Stori ya kusisimua - Taxi

Stori ya kusisimua - Taxi

Taxi - (65)

“Nani?”

“Dk. Masanja, meneja mkuu wa Udzungwa Beach Resort, eti anataka kuniona!”

“Sasa, kwani…” Elli alitaka kusema neno lakini akakatizwa na mtu aliyefungua mlango wa ile ofisi. Wote wakageuka na kumwona McDonald akiingia.

* * * * *

Winifrida alipotoka darasani alikimbilia nyuma ya jengo la darasa huku akilia kilio cha kwikwi na kusimama ukutani, aliyazungusha macho yake kutazama huku na kule akihisi kijasho chembamba kikimtoka licha ya kuwa eneo lile lilikuwa na upepo na ule ulikuwa ni msimu wa baridi. Moyo wake ulikuwa umepoteza kabisa utulivu.

C’mon, Winnie, just relax,” alijiambia mwenyewe akijipa moyo kuwaasiwe na wasiwasi. Alivuta pumzi ndefu za ndani kwa ndani kisha akazishusha taratibu huku akiminya midomo yake yenye maki.

Relax baby, things gonna be alright…” Winifrida alijiambia kwa sauti kana kwamba alikuwa akimwambia mtu mwingine. Kisha alianza kujifuta jasho kwa kitambaa laini kilichokunjwa kwa umaridadi.

Muda huo huo akamwona Zaituni akimjia huku akiwa na wasiwasi. Zaituni alimsogelea na kabla hajasema chochote Winifrida alimwashiria kuwa amwache kwanza.

Zaituni alitii, Winifrida akaendelea kufuta machozi huku Zaituni akimtazama kwa mshangao. Walibaki kimya kwa kitambo kirefu kila mmoja akiwa anatafakari, kisha Winifrida alishusha pumzi za ndani kwa ndani.

Zaituni hakuweza kuvumilia alimuuliza Winifrida kama alikuwa na tatizo lolote huku akiwa amemtulizia macho usoni. Winifrida hakutaka kuongea hivyo alimweleza Zaituni kuwa hakujisikia vizuri na alihitaji kwenda nyumbani kupumzika.

* * * * *

Saa sita mchana, Joyce alishuka kutoka kwenye teksi na kumlipa dereva wa teksi fedha yake kisha akaanza kupiga hatua zake taratibu na kwa mwendo wa madaha akilisogelea jengo la Nuru TV. Muda huo alikuwa amevaa gauni zuri la kitenge lililodariziwa vizuri kwa nyuzi za dhahabu na kuushika mwili wake wenye umbo maridhawa la namba nane.

Mkononi alikuwa amevaa bangili kadhaa za pembe, kilemba kikubwa kichwani na begani kwake alikuwa ametundika mkoba mzuri wa kike wa pundamilia uliomgharimu fedha nyingi.

Wakati akitembea aliliona gari dogo aina ya Range Rover Sport L494 la rangi ya bluu la mwanamuziki Dynamo Plus likiingia katika viunga vya maegesho vya jengo la Nuru TV na kuegeshwa kwenye eneo lile

Joyce alisimama huku akijishika kiuno chake, alionekana kuwa na shauku ya kuonana na mwanamuziki Dynamo Plus ambaye muda huo alikuwa anashuka kutoka kwenye gari lake akiwa na watu wengine wawili. Mlinzi wake na meneja wake, Bob Tole.

Dynamo Plus alikuwa amevaa suruali ya jeans rangi ya bluu ya kubana iliyochanwa chanwa maeneo ya mapajani hadi kwenye magoti na kuacha matobo, fulana ya kata mikono na jaketi la bluu juu yake. Usoni alivaa miwani mikubwa ya jua iliyoficha macho yake, kofia aina ya kapelo kichwani na mkononi alikuwa ameshika simu mbili kubwa za kisasa.

Aliposhuka kwenye gari alianza kupiga hatua kubwa akielekea ndani ya jengo huku akiwa amewekwa katikati na mlinzi wake aliyekuwa kushoto kwake na meneja wake, Bob Tole kulia kwake. Joyce alimsogelea haraka huku akiachia tabasamu pana, akamdaka juu kwa juu bila hata salamu.

“Afadhali nimekuona, ninataka kukushirikisha kwenye project yangu…” Joyce alisema huku akinyoosha mkono wake kumsalimia Dynamo Plus. Dynamo Plus naye alinyoosha mkono wake huku akiachia tabasamu.

Project gani tena, dada Joy?” Dynamo Plus aliuliza huku akilamba lips zake kubwa.

“Ngoja tuingine ndani nikupe proposal yangu… kwa kifupi nataka tuingie mkataba ili uwe unatumia mavazi yangu kwenye maonesho yako, najua kila mmoja wetu atabenefit. Wewe utapata mavazi bure kutoka kwangu lakini utasaidia kunitangazia biashara. Sijui unasemaje?” Joyce alisema huku akimtulizia macho yake Dynamo Plus.

“Mmh!” Dynamo Plus aliguna kidogo huku akiminya midomo yake mikubwa, kisha aligeuza shingo yake kumtazama Bob Tole huku akikunja sura yake, alionekana kufikiria kidogo, ingawa hakuonesha kukubaliana na wazo hilo.

Kilizuka kitambo kifupi cha ukimya. Joyce aliendelea kumtulizia macho yake akiwa na shauku ya kusikia majibu yake.

“Si wazo baya lakini sidhani kama itawezekana,” Dynamo Plus alisema huku akimtazama Bob Tole na kutingisha kichwa chake taratibu kuonesha kutokukubaliana na wazo la Joyce, kisha alianza kupiga hatua taratibu kueleka ndani.

Joyce alishusha pumzi ndefu akionesha kukata tamaa, hata hivyo alimfuata Dynamo Plus taratibu.

“Nadhani ingekuwa busara kama ungeiona kwanza proposal yenyewe kabla hujaikataa offer yangu,” Joyce alisema huku akimshika Dynamo Plus begani.

Dynamo Plus aliachia tabasamu na kuilamba tena midomo yake huku akimtupia jicho Bob Tole kama aliyekuwa anatafuta ushauri.

“Nadhani si wazo baya, tuione kwanza proposal yake kabla ya kuamua,” Bob Tole alishauri.

Okay, utampatia meneja wangu aione kwanza, halafu tutajua la kufanya,” Dynamo Plus alimwambia Joyce kisha akaelekea kwenye chumba kimoja cha studio za Nuru TV.

* * * * *

Katika barabara ya Morogoro kwenye majengo ya Umoja wa Vijana mwanadada Nyaso Gilbert alikuwa anatokea ndani ya jengo dogo lililo upande wa barabara ya Morogoro, kisha akaanza kutembea haraka huku akiyatupa macho yake huku na kule kutafuta teksi.

Nyaso alikuwa amevaa suruali ya jeans ya rangi ya bluu mpauko iliyombana kiasi na kulichora vyema umbo lake refu maridhawa lenye tumbo dogo na kiuno chembamba na juu alivaa blauzi ya rangi ya pinki. Shingoni alivaa kidani cha dhahabu chenye herufi “N”.

Miguuni alikuwa amevaa raba ngumu za rangi ya bluu na begani alikuwa amening’iniza mkoba mzuri wa rangi ya bluu wa thamani kubwa. Uso wake ulikuwa umefichwa na miwani myeusi.

Inaendelea...
 
Taxi - (66)

Muda huo huo aliliona gari aina ya Cadillac DeVille la muundo wa kizamani lililokuwa na kibao chenye maandishi ya “Taxi” juu yake likisimama mbele ya jengo la Shree Tanzania Swaminarayan Mandal, jirani na jengo alilokuwa akitokea, kisha watu wawili vijana wenye asili ya Kiasia wakashuka na kumlipa dereva.

Baada ya wale watu kushuka gari lile lilianza kuondoka taratibu kutoka eneo lile na kuifuata barabara ya Morogoro, Nyaso aliyekuwa akitembea kwa mwendo wa haraka kuelekea kule lilipokuwa gari alianza kupunga mkono wake juu kumwashiria dereva asimame.

“Taxi! Taxi!” Nyaso aliita kwa nguvu wakati lile gari likianza kumpita na kumfanya Sammy akanyage breki na kuliegesha gari lake kando ya barabara, akamsubiri huku akishusha pumzi za ndani kwa ndani.

Nyaso alilikimbilia gari na alipolifikia akafungua mlango wa nyuma na kuutupia mkoba wake kwenye siti kisha akaingia na kuketi huku akihema kwa nguvu.

“Nipeleke Makumbusho,” Nyaso alisema huku akishusha pumzi ndefu. Sammy aliliondoa gari lake taratibu bila kusema neno akaifuata barabara ya Morogoro hadi alipofika usawa wa viwanja vya Tanganyika Legion, kwenye taa za kuongozea magari barabarani katika eneo la Bakhresa, akakata kuingia barabara ya Mazengo.

Aliifuata barabara ya Mazengo na mbele kidogo akaikuta barabara ya Faya iliyokatiza kutoka kushoto kuelekea upande wake wa kulia, akaivuka na kuendelea mbele hadi alipoukuta mtaa wa Kibasira, akakata kushoto kuifuata ile barabara na mbele kidogo akaukuta mtaa wa Isevya ulioingia kulia kwake.

Aliifuata barabara ile ya Isevya akipita nyuma ya viwanja vya Don Bosco na kwenda kutokea barabara ya Malik. Hapo akakunja na kuingia kushoto akiifuata ile barabara ya Malik na mbele kidogo akaikuta barabara ya Umoja wa Mataifa iliyowapeleka hadi kwenye taa za kuongozea magari barabarani za Sarenda.

Hapo Sarenda akakunja na kuingia kushoto akiifuata barabara ya Ali Hassan Mwinyi, na safari ya kuelekea Makumbusho ikaendelea. Muda wote walikuwa kimya na hakuna yeyote kati yao aliyeonekana kumfahamu mwingine, japo Sammy alikuwa mume wa Joyce na Nyaso alikuwa msaidizi wa Joyce.

Nyaso alitoa simu yake ya mkononi na kutafuta namba za Joyce kisha akapiga simu na kuiweka kwenye sikio lake la kushoto huku akiuma midomo yake, baada ya simu kuita kwa sekunde kadhaa alisikia simu ikipokelewa na Joyce.

“Da’ Joy, nimefanikiwa na sasa narudi, jiandae nakuja kukuchukua twende zetu Ubungo Plaza,” Nyaso alisema huku akishusha pumzi za ndani kwa ndani.

Sammy alimtupia jicho Nyaso kupitia kioo cha katikati cha gari lake cha kuangalia nyuma. Alimtazama kwa makini sana na kukunja sura yake akionekana kujiuliza kama alikwisha muona sehemu yoyote. Hata hivyo hakuweza kumfahamu, hivyo safari iliendelea huku wote wakiwa kimya.

Gari lilipofika eneo la Makumbusho Nyaso alimwonesha Sammy eneo ambalo alipaswa kusimamisha gari lake, ilikuwa ni kando ya barabara ya Bagamoyo jirani na jengo la Nuru TV. Sammy hakuzima injini ya gari, alijiegemeza kwenye siti yake kisha alimtupia jicho Nyaso aliyeonekana akiangaza macho yake kutazama kwenye jengo la Nuru TV, kisha akatoa tena simu yake na kupiga namba ya Joyce.

“Da’ Joy, njoo basi nimeshafika. Nipo hapa kando ya barabara nakusubiri… haya fanya fasta basi,” Nyaso alisema huku akiminya midomo yake.

Sammy aliyatupa macho yake kutazama kule alikokuwa akiangalia Nyaso na kumwona mkewe Joyce akitokea ndani ya jengo la Nuru TV akiwa ameshika simu yake na kuanza kutembea haraka huku akitupa macho yake kuangalia huku na huko.

Sammy alishtuka sana na kujikuta akipagawa, moyo wake ulishikwa na mfadhaiko na kuyasahau mapigo yake kwa nukta chache. Mapigo yalipoanza tena alivuta pumzi ndefu, akazishusha taratibu huku mwili wake ukiingiwa na ganzi iliyoyafanya maungo yake yazizime!

Sammy alimtazama Joyce kwa macho yaliyojaa hofu kisha aligeuka kumtazama Nyaso, akataka kumuuliza jambo lakini akasita na kugeuka tena kumtazama Joyce kwa hofu. Muda huo hakujua afanye nini. Alijiwa na mawazo kuwa aondoe gari haraka, lakini sauti nyingine ikamwambia hakuwa na haja ya kuondoka bali asubiri, kwani kuna kitu kilikuwa mbioni kutokea.

Akiwa katika kutafakari mara akamwona mwanamuziki Dynamo Plus akitoka haraka ndani ya lile jengo na kuanza kumwita Joyce. Joyce alisimama kugeuka kumsubiri Dynamo Plus huku sura yake ikiwa na shauku ya kusikia uamuzi wake juu ya ile proposal aliyompa.

“Meneja wangu amenihakikishia kuwa proposal yako imekaa vizuri sana, naomba tupate lunch huku tukizungumza vizuri namna tunavyoweza kufanya kazi pamoja,” Dynamo Plus alimwambia Joyce huku akitabasamu.

Joyce alionekana kufurahi sana, alijikuta akimkumbatia Dynamo Plus huku akiachia tabasamu pana, kisha alimwachia na kumshika mkono, wakaongozana kuelekea kwenye kantini iliyopo nyuma ya jengo lile huku wakiwa wameshikana mikono na kutembea kama wapendanao.

Sammy alishusha pumzi za ahueni huku akiyakaza macho yake kuwatazama kwa makini. Alifurahia kwa kitendo cha Joyce kurudi alikotoka lakini hakufurahishwa kwa kitendo cha kumwona akiwa na mwanamuziki Dynamo Plus. Alitamani ashuke na kwenda kuwazaba makofi lakini akajizuia sana. Kwa kweli hakujua afanye nini!

Mara simu ya Nyaso ikaanza kuita, Nyaso aliitazama kwa makini na kuipokea kisha akaipeleka moja kwa moja kwenye sikio lake.

“Nyaso, kuna jambo la muhimu sana limejitokeza, ni kuhusu ile proposal yetu hivyo natakiwa kuongea na Dynamo Plus tuone cha kufanya, wewe nenda tu ukaniwakilishe,” Joyce alisema.

“Okay, basi haina tatizo da’ Joy…” Nyaso aliitikia na kukata simu kisha akamtazama Sammy ambaye alikuwa bado anaangalia kule kwenye jengo la Nuru TV huku donge la wivu likiwa limemkaba shingoni.

“Twende Ubungo Plaza, Boss wangu amepata dharura,” Nyaso alimwambia Sammy na kujiegemeza kwenye siti.

Sammy aligeuka kumtazama Nyaso kwa makini, alitaka kumuuliza kitu lakini akasita na kushusha pumzi, kisha akaliondoa gari lake taratibu pasipo kusema kitu huku akiendelea kuangalia kule walikoelekea Joyce na Dynamo Plus.

Usikose kuifuatilia taxi ili kujua inaelekea wapi...
 
Taxi - (67)

ILIPOISHIA JANA

Sammy alishusha pumzi za ahueni huku akiyakaza macho yake kuwatazama kwa makini. Alifurahia kwa kitendo cha Joyce kurudi alikotoka lakini hakufurahishwa kwa kitendo cha kumwona akiwa na mwanamuziki Dynamo Plus. Alitamani ashuke na kwenda kuwazaba makofi lakini akajizuia sana. Kwa kweli hakujua afanye nini!

Mara simu ya Nyaso ikaanza kuita, Nyaso aliitazama kwa makini na kuipokea kisha akaipeleka moja kwa moja kwenye sikio lake.

“Nyaso, kuna jambo la muhimu sana limejitokeza, ni kuhusu ile proposal yetu hivyo natakiwa kuongea na Dynamo Plus tuone cha kufanya, wewe nenda tu ukaniwakilishe,” Joyce alisema.

“Okay, basi haina tatizo da’ Joy…” Nyaso aliitikia na kukata simu kisha akamtazama Sammy ambaye alikuwa bado anaangalia kule kwenye jengo la Nuru TV huku donge la wivu likiwa limemkaba shingoni.

“Twende Ubungo Plaza, Boss wangu amepata dharura,” Nyaso alimwambia Sammy na kujiegemeza kwenye siti.

Sammy aligeuka kumtazama Nyaso kwa makini, alitaka kumuuliza kitu lakini akasita na kushusha pumzi, kisha akaliondoa gari lake taratibu pasipo kusema kitu huku akiendelea kuangalia kule walikoelekea Joyce na Dynamo Plus.

SASA ENDELEA...

Aliendesha gari lake huku donge kavu la wivu uliochanganyika na hasira likiwa limemkaba kooni, alijisikia vibaya sana, alidhani kwamba alikuwa amemruhusu mkewe kutimiza ndoto yake kumbe alikuwa akimsogeza mbuzi karibu na chui!

Ilibaki kidogo tu apate ajali barabarani, mawazo yake yalikuwa kwa mkewe Joyce na Dynamo Plus yaliyomfanya akose umakini barabarani, kichwa chake kilikuwa kimevurugwa.

Sasa alikuwa na mgogoro wa ndani kwa ndani (interpersonal conflict), sauti moja ilimwambia arudi akamfumanie mkewe, kisha awape kipigo wote wawili, lakini sauti nyingine ilimwambia asifanye hivyo kwa kuwa hakuwa na uhakika kama walikuwa na uhusiano wa kimapenzi. Isitoshe angeweza kujiharibia kwa kuwa Joyce angegundua kuhusu siri yake ya kuendesha teksi.

“Vipi kaka, kuna tatizo lolote?” Nyaso alimuuliza Sammy akiwa ameitambua hali ya kukosa umakini iliyojitokeza baada ya kutaka kusababisha ajali kwa mara ya pili wakati wakivuka taa za kuongozea magari barabarani katika eneo la Tume ya Sayansi na Teknolojia.

Sammy alijishtukia na kumtazama Nyaso, akaachia tabasamu huku akishusha pumzi za ndani kwa ndani, “Wala hakuna tatizo,” alijibu na kuongeza mwendo akiitafuta Bamaga.

* * * * *

Saa tatu kasoro robo ya usiku iliwakuta Sammy, Joyce na Winifrida wakiwa kwenye meza ya chakula wakila kimyakimya, kila mmoja alikuwa akitafakari lake. Muda huo Pendo alikwisha kula tayari alikuwa chumbani amelala.

Muda wote wakati wa mlo Sammy alikuwa anawaza mambo mbalimbali yaliyomjia kichwani kwake. Alifikiria kuhusu mwelekeo wa biashara yake baada ya mazungumzo yake na McDonald West na kudhani kuwa muda mwafaka wa kuongeza magari mengine mawili ulikwisha fika.

Changamoto kubwa ilikuwa ni jinsi ya kupata magari mazuri na ya kipekee ambayo yangemwezesha kuukabili ushindani. Alitamani sana kupata magari kama lile alilokuwa nalo sasa. Pia aliwaza kuhusu kile alichokishuhudia kule Nuru TV, alipomwona mkewe akiwa ameongazana na mwanamuziki wa kizazi kipya, Dynamo Plus huku wameshikana mikono.

Donge la hasira lililochanganyikana na wivu lilikuwa bado limemkaba kooni kwake. Lakini pamoja na mawazo kumwandama, chakula kilishuka vilivyo kutokana na ustadi wa mapishi ya mkewe. Hata hivyo, muda wote Joyce hakujua kilichokuwa kikiendelea kwenye akili ya mumewe, yeye alifurahia chakula alichopika mwenyewe.

Winifrida alikuwa mtulivu sana muda wote wa chakula tofauti kabisa na kawaida yake, alimtazama Sammy kwa jicho la kuibia huku akionekana kuwa mbali kimawazo. Alikuwa akijaribu kulinganisha maisha ya kaka yake Sammy na kile alichokishuhudia kwenye video ya mauaji na kuzidi kuchanganyikiwa.

Walimaliza kula na Winifrida akatoa vyombo, kisha walishushia matunda na baadaye maji, halafu Winifrida aliwaacha akaingia chumbani kwake kujipumzisha.

Sammy na Joyce walikwenda kuketi sebuleni kwenye masofa kila mmoja akiwa na kijiti mdomoni akijaribu kuondoa masalio ya nyama pamoja na masalio mengine kwenye meno. Waliketi pale kwani Joyce alitaka kufuatilia mfululizo wa mchezo wa kuigiza wa “Gereza la Kifo” uliorushwa kwenye runinga.

Hata hivyo, mawazo ya Sammy hayakuwa kwenye runinga, alikuwa anapanga jinsi ya kumuuliza mkewe kuhusu uhusiano wake na mwanamuziki Dynamo Plus.

Hakutaka kukurupuka kwani angeweza hata kujichongea endapo mkewe angegundua kuwa ile teksi iliyokusudiwa kumchukua na kumpeleka Ubungo Plaza ni gari la mumewe Sammy, na hata aliyekuwa akiendesha teksi ile hakuwa mwingine zaidi ya mumewe mwenyewe.

Ni dhahiri uso wa Sammy haukuonesha furaha ingawa alijitahidi kuwa na furaha mbele ya Joyce.

Joyce aliligundua jambo hilo baada ya kumtupia jicho mara kwa mara, alijaribu kuivumilia hali ile lakini alishindwa na kuamua kuvunja ukimya.

“Naona leo ni kama huna furaha, nini kimekukera, mume wangu?” Joyce aliuliza kwa sauti tulivu huku akiyatuliza macho yake kwenye uso wa Sammy, alimwangalia kwa makini.

Sammy alimtazama mkewe na kujaribu kutabasamu lakini bado alishindwa kuficha wivu na hasira. Alipumua kwa nguvu, na kujiegemeza kichovu kwenye sofa huku akimtazama mkewe kwa umakini. Wivu na udadisi vilimsonga kwa pamoja. Alihisi labda mkewe alishampa ‘tunda’ Dynamo Plus au mwanaume mwingine. Donge la hasira na wivu lilizidi kumkaba kooni.

Joyce alipinda midomo yake upande wa kushoto na kushusha pumzi ndefu kama aliyemaliza mbio ndefu.

“Unajua, kwa siku za karibuni, hasa siku hizi mbili nimeona umebadilika kwa kiasi fulani tofauti na kawaida yako, sijajua tatizo ni nini hasa!” Joyce alisema huku akiminya midomo yake kisha akashusha pumzi.

“Inawezekana nikawa na mabadiliko lakini ni kwa sababu nakupenda sana. Mwenyewe unajua jinsi tulivyoanza uhusiano wetu hadi kufunga ndoa…” Sammy alisema na kusita kidogo, akavuta pumzi ndefu kisha akazishusha taratibu akionekana kutafakari kwa sekunde kadhaa kabla hajayahamishia macho yake kumtazama tena Joyce ambaye muda huo alikuwa kimya akimtazama kwa makini.

“Nimekuruhusu kwa moyo mmoja kwenda kwa Madame Norah ili uweze kutimiza ndoto yako ya siku nyingi, ila nadhani uhuru niliokupa unaweza kuniumiza siku moja…” Sammy alianza kufunguka lakini Joyce alimkatisha kwa upole huku akionekana kushtuka kidogo.

“Kwa nini unasema hivyo, kwani umeona nini kutoka kwangu?” Joyce aliuliza huku uso wake ukionesha mshtuko wake.

“Hapa si suala la nimeona nini kwako bali unapaswa kutambua kuwa wewe ni mke wangu wa ndoa, ni mimi mwenye haki ya kuushika na kuutomasa huo mwili wako. Nakuomba jichunge sana usije kurubuniwa na wasanii na baadaye ukanisaliti kisa unatimiza ndoto…” Sammy alisema huku akijizuia kukasirika.

Inaendelea...
 
Taxi - (68)

“Sammy, naona sasa umefika mbali jamani! Kwa nini unifikirie hivyo? Unajua tulikula kiapo cha uaminifu siku ile kanisani. Ingawa siwezi kusema kuwa sikumbani na vishawishi… nakumbana navyo na wakati mwingine najuta ni kwa nini nilizaliwa mrembo, lakini sijawahi kukusaliti. Kwanza ni dhambi kubwa!” Joyce alisema kwa huzuni huku akimtazama Sammy kwa makini.

Walitazamana kwa kitambo kifupi. Joyce alikuwa ameyatuliza macho yake kwenye uso wa Sammy huku akionekana kuhuzunishwa sana na maneno ya mumewe. Alishusha pumzi.

“Sipendi kukuona katika hali hii. Najihisi kuumia sana unapoanza kuniwazia mambo ambayo sifikirii kuyafanya. Labda kama hupendezwi mimi kwenda kwa Madame Norah au kuna mambo fulani umeyaona kwangu ni vyema ukayaweka wazi badala ya kuniongelea kwa mafumbo…” Joyce alisema kwa sauti iliyoonesha kutetemeka baada ya donge la simanzi kuanza kumkaba kooni.

“Ngoja nikuulize… hivi tokea tuoane hujawahi kunisaliti? Hujawahi kutongozwa huko nje kweli? Achana na hawa wasanii wanaofinyafinya macho kila wakiona mwanadada mrembo, yaani mtu akomae kabisa?” Sammy alimuuliza Joyce akimtulizia macho usoni ili aweze kumsoma.

Joyce alionesha kushtuka sana na uso wake ulionesha maumivu makubwa. Alifungua mdomo na kutaka kusema lakini maneno yakawa hayatoki.

“Labda nifupishe mambo, kuna mtu amekuona ukiwa na mwanamuziki Dynamo Plus mnatembea mkiwa mmeshikana mikono kwa mahaba, unaweza kunieleza kuna nini kinaendelea kati yako na huyo kijana?” Sammy aliuliza kwa sauti tulivu akijitahidi kuzuia hasira.

Uso wa Joyce ulikuwa bado unaonesha maumivu makubwa, alimtazama Sammy kwa kitambo na kutingisha kichwa chake taratibu huku akivuta pumzi ndefu kisha akazishusha taratibu.

“Wala hakuna chochote kibaya kinachoendelea kati yetu,” Joyce alisema kwa sauti iliyoashiria huzuni.

“Kumbe kuna nini! Kama hakuna kibaya kinachoendelea basi kuna kizuri kinaendelea, unaweza kunieleza hicho kizuri ni kipi?” Sammy aliuliza huku akiwa ameyatuliza macho yake kwenye uso wa Joyce.

“Unajua… sikuwa nimekueleza kabla kwa kuwa sikujua ni msanii gani angekubali proposal yangu, isitoshe ni msaidizi wangu ndiye niliyekuwa nimemkabidhi jukumu hilo. Kwa kifupi kuna dili huenda nikaingia na Dynamo Plus la kutangaza mavazi yangu. Leo nilipoonana naye tulipanga na kukubaliana tukutane tena kesho ili kuona namna kila mmoja wetu anaweza kufaidika na mkataba huo kabla hatujausaini,” Joyce aliongeza kwa upole kabisa huku akimtazama Sammy kwa makini.

Japo alijitahidi kujielezea vizuri mbele ya Sammy lakini uso wake ulikuwa umesawajika. Sammy alibaki kimya akimtazama kwa utulivu huku akianza kujilaumu moyoni baada ya kuona kuwa alikuwa amemfikiria vibaya mkewe.

Joyce alishusha pumzi, hamu ya kuangalia mchezo wa kuigiza wa “Gereza la Kifo” kwenye runinga ilikuwa imetoweka, hakuweza tena kuuangalia hadi kipindi kilipoisha na kingine kilikuwa mbioni kuanza. Sebule ilikuwa imegubikwa na ukimya, kila mmoja alikuwa akitafakari ya kwake.

Joyce alimsogelea Sammy, akaweka kiganja chake shavuni pa mumewe huku akimtazama kwa ukaribu. Wakatazamana. Joyce akajaribu kutabasamu lakini sura yake ilishindwa kuficha huzuni aliyokuwa nayo. Sammy aliliona hilo na kujikuta akiwa hana jinsi zaidi ya kumwomba msamaha mkewe kwa kumkwaza.

“Unajua… moyo wa mtu ni kichaka, mtu anakuwa na vitu vingi kichwani na moyoni. Sisi wanawake tunaishi katika mazingira magumu sana. Sikatai kuwa tunakumbana na vishawishi vingi na wakati mwingine mtu unashindwa ufanye nini, ila inakuwa siri yako,” Joyce aliongea kwa sauti ya kitetemeshi.

“Kwa maana hiyo, kuna wanaume wameshawahi kufanya mapenzi na wewe? Kwa hiari au kwa nguvu?” Sammy aliuliza kwa udadisi. Wivu ulianza kumsonga moyoni.

“Sijamaanisha hivyo.”

“Sawa, vyovyote iwavyo, naomba usije ukanisaliti, nitakapogundua nitaumia sana,” Sammy alisema kwa sauti tulivu iliyojaa hisia.

Joyce alitingisha kichwa taratibu na kuinamisha sura yake, hakutaka kumpa Sammy fursa ya kuona matone ya machozi yaliyoanza kumchuruzika machoni.

“Naomba uniruhusu niende kulala,” alisema na kunyanyuka bila kusubiri ruhusa, akambusu Sammy kwenye paji la uso na kuanza kupiga hatua akielekea chumbani.

“Mama Pendo, naomba ukae kidogo,” Sammy alimwambia Joyce mara alipoanza kuvuta hatua kuelekea chumbani, na bila hiyana Joyce alirudi akaketi na kuinamisha uso wake chini akijaribu kuyaficha machozi yaliyokuwa yakimtoka.

Sammy alimtazama kwa kitambo na kushusha pumzi akijaribu kujiaminisha kwamba ni yeye peke yake aliyekuwa akiyafaidi mapenzi matamu ya mkewe, ingawa hakuwa na uhakika kutokana na uzuri aliojaaliwa mkewe.

Joyce alikuwa bado amejiinamia. Sammy alitaka kusema neno lakini akasita baada ya kumwona mtangazaji Maximilian Njamba wa kipindi cha runinga cha ‘Mbunifu Wetu’ akitangaza huku akilionesha gari aina ya Cadillac DeVille lenye kibao cha “Taxi” juu yake.

Sammy alishtuka sana, aligeuza shingo yake kumtazama Joyce na kumwona akiinua uso wake, akainuka haraka na kusimama mbele yake kwa namna ya kumziba asiweze kuona kilichokuwa kinaoneshwa kwenye runinga, kisha alichukua rimoti haraka na kuzima runinga kabla Joyce hajaona.

Akamshika Joyce kwa upole na kumnyanyua taratibu kwa mahaba, lengo likiwa kumwongoza waelekee chumbani lakini akashituka sana baada ya kugundua kuwa mkewe alikuwa analia! Mwili wake ulikuwa ukitikisika kutokana na kilio cha kwikwi, alionekana alishindwa kujizuia kulia.

Joyce alipogundua kuwa Sammy ameyaona machozi yake akalipuka, alianza kulia huku akitamka maneno ambayo Sammy hakuweza kuyatafsiri, yalikuwa yamechanganyikana na kilio. Hali hiyo ilimtisha Sammy kwani haikuwahi kutokea hapo kabla. Maswali mengi yalipita ndani ya kichwa chake, akihofu huenda Joyce aligundua jambo kutoka kwake, au aliambiwa na Winifrida kuhusu kile alichokuwa amemficha.

“Dah! Hii sasa kali!” Sammy aliwaza huku akihisi ubaridi ukimtambaa mwilini.

Itaendelea...
 
Taxi - (69)

Machozi yaliendelea kumtiririka Joyce. Aliinamisha uso wake chini huku akitia huruma. Alijitupa kifuani pa mumewe na kumkumbatia. Sammy naye alimkumbatia kisha alianza kumfuta machozi kwa kiganja chake cha mkono, akambusu katika paji la uso na kukilaza kichwa chake kifuani pake.

“Nini kimekusibu, mbona hata sielewi?” Sammy aliuliza kwa wasiwasi.

Kilio cha mkewe kilipungua na sasa alionekana kuweweseka. Sammy akaanza kumbembeleza huku akimwomba radhi kama kuna jambo lolote baya alilomkwaza huku akimsihi amueleze yaliyomsibu hadi kulia kiasi kile. Joyce alikusanya nguvu ili aweze kumweleza mumewe yaliyomsibu.

“Unajua, mume wangu, ghafla nimejikuta nikiwa kwenye wakati mgumu sana…” Joyce alianza kusema kwa sauti ya chini iliyobeba huzuni na mitetemo.

“Nimejaribu sana kujizuia nisilie mbele yako lakini nimeshindwa. Naona aibu hata kukueleza…” Joyce alisema na kuanza tena kulia lakini Sammy akambembeleza.

Joyce hakuona tena sababu ya kumficha kitu mumewe japo aliona aibu sana kumweleza. Alikusanya nguvu zote na kumtazama Sammy kwa huzuni, sura yake ilikuwa imesawajika.

“Ah… wacha tu nikuambie ukweli… ni kweli nilipanga kwenda kuonana na Dynamo Plus kesho, lakini…” Joyce alisita kidogo, akashusha pumzi huku akimtazama Sammy kwa wasiwasi. Alianza kuchezea vidole vyake huku akimtazama mumewe kwa machale.

“Sema, lakini nini?” Sammy alimsaili huku hisia mbaya zikianza kumwingia.

“Naomba usinichukie kwa kusema ukweli… nilikuwa nakwenda kuisaliti ndoa yetu kama njia ya kumshawishi kupata mkataba,” Joyce alisema na kuanza kulia tena.

Sammy alishtuka sana, alihisi mwili wake ukipigwa shot ya umeme kutokana na kile alichokisikia, japo angeweza kutarajia kitu kama hicho lakini hakutegemea kusikia kutoka kwa mhusika mwenyewe. Pamoja na mshituko, alijikaza na kuuma midomo, mapigo ya moyo wake yalikuwa yakienda mbio isivyo kawaida.

Muda wote Joyce alikuwa analia kilio cha kwikwi, Sammy alikuwa anamwangalia tu bila kufanya chochote. Sura yake kaikunja kwa hasira. Joyce aliendelea kulia kwa muda, kisha akajifuta machozi kwa kutumia upande wa kanga na kupiga magoti mbele ya Sammy ili kuomba msamaha.

Sammy alimsukuma kwa nguvu na kumfanya aanguke sakafuni chali, akashangaa sana kwa tukio lile. Alimtazama Sammy kwa hofu na kujikaza, akaacha kulia na kujikusanya kutoka pale sakafuni, akasimama.

“Baba Pendo, tafadhali usikasirikie, naapa haki ya Mungu sijawahi kukusaliti, sijui shetani gani alitaka kuniingia!” Joyce alisema kwa sauti ya chini ya kusihi kisha alianza kulia tena huku akifutika kichwa chake kwenye kifua cha mumewe.

“Hivi nyie wanawake mkoje, huyo mjinga mwenye mdomo mkubwa anawapa nini hadi mnazuzuka naye kiasi hiki? Au kutaka mkataba ni lazima mjiuze?” Sammy alihoji kwa ukali huku akimmuondoa Joyce kutoka kifuani pake. Alikuwa akihema kwa nguvu kutokana na hasira.

“Sasa nini kilichokufanya uniambie ukweli wakati ulifanya siri!” Sammy aliuliza huku akimkodolea macho Joyce.

“Nisamehe, mume wangu, najua unanipenda sana na kunijali ndiyo maana nimeshindwa kujizuia kulia mbele yako. Maneno yako yamenichoma sana hadi nimejiona mpumbavu, utadhani ulikuwa umeufunua moyo wangu ukaanza kuyasoma mawazo yangu, ningekuwa na moyo wa jiwe usingegundua chochote lakini moyo wangu ni wa nyama!” Joyce alisema huku akijikunyata mbele ya Sammy akiwa na hofu, hakuwahi kumwona Sammy ameghadhabika kiasi kile.

Muda wote Sammy alibaki kimya akiwa ameyatuliza macho yake usoni kwa Joyce. Macho ya Joyce hayakuficha chochote kiovu. Alikuwa ameuweka moyo wake bayana mbele ya mumewe.

“Nisamehe sana, mume wangu, naapa siwezi kukusaliti kabisa,” Joyce alisema kwa sauti ya huzuni.

Sammy alitaka kusema neno lakini akasita, moyo wa imani ukamwingia. Alimshika mkono Joyce na kumvutia kifuani kwake, akamkumbatia kwa kitambo, kisha akamwongoza kuelekea chumbani.

* * * * *

Saa nne usiku Mr. Oduya alikuwa ameketi kwenye ofisi yake binafsi ndani ya jengo lake la kifahari la ghorofa mbili lililokuwa katika eneo la Mikocheni jirani na Rose Garden. Lilikuwa jumba kubwa lenye uwa mpana na bustani ya kupendeza.

Ndani ya jengo hilo ndimo kulikuwa na ofisi pana yenye mazingira nadhifu na yaliyovutia kwa mpangilio wa samani za kisasa, ikiwa na zulia nene jekundu la manyoya sakafuni na meza ndefu ya ofisini yenye viti kumi na vinne. Viti saba upande wa kushoto na viti vingine saba upande wa kulia.

Mr. Oduya alikuwa ameketi kwenye kiti chake kikubwa cha kuzunguka kilichokuwa na magurudumu yaliyokiwezesha kusogea akiwa nyuma ya meza yake kubwa ya kiofisi mwisho wa ofisi ile upande wa kushoto. Alikuwa ameegemea kiti chake cha kiofisi akiwasikiliza wageni wake kumi na wanne.

Wageni hao walikuwa wajumbe wa kamati maalumu ya fitna na ushindi, muda huo walikuwa katika kikao maalumu chini ya uenyekiti wa Meneja Mkuu wa Udzungwa Beach Resort, Dk. Masanja na katibu alikuwa Balozi Mageuzi. Ajenda kuu ya kikao ilikuwa kupanga mikakati jinsi ya kumsaidia Mr. Oduya kushinda kinyang’anyiro cha kusaka nafasi ya kuteuliwa na Chama Cha Ukombozi kugombea urais wa nchi.

Katika muda ule, upepo mwanana ulikuwa unavuma kutokana na mvua ya rasharasha iliyokuwa inanyesha na kuyasonga songa mapazia marefu yaliyokuwa yamefunika madirisha matatu makubwa mle ofisini. Mara simu ya mkononi ya Mr. Oduya ikaanza kuita na kumshtua. Alipoitazama kwa makini akagundua kuwa mpigaji alikuwa mwanasheria wake, Adam Mafuru.

Mr. Oduya aliminya midomo yake huku akikunja sura, aliitazama saa yake ya mkononi huku akionekana kutafakari kidogo na kushusha pumzi, alijiondoa kutoka pale kwenye kiti alipokuwa ameketi na kuwataka radhi wageni wake, akatoka na kuelekea nje ya ofisi.

Alisimama ukumbini karibu na dirisha, akayatupa macho yake kuangalia nje na kuipokea ile simu kisha akaipeleka moja kwa moja kwenye sikio lake.

Mambo yanazidi kunoga, nini kitafuta baada ya hapo? Usikose kufuatilia kisa hiki cha kusisimua...
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom