Lowassa, Nchimbi kuwekwa kitimoto
Na Mwandishi Wetu
KAMATI Kuu ya Halmashauri Kuu ya Taifa ya CCM inaendelea na kikao chake mjini Dodoma leo baada ya kile kilichoanza wiki iliyopita jijini Dar es Salaam kuahirishwa kwa sababu mbalimbali yakiwemo majukumu ya nje ya nchi ya Mwenyekiti wa Taifa wa chama hicho, Rais Jakaya Kikwete.
Moja ya agenda zinazosubiriwa na wanachama wengi ni ile ya utata wa mkataba wa ubia wa jengo la umoja wa vijana wa CCM (UVCCM), ambao inadaiwa kuwa Mwenyekiti wa Baraza la wadhamini wa jumuia hiyo, Edward Lowassa alisaini bila ridhaa ya wajumbe wenzake na pia hauna maslahi kwa jumuia hiyo.
Wajumbe sita (majina tunayahifadhi) wa kamati hiyo waliozungumza na gazeti hili muda mfupi kabla ya kuanza kikao hicho, wamesema kuwa hawatakuwa tayari kumlinda mtu hata kama ni maarufu kiasi gani endapo itabainika hakufuata taratibu katika kulinda maslahi ya chama na jumuia zake.
Matamshi ya wajumbe hao yanathibitisha kuwa Lowassa huenda akawekwa kiti moto na kujikuta kwenye wakati mgumu kunusuru nafasi yake kisiasa ambayo tangu mwaka 2008 uanze amekuwa akiporomoka toka nafasi ya uwaziri mkuu hadi Mbunge baada ya kuwajibika kutokana na makosa ya baadhi wa maofisa serikalini juu ya mkataba wa ufuaji wa umeme wa dharura wa kampuni ya Richmond.
Wakizungumzia kuhusu mradi wa jengo la vijana mmoja wa wajumbe hao alisema kuwa, wataangalia kwa makini na kwamba hii si mara ya kwanza kuangalia miradi ya jumuia na kuwawajibisha wale wote waliohusika na kusisitiza kuwa kiboko kilichotumika kwa viongozi wa UWT Taifa kuhusiana na mradi wa jengo lililopo barabara ya Ali Hassan Mwinyi kitatumika kwa viongozi wa vijana endapo walifanya makosa.
"Hatuwezi kuwa na vigezo tofauti, kama makosa yamefanywa iwe kwa mwanachama wa kawaida au maarufu hukumu kichama ni ile ile na hatukuanza leo. Ikumbukwe huko Nyuma kamati kuu iliwahi kuvunja Baraza Kuu la jumuia hiyo na kumvua nyadhifa zote Mwenyekiti wake wa Taifa," amesema mjumbe huyo mwandamizi wa kamati hiyo.
Kutokana ma kauli hiyo Lowassa na Mwenyekiti wa Taifa wa jumuia hiyo, Emmanuel Nchimbi wanaweza kuwajibishwa endapo kamati kuu haitaridhishwa na maslahi ya ubia aliotiwa saini Januari 2, 2007 na Mwenyekiti wa baraza la wadhamini, Lowassa.
Aidha wajumbe hao wamesema kuwa agenda ya mradi wa vijana ni tofauti na kujadili majina ya walioomba kugombea nafasi za uongozi wa jumuiya hiyo katika ngazi za taifa hivyo hawatakuwa tayari kuunganisha agenda hizo kwa pamoja kila kimoja kitatolewa maamuzi yake kufuatana na maelezo tena ya kina.
Suala la Lowassa limekuwa gumzo kubwa hivi karibuni kutokana kukumbwa na tuhuma zilizoelekezwa kwake na mgombea wa kiti cha uenyekiti wa Umoja wa Vijana wa CCM, Nape Nnauye ambaye amefukuzwa uanachama wa umoja huo juzi.
Baraza Kuu la UVCCM juzi lilimvua uanachama Nape katika kinachodaiwa kuwa ni kukiuka maadili ya chama pamoja na kumwengua rasmi katika kinyang'anyiro cha kuwania uenyekiti wa umoja huo katika uchaguzi unaotazamiwa kufanyika baadaye mwaka huu.
Nape amekuwa gumzo kubwa katika uchaguzi huo kutokana na kulipua alichokiita bomu la ufisadi kuhusu mradi wa ujenzi wa jengo la Makao Makuu ya Umoja wa Vijana wa CCM jijini Dar es Salaam ambapo alidai Lowassa alisaini mkataba wa mradi huo kinyemela.
Kijana huyo amekuwa akiwataka mwenyekiti wa UVCCM anayemaliza muda wake, Dk. Emmanuel Nchimbi, Katibu Mkuu, Kaimu Katibu Mkuu, Francis Isaac na Mwenyekiti wa Bodi ya Wadhamini, Edward Lowassa wawajibishwe kwa kupitisha mradi ambao anadai hauna