Bishop Hiluka
JF-Expert Member
- Aug 12, 2011
- 7,147
- 14,711
- Thread starter
- #21
HEKAHEKA! 6
Na Bishop Hiluka
Nikiwa bado nimesimama pale nikajaribu kujiuliza, nini ilikuwa sababu ya wale maofisa wa usalama kutaka kunihoji ilhali niliamini kuwa sikuwa na kosa lolote na wala sikuwahi kuwa na historia yoyote ya uhalifu, achilia mbali kufikishwa polisi kwa tuhuma zozote.
Hata hivyo, nilipiga moyo konde huku nikijitahidi kuifukuza hofu iliyoanza kuniingia kwa kuwa nilikuwa natambua kuwa harakati dhidi ya ugaidi zilikuwa zimepamba moto na labda nilitakiwa kwa mahojiano mafupi kutaka kujua nyendo zangu.
Hapo nikakumbuka kuwa wiki mbili zilizotangulia nilikuwa nimesoma kwenye mtandao wa intaneti na baadaye kuona kwenye televisheni habari za matukio mawili yaliyodhaniwa kuwa na chembechembe za ugaidi yaliyotokea nchini Tanzania kwa kufuatana.
Tukio moja lilihusu mlipuko wa guruneti uliokuwa umetokea katika mkutano wa kampeni ya ‘Uzalendo’ ambao Waziri Mkuu ndiye aliyetarajiwa kuwa mgeni na badala yake akawakilishwa na Mkuu wa Mkoa, Daniel Luhopelo.
Katika tukio lile lililotokea katika viwanja vya Mnazi Mmoja jijini Dar es Salaam watu 6 walipoteza maisha, 83 walijeruhiwa akiwemo Daniel Luhopelo, huku 10 wakiwa katika hali mahututi.
Tukio la pili lilihusu uvamizi na uporaji wa silaha za kivita kwenye bohari kuu ya silaha iliyokuwa katika eneo la Kwembe nje kidogo ya jiji la Dar es Salaam na katika uvamizi huo askari kadhaa waliuawa.
Kwa matukio yale na mengine ambayo sikuyafahamu nikaamini kuwa walipaswa kujiridhisha kuwa hali ya amani inatamalaki nchini na mimi sikuwa tishio kwa usalama wa nchi hii, hasa kwa kuwa nilionekana mgeni.
Hata hivyo, sikujua kabisa wala sikutarajia kuwa mshtuko mkubwa ulikuwa unanisubiri mbele yangu!
Mara nikawaona maofisa usalama wawili waliokuwa wamevaa suti wakifunua makoti yao na kunionesha bastola zao zilizokuwa zimechomekwa vyema kwenye mishipi kiunoni, kisha yule kamishna msaidizi wa polisi akanitaka kunyanyua mikono yangu juu.
Niligwaya sana na mwili wangu ulianza kutetemeka lakini sikutaka kabisa kuionesha ile hali ya kugwaya, hivyo nilibaki nikiwatazama kwa makini na kuhoji kwanini ninyooshe mikono yangu juu kama mtuhumiwa wakati sikuambiwa kosa langu.
Mara nikamuona mmoja wa wale maofisa wa usalama akiitoa bastola yake na kuishika vizuri akiielekeza kwenye kichwa changu huku akiniamuru ninyooshe mikono yangu juu.
Kuona vile sikuwa mbishi, nikanyoosha mikono yangu juu nikiamini kuwa kitendo chochote cha kuendelea kuleta ubishi kwa wale maofisa wa usalama kingeweza kuyagharimu maisha yangu.
Niliponyoosha mikono yangu juu nikaamuriwa niiweke mikono kisogoni kisha nigeuke na kuuelekea ukuta. Nikafanya kama nilivyoamuriwa bila kuhoji.
Mmoja wa wale maofisa usalama akanisogelea haraka na kwa tahadhari kubwa kisha akaanza kunipekua kama nilikuwa na silaha yoyote, huku wale maofisa wengine wakiwa makini kuhakikisha sileti matata yoyote na endapo ingetokea nimeleta purukushani yoyote waweze kunituliza kwa wepesi zaidi.
Wakati nikipekuliwa nikajaribu kuhoji sababu za wao kutaka kunikamata namna ile kama jambazi sugu lakini nikaambiwa kuwa nitalijua kosa langu baadaye kwani nilikuwa nahitajika kwa mahojiano kidogo na kama ningeonekana kutokuwa na kosa basi ningeachiwa mara moja.
Sikuleta matata yoyote, hivyo nilifungwa pingu mikononi kisha nikachukuliwa hadi kwenye chumba kimoja maalumu katika jengo lile pale kiwanja cha ndege ambacho kilikuwa na utulivu wa kupita kiasi.
Na hapo tukawakuta maofisa wengine watatu ambao niliamini kuwa walikuwa ni maofisa wa usalama wa taifa walionikaribisha kwa tabasamu bashasha.
Nilisimama nikabaki kuwatazama, wakati huo wale maofisa walionileta mle ndani walikuwa bado wamenizingira huku wakiwa makini kuhakikisha kuwa sipati fursa yoyote ya kuleta rabsha.
Mpaka hapo bado sikuwa na hofu kabisa kwani nilifikiria kuwa yawezekana walikuwa wamenifananisha na mtu mwingine na baada ya mahojiano mafupi na kugundua kuwa mimi si yule mtu waliyekuwa wakimdhania basi wangeniomba radhi na kuniachia huru niende zangu.
“Kuanzia sasa upo chini ya ulinzi,” aliniambia mmoja wa wale maofisa wa usalama wa taifa tuliowakuta mle ndani, ambaye alionekana kuwa mkuu wa usalama au kiongozi wa wale maofisa wengine.
“Kwanini nawekwa chini ya ulinzi wakati hata siambiwi kosa langu ni nini?” nikauliza huku nikishangaa.
“Usijali, utaelezwa sasa hivi, keti tafadhali,” alisema yule ofisa mkuu wa usalama aliyeonekana kuwa kiongozi wa wale maofisa wengine akinikaribisha kwenye kiti kilichokuwa mbele ya meza ndefu iliyokuwa na umbo mstatili, ambayo nyuma yake lile jopo la wale maofisa usalama wa taifa walikuwa wameketi. Macho yao yote yalikuwa kwangu.
Nikaketi taratibu huku nikiyatembeza macho yangu taratibu kuwatazama wale maofisa usalama mmoja baada ya mwingine kabla ya kuweka kituo kwa yule ofisa mkuu wa usalama, ambaye wakati huo alikuwa ameketi mbele yangu tukitazamana.
Sikuwa na shaka yoyote kuwa nilikuwa nimefikishwa pale kwa sababu moja muhimu ya mahojiano wakihitaji kupata taarifa fulani walizodhani pengine nilikuwa nazifahamu.
Katika mahojiano kama yale nilifahamu kuwa ushirikiano wangu ndicho kilikuwa kitu pekee ambacho kingeweza kuniweka salama na kuniepushia matatizo zaidi, hasa ikizingatiwa kuwa katika kipindi kile harakati dhidi ya ugaidi duniani zilikuwa zimepamba moto kutokana na ugaidi kushika chati.
“Sijui nikuite Brown Senga, Godwin Sengerema au kwa jina la sasa la Maximilian Banda?” hatimaye yule ofisa mkuu wa usalama alivunja ukimya huku akinikazia macho.
Nikashangaa sana kusikia nikihusishwa tena kwa mara nyingine na jina la Brown Senga, hata hivyo, kilichonishangaza zaidi ni kuongezeka kwa jina la Godwin Sengerema. Nikajiuliza kulikuwa na nini kinaendelea kwa huyo mtu aliyeitwa Brown Senga!
Hata hivyo, pamoja na kujiuliza maswali yale nilijitahidi kuuficha mshangao wangu.
“Niite Maximilian Banda, hayo mengine si majina yangu,” nilimjibu yule ofisa wa usalama kwa sauti tulivu huku nami nikimkazia macho.
“Okay, nitakuita Maximilian kama unavyotaka…” alisema huku akiachia tabasamu.
“Kwa kifupi tulipata taarifa zako tangu tu ulipotua jijini Nairobi kwamba ulikuwa unakuja Dar es Salaam na mimi nikazipokea taarifa hizo kwa shauku huku nikiamini kuwa utatusaidia katika uchunguzi wetu wa mambo kadhaa ya kihalifu yaliyotendeka nchini wiki mbili zilizopita,” alisema yule ofisa mkuu wa usalama huku akiweka kituo kidogo na kunitazama kwa uyakinifu.
“Sina kitu chochote ninachoweza kuwasaidia kuhusu uhalifu, kwa kifupi sijui chochote,” niliongea kwa sauti tulivu huku nikiendelea kumkazia macho yule ofisa usalama.
Hata hivyo yule ofisa wa usalama alionekana kunipuuza, nilipomtazama wala sikuona tashwishwi yoyote katika uso wake.
“Pengine bado hujaelewa vizuri uzito wa jambo hili au taarifa tunazozihitaji kutoka kwako na hujui kwanini wewe upo hapa… hii ni kuhusiana na hali ya usalama wa nchi hii,” yule ofisa mkuu wa usalama akasema kwa msisitizo huku akiendelea kunitazama na macho yake yaliyokuwa yamehifadhi ghadhabu.
“Bado sijaelewa, ni nini kinachohusiana na usalama wa nchi hii ambacho mimi nina taarifa zake?” niliuliza kutaka kupata uhakika wa kile alichokuwa anakisema yule ofisa wa usalama kuhusiana na kutaka taarifa kutoka kwangu.
Itaendelea...
Na Bishop Hiluka
Nikiwa bado nimesimama pale nikajaribu kujiuliza, nini ilikuwa sababu ya wale maofisa wa usalama kutaka kunihoji ilhali niliamini kuwa sikuwa na kosa lolote na wala sikuwahi kuwa na historia yoyote ya uhalifu, achilia mbali kufikishwa polisi kwa tuhuma zozote.
Hata hivyo, nilipiga moyo konde huku nikijitahidi kuifukuza hofu iliyoanza kuniingia kwa kuwa nilikuwa natambua kuwa harakati dhidi ya ugaidi zilikuwa zimepamba moto na labda nilitakiwa kwa mahojiano mafupi kutaka kujua nyendo zangu.
Hapo nikakumbuka kuwa wiki mbili zilizotangulia nilikuwa nimesoma kwenye mtandao wa intaneti na baadaye kuona kwenye televisheni habari za matukio mawili yaliyodhaniwa kuwa na chembechembe za ugaidi yaliyotokea nchini Tanzania kwa kufuatana.
Tukio moja lilihusu mlipuko wa guruneti uliokuwa umetokea katika mkutano wa kampeni ya ‘Uzalendo’ ambao Waziri Mkuu ndiye aliyetarajiwa kuwa mgeni na badala yake akawakilishwa na Mkuu wa Mkoa, Daniel Luhopelo.
Katika tukio lile lililotokea katika viwanja vya Mnazi Mmoja jijini Dar es Salaam watu 6 walipoteza maisha, 83 walijeruhiwa akiwemo Daniel Luhopelo, huku 10 wakiwa katika hali mahututi.
Tukio la pili lilihusu uvamizi na uporaji wa silaha za kivita kwenye bohari kuu ya silaha iliyokuwa katika eneo la Kwembe nje kidogo ya jiji la Dar es Salaam na katika uvamizi huo askari kadhaa waliuawa.
Kwa matukio yale na mengine ambayo sikuyafahamu nikaamini kuwa walipaswa kujiridhisha kuwa hali ya amani inatamalaki nchini na mimi sikuwa tishio kwa usalama wa nchi hii, hasa kwa kuwa nilionekana mgeni.
Hata hivyo, sikujua kabisa wala sikutarajia kuwa mshtuko mkubwa ulikuwa unanisubiri mbele yangu!
Mara nikawaona maofisa usalama wawili waliokuwa wamevaa suti wakifunua makoti yao na kunionesha bastola zao zilizokuwa zimechomekwa vyema kwenye mishipi kiunoni, kisha yule kamishna msaidizi wa polisi akanitaka kunyanyua mikono yangu juu.
Niligwaya sana na mwili wangu ulianza kutetemeka lakini sikutaka kabisa kuionesha ile hali ya kugwaya, hivyo nilibaki nikiwatazama kwa makini na kuhoji kwanini ninyooshe mikono yangu juu kama mtuhumiwa wakati sikuambiwa kosa langu.
Mara nikamuona mmoja wa wale maofisa wa usalama akiitoa bastola yake na kuishika vizuri akiielekeza kwenye kichwa changu huku akiniamuru ninyooshe mikono yangu juu.
Kuona vile sikuwa mbishi, nikanyoosha mikono yangu juu nikiamini kuwa kitendo chochote cha kuendelea kuleta ubishi kwa wale maofisa wa usalama kingeweza kuyagharimu maisha yangu.
Niliponyoosha mikono yangu juu nikaamuriwa niiweke mikono kisogoni kisha nigeuke na kuuelekea ukuta. Nikafanya kama nilivyoamuriwa bila kuhoji.
Mmoja wa wale maofisa usalama akanisogelea haraka na kwa tahadhari kubwa kisha akaanza kunipekua kama nilikuwa na silaha yoyote, huku wale maofisa wengine wakiwa makini kuhakikisha sileti matata yoyote na endapo ingetokea nimeleta purukushani yoyote waweze kunituliza kwa wepesi zaidi.
Wakati nikipekuliwa nikajaribu kuhoji sababu za wao kutaka kunikamata namna ile kama jambazi sugu lakini nikaambiwa kuwa nitalijua kosa langu baadaye kwani nilikuwa nahitajika kwa mahojiano kidogo na kama ningeonekana kutokuwa na kosa basi ningeachiwa mara moja.
Sikuleta matata yoyote, hivyo nilifungwa pingu mikononi kisha nikachukuliwa hadi kwenye chumba kimoja maalumu katika jengo lile pale kiwanja cha ndege ambacho kilikuwa na utulivu wa kupita kiasi.
Na hapo tukawakuta maofisa wengine watatu ambao niliamini kuwa walikuwa ni maofisa wa usalama wa taifa walionikaribisha kwa tabasamu bashasha.
Nilisimama nikabaki kuwatazama, wakati huo wale maofisa walionileta mle ndani walikuwa bado wamenizingira huku wakiwa makini kuhakikisha kuwa sipati fursa yoyote ya kuleta rabsha.
Mpaka hapo bado sikuwa na hofu kabisa kwani nilifikiria kuwa yawezekana walikuwa wamenifananisha na mtu mwingine na baada ya mahojiano mafupi na kugundua kuwa mimi si yule mtu waliyekuwa wakimdhania basi wangeniomba radhi na kuniachia huru niende zangu.
“Kuanzia sasa upo chini ya ulinzi,” aliniambia mmoja wa wale maofisa wa usalama wa taifa tuliowakuta mle ndani, ambaye alionekana kuwa mkuu wa usalama au kiongozi wa wale maofisa wengine.
“Kwanini nawekwa chini ya ulinzi wakati hata siambiwi kosa langu ni nini?” nikauliza huku nikishangaa.
“Usijali, utaelezwa sasa hivi, keti tafadhali,” alisema yule ofisa mkuu wa usalama aliyeonekana kuwa kiongozi wa wale maofisa wengine akinikaribisha kwenye kiti kilichokuwa mbele ya meza ndefu iliyokuwa na umbo mstatili, ambayo nyuma yake lile jopo la wale maofisa usalama wa taifa walikuwa wameketi. Macho yao yote yalikuwa kwangu.
Nikaketi taratibu huku nikiyatembeza macho yangu taratibu kuwatazama wale maofisa usalama mmoja baada ya mwingine kabla ya kuweka kituo kwa yule ofisa mkuu wa usalama, ambaye wakati huo alikuwa ameketi mbele yangu tukitazamana.
Sikuwa na shaka yoyote kuwa nilikuwa nimefikishwa pale kwa sababu moja muhimu ya mahojiano wakihitaji kupata taarifa fulani walizodhani pengine nilikuwa nazifahamu.
Katika mahojiano kama yale nilifahamu kuwa ushirikiano wangu ndicho kilikuwa kitu pekee ambacho kingeweza kuniweka salama na kuniepushia matatizo zaidi, hasa ikizingatiwa kuwa katika kipindi kile harakati dhidi ya ugaidi duniani zilikuwa zimepamba moto kutokana na ugaidi kushika chati.
“Sijui nikuite Brown Senga, Godwin Sengerema au kwa jina la sasa la Maximilian Banda?” hatimaye yule ofisa mkuu wa usalama alivunja ukimya huku akinikazia macho.
Nikashangaa sana kusikia nikihusishwa tena kwa mara nyingine na jina la Brown Senga, hata hivyo, kilichonishangaza zaidi ni kuongezeka kwa jina la Godwin Sengerema. Nikajiuliza kulikuwa na nini kinaendelea kwa huyo mtu aliyeitwa Brown Senga!
Hata hivyo, pamoja na kujiuliza maswali yale nilijitahidi kuuficha mshangao wangu.
“Niite Maximilian Banda, hayo mengine si majina yangu,” nilimjibu yule ofisa wa usalama kwa sauti tulivu huku nami nikimkazia macho.
“Okay, nitakuita Maximilian kama unavyotaka…” alisema huku akiachia tabasamu.
“Kwa kifupi tulipata taarifa zako tangu tu ulipotua jijini Nairobi kwamba ulikuwa unakuja Dar es Salaam na mimi nikazipokea taarifa hizo kwa shauku huku nikiamini kuwa utatusaidia katika uchunguzi wetu wa mambo kadhaa ya kihalifu yaliyotendeka nchini wiki mbili zilizopita,” alisema yule ofisa mkuu wa usalama huku akiweka kituo kidogo na kunitazama kwa uyakinifu.
“Sina kitu chochote ninachoweza kuwasaidia kuhusu uhalifu, kwa kifupi sijui chochote,” niliongea kwa sauti tulivu huku nikiendelea kumkazia macho yule ofisa usalama.
Hata hivyo yule ofisa wa usalama alionekana kunipuuza, nilipomtazama wala sikuona tashwishwi yoyote katika uso wake.
“Pengine bado hujaelewa vizuri uzito wa jambo hili au taarifa tunazozihitaji kutoka kwako na hujui kwanini wewe upo hapa… hii ni kuhusiana na hali ya usalama wa nchi hii,” yule ofisa mkuu wa usalama akasema kwa msisitizo huku akiendelea kunitazama na macho yake yaliyokuwa yamehifadhi ghadhabu.
“Bado sijaelewa, ni nini kinachohusiana na usalama wa nchi hii ambacho mimi nina taarifa zake?” niliuliza kutaka kupata uhakika wa kile alichokuwa anakisema yule ofisa wa usalama kuhusiana na kutaka taarifa kutoka kwangu.
Itaendelea...