SEHEMU YA 113...
“Naomba baadaye! Waandishi naomba mnihoji baadaye!” alisema Richard, kwa jinsi Ibrahim alivyoonekana, jinsi alivyovaa shati lake na kuchomekea kinadhifu, akahisi kwamba alikuwa mwandishi wa habari.
“Ila bro!”
“Naomba uniache!” alisema Richard kwa hasira, tena kwa sauti ya juu, hakuonekana kuwa sawa, akaelekea kaunta, baada ya dakika chache akatoka nje, akaingia ndani ya gari lake, akaliwasha na kuondoka kurudi hospitalini.
**** Hali ya Malaika ilikuwa mbaya kitandani, ugonjwa wa Sickle Cell uliendelea kumtesa, alikuwa akilia, muda wote ule aliona dhahiri kwamba alikuwa akienda kufa.
Madaktari walikuwa wakihangaika kuyaokoa maisha yake, hawakutaka kumpoteza binti huyo aliyekuwa na sura ya kipole, kwao, hakukuwa na kitu ambacho kingewauma kama kuona msichana huyo akifariki dunia.
Madaktari walikuwa wakiingia kwa zamu, walimuwekea dripu za damu kwani alikuwa amepoteza damu kwa kiwango kikubwa sana. Alitia huruma pale kitandani alipokuwa na kwa jinsi alivyokuwa akisikia maumivu, alimuona malaika mtoa roho akiwa ameingia wodini kwa ajili yake.
Alibaki akimuomba Mungu, alimshukuru kwa kila kitu, alijua dhahiri kwamba alikuwa akienda kufa lakini alitaka Mungu ampe nafasi ya kufanya mambo yaliyo mema, pale alipokosea, arekebishe na kufariki kwa amani kabisa.
Hakuwahi kuwa na maisha mazuri, siku zote maisha yake yalitawaliwa na umasikini mkubwa. Hakuwa na pesa lakini alimuomba Mungu amponye ili aweze kuwasaidia watu wengine, wale waliokuwa na matatizo, awasaidie watoke kwenye matatizo hayo waliyokuwa nayo.
Alimuomba Mungu kwa dakika kadhaa, machozi yalikuwa yakimtoka, moyo wake ulimuuma mno, ilikuwa ni kama Mungu alisikia kilio chake kwani baada ya kusema Amen, akahisi mwili wake ukianza kurudi katika hali ya kawaida, maumivu aliyokuwa nayo katika mifupa yake yakaanza kupotea.
Moyo wake ukawa na furaha kubwa, hakuamini kile kilichokuwa kikitokea, alilia sana, wakati mwingine alikuwa na hisia kwamba kulikuwa na mtu aliyekuja kitandani pale, alikuwa akimshika kuanzia miguuni mpaka kichwani, alitamani kuzungumza kitu lakini akauona mdomo wake kuwa mzito.
itaendelea.