RIWAYA: UFUKWE WA MADAGASCAR
SEHEMU: 45
...cha lifti ukafunga na ile lifti ikaanza kushuka chini ya lile jengo. Mle ndani ya kile chumba cha lifti hakukuwa na mtu mwingine yeyote na hali ile niliipenda. Sasa akili yangu ikaanza kujiandaa namna ya kukabiliana na hatari yeyote ambayo ingejitokeza baada ya kufika chini ya lile jengo.
Sikufanikiwa kwani wakati kile chumba cha lifti kinafika ghorofa ya tatu ya lile jengo la Le Tulip Hôtel Africaine ghafla taa ya mle ndani ikazima na kisha kile chumba cha lifti kusimama. Kwa sekunde kadhaa nikaganda kama nyamafu nikishikwa na taharuki isiyoelezeka sambamba hofu kuanza kupenya taratibu moyoni mwangu. Hisia zangu zikanitanabaisha kuwa nilikuwa nimejitumbukiza kwenye hatari nyingine na tukio lile huwenda lingekuwa ni mtego wa kuninasa mzimamzima kama siyo hitilafu ya umeme ya kawaida.
Kutokana na mfumo wa kile chumba cha lifti hapakuwa na hewa iliyokuwa ikiingia au kutoka mle ndani hivyo nilianza kuishiwa pumzi taratibu huku nikitokwa na jasho jingi mwilini. Hata hivyo nilijipa uvumilivu huku nikijipa matumaini kuwa kama lile lingekuwa ni tatizo la umeme wa kawaida basi jenereta la umeme wa dharura wa lile jengo lisingechukua zaidi ya dakika tatu kabla kuwaka na hivyo safari yangu ingeendelea kama kawaida.
Hata hivyo kile nilichokuwa nikikiwaza hakikutokea kwani ule umeme haukurudi wala kile chumba cha lifti kuendelea na safari. Kwa zaidi ya dakika mbili nikakaa mle ndani na baada ya kuona hakuna uelekeo sikutaka kusubiri zaidi kwani hewa ya mle ndani ya kile chumba ilikuwa tayari imeanza kuwa nzito kiasi cha kunipelekea nianze kuhema kwa tabu. Haraka nikaingiza mkono mfukoni kuchukua kurunzi yangu ndogo ya kijasusi yenye mwanga mkali na kuanza kumulikamulika mle ndani. Kwa kufanya vile nikakiona kifuniko kidogo kilichokuwa sehemu ya juu katikati ya kile chumba cha lifti kikiwa kimefungwa kwa skrubu.
Bila ya kupoteza muda nikadandia kuta za kile chumba kwa miguu yangu na kuanza kufungua ule mfuniko kwa kisu changu kidogo chenye mkusanyiko wa vifaa vingi muhimu kama kiberiti cha gesi, bisbisi, uma mdogo, kijiko, opena na vifaa vingine vidogo vidogo muhimu. Baada ya muda mfupi nikawa nimefanikiwa kuufungua ule mfuniko na kuuweka kando huku moyoni nikiomba kuwa ule umeme wa lile jengo usirudi haraka kabla ya kukamilika kwa operesheni yangu.
Nilipouondoa ule mfuniko nikapenyeza kichwa changu kwenye lile tundu kule juu na kuanza kumulika. Kule juu kulikuwa na nyaya nyingi zinazopishana na machuma mengi yaliyoshikilia kile chumba cha lifti. Mle ndani hewa ilikuwa imeanza kuwa nzito na joto nalo lilikuwa likiongezeka taratibu. Nilianza kuzifuatilia zile nyaya na nilipohisi kuwa zisingenifaa chochote nikaamua kuachana nazo. Nilipoendelea kuchunguza vizuri nikauona mpira mwembamba uliopenya kwenye tundu ndogo kama la pipa la maji. Nilipoufuatilia ule mpira nikagundua kuwa ulikuwa ni mpira wa kiyoyozi cha kile chumba hivyo nikachukua kisu na kuukata kisha nikaanza kuuvuta. Muda mfupi uliofuata nikawa nimefanikiwa kuunyofoa ule mpira na hapo hewa safi na nyepesi ikaanza kupenya mle ndani na hapo akili yangu ikaanza kupata afya njema huku mwili wangu ukirudi katika hali yake ya kawaida. Sasa suala la hewa safi mle ndani likawa limerudi katika hali yake ya kawaida.
Nikaendelea kukwea juu zaidi ya kile chumba cha lifti nikipenya kwenye vile vyuma vya juu vilivyoshikilia kile chumba. Kulikuwa na mitambo mingine ya kuendeshea mjongeo wa kile chumba cha lifti ambayo hata nilipojitahidi kuichunguza mitambo ile bado sikuweza kufahamu namna ya ufanyakazi wake wa kazi. Baada ya kuvipita vile vyuma juu yake nikakutana na mfuniko mwingine wa chuma chepesi ambapo kulikuwa na nyaya nyingi za umeme zilizofungwa pamoja zilizokuwa zimepenya kwenye tundu dogo lililokuwa kwenye pembe ya ule mfuniko. Niliposogea karibu na kuchungulia kwenye lile tundu dogo kule juu nikaona uwazi mkubwa. Kwa msaada wa ile bisibis nikafungua kile kifuniko na kupenya zaidi kule juu. Muda mfupi baadaye nikawa nimetokezea sehemu salama zaidi iliyokuwa juu ya kile chumba katika eneo la wazi lililoniwezesha kuona vizuri kule juu ya kile chumba cha lifti na sehemu ya nje ya lile jengo kupitia kuta safi za kioo.
Upande wa kushoto eneo lile nikaliona bomba kubwa la chuma ingawa sikuweza kufahamu kuwa lile bomba lilikuwa likielekea wapi. Hata hivyo nilishawishika kulifuata lile bomba nikihisi kuwa huwenda lingekuwa msaada mkubwa katika kulitoroka eneo lile. Hivyo haraka nikalisogelea lile bomba na kujilaza juu yake kisha nikaanza kusota kwa tumbo nikielekea kule mbele lile bomba lilipokuwa likielekea. Lile bomba lilikuwa refu sana likipenya kwenye vipenyo kadhaa vya lile jengo.
Hatimaye nikafika sehemu ambapo lile bomba lilikuwa limebadili uelekeo na kuingia upande wa kulia. Nilipofika eneo lile sehemu ya chini nikaona vyumba vingi vinavyopakana na eneo kubwa la wazi. Hisia zangu zikanitanabaisha kuwa nilikuwa nimetokezea kwenye eneo la maliwato. Nilifurahi sana hivyo nikajiachia kwenye lile bomba na kutua kwenye vyoo vya wanaume vya ghorofa ile.
Kulikuwa na vyumba vitano vya vyoo eneo lile vilivyokuwa vikitazamana na eneo la wazi lenye masinki ya kunawia na vyoo vidogo vya marumaru vya haja ndogo ukutani. Mle ndani hapakuwa na mtu na mlango wa eneo lile ulikuwa umefungwa. Nikaachana na ule mlango wa eneo lile na kaingia kwenye choo kimoja. Nyuma ya kile choo kulikuwa na dirisha dogo la kioo linaloniwezesha kupenya vizuri hivyo nikafyatua komeo lake na kufungua lile dirisha. Halafu pasipo kupoteza muda nikapanda juu ya choo cha kukaa cha marumaru cha mle ndani kisha nikakanyaga tenki dogo la maji ya kusukumia uchafu na kuanza kupenya nikitoka nje ya kile chumba. Bado lile jengo lilikuwa limegubigwa na giza kila mahali na hali ile niliipenda sana kwani yeyote aliyekuwa akinifuatilia asingeweza kuniona kwa urahisi.
Mara baada ya kutoka kwenye lile dirisha nikaning’inia kwenye jukwaa dogo la zege lililokuwa chini ya lile dirisha huku nikitafuta namna ya kushuka kule chini ingawa sasa nilikuwa na matumaini ya usalama wangu kwani ule umbali wa kule chini ulikuwa umepungua. Nilipoendelea kuchunguza upande ule nikauona mti mmoja mkubwa wa kivuli hata hivyo matawi ya mti ule yalikuwa yameishia ghorofa ya pili hivyo ingenilazimu kushuka chini kwa ghorofa moja zaidi kabla ya kuyafikia matawi ya ule mti.
Sikuwa na namna nyingine ya kufanya hivyo nikaanza kuning’inia kwa tahadhari nikitoka dirisha la chumba kimoja kwenda dirisha la chumba kingine na ndani ya muda mfupi nikawa nimelifikia lile bomba dhaifu lililokuwa likitiririsha maji ya mvua kutoka kwenye paa la juu la lile jengo la ile hoteli. Nilipolifikia lile bomba nikaning’inia kwa tahadhari nikisota taratibu kushuka chini huku nikiwa mwangalifu lisije likakwanyuka na kuniangusha chini. Hivyo baada ya muda mfupi nikawa nimefanikiwa kulifikia paa dogo la dirisha la chumba kimoja cha ghorofa ya pili hivyo nikaliacha lile bomba na kurukia juu ya lile paa dogo la lile dirisha.
Nikiwa pale juu ya lile paa nikatulia kwa muda nikayatembeza macho yangu kulipeleleza vizuri eneo lile. Sikumuona mtu yeyote hivyo hali bado ilikuwa shwari na bila kupoteza muda nikajilaza tena juu ya lile paa nikianza kusota taratibu nikilifuata tawi moja la mti mkubwa wa kivuli uliokuwa kando kidogo na lile dirisha. Hatimaye nikawa nimelipata tawi moja imara lenye uwezo wa kuubeba uzito wangu bila mashaka yoyote. Taratibu na kwa tahadhari ya hali ya juu nikaanza kukwea lile tawi nikishuka chini ya ule mti. Macho yangu bado yalikuwa makini kulichunguza eneo lile. Muda mfupi uliofuata nikawa nimefanikiwa kushuka chini ya ule mti. Hata hivyo kabla ya kuondoka eneo lile nikatulia kidogo nikipeleleza kama kungekuwa na mtu yeyote eneo lile na niliporidhika kuwa bado nilikuwa salama nikachepuka na kuanza kutembea kwa tahadhari kando ya ukuta wa Le Tulip Hôtel Africaine nikipita kwenye vichaka vya maua ya kupandwa kuelekea mbele ya ile hoteli.
Wakati nikitembea nikawa nikiwakumbuka wale watu waliokuwa wakinifuatilia kule nyuma na lile gari jeupe Landcruiser na hatimaye kuzuiliwa na kile kizuizi cha askari jeshi kule barabarani na hapo nikajikuta nikiwahusisha wale watu na hawa niliofanikiwa kuwatoroka kwenye ile korido ya ghorofa ya tano ya lile jengo la hoteli muda mfupi uliopita. Sasa nilianza kuamini kuwa mpango wa kutekwa kwa Balozi Adam Mwambapa usiku ule kule nyumbani kwake ulikuwa umepangwa na kutekelezwa na kikundi cha askari jeshi wachache wa jeshi la wananchi wa Burundi huku nikishindwa kuelewa lengo lao.
Mvua bado ilikuwa ikiendelea kunyesha na giza zito lilikuwa limetanda kila mahali. Nilichokuwa nikiwaza kichwani ni kuondoka haraka eneo lile kabla masaibu mengine hayajanikuta eneo lile. Nikaendelea kutembea kwa tahadhari nikilizunguka lile jengo la hoteli kuelekea kule mbele nilipokuwa nimeegesha gari langu. Nilikuwa na kila hakika kuwa wale watu waliokuwa wakinifuatilia kule ghorofani wakati watakapofanikiwa kukifungua kile chumba cha lifti na kushikwa na mshangao mimi ningekuwa tayari niko mbali na eneo lile nikitokomea na jambo hilo lingenipa faraja sana.
Hata hivyo mambo hayakwenda kama nilivyokuwa nimetarajia kwani wakati nikifikia mbele ya lile jengo la hoteli mara nikaliona gari moja la jeshi aina ya Nissan Patrol likiingia kwa kasi na kuegesha katika maegesho ya mbele ya ile hoteli. Kisha kabla ya mlango wa lile gari kufunguliwa haraka nikamuona mtu mmoja akichepuka kutoka sehemu ya mbele ya ile hoteli na kulifuata lile gari. Nilipozidi kuchunguza nikagundua kuwa yule mtu alikuwa miongoni mwa wale watu wawili niliotoka kupambana nao na hatimaye kufanikiwa kuwatoroka kule juu ghorofani kwenye ile korido ingawa sikuweza kufahamu yule mwenzake alikuwa wapi kwa wakati ule. Yule mtu alipofika kwenye lile gari kioo cha dirishani kikashushwa na hapo nikamuona yule mtu akiongea na mtu mwingine pale dirishani huku akimuelekeza kwa kidole juu ya lile jengo la ghorofa la ile hoteli.
Nilihisi jambo fulani lisilo la kawaida kuelekea kutokea eneo lile hata hivyo sikuweza tena kulifikia lile gari langu pale kwenye yale maegesho kwani lile gari Nissan Patrol lilikuwa limechukua nafasi kando ya gari langu baada ya gari jingine lililokuwa pale kuondoka. Haukupita muda mrefu mara nikaona milango ya lile gari Nissan Patrol ikifunguliwa kisha wakashuka wanaume kumi na moja pamoja na mbwa wawili wakubwa aina ya German Shephered wenye urefu sawa na ule wa ndama wa kisasa. Lile gari Nissan Patrol lilikuwa dogo kuweza kuwabeba wale watu wote hata hivyo kwa kuwa ililazimishwa basi iliwezekana. Sasa nilitambua kuwa kikosi cha kunisaka kilikuwa kimeongezwa kama moja ya mkakati makini wa kuhakikisha kuwa sipati mwanya wowote wa kutoroka.
Wale watu walioshuka kutoka kwenye lile gari walikuwa wamevaa makoti marefu ya kijeshi ya mvua na mikononi walikuwa wameshika bunduki. Muda mfupi uliofuata nikawaona watu wawili wakielekea pale kwenye gari langu baada ya kuelekezwa na yule mtu wa awali. Wale watu walipofika wakalizunguka gari langu na kuanza kulikagua kwa tahadhari kisha nikamuona mmoja akitia utundu na kufungua mlango wa lile gari langu akiingia mle ndani. Sikuweza kufahamu kwa haraka kuwa lipi lilikuwa lengo la yule mtu hata hivyo nilihisi kuwa chochote ambacho kingefanyika ndani ya lile gari bila shaka kingekuwa katika moja ya mikakati yao mingi ya kutaka kunikamata kama siyo kuniangamiza kabisa.
Wakati wale watu wakiendelea kushughulika na gari langu mara nikamuona yule mtu wa awali aliyevaa suti akiongozana na watu watatu miongoni mwa wale watu walioshuka kutoka kwenye lile gari la jeshi wakielekea kwenye ile hoteli. Wale watu sita waliosalia nikawaona wakijigawa katika makundi mawili yenye watu watatu na kila kundi moja likawa likiongozwa na mbwa mmoja. Kundi moja likashika uelekeo wa upande wa kushoto wa lile jengo la hoteli na kundi jingine likashika uelekeo wa upande wa kulia wakija kwenye ile kona ya lile jengo nilipokuwa nimejibanza.
Nikiwa nimeanza kuhisi hatari ambayo ingenikabili sikutaka kuendelea kusubiri zaidi eneo lile kwani kwa namna moja au nyingine sikuona tena kama kungekuwa na uwezekano wa kuondoka pale kwa kutumia lile gari langu. Hivyo taratibu nikayaacha yale maficho yangu na kuanza kuondoka eneo lile nikirudi kule nyuma ya lile jengo nilipotoka huku nikiwaza namna ya kulitoroka eneo lile kabla wale watu hatari hawajanifikia.
Mvua kubwa ilikuwa ikiendelea kunyesha na nilitambua kuwa hali ile ingeweza kuathiri uwezo wa wale mbwa kunusa ardhini. Hata hivyo niliamini kuwa pale ambapo wale mbwa wangeniona isingewachukua muda mfupi kabla ya kunifikia na hiyo ingekuwa hatari zaidi kwangu.
Nilikumbuka kuwa nyuma ya lile jengo la hoteli kulikuwa na msitu mkubwa wa miti ya kupandwa hata hivyo kulikuwa na kipande kirefu cha uwanda kabla ya kuufikia ule msitu ambao hata hivyo nilikuwa mgeni kabisa wa mazingira yale. Nafsi yangu ikanitanabaisha kuwa ndani ya ule ndiyo ingekuwa sehemu salama ya kukimbilia katika kuisalimisha roho yangu. Hivyo mara tu baada ya kufika nyuma ya ile hoteli nikachepuka nikiliacha lile jengo kwa tahadhari na kuanza kukimbia kuelekea kwenye ule msitu. Hata hivyo kabla sijafika mbali na eneo lile mara ghafla umeme wa lile jengo la hoteli ukarudi na hivyo kupelekea taa za nyuma ya lile jengo kuwaka na kuangaza kila mahali. Kwa kweli nililaani vibaya kitendo kile cha umeme kurudi mapema kabla sijatimiza azima yangu. Nilipogeuka kutazama upande wa kushoto wa ile hoteli nikawaona watu wawili miongoni mwa wale watu watatu waliopita upande wa kushoto wa ile hoteli. Yule mwenzao mmoja aliyekuwa na yule mbwa sikumuona na wala sikuweza kutambua kuwa alikua ameshika uelekeo upi.
Wale watu wakawa kama waliosita ghafla baada ya kuniona eneo lile na mimi kuona vile hofu ikaniingia moyoni haraka na hivyo kushawishika kuwa nianze kutimua mbio. Hata hivyo nilijionya juu ya kuanza kutimua mbio za ghafla kwani kwa namna moja au nyingine nilihisi kuwa kwa kufanya vile ningeweza kutengeneza hakika juu ya hisia za wale watu dhidi yangu. Hivyo nikaamua kukazana nikiongeza urefu wa hatua zangu kuelekea kule msituni huku nikiwatazama wale watu kwa jicho la pembe. Hata hivyo baada ya kutafakari nikagundua kuwa ile ilikuwa hila dhaifu sana ya kuweza kuwahadaa watu wale kwani kitendo cha wale watu kuniona nikiharakisha kutembea kikawapelekea na wao waanze taratibu kutimua mbio wakinifuata. Kuona vile nikazidi kuchanganya miguu nikikimbia kistaarabu hata hivyo wale watu hawakuniacha kwani haraka nikawaona wakiaongeza mbio na kukatisha chini ya miti ya kivuli ya eneo lile kunifuata.
Hatimaye sikuona tena sababu ya kuendelea kupoteza muda kwa kujifanya kuwa watu wale hawakuwa na hamsini na mimi hivyo nikakusanya nguvu na kuanza kutimua mbio za uhakika nikikatisha kwenye ule uwanda kuelekea kule msituni huku nikiwa nimechukua tahadhari za kila namna. Nilipogeuka nyuma kutazama nikawaona wale watu nao wakitimua mbio...ITAENDELEA