Taxi - (70)
ILIPOISHIA
Wageni hao walikuwa wajumbe wa kamati maalumu ya fitna na ushindi, muda huo walikuwa katika kikao maalumu chini ya uenyekiti wa Meneja Mkuu wa Udzungwa Beach Resort, Dk. Masanja na katibu alikuwa Balozi Mageuzi. Ajenda kuu ya kikao ilikuwa kupanga mikakati jinsi ya kumsaidia Mr. Oduya kushinda kinyang’anyiro cha kusaka nafasi ya kuteuliwa na Chama Cha Ukombozi kugombea urais wa nchi.
Katika muda ule, upepo mwanana ulikuwa unavuma kutokana na mvua ya rasharasha iliyokuwa inanyesha na kuyasonga songa mapazia marefu yaliyokuwa yamefunika madirisha matatu makubwa mle ofisini. Mara simu ya mkononi ya Mr. Oduya ikaanza kuita na kumshtua. Alipoitazama kwa makini akagundua kuwa mpigaji alikuwa mwanasheria wake, Adam Mafuru.
Mr. Oduya aliminya midomo yake huku akikunja sura, aliitazama saa yake ya mkononi huku akionekana kutafakari kidogo na kushusha pumzi, alijiondoa kutoka pale kwenye kiti alipokuwa ameketi na kuwataka radhi wageni wake, akatoka na kuelekea nje ya ofisi.
Alisimama ukumbini karibu na dirisha, akayatupa macho yake kuangalia nje na kuipokea ile simu kisha akaipeleka moja kwa moja kwenye sikio lake.
SASA ENDELEA...
“Unasemaje?” alimdaka Mafuru juu kwa juu pasipo hata salamu.
“Boss, nimeliona gari!” Mafuru alisema kwa sauti iliyoonesha wasiwasi na yenye kitetemeshi.
“Gari gani?” Mr. Oduya aliuliza kwa pupa huku akiwatupia jicho wageni wake.
“Cadillac DeVille uliloagiza liteketezwe…” Mafuru alisema na kumfanya Mr. Oduya ahisi kama mwili wake ukiraruka vipande viwili. Moyo wake ulipiga mshindo mkubwa! Alihisi pumzi zikimpaa na moyo wake ukianza kwenda mbio isivyo kawaida.
“Una uhakika?” Mr. Oduya aliuliza akihisi labda hakuwa amemsikia vizuri. Muda huo pumzi zilizotoka hazikulingana na zile zilizoingia kwenye mapafu yake.
“Ndiyo, wa asilimia zote,” Mafuru alisema kwa msisitizo.
Mr. Oduya alivuta pumzi ndefu na kuzishusha taratibu huku akiwa haamini alichokuwa akielezwa na Mafuru.
“Umeliona wapi?” aliuliza kutaka uhakika.
“Kwenye televisheni, kuna mtangazaji wa televisheni alikuwa analionesha kwenye kipindi chake cha Mbunifu Wetu…” Mafuru alisema na kumfanya Mr. Oduya ahisi kizunguzungu.
Alijiegemeza kwenye ukuta huku akipitisha mkono wake wa kulia kichwani akianzia kwenye paji la uso wake hadi kisogoni. Kwa mara ya kwanza alihisi kuogopa sana. Hakuwa na neno, kikazuka kitambo kirefu cha ukimya mzito, Mr. Oduya alianza kupiga hatua za taratibu kuzunguka pale ukumbini.
Habari ile aliyopewa na Mafuru ilikuwa imemshtusha sana. Taratibu ghadhabu ilianza kuchipua ndani yake.
“Una uhakika ni gari letu?” hatimaye Mr. Oduya aliuliza tena baada ya ukimya wa muda mrefu. Sauti yake ilikuwa ya kutetemeka kutokana na hofu na hasira kwa pamoja.
“Sana, hata rangi yake bado ni ileile haijabadilishwa, ndiyo maana nimekupigia simu, mzee,” Mafuru alijibu kwa sauti iliyoashiria wasiwasi mkubwa.
Kikapita tena kitambo kifupi cha ukimya, kisha Mr. Oduya akakata simu. Sasa alijiona yu hatarini kuliko hata hatari yenyewe. Akatafuta namba za Spoiler na kumpigia simu.
“Nakuhitaji hapa kwenye ofisi ya Mikocheni jirani na Rose Garden haraka iwezekanavyo!” Mr. Oduya alisema kwa sauti yenye kuashiria ghadhabu.
“Nipo mbali, bosi,” Spoiler alisema kwa sauti yenye wasiwasi kidogo.
“Silas!” Mr. Oduya aliita kwa kufoka kisha akapiga ngumi ukutani. “Uwe mbali ama karibu, nakuhitaji hapa Mikocheni haraka!” aliposema hivyo akakata simu yake na kurudi ofisini alikokuwa amewaacha wageni wake.
Alikuwa yu moto haswa na kichwa chake kilikuwa kinamgonga huku mikono ikimtetemeka. Alihisi baridi ya hofu ikipenya hadi kwenye mifupa na mapigo ya moyo wake yalidunda dabali. Muda ule alihisi hakuwa huru nafsini mwake hata kidogo. Alitamani kupiga yowe la hasira na sauti yake ikamsaliti. Kwa nini apige yowe, haoni kama angewapa watu faida?
Wageni wake walimtazama kwa mshangao mkubwa jinsi alivyobadilika. Ukimya mkubwa ulitamalaki ndani ya ile ofisi pana iliyojaa watu kumi na watano. Ulikuwa ukimya uliomfanya kila mtu mle ndani akiogope hata kivuli chake! Mr. Oduya aliketi kwenye kiti chake akiwa na fadhaa.
“Kuna tatizo lolote?” Balozi Mageuzi aliuliza baada ya kumwona Mr. Oduya akiwa amenywea kama aliyekuwa amepigwa na shoti ya umeme.
“Kuna tatizo dogo la kiufundi limejitokeza,” Mr. Oduya alijitutumua na kumjibu Balozi Mageuzi, moyo ulikuwa ukimwenda msobemsobe.
“Tatizo hilo linahusiana na masuala yetu ya siasa?” Dk. Masanja naye alimuuliza haraka huku akimkodolea macho kwa wasiwasi.
“Hapana, ni tatizo la kifamilia, natakiwa kulishughulikia haraka na kila kitu kitakuwa sawa,” Mr. Oduya alisema huku akijipa ujasiri uliokuwa umetoweka muda mfupi uliopita.
Kisha aliwaomba wajumbe waahirishe kikao ili apate muda wa kushughulikia jambo la dharura lililojitokeza usiku ule na kulikamilisha kabla hakujapambazuka. Baadhi ya wajumbe walijaribu kumdadisi lakini hakuwa tayari kuwaleleza jambo lenyewe. Hawakuwa na nanmna nyingine zaidi ya kukubali. Wakaondoka kwa makubaliano ya kukutana siku nyingine, katika sehemu nyingine itakayopangwa.
Alipobaki peke yake Mr. Oduya aliitazama saa yake ya mkononi kwa minajili ya kujua muda. Ilikuwa saa sita na robo usiku. Mishale ya saa na dakika kwenye simu ilimfanya azidi kupungukiwa subira. Zilikaribia kutimia saa mbili tangu alipomtaka Spoiler afike nyumbani kwake. Alisema yupo mbali, mbali ya wapi? Mr. Oduya alijiuliza.
Alitoka nje na kusimama chini ya mti wa kivuli kwenye uzio wa jumba lile, jirani na kilipo kibanda cha walinzi kando ya geti kubwa la kutokea. Muda ule eneo lile lilikuwa na ukimya mno.
Kulikuwa na watu wanne, Mr. Oduya mwenyewe, dereva wake Madjid na walinzi wake binafsi wawili waliokuwa makini kuhakikisha usalama upo. Hata hivyo, walinzi wale hawakushangaa kumwona Mr. Oduya akiwa pale muda huo akizunguka zunguka, mikono kaiweka nyuma na kichwa kakiinamisha chini.
Ilikuwa kawaida yake alipokuwa na mambo nyeti kuitumia nyumba ile kwa ajili ya kukutana na washirika wake, kwa mambo nyeti. Wakati mwingine alikuja pale alipokuwa amekorofishana na mkewe Dk. Oduya, kwani ilikuwa inatokea kiasi cha kumfanya mzee ashindwe kulala nyumbani.
Mara wakasikia muungurumo wa gari likija eneo lile na kusimama kwenye eneo maalumu la maegesho nje ya jumba lile. Kutokana na haraka aliyokuwa nayo, Mr. Oduya hakusubiri, alimtuma dereva wake achungulie nje kuona ni nani aliyekuwa amefika pale. Madjid alichungulia haraka kwa tahadhari na kumweleza Mr. Oduya kuhusu ujio wa Spoiler.
Spoiler alikuwa peke yake ndani ya gari na hakuteremka, alibaki kwenye usukani akiwa ametahayari. Mr. Oduya alitoka na kwenda kumkabili Spoiler. Alimtazama kwa macho yaliyokuwa yakiwaka kwa ghadhabu.
“Kwa nini uliniongopea?” Mr. Oduya alimuuliza Spoiler kwa sauti yenye ghadhabu.
Spoiler alishtuka sana, alimtazama Mr. Oduya kwa hofu akiwa haelewi kilichokuwa kinaendelea. Alifungua mdomo wake kutaka kuuliza lakini sauti yake ikamsaliti, hakuna kilichotoka mdomoni. Akapandisha mabega yake juu na kuyashusha.
Inaendelea...
CC
the_legend Norshad bobefu zoefu Pablo PAKAYA Ibney blackstarline Bryece Tater Bigjahman moneytalk marybaby nipo2 ram kisukari Smart911 Madame S carbamazepine Astelia culture gal Prisoner of hope Mine eyes kuku mweus Thad hearly Shunie moneytalk Tumosa Mine eyes Kudo swahiba92 ludist Toyota escudo Clkey macson3 boga la kiangazi LEGE Smart911 Richard irakunda skfull popie Krizy Beat hearly nipo2 MWINDAJI HARAMU kakhulu Katavi Norami mbududa iron2012 popie Bughy Harry Mlenge Kacheda mjasiliamali Laki Si Pesa cocochanel kinusikwetu big jambo mludego Shupavu Kacheda mjasiliamali Mweweso Songa Heri esiankiki mnadhimu mkuu wa jf