Nchimbi afa na umri wagombea UVCCM
*Makamba 'awabwatukia' wanaoandaa mauti ya CCM
Na Joyce Kassiki, Dodoma
WAKATI Katibu Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Bw. Yusuf Makamba akiwataka wanachama wa Umoja wa Vijana wa CCM (UVCC) kuacha tabia ya kukichafua chama hicho kwa kukisema vibaya hadharani, Mwenyekiti wa Umoja huo, Dkt. Emmanuel Nchimbi amewataka vijana hao kuchagua wagombea wenye umri unaokubalika ili kujenga timu imara .
Bw. Makamba aliyasema hayo jana alipokuwa akizungumza kwenye Kikao cha Baraza Kuu la Umoja wa Vijana wa CCM ambacho pamoja na mambo mengine, kilichuja majina ya wagombea nafasi mbalimbali za Jumuiya hiyo.
Katibu huyo, alisema kufanya hivyo ni sawa na kukiletea chama mauti kwani tabia hiyo inaweza kuibomoa UVCCM na wakati huo huo kudhalilisha chama.
Alisema Jumuiya za vijana ndio chimbuko la kupata viongozi wa juu wa Taifa hivyo vijana hawana budi kukipenda chama chao na kuepuka majungu yanayoweza kukibomoa chama hicho.
"Mambo mengine yanayofanywa na vijana ni mauti kwa chama,kuisema Jumuiya ni kuibomoa Jumuiya hiyo na chama kwa ujumla halafu baadaye tutakosa viongozi mahiri wanaoweza kuongoza nchi,"alionya Bw. Makamba
Awali akifungua kikao hicho, Mwenyekiti wa UVCCM,Bw. Emmanuel Nchimbi aliwataka wajumbe wa Baraza hilo kuchagua vijana wenye uwezo wa kuongoza badala ya kuangalia sura na jina la mtu.
Alisema ili kupata viongozi wazuri watakaongoza Jumuiya hiyo kwa kipindi cha miaka mitano, wajumbe hawana budi kuchagua wanachama wenye umri stahili na kupima utendaji wa wagombea hao.
Akifafanua suala la umri, Bw. Nchimbi, aliwataka wajumbe hao kutomwonea haya mgombea yeyote aliyevuka umri kwani lengo la umoja huo ni kuwa na timu nzuri ya Baraza lijalo.
Aliwataka vijana kuwa na mapenzi mema na chama chao badala ya kujenga chuki na ubinafsi jambo ambalo alisema linasababisha makundi yasiyokuwa na msingi ndani ya Jumuiya hiyo na chama kwa ujumla.
Kauli ya Mwenyekiti huyo imeonesha kuweka wazi msimamo wake kuhusu vuta ni kuvute kati yake na mmoja wa wagombea nafasi ya Uenyekiti wa UVCCM, Bw. Nape Nnauye ambaye anadaiwa kuvuka umri huo.
Bw. Nnauye mwanasiasa kijana machachari, amekuwa akipinga jambo hilo na kuliona kama 'fitna za kuchongwa' dhidi yake baada ya kufichua kile alichoeleza, ufisadi mkubwa ndani ya mradi wa ujenzi wa jengo la kitega uchumi cha Jumuiya hiyo lililopo kando ya barabara ya Morogoro, jijini Dar es Salaam.
Katika sakata hilo, Bw. Nnauye alimshutumu moja kwa moja Mwenyekiti wa Bodi ya Wadhamani wa UVCCM, Bw. Edward Lowassa na viongozi wengine wa juu, kuingilia mkataba huo aliobainisha kuwa hauna maslahi kwa umoja huo.
Kauli ya kada huyo kijana, imezua mtafaruku mkubwa na migongano ya kauli ndani ya chama hicho kikongwe nchini, huku kundi moja likimuunga mkono na kutaka hatua zaidi zichukuliwe kubaini kasoro za mkataba huo na kundi lingine likipingana na jambo hilo na kumwona amekiuka taratibu za chama hicho kwa kuanika jambo hilo hadharani.