Taxi - (67)
ILIPOISHIA JANA
Sammy alishusha pumzi za ahueni huku akiyakaza macho yake kuwatazama kwa makini. Alifurahia kwa kitendo cha Joyce kurudi alikotoka lakini hakufurahishwa kwa kitendo cha kumwona akiwa na mwanamuziki Dynamo Plus. Alitamani ashuke na kwenda kuwazaba makofi lakini akajizuia sana. Kwa kweli hakujua afanye nini!
Mara simu ya Nyaso ikaanza kuita, Nyaso aliitazama kwa makini na kuipokea kisha akaipeleka moja kwa moja kwenye sikio lake.
“Nyaso, kuna jambo la muhimu sana limejitokeza, ni kuhusu ile proposal yetu hivyo natakiwa kuongea na Dynamo Plus tuone cha kufanya, wewe nenda tu ukaniwakilishe,” Joyce alisema.
“Okay, basi haina tatizo da’ Joy…” Nyaso aliitikia na kukata simu kisha akamtazama Sammy ambaye alikuwa bado anaangalia kule kwenye jengo la Nuru TV huku donge la wivu likiwa limemkaba shingoni.
“Twende Ubungo Plaza, Boss wangu amepata dharura,” Nyaso alimwambia Sammy na kujiegemeza kwenye siti.
Sammy aligeuka kumtazama Nyaso kwa makini, alitaka kumuuliza kitu lakini akasita na kushusha pumzi, kisha akaliondoa gari lake taratibu pasipo kusema kitu huku akiendelea kuangalia kule walikoelekea Joyce na Dynamo Plus.
SASA ENDELEA...
Aliendesha gari lake huku donge kavu la wivu uliochanganyika na hasira likiwa limemkaba kooni, alijisikia vibaya sana, alidhani kwamba alikuwa amemruhusu mkewe kutimiza ndoto yake kumbe alikuwa akimsogeza mbuzi karibu na chui!
Ilibaki kidogo tu apate ajali barabarani, mawazo yake yalikuwa kwa mkewe Joyce na Dynamo Plus yaliyomfanya akose umakini barabarani, kichwa chake kilikuwa kimevurugwa.
Sasa alikuwa na mgogoro wa ndani kwa ndani (interpersonal conflict), sauti moja ilimwambia arudi akamfumanie mkewe, kisha awape kipigo wote wawili, lakini sauti nyingine ilimwambia asifanye hivyo kwa kuwa hakuwa na uhakika kama walikuwa na uhusiano wa kimapenzi. Isitoshe angeweza kujiharibia kwa kuwa Joyce angegundua kuhusu siri yake ya kuendesha teksi.
“Vipi kaka, kuna tatizo lolote?” Nyaso alimuuliza Sammy akiwa ameitambua hali ya kukosa umakini iliyojitokeza baada ya kutaka kusababisha ajali kwa mara ya pili wakati wakivuka taa za kuongozea magari barabarani katika eneo la Tume ya Sayansi na Teknolojia.
Sammy alijishtukia na kumtazama Nyaso, akaachia tabasamu huku akishusha pumzi za ndani kwa ndani, “Wala hakuna tatizo,” alijibu na kuongeza mwendo akiitafuta Bamaga.
* * * * *
Saa tatu kasoro robo ya usiku iliwakuta Sammy, Joyce na Winifrida wakiwa kwenye meza ya chakula wakila kimyakimya, kila mmoja alikuwa akitafakari lake. Muda huo Pendo alikwisha kula tayari alikuwa chumbani amelala.
Muda wote wakati wa mlo Sammy alikuwa anawaza mambo mbalimbali yaliyomjia kichwani kwake. Alifikiria kuhusu mwelekeo wa biashara yake baada ya mazungumzo yake na McDonald West na kudhani kuwa muda mwafaka wa kuongeza magari mengine mawili ulikwisha fika.
Changamoto kubwa ilikuwa ni jinsi ya kupata magari mazuri na ya kipekee ambayo yangemwezesha kuukabili ushindani. Alitamani sana kupata magari kama lile alilokuwa nalo sasa. Pia aliwaza kuhusu kile alichokishuhudia kule Nuru TV, alipomwona mkewe akiwa ameongazana na mwanamuziki wa kizazi kipya, Dynamo Plus huku wameshikana mikono.
Donge la hasira lililochanganyikana na wivu lilikuwa bado limemkaba kooni kwake. Lakini pamoja na mawazo kumwandama, chakula kilishuka vilivyo kutokana na ustadi wa mapishi ya mkewe. Hata hivyo, muda wote Joyce hakujua kilichokuwa kikiendelea kwenye akili ya mumewe, yeye alifurahia chakula alichopika mwenyewe.
Winifrida alikuwa mtulivu sana muda wote wa chakula tofauti kabisa na kawaida yake, alimtazama Sammy kwa jicho la kuibia huku akionekana kuwa mbali kimawazo. Alikuwa akijaribu kulinganisha maisha ya kaka yake Sammy na kile alichokishuhudia kwenye video ya mauaji na kuzidi kuchanganyikiwa.
Walimaliza kula na Winifrida akatoa vyombo, kisha walishushia matunda na baadaye maji, halafu Winifrida aliwaacha akaingia chumbani kwake kujipumzisha.
Sammy na Joyce walikwenda kuketi sebuleni kwenye masofa kila mmoja akiwa na kijiti mdomoni akijaribu kuondoa masalio ya nyama pamoja na masalio mengine kwenye meno. Waliketi pale kwani Joyce alitaka kufuatilia mfululizo wa mchezo wa kuigiza wa “Gereza la Kifo” uliorushwa kwenye runinga.
Hata hivyo, mawazo ya Sammy hayakuwa kwenye runinga, alikuwa anapanga jinsi ya kumuuliza mkewe kuhusu uhusiano wake na mwanamuziki Dynamo Plus.
Hakutaka kukurupuka kwani angeweza hata kujichongea endapo mkewe angegundua kuwa ile teksi iliyokusudiwa kumchukua na kumpeleka Ubungo Plaza ni gari la mumewe Sammy, na hata aliyekuwa akiendesha teksi ile hakuwa mwingine zaidi ya mumewe mwenyewe.
Ni dhahiri uso wa Sammy haukuonesha furaha ingawa alijitahidi kuwa na furaha mbele ya Joyce.
Joyce aliligundua jambo hilo baada ya kumtupia jicho mara kwa mara, alijaribu kuivumilia hali ile lakini alishindwa na kuamua kuvunja ukimya.
“Naona leo ni kama huna furaha, nini kimekukera, mume wangu?” Joyce aliuliza kwa sauti tulivu huku akiyatuliza macho yake kwenye uso wa Sammy, alimwangalia kwa makini.
Sammy alimtazama mkewe na kujaribu kutabasamu lakini bado alishindwa kuficha wivu na hasira. Alipumua kwa nguvu, na kujiegemeza kichovu kwenye sofa huku akimtazama mkewe kwa umakini. Wivu na udadisi vilimsonga kwa pamoja. Alihisi labda mkewe alishampa ‘tunda’ Dynamo Plus au mwanaume mwingine. Donge la hasira na wivu lilizidi kumkaba kooni.
Joyce alipinda midomo yake upande wa kushoto na kushusha pumzi ndefu kama aliyemaliza mbio ndefu.
“Unajua, kwa siku za karibuni, hasa siku hizi mbili nimeona umebadilika kwa kiasi fulani tofauti na kawaida yako, sijajua tatizo ni nini hasa!” Joyce alisema huku akiminya midomo yake kisha akashusha pumzi.
“Inawezekana nikawa na mabadiliko lakini ni kwa sababu nakupenda sana. Mwenyewe unajua jinsi tulivyoanza uhusiano wetu hadi kufunga ndoa…” Sammy alisema na kusita kidogo, akavuta pumzi ndefu kisha akazishusha taratibu akionekana kutafakari kwa sekunde kadhaa kabla hajayahamishia macho yake kumtazama tena Joyce ambaye muda huo alikuwa kimya akimtazama kwa makini.
“Nimekuruhusu kwa moyo mmoja kwenda kwa Madame Norah ili uweze kutimiza ndoto yako ya siku nyingi, ila nadhani uhuru niliokupa unaweza kuniumiza siku moja…” Sammy alianza kufunguka lakini Joyce alimkatisha kwa upole huku akionekana kushtuka kidogo.
“Kwa nini unasema hivyo, kwani umeona nini kutoka kwangu?” Joyce aliuliza huku uso wake ukionesha mshtuko wake.
“Hapa si suala la nimeona nini kwako bali unapaswa kutambua kuwa wewe ni mke wangu wa ndoa, ni mimi mwenye haki ya kuushika na kuutomasa huo mwili wako. Nakuomba jichunge sana usije kurubuniwa na wasanii na baadaye ukanisaliti kisa unatimiza ndoto…” Sammy alisema huku akijizuia kukasirika.
Inaendelea...