Stori ya kijasusi - HEKAHEKA!

Stori ya kijasusi - HEKAHEKA!

HEKAHEKA! 9

Na Bishop Hiluka

Hata hivyo, ilikuwa ni mara yangu ya kwanza kuona choo kama kile. Kilikuwa ni choo cha aluminium na kilikuwa tofauti kabisa na vyoo vingine vya pale uwanjani, hiki kilikuwa cha aina yake, kisafi sana kiasi kwamba mtu ungeweza hata kutengewa chakula na ukala bila ya kuhisi kinyaa.

Nilitegemea kuwa baada ya kukosa dawa za kulevya katika mizigo yangu wangenirejeshea uhuru wangu na kuniachia niende zangu nyumbani. Lakini haikuwa hivyo.

Walinirudisha tena kwenye kile chumba cha mahojiano. Sasa wakaacha habari za dawa za kulevya, wakahamia katika masuala ya uhalifu na vikundi vya kigaidi. Hapo nikashangaa sana!

Je, nini kitaendelea?...

“Tueleze, washirikia wenzako wako wapi na silaha mlizopora ili kutekeleza mipango yenu haramu mmezificha wapi?” yule ofisa mkuu wa usalama aliniuliza mara tu nilipoketi kwenye kiti mbele yake.

“Sifahamu chochote kuhusu silaha wala mipango haramu kama unavyosema,” nikamjibu yule ofisa mkuu wa usalama nikionesha kuchoshwa na maswali yao.

Yule ofisa usalama alinitazama kwa makini zaidi kisha akaongea kwa msisitizo huku akiendelea kunitazama.

“Nimekwishakuonya kuwa huwa siwavumilii kabisa waongo, elewa mimi ni mtu mwema sana lakini siyo mpumbavu kama unavyodhani, tumeelewana?”

“Nimekuelewa lakini mimi sifahamu chochote kuhusu uhalifu wala silaha unazosema na sina washirika wowote katika uhalifu,” nikaongea kwa msisitizo.

“Tuambie wenzako wako wapi na silaha mlizopora mmezificha wapi?” akazidi kuniuliza kwa kusisitiza.

“Wenzangu akina nani?”

“Wenzako ulioshirikiana nao kuvamia bohari kuu ya silaha na kupora silaha ili kufanya matukio ya ugaidi hapa nchini, tunajua mna mtandao mpana na wewe ndiye kiongozi wa ugaidi huu!”

“Kwa kweli sifahamu chochote kuhusu huo mtandao wa uhalifu unaosema wala hizo silaha.”

“Mmezificha wapi?” sasa yule ofisa mkuu wa usalama aliongea kwa sauti kali huku akianza kushindwa kudhibiti hasira zake.

“Kwa jinsi ninavyopenda amani kama ningekuwa na taarifa zozote kuhusu uhalifu mnaonituhumu nadhani nisingeshindwa kuwapa taarifa hizo,” nikajitetea huku nikiwa nimechanganyikiwa.

Yule ofisa usalama alinipuuza, badala yake akaruhusu tabasamu la kifedhuli kuchanua usoni kwake, kisha nikamuona akimpa ishara fulani kwa kichwa ofisa mmoja wa usalama aliyekuwa amesimama kando, ishara ambayo sikufahamu maana yake.

Na hapo yule ofisa usalama aliyepewa ishara ile akaondoka haraka na kufungua mlango kisha akatoka ndani ya chumba kile akielekea nisikokujua.

Wakati huo huo nikamuona yule ofisa mkuu wa usalama akiinuka na kuanza kupiga hatua taratibu kunisogelea huku akiwa amekunja uso wake na kutengeneza matuta usoni.

Nilimtazama kwa wasiwasi wakati akizidi kunisogelea huku nikiwa sijui anataka kufanya nini. Nilitamani kuinuka na kutimua mbio lakini sikuweza, hivyo nilisubiri kuona mwisho wake.

“Ni vyema ukasema ukweli vinginevyo utapata mateso makali sana, maana tunachohitaji ni taarifa zote muhimu kabla ya hii nchi haijaangukia kwenye machafuko,” yule ofisa usalama akaninong’oneza sikioni maneno yaliyonishtua sana.

Kisha akasimama na kunitazama kwa kitambo huku akiuma mdomo wake wa chini. Nilibaki kimya nikiwa nimemtumbulia macho maana sikujua nimjibu nini.

“Hivi unadhani tumekuleta hapa ili kupiga stori au kupoteza muda wetu!” yule ofisa mkuu wa usalama akanionya na kisha muda uleule alianza kupiga hatua taratibu kurudi kule alikotoka na kuketi kwenye kiti chake huku akinitazama kwa hasira.

“Pengine bado hujaelewa vizuri uzito wa jambo hili lililosababisha vifo vya askari wetu na wananchi wasio na hatia, na kwanini wewe upo hapa…” alisema yule ofisa na kuongeza.

“Kwa akili yako ulidhani kusafiri nje ya nchi kila unapokuwa umeandaa matukio ya uhalifu ili yatokee wakati wewe uko nje ya nchi tusingeweza kubaini kama wewe ndiye uliye nyuma ya mipango hii?” yule ofisa mkuu wa usalama akaniuliza huku akiendelea kutabasamu.

Sikujibu kitu bali nilibaki nikimtazama kwa mshangao huku hasira ikiwa imenikaba kooni. Sikujua kwanini nilikuwa nikiulizwa maswali ambayo kwa kweli sikuwa na majibu yake!

Muda huo huo ule mlango ukafunguliwa kisha yule ofisa usalama akaingia akiwa ameongozana na mwanamke mmoja mrefu kiasi aliyevaa gauni fupi jepesi la rangi ya pinki na mtandio mwepesi huku ndani ya lile gauni akiwa amevaa suruali ya jeans ya rangi ya bluu.

Yule mwanamke alifika na kusimama mbele yangu, na hapo nikainua uso wangu kumtazama usoni, haikunichukua muda mrefu kumtambua.

Alikuwa ni yule mwanamke chotara mwenye mtoto niliyesafiri naye kutoka Nairobi hadi Dar es Salaam. Lakini safari hii hakuwa na mtoto wake wala mizigo.

Yule mwanamke alinitazama kwa makini huku chuki ya waziwazi dhidi yangu ikijionesha kwenye macho yake wakati akinitazama.

“Unamfahamu huyo mwanamke aliyeko mbele yako?” yule ofisa mkuu wa usalama akaniuliza kwa udadisi.

“Hapana, simfahamu kabisa,” nikajibu huku nikitingisha kichwa changu kukataa.

“Una uhakika kuwa humfahamu?” aliniuliza tena huku akiwa amenikazia macho.

“Kweli simfahamu na sina sababu ya kuongopa,” nikamjibu yule ofisa usalama kwa kujiamini.

“Mbona yeye anakufahamu?”

“Hilo mimi sijui, labda muulizeni ananifahamu kivipi, ila kitu pekee ninachojua ni kwamba tumesafiri wote kwenye ndege moja ya KLM ingawa yeye alipandia Nairobi, basi!” nikajibu kwa hakika, hata hivyo jibu langu lilionesha halikunisaidia.

“Babra…” yule ofisa usalama akamwita yule mwanamke chotara.

“Abee!” yule mwanamke chotara ambaye sasa nilimtambua kwa jina la Babra aliitika kwa unyenyekevu huku akiyaondoa macho yake kutoka kwangu na kuyahamishia kwa yule ofisa usalama aliyemwita.

“Unamfahamu huyu mtu aliyeketi mbele yako?”

“Ndiyo namfahamu,” alijibu Babra kwa kujiamini huku akiyarudisha macho yake kwangu.

“Unaweza kutuleza unamfahamu kivipi?” yule ofisa usalama akamwuliza Babra kwa sauti tulivu.

“Namfahamu kama shemeji yangu, anaitwa Brown Senga ingawa yeye anataka watu wamwite Godwin Sengerema, na alikuwa anaishi na mdogo wangu Jasmine ambaye walikutana miaka sita iliyopita,” alianza kuelezea Babra huku akinitazama kwa chuki.

“Enhe, endelea kutuelezea jinsi unavyomfahamu,” yule ofisa usalama akasema huku akibetua kichwa chake.

“Niseme tu kuwa mwanzoni nilimuona ni mtu mchesi, mstaarabu na mwema sana kwani alionesha kumpenda sana mdogo wangu Jasmine ingawa nilimuona kuwa alikuwa na wivu sana kwa Jasmine, hivyo kila wakati alimpapatikia na alikuwa tayari kumtimizia chochote alichokitaka…” alinyamaza na muda huo nilimuona akimeza funda la mate kutowesha koo lake.

“Lakini kilichonishangaza ni kuwa alikuwa akikwepa sana kuongelea mambo yaliyohusu familia yake na wala hakupenda kupiga picha huku akisisitiza kuwa uhusiano wake na Jasmine usiwe wa wazi na ujulikane na watu wachache sana akidai kuwa hakutaka kumwingiza Jasmine katika hatari. Nilishangaa na nilikuwa nikimuuliza sana kuhusu kazi aliyokuwa akiifanya, maana nilimfahamu kama mfanyabiashara wa madini, hivyo niliuliza biashara hiyo ilihusianaje na kumuingiza Jasmine katika hatari, lakini Brown hakupenda sana kuongelea mambo ya kazi yake, na ilionekana kuwa hata Jasmine alikuwa akikubaliana naye kwa kila kitu!

“Alikuwa mtu wa safari nyingi sana na za ghafla na siku zote alikuwa na marafiki tofauti ambao sikuwa nikiwaelewa. Nikamshawishi Jasmine kuwa makini na amchunguze taratibu kabla hajaamua kuishi naye ili kufahamu zaidi undani wake na awafahamu wazazi wake na jamaa zake, lakini Brown aligundua na kumtaka Jasmine asipende kunisikiliza mimi kwani nilikuwa nataka kumpotosha, ili mradi wao walikuwa wanampenda sana na alimtimizia kila kitu bila ya matatizo yoyote hakukuwa na haja ya kuchunguzana.

“Siku moja nilikwenda kuwatembelea walipokuwa wanakaa, Brown alikuwa ametoka, nikamkuta Jasmine akifanya usafi chumbani kwake huku akipekua kila sehemu na kuiona bunduki aina ya SMG iliyokuwa imefichwa mahala fulani ndani ya kabati la ukutani. Jasmine alinionesha na sote tulishikwa na wasiwasi sana kwani tulianza kuhisi kuwa Brown alikuwa akijishughulisha na vitendo vya uhalifu. Jioni aliporudi kutoka kazini Jasmine alimuuliza kuhusu ile bunduki na Brown alimuelezea kuwa yeye kama mfanyabiashara mkubwa wa madini alipaswa kuwa na silaha kama ile kujilinda, kwani huko migodini wanakumbana na watu wa kila aina na kumuonya Jasmine kuwa asiitoe siri ile kwa mtu yeyote.”

“Lakini pia alipoona mimi ninazidi kuwa na mashaka naye waliamua kuhama walipokuwa wakiishi na kuhamia sehemu nyingine ambayo sikuijua na wakaamua kubadilisha namba zao za simu, na ninahisi pia alimkataza Jasmine asiwasiliane na mimi, na kwa kuwa alimpenda sana Brown akamsikiliza. Sikutaka kujishughulisha nao na kwa muda huo mimi na mume wangu tukawa kwenye pilika pilika za kuhamia jijini Nairobi nchini Kenya.

Itaendelea...
 
HEKAHEKA! 10

Na Bishop Hiluka

“Lakini pia alipoona mimi ninazidi kuwa na mashaka naye waliamua kuhama walipokuwa wakiishi na kuhamia sehemu nyingine ambayo sikuijua na wakaamua kubadilisha namba zao za simu, na ninahisi pia alimkataza Jasmine asiwasiliane na mimi, na kwa kuwa alimpenda sana Brown akamsikiliza. Sikutaka kujishughulisha nao na kwa muda huo mimi na mume wangu tukawa kwenye pilika pilika za kuhamia jijini Nairobi nchini Kenya.

“Lakini kwa muda mfupi niliomfahamu Brown niligundua kwamba alikuwa ni mtu wa mambo mengi na marafiki wengi sana, walioonekana wana nyazifa tofauti wakiwemo wanajeshi, waliokuwa wakifika pale nyumbani kwake mara kwa mara lakini kwa uficho na kila walipofika walitumia muda mrefu na Brown wakiwa peke yao maktaba wakijadili mambo fulani waliyoyajua wenyewe. Na kwa kuwatazama tu usingeshindwa kugundua kuwa wote waliokuwa wakifika pale walikuwa na tabia zinazofanana, wacheshi, wakarimu na marafiki wazuri kama alivyo Brown,” Babra alinyamaza kidogo, akayahamisha macho yake kutoka kwangu na kutazama kando huku akionekana kuwaza mbali sana.

“Unaweza kuwakumbuka baadhi ya hao watu waliokuwa wakifika hapo kwa Brown kuonana naye?” yule ofisa mkuu wa usalama alimuuliza Babra huku akionekana kuwa makini zaidi.

“Kwa kweli walikuwa wakija watu wengi wa aina tofauti kama nilivyoeleza, ila kwa kuwa mimi sikuishi pale ilikuwa vigumu kuwambuka labda kama itokee nionane nao tena. Ila yupo mmoja ninayemkumbuka kwa jina moja la Trésor, kwani mara nyingi nilikuwa nikimsikia Brown akimtaja wakati akimwita hivyo na alikuwa akiongea naye mara kwa mara kwenye simu,” alisema Brown huku akinitazama kwa jicho la wizi.

“Ni nani huyo Trésor?” aliuliza tena yule ofisa wa usalama.

“Alikuwa rafiki mkubwa wa Brown na kwa haraka niliweza kubaini kuwa alikuwa mtu wa Rwanda kwa mwonekano wake na hata lafudhi ya Kiswahili chake, na bila shaka walikuwa wakifanya biashara pamoja kwani mara nyingi alikuwa akimpitia pale kwake,” alisema Babra huku akishusha pumzi.

“Kwa hiyo baada ya wao kuhama pale walipokuwa wakiishi na wewe kuhamia Nairobi ikawaje?”

“Kilipita kitambo kirefu bila kuonana nao wala kusikia habari zao lakini siku moja nilishangaa nilipomuona Jasmine akifika nyumbani kwangu jijini Nairobi kunisalimia na nilipomuuliza amepajuaje akaniambia kuwa Brown ndiye aliyemuelekeza na kwamba yeye hakutaka tujue kama yupo pale jijini Nairobi kutokana na shughuli alizokuwa akizifanya,” alisema Babra kwa huzuni na mara nikamuona kama aliyekuwa anafikiria kitu fulani, muda huo huo nikaiona michirizi ya machozi kwenye mashavu yake.

“Sikujua Brown alipajuaje pale kwangu, na katika maongezi yetu niligundua kuwa Jasmine alikuwa amebadilika sana kitabia, alikuwa ametumbukia kwenye ulevi na utumiaji wa dawa za kulevya, na hakuwa tena mtu wa kuaminika kwani alijiingiza kwenye masuala ya uhalifu wa mitandaoni, uhalifu wa kutumia silaha na hata utapeli,” alisema huku akiwa analia.

Muda wote ule wale maofisa wa usalama walikuwa kimya wakimsikiliza Babra huku wakinitazama kwa makini. Nilijikuta nikivutiwa kukisikiliza kile kisa kumhusu mtu aliyeitwa Brown Senga na kusahau kuwa yale maelezo yalikuwa yakitolewa ili kunikandamiza nionekane nina hatia ya uhalifu.

“Siku mbili tangu nionane na Jasmine likatokea tukio la kutoweka kwa kaimu mkurugenzi wa masuala ya teknolojia wa tume ya uchaguzi nchini Kenya (IEBC), Christopher Chege Msando na kisha akapatikana akiwa ameuawa katika eneo la Kikuyu lililo viungani mwa mji wa Nairobi baada ya kuteswa sana. Katika upelelezi wa watu wa usalama ilisemekana kuwa siku ile alikuwa na msichana mmoja chotara ambaye walikuwa wanamsaka na walipoonesha picha za CCTV nilishtuka sana baada ya kumtambua yule msichana kuwa alikuwa Jasmine, kwa kweli nilishtuka sana, nikajaribu kuwasiliana na Jasmine bila mafanikio,” alinyamaza na kufuta machozi.

“Ndipo baada ya miezi kadhaa nikasikia kuhusu tukio la wizi wa pesa kwenye Benki ya Wananchi lililomhusisha pia Jasmine. Kwa kweli huyu bwana kamsababishia mdogo wangu matatizo makubwa kwa kumwingiza kwenye uhalifu kisha yeye akatokomea tusikokujua…” alibwata Babra huku akinielekezea kidole kwa hasira.

“Siyo kweli, mwongo mkubwa huyu mwanamke, naomba msimuamini maneno yake,” nikamkata kauli huku nikiongea kwa kujiamini.

“Kama unadhani kuwa yeye ni muongo kwanini hujiulizi kuwa tumezipata wapi taarifa zako na nyaraka zako zikiwemo pasipoti zako kama siyo yeye aliyesaidia kutupa taarifa zako?” yule ofisa usalama akaniuliza huku akinitazama kwa ukali.

“Mimi siye mmiliki wa pasipoti hizo na wala sijui habari hizi mmezitoa wapi! Kama taarifa zenu mmezipata kutoka kwa mwanamke huyu amewadanganya, simjui na wala sijawahi kumuona kabla ya leo,” nilisema kwa kubwata huku donge la hasira likiwa limenikaba kooni.

“Sioni sababu kwanini nikusingizie, Brown, kwanza sina ugomvi na wewe hata kama umesababisha kifo cha mdogo wangu. Inamaana hukumbuki kuwa uliwahi kumtorosha Jasmine ukampeleka kuishi kwenye jumba lako la kifahari huko Avenue Gikondo jijini Kigali? Hukumbuki ulivyokuja kumuumiza baadaye na kuyafanya maisha yake yawe ya majonzi?” Babra akasema kwa kusisitiza na kuniacha na mshangao usioelezeka.

“Hukumbuki kuhusu lile tukio la uporaji pale Benki ya Wananchi? Uliamua kumtumia Jasmine kwenye ule wizi kwa kuwa uliona umezitawala akili zake na ulipofanikiwa azma yako ukamwacha afe. Au kwa kuwa Jasmine amekufa na hawezi kujitetea tena basi huoni taabu kumkana?” aliniuliza Babra kwa hasira huku akitokwa machozi. Sasa alikuwa analia kwa uchungu mkubwa.

Loh! Maelezo ya Babra ambaye wakati wote alikuwa amesimama mbele yangu yakasababisha tumbo langu lianze kunisokota kama niliyevamiwa na maradhi mabaya ya kipindupindu.

Maelezo yake ni kama aliyepigilia msumari wa mwisho katika jeneza langu tayari kwa safari ya maziko. Nilikuwa nimesingiziwa vibaya kiasi kwamba sikufahamu haraka nijitetee vipi na badala yake nikabaki mdomo wazi huku koo langu likikauka.

Sikuwa na shaka yoyote kuwa njia ya kuelekea gerezani ilikuwa nyeupe kwangu na mwisho wangu ulikuwa umewadia, na hapo nikaanza kuilaani vibaya nafsi yangu huku nikijuta kupata wazo la kurudi Tanzania.

Kwa maneno yale ya Babra, kwa kweli hali ya mambo ilivyokuwa kwa wakati huo ikawa imenichanganya sana na kuanza kunikatisha tamaa. Niliona ni kama lilikuwa tukio la kufikirika lakini haikuwa vile, kwani lilikuwa ni tukio la kweli na lililonishangaza sana.

Hata hivyo, niliona kuwa kukaa kimya na kuuruhusu uongo ule uaminike isingefaa.

“Muongo mkubwa huyu mwanamke, msimuamini maneno yake hata kidogo,” nikaongea kwa kujiamini.

Yule ofisa wa usalama akaonekana kunipuuza tena badala yake akafungua tena ule mkoba wake mweusi uliokuwa chini ya meza.

Sikuelewa alikuwa akitaka kufanya nini hadi pale alipochukua bahasha moja kubwa ya kaki na kumimina vitu vilivyokuwa ndani ya ile bahasha pale juu meza.

Niliyakaribisha macho yangu kutazama pale mezani na ghafla nikapigwa butwaa huku midomo yangu ikinikauka.

Pale mezani niliziona picha nne kubwa zilizonionesha nikiwa katika maeneo mbalimbali, picha moja ilinionesha nikiwa na watu wawili, mwanamume mmoja mrefu mwenye umbo kakamavu na msichana mrembo aliyefanana sana na Babra.

Tulikuwa tumesimama katika eneo ambalo sikuweza kulifahamu vyema tukionekana kupanga mambo fulani, yule mwanamume sikumfahamu lakini yule msichana niliamini kuwa ndiye Jasmine aliyesemwa na Babra.

Picha mbili zilinionesha nikiwa viwanja viwili tofauti vya ndege katika siku tofauti nikiwa na watu ambao sikuweza kuwafahamu, moja nikiwa uwanja wa kimataifa wa Julius Nyerere na nyingine nikiwa uwanja wa kimataifa wa Kilimanjaro.

Itaendelea...
 
HEKAHEKA! 11

Na Bishop Hiluka

Tulikuwa tumesimama katika eneo ambalo sikuweza kulifahamu vyema tukionekana kupanga mambo fulani, yule mwanamume sikumfahamu lakini yule msichana niliamini kuwa ndiye Jasmine aliyesemwa na Babra.

Picha mbili zilinionesha nikiwa viwanja viwili tofauti vya ndege katika siku tofauti nikiwa na watu ambao sikuweza kuwafahamu, moja nikiwa uwanja wa kimataifa wa Julius Nyerere na nyingine nikiwa uwanja wa kimataifa wa Kilimanjaro.

Picha ya mwisho ilinionesha nikitoka kwenye mlango wa ofisi ambao ulikuwa na maandishi ‘Ofisi ya Meneja’ huku nikisindikizwa na mwanamume mmoja mfupi mnene na mweusi, mazingira yalionesha kuwa ilikuwa ni ndani ya benki ambayo sikuifahamu lakini nilihisi huenda ndiyo ilikuwa Benki ya Wananchi.

Nilizitazama kwa makini zile picha nikashangaa sana, zilikuwa ni picha zenye sura yangu kabisa ingawa nilionekana nimenyoa nywele zote na kubaki na kipara na nilikuwa nimefuga ndevu nyingi!

Wazo la haraka likanijia akilini mwangu kuwa zile picha zilikuwa zimetengenezwa kwenye kompyuta kwa kuunganisha sura yangu na kiwiliwili cha mwanamume mwingine aliyekuwa na mwili kama wangu ili kutaka kunimaliza.

Hata hivyo, nililifuta lile wazo kwani nilijiuliza kuwa ikiwa walikuwa wameunganisha sura yangu na kiwiliwili cha mtu mwingine, je, walizipata wapi zile picha zenye sura yangu? Pia ukiziangalia kwa makini zile picha zilionekana kuwa halisi kabisa.

Lakini swali likabaki kuwa, mbona sijawahi kunyoa nywele zote kichwani kwa mtindo ule na wala sijawahi kufuga ndevu nyingi kwa mtindo ule kama ilivyoonekana kwenye zile picha? Kwa kweli nilijikuta nikianza kuchanganyikiwa.

“Mmezipata wapi hizi picha?” nilimuuliza yule ofisa wa usalama kwa mshangao.

“Hizi ni picha zilizopatikana kwenye camera za CCTV zilizowekwa katika maeneo husika isipokuwa hiyo uliyosimama na Jasmine ambayo ilichukuliwa kwa siri kutoka kwenye simu, je, bado unaendelea kusisitiza kwamba tumekufananisha?” alinijibu yule ofisa wa usalama huku akiniangalia kwa tabasamu.

“Huu ni uongo kabisa! Hizo picha siyo zangu, mtakuwa mmezitengeneza kwenye photoshop ili kunipakazia,” nilisema kwa hasira huku nikitaka kusimama pale nilipoketi.

Kabla sijafanikiwa kusimama nikashtukia nikitulizwa kwa kuzabwa kofi la sikioni lililonisababishia maradhi ya ukiziwi kwa dakika kadhaa.

“Tunazo njia nyingi za kukulazimisha uongee ukweli lakini sura yako nzuri inaashiria kuwa u mtu usiyependa matata, hivyo tusingependa kufikia huko endapo utashirikiana nasi,” yule ofisa usalama aliniambia, kisha akaunyanyua juu ule mkoba wake mweusi na kunionesha.

“Bado tuna ushahidi mwingi tu kukuhusu na kuna watu takriban kumi wanaokufahamu ambao wapo tayari kutoa ushahidi dhidi yako, lakini hapa si mahala pake kwa sasa,” alisema na kuirudisha ile bahasha kwenye ule mkoba.

Kisha nikamuona akimwashiria kitu yule ofisa usalama aliyekuja na Babra na mara yule ofisa usalama akaondoka na kutoka nje akiwa ameongozana na Babra.

Wakati Babra na yule ofisa usalama wakitoka mawazo mengi yakaanza kupita kichwani kwangu, nilijiuliza kuwa huenda ni kweli niliitwa Brown Senga na pengine nilikuwa nimekumbwa na tatizo la kupoteza kumbukumbu maarufu kama ‘amnesia’.

Nikakumbuka kisa cha rafiki yangu Martin (katika mkasa uliopewa jina la Faraja) aliyewahi kupoteza kumbukumbu baada ya ajali, akaishi akiwa mtu mwingine kabisa, akaoa na kufanya kazi za vibarua vya kutwa, huku ndugu na jamaa zake wakiamini kuwa alikuwa amekufa!

Ajali iliyompata Martin ilisababisha ubongo wake kuhama kutoka katika sehemu yake ya kawaida na hivyo kupata tatizo la kupoteza kumbukumbu lililojulikana kama ‘retrograde amnesia’, yaani kutokuwa na uwezo wa kukumbuka taarifa zozote za kabla ya ajali hiyo.

“Okay, bila shaka sasa upo tayari kutueleza bila kuficha, wenzako wako wapi na silaha mlizopora mmezificha wapi?” yule ofisa usalama akaniuliza huku akiwa amenikazia macho.

“Sielewi kwanini mnang’ang’ania kuniuliza swali hilo, si mkawaulize hao watu mnaodai kuwa wana ushahidi dhidi yangu, eh?” nikamuuliza yule ofisa usalama na kabla sijamaliza nikashtukia nikizabwa makofi mawili ya nguvu yaliyonipa kisulisuli.

“Tuambie Brown, washirika wenzako wako wapi na silaha mmezificha wapi?” yule ofisa aliniuliza tena akionekana kuanza kupandwa na hasira.

“Sasa kwanini mnanipiga, kosa langu ni lipi?” nilimuuliza yule ofisa usalama kwa hasira.

“Mimi ningekuwa nafahamu chochote kuhusu hizo silaha mnazozizungumzia ningekwisha waambia mahali zilipo, sina sababu ya kuwasumbua,” nilisema huku nikiwa nimekasirika sana.

“Hivi unafahamu kuwa kushiriki kitendo chochote cha ugaidi na kutaka kuifanya nchi isiwe na amani ni uhaini na malipo yake ni kifo?”

“Nafahamu,” nikajibu kwa kifupi.

“Okay, mmezificha wapi na washirika wenzako ni kina nani?”

Kwa kweli nilijikuta nashindwa kujibu na kubaki nashangaa. Nikiwa bado natafakari neno la kusema mara mlango wa kile chumba cha mahojiano ukafunguliwa, akaingia mwanamke mmoja mrefu mwenye umbo zuri la kimazoezi na haiba ya kuvutia.

Mwanamke yule alionekana mchangamfu sana lakini akiwa makini kuliko hata simba jike, akiwa ameongozana na walinzi wawili.

Alikuwa na ngozi ya rangi ya maji ya kunde mwenye nywele nyeusi ndefu na laini alizokuwa amezifunika kwa kofia nyeusi ya kapelo. Alikuwa na sura ya duara na macho yake yalikuwa makubwa ya kike lakini yaliyokuwa makini zaidi.

Alikuwa amevaa miwani mikubwa ya macho na suruali ya Jamsuit ya rangi ya samawati iliyolionesha vyema umbo lake refu maridadi lenye kiuno chembamba lakini kilichokuwa imara kikiwa kimebeba minofu ya mapaja iliyokaza kutokana na mazoezi. Miguuni alikuwa amevaa buti ngumu za ngozi za rangi nyeusi.

Harufu nzuri ya manukato ghali aliyokuwa amejipulizia mwilini ilitamalaki mle ndani na kuzifanya pua zangu zipate uhai mpya na kunisahaulisha kwa muda masahibu ya kuhojiwa na wale maofisa wa usalama.

Maofisa wote wa usalama mle ndani walipomuona yule mwanamke wakasimama kwa ukakamavu na kwa heshima huku wakionesha utii mkubwa.

Kisha yule mwanamke akageuka kunitazama kwa utulivu kwa kitambo na kuachia tabasamu kabambe kabla hajanisogelea na kusimama jirani na mimi huku akiendelea kunitazama kwa uyakinifu zaidi na kubetua kichwa chake.

Nikamtambua, kwa kuwa nilikuwa nimemuona mara kadhaa kwenye vituo vya runinga vya CNN, Aljazira na BBC, na kusoma habari zake magazetini na kwenye mitandao ya intaneti. Alikuwa ni mwanamke wa kwanza kuwa Mkurugenzi Mkuu wa Idara ya Usalama wa Taifa.

Mwanamke yule aliitwa Pamela au maarufu kama Madame Pamela na alikuwa na umri wa miaka 46. Historia ilionesha kuwa alikuwa amejikita kwenye kazi ya ujasusi kwa takriban miaka 25, hatua hiyo ilikuwa miongoni mwa sifa kubwa zilizomfikisha katika nafasi ile na kuwa mwanamke wa kwanza kuiongoza taasisi hiyo nyeti.

Madame Pamela ambaye alikuwa jasusi mbobezi aliwahi kulihudumia taifa katika masuala mbalimbali aliyopangiwa kabla ya kuteuliwa kushika nafasi hiyo ya juu na kuthibitishwa kuwa Mkurugenzi Mkuu wa Usalama wa Taifa na baadaye kula kiapo cha utiifu.

Maelezo zaidi yalieleza kuwa kuthibitishwa kwa Madame Pamela kuwa bosi wa Usalama wa Taifa kulikuja baada ya malalamiko kuwa taasisi hiyo ilianza kupoteza imani na iliaminika kuwa Madame Pamela angeweza kurudisha imani kwa kuwa alikuwa makini na aliyefanya kazi zake kwa weledi mkubwa akiwa ameshiriki kwenye oparesheni nyingi tata.

Madame Pamela alikuwa komandoo, shushushu na jasusi wa kuogopwa aliyekuwa amepata mafunzo ya kijasusi kwa nyakati tofauti katika nchi za Israel, China na Marekani na alisifika kama ‘mwanamke wa chuma’ baada ya kuongoza kwa mafanikio kikosi maalumu cha usalama cha nchi za Afrika Mashariki kilichopewa kazi ya kuwahoji watuhumiwa wa matukio ya ugaidi waliokuwa wamehusishwa na kundi la Al Shabab baada ya matukio ya kigaidi kutawala katika nchi za Afrika Mashariki.

Itaendelea...
 
HEKAHEKA! 12

Na Bishop Hiluka

Madame Pamela alikuwa komandoo, shushushu na jasusi wa kuogopwa aliyekuwa amepata mafunzo ya kijasusi kwa nyakati tofauti katika nchi za Israel, China na Marekani na alisifika kama ‘mwanamke wa chuma’ baada ya kuongoza kwa mafanikio kikosi maalumu cha usalama cha nchi za Afrika Mashariki kilichopewa kazi ya kuwahoji watuhumiwa wa matukio ya ugaidi waliokuwa wamehusishwa na kundi la Al Shabab baada ya matukio ya kigaidi kutawala katika nchi za Afrika Mashariki.

Alijiunga na idara ya Usalama wa Taifa akiwa na umri wa miaka 21 tu, ilikuwa ni baada tu ya kuhitimu masomo yake katika Chuo Kikuu cha Kentucky, na amewahi kuwa mkuu wa vitengo mbalimbali vya ujasusi, ikiwamo cha kupambana na ugaidi kilichofanya kazi nzuri sana ili kuhakikisha Tanzania na nchi za Afrika Mashariki zinakuwa salama.

Jina lake kamili aliitwa Pamela Mtokambali akiwa amekulia katika nchi za Tanzania, Uingereza na Canada ambako baba yake, Aleck Mtokambali aliyekwenda kufanya kazi kama balozi akiiwakilisha nchi ya Tanzania katika nchi hizo.

Madame Pamela alianza elimu yake ya msingi nchini Tanzania kisha akaendelea nchini Uingereza na baadaye alijiunga na Chuo Kikuu cha Kentucky, ambako alihitimu Shahada ya Sanaa katika Sayansi ya Jamii.

Kisha alisoma Shahada ya Umahili katika Mawasiliano, Lugha na Uandishi katika Chuo Kikuu cha Technion – Israel Institute of Technology cha nchini Israel na baadaye akasoma na kuhitimu Shahada ya System Analysis katika chuo hicho hicho.

Tangu alipojiunga na idara ya Usalama wa Taifa akiwa na miaka 21 Pamela ameshiriki operesheni tofauti kama jasusi wa taasisi hiyo katika nchi mbalimbali. Operesheni ya kwanza aliyopangiwa kufanya ilikuwa nchini Sudan katika eneo la Darfur.

Baadaye alishiriki na kusaidia oparesheni za majeshi ya umoja wa nchi za Afrika kukikomboa kisiwa cha Anzuwani kutoka mikononi mwa majeshi ya Muhamad Bakari katika visiwa vya Comoro.

Kisha alishiriki katika oparesheni za kiintelijensia na kijasusi nchini Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo, Cameroon na nchini Lebanon kwenye oparesheni maalumu za kupambana na ugaidi.

Ni huko Lebanon alikofanya oparesheni kabambe ya kupambana na ugaidi iliyofanikiwa sana na kumpa sifa kubwa huku ikikaribia kuyagharimu maisha yake na kumwachia makovu mawili ya risasi yaliyokuwa kwenye paja lake la mguu wa kulia na kovu jingine la kisu lililokuwa kwenye bega lake.

Ilisemekana kuwa kila sehemu aliyopelekwa alifanya kazi kwa umakini mkubwa na kupata mafanikio. Kisha alitajwa kuwa ofisa mtendaji wa kikosi cha kupambana na ugaidi kabla ya kuwa ofisa mtendaji wa idara ya rasilimali watu ndani ya idara ya Usalama wa Taifa.

Pamela Mtokambali aliwahi kuolewa na mwanausalama mwenzake na shushushu aliyebobea, James Gayo ambaye aliwahi kuwa naibu mkurugenzi mkuu wa idara ya Usalama wa Taifa kabla ya kuteuliwa na Rais kuwa Mbunge na Waziri wa Utawala Bora, na ndoa yao ilidumu kwa miaka tisa tu kisha wakatalikiana.

Ilisemekana kuwa baada ya Madame Pamela kutalikiana na mumewe hakutaka kuolewa tena na walibahatika kuwa na mtoto mmoja wa kike huku ikisemekana kuwa Madame Pamela alikuwa hatumii kabisa mitandao ya kijamii…

‘Hmm… kama baba shushushu aliyebobea na mama naye shushushu aliyebobea sijui mtoto wao atakuaje!’ niliwaza na hapo nikajikuta nikitamani kucheka.

“Mmefanya kazi nzuri sana kumkamata huyu jasusi hatari…” sauti ya Madame Pamela ilinizindua kutoka kwenye lindi la mawazo na hapo nikainua uso wangu kumtazama Madame Pamela kwa makini.

“Kwa taarifa za uhakika, jina lake halisi ni Brown Senga, si Mtanzania kama anavyotaka kuwaaminisha watu ila ni Mnyarwanda wa kabila la Kihutu aliyeingia nchini na wazazi wake akiwa na miaka kumi kipindi kile cha mauaji ya kimbali yaliyoikumba nchi ya Rwanda, na taarifa tulizonazo ni kwamba hajawahi kuukana uraia wa Rwanda ambako ndiko chimbuko la wazazi wake. Alijifunza vizuri Kiswahili na kumalizia elimu yake ya msingi na baadaye akapata elimu ya sekondari hapa Tanzania akitumia jina la Godwin Sengerema. Umri wake ni miaka therathini na mbili…

“Huyu ni jasusi hatari sana, mbobezi wa ujasusi wa kimtandao ambaye amekuwa akikodiwa kupanga matukio ya kigaidi kwenye nchi tofauti za Kiafrika… ndiye aliyeratibu tukio la kigaidi katika mkutano wa Bulawayo nchini Zimbabwe ambao Rais wa Zimbabwe alinusurika kuuawa na guruneti. Tunazo video kutoka uwanja wa michezo wa White City siku ya tukio, na kuna picha zilizopigwa na watu wa usalama siku ile mkutano wa rais wa nchi hiyo uliposhambuliwa na guruneti, baada ya kumshuku kutokana na mazungumzo yake…

“Pia anahusishwa kupanga tukio la mlipuko wa guruneti katika mkutano wa Waziri Mkuu wa Ethiopia kwenye bustani kuu ya Meskel mjini Addis Ababa, ambapo watu 83 walijeruhiwa huku 6 wakiwa katika hali mahututi. Yapo matukio mengine anayohusishwa nayo katika nchi za Rwanda, Burundi, Kenya na mashariki mwa DR Congo,” Madame Pamela alitoa maelezo yaliyonishtua sana.

“Alisoma katika chuo cha Technion – Israel Institute of Technology akitumia jina la Godwin Sengerema na amewahi kuwa Mkufunzi katika Chuo Kikuu cha Dar es Salaam kitengo cha TEHAMA, kabla hajaacha kazi na kuamua kwenda nchini Rwanda ambako aliondoka tena kurudi nchini Israel, safari hii akitumia pasipoti ya Rwanda yenye jina la Brown Senga na alijiunga na Chuo kikuu cha Birzeit kusomea uhandisi wa umeme na inasemekana kuwa akiwa nchini Israel alitumia pia mwanya huo kujiunga na programu maalumu ya kijasusi na kupata mafunzo ya kujihami, hasa karate na judo, na kufanikiwa kupata mkanda mweusi, kiwango cha third degree…

“Baadaye akaenda nchini Zambia ambako aliajiriwa kama mkufunzi wa uhandisi umeme katika taasisi ya Electrical Maintenance Lusaka Ltd iliyopo jijini Lusaka, alikofanya kazi kwa miaka miwili tu akaacha na kurudi tena Tanzania akitumia jina la Godwin Sengerema na kuamua kujikita kufanya biashara ya madini.

“Kwa kipindi fulani aliondoka nchini katika mazingira ya kutatanisha akaelekea nchini Rwanda ambako alitumia tena pasipoti ya Rwanda yenye jina la Brown Senga na kwenda nchini Libya, inaaminika kuwa huko alipata mafunzo zaidi ya ujasusi na kuwa 'mhalifu wa daraja la kwanza' na ndipo alipoanza rasmi harakati za ugaidi kwa kukodiwa huku akijificha kwenye kivuli cha mfanyabiashara wa madini kutoka Tanzania…” kufika hapo Madame Pamela akaweka tena kituo kidogo na kuendelea baada ya kukohoa kidogo ili kusafisha koo lake.

“Amekuwa akipanga mambo yake kwa ustadi mkubwa huku akihakikisha washirika wenzake hawajuani na wala hawamjui bosi wa uhalifu na huwa haachi alama, moja ya vitu vinavyomsaidia kufanya matukio ya uhalifu kwa mafanikio bila kuhusishwa wala kuacha alama ni uwezo wake wa kupanga mikakati ya utekelezaji! Ni dhahiri kuwa mafunzo ya kijasusi aliyoyapata yamemsaidia sana kuwa mwanamkakati mzuri wa kiufundi wa matukio!

“Kwanza kabisa Brown huzuru eneo analotaka kufanyia uhalifu kazi ambayo huifanya kwa umakini mno, kisha hutafiti juu ya tukio lenyewe atakavyolitekeleza kwa kusoma mandhari yanayozunguka eneo husika na akishajiridhisha hutafuta washirika anaodhani watamfanyia kazi, huwalenga hasa watu wenye makandokando kwa kuwatishia kutoa siri zao nje endapo hawatampa ushirikiano…

“Kwa mfano, kwenye lile tukio la kigaidi la wizi mkubwa wa pesa katika Benki ya Wananchi alitafiti na kudukua mawasiliano yao ndipo alipojua siku ambazo wanakuwa na kiasi kikubwa cha fedha na kuwatafiti wafanyakazi wa benki husika akizingatia kuhusu zamu zao za kazini, udhaifu wao, vitu wanavyopendelea na haiba zao…

“Alipogundua udhaifu wa meneja wa benki hiyo, Lister Manda kuwa aliwahi kuhusika kwenye mauaji ya watu wenye ualbino, hasa tukio la kumteka na kumuua binti mdogo wa miaka kumi mwenye ualbino kutoka mkoani Geita kisha akachukua viungo vyake na kuvizika katika nyumba yake na eneo hilo kupanda mti wa matunda ili mambo yake yafanikiwe, basi akaamua kumtishia kutoa siri endapo angekataa. Kwa sasa meneja huyo tunamshikilia na tutamfikisha mahakamani…

Itaendelea...
 
HEKAHEKA! 13

Na Bishop Hiluka

“Alipogundua udhaifu wa meneja wa benki hiyo, Lister Manda kuwa aliwahi kuhusika kwenye mauaji ya watu wenye ualbino, hasa tukio la kumteka na kumuua binti mdogo wa miaka kumi mwenye ualbino kutoka mkoani Geita kisha akachukua viungo vyake na kuvizika katika nyumba yake na eneo hilo kupanda mti wa matunda ili mambo yake yafanikiwe, basi akaamua kumtishia kutoa siri endapo angekataa. Kwa sasa meneja huyo tunamshikilia na tutamfikisha mahakamani…

“Na ukichunguza vizuri utagundua kuwa matukio mengi ambayo Brown anahusishwa kuyaandaa yametekelezwa jioni ya siku ya Ijumaa ya mwisho wa mwezi na hii ni mbinu inayomsaidia sana na huitumia siku hii kwa sababu za kisaikolojia kwa kuwa jioni ya Ijumaa ya mwisho wa mwezi watu wengi wanakuwa hawako makini kutokana na weekend kuanza, na hata tukio la ugaidi na uporaji wa silaha katika bohari kuu ya silaha kule Kwembe lilifanyika jioni ya Ijumaa ya mwisho wa mwezi,” Madame Pamela alimaliza taarifa yake na kunikazia macho yenye ghadhabu.

Loh… taarifa zile zikasababisha kutokea kitambo kirefu cha ukimya mle ndani ya chumba kile cha mahojiano huku watu wote wakinitazama kwa mashaka utadhani walikuwa wameona kiumbe cha ajabu kutoka sayari nyingine.

Kwa kweli nilishtushwa sana na taarifa zile na kwa kiwango fulani nilijikuta nikianza kukata tamaa ya kuokoka katika mkasa ule. Kwa wasifu ule niliamini kabisa kuwa huyo mtu aliyeitwa Brown Senga alikuwa mtu hatari sana kuliko hata hatari yenyewe. Hata hivyo, sikuacha kujitetea.

“Uongo mkubwa, mimi siyo Brown Senga mnayemzungumzia, nipo tayari kuthibitisha hilo…” nilijaribu kujitetea na kabla sijamaliza kusema ofisa mmoja wa usalama aliyekuwa amesimama karibu yangu akanizaba kibao kikali cha uso na kunisababishia maumivu makali.

“Hujaulizwa, unajibujibu nini!” alisema kwa ukali.

Nilikaa kimya huku nikiugulia maumivu, na muda ule ule nikamshuhudia Madame Pamela akiongea jambo kwa sauti ya chini na yule ofisa mkuu wa usalama aliyekuwa akinihoji, na katika maongezi yao walijitahidi sana kutumia maneno maalumu ya mafumbo ya kiintelijensia ambayo sikuweza kabisa kuelewa yalikuwa yanamaanisha nini.

Baada ya majadiliano mafupi mwishoni nikamsikia Madame Pamela akitamka maneno yaliyoninyong’onyesha zaidi.

“Tunahitaji taarifa zote muhimu kutoka kwa mtu huyu kwa namna yoyote ile. Nimeshawasiliana na Pay Master, ameniambia apelekwe CMI kwa mahojiano maalumu,” alisema Madame Pamela na kuanza kupiga hatua kuondoka huku yule ofisa mkuu wa usalama na wale maofisa usalama wengine wakiinuka.

Muda ule ule wale maofisa wa usalama walionileta mle ndani wakanizingira huku wakinielekezea bastola zao kichwani, kuona hivyo nikafumba macho yangu.

Moyo wangu ukapiga kite huku akili yangu ikisimama na baridi nyepesi ikaanza kusambaa mwilini.

“Mnataka kunifanya nini?” nikawauliza wale maofisa usalama kwa wasiwasi huku nikiitupia jicho saa yangu ya mkononi iliyonitanabaisha kuwa ilikuwa tayari saa tano usiku.

“Unajali nini wewe, tunakupeleka sehemu salama zaidi ambako utaweza kutueleza bila usumbufu kuhusu washirika wenzako na mahali mlikozificha silaha,” alinijibu yule ofisa usalama aliyekuwa ameshika pingu na kusimama mbele yangu huku akiachia tabasamu la kifedhuli usoni mwake.

Nikabaki kimya nikiwatumbulia macho huku jasho jepesi likinitoka sehemu mbalimbali za mwili wangu. Badala ya ubaridi sasa joto la woga wa aina yake likaanza kunitambaa mwilini na mapigo ya moyo wangu yakibadili mwendo wake na kwenda mbio isivyo kawaida!

Alinifunga zile pingu mikononi kisha nikaongozwa kuelekea nje ya kile chumba nikiwa chini ya ulinzi mkali. Hapo nikajua kuwa safari ya kuelekea kwenye mateso zaidi ilikuwa imeanza na kwa kweli sikuweza kufahamu vizuri ni wapi nilikuwa napelekwa.

Maofisa wawili walibeba mizigo yangu na kutufuata nyuma, hadi tulipotokea kwenye lango moja ambako kulikuwa na eneo tulivu kabisa.

Hapo nje tuliyakuta magari matano maalumu kwa ajili ya misafara ya kusafirisha wahalifu hatari na eneo lote lilikuwa limetanda askari wa kikosi maalumu cha kupambana na uhalifu hatari kama ujasusi, uzandiki, hujuma na ugaidi waliokuwa wamejiweka tayari muda wote kwa ajili ya kuboresha ulinzi.

Wale askari walikuwa wamevaa kofia nyekundu za bereti kichwani, fulana za rangi ya hudhurungi, suruali za kombati na buti ngumu za ngozi miguuni.

Walikuwa vijana warefu na wakakamavu wakiwa imara kabisa. Wote walikuwa wameshika bunduki aina ya Sub Machine Gun mikononi tayari kuzitumia wakati wowote endapo ingetokea rabsha yoyote.

Nilipowatazama usoni sikuona mazingira yoyote ya urafiki katika nyuso zao.

Katikati ya yale magari kulikuwa na gari moja maalumu lenye muundo maalumu wa magari yanayotumiwa kusafirishia watuhumiwa hatari duniani kama wahaini dhidi ya serikali, magaidi hatari au watuhumiwa wa mauaji ya kimbari na wafanyabiashara wakubwa wa dawa za kulevya waliokamatwa na vyombo vya dola.

Nilifunikwa kichwani na mfuko mweusi ulionifanya nisiweze kuona chochote na kupandishwa sehemu ya kati ya lile gari kwenye chumba kidogo kilichopakana na ukuta wa nyaya ngumu pande zote ili kumtenganisha mtuhumiwa hatari na dereva wa lile gari kwa upande wa mbele na walinzi wa msafara kwa upande wa nyuma.

Muda uleule mlango wa kile chumba cha gari nilichoingizwa ukafungwa kwa nje kisha askari wengine wa kikosi maalumu wakapanda na kukaa kwenye sehemu ya nyuma ya lile gari.

Bila kupoteza muda madereva wakatia moto magari na hapo safari ikaanza. Kwa namna ilivyokuwa nilihisi kuwa msafara wetu wa magari matano uligawanywa kwa magari mawili kutangulia mbele yetu na mawili yalikuwa nyuma yetu.

Safari ya kutoka pale katika eneo la uwanja wa ndege wa Julius Nyerere ikawa imeanza na kwa kweli sikuweza kufahamu vizuri jiografia ya eneo tulilokuwa tukielekea kwa vile usoni nilikuwa nimefunikwa ule mfuko mweusi.

Hata hivyo, hisia zangu zilinitanabaisha kuwa baada ya kutoka pale uwanja wa ndege magari yaliingia katika Barabara ya Nyerere na kukata kona yakiingia upande wa kulia kisha safari ya kuelekea mjini ikashika kasi.

Kwa hisia tu nilibaini kuwa msafara wetu ulitanguliwa na pikipiki maalumu yenye king’ora kwa ajili ya kuyataka magari mengine yaliyokuwa barabarani yakae kando wakati tukipita.

Kwa kweli kwa jinsi msafara ule ulivyokuwa umeshika kasi utadhani aliyekuwa akipita barabarani alikuwa Rais wa nchi nilijikuta nikikata tamaa japo sikuwa na mpango wa kutaka kutoroka.

Wakati tukiendelea na safari nilitamani sana kujua tulikokuwa tukielekea lakini sikuweza. Nilianza kujilaumu sana kwa kutomsikiliza Susan, niliamini kuwa alikuwa na maono aliponitaka niahirishe safari yangu lakini nikakataa.

Nikajikuta nikiilaumu sana siku hiyo ambayo ilikuwa ya hekaheka sana kwangu, maana katika kipindi cha saa kumi na mbili tu tayari nilikuwa nimekwishapata jambajamba mara mbili kwenye viwanja vya ndege viwili tofauti!

Maana kabla ya mkasa huu wa uwanja wa ndege wa kimataifa wa Julius Nyerere jijini Dar es Salaam, nilikuwa nimepatwa na mkasa uliofanana na huo katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Schiphol jijini Amsterdam, katika siku hiyo hiyo moja ya safari! Kwa kweli siku hiyo ilikuwa ni siku ya hekaheka!

Je, nini kitatokea? Usikose kufuatilia simulizi hii ya kijasusi...
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom