Simulizi:Biashara Ya Kifo

Simulizi:Biashara Ya Kifo

Shunie

JF-Expert Member
Joined
Aug 14, 2016
Posts
157,400
Reaction score
465,165
Mtunzi Nyemo Chilongani sehemu ya 01

SEHEMU YA 01

Mvua kubwa ilikuwa ikinyesha, mitaro midogo ikaanza kujaa maji huku baridi likianza kupiga kwa nguvu ndani ya jiji la Dar es Salaam.

Waliokuwa ndani ya nyumba zao, wakajifungia huku wale waliokuwa barabarani wakinunua miamvuli kwani mvua ile kubwa haikuonekana kuwa na dalili za kupungua hata mara moja.

Watu wengine walikuwa wakikimbilia sehemu zilizokuwa na uwezo wa kuzuia wasilowanishwe na mvua hiyo, wengine, walikubaliana na kile kilichokuwa kikiendelea hivyo kuendelea na kazi zao au safari zao huku wakiendelea kulowa.

Nje ya nyumba moja kubwa, msichana mrembo, mwenye sura nzuri, aliyekuwa na umbo lenye mvuto ambalo vijana wa sasa wangeliita namba nane alikuwa amesimama huku mkononi mwake akiwa ameshika furushi la nguo lililokuwa na nguo nyingi zilizofungwa kwa khanga.

Pale alipokuwa, macho yake yalikuwa mekundu, alikuwa na kitu moyoni mwake, hakuonekana kuwa mwenye furaha hata mara moja, baada ya dakika chache, machozi yale yaliyojikusanya machoni mwake yakaanza kumbubujika mashavuni mwake.

Msichana huyu aliitwa kwa jina la Irakoze, baba yake alikuwa Mnyarwanda na mama yake alikuwa Mnyaturu kutoka mkoani Singida.

Historia ya maisha yake ilianzia mbali, miaka miwili iliyopita, alikuwa akiishi mkoani Singida ambapo baadaye mwanamke aliyeitwa kwa jina la Hadija aliyetoka jijini Dar es Salaam akafika kijijini kwao na kumchukua kwa lengo la kwenda kufanya kazi katika nyumba yake iliyokuwa Magomeni jijini Dar.

Hilo ndilo lilikuwa lengo lake, aliporuhusiwa kumchukua, akaenda naye Dar ambapo huko baada ya kuishi kwa mwezi mmoja tu, wanaume wakaanza kumtongoza kwani ule urembo aliokuwa nao ulimvuta kila mtu aliyekuwa akimwangalia.

Uoga ulimjaa moyoni mwake, maneno aliyopewa na Bi Hadija kwamba kama angefanya ujinga na wanaume hao basi angefukuzwa na kurudishwa kijijini, ukamuogopesha na hivyo kila mwanaume aliyemfuata, alimwambia kwamba hamtaki.
Screenshot_20190325-153457.jpeg
 
SEHEMU YA 02

Ilimsaidia, aliendelea kunawiri kila siku lakini baada ya mwaka na miezi minne kukatika, mume wa Bi Hadija, mzee Saidi akashindwa kuvumilia, umbo matata alilokuwa nalo Irakoze likamchanganya, kila alipokuwa akimuona, akashindwa kuvumilia, hivyo akaanza kumzengea.

Visa vikaanza, mzee Saidi akashindwa kuvumilia, umbo la msichana yule na sura yake vilimchanganya mno hivyo kuanza harakati zake ndani ya nyumba. Kitu cha kwanza kabisa alichokifanya ni kuomba likizo kazini, alitaka awe anabaki nyumbani na binti huyo afanye yake wakati mkewe akiwa kazini.

“Unaogopa nini Irakoze? Hebu sogea hapa kitandani,” alisema mzee Saidi, pepo la ngono lilimshika, hakutaka kuelewa kitu chochote kile, mwili wake uliwehuka, kila alipomwangalia Irakoze, alimchanganya, umbo lake, makalio yake yaliyojaajaa yalimuacha hoi, hakutaka kukubali.

“Sitaki baba, sitaki,” alisema Irakoze huku akijifanya kubisha mlangoni alipokuwa amesimama, cha ajabu, hakutaka kutoka chumbani humo.

Mzee Saidi hakutaka kulaza damu, tayari aliona kila kitu kilikuwa sawa japokuwa hakuweka usiriazi katika kumlaghai msichana huyo kuja kitandani pale alipokuwa, alichokifanya ni kusimama na kuanza kumsogelea, alipomfikia, akamshika mkono na kuanza kumvutia kwake, muda wote huo Irakoze alikuwa akiangalia chini, uso wake ulijawa na aibu mno.

“Naogopa baba,” alisema Irakoze.
“Unaogopa nini?”
“Mama atajua.”
“Atajuaje? Utamwambia?”
“Hapana!”
“Sasa atajuaje?”

Irakoze akakosa jibu, ukimya wake ulikuwa ni kama jibu lililomruhusu mzee Saidi kufanya kile alichotaka kukifanya, akamvuta, msichana huyo, akaanza kupiga hatua kuelekea kitandani, kilichofauata ni kufanya mapenzi kitandani hapo.

Huo ulikuwa mwanzo wa kudokoa asali, baada ya hapo, wakajikuta wakiingia kwenye dimbwi zito la mahaba, kila siku mzee Saidi alipokuwa akiamka, mtu wa kwanza aliyetaka kumuona alikuwa Irakoze tu.

Penzi la msichana huyo likamlevya, hakutaka kusikia chochote kile, alichokuwa akikitaka ni mapenzi motomoto tu. Hata mzee Saidi aliporudi kazini, kuna siku alikuwa akitoroka kazini na kurudi nyumbani, huko, alikuwa akifanya mapenzi na msichana huyo tu.
 
SEHEMU YA 03

Kila kitu kilichokuwa kikiendelea ndani ya nyumba kilikuwa siri kubwa, Bi Hadija hakugundua chochote kile kwani maigizo waliyoyafanya wawili hao yalimpigwa upofu mkubwa, hakujua kama nyuma ya pazia alikuwa akiibiwa.

“Lakini nilikwambia kwenye simu mke wangu!” alisema mzee Saidi, alikuwa kilalamika.

“Najua mume wangu, ila nikasahau kabisa kumwambia Irakoze kama ulikuwa ukihitaji upikiwe samaki,” alisema Bi Hadija.

“Aiseee! Sasa hapa kuna umuhimu wa huyu msichana kumnunulia simu, vinginevyo kuna siku tunaweza kugombana kitu ambacho sitaki kitokee,” alisema mzee Saidi.

Hiyo ndiyo ilikuwa mbinu aliyoitumia, alitaka kuwasiliana na Irakoze kwa karibu mno, kitendo cha kurudi nyumbani ghaflaghafla kingemfanya siku kukutana na mke wake nyumbani hapo hivyo kufumwa, alichokitaka ni kuwasiliana na msichana huyo tu.
Bi Hadija hakujua, kwa fedha zake, akanunua simu na kumpa Irakoze pasipo kujua kwamba ndiyo kwanza aliliua pendo lake kwa mume wake.

Hiyo ikawa nafasi nzuri kwa mwanaume huyo kuwasiliana na Irakoze ambapo kama Bi Hadija hakuwepo nyumbani, walikumbatiana, walibusiana na kupetiana kama kawaida yao.
“Siku mama akijua!”
“Unahisi atafanyaje?”

“Atanifukuza.”
“Hawezi! Mimi ndiye kidume humu ndani!”
“Kweli?”
“Ndiyo! Hebu sogea kwanza unibusu hapa,” alisema mzee Saidi.

Hakukuwa na mtu aliyekuwa akimpenda kama mume wake, alimwamini sana kwani katika miaka yao kumi na tano ya ndoa hakuwahi kusikia hata siku moja akitoka nje ya ndoa yao. Alimthamini na kujiona amepata mume wa ukweli, mume aliyejua kulea na kupenda.

Siku ya kwanza aliposikia tetesi kwamba kulikuwa na uwezekano wa mume wake kutembea na mfanyakazi wake, alibisha sana na kuona kwamba watu walitaka kuivunja ndoa yao iliyodumu kwa kipindi kirefu.

Masikio akayaziba pamba, hakutaka kusikia chochote kile kutoka nje. Kadiri siku zilivyozidi kwenda mbele, tetesi zile zilizidi kuvuma kiasi kwamba akahitaji kuhakikishiwa kwa macho yake, hakutaka kusikia tena hivyo kuanza mishemishe kwa kuwaweka walinzi ili siku mume wake akitoroka kazini, apigiwe simu.
 
SEHEMU YA 04.

“Nitakupigia tu shosti’angu! Mimi tena nishindwe! Hata ukitaka nivae dela wakati wa kwenda kufumania, nipo radhi na kikundi changu cha msuto,” alisema mwanamke ambaye kila siku alikuwa akimsisitizia kwamba alikuwa akichangia mapenzi yake na msichana wake wa kazi.

Siku zikaendelea kukatika, ilikuwa ni kama watu hao wamejua vile, mzee Saidi hakuwa akirudi nyumbani. Wanawake wa mtaani walizidi kusubiri lakini mzee huyo alisitisha zoezi lake la kutoroka kazini na hivyo kutulia hukohuko.

Baada ya mwezi mmoja kupita, mzee Saidi akaonekana akianza kuelekea nyumbani kwake, kama kawaida yake gari lake alilipaki mbali na nyumbani hapo ili hata mkewe akirudi, asiweze kujua kama alikuwa ndani.

“Shoga! Amekuja. Njoo haraka,” aliongea mwanamke huyo, alikuwa akimwambia Bi Hadija kwenye simu.

Wala hazikupita dakika nyingi, Bi Hadija akafika mahali hapo. Kijasho chembamba kilikuwa kikimtoka, mwili ulimtetemeka kwa hasira, alichokuwa ameambiwa, kilimtia hasira mno, akajikuta akiwa na presha kubwa ya kuingia ndani kwa lengo la kufumania.

“Subiri kwanza,” alisema mwanamke huyo, tayari wanawake wenzake walikwishakusanyika mahali hapo.
“Nina presha, niacheni niende.”
“Usiwe na presha. Ngoja kwanza tuvae madela yetu,” alisema mwanamke huyo huku wanawake waliokuwa mahali hapo wakienda makwao na kuanza kuvaa madela tayari kwa kufumania.

Wakati mambo yote hayo yakiendelea, kama kawaida, ndani ya nyumba, Irakoze na mzee Saidi walikuwa chumbani kama walivyozaliwa, walikuwa wakipeana mapenzi motomoto pasipo kujua kwamba wakati mzee huyo akiingia ndani na kupokelewa kwa mabusu mfululizo, walisahau hata kufunga mlango.

Wanawake hao wakaingia ndani na kuanza kuelekea chumbani. Mwendo wao ulikuwa ni wa kunyata huku Bi Hadija akiwa na hasira mno.
|
|
Je, nini kitaendelea?
SImulizi hii itafika hadi mwisho. Usiogope.
 
SEHEMU YA 05

Hawakujua kitu kilichokuwa kikiendelea nje, hawakujua kama kundi la wanawake likiongozwa na mama mwenye nyumba liliingia ndani na kukisogelea chumba walichokuwa huku wakiwa wamelaliana kimahaba.

Ghafla, huku wakiwa wametekwa na uwepo wa mahaba mahali hapo, wakashtukia mlango ukifunguliwa na kundi zima la wanawake hao kuingia ndani. Kwanza wakashtuka, wakawaangalia vizuri wanawake wale, alikuwepo mke wake pia.

Mzee Saidi akashtuka zaidi, hakuamini kile alichokuwa akikiona, mdomo wake ukawa mzito kusema chochote kile.

Mkewe alionekana kuvimba kwa hasira, hakuamini alichokiona chumbani humo, mume wake ambaye kila siku alimuamini ndiye yule aliyekuwa na mwanamke kitandani kwake, tena mfanyakazi wake aliyemtoa kijijini.

Irakoze alivyoona hivyo, akaanza kuomba msamaha huku machozi yakimbubujika mashavuni mwake. Hata kabla Bi Hadija hajazungumza lolote lile, akamvamia msichana huyo wa kazi na kuanza kumpiga.

Kundi lile la wanawake halikugombelezea, lilikuwa likishadadia kile kilichokuwa kikiendelea chumbani pale. Ni mzee Saidi ndiye aliyechukua jukumu la kuanza kuamulia lakini Bi Hadija hakushikika, alikuwa akitukana hovyo.

“Wewe malaya kweli unaamua kunichukulia mume wangu, tena unalala naye kitandani kwangu, sasa utanitambua,” alisema Bi Hadija huku akimshambulia Irakoze.

“Hadija, hebu muache mtoto wa watu.”
“Unagombelezea? Malaya mkubwa wewe, unagombelezeaaaaa?” Ugomvi ulikuwa mkubwa, wanawake wale wengine walikuwa wakizungumza maneno yenye kumuumiza Irakoze juu ya kile alichokuwa amekifanya, kila mmoja alimshutumu huku wengine wakimpiga masingi na kumzomea.

Irakoze aliumizwa kutokana na kipigo alichopewa lakini hakuwa na jinsi, kama maji, tayari yalikwishamwagika na hivyo kufukuzwa nyumbani hapo. Hakutakiwa kukaa, mchana huohuo akafukuzwa na kuondoka nyumbani hapo huku akilia, furushi la nguo zake lilikuwa mikononi mwake.

Alijutia kitendo alichokuwa amekifanya, alianza kujuta kwani kilimuumiza mno. Alipiga hatua kuelekea Magomeni Mikumi ambapo huko akachukua barabara ndogo iliyokuwa ikielekea Mwembe Chai kupitia ilipokuwa nyumba ya marehemu Sheikh Yahya.
 
SEHEMU YA 06

Alipofika njiani, mvua kubwa ikaanza kunyesha, hakuwa na jinsi, alichokifanya ni kwenda kwenye nyumba moja aliyoiona kufaa na kisha kujikinga na mvua ile iliyokuwa ikinyesha mno.

Hapo ndipo akachukua muda mwingi kuanza kulia, “Nitakwenda wapi mimi? Nitakwenda wapi mimi?” alijiuliza huku akilia.

Mvua ilichukua zaidi ya nusu saa mpaka kuacha kunyesha.

Alipoona imeacha, hapo ndipo akalishika furushi la nguo zake na kisha kusonga mbele. Alikuwa akielekea wapi? Hakujua, alihitaji kuondoka mbali na nyumba ya mzee Saidi

Alikwenda na barabara hiyo mpaka alipokuta njia panda, barabara moja ilikuwa ikielekea Mwembe Chai na nyingine Mburahati, alichokifanya ni kuchukua barabara ya kuelekea Mburahati ambapo aliamini kwamba angeweza kupata msaada wowote ule.
Alisonga mbele, furushi lilikuwa kichwani mwake huku akibubujikwa na machozi.

Aliona dunia imemgeukia, hakuwa na pa kukimbilia zaidi ya kwenda mbele kama mtu aliyekuwa akibahatisha sehemu fulani.

Safari yake iliishia nje ya nyumba moja, haikuwa ya kifahari, ilikuwa nyumba ambayo kwa kiasi fulani ilionekana kuchoka. Kulijaa matope lakini hakutaka kujali, kwa kuwa kulikuwa na kibaraza, akaenda na kutulia hapo.

Kumbukumbu za maisha yake zikaanza kujirudia kama mkanda wa filamu kichwani mwake, alikumbuka mengi tangu siku ya kwanza alipofika jijini Dar es Salaam mpaka siku hiyo.

Alihuzunika na kujutia uamuzi wake wa kutembea na mzee Saidi, ila pamoja na hayo yote, alitakiwa kupambana kwani alijua kwamba huo usingekuwa mwisho wa maisha yake.

“Habari yako!” ilisikika sauti ya mwanamke mmoja, alikuwa amefika nyumbani hapo huku mkononi akiwa ameshika Biblia.

“Salama! Shikamoo mama!”
“Marahaba binti mzuri, hujambo?”
“Sijambo!”

Baada ya salamu ile, mwanamke yule hakuongea kitu chochote kile zaidi ya kufungua mlango na kuingia ndani. Irakoze hakutoka kibarazani hapo, aliendelea kukaa huku akionekana kuwa na mawazo mengi.
 
SEHEMU YA 07

Mpaka inafika saa kumi na mbili jioni, bado hakujua aende wapi, hakuijua vizuri Dar es Salaam kwani kipindi cha miaka miwili kukaa ndani ya jiji hilo, hakuwa mtembeaji, alikuwa mtu wa kutulia tu nyumbani, akitoka, kaenda gengeni na kurudi nyumbani.

Huku akiwa kwenye lindi la mawazo, tena watu waliokuwa wakipita njia wakimshangaa, ghafla akasikia mlango ukifunguliwa na mwanamke yule kutoka.

Akashtuka kumuona Irakoze mahali pale, hapo ndipo alipogundua kwamba inawezekana binti yule alikuwa na tatizo kubwa, hivyo akamfuata kwa lengo la kuzungumza naye.

“We binti,” alimuita Irakoze, akauinua uso wake, macho yalikuwa mekundu.
“Abeee...!”

“Kuna nini kinaendelea? Mbona upo hapa kwa kipindi kirefu?’ aliuliza mwanamke yule.

Irakoze hakujibu kitu zaidi ya kuanza kulia, alionekana kuwa mtu aliyepitia mambo mengi mno, mwanamke yule aliligundua hilo hivyo akaanza kumbembeleza anyamaze, aliponyamaza, akaomba kusimuliwa kile kilichotokea mpaka siku hiyo kuwa mahali pale, Irakoze akaanza kumsimulia.

Hakutaka kuficha kitu chochote kile, kwa kipindi hicho, alitakiwa kuhadithia ukweli ili aone kama angeweza kusaidiwa au la.

Kila alipokuwa akimsimulia mwanamke yule, kuna kipindi alinyamaza na kuanza kulia, alibembelezwa na kuendelea tena.
“Pole sana kwa matatizo yaliyokukuta,” alisema mwanamke yule kwa sauti ya huruma huku akiiweka rozali yake shingoni mwake.

Huo ndiyo ukawa mwanzo wa Irakoze kufahamianana mwanamke yule, hakutaka kumuacha, historia fupi ya maisha yake ambayo alimsimulia ilimgusa moyoni mwake hivyo kuamua kumsaidia.

Hakutaka msichana huyo aondoke, kwa kuwa alikuwa na uwezo wa kumsaidia, akaamua kumsaidia huku akimtafutia sehemu nyingine ambayo angeweza kufanya kazi kama alivyokuwa akifanya kwa mzee Saidi.

Hiyo wala haikuchukua muda mrefu, mwanamke yule akamuita na kumwambia kwamba kulikuwa na sehemu ambayo alitakiwa kwenda kufanya kazi, haikuwa kwa mtu wa kawaida, alitakiwa kwenda kufanya kazi kwa padri wa kanisa alilokuwa akisali.

“Kwa padri?”
“Ndiyo!”
“Mmmh!”
“Vipi tena?”
“Nitaweza kweli?”
“Utaweza, wala usihofu.”
 
SEHEMU YA 08

“Na yakitokea kama yaliyotokea kwa mkewe?”
“Usijali. Mapadri huwa hawaoi, anaishi peke yake, na ni mtumishi wa Mungu, hawezi kumtenda Mungu dhambi,” alisema mwanamke yule.

Hiyo ikaonekana kuwa nafuu kwa Irakoze, kwa kuwa aliambiwa kwamba padri huyo alikuwa akiishi peke yake, akaamini kwamba kusingekuwa na tatizo lolote lile ambalo lingetokea, hivyo akakubliana na mwanamke yule hivyo siku iliyofuata kwenda huko kwa padri huyo kijana, aliyekuwa na sura nzuri ambapo mara baada ya Irakoze kumuona kwa mara ya kwanza tu, akatokea kumpenda. Huyo aliitwa padri Benedicto.
|
|
Je, nini kitaendelea?
 
SEHEMU YA 09

Alijulikana kwa jina la Pius Massawe, Mchaga kutoka mkoani Kilimanjaro, alikuwa kijana mwenye sura nzuri kiasi kwamba wanawake wengi wakatokea kumpenda kutokana na uzuri wa sura aliokuwa nao.

Wasichana wengi kutoka katika Shule ya Sekondari ya Majengo mkoani humo walivutiwa na Pius lakini kijana huyo hakutaka kabisa kujihusisha na mambo ya mapenzi kabisa.

Wasichana hao hawakutaka kuvumilia, waliamua kumfuata na kumwambia ukweli kwamba walikuwa wakimpenda lakini Pius hakutaka kukubaliana nao, aliwakataa kitu kilichowafanya watu wengi kumshangaa.

Uvumi ukaanza kusikika kwamba Pius alikuwa akishiriki mapenzi ya jinsia moja, uvumi huo ulivuma kwa kasi lakini yeye mwenyewe hakutaka kulizungumzia suala hilo, alijua kwamba kulikuwa na maneno mengi yangesemwa, kwake, hizo zote alizichukulia kama changamoto.

Mbali na uzuri wa sura aliokuwa nao, Pius alikuwa na uwezo mkubwa darasani, katika kila mtihani, alikuwa akiongoza kitu kilichowachanganya watu wengi kabla ya kugundua kwamba mtu huyo alikuwa na akili za kuzaliwa, yaani kile alichokuwa akifundishwa leo, hakuweza kukisahau hata kama ni miaka mingapi ingepita.

Wanawafunzi wengi walikimbilia kwake kufundishwa, Pius hakuwa na maringo, alimfundisha kila mtu japokuwa wanawake wengi walitumia njia hiyo kumtongoza lakini bado msimamo wake ulibaki kuwa uleule kwamba asingeweza kutembea na msichana yeyote yule shuleni hapo.

“Kwani tatizo nini Pius?” aliuliza msichana Thedosia, japokuwa alisifika kwa uzuri shuleni hapo kwa upande wa wanawake, lakini kwa Pius alionekana si chochote.

“Ninataka kuwa padri.”
“Kweli?”
“Ndiyo!”
“Kwa hiyo hautooa?”

“Hakuna tatizo. Siwezi kufanya mapenzi na msichana yeyote,” alisema Pius huku akimwangalia msichana huyo usoni.
Huo ndiyo ulikuwa msimamo wake, hakutaka kufanya mapenzi na msichana yeyote yule.

Pius alikuwa kijana wa tofauti na wengine, alihusudu sana ibada, kila siku alipokuwa akihitajika kwenda kanisani, alikwenda, alipofika huko, alikaa katika kiti cha mbele kabisa na kuanza kusali.

Kila alipokuwa, rozali ilikuwa mkononi mwake, na kama haikuwa mkononi, aliichukua na kuivaa shingoni. Alikuwa hivyo, nyumbani napo kulikuwa kama shuleni.
 
SEHEMU YA 10

Uzuri wa sura yake ulizidi kuwatetemesha wanawake wengi, wengine walijipendeza waziwazi lakini hakuwa na habari nao, alichokuwa akikihitaji ni kuwa padri tu.
Alipomaliza kidato cha nne na akajiunga na cha tano katika Shule ya Sekondari ya Tambaza iliyokuwa jijini Dar es Salaam.

Kila alipofika, Pius alikuwa gumzo, japokuwa alipokuwa mkoani Kilimanjaro aliambiwa kwamba atakapofika Dar es Salaam basi msimamo wake ungeweza kulegea lakini huko akawa vilevile kiasi kwamba watu wakampa jina la padri kitu kilichomfurahisha mno.

Alipomaliza kidato cha sita kwa masomo ya kawaida, akafaulu lakini akajiunga na chuo cha upadri kilichokuwa Morogoro na kisha kuanza masomo rasmi.

Haikuwa kazi ngumu, alizingatia masomo yake, kila siku asubuhi alikuwa akiamka na wenzake na kwenda kanisani kusali, walipomaliza na ndipo walipoendelea na mambo mengine.

Alisoma huko kwa muda wa miaka mitatu na ndipo walipoandaliwa kwenda kumalizia masomo ya mwisho katika Jiji la Venice nchini Italia. Ilikuwa furaha kwake kwani alibakiza hatua chache kabla ya kufika pale alipotaka kufika.

Kutoka Venice mpaka Vatican haikuwa mbali sana, mara kwa mara alikuwa akielekea huko na kukutana na viongozi wa dini ya Kiroma na kuzungumza nao mawili-matatu kitu kilichomfanya kujisikia vizuri na kuahidi kushinda kile kilichobakia mbele yake.

Huko ndipo alipopewa jina la Benedicto badala la lile la Pius alilokuwa akilitumia kabla. Baada ya kukaa huko Venice kwa miaka miwili ndipo aliporudi nchini Tanzania na kupewa kanisa huku akijulikana kwa jina la Padri Benedicto.

Kanisa likajaza wanawake wengi kuliko wanaume, tetesi zilizokuwa zikisikika kwamba kanisa hilo lilikuwa na padri aliyekuwa na sura nzuri iliwachanganya wanawake wengi na hivyo kutaka kwenda huko kushuhudia kwa macho yao.

Walipomuona, waliamini kwamba duniani kulikuwa na wanaume wenye sura nzuri mno, kila walipomwangalia padri wao, walimtamani mno.

“Jamani hii sheria ya mapadri kuoa si ipitishwe tu, nahisi kama bahati inaweza kuniangukia,” alisikika akisema msichana mmoja.
 
SEHEMU YA 11

“Bahati ya nini?”
“Kuolewa na padri Benedicto, ninampenda sana jamani!”
“Wewe Upendo, humuogopi Mungu!”
“Namuogopa, lakini kwa nini ameamua kutupa jaribu kubwa namna hii?”

Padri Benedicto alikuwa akiishi peke yake nyumbani kwake, wafanyakzi wengi wa ndani aliokuwa akiwahitaji walikuwa wa kiume tu ambao wengi alikorofishana nao na mwisho wa siku kuwafukuza kihekima.

Baada ya kufukuza wafanyakazi watano, akaamua kuishi peke yake, hakutaka tena kuwa na mfanyakazi yeyote nyumbani kwake kwani aliona kama angeweza kufanya kazi peke yake pasipo mfanyakazi yeyote yule.

“Ila kuna msichana ana matatizo sana, naomba aje akusaidie padri,” alisema mama John, mwanamke aliyekuwa ameonana na Irakoze.
“Nimsaidie vipi?”
“Aje kufanya kazi hapa!”
“Msichana?”
“Ndiyo!”

“Hapana! Haiwezekani hata kidogo.”
Japokuwa padri Benedicto alikataa lakini mama John hakuacha kumbembeleza akubaliane naye kwani mtu kama yeye alihitaji mfanyakazi wa kike kwa ajili ya kufanya usafi wa nyumba muda wote kitu ambacho kwa kiasi fulani kikaanza kumuingia padri huyo.

Mbali na kumwambia hivyo, pia alimsimulia historia ya kusikitisha ya msichana Irakoze kiasi kwamba padri akaingiwa na huruma na kuona kwamba kumsaidia msichana huyo ilikuwa kama baraka kwa Mungu kwa kuwa ameamua kumtoa mtu fulani kutoka sehemu moja ya chini na kumuweka sehemu ya juu.

Wakakubaliana na hivyo mama John kuelekea nyumbani ambapo akamchukua Irakoze na kuelekea naye nyumbani hapo. “Ni mzuri mno, sijawahi kuona mwanaume mzuri kama huyu,” alijisemea Irakoze katika kipindi alichomuona padri Benedicto kwa mara ya kwanza.

Hiyo ndiyo ikawa siku ya kwanza kukutana kwa watu hao, Irakoze akaanza kazi ndani ya nyumba hiyo. Alikuwa msichana mwenye heshima kubwa, kila siku alikuwa mtu wa kuvaa mavazi marefu ambayo aliamini kwamba yasingemtia majaribu padri huyo.

Waliheshimiana mno, kila siku asubuhi walikutana sebuleni, walishikana mikono na kuanza kusali kisha kuendelea na ratiba nyingine.
 
SEHEMU YA 12

Katika kipindi chote hicho, Irakoze alikuwa kwenye mapenzi ya dhati kwa padri huyo, alitamani kumwambia ukweli kwamba alimpenda lakini aliogopa kufanya hivyo, akabaki akiugulia moyoni mwake tu.

Siku zikaendelea kukatika, heshima ilikuwa kubwa ndani ya nyumba, Irakoze aliendelea kufanya kazi ndani ya nyumba hiyo huku kila siku akijitoa kitendo kilichomfurahisha Padri Benedicto kiasi kwamba alijiona kuchelewa mpaka kuchukua uamuzi wa kumuajiri mfanyakazi wa kike.
“Nakuja, niandalie chakula,” alisema padri Benedicto.

Siku hiyo hakuwepo nyumbani, alikuwa kanisani akiendelea na huduma, mawingu mazito yalitanda angani kuonyesha kwamba muda wowote ule mvua ingeweza kunyesha. Mara baada ya kumaliza kila kitu likiwa suala la kupika chakula, Irakoze akachukua khanga yake na kuelekea bafuni kuoga.

Alipokuwa huko, akasikia mvua kubwa ikianza kunyesha huku kiubaridi kikianza kuongezeka. Alichokifanya, akatoka bafuni na khanga yake kisha kutoa ndoo nje kwa ajili ya kukinga maji ya mvua yaliyokuwa yakidondoka.

Mwili wake ukalowa, khanga ikanata mwilini mwake, umbo lake lenye mvuto, makalio yaliojaajaa yakawa yanaonekana vizuri kabisa. Hakuwa na wasiwasi wowote ule, alikuwa peke yake nyumbani hapo hivyo aliendelea kufanya kazi yake.
 
SEHEMU YA 13

Wakati yupo hapo akiendelea kukinga maji, mara geti likafunguliwa na Padri Benedicto kuingia. Irakoze hakumuona padri huyo, aliendelea kukinga maji huku wakati mwingine akijimwagia, kifua chake kikanata kwenye ile khanga, kila kitu mwilini mwake kilionekana wazi.

Padri Benedicto alipoona hivyo, moyo wake ukashtuka, hakupiga hatua, alibaki akimwangalia Irakoze huku akiwa na mwamvuli wake.

Alibaki akimeza mate na maeneo ya zipu yake kuanza kusogea mbele. Alichanganyikiwa, kila alipojitahidi kuyaamisha macho yake, yaligoma kabisa kuhama.

Mpaka Irakoze anageuka na kumwangalia padri huyo, alikuwa hoi, kwa kujishtukia, Irakoze akamsalimia na kisha kuelekea ndani, sehemu ya nyuma ilikuwa ikichezacheza, padri akaona haiwezekani, japokuwa hakuwahi kulala na mwanamke yeyote maishani mwake, uzalendo ukamshinda, pepo la ngono likamwingia, mwili wake ukaanza kumsismka huku akihisi vijidudu fulani vikianza kumtembelea mwilini mwake, naye akaanza kuelekea ndani huku akiwa amechanganyikiwa kimahaba, pepo la ngono lilishamvaa, hakukubali, alitaka kuonekana kwamba hata na yeye alikuwa mwanaume.
|
|

iTAENDELEA
 
Back
Top Bottom