Simulizi:Biashara Ya Kifo

Simulizi:Biashara Ya Kifo

Sehemu ya 14

Usiku mzima Annabel alikuwa akilia, hakuamini kile kilichokuwa kimetokea, alibaki akisononeka sana, hakujua wale watu walimteka walikuwa nani na walihitaji nini. Hapo ndipo maswali mengi kuhusu Ethan yalipoanza kumjia kichwani mwake.

Yule Ethan alikuwa nani? Na kwa nini alikuwa akitafutwa vile, kila alipojiuliza alikosa jibu. Ndani ya chumba kile kulikuwa na mateso makubwa, kitendo cha kukaa mule huku kukiwa hakuna mwanga na hata sakafu kuwa na unyevuunyevu kilionekana kuwa mateso makubwa.

Ilipofika mchana, mlango ukafunguliwa na Thorn kuingia ndani, alionekana kuwa na kitu alichotaka kumwambia Annabel, alichokifanya ni kumuita na kumwambia amfuate, Annabel akafanya hivyo.

Wakaelekea mpaka katika ehemu moja iliyokuwa pembeni kabisa, aliliona jiji la Dar es Salaam huku jengo kubwa la The Prince likionekana pale alipokuwa.

Mahali hapo melini alipokuwa amepelekwa, kulikuwa na Wazungu wengine wawili, Bruno na Stephen, akawekwa kati.
“Tunamtaka Ethan,” alisema Thorn, alionekana kuwa na hasira mno. Annabel akanyamaza.

“Ungependa kuendelea kukaa kwenye meli hii zaidi?” aliuliza Bruno.
“Hapana!”
“Basi tuambie Ethan yupo wapi.”
“Aliondoka.”

“Kwenda wapi?”
“Sijajua! Kwani amefanya nini?”
“Hautakiwi kujua. Tunaomba namba yake,” alisema Bruno.

Hilo ndilo walilolitaka, kukaa na Annabel ndani ya meli ile halikuwa lengo lao, walichokita ni kumpata Ethan ambaye mpaka muda huo hawakujua alikuwa wapi. Aliteseka sana, alilia usiku kucha, kitendo cha kuambiwa kwamba ni namba ya Ethan ndiyo iliyokuwa ikihitajika, hilo halikuwa tatizo, akawapa.
“Asante,” alisema Thorn.

Akaichukua ile namba na kisha kuanza kupiga simu. Muda wote huo Annabel alikuwa akitoa kilio cha chini kilichojaa kwikwi, hakutaka kutoa namba ya Ethan lakini kutokana na mateso makubwa aliyokutana nayo ndani ya chumba kile, hakuwa na jinsi.

“Ethan, unazungumza na Thorn, tunakuhitaji wewe kabla ya saa tisa, kama hautofika, huyu msichana hautoweza kumuona tena,” alisema Thorn mara baada ya simu kupokelewa.

“Thorn, nisikilize, huyo msichana hajawafanya kitu, mwacheni aende zake,” alisikika Ethan simuni huku akilalamika.
“Ataondoka utakapokuja.”
“Thorn.....”

“Tukutane kwenye Hoteli ya Kingstar, jirani na hapo ulipo saa kumi jioni, utakaokuja, tutamwacha huru,” alisema Thorn, Ethan akashusha pumzi nzito, hapohapo Thorn akakata simu.
****
 
Ubarikiwe asee

Ngoja niagize kisindikizio kabisaaa sishushi simu chini mpaka nitakapokuwa sambamba nanyi

Nisamehe kwa ukimya, nadhani utakuwa uliniwazia kama mtu mwenye kiburi, siko hivyo haka ka silidi kalinipotea

Sent using Jamii Forums mobile app
Hapana bwana siwezi kukuwazia vibaya hivyo najua jf notification ni janga
 
Sehemu ya 15

Japokuwa Ethan alikuwa na hofu kukutana na Wazungu wale waliokuwa wamemfuata nchini Tanzania lakini hakuwa na jinsi, alitakiwa kuonana nao ili mpenzi wake, Annabel aachwe huru na yeye kufikishwa huko walipotaka kumfikisha.

Kwenda katika Hoteli ya Kingstar halikuwa tatizo na kwa sababu haikuwa mbali na hoteli aliyokuwa amefikia, alihakikisha anafika huko muda aliopangiwa pasipo kuchelewa.

Alijua kwamba alifanya kosa kubwa, kitendo cha kufanya kazi ile huku akijua kwamba aliagizwa na ndiyo ilikuwa kazi iliyomuingizia kiasi kikubwa bosi wake, lilikuwa kosa lisiloweza kuvumilika kwa bosi huyo.

Ilipofika saa tisa na nusu alasiri, tayari alikuwa katika hoteli hiyo ambapo baada ya dakika chache Thorn akatokea huku akiwa peke yake kitu ambacho hakikuwa makubaliano yao.
“Vipi?” aliuliza Ethan.

“Vipi nini?”
“Mpenzi wangu yupo wapi?”
“Subiri kwanza! Usiwe na presha.”
“Ninataka kumuona Annabel kwanza, vinginevyo siendi popote pale,” alisema Ethan huku akionekana kumaanisha alichokuwa akisema.

“Usiwe na haraka sana, sikuweza kumleta mahali hapa, inuka tuondoke, hakuna muda wa kupoteza,” alisema Thorn huku akimwangalia Ethan.
“Hapana! Siwezi kwenda popote pasipo Annabel.”

“Kweli?” aliuliza Thorn huku akionyesha bastola iliyokuwa kiunoni mwake.
Hicho ndicho kilichomuogopesha, alimfahamu vilivyo Thorn, alionekana kuwa mwanaume mpole, mwenye tabasamu wakati wote lakini roho yake ilikuwa tofauti na muonekano wake wa nje. Alikuwa mtu aliyependa sana kuua, alipenda kuwatesa watu na hata alipokuwa akipewa amri ya kuua, alilitekeleza suala hilo kwa haraka sana.

Alipoonyeshewa bastola ile, hakuwa na jinsi, hakutaka kukataa, aliamini kwamba endapo angekataa basi kungekuwa na kitu kingine kabisa na inawezekana historia ya maisha yake ikabadilikia hapo, alichokifanya ni kusimama na kuanza kuondoka na mwanaume huyo.

Walizungumza kama marafiki, Ethan hakutakiwa kuonyesha hofu yoyote ile, walipofika barabarani wakachukua teksi na kuanza kuelekea sehemu ilipokuwa boti ndogo ambayo wangeichukua na kuelekea kule ilipopaki meli ile ya mizigo.

Hawakuchukua muda mrefu wakafika ufukweni, wakateremka na kuanza kuelekea katika boti moja iliyokuwa imepakiwa pembeni, wakapanda na safari ya kuifuata meli iliyoonekana kwa mbali kuanza.

Kichwa cha Ethan kilifikiria mambo mengi, alijiwa na wazo la kutoroka kwa kuzama baharini na mwisho wa siku kupiga mbizi ili aweze kuondoka mikononi mwa Thorn ya watu hao lakini kitu kilichomsumbua moyoni mwake ni uwepo wa Annabel katika mikono ya watu hao tu.

Hakuwa tayari kurudi nchini Marekani, aliyazoea maisha ya Tanzania, alitaka kuhakikisha hapelekwi nchini Marekani kirahisi kama walivyotaka kufanya watu hao. Alitakiwa kupambana kama mwanaume lakini kitu kilichoonekana kuwa kigumu ni kwamba alikuwa na msichana Annabel tu.

“Siwezi kufanya kazi yenu tena,” alisema Ethan huku akimwangalia Thorn usoni.
“Una uhakika?”
“Ndiyo!”

“Basi tutawasiliana na mzee tumwambie, yeye atatuambia tufanye nini! Kama kukuua kwa mikono yake au atuachie sisi tukuue,” alisema Thorn.

Mashine ilizidi kuunguruma na boti ilizidi kusonga mbele, muda wote huo Ethan alikuwa akifikiria kutoroka mikononi mwa Thorn tu. Bado moyo wake haukutaka kuwa tayari kujiona akiingia nchini Marekani na kukabidhiwa mikononi mwa bwana Cook, kama mwanaume, alitakiwa kupambana, hata kama angeuawa wakati akipambana, kwake ingekuwa fahari.
Hawakuchukua dakika nyingi wakawa wamekwishafika katika meli ile ambapo wakapewa kamba ambayo wakaishika na kuanza kuingia melini mule.

Bruno na Stephan walipomuona Ethan, nyuso zao zikajaa tabasamu pana, kazi kubwa waliyokuwa wamepewa ilionekana kukamilika.
 
Sehemu ya 16

“Mmeshanipata, muacheni Annabel aondoke,” alisema Ethan.
“Haondoki mtu hapa!”

“Sasa mnataka mumpeleke Marekani akafanye nini? Hili ni suala langu na nyie, yeye hausiki na chochote kile,” alisema Ethan huku akianza kuingiwa na hasira.

“Usijali, hatofika Marekani, tutamtupa baharini, ngoja tufike kina kirefu, tukimwacha, atatoa siri na hivyo kukamatwa,” alisema Thorn.

Walichokifanya ni kumchukua Ethan na kisha kumpeleka katika chumba kile alichofungwa Annabel, alipoingizwa, hakumuona Annabel kutokana na giza nene lililokuwemo mule ndani. Giza lile tu, kwake likaonekana kuwa mateso makubwa, hakujua Annabel alikuwa wapi, alichokifanya ni kuanza kumuita.

“Annabel...” alimuita msichana huyo huku akiwasha simu yake, hata kabla msichana huyo hajaitikia, Ethan alishtukia akipigwa kibao kimoja kizito mpaka simu kumdondoka, alikuwa Annabel.

“Kwa nini umenifanyia hivi?’ aliuliza Annabel huku akimshika fulana Ethan.
“Nisikilize kwanza mp....” alisema lakini hata kabla hajamaliza sentensi yake, akashtukia akipigwa kibao kingine.

“Kwa nini? Kwa nini?” aliuliza msichana huyo, alionekana kuwa na hasira mno.
“Mpenzi! Naomba unisamehe.”
“Wewe ni nani?”
“Ethan.”

“Nakuuliza wewe ni nani?”
“Annabel subiri, punguza hasira, tutazungumza mengi,” alisema Ethan.
“Niambie kwanza, wewe ni nani na hawa ni wakina nani?’ aliuliza Annabel.

Ethan hakuzungumza kitu, alibaki kimya huku akimwangalia msichana huyo kwa msaada wa mwanga wa simu yake, ni kweli alijiona kufanya kosa kubwa, kitendo cha kumficha msichana huyo kwamba alikuwa nani na wale watu walikuwa wakina nani kilimuumiza sana.

Annabel alilia na kulia, Ethan akamsogela na kisha kumkumbatia, alikuwa msichana wake, aliyemthamini, msichana aliyekuwa na nguvu kubwa katika maisha yake, hakutaka kumuona akilia, kitendo cha kububujikwa na machozi mashavuni mwake kilimuumiza mno.
“Nisamehe mpenzi,” alisema Ethan huku akiwa amemkumbatia.

“We..we ni n..an..i..?” aliuliza Annabel kwa sauti ya kilio kilichojaa kwikwi.
“Kuna mengi ya kuzungumza ila amini kwamba umeubadilisha moyo wangu Annabel,” alisema Ethan huku akiwa amemkumbatia msichana huyo.
“Niambie wewe ni nani.”
“Mimi ni muuaji mstaafu.”
“Umemuua nani?”

“Nimeua watu wengi kabla ya kukutana na wewe ambaye umeyabadilisha maisha yangu,” alijibu Ethan kwa sauti ndogo.
“Naomba usinidanganye.”
“Siwezi kukudanganya, mimi ni muuaji,” alisema Ethan.

Hapo ndipo Ethan alipoanza kumsimulia Annabel historia fupi ya maisha yake namna alivyokuwa akifanya kazi kwa mzee Sanchez mpaka alipoacha baada ya mzee huyo kufariki na hatimaye kuhamia kwa bwana Cook ambaye aliamua kuachana naye mara baada ya kukutana na msichana huyo mrembo.

Hakutaka kumficha kitu chochote, aliona kwamba huo ndiyo ulikuwa muda wa kumwambia ukweli juu ya kila kitu alichokuwa amekifanya, vitu vilivyomfanya kuwa mahali hapo kipindi hicho.

Annabel alilia sana, alimlalamikia mno kwa kumwingiza katika matatizo, lakini katika yote hayo, aligundua kwamba kama kutokea, tayari mambo yote hayo yalikuwa yametokea na kilichobaki ni kupanga nini cha kufanya baada ya hapo.

Akamsamehe kwa kila kitu, walichokubaliana ilikuwa ni lazima watoroke, hawakutaka kufika Marekani, Ethan alimfahamu bwana Cook, alikuwa mtu mwenye roho mbaya ambaye kwenye mambo ya biashara hakuonekana kuwa na mchezo hata kidogo.

“Sitaki kufika Marekani, ikitokea ikawa hivyo, ni lazima tutauawa,” alisema Ethan huku akimshika Annabel.
“Kwa hiyo tufanye nini?”
“Ni lazima tutoroke.”
“Tutaweza?”

Yote niachie mimi, hatufiki Marekani salama, kama kutuua, bora watuue ila si kufika mikononi mwa bwana Cook,” alisema Ethan, muda huo tayari meli ikang’oa nanga na safari ya kuelekea nchini Marekani kuanza kwa kupitia Afrika Kusini.
*****
Mpango uliokuwepo ni wa kutoroka ndani ya meli ile, hawakujua ni jinsi gani wangetoroka lakini kitu pekee walichokijua ni kwamba hawakutakiwa kufika nchini Marekani.

Unyevuunyevu wa ndani ya chumba kile uliwaweka kwenye wakati mgumu, hakukuwa na mtu aliyekaa chini, walibaki wakiwa wamesimama na kila miguu ilipochoka, walikuwa wakichuchumaa tu.

Bahari ilitulia, walisikia upepo ukipiga kwa nje huku kelele ya injini ikisikika chumbani mule walipokuwa.

Hawakuwa wakijua Kaskazini ulikuwa upande gani, Magharibi wala pande nyingine za dunia.

Ndani ya meli hiyo, Thorn na wenzake walikuwa na furaha mno, hawakutegemea kama wangefanikiwa kumpata Ethan ambaye kwao alionekana kuwa lulu zaidi ya madini yoyote yale.

Walichokifanya ni kusherehekea tu, walitoa mizinga ya pombe kali na kuanza kunywa, walipongezana na kugongesheana glasi zao, kila kitu kilichokuwa kikiendelea ilikuwa ni shangwe tele.

“Hatimaye tumefanikiwa, ni lazima tutapiga hela sana tukifika,” alisema Thorn kwa sauti ya kilevi.
“Ndiyo hivyo! Kwanza tukifika Afrika Kusini tumtupe baharini yule mwanamke,” alisema Bruno.

“Sawasawa. Hakuna tatizo, hatakiwi kufika Marekani kabisa,” alisema Stephan huku akionekana kuwa mwenye furaha tele.

Hiyo ndiyo ilikuwa mipango yao, Annabel hakutakiwa kufika nchini Marekani, iwe isiwe ilikuwa ni lazima kutupwa baharini na sehemu ambayo walikuwa wameipanga ilikuwa ni Afrika Kusini, sehemu ambapo bahari mbili za Indi na Atlantiki zilipokuwa zikikutana.

Mtu ambaye alikuwa akihitajika alikuwa Ethan tu na si mwingine, kila walipokuwa wakisherehekea walikumbuka kile walichotaka kukifanya. Baada ya siku mbili, huku wakiingia na kutoka ndani ya chumba kile kwa ajili ya kuwapa chakula, wakafika nchini Malawi ambapo hawakutaka kusimama, waliunganisha na kuanza kuitafuta Msumbiji.

“Tukifika Afrika Kusini, kitu cha kwanza ni kununua pombe,” alishauri Bruno.
“Hakuna tatizo, tena pale kuna pombe nyingi, zenye ulevi wa hali ya juu, hakuna tatizo,” alisema Thorn huku kila mmoja akionekana kuwa na furaha.

Upande wa pili Ethan hakutaka kutulia, alikuwa akihangaika huku na kule, kazi kubwa aliyokuwa nayo ni kutafuta njia ya kuweza kutoka ndani ya chumba kile kilichoonekana kuwa na mateso makali.

Kulikuwa na maboksi mengi, hawakuelewa yalikuwa ni maboksi ya nini, waliachana nayo, waliyasogeza huku na kule na mishemishe za kutafuta jia ya kutokea kuendelea. Waliangalia kila sehemu ili kuona kama wangeweza kuona tundu au kitu chochote kile na waweze kujitoa lakini hawakuambulia kitu.

Kuna kipindi walikata tamaa, wakaona kwamba iwe isiwe ilikuwa ni lazima kufika nchini Marekani. Ethan akaonekana kuchoka, hakujua ni kipi kingine alitakiwa kufanya kwani chumba kilionekana kutimia.

Meli ilizidi kusonga mbele, kila baada ya masaa sita, mmoja wa Wazungu wale aliingia ndani na kisha kuwapatia chakula na kuondoka zake.

Wakati mwingine kitu alichokuwa akikifikiria Ethan ni kupambana na yeyote ambaye angewaletea chakula na hatimaye kuondoka melini humo, ila swali kubwa lililomjia kichwani, wangetorokaje na wakati walikuwa katikati ya bahari?
“Haya maboksi yana nini?” aliuliza Annabel.
 
Sehemu ya 17

“Mmmh! Hebu subiri,” alisema Ethan, hapohapo akaanza kufungua boksi moja baada ya jingine, alichokikuta ndani hakuamini, kulikuwa na dola nyingi zilizokuwa zikisafirishwa kuelekea nchini Marekani, kwa maana hiyo aliona kwamba kama wangefanikiwa kulichukua hata boksi moja, basi wangekuwa matajiri.

“Utajiri huu,” alisema Ethan huku akionekana kushtuka.
“Fedha za nani hizi?”

“Atakuwa bwana Cook! Ni mtu anayejishughulisha na biashara nyingi haramu, bila shaka hizi ni fedha zake zilizotoka Afrika na Asia, kama itawezekana, tunaondoka na zote,” alisema Ethan.

“Kivipi? Tutaweza?”
“Niachie mimi.”
*****

Askofu Benedicto alichanganyikiwa, hakujua ni kitu gani kilichokuwa kikiendelea, akili yake haikutulia, mawazo yalimsonga sana na muda wote alikuwa akimfikiria binti yake tu. Hakujua mahali alipokuwa, kitendo cha Ethan kumsimulia historia ya maisha yake ilimuogopesha na kubaki akijiuliza huyo bwana Cook alikuwa nani.

Kitu alichokifikiria na ambacho kilikuja kwa haraka kichwani mwake ilikuwa ni lazima aende kituo cha polisi na kutoa taarifa juu ya kupotea kwa binti yake, swali pekee lililokuja kichwani mwake, akifika huko aseme nani aliyepotea? Binti yake? Ugumu ukawa hapo.

Japokuwa alikuwa na swali hilo gumu lakini hakutaka kujali, alichotaka kukiona ni binti yake akiwa mikononi mwake tu.

Kila kitu kilichokuwa kikiendelea kilikuwa siri yake, hakutaka kumpa taarifa Irakoze kwa kuamini kwamba angechanganyikiwa katika masomo yake, alipoulizwa kwamba Annabel aliendeleaje, alimwambia anaendelea vizuri.

“Karibu baba askofu,” alisema polisi mmoja aliyekuwa kaunta.
“Asante sana, nimekuja kutoa taarifa,” alisema askofu Benedicto.

“Taarifa gani askofu?”
“Mtoto wa dada yangu ametekwa,” alijibu askofu.

Hapohapo polisi akachukua daftari na kuanza kuandika maelezo ya askofu Benedicto.

Alikuwa mtu mwenye jina kubwa, aliyejulikana sana hata zaidi ya masupastaa wengine, kuwa kiongozi wa dini katika dhehebu kubwa kulimfanya kuwa na jina Afrika Mashariki nzima.

Polisi wengine ambao walimuona mahali pale wakamsogelea na kuanza kuzungumza naye, kila mmoja alijisikia fahari kuwa karibu na askofu huyo kiasi kwamba wengine wakadiriki hata kupiga naye picha za ukumbusho kwani kumuona tofauti na kanisani lilikuwa jambo gumu.

“Hakuna tatizo askofu, tutaanza kufanya kazi,” alisema polisi yule.
“Nitashukuru sana. Ila kwanza anzeni na huyu Ethan, kuna mengi anafahamu,” alisema askofu.

Katika maelezo aliyoyatoa kituoni hapo alimwandika mpaka Ethan na kuwaambia mahali alipokuwa akipatikana, alipanga katika Hoteli ya New Africa iliyokuwa Posta jijini Dar es Salaam.

Walipoambiwa hivyo, hapo ndipo walipoanza kufuatilia, wakawaita polisi wawili ambao walishughulika sana na masuala ya kipelelezi na kuwaambia waanze kufuatilia huko ili kujua ni wapi pa kuanzia.

Walipofika huko, wakamuulizia Ethan ambapo wakaambiwa kwamba alikuwepo ila mchana wa siku iliyopita aliondoka kuelekea katika Hoteli ya Kingstar ambapo hakukuwa mbali na hapo ilipokuwa hoteli hiyo.

Wakaelekea katika hoteli hiyo, vyote hivyo walitaka kufahamu mahali alipokuwa Ethan, walipofika na kujitambulisha kisha kuulizia, wakachuuliwa na kupelekwa katika chumba kimoja kilichokuwa na kompyuta tano na kisha kuambiwa wakae vitini.

Hapo, wakaanza kuonyeshewa video kadhaa za siku iliyopita kutoka katika kamera za CCTV zilizokuwa katika maeneo makubwa ya hoteli hiyo.

Walimwona mwanaume mmoja akizungumza na Mzungu, walikuwa ni watu pekee waliokuwa wakizungumza katika muda huo walioambiwa.

Walichokifanya ni kuanza kuwafuatilia kwa ukaribu ili kuona baada ya hapo ni kitu gani kilifuata. Walizungumza kadhaa, walionekana kama kutokukubaliana kitu fulani.

Polisi wale wakawaangalia vizuri ndipo walipomuona Mzungu yule akimuonyeshea bastola Ethan kwa siri.
“Kuna kitu,” alisema polisi mmoja.
“Hata mimi! Hebu tucheki kwanza,” alisema polisi mwingine.

Waliendelea kufuatilia kila hatua, waliwaona watu wale wakisimama na kuondoka, wakajua kwamba kulikuwa na sehemu waliyokuwa wakienda na Ethan alikuwa akifuata kwa kuwa alionyeshewa bastola.

Kwa mbali wakawaona wakiingia kwenye teksi moja na kuondoka mahali hapo, walipoelekea, hawakujua palikuwa wapi. Hawakutaka kukaa mahali hapo, walichokifanya ni kutoka na kuelekea kule kulipokuwa na teksi.

Walitaka kufahamu kile kilichokuwa kimeendelea baada ya hapo, walitaka kufahamu mahali walipoelekea, walichokifanya ni kumuuliza dereva teksi mmoja katika ya wengi waliokuwepo mahali hapo.

“Mzungu! Jana, labda aulizwe Ahmad,” alisema dereva teksi mara baada ya kuulizwa kuhusu Mzungu wa jana yake.
“Huyo Ahmad yupo wapi?”
“Yupo kule mbele. Teksi ile kule,” alijibu huku akiionyooshea kidole.

Walichokifanya ni kumfuata huyo Ahmed na kuanza kumuuliza kuhusu Mzungu wa jana ambaye alimkodi kwenye teksi yake akiwa na kijana mmoja wa Kiafrika.
“Mmmh! Kuna nini jamani? Gaidi nini?” aliuliza Ahmed.

“Kwa nini?”
“Jana yule Mwafrika hakuwa akijiaminiamini, nyie nao mnanitia wasiwasi,” alijibu Ahmed.
“Uliwapeleka kuelekea wapi?”
“Coco Beach!”

“Mmmh! Kufanya nini huko?”
“Sijui! Niliachana nao hapo, wakawa wameelekea ufukweni, sijui walikwenda kuogelea!” alijibu Ahmed.

“Hebu tupeleke huko,” alisema polisi mmoja, wakaingia ndani ya teksi ile na kuanza kuelekea huko Coco Beach, kila walipojifikiria sababu iliyowafanya kwenda ufukweni, wakakosa jibu.
****
 
Sehemu ya 18

Wapelelezi wale hawakutaka kubaki mahali hapo, walichokifanya ni kuondoka kuelekea ufukweni huko ili waone kama wangeweza kupata kitu chochote ambacho kingeweza kuwasaidia. Walipofika Osterbay, wakaanza kuelekea katika ufukwe wa Coco.

Huko, hawakuona dalili zozote za kuwepo kwa watu hao, walichokifanya ni kuwauliza vijana fulani ambao makazi yao makubwa yakiwa huko huku vichwa vyao vikiwa na mipango ya kuzamia na kwenda Ulaya au Marekani, vijana hawa walijiita Beach Boys.

“Nani huyo?” aliuliza kijana mmoja mara baada ya kuulizwa kuhusu Ethan na Mzungu yule.
“Kijana mmoja alifika hapa akiwa na Mzungu!”

“Mmh! Wala sijamuona, ilikuwa lini?”
“Jana!”
“Sijui kwa kweli, kawaulize beach boys wengine, wale pale,” alisema kijana mmoja huku akiwanyooshea vidole wenzake.

Wapelelezi wale hawakuwa na jinsi, walichokifanya ni kuwasogelea vijana hao wengine na kuwauliza, hawakuwa wamewaona watu hao, waliuliza na kuuliza na mwisho wa siku kuamua kuondoka zao.
“Kwa hiyo!”

“Tukatoe taarifa kwamba tunaendelea, tutampata tu,” alisema mpelelezi mmoja wakati wakiwa wanarudi.
*****
Meli iliendelea kukata mawingu, mateso ndani ya chumba ile yalikuwa makubwa mno. Ethan hakutaka kuendelea kubaki ndani ya chumba kile, kitu alichokifikiria kwa kipindi hicho ni kutoroka huku akiwa na mpenzi wake, Annabel na fedha zilizokuwa kwenye maboksi waliyokuwa nayo ndani ya chumba kile.

Bado akili yake ilikuwa ikisumbuka ni kwa namna gani angeweza kufanikiwa kutoka ndani ya chumba kile salama, aliendelea kupekua huku na kule lakini kikafika kipindi akachoka, hakutaka kuendelea tena, akaacha kwa kuamini kwamba singeweza kufanikiwa.

“Vipi?” aliuliza Annabel.
“Yaani nimeshindwa kujua chochote kile,” alisema Ethan.
“Kwa hiyo tumeshindwa?”
“Inawezekana.”

“Na kwa hiyo tunarudi Marekani?”
“Kurudi haiwezekani, hata kama tumeshindwa, sawa, ila kurudi Marekani, haiwezekani,” alisema Ethan.

Walitumia wiki nzima na ndipo meli ikaanza kuingia Afrika Kusini. Thorn na wenzake walifurahi sana kwani waliamini baada ya hapo, wangeanza safari nyingine ya kuelekea Marekani kwani wangafanikiwa kutoka kwenye Bahari ya Indi na kuingia kwenye Bahari ya Atlantika ambayo ndiyo ilikwenda mpaka nchini Marekani.

Walipofika umbali wa kilometa ishirini kabla ya kuifikia Bahari ya Atlantiki, walichokifanya ni kushusha boti walizokuwa nazo kisha kuelekea nchi kavu kwa ajili ya kununua pombe na kunywa.

Walipofika katika Mji wa Nangame katika Jimbo la Kwa Zulu Natal, wakanunua pombe kali huku wakitumia siku hiyo kulala na wanawake ambao kwao waliwapa kipaumbele huku kule melini wakiwa wamewaacha nahodha na wafanyakazi wake kwa kuamini kwamba ulinzi ungeimarishwa.

Ndani ya meli bado Ethan alikuwa akijifikiria namna ya kutoka ndani ya meli hiyo, chumba kilikuwa na giza mno, hakuweza kujua mahali walipokuwa na walikuwa wakielekea wapi.

Walipofika karibu na Nangame, sehemu ambayo meli ile ilisimama kwa siku nzima, Ethan akashtuka, haikuwa kawaida meli kusimama, tena injini zikiwa zimezimwa kabisa, hapo akajua kwamba walikuwa wamefika sehemu na kuweka kituo.
“Meli imesimama?” aliuliza Ethan.

“Umejuaje?”
“Unasikia injini ikilia?”
“Hapana!”
“Itakuwa imesimama, inamaanisha kwamba tumefika kwenye kituo,” alisema Ethan.

“Kwa hiyo tufanye nini?”
“Kama tupo kwenye kituo, hawa watu hawatakuwepo, hebu subiri,” alisema Ethan.

Alichokifanya ni kuusogelea mlango na kisha kuanza kuugonga. Aliugonga kwa dakika kadhaa mara akasikia sauti za miguu ya mtu ikija kule walipokuwa, alichokifanya ni kusikilizia mpaka pale sauti zile zilipoacha kusikika mara baada ya kuufikia mlango ule.

“Kuna mtu humu?” ilisikika sauti ikiuliza.
“Ndiyo! Kuna mtu.”
“Wewe ni nani? Mzamiaji?”
“Hapana!”

“Kumbe wewe ni nani?”
Ethan hakujibu kitu, kwanza akabaki kimya, kitu kilichomjia kichwani mwake ni kwamba mtu huyo hakujua uwepo wao ndani ya meli ile na ndiyo maana alikuwa na maswali mengi ambayo ndiyo yaliyomuonyeshea kile alichokuwa amekifikiri.

“Mimi ni mzamiaji kaka,” alisema Ethan.
“Si umesema wewe si mzamiaji?”
“Mimi ni mzamiaji kaka.”

“Sawa! Ulikuwa unakwenda wapi?”
“Popote pale, nilitaka kwenda Ulaya tu.”
“Haiwezekani! Ni lazima nikushushe,” alisema jamaa yule.
“Kwani hapa ni wapi?”
“Afrika Kusini.”

“Hapahapa kaka kunatosha, wewe nishushe tu kisiri, hata hapa natumaini nitaishi kama nipo Ulaya,” alisema Ethan.
“Unajua kupiga mbizi?”
“Najua sana tu, nisaidie kaka, naomba unisaidie” alisema Ethan.

Aliongea kwa kujiamini sana kiasi kwamba ingekuwa ngumu kugundua kwamba mtu huyo alikuwa akidanganya, kijana huyo, pasipo kujua uwepo wa watu hao humo ndani akawafungulia mlango huku lengo lake likiwa ni kumtorosha kisiri ili asiweze kuonekana na watu wengine kwa kujua kwamba angeweza kuuawa.

Ile alipofungua mlango tu, akajikuta akivutwa ndani, akazibwa mdomo wake, akabaki akikukuruka kwa kutaka kujitoa mikononi mwa Ethan lakini hakufanikiwa, alishikwa vilivyo.

“Nisikilize,” alisema Ethan.
“Nakusikiliza, naomba usiniue,” alisema kijana yule huku akiogopa.
“Sina haja ya kukuua, nisikilize, ninataka boti ya kuondoka humu ndani,” alisema Ethan.
 
Sehemu ya 19

“Boti...boti...haturuhusiwi kuzitoa.”
“Hapana! Lazima utoe hata moja, ninataka ufanye hivyo, ninahitaji kuondoka humu,” alisema Ethan, hata sauti yake aliibadilisha na kuwa nzito.
“Naomba usiniue,” alisisitiza kijana yule.
“Sihitaji kukuua. Nitakupa fedha ili unisaidie,” alisema Ethan.
“Sawa.”

Alichokifanya ni kuyafuata maboksi yale, akalichana boksi moja na kisha kutoa bunda moja la dola laki moja na kisha kumpelekea kijana yule na kumgawia. Zilikuwa fedha nyingi mno ambazo asingeweza kuzipata hata kama angefanya kazi mfululizo ndani ya meli ile. Tamaa ikamuingia.
“Ukinifanyia kazi yangu, nakupa nyingine.”

“Kazi gani? Nipo tayari.”
“Ninahitaji kupata boti kwanza,” alisema Ethan.
“Mmmh!”
“Ni ngumu kuipata?”

“Ni ngumu sana, niambie kingine.”
“Nataka kwenda kwenye chumba cha chini ambacho kitanifanya niyaone maji vizuri kwa kupitia kwenye dirisha dogo,” alisema Ethan.

“Sawa. Ila ili iweje?”
“Unataka hela hutaki?”
“Nataka!”

“Subiri!” alisema Ethan na kisha kulifuata boksi lile na kutoa bunda jingine la fedha na kumpatia kijana yule.
“Inawezekana?”

“Bila shaka, inawezekana,” alisema kijana yule.
“Nitataka uje kunifungulia mlango wakati meli inaanza kuondoka,” alisema Ethan.
“Hakuna tatizo.”

Kila kitu kilichokuwa kikifanyika ndani ya meli hiyo ilikuwa siri kubwa. Bwana Cook alikuwa akijihusisha na biashara nyingi haramu za madawa ya kulevya na ngozi za binadamu, hakukuwa aliyekuwa akilifahamu hilo katika meli ile zaidi ya nahodha ambaye alimwamini sana.

Ndani ya meli ile kulikuwa na maboksi matano, yote yalijaa fedha kutokana na malipo aliyokuwa amelipwa barani Asia na Afrika. Fedha hizo alitaka kuzisafirisha kwa kutumia meli kwani aliogopa kutumiwa benki kwa kuhofia kushtukiwa hivyo kufuatiliwa.

Wafanyakazi wengine hawakujua hilo, walichokuwa wakikijua ni kwamba wao walikuwa wavuvi wa samaki wakubwa. Uwepo wa Ethan na Annabel ndani ya meli ile ilikuwa siri kubwa mno, hakukuwa na aliyekuwa akifahamu zaidi ya nahodha tu.

Hata uwepo wa maboksi yale yaliyokuwa na fedha ilikuwa siri kubwa, hakutakiwa mtu yeyote afahamu hilo kutokana na uaminifu kuwa mdogo. Hiyo ndiyo ilikuwa sababu ya kijana yule kudanganyika kirahisi kwamba Ethan alikuwa mzamiaji aliyetaka kuelekea Marekani au Ulaya.
Alipopewa fedha zile, alishangaa, zilikuwa nyingi, ilikuwaje mzamiaji awe na fedha nyingi kiasi kile?

Hakutaka kujiuliza maswali mengi, alichokiagalia ni fedha tu, hivyo akataka kufanya kama vile Ethan alivyotaka afanye, wakati meli inaondoka, akamchukua na kumpeleka katika moja ya vyumba vilivyokuwa chini ambapo huko tungesema kwamba kilikuwa chini ya bahari.
****
 
Sehemu ya 20

Siku ya kwanza ikakatika, ya pili kuingia na hatimaye wiki nzima, bado hakukuwa na taarifa za kuridhisha kutoka kwa polisi juu ya kile kilichokuwa kimeendelea katika upepelezi wao juu ya Annabel.

Kila alipokuwa akienda kituoni kuulizia, askofu hakupewa majibu ya kueleweka, alikuwa akiambiwa hivi na vile, njoo kesho bado wapelelezi wetu wanaendelea kufuatilia. Hakuwa na amani, alikosa furaha, hakujua ni kitu gani alitakiwa kukifanya ili aweze kumpata binti yake.

Hakutaka kumwambia Irakoze kwani alijua ni kwa jinsi gani angechanganyikiwa, alichokifanya ni kufuatilia kimyakimya na mwanamke huyo kila alipokuwa akiuliza, jibu lilikuwa lilelile kwamba Annabel anaendelea vizuri.

“Naomba nizungumze naye mana’ke simuni hapatikani,” alisikika Irakoze.
“Amelala! Akiamka nitakupa uongee naye,” alisema askofu Benedicto.

Kila siku alikuwa akidanganya huku akifuatilia kituoni lakini majibu yalikuwa yaleyale. Kwa sababu polisi walimfahamu sana askofu Benedicto, walichokifanya ni kutoa taarifa katika vituo vingine na hata kwenye vyombo vya habari ambapo huko wakatangaza kwamba kulikuwa na msichana aliyekuwa ametekwa na kupelekwa pasipojulikana.

Watu wakashtuka, hawakuamini kama kweli katika Tanzania hii kungekuwa na mtu ambaye angetekwa kwani mambo kama hayo yalikuwa yakisikika nchi za nje tu.

Kitendo cha picha za Annabel kuanza kusambazwa kwenye magazeti mbalimbali, askofu akahofu na kuona kwamba Irakoze angegundua kile kilichokuwa kikiendelea, alichokifanya ni kumpa taarifa tu kwani hakuwa na jinsi.
“Unasemaje?”

“Annabel hajulikani alipo.”
“Tangu lini?”
“Majuzi, yaani hapa nimechanganyikiwa,” alisema askofu.
“Nakuja,” alisikika Irakoze na kukata simu.

Hakuwa na jinsi, alitakiwa kufanya kile alichokifanya, alijua kwamba Irakoze angeumia sana lakini hakukuwa na jinsi, alitakiwa kumwambia kila kitu kilichokuwa kimetokea. Baada ya masaa mawili, Irakoze alifika nyumbani hapo, macho yake yalikuwa mekundu kwa sababu ya kulia sana.

“Niambie binti yangu yupo wapi,” alisema Irakoze huku akibubujikwa na machozi.
“Subiri kwanza.”

“Niambie binti yangu yupo wapi,” alisema Irakoze na kuanza kulia kwa sauti kubwa.
Askofu akapata kazi kubwa ya kuanza kumbembeleza, ni kweli alitakiwa kulia, mapenzi mazito aliyokuwa nayo kwa binti yake yalimfanya kuumia mno pale aliposikia kwamba alikuwa ametekwa na watu wasiojulina.

Alichokifanya askofu ili kujiondoa lawama ni kumwambia Irakoze kila kitu kilichokuwa kimetokea hasa kuhusu Ethan aliyeonekana kuwa chanzo cha kila kitu.

Irakoze akajikuta akichukia, akamchukia Ethan kuliko mtu yeyote yule, hakuamini kama uwepo wa mwanaume yule ndiyo ungemfanya binti yake kutekwa na kutokujulikana mahali alipokuwa.

Alipouliza kuhusu Ethan, hata naye hakuwa akijulikana alipokuwa, hilo likamuumiza zaidi na kuona kama tayari binti yake alikuwa ameuawa na watu hao. Akajilaumu kwa kitendo cha kumwamni Ethan na kumpa nafasi ya kufika nyumbani pale huku wakati mwingine wakimwacha na binti yao.

Hawakujua wafanye nini, huo haukuwa muda wa kulaumiana au kujutia kile kilichokuwa kimefanyika, walichotakiwa kukifanya kwa wakati huo ni kukubaliana na ukweli kwamba binti yao hakuwa mikononi mwao.

Irakoze hakurudi tena chuoni, akaamua kuachana na masomo hayo na kuwa mwanamke wa nyumbani tu. Kichwa chake kilichanganyikiwa mno, kila wakati alikuwa mtu wa majonzi na hakuweza kunyamaza, alikuwa mtu wa kububujikwa na machozi tu.

Siku ziliendelea kukatika, Askofu Benedicto hakutaka kundoka nyumbani hapo, hakutaka kwenda kanisani na siku zte alitoa udhuru kwamba kulikuwa na kitu alichokuwa akikifanya hivyo asingeweza kwenda kanisani kitu ambacho hakikuwa na tatizo lolote lile.

“Annabel atarudi tu, atapatikana wala usiwe na wasiwasi,” alisema askofu huku akimwangalia Irakoze usoni. Mwanamke huyo hakuzungumza kitu zaidi ya kulia tu.
*****

Walipomaliza kunywa pombe na wanawake wao, wakawachukua na kwenda nao hotelini ambapo huko wakalala huku wakifanya nao anasa usiku mzima. Asubuhi na mapema waliamka huku pombe zikiwa kichwani, hawakutaka kubaki mahali hapo, walichokitaka ni kuondoka kuelekea nchini Marekani, safari ndefu ambayo ingewachukua hata miezi miwili baharini.

Walipoondoka hotelini, wakaelekea ufukweni ambapo wakachukua boti zao na kuanza kurudi kule ilipokuwa meli yao, umbali wa kilometa mbili kutoka pale walipokuwa.

Ndani ya boti walikuwa na mizinga ya pombe kali, walikuwa wakisherehekea huku wakigongesheana chupa zao kwa furaha kubwa.

Walichukua dakika kumi kuifikia meli ile ambapo wakarushiwa kamba na kisha kuingia melini huku wafanyakazi hao wakifanya machakato mzima wa kuipandisha boti ile melini.
“Wale wapumbavu wapo?” aliuliza Thorn kwa sauti ya kilevi, alikuwa akimuuliza nahodha.

“Wapo!”
“Mmewapa chakula?”
“Hapana!”
“Kawapeni! Yule mwanamke hana muda mrefu atakufa, tunataka kumtupa baharini katika mpaka wa bahari,” alisema Thorn.

“Sawa!”
Kwa kuwa uwepo wa watu hao ndani ya meli ile ilikuwa siri kubwa, nahodha akaenda peke yake huku akiwa ameshika sinia lililokuwa na chakula, alipofika nje ya mlango ule, aliufungua kisha kulitupia sinia lile ndani na kisha kuufunga na kurudi.

“Tayari?” aliuliza Thorn.
“Ndiyo! Nishawatupia.”
“Sawa.”
 
Sehemu ya 21

Usiku ulikuwa umeingia, safari ya kuelekea nchini Marekani ilikuwa ikiendelea kama kawaida. Walikuwa wamebakiza umbali wa kilometa kama kumi ili kufika katika eneo ambalo bahari ya Indi ilikuwa ikikutana na Bahari ya Atlantiki, sehemu pekee ambayo walipanga kumtupa Annabel na kuendelea na safari yao.

Kila mmoja melini alionekana kuwa na furaha tele, walikuwa wakigongesheana chupa zao na kuendelea kunywa huku wakipiga kelele ambazo zilionekana kuwa kero kwa wafanyakazi ambao hawakuwa wakinywa kama wao.

Kijana ambaye tayari mfukoni mwake alikuwa na dola laki mbili kila wakati alikuwa akiangalia saa yake tu, alikuwa akisubiri muda ambao angekwenda kumtoa Ethan na kumpeleka katika chumba ambacho alitaka kwenda.

Ilipofika saa mbili usiku, harakaharaka akaelekea katika chumba kile, alichokifanya ni kuufungua mlango na Ethan kutoka huku akiwa amelivua shati lake na kulifunga kiunoni tayari kwa kufanya kile alichotaka kukifanya.
“Vipi?”
“Nipo tayari! Twende.”

Kijana yule akamchukua Ethan kisiri tena huku wakati mwingine akijificha kila aliposikia watu wakija upande waliokuwepo, walitembea mpaka walipofika katika mlango mkubwa ambapo hapo alimfungulia na kumwambia aingie ndani.

“Tuingie wote.”
“Kwa nini?”
“Wewe tuingie,” alisema Ethan na kijana yule kuingia naye.

Walipofika ndani, Ethan hakutaka kujificha, alimwambia kijana yule kile alichotaka kukifanya, alimwambia dhahiri kwamba hakuwa mzamiaji kama alivyomwambia bali alikuwa mtu aliyetekwa ambaye alikuwa akirudishwa nchini Marekani tayari kwa kuuawa.

Kijana yule alibaki kimya akimsikiliza. Yeye mwenyewe akabaki akishangaa kwani ndani ya meli ile hakukuwa hata na mfanyakazi mmoja aliyekuwa akijua kama humo ndani kulikuwa na mtu ambaye alikuwa akipelekwa nchini Marekani.

“Huyo mwanamke yupo wapi?”
“Nimemuacha ndani,” alijibu Ethan.
“Sawa! Kwa hiyo unataka kufanya nini mpaka umeniambia nikulete humu?” aliuliza kijana yule.

“Nataka kuzamisha meli.”
“Unasemaje?”
“Nataka kuzamisha meli, sipo tayari kurudi nchini Marekani,” alisema Ethan.
“Utaizamishaje?”

“Unakiona kidirisha kile cha kioo?”
“Ndiyo!”
“Unayaona yale maji?”
“Ndiyo! Basi ndivyo nitakavyofanya, kwa kuwa chumba hiki kipo chini, yaani chini ya bahari kwa chini, nikipasua kioo kile, maji yataingia, basi na meli itazama,” alisema Ethan.

“Mmmh!”
“Ndiyo hivyo, andaa boya lako, hakuna kurudi Marekani hapa, baada ya hapa, mimi, wewe na mke wangu tutaondoka, nenda kaandae boti tayari kwa kuondoka nayo, meli itakapoanza kuzama, njoo na boti katika upande wa chumba chetu, baada ya hapo, nakuahidi utakwenda kuwa milionea. Sawa?” aliuliza Ethan.
“Sawa!”

Kazi ikabaki kwa Ethan, akaanza kukivunja kioo kile kigumu kwa kutumia kipande cha chuma kilichokuwa pembeni. Japokuwa kilipiga kelele sana lakini hakukuwa na mtu aliyesikia kutoka na chumba kile kuwa karibu na injini ya meli hiyo.

Wala hazikupita dakika nyingi, kioo kile kikaanza kutoa ufa, Ethan hakuacha, aliendelea kukipiga zaidi na zaidi na baada ya muda fulani, kioo kile kikaachia na maji kuanza kuingia ndani ya meli ile, hakutaka kukaa hapo, alichokifanya ni kuufungua mlango na kuanza kutoka kwa kunyata kuelekea ndani ya chumba kile alichokuwemo Annabel.
 
Back
Top Bottom