Stori ya kusisimua - Taxi

Taxi - (59)

ILIPOISHIA JANA

Walitazamana, Joyce naye aliachia tabasamu kabambe huku akishusha pumzi za ndani kwa ndani.

“Habari yako dada yangu?” Dynamo Plus alisalimia huku akinyoosha mkono wake kumpa Joyce.

“Salama, sasa mambo si hayo? Kwani ulivyonisalimia umekufa?” Joyce alisema na kumfanya Dynamo Plus acheke kidogo.

“Nimefurahi sana leo nimekutana na wewe, mimi ni shabiki wako. You are my favorite musician,” Joyce alisema huku tabasamu pana likishindwa kwenda likizo usoni kwake.

Dynamo Plus alijisikia fahari sana kusifiwa na Joyce, aliendelea kuung’ang’ania mkono wa Joyce huku akimtazama kwa makini usoni.

“Nafurahi kusikia kwamba hata watu kama ninyi mnazikubali kazi zangu,” Dynamo Plus alisema huku akishusha pumzi.

SASA ENDELEA...

“Kwani mimi nina tofauti gani na watu wengine?” Joyce aliuliza huku akimkazia macho Dynamo Plus.

“Wewe ni mtu mkubwa, watu kama ninyi muda mwingi mko bize, sina hakika hata kama mnapata muda wa kusikiliza nyimbo zetu,” Dynamo Plus alisema huku akipitisha ulimi kuilamba midomo yake mikubwa.

“Nina ukubwa gani mimi!” Joyce alisema na kuangua kicheko hafifu, akaendelea, “Tuyaache hayo, Aisha yuko wapi siku hizi? Nimemmisi sana,” Joyce aliuliza huku macho yake yakiwa yameweka kituo usoni kwa Dynamo Plus.

“Aisha dada’angu! Kwani mnafahamiana?” Dynamo Plus aliuliza kwa mshangao baada ya kufikiria kidogo.

“Ni best wangu sana, nilisoma naye kidato kimoja Sekondari ya Wasichana ya Tabora.”

“Anaishi Sweden siku hizi. Nimefurahi sana kukufahamu dada…” Dynamo Plus alisema na kuonekana kusita kidogo na kuachia kicheko hafifu huku akishika kichwa chake kuonesha kuwa amelisahau jina la Joyce.

“Joyce… Mrs. Joyce Kambona,” Joyce alisema huku akiachia tabasamu.

Oh yes, dada Joyce… you are a fashion designer, right?” Dynamo Plus alisema huku akimtazama Joyce kwa makini. Joyce aliachia tabasamu pana zaidi la bashasha.

Yeah! How do you know?” Joyce aliuliza huku akihisi furaha moyoni kwa kuwa Dynamo Plus alionesha kumfahamu.

“Nadhani tumewahi kukutana, pia nimekuwa nikisikia habari zako. Hasa Madame Norah amekuwa anakuongelea sana. She real admires you!” Dynamo Plus alisema na kumfanya Joyce azidi kujisikia fahari baada ya kugundua kuwa kumbe watu walikuwa wanaongelea habari zake.

* * * * *

Saa kumi alasiri, kwenye viunga vya maegesho ya magari vya mgahawa wa kisasa wa Elli’s, mtangazaji na mtayarishaji wa kipindi maarufu cha ‘Mbunifu Wetu’ katika kituo cha runinga cha Mzizima, Maximilian Njamba alikuwa amesimama kwa mbali akionesha kidole chake lilipokuwa limeegeshwa gari aina ya Cadillac DeVille lenye muundo wa kizamani likiwa na kibao cha “Taxi” juu yake.

Maximilian Njamba alikuwa mwanamume wa makamo mwenye umri wa kati ya miaka arobaini na tano na hamsini, si mrefu wala mfupi kwa kimo, pia hakuwa mwembamba wala mnene na alikuwa na sura ya ucheshi muda wote.

Alasiri ile Maximilian alikuwa amevaa kofia nyeusi ya pama, shati la mikono mirefu la pundamilia, suruali pana ya kijivu na viatu vyeusi ya ngozi miguuni.

Alikuwa amefika katika mgahawa wa kisasa wa Elli’s baada ya kuambiwa na rafiki yake kuhusu uwepo wa gari aina ya Cadillac DeVille lililosajiliwa kuwa teksi, alipoliona alijikuta akiupenda sana ubunifu uliotumika kulifanya lile gari kuwa la kibiashara.

Muda ule alikuwa ameshika kipaza sauti chenye nembo ya Mzizima TV akiwa mbele ya mpiga picha wake. Alikuwa akielezea jinsi alivyovutiwa sana na ubunifu uliotumika kwenye lile gari aina ya Cadillac DeVille.

Hii ilikuwa baada ya kumtafuta mmiliki wa gari lile, Sammy Kambona na kutaka kufanya naye mahojiano lakini Sammy alikataa katakata na kumuonya Maximilian asijaribu kulipiga picha gari lake bila idhini yake.

Kwa kuwa Maximilian aliiona ile teksi kama njia nzuri ya kuhamasisha ubunifu aliamua kuitumia ile fursa adimu ili kuwavutia watazamaji wa kipindi chake waweze kuhamasika kufikiria ‘nje ya boksi’ kwa kufanya vitu ambavyo watu wengine wangedhani haviwezekani.

Lakini tatizo lilikuwa ni Sammy, alikuwa amekataa kuhojiwa wala kupigwa picha, hivyo Maximilian aliamua kuvizia, pindi Sammy alipoingia ndani ya ule mgahawa wa Elli’s, akasimama kwa mbali lakini akihakikisha lile gari linaonekana kwenye kamera na kumtaka mpiga picha wake kulivuta gari karibu ili liweze kuonekana vyema.

Baada ya mpiga picha kuweka sawa mitambo yake na kumpa ishara kuwa alikuwa tayari, Maximilian alianza kazi iliyompeleka pale huku akiwa makini.

“Huu ni ubunifu wa hali ya juu sana, ila tunasikitika mmiliki wake amekataa kufanya mahojiano nasi, tungefahamu alifikiria nini kulifanya gari hili aina ya Cadillac DeVille lililotengenezwa zaidi ya miaka hamsini iliyopita kuwa teksi! Kwa kweli hii ni teksi inayovutia hasa, na kila mtu angependa kuwa abiria wake…” alisema yule mtangazaji wa kipindi maarufu cha ‘Mbunifu Wetu’ kilichorushwa na Mzizima TV.

“Na cha ajabu zaidi, licha ya kuwa ni gari la kizamani lakini ni kama mpya, haina matatizo yoyote na inaweza kukufikisha kokote uendako pasipo hofu ya kuharibika njiani… sasa ngoja nisikie maoni ya wakazi wa jijini Dar es Salaam kuhusu gari hili,” alisema Maximilian na kuelekea mtaani akijaribu kupata maoni ya wakazi wa jiji la Dar es Salaam.

Aliwauliza hasa wakazi walioishi jirani na eleo la mgahawa wa Elli’s kama wameshawahi kuliona gari aina ya Cadillac DeVille la muundo wa kizamani lililokuwa likitumika kama teksi na nini maoni yao kuhusu gari lile.

Wapo wakazi waliosema kuwa hawajawahi kuliona na wale walioliona walionekana kusifia sana akili ya kibunifu iliotumika kulifanya lile gari aina ya Cadillac DeVille la muundo wa kipekee kuwa teksi, wakidai kuwa lilikuwa ile hali ya upekee ingeweza kuwavutia watu wengi kutaka kuwa abiria wake na hivyo kulifanya gari liwe bidhaa adimu.

Wapo waliodai kuwa japo walikuwa wameliona ndani ya siku chache tu lakini tayari lilikwisha fahamika sana utadhani lilikuwa lina zaidi ya mwaka mmoja, wote walikiri kuwa wangependa kuwa abiria siku moja kutokana na upekee wake.

* * * * *

Saa moja jioni Sammy alikuwa anatoka ndani ya mgahawa wa kisasa wa Elli’s uliopo Ilala Sharif Shamba na kutembea haraka akikatiza kwenye viunga vya maegesho ya magari vya mgahawa ule, akalifikia gari lake aina ya Cadillac DeVille na kufungua buti la gari.

Inaendelea...

CC the_legend Norshad bobefu zoefu Pablo PAKAYA Ibney blackstarline Bryece Tater Bigjahman moneytalk marybaby nipo2 ram kisukari Smart911 Madame S carbamazepine Astelia culture gal Prisoner of hope Mine eyes kuku mweus Thad hearly Shunie moneytalk Tumosa Mine eyes Kudo swahiba92 ludist Toyota escudo Clkey macson3 boga la kiangazi LEGE Smart911 Richard irakunda skfull popie Krizy Beat hearly nipo2 MWINDAJI HARAMU kakhulu Katavi Norami mbududa iron2012 popie Bughy Harry Mlenge Kacheda mjasiliamali Laki Si Pesa cocochanel kinusikwetu big jambo mludego Shupavu Kacheda mjasiliamali Mweweso Songa Heri esiankiki
 
Taxi - (60)

Alitoa supana, akaanza kukifungua kibao chenye maandishi ya “Taxi” kilichokuwa kimepachikwa juu ya gari na kukitoa, kisha akakificha ndani ya buti la gari. Alipomaliza akafunga buti na kuingia kwenye gari.

Jioni ile aliokuwa na mawazo na alichoka sana, nadhani ilitokana na pilika pilika za kutwa nzima za kupeleka abiria huku na kule ambazo hakuwa amezizoea. Alifunga mkanda wa siti yake na kuliondoa gari taratibu kutoka kwenye maegesho ya magari ya ule mgahawa wa Elli’s na kuingia barabarani.

Muda huo gari lilionekana likiwa halina kibao cha kulitambulisha kuwa ni teksi, aliamua kufanya vile kila siku alipotaka kurudi nyumbani hadi siku ambayo angemweleza ukweli mkewe.

Saa moja jioni jiji la Dar es Salaam lilikuwa limemezwa na pilika pilika za aina yake za watu zilizoshamiri katikati na kwenye viunga vya jiji hilo kubwa zaidi Tanzania na hali ya hewa ilikuwa ya joto sana kama kawaida ya jiji hilo.

Uso wa Sammy ulikuwa umesawajika, alikuwa na mawazo mengi kwani hakutegemea kama Winifrida angeweza kugundua siri yake mapema vile kuwa lile gari lilitumika kama teksi. Aliendesha gari lake kwa utulivu hadi alipofika nyumbani kwake eneo la Tabata Chang’ombe.

Akionekana kuchoka sana, alifika mbele ya nyumba yake kwenye geti kubwa la mbele akapiga honi mara moja tu na kuinamisha kichwa chake kwenye usukani akisubiri kufunguliwa geti, mara usingizi mwepesi ukamchukua.

Alikuja kushtuliwa na Winifrida aliyekuwa anagonga kwenye kioo cha dirisha lake, Sammy aliinua kichwa chake kumtazama Winifrida, akaachia tabasamu na kuliingiza gari lake ndani kisha akalizima na kushuka akibeba mkoba wake wa kiofisi.

Alitembea taratibu kuelekea ndani na mlangoni akapishana na Joyce aliyekuwa akielekea dukani. Walisalimiana na Sammy akaingia ndani na kuelekea moja kwa moja chumbani kwake alikokwenda kuuweka mkoba wake wa kiofisi na kuanza kuvua nguo zake.

Alianza kwa kuvua koti lake na kulitupa kitandani, akalegeza tai yake na kuivua ikifuatiwa na shati, vyote akavitupia kitandani kisha akavua viatu na kuviweka kwenye stendi maalumu ya viatu, halafu akavua soksi na kuzitupia kitandani na mwisho akavua suruali na kutoa mkanda kisha akaitupia kitandani. Alipomaliza alivaa bukta na fulana nyepesi.

Akachukua shati lake alilovua na kuanza kusachi kwenye mifuko ya shati, akatoa vijiti vitatu na nusu vya kuchokonolea meno na kuvitupa ndani ya kapu dogo la taka lililokuwa limewekwa kwenye kona moja mle chumbani.

Kisha alichukua koti lake na kupekua kwenye mifuko akianza na mifuko ya nje kabla hajahamia mifuko ya ndani, akatoa kadi fulani mbili tatu, mojawapo ikiwa ile kadi aliyopewa na abiria wake mzungu na karatasi fulani, akaviweka kando na kuchukua suruali yake.

Alianza kukagua mifuko ya mbele kwanza kwa kutoa nje vitambaa vyake, akatoa simu yake ya mkononi na kuiweka kitandani, kisha alitomasa mfuko wa nyuma lakini hakuhisi kitu. Aliamua kuingiza mkono uliotoka patupu! Hakukuwa na kitu.

Akaiachia suruali ile ikaanguka chini kisha akashika kiuno akionekana kufikiria kidogo. Alionekana kung'aa macho akionekana kujiuliza maswali kisha akatazama kitandani. Alionekana kushtuka na kutoka chumbani haraka, akamkuta Winifrida akiwa ameketi sebuleni.

“Hebu niangalizie pochi yangu, nadhani nimeiacha ndani ya gari,” Sammy alimwambia Winifrida na kujibwaga juu ya sofa, mara akagutuka na kuinuka haraka, akaingia chumbani kwake kwa kujikongoja.

Aliuchukua mkoba wake wa kiofisi na kuufungua, akaangalia ndani na kuiona pochi yake. Akaifungua na kuziona fedha, alizihesabu kwa macho. Zilizokuwa kama noti kumi na mbili za shilingi elfu kumi kumi na noti nyingine kadhaa za elfu tano tano na elfu mbili mbili. Sammy aliachia tabasamu na kuiweka vizuri pochi yake ndani ya droo iliyokuwa kando ya kitanda.

Kisha alizichukua nguo zake pamoja na soksi na kuzitumbukiza kwenye tenga la nguo chafu lililokuwa limewekwa sehemu fulani ndani ya kile chumba. Kama aliyekumbuka kitu, aligeuza shingo yake na kujiangalia kwenye kioo kirefu cha meza ya vipodozi. Kisha alitoka kuelekea sebuleni na hapo akawaona Winifrida na Joyce wakiingia huku wameongozana.

“Sijaiona,” Winifrida alimwambia Sammy.

“Usijali nimekwisha iona, ilikuwa kwenye mkoba wangu!” Sammy alisema na kujibwaga tyena kwenye sofa, akavuta pumzi ndefu na kuzishusha taratibu huku akifumba macho yake. Alionekana kuzama kwenye mawazo.

Winifrida aliketi kwenye sofa huku akimtazama Sammy kwa kuvizia vizia. Joyce alielekea moja kwa moja jikoni na baada ya muda mfupi aliandaa meza kwa ajili ya chakula cha jioni na kusogea mbele ya Sammy, akasimama kwa heshima.

“Karibu chakula, Baba Pendo,” Joyce alisema huku akimwangalia Sammy kwa makini usoni.

Sammy alishtuka na kufumbua macho yake, akamtazama Joyce kwa kitambo kidogo bila kusema neno, kisha aliachia tabasamu kwa mbali na kujizoazoa taratibu kutoka pale kwenye sofa na kuelekea kwenye meza ya chakula.

“Naona leo hauko sawa, kuna tatizo?” Joyce alimuuliza Sammy huku akiwa bado anamwangalia kwa udadisi.

“Nimechoka tu,” Sammy alisema huku akiketi kwenye kiti chake.

Meza ya chakula ilikuwa imejaa mapochopocho: kulikuwa na wali mweupe, mchuzi mzito wa kuku, bakuli lenye nyama za kuku, bakuli la maharage yaliyoungwa kwa nazi, bakuli la mboga za majani, bakuli la saladi, matunda mchanganyiko kwenye sinia pamoja na jagi la maji ya kunywa na bilauri nne.

Ilikuwa imekwishatimu saa mbili na nusu usiku wakati Sammy na familia yake wakikaa mezani kwa ajili ya chakula cha jioni. Joyce alimnawisha Sammy mikono, kisha akamnawisha Pendo na kuwakaribisha.

Inaendelea...
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom