Simulizi: Penzi ama kaburi?

Simulizi: Penzi ama kaburi?

Sehemu ya 41.

“Sasa unataka nifanye nini?”
“Umeuliza swali zuri sana....” alisema Alex, hapohapo akaanza kutoa tabasamu pana usoni mwake.

Alex alikuwa mshauri mzuri wa mahusiano, aliwasaidia watu wengi na katika kipindi hicho alijiwekea uhakika kwamba ni lazima kwa ushauri ambao angeutoa kwa msichana huyo, mwisho wa siku angeweza kubadilika kabisa.
Waliendelea kuzungumza kwa pamoja, walifurahi na wakati mwingine walikuwa wakigongesheana mikono kumaanisha walikuwa wakikubaliana kwenye kila kitu.

Shadya alikuwa msichana wa Kipemba, mzuri, mwenye mvuto wa kila aina, yaani kama ingemtia machoni mwake kwa siku moja tu basi ungekiri kwamba kwenye maisha yako utakuwa umewahi kumuona mwanamke mzuri, pengine kuliko wote uliowahi kuwaona.

Alex alizungumza naye lakini akili yake haikuwa hapo, Shadya alimchanganya na ndiyo maana hata ushauri wa kimapenzi aliokuwa akimpa msichana huyo ulimfanya kuonekana kama mwanaume fulani aliyekuwa akijua kupenda, yaani mwanamke ambaye alikuwa akitoka naye kimapenzi wakati huo inawezekana alikuwa mwenye bahati kuliko wanawake wote katika dunia hii.

Mawazo ya Shadya kwa Gibson yalipotea kwa muda, kwanza alikuwa makini na huyo Alex ambaye alikuwa akiongea kwa mbwembwe nyingi mbele yake.

Baada ya dakika kadhaa, safari ikaanza na kueleka huko walipokuwa wakielekea. Kitu kimoja ambacho kilikuja kichwani mwa Alex ni kuchukua namba ya msichana huyo, ikiwezekana, siku moja ajaribu bahati yake.

“Ila atakubali?” alijiuliza kimyakimya.
“Hawezi kukataa! Yaani ushauri wote huu niliompa akatae? Mh! Haiwezekani, ngoja nijaribu!” alijisemea Alex, hapohapo akamwambia Shadya kuhusu namba yake.
“Wewe namba ya nini?”
“Nataka nikafungie maandazi!” alijibu na kutoa tabasamu. Shadya akaanza kucheka.

“Una vituko wewe mwanaume!”
“Ila sikushindi wewe, yaani mpaka leo hujui namba ni ya kazi gani!” alisema Alex, wote wakacheka tena.
 
Sehemu ya 42.

Kwa jinsi alivyokuwa akizungumza, utani aliokuwa amemletea na mambo mengine, Shadya hakutaka kukataa kutoa namba yake, haraka sana akampa mwanaume huyo na hata alipoteremka maeneo ya huko Mwenge tayari kwa kwenda Sinza, tayari Alex alijisemea ilikuwa ni lazima amchukue msichana huyo.

Shadya akachukua bodaboda na kuanza kumpeleka katika mgahawa wa Napoleon uliokuwa Sinza Kumekucha. Mawazo juu ya Gibson yakaanza kujirudia tena kichwani mwake.

Mwanaume huyo alimchanganya, ilifika kipindi kama alianza kuwachukia wanaume wote waliokuwa wakipita mbele yake lakini kuna kipindi alijiona kufanya hivyo ulikuwa ni utoto mkubwa.

Hakuchukua muda akafika hapo, akateremka na kuelekea huko. Gibson hakuwepo, akampigia simu na kumwambia tayari alifika, hivyo akaambiwa asubiri.
Akatafuta sehemu na kukaa, akaagiza juisi na kuanza kunywa taratibu.

Moyo wake kipindi cha nyuma uliamini kabisa huyo Gibson ndiye ambaye angekuwa mwanaume wake wa kufa na kuzikana na ndiyo maana aliamua kuanza kumpotezea Ngwali kumbe hakuwa mwanaume sahihi.

Alimpenda mtu huyo, alikuwa tayari kufanya kitu chochote kile lakini si kumkosa. Aliendelea kusubiri mpaka baada ya dakika kama kumi hivi, Gibson akafika mahali hapo, akasimama na kumkumbatia.

“Unanukia vizuri!” alimwambia mwanaume huyo.
“Ahsante sana,” alijibu Gibson huku akimwangalia Shadya.
Msichana huyo akajisikia raha, hakuamini kama hatimaye alikuwa mbele ya mwanaume huyo, mtu aliyeamini alikuwa akimpenda kuliko yeyote katika dunia hii.

Alitamani kumwambia Gibson maneno yote matamu na mazuri ili aone ni kwa jinsi gani alikuwa akimpenda lakini alishindwa kumwambia hayo kwa kuwa alihitaji kusikia msimamo wake.
“Mbona umebadilika sana?” aliuliza Shadya.

“Nimekuwaje mpenzi?” aliuliza Gibson.
Shadya akaanza kulalamika kama mara ya kwanza. Gibson alikuwa kimya, siku hiyo hakutakiwa kumuonea huruma Shadya, kama angejifanya kuwa baba huruma ilimaanisha angeharibu mambo kwa Paula kwani msichana huyo angemng’ang’ania mwanzo mwisho, ilikuwa ni lazima ajivike sura ya nyani.
“Nipo bize sana!” alisema Gibson.
“Hata kwa mpenzi wako?”
 
Sehemu ya 43.

“Shadya! Maisha yananichanganya sana. Unajua unapokosa pesa wakati mwingine mpaka mapenzi huyafikirii kabisa,” alisema Gibson maneno yaliyouchoma moyo wa Shadya vilivyo, lakini akatoa tabasamu kama aliridhika na maneno hayo.

“Oh! Pole kwa ubize mpenzi! Naomba uniambie kitu kimoja,” alisema Shadya.
“Kitu gani?”
“Kuhusu msimamo wako!”
“Upi?”
“Juu yangu! Ni kwamba tunaendelea kuwa wapenzi ama basi?” aliuliza msichana huyo.

Hakutaka kujishtukia kuuliza swali hilo, kama mwanamke ilikuwa ni lazima aujue msimamo wake, kama angeona aibu kuuliza maswali hayo ilimaanisha hakuwa siriazi na maisha yake.

Ni kweli alimpenda mno Gibson lakini muda huo ulikuwa ni wakati wa kujua ukweli wake, kama kweli alihitaji kuendelea kuwa naye ama la!”
Shadya unajua na...”

“Gibson! Usirukeruke! Ninahitaji kuujua msimamo wako! Wewe ni mwanaume, niambie ukweli, sihitaji kupoteza muda kwa mwanaume ambaye sina nafasi kwake, sipendi kuumizwa, sipendi kulia, ninahitaji nijue msimamo wako!” alisema Shadya, kwa jinsi alivyokuwa akizungumza, ni kama mwanaume aliyekuwa akimwambia mwanamke.

“Naomba muda nijifikirie!”
“Gibson! Hilo ni jibu tosha kwamba sina nafasi kwako, huwezi ukahitaji muda wa kujifikiria juu yangu na wakati unajua mimi ni mpenzi wako. Mapenzi yameshuka, nashukuru kuna mambo nimejifunza kwako,” alisema Shadya huku akionekana kutia huruma.
Ghafla meseji ikaingia kwake. Ilikuwa ni ya Alex.

“Namba yangu huyo,” ujumbe ulisomeka, akausoma, hapohapo akaujibu.
“Nashukuru! Naomba nikuulize swali, nijibu haraka sana.

Kama mwanaume ameniumiza, nikiwa naongea naye, natakiwa nifanye nini ili naye achanganyikiwe?” aliandika, baada ya sekunde kama thelathini ukajibiwa.
“Kill him with your smile!” (muue kwa tabasamu lako) uliandika ujumbe kutoka kwa Alex.

“Sawa!” akaujibu.
“Tena muonyeshe kama hujaumia, yaani kuwa poa, hata kama unalia moyoni.”
“Nimekuelewa!”

Muda wote huo Gibson alikuwa kimya, alimwangalia Shadya ambaye alionekana kuwa bize kidogo na simu yake, alipouinua uso wake, ulitawaliwa na tabasamu pana.
 
Sehemu ya 44.

Gibson akashtuka, hakutarajia kuliona tabasamu hilo usoni mwa msichana huyo, alimuuliza maswali yaliyoonyesha kwamba siku hiyo ungekuwa mwisho wa uhusiano wao, alikuwa na uhakika alipendwa, lile tabasamu lilishindwa kumpa majibu sahihi, kama alikuwa akifanya hivyo, inamaanisha alifurahia ama?
“Gibson! Endelea na maisha yako baba!” alisema Shadya kwa tabasamu pana.

“Shadya!”
“Nimekupa nafasi! Unajua hakuna muda wa kulazimishana mapenzi. Mwanamke natakiwa kupendwa, kupetiwapetiwa, hakuna mwanamke anayependa kuona mpenzi wake akiwa bize, yaani bize hata huna dakika na mimi! Naomba niondoke! Najisikia furaha nafsini mwangu,” alisema msichana huyo, uso wake ulikuwa na tabasamu pana kupita kawaida.

“Shadyaaaaaa.....wait......”
Msichana huyo hakujali, akaita bodaboda, akapanda na kuondoka zake. Gibson alibaki akiiangalia bodaboda ile, alitegemea baada ya kuachana na msichana huyo angelia, angehuzunika, angekasirika lakini ndiyo kwanza alimuacha huku akiwa na tabasamu pana moyoni mwake.

Akachanganyikiwa!
Alipokuwa kwenye bodaboda hapo ndipo Shadya alipoanza kulia, moyo wake ulichoma mno, hakuamini kilichokuwa kimetokea. Alihisi akiwa na maumivu makali moyoni mwake kupita kawaida.
Aliingia pupa kwa Gibson, akamvua nguo zake kisha kumuacha.

Hapo ndipo akasikia maumivu makali ya kutengana na mtu na wakati mwingine alihisi kabisa mauamivu hayohayo ndiyo ambayo aliyasikia Ngwali kila alipokuwa akimtafuta kwa lengo la kuzungumza naye.

Akapelekwa mpaka chuo, akateremka, bodaboda alishangaa kumuona akiwa analia, hakutaka kuuliza, akachukua pesa yake na kuondoka.
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom