Ndugu yangu mpendwa Zemarcopolo, pole sana kwa hali hii inayokusibu. Mimi siungi na wala sipingi mgomo huu. Siungi kwa sababu majeruhi ni wagonjwa ambao ni ndugu,jamaa zangu na hata mimi mwenyenyewe kwa maana ugonjwa haupi hodi. Sipingi kwa sababu majeruhi wa kwanza kaitka sakata la mgomo huu wa madaktari ni UKWELI. Serikali haisemi ukweli, watanzania hawasemi ukweli na hakika tumekuwa wabinafsi mno kutojua kilio cha madaktari na watumishi wengine wa Tanzania.
Madaktari na walimu huwa wanasikilizwa labda kuliko watumishi wengine wote wa nchi hii. Sababu kubwa ni wingi wao na umuhimu wa dhahiri wa kazi zao. Watumishi wengine wengi na hata wanasiasa( sijasema wote) wamekuwa wa kihongwa/kupokea rushwa kwa kisingizio cha ugumu wa maisha. Kwa kisingizio hicho wamejilimbikizia utajiri wa kutisha kiasi kwamba hoja ya ugumu wa maisha inakosa mashiko.
Watu ambao ukwasi wao ni mkubwa hawakutani na madaktari wetu katika hospitali za serikali, hii inatoa picha kuwa madaktari wapokea rushwa wamekuwa wakipokea rushwa ya kukidhi ugumu wa maisha kwa maana halisi. Ninaongelea madaktari wanaowaona na kuwatibu wagonjwa na sio madaktari watawala wa Wizara ya afya, mashirika ya kimataifa( WHO,WB,Global Fund, TACAIDS, Benjamini Mkapa foundation, Bill Clinton foundation nk.). Rushwa ya kujikumu inayotolewa na walala hoi wa nchi hii ni kero kubwa kwa maana inawagusa watu masikini sana na walio wengi. Ndio maana inapigiwa kelele sana.
Anayesema madaktari hawafanyi kazi aende kwenye hospital za umma asubuhi aone umma unaokuwa pale ndipo atakapojua mgogoro unao wasibu madaktari wa hospitali za serikali. Asipo jipa ruhusa ya kunywa chai atashinda njaa. Na hakuna mfumo wa kumtetea. Chai hiyo anayokwenda kunywa sio chai itokanyo na mfumo ni chai inayochangiwa na mke/mme na watoto kwa maana atapunguza stahili ya familia kwa ajili ya chai, ambayo ni muhimu sana kwake ili aendelee kutoa huduma!
Ukienda BoT, Wizara ya Fedha, NHIF, LAPF, TRA, Tume ya mawasiliano,PSPF,PPF,NSSF na mashirika mengine ambayo nayo ni ya Kitanzania ukaona chai, vitafunio, soda, maziwa vivyoshushwa kutoka kwenye magari kwa ajili ya watenda kazi wa ofisi hizo, ukienda majumbani kwao ukaona nyumba bora za kifahari wanazoishi watumishi hawa, ukaona usafiri wanao utumia na ambao unamilikiwa na wao, ndipo utakapo ona kuwa utume/wito wa kazi za madaktari na walimu wetu ni dhihaka isio kuwa na mfano.
Katika mazingira kama haya kwa nini wasigome na kugomea sifa hizi bandi wanazopewa leo? Haki iko wapi?