Stori ya kusisimua - Taxi

Taxi - (70)

ILIPOISHIA

Wageni hao walikuwa wajumbe wa kamati maalumu ya fitna na ushindi, muda huo walikuwa katika kikao maalumu chini ya uenyekiti wa Meneja Mkuu wa Udzungwa Beach Resort, Dk. Masanja na katibu alikuwa Balozi Mageuzi. Ajenda kuu ya kikao ilikuwa kupanga mikakati jinsi ya kumsaidia Mr. Oduya kushinda kinyang’anyiro cha kusaka nafasi ya kuteuliwa na Chama Cha Ukombozi kugombea urais wa nchi.

Katika muda ule, upepo mwanana ulikuwa unavuma kutokana na mvua ya rasharasha iliyokuwa inanyesha na kuyasonga songa mapazia marefu yaliyokuwa yamefunika madirisha matatu makubwa mle ofisini. Mara simu ya mkononi ya Mr. Oduya ikaanza kuita na kumshtua. Alipoitazama kwa makini akagundua kuwa mpigaji alikuwa mwanasheria wake, Adam Mafuru.

Mr. Oduya aliminya midomo yake huku akikunja sura, aliitazama saa yake ya mkononi huku akionekana kutafakari kidogo na kushusha pumzi, alijiondoa kutoka pale kwenye kiti alipokuwa ameketi na kuwataka radhi wageni wake, akatoka na kuelekea nje ya ofisi.

Alisimama ukumbini karibu na dirisha, akayatupa macho yake kuangalia nje na kuipokea ile simu kisha akaipeleka moja kwa moja kwenye sikio lake.

SASA ENDELEA...

“Unasemaje?” alimdaka Mafuru juu kwa juu pasipo hata salamu.

“Boss, nimeliona gari!” Mafuru alisema kwa sauti iliyoonesha wasiwasi na yenye kitetemeshi.

“Gari gani?” Mr. Oduya aliuliza kwa pupa huku akiwatupia jicho wageni wake.

“Cadillac DeVille uliloagiza liteketezwe…” Mafuru alisema na kumfanya Mr. Oduya ahisi kama mwili wake ukiraruka vipande viwili. Moyo wake ulipiga mshindo mkubwa! Alihisi pumzi zikimpaa na moyo wake ukianza kwenda mbio isivyo kawaida.

“Una uhakika?” Mr. Oduya aliuliza akihisi labda hakuwa amemsikia vizuri. Muda huo pumzi zilizotoka hazikulingana na zile zilizoingia kwenye mapafu yake.

“Ndiyo, wa asilimia zote,” Mafuru alisema kwa msisitizo.

Mr. Oduya alivuta pumzi ndefu na kuzishusha taratibu huku akiwa haamini alichokuwa akielezwa na Mafuru.

“Umeliona wapi?” aliuliza kutaka uhakika.

“Kwenye televisheni, kuna mtangazaji wa televisheni alikuwa analionesha kwenye kipindi chake cha Mbunifu Wetu…” Mafuru alisema na kumfanya Mr. Oduya ahisi kizunguzungu.

Alijiegemeza kwenye ukuta huku akipitisha mkono wake wa kulia kichwani akianzia kwenye paji la uso wake hadi kisogoni. Kwa mara ya kwanza alihisi kuogopa sana. Hakuwa na neno, kikazuka kitambo kirefu cha ukimya mzito, Mr. Oduya alianza kupiga hatua za taratibu kuzunguka pale ukumbini.

Habari ile aliyopewa na Mafuru ilikuwa imemshtusha sana. Taratibu ghadhabu ilianza kuchipua ndani yake.

“Una uhakika ni gari letu?” hatimaye Mr. Oduya aliuliza tena baada ya ukimya wa muda mrefu. Sauti yake ilikuwa ya kutetemeka kutokana na hofu na hasira kwa pamoja.

“Sana, hata rangi yake bado ni ileile haijabadilishwa, ndiyo maana nimekupigia simu, mzee,” Mafuru alijibu kwa sauti iliyoashiria wasiwasi mkubwa.

Kikapita tena kitambo kifupi cha ukimya, kisha Mr. Oduya akakata simu. Sasa alijiona yu hatarini kuliko hata hatari yenyewe. Akatafuta namba za Spoiler na kumpigia simu.

“Nakuhitaji hapa kwenye ofisi ya Mikocheni jirani na Rose Garden haraka iwezekanavyo!” Mr. Oduya alisema kwa sauti yenye kuashiria ghadhabu.

“Nipo mbali, bosi,” Spoiler alisema kwa sauti yenye wasiwasi kidogo.

“Silas!” Mr. Oduya aliita kwa kufoka kisha akapiga ngumi ukutani. “Uwe mbali ama karibu, nakuhitaji hapa Mikocheni haraka!” aliposema hivyo akakata simu yake na kurudi ofisini alikokuwa amewaacha wageni wake.

Alikuwa yu moto haswa na kichwa chake kilikuwa kinamgonga huku mikono ikimtetemeka. Alihisi baridi ya hofu ikipenya hadi kwenye mifupa na mapigo ya moyo wake yalidunda dabali. Muda ule alihisi hakuwa huru nafsini mwake hata kidogo. Alitamani kupiga yowe la hasira na sauti yake ikamsaliti. Kwa nini apige yowe, haoni kama angewapa watu faida?

Wageni wake walimtazama kwa mshangao mkubwa jinsi alivyobadilika. Ukimya mkubwa ulitamalaki ndani ya ile ofisi pana iliyojaa watu kumi na watano. Ulikuwa ukimya uliomfanya kila mtu mle ndani akiogope hata kivuli chake! Mr. Oduya aliketi kwenye kiti chake akiwa na fadhaa.

“Kuna tatizo lolote?” Balozi Mageuzi aliuliza baada ya kumwona Mr. Oduya akiwa amenywea kama aliyekuwa amepigwa na shoti ya umeme.

“Kuna tatizo dogo la kiufundi limejitokeza,” Mr. Oduya alijitutumua na kumjibu Balozi Mageuzi, moyo ulikuwa ukimwenda msobemsobe.

“Tatizo hilo linahusiana na masuala yetu ya siasa?” Dk. Masanja naye alimuuliza haraka huku akimkodolea macho kwa wasiwasi.

“Hapana, ni tatizo la kifamilia, natakiwa kulishughulikia haraka na kila kitu kitakuwa sawa,” Mr. Oduya alisema huku akijipa ujasiri uliokuwa umetoweka muda mfupi uliopita.

Kisha aliwaomba wajumbe waahirishe kikao ili apate muda wa kushughulikia jambo la dharura lililojitokeza usiku ule na kulikamilisha kabla hakujapambazuka. Baadhi ya wajumbe walijaribu kumdadisi lakini hakuwa tayari kuwaleleza jambo lenyewe. Hawakuwa na nanmna nyingine zaidi ya kukubali. Wakaondoka kwa makubaliano ya kukutana siku nyingine, katika sehemu nyingine itakayopangwa.

Alipobaki peke yake Mr. Oduya aliitazama saa yake ya mkononi kwa minajili ya kujua muda. Ilikuwa saa sita na robo usiku. Mishale ya saa na dakika kwenye simu ilimfanya azidi kupungukiwa subira. Zilikaribia kutimia saa mbili tangu alipomtaka Spoiler afike nyumbani kwake. Alisema yupo mbali, mbali ya wapi? Mr. Oduya alijiuliza.

Alitoka nje na kusimama chini ya mti wa kivuli kwenye uzio wa jumba lile, jirani na kilipo kibanda cha walinzi kando ya geti kubwa la kutokea. Muda ule eneo lile lilikuwa na ukimya mno.

Kulikuwa na watu wanne, Mr. Oduya mwenyewe, dereva wake Madjid na walinzi wake binafsi wawili waliokuwa makini kuhakikisha usalama upo. Hata hivyo, walinzi wale hawakushangaa kumwona Mr. Oduya akiwa pale muda huo akizunguka zunguka, mikono kaiweka nyuma na kichwa kakiinamisha chini.

Ilikuwa kawaida yake alipokuwa na mambo nyeti kuitumia nyumba ile kwa ajili ya kukutana na washirika wake, kwa mambo nyeti. Wakati mwingine alikuja pale alipokuwa amekorofishana na mkewe Dk. Oduya, kwani ilikuwa inatokea kiasi cha kumfanya mzee ashindwe kulala nyumbani.

Mara wakasikia muungurumo wa gari likija eneo lile na kusimama kwenye eneo maalumu la maegesho nje ya jumba lile. Kutokana na haraka aliyokuwa nayo, Mr. Oduya hakusubiri, alimtuma dereva wake achungulie nje kuona ni nani aliyekuwa amefika pale. Madjid alichungulia haraka kwa tahadhari na kumweleza Mr. Oduya kuhusu ujio wa Spoiler.

Spoiler alikuwa peke yake ndani ya gari na hakuteremka, alibaki kwenye usukani akiwa ametahayari. Mr. Oduya alitoka na kwenda kumkabili Spoiler. Alimtazama kwa macho yaliyokuwa yakiwaka kwa ghadhabu.

“Kwa nini uliniongopea?” Mr. Oduya alimuuliza Spoiler kwa sauti yenye ghadhabu.

Spoiler alishtuka sana, alimtazama Mr. Oduya kwa hofu akiwa haelewi kilichokuwa kinaendelea. Alifungua mdomo wake kutaka kuuliza lakini sauti yake ikamsaliti, hakuna kilichotoka mdomoni. Akapandisha mabega yake juu na kuyashusha.

Inaendelea...

CC the_legend Norshad bobefu zoefu Pablo PAKAYA Ibney blackstarline Bryece Tater Bigjahman moneytalk marybaby nipo2 ram kisukari Smart911 Madame S carbamazepine Astelia culture gal Prisoner of hope Mine eyes kuku mweus Thad hearly Shunie moneytalk Tumosa Mine eyes Kudo swahiba92 ludist Toyota escudo Clkey macson3 boga la kiangazi LEGE Smart911 Richard irakunda skfull popie Krizy Beat hearly nipo2 MWINDAJI HARAMU kakhulu Katavi Norami mbududa iron2012 popie Bughy Harry Mlenge Kacheda mjasiliamali Laki Si Pesa cocochanel kinusikwetu big jambo mludego Shupavu Kacheda mjasiliamali Mweweso Songa Heri esiankiki mnadhimu mkuu wa jf
 
Taxi - (71)

“Gari ulilipeleka wapi?” Mr. Oduya aliuliza tena huku akionekana kuchemkwa kwa hasira. Alizidi kumkodolea macho Spoiler.

“Gari gani?” Spoiler aliuliza kwa mshangao uliochanganyika na wasiwasi.

“Cadillac DeVille nililoagiza liteketezwe miaka mitatu iliyopita.”

“Mbona lilikatwakatwa kisha likauzwa kama chuma chakavu!” Spoiler alisema huku mshangao ukiwa haujamtoka usoni.

“Una uhakika?” Mr. Oduya alimuuliza Spoiler akiwa bado amemtulizia macho yake usoni.

“Nilimpa kazi hiyo Jonas Odilo, yule jamaa wa duka la vipuri vya magari pale Shaurimoyo na alinihakikishia kuwa ameifanya kazi hiyo kwa umakini mkubwa kama nilivyomwambia.”

“Kama lilikatwakatwa mbona leo limeoneshwa kwenye televisheni. Kwanza kwa nini umwachie mtu kulikatakata wakati wakati nilikutaka uliteketeze mwenyewe na kisibaki kitu?” Mr. Oduya aliuliza tena na kulamba midomo yake iliyokuwa imekauka.

Spoiler hakuna na jibu, alimkodolea macho Mr. Oduya huku akiihisi ghadhabu ambayo ingemshukia muda wowote.

I’m disappointed, very disappointed,” (Nimefadhaika, tena sana) Mr. Oduya alisema huku akimtazama Spoiler kwa hasira.

Spoiler alishusha pumzi za ndani kwa ndani huku akiuinamia usukani wa gari lake kama mtu aliyeelemewa na mzigo mzito wa mawazo. Alitulia hivyo kwa sekunde kadhaa mpaka alipokusanya nguvu. Kisha alikiinua kichwa chake na kumtazama Mr. Oduya huku akitikisa kichwa chake kulia na kushoto. “Basi atakuwa ametuzunguka.”

Mr. Oduya alionekana kuduwaa. Alitulia akimtazama Spoiler kwa hasira.

“Kwa hiyo nifanye nini, mkuu?” hatimaye Spoiler aliuliza kwa fadhaa kama punguani aliyeingoja kwanza akili yake irudi toka ilikokimbilia.

“Unaniuliza ufanye nini?” Mr. Oduya alifoka kwa hasira. “Ina maana hujui cha kufanya?”

“Hapana mkuu!” Spoiler alisema haraka huku mapigo ya moyo wake yakienda mbio isivyo kawaida, “nilidhani labda una jambo la kuniambia. Hata hivyo usijali, kutakapopambazuka nitajua cha kufanya,” Spoiler alisema na kuwasha gari lake kisha akamuaga Mr. Oduya na kuanza kuondoka.

“Silas!” Mr. Oduya aliita, Spoiler alikanyaga breki na kugeuza shingo yake kumtazama Mr. Oduya kwa wasiwasi.

“Naomba kazi hiyo iwe nadhifu ambayo haitaacha alama yoyote nyuma ya kukutilia mashaka,” Mr. Oduya aliongeza. Spoiler aliitikia kwa kichwa na kuliondoa gari lake kwa mwendo wa kasi uliosababisha magurudumu yachimbe ardhi.

* * * * *

Saa tatu asubuhi, ndege ya shirika la ndege la Tanzania (ATCL) aina ya Airbus 220-300 ilikuwa ikizunguka angani kutafuta uelekeo mzuri wa kutua katika Kiwanja cha Ndege cha Kimataifa cha Julius Nyerere (JNIA) kilicho kilomita 12 kusini magharibi mwa jiji la Dar es Salaam.

Ndege hiyo ilikuwa inatokea jijini Mwanza ikiwa na abiria takriban mia moja. Kati ya abiria walioabiri ndege hiyo alikuwemo mwanadada Tunu Michael, aliyekuwa anatokea jijini Mwanza.

Tunu ambaye hakuwa amezidi miaka therathini, alikuwa msichana mrefu na maji ya kunde na mwenye umbo matata lenye kuweza kuitaabisha vibaya nafsi ya mwanaume yeyote. Alikuwa na nywele fupi na laini alizozitia rangi ya dhahabu. Alikuwa na sura ya duara yenye macho legevu na pua ndefu, midomo yake ilikuwa na kingo pana kiasi zilizopakwa rangi nzuri ya pink.

Alikuwa na vishimo vidogo mashavuni mwake vilivyofanya wanaume wababaike kidogo kwa uzuri wake kila walipomtazama. Asubuhi ile alikuwa amevaa blauzi ya pinki ya mikono mirefu iliyoyaficha vyema matiti yake imara madogo na suruali nyeupe ya jeans iliyombana na kuzuiwa na kiuno chake chembamba kiasi chenye misuli imara.

Miguuni alikuwa amevaa viatu vya ngozi vya rangi ya pink vyenye vikanyagio virefu vya mchuchumio na kumfanya azidi kuonekana mrembo kwelikweli. Mbali ya urembo aliokuwa nao, alikuwa msomi akiwa amebobea kwenye masuala ya teknolojia ya habari na mawasiliano (ICT), kiasi cha kucheza na kompyuta kwa kadri alivyotaka.

Wakati ndege aina ya Airbus 220-300 ilipokuwa ikielekea kutua, Tunu alikuwa akitazama mandhari tulivu ya kiwanja cha ndege cha Julius Nyerere kupitia dirishani, aliajabia uzuri wa kiwanja hicho, hasa jengo namba tatu la abiria, ambalo lilikuwa limekwisha anza kutumika.

Akiwa ameanza kuzama kwenye mawazo akifikiria kile alichokuja kukifanya jijini Dar es Salaam, mara akashtuliwa na mtikisiko mdogo uliotokea mle ndani ya ndege baada ya magurudumu ya ndege ile kugusa kwenye ardhi ya kiwanja cha ndege.

Ndege ilianza kwenda kasi ikipita katika barabara ndefu iliyotiwa lami na kuwekwa michoro elekezi kwa rubani wa ndege, kisha ikapunguza mwendo na kwenda kusimama mbele ya jengo namba mbili la kiwanja cha ndege.

Muda mfupi baada ya ndege kusimama na milango ya ile ndege kufunguliwa huku ngazi zikiwekwa sawa, abiria walianza kufungua mikanda ya siti zao na kuanza kushuka taratibu.

Tunu aliinuka kutoka kwenye kiti chake, akahangaika kuchukua begi lake dogo la rangi ya kijivu kutoka sehemu maalumu ya kuwekea mizigo kwenye sehemu ya juu ya ile ndege na kujiunga kwenye foleni ya abiria waliokuwa wakishuka.

Waliposhuka kwenye ndege waliingia kwenye jengo namba mbili la kiwanja cha ndege huku akili yake ikijikita katika kutafakari ni kwa namna gani atafanikiwa kutimiza kile kilichompeleka Dar es Salaam.

Baada ya muda alikuwa ametoka ndani ya lile jengo na kutokezea eneo la mbele la ule uwanja wa ndege katika sehemu kulipokuwa na maegesho ya magari.

Aliangaza macho yake huku na huko akionekana kutafuta kitu kisha akatoa simu yake na kuanza kutafuta namba fulani kutoka kwenye orodha ya majina ndani ya simu, kabla hajapiga akahisi mkono wa mwanamume ukimshika begani na kumshtua.

Aligeuka kumtazama aliyemgusa na kumwona mwanamume mmoja mrefu, mwenye umbo kakamavu la kimichezo akimtazama kwa uso wa tabasamu la furaha. Alikuwa na sura ya ucheshi na umri wake haukuzidi miaka therathini na mbili, alikuwa amevaa shati la kitenge la mikono mirefu, kofia nyeusi ya pama, suruali ya bluu ya dengrizi na viatu vya ngozi miguuni.

Inaendelea...
 
Taxi - (72)

“Karibu sana Dar es Salaam,” yule mwanamume alisema huku akikumbatiana na Tunu.

“Ahsante sana, Victor,” Tunu aliitikia kwa furaha huku akimwachia yule mwanamume.

“Nisamehe kwa kuchelewa kidogo kuja kukupokea, gari langu liliniletea shida wakati najiandaa kuja, ilibidi niliache kwa jamaa yangu na nichukue gari lake ili nikuwahi,” Victor alisema huku tabasamu usoni kwake likizidi kuchanua.

“Oh! pole sana, hata hivyo hujachelewa,” Tunu alimtia moyo Victor, kisha aliongeza, “Vipi hapa Dar, kazi zinaendeleaje?”

“Hapa mambo ni faya kama ulivyotuacha. Naona siku hizi hata hupumziki, mwezi uliopita ulikuwa nchini Israel, juzi umetoka Afrika Kusini na leo tena kiguu na njia umekuja Dar es Salaam!” Victor alisema na kumfanya Tunu acheke kidogo.

“Unajua huwa siwezi kulala wakati naona kuna kazi inanisubiri,” Tunu alisema huku akianza kupiga hatua taratibu, “Hata hivyo, nilitakiwa niende jijini Arusha kuna kazi moja natakiwa nikaifanye wiki hii, lakini nimelazimika kuiweka pembeni kwanza ili kuja kumalizia kwanza kiporo changu nilichokiacha miaka mitatu iliyopita.”

“Hujaniambia hasa ni kazi ipi unayokuja kuifanya Dar?” Victor alimsaili Tunu huku akiwa na shauku.

“Usijali, muda ukifika utaijua. Kwa sasa wacha nipambane kwanza na hali yangu,” Tunu alisema huku akiangua kicheko hafifu.

Walilifikia gari alilokuja nalo Victor, aina ya Toyota Rav4 jeusi na kuingia kisha safari ya kuondoka kiwanjani pale ikaanza. Kwa dakika zisizopungua tano walisafiri katika barabara nzuri ya lami ya kutokea pale kiwanjani iliyokatisha katikati ya bustani nzuri ya maua, na muda mfupi baadaye walilivuka geti la kutokea.

Ndani ya gari walikuwa wawili tu na muda wote hakuna aliyemsemesha mwenziwe, Tunu alikuwa amezama kwenye kutazama mandhari yale baada ya kutengana nayo kwa muda mrefu. Walipofika mwisho wa barabara ile Victor alikunja kona kuingia kulia akiifuata barabara ya Nyerere iliyoelekea katikati ya mji akiwa katika mwendo wa wastani.

* * * * *

Saa tatu asubuhi kwenye duka la kuuza vipuri vya magari, katika mtaa wa Lindi eneo la Shaurimoyo jijini Dar es Salaam, Spoiler aliyekuwa ameghadhabika sana alimbamiza Jonas Odilo kwenye meza katika ofisi ndogo iliyokuwa ndani kwenye duka la kuuza vipuri vya magari. Spoiler alikuwa ameipandisha juu miwani yake myeusi ya kuficha macho.

Jonas alikuwa mwanamume mwenye umri wa kati ya miaka 35 na 40, alikuwa mfupi mnene mwenye misuli imara ya mikononi iliyotuna kikamilifu na kumfanya aonekane kama bondia. Alikuwa na nywele fupi na uso mpana uliotulia kama maji ya mtungini. Asubuhi hiyo alivaa suruali nyeusi ya jeans na shati la rangi ya samawati lenye mistari ya bluu.

Alikuwa na uso uliotahayari na alimtazama Spoiler kwa hofu kubwa. Spoiler alikuwa amefika pale akiwa ameongozana na Dulla Mcomoro mwenye umbo kakamavu kama wachezaji wa mpira wa kikapu wa Marekani aliyekuwa amesimama karibu ya mlango akiwa makini kuhakikisha watu walioko nje hawajui kilichokuwa kinaendelea ndani ya ofisi ya duka hilo.

Dulla Mcomoro alikuwa amevaa miwani myeusi ya jua iliyokuwa imeyaficha macho yake makubwa na mekundu yenye uchovu lakini yaliyokuwa na kila dalili ya kuonya na muda wote.

Spoiler aliyazungusha macho yake kuangalia ndani ya ofisi ya Jonas ndani ya lile duka la kuuza vipuri vya magari akiwa kakunja sura yake, alikuwa bado kamkandamiza Jonas juu ya meza. Jonas alimtupia jicho Spoiler kwa hofu. Alipumua kwa shida akiwa bado amekandamizwa kichwa chake juu ya meza.

Spoiler alitoa kisu chake kutoka kwenye ala yake iliyokuwa kiunoni na kukisogeza karibu ya macho ya Jonas aliyekiona na kuanza kutetemeka kama aliyepagawa na mapepo.

“Kwa nini ulitusaliti?” Spoiler alimuuliza Jonas huku akimkazia macho yenye ghadhabu.

“Ni tamaa tu ndugu yangu. Jamaa alinishawishi nimuuzie, kwa kuwa alikuwa anasafiri nalo kwenda Botswana nikamuuzia!” Jonas alijaribu kujitetea kwa sauti ya kitetemeshi. Spoiler alimwinua na kumbana ukutani. Akamkodolea macho yake yenye kutisha huku akimuelekezea kisu shingoni.

Jonas alifumba macho yake huku akiendelea kutetemeka. Alimeza funda kubwa la mate kutowesha koo lake lililokauka ghafla.

“Gari uliliuza kwa nani?” sauti ya Spoiler ilimshtua Jonas na kumfanya afumbue macho yake na kukutana na macho yaliyokuwa yakiwaka kwa ghadhabu.

“Nimelisahau jina lake lakini ninazo nyaraka zote tulizoandikishana wakati wa kuuziana,” Jonas alisema kwa woga na hapo Spoiler akamwachia na kumsukumia kwenye meza.

“Zilete haraka, vinginevyo nitakuua.”

Jonas alifungua droo ya meza yake na kutoa faili kubwa, akaanza kulipekua kwa takriban dakika mbili na kutoa karatasi fulani, akampa Spoiler kwa mkono uliotetemeka. Spoiler alizipokea na kuzitupia jicho haraka haraka, kisha akaziweka mfukoni na kumkabili tena Jonas.

Dulla Mcomoro aliitupia jicho la wasiwasi saa yake ya mkononi na kuchungulia ndani ya kile chumba cha ofisi walichokuwemo Spoiler na Jonas.

“Tumebakiwa na sekunde hamsini tu,” Dulla Mcomoro alimwambia Spoiler huku akimwonesha saa yake.

“Ngoja nimalizie kazi,” Spoiler alisema huku akimkandamiza Jonas kwenye ukuta na kumwelekezea kisu chake. Muda huo huo wakasikia sauti za watu wawili wakiingia ndani ya lile duka na mmoja alikuwa anamwita Jonas.

Spoiler alishtuka na kumwachia Jonas. Alimtazama kwa ghadhabu na kurudisha kisu chake kwenye ala yake, kisha aliivaa miwani yake myeusi ili kuficha macho yake yenye ghadhabu.

“Hatujamalizana bado, nitarudi!” Spoiler alisema na kugeuka kisha akaanza kupiga hatua kutoka eneo lile haraka. Aliwapita wale wateja wawili wanaume waliokuwa wamesimama mle dukani wakisubiri kuhudumiwa.

Itaendelea...
 
Taxi - (73)

Alifika kwenye gari lao aina ya Toyota Hilux double cabin la rangi ya bluu lililokuwa na namba bandia na kumkuta Dulla Mcomoro akiwa ameketi kwenye usukani na gari likiwa linaunguruma taratibu. Akapanda na gari likaondoka kwa kasi kutoka eneo hilo huku watu waliokuwepo eneo lile wakiwa hawajui kilichokuwa kimefanyika mle ndani ya duka la kuuza vipuri.

Jonas akiwa bado ana hofu, alitoka kwenye chumba kidogo cha ofisi yake na kuwatazama wateja waliokuwa wanamsubiri. Alikuwa na uso uliosawajika sana na mapigo ya moyo wake yalikuwa yakienda mbio isivyo kawaida.

“Samahani jamani, leo sifanyi biashara kuna sehemu natakiwa kwenda,” Jonas alisema na kuanza kufunga milango ya duka lake huku akiwa na wasiwasi. Wale wateja walishangaa sana, walijaribu kumuuliza kama kulikuwa na tatizo lakini hakuwa tayari kueleza chochote.

Alipomaliza kufunga milango akaingia kwenye gari lake aina ya Toyota Carina na kuondoka haraka akipanga kutofungua duka hadi pale ambapo angehakikisha hali ni shwari, kwani hakutaka kina Spoiler wakirudi tena wamkute pale dukani. Aliondoka akiwaacha wateja wake wanashangaa.

* * * * *

Gari aina ya Toyota Rav4 jeusi lililokuwa likiendeshwa na Victor lilikuwa katika mwendo wa wastani kaatika barabara ya Nyerere eneo la Kamata likielekea Mnazi Mmoja. Victor alikuwa makini barabarani na wakati huo Tunu alikuwa ameketi kwenye siti akiwa anaangalia nje kupitia ukuta msafi wa kioo wa dirisha la gari hilo.

Alikuwa amezama akilitazama anga la Maanani. Kwa dakika zote alizoketi ndani ya lile gari tangu Kiwanja cha Ndege cha Kimataifa cha Julius Nyerere alikuwa akiwashuhudia walimwengu wakiwa katika pilika pilika za kuisaka fedha ndani ya jiji la Dar es Saalaam katika siku ile mpya.

Alijikuta tu akitamani afike haraka alikokuwa amepanga kwenda asubuhi ile kabla hajaelekea nyumbani kupumzika, na alikuwa akiomba kimoyomoyo amkute mtu aliyekuwa akimfuata pale Mnazi Mmoja. Kimtazamo tu ungeweza kutambua kuwa Tunu alikuwa katika wakati mgumu sana.

Kichwani kwake alikuwa na maswali mengi sana yaliyokosa majibu. Alijiuliza kama kwa miaka mitatu tangu alipolazimika kuondoka Dar es Salaam, ni nini kilichokuwa kikiendelea? Alivuta pumzi ndefu na kuzishusha taratibu kisha akaegemeza kichwa chake kwenye siti na kufumba macho yake.

Fadhaa ilijitokeza kwenye uso wake, aliapa kutorudi nyuma, hasa alipokumbuka masahibu yaliyompata miaka mitatu iliyopita yakikaribia kuyagharimu maisha yake. Muda wote Victor aliendesha kimya na alikuwa akimtupia jicho Tunu bila kusema neno.

* * * * *

Saa nne kasoro dakika kumi, katika mapokezi ya kituo cha televisheni cha Mzizima eneo la Mnazi Mmoja, Sammy alikuwa amesimama mbele ya kaunta ya mapokezi ya kituo kile cha televisheni akifoka. Alikuwa anapumua kwa nguvu huku akiwakazia macho wahudumu wa mapokezi.

Sehemu ya mapokezi ya kituo cha televisheni cha Mzizima ilikuwa katika sehemu ya chini ya jengo la ghorofa kumi na mbili lililopo barabara ya Lumumba jirani na bustani ya Mnazi Mmoja.

Sehemu ile ilikuwa na umbo la nusu duara iliyozungukwa na meza nzuri ya kaunta ya mbao ya mti wa mpodo na ilikuwa ikitazamana na viti vyeusi vya ngozi laini kwa ajili ya wateja waliofika hapo na kusubiri kuhudumiwa.

Kulikuwa na wahudumu watatu pale mapokezi, wawili wanawake na mmoja mwanamume waliokuwa katika sare zao nadhifu za kazi, mashati meupe ya mikono mirefu yenye kola za rangi ya kijivu yakiwa na nembo ya Mzizima TV kifuani na suruali za rangi ya kijivu. Shingoni walivaa wamevaa tai ndogo nyeusi zilizowapendeza.

Kwenye viti vyeusi vya ngozi laini vya kusubiria kulikuwa na wateja wawili watatu waliokuwa wameketi wakimtazama Sammy kwa mshangao wakati akifoka mbele ya wale wahudumu wa mapokezi.

“Naona ananitafuta ubaya, nilikataa kabisa gari langu lisipigwe picha, kwa nini apige picha bila ruhusa yangu na kurusha kwenye kipindi chake? Naondoka lakini mwambieni huyo mtayarishaji kuwa tutakutana mahakamani!” Sammy alisema kwa hasira na kuanza kuondoka.

Alitoka nje akiwa bado ana hasira, aliusukuma mlango mkubwa wa kioo na kutoka nje kisha akaanza kuzishuka ngazi takriban kumi za varanda pana yenye sakafu nzuri ya tarazo na kupishana na Tunu aliyekuwa anaingia ndani ya lile jengo. Wakati wakipishana walitazamana kwa makini. Hakuna aliyemsalimia mwingine lakini macho yao yaliongea zaidi ya ambavyo wangeongea kwa midomo yao.

Tunu alizikwea zile ngazi za varanda haraka haraka kisha akausukuma mlango mkubwa wa kioo na kutokomea ndani. Alitokea kwenye sehemu ya mapokezi ya kituo cha televisheni ya Mzizima na kwenda moja kwa moja hadi kwenye mapokezi ya kile kituo cha televisheni.

Alifika na kusimama mbele ya mhudumu mmoja wa kiume. Kabla hajamuuliza chochote akamuona Maximillian, mtangazaji wa kipindi cha “Mbunifu Wetu” aliyekuwa akija pale mapokezi huku akiwa na wasiwasi. Maximmilian alikuwa akiyazungusha macho yake kutazama huku na huko kwa wasiwasi.

“Kaondoka?” Maximillian alimuuliza yule mhudumu wa kiume.

“Eeh! Ila kakasirika huyo! Amesema mtakutana mahakamani,” yule mhudumu alisema, kisha akamgeukia Tunu, “Anti, nikusaidie?”

Tunu aliyekuwa akimtazama Maximillian alishusha pumzi za ndani kwa ndani na kugeuza shingo yake kumtazama yule mhudumu mara moja.

“Nilitaka kumuulizia huyu kaka, bahati nzuri nimemuona,” Tunu alimwambia yule mhudumu kwa sauti tulivu na kumkabili Maximillian, “Samahani, kaka’angu!”

Maximillian aligeuza shingo yake kumtazama Tunu kwa makini. Tunu aliachia tabasamu pana la kirafiki huku akimsogelea. Maximillian naye alijikuta akiachia tabasamu, huku akionekana kuvutiwa na Tunu. Walitazama kwa sekunde chache kila mmoja akiwa kimya. Macho yao yaliongea mengi kuliko ambavyo wangeweza kuongea kwa mdomo.

Taxi imezua mambo. Kujua kitakachoendelea usikose kufuatana nami katika safari hii ya kusisimua...
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom