SEHEMU YA 43
“Naomba tuachane, naomba unisamehe kwa kukupotezea muda wako. Nahitaji kuwa huru, ninahitaji kuwa na furaha maisha yangu, najua kuna siku utakuja kujua kila kitu, ila naomba tuachane Nandy, ukipata mwanaume mwingine wa kukuoa, acha akuoe, ila naomba unisahau, naomba usahau kila kitu kuhusu mimi,” alisema Dickson kwa sauti ndogo.
Nandy alichanganyikiwa, alimwangalia Dickson mara mbili-mbili, hakuamini alichokuwa akikisikia. Yeye mwenye machozi yakaanza kumtiririka, alihisi kama alikuwa ndotoni ambapo baada ya muda fulani angeamka na kujikuta akiwa kitandani.
Dickson yuleyule aliyekuwa amemwambia kwamba anampenda, Dickson yuleyule aliyemthamini na kumruhusu autoe usichana wake ndiye ambaye alikuwa mbele yake na kumwambia kwamba waachane.
Alihisi kichwa kumuuma, alihisi kitu chenye ncha kali kikiuchoma moyo wake, pale alipokuwa akaanza kutetemeka, japokuwa mgahawa huo ulikuwa ufukweni tena wakipigwa na upepo mkali wa baridi, akaanza kutiririkwa na kijasho chembamba.
“Dickson...” aliita Nandy.
“Naomba uniache Nandy! Sistahili kuwa mume wako,” alisema Dickson, hakutaka kubaki mahali hapo, akasimama na kuanza kuondoka.
Nandy akasimama pia, akaanza kumfuata Dickson huku akimuita. Kila mtu aliyekuwa hapo akabaki akishangaa, ilikuwa sehemu tulivu, kulikuwa na wapendanao ambao walikuwa wakiongea mambo yao lakini kelele za kuita za Nandy zilimshtua kila mtu mahali hapo.
“Dickson....Dickson...” aliita, Dickson akapotea machoni pake, akashindwa kusonga mbele, akahisi miguu yake ikikosa nguvu, kizunguzungu kikamuanza, hakupiga hatua zaidi, hapohapo akaanguka na kupoteza fahamu. Hakujua ni kitu gani kiliendelea baada ya hapo.
Je, nini kitaendelea?