Mvutano mkali watarajiwa mkutano wa Vijana CCM Dodoma
Kizitto Noya na Saa Mohamed
Mwananchi
Date::9/6/2008
MVUTANO mkubwa unatarajiriwa kutawala kikao cha Baraza Kuu la Umoja wa Vijana wa Chama Cha Mapinduzi (UVCCM), kinachoketi Jumapili kuchambua majina ya wagombea wa nafasi ya mwenyekiti mjini Dodoma.
Kikao cha Baraza Kuu ni cha tatu kuchuja majina ya wagombea hao baada ya Sekretarieti ya UVCCM iliyoketi jijini Dar es Salaam na Kamati yake ya Utekelezaji iliyokaa Agosti 16 na 17 mjini Dodoma.
Tofauti na vikao vya Sekretarieti na Kamati ya Utekelezaji, Baraza Kuu la Vijana, linatarajiwa kuwagawa wajumbe wakati wa kujadili jina la Mjumbe wa Baraza hilo na Halmashauri Kuu ya CCM (NEC), Nape Nnauye kutokana na msimamo wake wa wazi kupinga ufisadi ndani ya jumuiya hiyo.
Tayari Nape amekwishawekewa alama mbaya ya F za kutompendekeza kuwania nafasi hiyo na baadhi ya wajumbe wanaamini kuwa kitendo hicho kimetokana na msimamo wake kupinga ufisadi aliodai unafanywa na watendaji wakuu wa UVCCM kuhusiana na Mkataba wa Jengo la Umoja wa Vijana.
Kikao cha kwanza kumwengua Nape ni Kamati ya Utekelezaji chini ya Mwenyekiti wa Jumuiya hiyo, anayemaliza muda wake Dk Emmanuel Nchimbi ambacho kilimwekea alama F inayomaanisha kuwa hafai kugombea nafasi hiyo kwa kigezo cha umri.
Kikao hicho kilimpa Nape alama F na kuwapendekeza wagombea wengine watano kuwania nafasi hiyo baada ya kupitia vyeti vya wagombea hao na kubaini kuwa Nape alizaliwa Novemba 26 mwaka 1977.
Majina yaliyopendekezwa ni Zainab Kawawa, Said Mtanda, Benno Malisa, Hussein Bashe na Suleiman Suleiman.
Hata hivyo, uamuzi wa kumwengua Nape uliwagawa wajumbe wa kikao hicho baada ya kundi moja kuridhia na lingine kukataa kutokana na kuamini kuwa uamuzi huo umetokana na msimamo wa Nape kupinga ufisadi.
Sababu zilizotolewa na upande uliounga mkono kuondolewa kwa Nape ni kutetea maamuzi ya vikao vyake vilivyopitisha kanuni ya kikomo cha umri katika uwania nafasi hiyo.
Msimamo huo wa Nape ndio uliofanya nyota yake izidi kung'ara na hivi karibuni alipotambulishwa bungeni alishangiliwa na wabunge na kutakiwa mafanikio na Spika, Samuel Sitta, hatua ambayo inaonyesha dhahiri kuwa anaungwa mkono katika mapambano yake dhidi ya ufisadi.
Zengwe la umri ni kanuni iliyoingizwa kwenye taratibu za Uchaguzi wa UVCCM mwaka 2003 wakati Mwenyekiti wa sasa, Dk Emmanuel Nchimbi anawania nafasi hiyo kwa mara ya pili, ikilenga kumuengua, lakini busara ya Kamati Kuu ya CCM iliiweka pembeni kwa muda.
Kulingana na kanuni hiyo, umri wa mwisho wa kugombea ni miaka 30 ili kiongozi husika asizidi miaka 35 akiwa madarakani umri ambao ni wa mwisho wa uanachama wa UVCCM.
Hata hivyo, ingawa Mkurugenzi wa uchaguzi huo, Francis Isack hakutaka kueleza mamlaka ya kikao cha Baraza Kuu la UVCCM, katika kuamua hatima ya wagombea, kikanuni, maamuzi ya kikao hicho yanafuta maamuzi ya vikao vyote vya awali vya jumuiya hiyo dhidi ya wagombea hao.
Nape aliliambia Mwananchi Jumapili jana kuwa, ana hakika Baraza Kuu litatenda haki dhidi yake kwani anaamini si wajumbe wote wa baraza hilo wanaotaka ufisadi uendelee kuitafuna jumuiya hiyo.
Alisema kikao hicho kinampa matumaini mapya ya safari yake kuusaka uenyekiti wa jumuiya hiyo na ndicho kitakachotoa dira na mtazamo wa wajumbe kuhusu ufisadi.
"Mimi naamini kwamba wajumbe wa kikao hicho wana busara kubwa na ninaamini ukweli wa mambo utajulikana hapo. Baraza lina busara nyingi na naamini wajumbe watatumia busara kusafisha jina langu," alisema Nape.
Akizungumzia mchakato huo kwa ujumla, Nape alisema anasikitika kuona baadhi ya wanasiasa wameacha kando hoja na kuanza kuingiza unafiki kwa masilahi binafsi.
"Mimi ushauri wangu kwa wanasiasa waache unafiki, tushindane kwa hoja za leo. Kwa wanahabari naomba wafuate maadili badala ya kukubali kutumiwa kwa masilahi ya wanasiasa wachache," alisema.
Mkurugenzi wa Uchaguzi huo, Francis Isack alithibitisha jana kuwepo wa kikao hicho leo na kusema kimsingi kikao hicho ni kikubwa kuliko vikao vingine vyote katika mchakato huo.
"Siwezi kukutajia agenda, lakini ni kweli Baraza linakaa kesho (leo) kuchuja majina ya wagombea," alisema Isack ambaye awali aligoma kuzungumzia suala hilo kabisa.
Kikao cha Baraza Kuu kitafuatiwa na Sekretarieti ya CCM chini ya Katibu Mkuu wake, Yusuf Makamba, kikao cha Kamati ya Maadili ya CCM, Kamati Kuu (CC) na Kikao cha Halmashauri Kuu ya CCM (NEC) vyote chini ya Mwenyekiti Jakaya Kikwete.
Nape aliwasha moto ndani ya UVCCM muda mfupi baada ya kuchukua fomu za kuwania nafasi hiyo na kuwatuhumu watendaji wakuu wa jumuiya akiwamo Mwenyekiti wa Baraza la Wadhamini, Edward Lowassa kwamba wanahusika na mkataba tata wa Jengo la Makao Makuu ya Jumuiya hiyo.
Watendaji wengine aliowatuhumu kuhusika na mkataba huo ni Mwenyekiti wa Jumuiya hiyo anayemaliza muda wake, Dk Emmanuel Nchimbi na aliyekuwa Katibu Mkuu wa Jumuiya hiyo Amos Makala.
Wachambuzi wa masuala ya siasa wameeleza kuwa, hawashangai kuona Nape anapata wakati mgumu katika hatua za awali za mchakato huo kwenye jumuiya ya vijana kwa kuwa viongozi wa vikao hivyo ni baadhi watendaji aliowatuhumu kwa ufisadi.