HEKAHEKA! 14
Na Bishop Hiluka
Wakati tukiendelea na safari nilitamani sana kujua tulikokuwa tukielekea lakini sikuweza. Nilianza kujilaumu sana kwa kutomsikiliza Susan, niliamini kuwa alikuwa na maono aliponitaka niahirishe safari yangu lakini nikakataa.
Nikajikuta nikiilaumu sana siku hiyo ambayo ilikuwa ya hekaheka sana kwangu, maana katika kipindi cha saa kumi na mbili tu tayari nilikuwa nimekwishapata jambajamba mara mbili kwenye viwanja vya ndege viwili tofauti!
Maana kabla ya mkasa huu wa uwanja wa ndege wa kimataifa wa Julius Nyerere jijini Dar es Salaam, nilikuwa nimepatwa na mkasa uliofanana na huo katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Schiphol jijini Amsterdam, katika siku hiyo hiyo moja ya safari! Kwa kweli siku hiyo ilikuwa ni siku ya hekaheka!
Alfajiri ya siku ile nikiwa na Susan na binti yetu, Pamela aliyekuwa na miaka minne, tulitoka nyumbani kwetu Stadsdeel Nieuw-West jijini Amsterdam na kuelekea katika Kiwanja cha Ndege cha Kimataifa cha Schiphol.
Tulifika pale uwanja wa ndege asubuhi ya saa kumi na mbili kasoro dakika ishirini, ikiwa ni dakika hamsini kabla ndege niliyotarajia kusafiria nayo haijaruka.
Kiwanja cha Ndege cha Kimataifa cha Schiphol jijini Amsterdam, ambacho jina lake kamili kwa Kiholanzi kikiitwa Luchthaven Schiphol, kilikuwa kiwanja kikubwa sana cha kisasa kikiwa kati ya viwanja vya ndege vikubwa duniani chenye kupokea abiria zaidi ya milioni 46 kwa mwaka, idadi iliyokifanya kushika nafasi ya tatu barani Ulaya na nafasi ya 12 duniani.
Kiwanja hicho cha ndege kipo kilomita 9 kusini magharibi ya Amsterdam katika manispaa ya Haarlemmermeer kikiwa na kituo (terminal) kikubwa kimoja kilichokuwa kimegawanywa katika vituo vikubwa vitatu vya kuondokea (Departure Halls).
Tulifika pale uwanjani tukaingia moja kwa moja katika eneo la chini la Departure Hall 2 kwenye geti namba E-10 na haraka haraka nilikaanza mchakato wa kukamilisha taratibu zote za uhamiaji pale uwanja wa ndege kabla ya kuondoka.
Niliwaacha Susan na Pamela wakilinda mizigo yangu nikapanga foleni kwenye dirisha la ofisi ya uhamiaji pale uwanjani kisha nikapenyeza vibali vyangu vyote vya kusafiria kwenye dirisha dogo la kioo la chumba kilichomhifadhi msichana mmoja mlimbwende aliyekuwa na sura ya uchangamfu.
Msichana yule ofisa uhamiaji akavipokea vibali vyangu vya kusafiria huku akiliachia tabasamu lake maridhawa na kulifanya lizisumbue fikra zangu.
Japo mchumba wangu Susan alikuwa mrembo kwelikweli lakini nilikuwa mgonjwa kwa walimbwende kama huyu na sikuwa nikiridhika, nilimtamani kila msichana mrembo niliyemuona mbele yangu.
Mambo yote yalikuwa chapuchapu kwani yule ofisa uhamiaji alimaliza haraka kuingiza taarifa zangu kwenye kompyuta yake kisha akagonga mhuri kwenye hati yangu ya kusafiria na hivyo safari yangu kuelekea nchini Tanzania ikawa imeidhinishwa rasmi.
Bila kupoteza muda nikaipokea pasi yangu ya kusafiria na kuitia mfukoni huku tabasamu langu la kichokozi likichomoza na kuzisumbua vibaya hisia za yule ofisa uhamiaji.
Kisha nikanyoosha mkono wangu kumpa, wakati tukipeana mkono wa kuagana na yule ofisa uhamiaji nikapitisha kidole changu cha shahada katikati ya kiganja chake kumtekenya, kitendo kile kikamfanya yule ofisa uhamiaji ashtuke na kuruka huku akiutoa haraka mkono wake kutoka kwenye kiganja changu.
Sikuishia hapo, nikamkonyeza kidogo kumchombeza lakini nikihakikisha Susan haoni kitendo kile. Nikashukuru kuwa Susan alikuwa hajashtukia mchezo ule vinginevyo kwa jinsi nilivyokuwa namfahamu Susan, kwa vyovyote moto ungewaka palepale.
Wakati yule ofisa uhamiaji akiwa bado ana mshangao usoni kwake nikamnong’oneza kuwa siku nikirudi Amsterdam nitamtafuta, kisha nikanza kuzitupa hatua zangu kwa utulivu kuliacha eneo lile.
Yule ofisa wa uhamiaji hakujibu bali alibaki ameduwaa huku macho yake yakinisindikiza nyuma yangu hadi pale nilipopotea mbele ya macho yake.
Kwa kusaidiwa na mchumba wangu Susan tulichukua mizigo yangu na kwenda kupanga foleni kwa ajili ya ukaguzi wa mizigo.
Wakati zamu yangu ikikaribia mara nikahisi mchafuko mbaya wa tumbo huku dalili za kuendesha zikiibuka. Katika hali ile nilijikuta nikihitaji sana kukimbilia maliwatoni hivyo nilikuwa natweta huku jasho likinitoka.
Kutokana na hali ile ya kubabaika, ofisa mmoja wa usalama wa eneo lile aliniona akanishtukia kisha alituchukua kando mimi na Susan kwa ajili ya upekuzi zaidi wa mizigo yetu.
Na baada ya kufanya upekuzi wa mizigo yangu katika kila eneo yule ofisa usalama aliomba usaidizi wa kupata ofisa mwingine ili kufanya upekuzi zaidi.
Wakati tukimsubiri ofisa usalama mwingine afike ndipo nikafanya kosa kubwa kwa kumwambia yule ofisa usalama kuwa nilihitaji sana kwenda maliwato kwa kuwa nilikabiliwa na mchafuko wa tumbo.
Yule ofisa usalama alinitazama kwa makini zaidi kisha akaniuliza ikiwa nilikuwa nimekula au kunywa chochote kibaya usiku wa kuamkia alfajiri ile nami nilimjibu kuwa sikuwa nimekula wala kunywa chochote kibaya.
Aliniuliza tena ikiwa nilimhitaji daktari wa kunichunguza tumbo langu ili kujua kilichokuwa kikinisumbua, nikasema nilikuwa sawa, bali nilichohitaji ilikuwa kwenda maliwatoni tu.
Yule ofisa usalama alinitazama katika mtizamo ambao baadaye niligundua kuwa hatukuwa tumeelewana kuhusu kilichokuwa kikinisumbua. Yule ofisa usalama alisisitiza kuwa mchafuko wa tumbo langu ulisababishwa na kumeza mihadarati niliyokuwa nikijaribu kuisafirisha.
Kwa kuwa hali ya mchafuko wa tumbo ilinifanya kutweta na jasho jingi kunitoka, yule ofisa usalama hakutaka kunipa nafasi ya kutoroka kutoka eneo lile wala kwenda maliwato.
Nilijaribu kumwelewesha lakini hakutaka kunielewa na mara nikawaona maofisa wengine wawili wa usalama wakifika eneo lile wakiwa na mbwa, na wakatuchukua mimi na familia yangu hadi kwenye kibanda maalumu cha walinzi wa uwanja ule na hapo tukasubiri ukaguzi zaidi wa mizigo yetu kwa kutumia mashine maalumu.
Baada ya ukaguzi nikachukuliwa tena hadi kwenye chumba maalumu cha mahojiano, ambako ofisa wa polisi alijaribu kuligusagusa tumbo langu wakati akiniuliza maswali kama nimeshawahi kusumbuliwa na tatizo la aina ile na kama kuna dawa zozote maalumu nilizozoea kutumia nilipotokewa na tatizo kama lile.
Nilimweleza kuwa “bila shaka huwa nakunywa Imodium, lakini sijanywa leo.”
Yule ofisa wa usalama aliniambia kuwa, nilipaswa kuwa na subira wakati tukimsubiri daktari ili anifanye uchunguzi wa tumbo langu.
Nilijaribu kumwelezea kuwa shida yangu haikuwa kumwona daktari bali nilihitaji huduma ya maliwato, lakini haikuwa rahisi kuniruhusu muda ule.
Tulisubiri pale kwa dakika kadhaa, mchumba wangu Susan na mwanetu Pamela walikuwa wanalia kilio cha kwikwi; wale maofisa wa polisi walionekana kucheka kwa dharau na kutusanifu. Hatimaye mtu mmoja alifika ili kunifanyia uchunguzi lakini niligundua kuwa hakuwa daktari bali ni ofisa usalama.
Niliamua kumuuliza yule ofisa usalama kuhusu uwezo wake wa kidaktari lakini niliambiwa kuwa sikuwa na uchaguzi mwingine bali kuwasikiliza. Niliondoka nikiongozana na yule ofisa usalama.
Tulifika kwenye mlango mmoja na kusimama, hapo yule ofisa usalama akanionesha kwa kidole huku akiniambia kuwa niingine maana kile kilikuwa chumba cha maliwato.
“Dah, hatimaye ninapata nafasi ya kujisaidia!” nikawaza kwa furaha.
Nilipoingia ndani ya kile chumba, yule ofisa usalama pia akaingia akinifuata. Nikiwa mle ndani nikagundua kuwa kile chumba kilikuwa ni choo maalumu cha kutolea dawa za kulevya kwa njia ya haja kubwa kama nilichokuja kukikuta katika uwanja wa Julius Nyerere jijini Dar es Salaam.
Nilibaki nimeshangaa nikimtazama yule ofisa usalama lakini yeye aliniambia kuwa alikuwa anataka kushuhudia iwapo nilikuwa nasema ukweli au la! Na aliniambia kuwa iwapo nilitaka kujisaidia mbele yake hakuwa na shida.
Wakati nikitaka kumwomba anipishe kwa muda ili nijisaidie kwa uhuru zaidi nilijikuta nikishindwa kuhimili zaidi mchafuko wa lile tumbo, hivyo sikujali tena kama alikuwa akinishuhudia. Nilishusha haraka suruali yangu, nikaachia mzigo nikimwaga haja kama maji huku nikipiga mabomu ya kutosha.
Itaendelea...