Laiti Ningejua! 1
Mtunzi Bishop Hiluka
HII haikuwa mara yangu ya kwanza kufika wilaya ya Rufiji hususan katika mji wa Ikwiriri, mji mdogo uliopo kusini kwa Dar es Salaam katika Mkoa wa Pwani. Nilikuwa nimefika hapo Ikwiriri mara moja na hii ilikuwa ni mara yangu ya pili.
Kwa kiasi fulani sikuwa mgeni kabisa wa mazingira ya Ikwiriri ingawa mara ya kwanza nilipokwenda katika mji ule sikukaa kwa zaidi ya siku tatu. Kama ilivyokuwa mara ya kwanza, safari hii tena nilipokwenda katika mji wa Ikwiriri nilikuwa pale kibiashara na nilifikia nyumbani kwa rafiki yangu, Amir Ngwali, aliyekuwa anaishi Barabara ya Mtunda nje kidogo ya mji wa Ikwiriri.
Kama kawaida yangu, siku ile pia nilikuwa katika mwonekano wa kileo zaidi nikiwa nimevaa suruali ya jeans ya rangi nyeusi, buti ngumu za ngozi miguuni, shati maridadi la rangi ya samawati aina ya Levi’s nililokuwa nimelichomekea vizuri kiunoni, saa ya mkononi aina ya Seiko na kofia nyeusi ya kapelo.
Kwa ujumla nilikuwa mtanashati niliyejipenda mno kuanzia ndani ya chumba changu hadi mwili wangu, ilikuwa ni nadra sana kunifumania nikiwa nimerudia kuvaa nguo niliyoivaa jana yake.
Nikiwa katika umri wa miaka therathini nilikuwa mrefu na maji ya kunde mwenye umbo la kimichezo, nilikuwa mcheshi sana na mtu wa kujichanganya na watu wengine.
Sikuwa mbumbumbu, nilikuwa nina elimu nzuri tu ya biashara, kwani nilihitimu shahada ya kwanza ya Biashara katika Masoko (B.Com. in Marketing) kutoka katika Shule ya Biashara ya Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDBS), miaka mitano iliyokuwa imepita.
Baada tu ya kumaliza masomo yangu ya biashara pale Chuo Kikuu cha Dar es Salaam nilizunguka kutafuta ajira lakini baadaye nikaamua kujiajiri mwenyewe baada ya kuona mshahara niliokuwa nikitajiwa ulikuwa hauendani na matarajio yangu.
Kimsingi niliamua kuwa mtu wa dili au ukipenda unaweza kuniita ‘mishen tauni’, na ili kufanikiwa zaidi katika dili zangu niliamua kuwa mtu wa kujichanganya sana.
Tabia yangu ya kujichanganya na watu wa aina mbalimbali kwenye dili ambazo zingine wala hazikuhitaji kisomo na bila kujali elimu yangu, kwa kiasi fulani zilinifanya nianze kupata mafanikio makubwa kimaisha na kufanya watu walionifahamu kunipachika jina la utani la ‘the Jackal of all trades’, yaani dalali wa biashara zote.
Nilifanikiwa kufungua ofisi yangu ya udalali na ushauri wa biashara iliyokuwa katika eneo la Buguruni Rozana, na nilikuwa nimeajiri watu sita, mimi nikiwa ndiye mkurugenzi mtendaji wa kampuni.
Pia nilikuwa nimejenga nyumba kubwa ya kisasa iliyokuwa nje ya jiji la Dar es Salaam, katika eneo la Zingiziwa, Chanika na pia nilimiliki viwanja viwili vitatu katika maeneo tofauti jijini Dar es Salaam.
Katika maisha yangu ua utafutaji, sikupenda kabisa kujihusisha na wasichana ndiyo maana ilikuwa vigumu sana kunikuta na msichana. Lakini kwa vile binadamu hawana dogo wakaanza kusema eti huenda nilikuwa na matatizo mwilini mwangu, ndiyo maana nilikuwa naishi peke yangu licha ya kuwa na uwezo na pia kushobokewa na warembo.
Wakati najiandaa kuondoka pale nyumbani kwa Amir nikiwa mbioni kurudi jijini Dar es Salaam yalipo makazi yangu, ilikuwa yapata saa nne asubuhi, Amir na mke wake, Mwanamvua Mbonde walinisindikiza huku wakilalamika kuwa nimekuwa nikifika Ikwiriri na kukaa siku moja au mbili tu kisha naondoka, walitamani siku nyingine nikae pale kwa zaidi ya wiki.
Pia Mwanamvua alikuwa haachi kulalamika akitaka amuone mke mwenzake, kwa maana nyingine ni kwamba alikuwa akinisisitiza nioe ili washerehekee harusi yangu kabla ujana haujaisha maana sasa nilianza kuelekea kwenye utu uzima.
Tulipotoka nje ya nyumba ya Amir nikawaona watu wawili-watatu wa bodaboda waliokuwa wameegesha pikipiki zao chini ya mti mkubwa kando ya ile barabara iliyokuwa ikielekea Mtunda, na walikuwa umbali wa kama mita hamsini hivi kutoka katika ile nyumba ya Amir.
Katika umbali ule dereva mmoja wa bodaboda mjanja akaniwahi haraka kabla ya wenzake hawajashtuka baada ya kuhisi hitaji langu. Aliponiona tu alipiga honi huku akiniashiria nipande ile bodaboda, na kama vile haitoshi aliiwasha bodaboda yake haraka na kunifuata pale pale nje ya nyumba ya Amir tulipokuwa tumesimama.
Kwa mwonekano tu yule dereva wa bodaboda alikuwa ni mtu mzima aliyekadiriwa kuwa na umri usiopungua miaka arobaini na tano. Alikuwa mrefu na mwembamba mwenye sura ya ucheshi na alikuwa amevaa shati la bluu na jaketi jeusi, suruali ya kijivu na raba miguuni.
Alitusalimia kwa bashasha huku akionekana kutaniana na Amir, kisha nikapanda kwenye ile bodaboda pasipo hata kusubiri. Mara tu nilipopanda kwenye ile bodaboda yule dereva wa bodaboda akanisemesha kwa lugha ya Kindengereko na alipoona kuwa sielekei kumuelewa aliamua kubadili lugha na kunisemesha kwa Kiswahili.
“Kwani wewe si mtu wa hapa Ikwiriri?” yule dereva wa bodaboda akaniuliza kwa mshangao.
“Mimi siyo Mndengereko, mimi ni mtu wa Kigoma,” niliongea kwa utulivu huku nikimtazama kwa makini.
“Oh! Kumbe wewe ni Muha wa Kigoma? Karibu sana Ikwiriri. Mimi ni Mndengereko al-watan hapa Ikwiriri. Hakuna asiyenifahamu hata ukimuuliza mtoto mdogo tu atakwambia anamjua Kindeka mzee wa mabodaboda ni nani, au siyo Amir?” alisema yule dereva wa bodaboda kwa tambo nyingi huku akigeuza shingo yake kumtazama Amir na kuachia kicheko hafifu.
Amir na mke wake pia walicheka kicheko hafifu bila kusema neno. Mimi nilibaki kumtazama tu yule yule dereva wa bodaboda kwa makini huku nikiachia tabasamu laini ambalo baadaye likageuka kicheko hafifu.
“Lakini si kila mtu anayetoka Kigoma ni Muha, yapo pia makabila mengine kama Wabembe, Watongwe, Wamanyema…” nilimwambia yule dereva wa bodaboda, ambaye sasa nililifahamu jina lake kuwa aliitwa Kindeka.
“Kumbe!” akadakia yule dereva wa bodaboda kabla hata sijamaliza maelezo yangu huku akionekana kushangaa sana.
“Ndiyo, si hao tu, pia utawakuta Wanyamwezi, Wasukuma, Wafipa na watu wenye asili ya Congo, Rwanda na Burundi,” nikazidi kumweleza yule dereva wa bodaboda na kuzidi kumshangaza.
“Ooh, kwa hiyo wewe ni kabila gani?” aliniuliza yule dereva bodaboda huku akigeuza shingo yake kunitazama usoni kwa shauku kubwa ya kutaka kujua.
“Mimi ni Mmanyema ingawa siwezi kuzungumza lugha ya Kimanyema kwa sababu nimekulia jijini Dar es Salaam.”
Maelezo yangu yakamfanya yule dereva wa bodaboda ageuke kabisa na kunitazama usoni kwa makini kisha akaangua kicheko hafifu kabla kuniambia.
“Sishangai kwa nini vijana wengi wa zama hizi hawajui kuzungumza lugha zao za asili, wengi wanadhani labda ni ushamba au labda ni kutokwenda shule,” alisema yule dereva wa bodaboda huku akiangua tena kicheko.
Maelezo yale yakatufanya watu wote kwa pamoja tuangue kicheko cha katikati ya maongezi na kabla kicheko kile hakijafika ukomo wake, yule dereva wa bodaboda akageuka tena na kuniuliza, “Lakini bado hujaniambia tunaelekea wapi, Bosi?”
“Nipeleke stendi ya mabasi ya kuelekea jijini Dar es Salaam,” nilimjibu yule dereva wa bodaboda kwa utulivu huku nikiwa nimekwisha kaa vizuri na begi langu nikiwa nimelivaa mgongoni.
“Ooh, kumbe unaelekea Bongo? Nilisahau kama umeniambia unakaa Dar es Salaam!” akasema yule dereva wa bodaboda na kuangua tena kicheko hafifu na kuongeza, “Au kwa sasa unaishi hapa kwetu Ikwiriri?”
“Hapana, bado naishi Dar es Salaam, Ikwiriri nakuja kutembea tu mara moja moja,” nilimjibu yule dereva wa bodaboda kisha nikawaaga wenyeji wangu, Amir na mkewe kwa bashasha zote.
Kitambo kifupi cha ukimya kikafuatia wakati yule dereva wa bodaboda akiiondoa ile bodaboda kutoka pale kwenye nyumba ya Amir. Hakuwa na mbwembwe kama ilivyokuwa kwa vijana wengi waliokuwa wakiendesha bodaboda kupenda kupiga lesi.
Itaendelea...