na joto lake likizidi kupanda. Akaubusu tena ule mto kama aliyepatwa na wazimu. Hakuamini kama yote yale alikuwa anafanya na ule mto, wala Jackson hakuwako.

Aliendelea kuubusu ule mto mpaka aliporudiwa na fahamu. Akaona haya, japo Pendo alikuwa amelala na hapakuwa na mtu mwingine aliyeuona upumbavu wake. Aliusukuma ule mto pembeni, akaridhika kuwa alikuwa na Jackson muda ule.

“Lo, Jackson! Laiti ningekuwa na uwezo ningehama naye hapa duniani, nikajifiche naye pahala pa peke yetu, sina hofu ya pute wala vijicho, ni mimi na yeye tu, kutwa kucha,” Winifrida aliwaza na kushusha pumzi.

Akakumbuka alivyokutana na Jackson mara ya kwanza, ilikuwa mwaka uliokuwa umetangulia, miezi sita tu iliyokuwa imepita, wakati huo Winifrida akiwa kidato cha tatu na Jackson akiwa kidato cha nne. Ilikuwa ni katika mashindano ya ujirani mwema yaliyofanyikia Shule ya Sekondari ya Azania na kuzikutanisha shule kongwe za jijini Dar es Salaam.

Siku ile wanafunzi wa Zanaki walipanda jukwaani kuonesha mchezo wa kuigiza ulioitwa ‘Hadi Lini!’ na yeye Winifrida alicheza nafasi ya mhusika mkuu. Ulikuwa mchezo uliomwelezea mwanamke jasiri aliyepambana kunusuru ndoa yake pale mumewe aliyempenda alipoamua kumsahau na kumpenda mwanamke mwingine, baada ya kufanikiwa.

Winifrida alicheza nafasi ya mke mtii kwa ndoa yake ambaye mume wake alipata penzi jipya. Alicheza nafasi hiyo kwa uthabiti na kuuvaa uhalisia wa kweli, hasa pale aliposimamia kile alichokiamini na kuwafanya nusu ya watazamaji wasisimkwe na kupiga kelele za shangwe.

Walipomaliza tu onesho lao Jackson alimfuata alipokuwa amesimama na wenzake na kumpongeza. Winifrida alibinya mikono yake kwa shauku, raha iliyoje kupongezwa na kijana kama Jackson. Ni yeye Winifrida aliyetamani kumpongeza kwanza Jackson kwa onesho lake lililomsisimua kila mtu ukumbini. Ni Jackson aliyepanda jukwaani kabla yao.

Jackson alikuwa amejaaliwa sauti tamu na kipaji cha kuimba na alipokuwa jukwaani kila mtu alipagawa! Winifrida alihisi damu ikimchemka, roho ikamlipuka, miguu ikamcheza na moyo kumpapatika.

Kwa kweli Jackson alijaaliwa sauti nzuri na alijua hasa kuburudisha mashabiki awapo jukwaani, ndiyo maana haikuwashangaza wengi kuona wimbo wake wa ‘Nadhiri Yangu’ aliokuwa ameuachia kipindi hicho ukifanya vizuri sana kwenye vituo mbalimbali vya redio na runinga kuliko hata nyimbo za wakongwe.

Inaendelea...
 
Taxi - (62)

Sasa Jackson na Winifrida walikuwa wamesimama wakitazamana kwa makini, kila mmoja alikiona kitu fulani kwenye macho ya mwenzake. Penzi changa! Kwa muda mfupi tu waliosimama na kupongezana ulitosha kuwajulisha kuwa kila mmoja alikuwa amevutiwa na mwingine. Na kuanzia siku hiyo ukawa mwanzo wa kuchipua kwa penzi lao, ingawa hadi wakati huo hawakuwa wamekutana kimwili.

Kabla ya hapo, Winifrida hakuwa akijihusisha kabisa na uhusiano wowote wa kimapenzi japo hakuacha kubughudhiwa kila alipopita mtaani, kama alivyojiwekea nadhiri kutojiingiza katika uhusiano wa kimapenzi hadi amalize shule, ni hivyo hivyo alivyoishi. Hakuringia uzuri wake lakini hakutaka pia usumbufu unaopitiliza kutoka kwa wavulana.

Kuanzia kidato cha kwanza hadi hapo alipofikia alikuwa na msimamo thabiti sana, hata hivyo, maringo yake yalifichwa na werevu wake darasani. Ilikuwa ni warembo wachache sana wa aina yake waliofanya vizuri kimasomo, jambo hilo liliwavutia walimu na wanafunzi waliopenda maendeleo kimasomo.

Lakini sasa Jackson alikaribia kumfanya aivunje nadhiri yake aliyojiwekea. Japo alikuwa amemwambia Jackson asubiri kwanza amalize kidato cha nne lakini Jackson alikuwa na maneno matamu sana yaliyokaribia kumtia wazimu.

Winifrida alianza kuwa mzembe darasani, badala ya kumsikiliza mwalimu, mawazo yake yote yalikuwa kwa Jackson.

Ndiyo maana haikushangaza siku ile mchana aliamua kutoroka shule na kuandamana na Jackson kwenda nyumbani kwao Kiwalani, alikuwa tayari kwenda kumpa penzi, lakini kaka yake Sammy… ah, sijui alitoka wapi na kutibua mipango yao!

Winifrida alijiona kuwa hakuwa huru kama wasichana wenzake. Alidhani kuwa hapa duniani hakuna kitu kizuri kuliko uhuru; uhuru wa kufanya apendacho duniani.

Kwa mara ile ile aliutamani ukubwa ikiwa udogo maana yake ni kudhibitiwa, lakini pia aliuchukia ukubwa ikiwa maana yake kudhibiti wadogo. Sasa alikwisha ingia katika mtihani mgumu wa mapenzi. Alimfikiri Jackson kila wakati, akimwona kila pahala, tangu katika sahani ya chakula hadi kitandani.

Alichukua begi lake la madaftari na kupekenyua sehemu fulani kwenye mifuko ya lile begi na kutoa simu yake ya mkononi aliyokuwa akiificha ili isionwe na kaka yake au wifi yake. Ilikuwa ni simu aina ya Huawei aliyonunuliwa na Jackson ili kuwarahisishia mawasiliano.

Alifungua sehemu ya kuhifadhi majina na kulitafuta jina la Jackson, alipoliona alilitazama kwa makini akitamani kumpigia simu, lakini akasita.

Mara akakumbuka jambo na kuinuka haraka, akalifuata kabati la nguo na kulifungua, akapekua pekua kwenye nguo zake na kutoa kadi ndogo ya kuhifadhi kumbukumbu kwenye simu (Micro SD). Ni kadi aliyoipata kwenye gari la Sammy siku ya kwanza tu Sammy alipokuja na gari nyumbani.

Winifrida aliketi juu ya kitanda, akatabasamu huku akiiangalia kwa makini ile kadi ndogo ya kuhifadhi kumbukumbu kwenye simu kisha akageuka kumwangalia Pendo aliyekuwa anakoroma. Aliifungua ile simu na kuiweka ile kadi ndani yake.

Ile kadi ilionekana kujaa picha, sauti na video. Winifrida alipotaka kuingiza picha zake yakatokea maandishi kwenye kioo cha simu yake: “Micro SD is Full do you want to format it?” Winifrida alishusha pumzi huku akiangalia juu, aliwaza kidogo na kuuma midomo yake.

Alitaka kufuta vitu vilivyokuwemo lakini akasita na kuamua kuifungua ile kadi kuona kilichokuwemo. Alikuta picha kadhaa za jengo la kisasa lenye chumba chenye vifaa ambavyo hakuvielewa, video moja na sauti ya kurekodiwa. Aliamua kuisikiliza ile sauti na alichokisia kilimtisha sana.

Ilikuwa ni rekodi ya maongezi ya simu kati ya mtu mmoja aliyeonekana kuwa ni mwanasiasa au mtu mwenye mamlaka makubwa serikalini na muuaji wa kukodiwa. Katika maongezi yao walikuwa wanapanga mikakati ya mauaji ya mtu waliyekuwa wakimtaja kwa jina la JM.

Winifrida aliyasikiliza kwa makini maongezi yao huku akihisi kuogopa mno. Ubaridi wa woga wa aina yake ulimtambaa mwilini na mapigo ya moyo wake yalibadili mwendo wake na kwenda mbio isivyo kawaida! Nywele kichwani kwake zilisimama na mwili kusisimka. Hakumaliza kusikiliza maongezi, akayaondoa na kuamua kutazama ile video.

Lahaula! Alijilaumu kwa nini aliitazama ile video. Ilikuwa video ya mauaji ya kutisha, hakuamini alichokiona, alidhani labda ni sinema ya kutengenezwa. Lakini alipoitazama vizuri alihisi ilikuwa na uhusiano na yale maongezi aliyoyasikia awali. Hata hivyo, kuna jambo lilimshtua zaidi, gari la Sammy lilionekana kwa mbali!

“Lilifuata nini gari la Sammy kwenye ile video ya mauaji?” Winifrida alijiuliza swali lile na maswali mengine kibao: Je, mauaji yale yalikuwa yanahusiana vipi na Sammy? Ile kadi ya kumbukumbu kwenye simu aliyoikuta kwenye gari la Sammy ilifikaje? Je, Sammy alikuwa anaelewa chochote kuhusiana na yale mauaji?

Winifrida alijawa na hofu kubwa. Kichwa chake kilikuwa kimejawa na mawazo na kuchanganyikiwa kwa wakati mmoja. Alijihisi moyo wake ukilemewa na msukumo mkubwa wa damu na asijue la kusema. Hakuwa na majibu ya yale maswali.

Aliogopa sana na kuitoa ile kadi haraka, akaificha kabatini huku akihisi kama Sammy alikuwa akimchungulia dirishani, kwa mara ya kwanza alianza kumwogopa kaka yake. Alipanda kitandani, akajilaza na kujifunika shuka gubigubi huku akijikunyata kwa woga.

Taxi imeanza kuzua mambo! Usikose kuifuatilia simulizi hii ya kusisimua ili kuujua mwisho wake. Ciao...
 
Taxi - (63)

ILIPOISHIA

Winifrida aliyasikiliza kwa makini maongezi yao huku akihisi kuogopa mno. Ubaridi wa woga wa aina yake ulimtambaa mwilini na mapigo ya moyo wake yalibadili mwendo wake na kwenda mbio isivyo kawaida! Nywele kichwani kwake zilisimama na mwili kusisimka. Hakumaliza kusikiliza maongezi, akayaondoa na kuamua kutazama ile video.

Lahaula! Alijilaumu kwa nini aliitazama ile video. Ilikuwa video ya mauaji ya kutisha, hakuamini alichokiona, alidhani labda ni sinema ya kutengenezwa. Lakini alipoitazama vizuri alihisi ilikuwa na uhusiano na yale maongezi aliyoyasikia awali. Hata hivyo, kuna jambo lilimshtua zaidi, gari la Sammy lilionekana kwa mbali!

“Lilifuata nini gari la Sammy kwenye ile video ya mauaji?” Winifrida alijiuliza swali lile na maswali mengine kibao: Je, mauaji yale yalikuwa yanahusiana vipi na Sammy? Ile kadi ya kumbukumbu kwenye simu aliyoikuta kwenye gari la Sammy ilifikaje? Je, Sammy alikuwa anaelewa chochote kuhusiana na yale mauaji?

Winifrida alijawa na hofu kubwa. Kichwa chake kilikuwa kimejawa na mawazo na kuchanganyikiwa kwa wakati mmoja. Alijihisi moyo wake ukilemewa na msukumo mkubwa wa damu na asijue la kusema. Hakuwa na majibu ya yale maswali.

Aliogopa sana na kuitoa ile kadi haraka, akaificha kabatini huku akihisi kama Sammy alikuwa akimchungulia dirishani, kwa mara ya kwanza alianza kumwogopa kaka yake. Alipanda kitandani, akajilaza na kujifunika shuka gubigubi huku akijikunyata kwa woga.

SASA ENDELEA...

* * * * *

Saa tatu na nusu asubuhi, katika Shule ya Sekondari ya Zanaki, Winifrida alikuwa ameketi darasani akiwa mkimya mno jambo lililowashangaza wanafunzi wenzake, kwani haikuwa kawaida yake kutulia vile. Kwa tabia yake ya uchokozi kwa wengine na sauti yake kali ilikuwa rahisi kuhisi uwepo wake, na siku ambayo hakufika shule kila mtu angejua kuwa hayupo.

Hata hivyo, kimya cha siku ile kilikuwa cha sauti tu, kwani kichwani mwake mlikuwa mmejaa mawazo yaliyokuwa yakisokotana na kumfanyia kelele ambazo mtu yeyote hakuweza kuzisikia ila yeye mwenyewe.

Hakuwa na furaha kabisa moyoni mwake kutokana na kumbukumbu mbaya ya picha alizozishuhudia usiku uliokuwa umetangulia kwenye kadi ya simu aliyoiokota kwenye gari la kaka yake.

Ndani ya darasa lile la kidato cha nne kulikuwa na utulivu mkubwa, wanafunzi walikuwa wakimsikiliza mwalimu wao wa sayansi, Mwalimu Josephat Igembe. Hata hivyo, Winifrida aliyeonekana kama alikuwa akimsikiliza Mwalimu Igembe kwa makini, aliishia kumwangalia tu pasipo kusikia chochote alichoongea, mawazo yake yote yalikuwa mbali kabisa, nje ya zile kuta nne za darasa.

Kila mara alijitahidi kuyarudisha mawazo yake yawemo darasani, na hata alipopata nafasi ya kumsikiliza mwalimu, Kiingereza chake kilikuwa rahisi sana, lakini ule ujumbe uliokuwemo katika maana ndiyo uliokuwa mgumu. Winifrida aliviajiri viungo vyote vya mwili wake vimfikishie ujumbe, lakini wapi!

Maneno yaliteleza kinywani mwa Mwalimu Igembe utadhani maji yakiteremka mlima, kwa hali hiyo aliacha wazi masikio yake na kuyasabiria maneno ya mwalimu yule ili kuelewa maana ya neno moja moja.

Mara alishangaa kuona wanafunzi wenzake wote wakigeuka kumtazama kwa mshangao, na yeye akawatazama kwa mshangao. Kabla hajujua kulikoni, akashtuliwa na sauti ya Mwalimu Igembe, “Winifrida, mbona ni swali rahisi kabisa, sijui kwa nini unafikiria kiasi hicho!”

Winifrida alimkodolea macho Mwalimu Igembe, hakujua ajibu nini kwani hata swali lenyewe hakuwa amelisikia. Alishusha pumzi ndefu huku akiiminya midomo yake.

“Okay, mwingine anayejua jibu lake atusaidie, naona Winifrida leo hayuko sawa, pengine akili kazisahau nyumbani!” Mwalimu Igembe alisema na kuwafanya wanafunzi wote, isipokuwa Winifrida, wacheke. Hata hivyo, hali hiyo ilimfanya Winifrida ashushe pumzi za ahueni japo alikuwa anatweta kama aliyekuwa amekoswa na risasi.

“Sijui nifanye nini sasa? Naona hali hii inaanza kuathiri hata masomo yangu! Naogopa nikimuuliza kaka naweza kusababisha matatizo makubwa na nikimwambia wifi sijui kama atanielewa! Na hata akinielewa itakuwaje endapo ni kaka Sammy ndiye mhusika wa tukio lile? Halafu watakapojua kuwa nina simu watataka kujua nimeipata wapi? Ah… Mungu niepushe na balaa hili…” Winifrida aliwaza, mara mawazo yake yote yalivutwa na picha za tukio la mauaji, sasa alikuwa kama anaona tukio lile likifanyika mbashara mbele ya macho yake

Aliwaona wanaume wawili ambao walizishika bastola zao sawasawa kwenye mikono yao, wakazielekeza kwa mwanamume mmoja na kummiminia risasi kama mvua, kisha wakamweka kwenye kiroba na kukiburuta kuelekea nje…

Winifrida alijikuta akipiga kelele kwa nguvu bila kujitambua, darasa zima wakageuka kumtazama kwa mshangao. Mwalimu pia aliacha kufundisha na kugeuka kumtazama kwa mshangao, hakuelewa nini kilikuwa kimemsibu Winifrida siku hiyo.

"Is she dreaming?” (Anaota?) Mwalimu Igembe aliwauliza wanafunzi wengine huku akishangaa sana.

Darasa lote wakacheka kwa nguvu, lakini kicheko chao kilikatika ghafla baada ya kumwona Winifrida akilia kwa hofu huku akitetemeka sana, na kabla hawajajua kilichokuwa kinaendelea walimwona akisimama na kutoka nje mbio huku akilia.

“Zaituni, mfuate ujue ana tataizo gani?” Mwalimu Igembe alimtaka mwanafunzi mmoja wa kike aliyekuwa rafiki mkubwa wa Winifrida kumfuata.

Zaituni aliinuka na kutoka nje haraka kumfuata Winifrida huku wanafunzi wengine wakibaki wamepigwa na butwaa. Darasa lote lilikuwa na utulivu mkubwa sana.

* * * * *

Saa nne kasorobo asubuhi, Sammy na Elli walikuwa wanaingia katika ofisi za West Car Rentals zilizopo kwenye ghorofa ya kwanza ya jengo la ghorofa mbili lililoko katika barabara ya Ali Hassan Mwinyi eneo la Upanga Mashariki, jijini Dar es Salaam.

Baada ya kujadiliana kuhusu mwenendo wa biashara ya Sammy hatimaye walikubaliana kwenda kumwona rafiki wa Elli aliyemiliki kampuni ya ukodishaji magari kwa ushauri zaidi, wakiamini kuwa Sammy angejifunza mengi na pengine kubadili mtazamo wake kuhusu biashara ya teksi.

Walipoingia ndani waliurudishia mlango taratibu na kusimama wakiwatazama watu sita waliowakuta mle ndani wakiwa wamekaa kwenye makochi, katika eneo la mapokezi ya ofisi ile, kati yao Waafrika walikuwa wawili vijana na wazungu wanne, wanawake wawili na wanaume wawili.

Wale watu waliokuwa mle ndani waligeuza shingo zao kuwatazama Sammy na Elli, kasoro mwanadada mmoja aliyeonekana kutingwa mno na shughuli kwenye kompyuta yake.

Inaendelea...

CC the_legend Norshad bobefu zoefu Pablo PAKAYA Ibney blackstarline Bryece Tater Bigjahman moneytalk marybaby nipo2 ram kisukari Smart911 Madame S carbamazepine Astelia culture gal Prisoner of hope Mine eyes kuku mweus Thad hearly Shunie moneytalk Tumosa Mine eyes Kudo swahiba92 ludist Toyota escudo Clkey macson3 boga la kiangazi LEGE Smart911 Richard irakunda skfull popie Krizy Beat hearly nipo2 MWINDAJI HARAMU kakhulu Katavi Norami mbududa iron2012 popie Bughy Harry Mlenge Kacheda mjasiliamali Laki Si Pesa cocochanel kinusikwetu big jambo mludego Shupavu Kacheda mjasiliamali Mweweso Songa Heri esiankiki
 
Taxi - (64)

Mwanadada yule aliitwa Cynthia West, alikuwa na umri wa miaka 25, sura yake ilikuwa ndefu kiasi na pua ndogo ndefu. Alivaa sketi fupi iliyoishia sentimita chache juu ya magoti yake, ilikuwa nyeusi yenye miraba myeupe, blauzi nyeupe ya mikono mirefu na viatu vyeusi vyenye vikanyagio virefu vya mchuchumio

Alikuwa chotara wa kizungu mwenye shingo ndefu kiasi iliyobeba mabega ya kike na shingoni alivaa kidani cha dhahabu kilichoning’inia kifuani kwake na kuzama katikati ya uchochoro wa matiti yake ya ukubwa wa wastani.

Elli na Sammy waliwasalimia kwa Kiswahili wale watu waliowakuta mle ndani. Ni wale Waafrika pekee walioitikia ile salamu kwa pamoja, kasoro wale wazungu na yule mwanadada aliyeko kwenye kompyuta.

Kisha Sammy na Elli waliwasalimia wale wazungu kwa Kiingereza huku wakipunga mikono yao ya kulia na kuwafanya wale wazungu waitikie kwa bashasha zote.

Muda huo yule mwanadada aliyeko kwenye kompyuta aliinua uso wake mara moja na kuwaangalia Sammy na Elli. Macho yake yakagongana na yale ya Elli na Sammy. Yule mwanadada akaachia tabasamu pana na kurudisha macho yake kwenye kompyuta.

“Cynthia, hujambo dada’angu?” Elli alimsalimia yule binti kwa bashasha.

“Sijambo, kaka Elli, shikamoo,” Cynthia alisema huku akiacha kuchapa huku akiendelea kutabasamu.

“Marahaba. Pole na kazi,” Elli aliitikia huku akimsogelea.

“Asante, karibuni sana,” Cynthia aliitikia kisha akageuza shingo yake kumtazama Sammy huku akiendelea kutabasamu.

“Shikamoo,” alimsalimia Sammy kwa hesima zate.

“Marhaba, za kazi?” Sammy aliitikia huku naye akitabasamu.

“Nzuri,” Cynthia alisema huku akiyarudisha macho yake kwenye kompyuta mara moja na kuyarudisha tena macho yake kuwaangalia wageni wake huku akionekana ni mtu mwenye furaha muda wote.

Kabla Elli hajamuuliza Cynthia chochote mlango wa ofisi ile ulifunguliwa na mwanamume mmoja mnene na mrefu aliyefuga rasta aliingia. Alikuwa pia chotara wa kizungu na aliitwa McDonald West. Alipowaona Elli na Sammy aliwasogelea haraka huku akimtazama Elli kwa mshangao kama vile hakuwa ametegemea kumwona pale muda ule.

“Umepaa?” McDonald alimdaka Elli juu kwa juu bila hata ya salamu.

“Wala sijapaa, barabara tuliyojia haikuwa na foleni kabisa, askari wa usalama barabarani walikuwa wakiziita gari, nadhani kuna mkubwa fulani alikuwa anaandaliwa kupita,” Elli alisema huku akinyoosha mkono wake kumsalimia McDonald. Wakasalimiana kwa furaha kisha McDonald aliwakaribisha ofisini kwake.

Kilikuwa ni chumba cha ofisi cha ukubwa wa kawaida chenye samani chache muhimu za kiofisi. Kulikuwa na zulia lenye rangi za bendera ya taifa la Tanzania sakafuni, meza kubwa ya kiofisi ambayo juu yake kulikuwa na kompyuta aina ya Acer i5 na kioo cha flat, kiti kirefu cha ngozi halisi cha kiofisi chenye magurudumu madogo yaliyokiwezesha kusogea, na kilikuwa kinazunguka.

Mbele ya ile meza kulikuwa na viti viwili pamoja na kochi moja la sofa kwa ajili ya wageni, meza ya kioo ya pembe nne na chini ya meza ile kulikuwa na magazeti na majarida kadhaa yaliyoandikwa “Dar Guides”. Juu ya meza ile kulikuwa na vitabu, nakala chache za magazeti ya siku ile na nakala kadhaa za ramani kubwa ya Tanzania ikionesha maeneo ya vivutio vya utalii.

Kwa pembeni kulikuwa na rafu iliyopangwa vitabu na majarida chungu nzima ya utalii na ukutani kulikuwa na ramani kubwa ya Tanzania, yenye kuonesha maeneo mbalimbali yenye vivutio. Elli na Sammy waliketi kwenye viti vilivyokuwa mbele ya meza ya McDonald.

“Uliponipigia simu nilikuwa maeneo ya Muhimbili nikadhani huenda ningekuwahi, enhe nipe habari?” McDonald alisema baada ya Elli na Sammy kuketi kitako.

“Ni kama nilivyokueleza, huyu ni ndugu yangu, anaitwa Sammy…” Elli alianza kuelezea huku akimwoneshea Sammy kwa McDonald.

“Sasa, ngoja kwanza niwatoe hawa jamaa hapo mapokezi, wametokea Uswisi jana na walipaswa kuwa safarini kuelekea Iringa leo hii…” McDonald alisema na kuinuka, akatoka nje ya ofisi yake akiwaacha Sammy na Elli.

Muda huo huo simu ya Sammy ilianza kuita, alipoiangalia kwa makini akagundua kuwa ilikuwa simu kutoka kwa Dk. Masanja. Sammy alisita kidogo kisha akaamua kuipokea.

“Hello!” alisema mara tu alipoiweka kwenye sikio. Akasikia mwangwi wa sauti yake ukimrudia, akashtuka. Hii ilimaanisha kuwa simu ilikuwa imewekwa sauti ya juu ‘Loud speaker’ ili kumwezesha mtu au watu wa upande wa pili kusikia yanayoongelewa upande wa pili wa simu pasipo kuiweka sikioni.

“Hujambo, kijana wangu?” ilikuwa sauti ya Dk. Masanja aliyeongea kwa sauti tulivu.

“Sijambo, shikamoo.”

“Marhaba, vipi unaweza kuwa na nafasi ufike hapa ofisini kwangu leo?” Dk. Masanja alisema kwa sauti tulivu.

“Leo! Sidhani kama nitaweza kufika, nipo mbali kidogo, labda kesho kama itawezekana,” Sammy alisema huku akionesha kusita. Akasikia sauti ya Mr. Oduya ikiongea upande wa pili wa simu kumtaka Dk. Masanja amuulize alipo ili wamfuate. Sammy alishtuka kidogo, hata hivyo hakutaka kumwonesha Elli kuwa alishtuka.

“Kwani upo wapi, naweza hata kukufuata huko huko uliko!” Dk. Masanja alimuuliza Sammy.

Sammy alibaki kimya kwa muda akifikiria nini aongee, kwani alianza kuhisi kuwa kulikuwa na jambo lisilo la kawaida likiendelea. Alikumbuka jinsi alivyogombana na Mr. Oduya walipokutana ofisini kwa Dk. Masanja pale alipomtaka awe mshirika wake. Akajiuliza, huyo mzee alikuwa anamtakia nini!

Sammy, are you there?” Dk. Masanja aliuliza kwa wasiwasi baada ya kuona kimya.

“Mmh… kwani ulikuwa unasemaje mzee, wangu? Labda naweza kukujibu hata humu kwenye simu.”

“Ah, kuna mambo haipendezi kuyaongea kwenye simu, ndiyo maana nilitaka kujua upo wapi!”

“Kuna tatizo lolote?” Sammy aliuliza huku akikunja sura yake na kuminya midomo.

“Hakuna, kuna mambo fulani nataka nikushirikishe,” Dk. Masanja alisema na kushusha pumzi.

“Unishirikishe?” Sammy aliuliza huku akiwa bado amekuja sura yake.

“Ndiyo, kwani kuna ubaya kukushirikisha? Au mimi na wewe tumeshakuwa na uadui siku hizi?”

“Hakuna ubaya, lakini kwa leo haitawezekana. Nipo nje ya mji na ninatarajia kurudi kesho.”

“Kesho saa ngapi nikutegemee?”

“Ngoja nione halafu nitakujulisha,” Sammy alisema na kukata simu, akashusha pumzi za ndani kwa ndani. Elli alimtazama kwa makini.

Itaendelea...
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom