mwamba c
JF-Expert Member
- Jan 2, 2017
- 690
- 2,363
- Thread starter
- #101
RIWAYA: UFUKWE WA MADAGASCAR
SEHEMU: 39
Mtunzi:Kelvin Mponda
...wakigeuka na kunitazama kwa mashaka wakiendelea kuzipanda zile ngazi kwa bidii. Sikugeuka tena nyuma kuwatazama badala yake nikakazana kuzitupa hatua zangu kuendelea mbele na safari.
Nilipomaliza kushuka zile ngazi nikawa nimetokezea kwenye korido ya ghorofa ya nne ambapo nilishika uelekeo wa upande wa kushoto nikielekea mwisho wa ile korido sehemu kulipokuwa na lifti ya lile jengo ili nishuke chini. Hata hivyo wakati nilipokuwa nikiikaribia ile sehemu ya lifti ya lile jengo mara ghafla nikakiona kile chumba cha lifti kikitia nanga kwenye korido ya ile ghorofa ya nne kisha mlango wake ulipofunguka akatoka mwanaume mmoja mweusi, mrefu na mwenye misuli imara ya nguvu mwilini huku akiwa amenyoa upara. Macho ya mtu yule yalikuwa yamefichwa vizuri nyuma ya miwani nyeusi. Yule mtu alikuwa amevaa suti nyeusi ambayo kutokana na ukubwa wa mwili wake wenye misuli imara suti ile ilionekana kama ambayo haimtoshi vizuri kwa namna ilivyombana katika baadhi ya maeneo ya mwili wake huku weusi wa ile suti na rangi yake vikimpelekea aonekane kama mpingo.
Kitendo cha kumuona yule mtu akija ule upande wangu kikaupelekea moyo wangu ulipuke kwa hofu huku kwa tahadhari nikiipapasa bastola yangu chini ya lile sinia nililolibeba mkononi baada ya kuanza kuhisi hali ya hatari. Yule mtu kuona vile akawahi kuupeleka mkono wake kwenye mfuko wa koti lake la suti huku akinikazia macho kunitazama kwa makini. Nikameza fundo kubwa la mate huku nikijitahidi kutabasamu hata hivyo ni kama tabasamu langu liliishia njiani kwa hofu na kunipelekea nionekane kama ninayetaka kucheka pasipo kitu cha kuchekesha. Yule mtu aliponikaribia akazidi kukaza uso wake kunitazama huku taratibu akipunguza urefu wa hatua zake huku mkono wake mmoja ukiwa bado upo kwenye mfuko wa ndani wa koti lake la suti. Haraka nikagundua kuwa alikuwa akiipapasa bastola yake mfukoni tayari kukabiliana na chochote.
Hofu ikiwa imeanza kuniingia nikapiga moyo konde na kumeza funda kubwa la mate kuitowesha hofu iliyoanza kujengeka nafsini mwangu na katika harakati za kurudisha hali ya kujiamini wakati nikipishana na yule mtu nikamuuliza huku nikilazimisha tabasamu la kirafiki usoni mwangu.
“Y at-il quelque chose de mal patron?”. Kuna tatizo lolote bosi?.
“Occupe toi de tes affaires”. Fuata mambo yako. Yule mtu akanijibu kwa jeuri huku taratibu akiutoa mkono wake mfukoni na kunipiga kumbo hafifu huku akiendelea na safari yake. Kwa sekunde kadhaa moyo wangu ukawa ni kama ulioshika ganzi huku baridi nyepesi ikisambaa mwilini mwangu. Hata hivyo nilijitahidi kwa kila namna kuimeza hofu yangu huku nikiendelea mbele na safari yangu pasipo kugeuka nyuma.
Wakati nikikifikia kile chumba cha lifti nikagundua kuwa kilikuwa kimepanda ghorofa ya juu kumpeleka mtu mwingine hivyo nikabonyeza kitufe cha kushuka chini kuiita ile lifti. Ile lifti iliposhuka na mlango wake kufunguka haraka nikaingia mle ndani na kubonyeza kitufe cha kushuka ghorofa ya chini kabisa ya lile jengo.
Wakati nikishuka chini ya lile jengo la ile hoteli mawazo mengi yakawa yakipita kichwani mwangu. Kupitia wale wanaume wawili niliopishana nao wakati nikishuka zile ngazi kuelekea ghorofa ya nne ya lile jengo na yule mtu matata niliyepishana naye muda mfupi uliopita kwenye ile korido. Sasa nilikuwa na hakika kuwa uwepo wangu kwenye lile jengo la hoteli ulikuwa ukifahamika na adui zangu lakini vilevile nilipokumbuka juu ya vile vifaa vya kijasusi nilivyovigundua kwenye miili ya wale watu niliopambana nao kule ofisini. Ilikuwa ni ishara tosha kuwa nilikuwa nimejitumbukiza kwenye mkasa hatari wa mapambano dhidi ya watu wenye ujuzi wa hali ya juu katika masuala ya kijasusi. Hivyo nafsi yangu ikazidi kunionya kuwa niwe makini sana na nyendo zangu.
Ndani ya muda mfupi kile chumba cha lifti kikawa kimefika ghorofa ya chini kabisa ya lile jengo la ile hoteli New Parador Residence. Mlango wa kile chumba cha lifti ulipofunguka nikatoka nje na kupishana na wanaume wengine wawili ambao haraka waligeuka na kunitazama kabla hawajaingia kwenye ile lifti. Mara tu nilipotoka kwenye kile chumba cha lifti sikutaka kutoka nje ya lile jengo kwa kupitia ule mlango mkubwa uliokuwa sehemu ya mbele ya ile hoteli. Hivyo haraka nikashika uelekeo wa upande wa kushoto nikipotelea gizani nyuma ya ile sehemu ya mapokezi ya ile hoteli huku nikijitahidi kutoyavuta macho ya mtu yeyote ambaye angekuwa akinitazama.
Sikuwa mwenyeji wa mazingira yale hivyo kwa kila namna nilijitahidi kuwa mwangalifu. Nyuma ya ile sehemu ya mapokezi nikatokezea kwenye korido pana yenye mwanga hafifu. Nikaanza kuufuata uelekeo wa korido ile pasipo kutambua ilikuwa ikielekea wapi huku mara kwa mara nikigeuka nyuma kutazama kama kulikuwa na mtu yoyote ambaye angekuwa akinifuatilia. Sikumuona mtu yoyote hivyo hali bado ilikuwa shwari. Nilipofika kule mbele nikagundua kuwa ile korido ilikuwa imebadili uelekeo na kufuata upande wa kulia na niliposoma kibao elekezi kwenye ile korido nikagundua kuwa ule uelekeo ulikuwa ni wa kwenda kwenye sehemu za maliwato ya wahudumu wa ile hoteli. Hivyo nikauacha ule uelekeo na kuanza kushuka ngazi zilizokuwa mbele ya kona ya ile korido sehemu yenye giza. Niliporidhika kuwa nimetokomea kabisa gizani sehemu ile nikalitelekeza chini lile sinia kisha nikazivua zile sare za mhudumu wa ile hoteli na kulivaa vyema lile koti langu jeusi la mvua. Ile chupa ya mvinyo mwekundu wa gharama wa kifaransa Château Lascombes nikaitia kwenye mfuko wa koti langu na kuzidi kushuka zile ngazi gizani.
Nilipofika chini kabisa ya zile ngazi nikashika uelekeo wa upande wa kushoto nikitembea katika uchochoro mwembamba wenye giza nene. Nilitamani kuwasha kurunzi yangu mkononi hata hivyo nilijikuta nikisita kufanya vile baada ya kuhisi kuwa mwanga wake ungeweza kumvuta mtu yeyote ambaye angekuwa eneo lile.
Baada ya safari fupi hatimaye nikaanza kuuona mwanga hafifu wa taa kabla ya kusikia maongezi ya watu eneo lile. Nilipochunguza nikagundua kuwa nilikuwa nimetokezea kwenye sehemu ya jiko la ile hoteli na wakati nikiendelea kutembea nikahisi kuwa nilikuwa nikilikaribia zaidi lile eneo la jiko la ile hoteli. Kwa mbali niliweza kuwaona wapishi katika sare zao za kazi wakiendelea na shughuli zao kwenye jiko lile. Hewa ya mle ndani ilikuwa nzito kidogo kutokana na moshi mwingi na joto kali ambalo lilikuwa likitoka kwenye ile sehemu ya lile jiko.
Niliendelea kutembea kwa utulivu na nilipokaribia lile jiko upande wa kulia nikaiona korido nyingine ambayo chini yake ilikuwa imetandazwa mabomba mengi ya maji, gesi na nyaya za umeme huku eneo lile likitawaliwa na harufu ya mnuko wa mafuta ya vyakula.
Hatimaye nikauacha ule uelekeo wa lile jiko la ile hoteli na kuanza kuifuata ile korido ya upande wa kulia kwa tahadhari huku mara kwa mara nikigeuka na kutazama nyuma kama kungekuwa na mtu yeyote akinifuatilia. Baada ya umbali mfupi wa safari yangu mara nikauona mlango mmoja wa chumba cha stoo. Nilipochunguza vizuri nikagundua ule mlango ulikuwa wazi na ndani yake kulikuwa na watu kutokana na minongʾono hafifu iliyokuwa ikisikika. Kwa tahadhari nikaupita mlango wa kile chumba na kuendelea mbele na safari yangu na baada ya hatua chache nikakutana na korido nyingine inayokatisha mbele yangu. Nilipofika kwenye ile korido nikasimama na kuanza kulichunguza eneo lile kwa makini.
Kulikuwa na giza zito eneo lile ingawa kupitia mwanga hafifu uliopenya kutoka lile eneo la jiko niliweza kuona kwa shida mandhari yale. Ile korido kwa upande wa kulia ilikuwa ikielekea kwenye tenki kubwa la maji ya akiba ya ile hoteli na nilipochunguza vizuri nikagundua kuwa hakukuwa na uelekeo mwingine baada ya ile sehemu yenye lile tenki la maji. Hivyo nikaamua kushika uelekeo wa upande wa kushoto nikitembea katikati ya korido nyembamba inayotazamana na vyumba vyenye mitambo ya umeme huku bastola yangu ikiwa imetuama vyema mkononi.
Baada ya muda mfupi nikawa nimetokezea kwenye sehemu kubwa ya wazi yenye mitambo mingine mikubwa ya umeme wa lile jengo likiwemo jenereta kubwa umeme wa dharura. Nilipofika pale nikasimama tena nikiyapeleleza vizuri mazingira yale na kwa kufanya vile upande wa kulia nikauona mlango mkubwa wa wavu na nondo za chuma kuelekea sehemu ya nyuma ya ile hoteli. Hisia zangu zikanieleza kuwa angalau nilikuwa kwenye eneo salama lenye unafuu wa kutoroka kwangu ingawa kwa namna moja au nyingine nilikuwa nikiamini kuwa mpaka kufikia wakati ule lile jengo la ile hoteli New Parador Residence lingekuwa chini ya uangalizi mkali wa watu waliokuwa wakifanya mawasiliano na wale watu niliopambana nao kule juu kwenye ile ofisi ya meneja wa ile hoteli ghorofani.
Nilipoitazama saa yangu ya mkononi nikagundua kuwa muda ulikuwa umeenda sana hata hivyo nilihisi mafanikio kidogo katika kazi yangu. Hatimaye nikaikamata vyema bastola yangu mkononi na kuanza kulitoroka taratibu eneo lile lakini mara moja nikiwa katika harakati zile mara nikajikuta nikimezwa na mshtuko wa aina yake. Moyo wangu ukapiga kite kwa nguvu na kupoteza utulivu huku nywele kichwani zikinicheza.
Hatua chache kutoka pale lilipokuwa lile jenereta la umeme wa dharura wa lile jengo la hoteli kulikuwa na mtu aliyesimama na sikuweza kuelewa ni kwa namna gani mtu yule hakuweza kushtukia uwepo wangu eneo lile. Ingawa kulikuwa na giza zito lakini miali hafifu ya mwanga wa taa uliopenya kutoka nje ya lile jengo uliniwezesha kumuona kwa shida kidogo yule mtu. Alikuwa mrefu zaidi yangu mwenye umbo lenye afya njema na alikuwa amevaa suti nadhifu ambayo sikuitambua haraka rangi yake kutokana na giza la ile sehemu na nilipomchunguza vizuri yule mtu nikagundua kuwa mkononi alikuwa ameshika bastola.
Yule mtu alikuwa akitazama upande mwingine wa lile eneo huku akiyatembeza macho yake huku na kule kama atafutaye kitu na hapo nikawaza kuwa huwenda yule mtu alikuwa mbali na lile eneo muda mfupi uliopita kabla ya kufika pale. Niliwahi haraka kurudi nyuma na kujibanza kwenye kona moja ya ukuta wa eneo lile huku kwa makini macho yangu yakimtazama yule mtu.
Kitambo kifupi cha ukimya kikaumeza mshtuko wangu huku nikiendelea kumtazama yule mtu kwa makini na bastola yangu mkononi. Baada ya kitambo kifupi mara nikamuona yule mtu akianza kuzitupa hatua zake kwa tahadhari kuja pale nilipojibanza huku akionekana kama aliyehisi jambo fulani. Macho yangu yakiwa makini kumtazama yule mtu nikaanza kujiandaa kumkabili. Hata hivyo kabla hajanifikia mara nikaona taa ndogo ya kijani ikiwaka kwenye sehemu ya ukosi wa koti lake la suti shingoni. Tukio lile likampelekea yule mtu asite kuendelea mbele na safari yake badala yake haraka akaupeleka mkono wake shingoni kurekebisha kifaa chake cha mawasiliano. Uzoefu wangu ukanitanabaisha kuwa kulikuwa na mtu mwingine mbali na eneo lile aliyekuwa akitaka kuwasiliana na yule mtu bahati mbaya sana maneno machache ya lugha waliotumia kuwasiliana watu wale sikuielewa ingawa nilikuwa na kila hakika kuwa ilikuwa ni lugha ya kirundi.
Muda mfupi baada ya mawasiliano kwenye kile kifaa cha mawasiliano cha yule mtu kukatika hewani mara nikamuona yule mtu akisitisha kuja pale nilipokuwa nimejibanza na badala yake haraka akabadili uelekeo akikatisha kwenye ile korido niliyotoka na kutokomea gizani. Kwa sekunde kadhaa nikaendelea kujibanza eneo lile huku nikiupisha utulivu nafsini mwangu. Ile sauti ya hatua hafifu za yule mtu taratibu ikaendelea kutokomea mbali na eneo lile na hatimaye kukoma kabisa. Sasa nilikuwa na kila hakika kuwa yule mtu alikuwa shirika moja pamoja na wale watu hatari waliokuwa wakiisaka roho yangu kwa udi na uvumba.
Kitambo kifupi cha ukimya kikapita wakati nikiendelea kufanya tathmini ya hali ya usalama wa eneo lile. Nilipojiridhisha kuwa hapakuwa na mtu mwingine eneo lile taratibu nikayaacha maficho yale kwa tahadhari na kuelekea kwenye ule mlango mkubwa wa nondo na wavu. Nilipofika na kuuchunguza vizuri ule mlango nikagundua kuwa lile geti lilikuwa limefungwa kwa mnyororo mkubwa na kufuli moja imara hata hivyo sikupata upinzani wowote kwani mfukoni nilikuwa na funguo zangu maalum kwa ajili ya kushughulika na maeneo korofi kama yale. Hivyo kwa tahadhari nikaifungua ile kufuli na kisha kuufungua na ule mnyororo. Nilipotoka nje nikaurudishia vizuri ule mlango na kulifunga lile geti kama nilivyolikuta.
Sasa nilikuwa nimetokezea sehemu ya nyuma ya lile jengo la New Parador Residence na mbele yangu niliweza kuona mabwawa matatu makubwa ya kupigia mbizi katika uwanja mkubwa wenye nyasi nzuri za kijani kibichi. Mabwawa yale yalikuwa yamezungukwa na viti maalum vya kupumzika chini ya miavuli mikubwa yenye rangi za kupendeza. Umbali mfupi baada ya ile sehemu yenye yale mabwawa ya kupigia mbizi kulikuwa na viwanja vitatu vikubwa vya michezo. Kiwanja kimoja cha mpira wa kikapu, kingine cha mpira wa mikono na kiwanja cha mwisho kilikuwa cha mazoezi ya viungo ya kawaida.
Eneo kubwa lililosalia lilikuwa ni la kiwanja cha mpira wa golf hata hivyo kiwanja kile kilizungukwa na sehemu nzuri zenye viti visivyohamishika vya kupumzika vilivyokuwa chini ya miti mirefu ya vivuli. Mandhari ile ilikuwa ni ya kupendeza sana hata hivyo nilipoendelea kulichunguza lile eneo sikuweza kumuona mtu yeyote ingawa hali ile haikuwa kigezo tosha cha kunihakikishia kuwa eneo lile halikuwa chini ya ulinzi.
Nikiwa bado nayatathmini vizuri mazingira yale kando ya ule mlango mkubwa wa wavu na nondo mara ghafla nikauona mwanga mkali wa kurunzi ikimulika mulika mle ndani kwenye lile eneo la chini la lile jengo nilipotoka muda mfupi iliopita. Haraka nikawahi kusogea kando na kujibanza huku nikichungulia na kutazama mle ndani. Kwa kufanya vile nikawaona wanaume wawili wakiwa na bastola zao mikononi huku mmoja akiwa ameshika kurunzi mkononi mwake.
Kulikuwa na mabishano hafifu baina yao ingawaje sikuweza kuambulia kitu kupitia ile lugha waliyokuwa wakiizungumza ambayo niliihisi kuwa ilikuwa ni lugha ya kirundi. Hata hivyo kupitia vitendo niliweza kuhisi kiini cha mabishano yale baina ya wale watu wawili.
Yule mtu aliyeshika ile kurunzi mkono wake mwingine ulikuwa umezishika zile sare za mhudumu wa ile hoteli ambazo muda mfupi uliopita nilikuwa nimetoka kuzivua na kuzitelekeza mle ndani gizani. Yule mtu alikuwa akimuonesha mwenzake zile nguo huku akimfokea kwa jazba dhahiri akionekana kushikwa na hasira. Kupitia tukio lile nikafahamu kuwa mpango wangu wa kutoroka kwenye lile jengo haukuwa siri tena kwani wale watu hatari tayari walikuwa wameingʾamua vyema hila yangu...ITAENDELEA
SEHEMU: 39
Mtunzi:Kelvin Mponda
...wakigeuka na kunitazama kwa mashaka wakiendelea kuzipanda zile ngazi kwa bidii. Sikugeuka tena nyuma kuwatazama badala yake nikakazana kuzitupa hatua zangu kuendelea mbele na safari.
Nilipomaliza kushuka zile ngazi nikawa nimetokezea kwenye korido ya ghorofa ya nne ambapo nilishika uelekeo wa upande wa kushoto nikielekea mwisho wa ile korido sehemu kulipokuwa na lifti ya lile jengo ili nishuke chini. Hata hivyo wakati nilipokuwa nikiikaribia ile sehemu ya lifti ya lile jengo mara ghafla nikakiona kile chumba cha lifti kikitia nanga kwenye korido ya ile ghorofa ya nne kisha mlango wake ulipofunguka akatoka mwanaume mmoja mweusi, mrefu na mwenye misuli imara ya nguvu mwilini huku akiwa amenyoa upara. Macho ya mtu yule yalikuwa yamefichwa vizuri nyuma ya miwani nyeusi. Yule mtu alikuwa amevaa suti nyeusi ambayo kutokana na ukubwa wa mwili wake wenye misuli imara suti ile ilionekana kama ambayo haimtoshi vizuri kwa namna ilivyombana katika baadhi ya maeneo ya mwili wake huku weusi wa ile suti na rangi yake vikimpelekea aonekane kama mpingo.
Kitendo cha kumuona yule mtu akija ule upande wangu kikaupelekea moyo wangu ulipuke kwa hofu huku kwa tahadhari nikiipapasa bastola yangu chini ya lile sinia nililolibeba mkononi baada ya kuanza kuhisi hali ya hatari. Yule mtu kuona vile akawahi kuupeleka mkono wake kwenye mfuko wa koti lake la suti huku akinikazia macho kunitazama kwa makini. Nikameza fundo kubwa la mate huku nikijitahidi kutabasamu hata hivyo ni kama tabasamu langu liliishia njiani kwa hofu na kunipelekea nionekane kama ninayetaka kucheka pasipo kitu cha kuchekesha. Yule mtu aliponikaribia akazidi kukaza uso wake kunitazama huku taratibu akipunguza urefu wa hatua zake huku mkono wake mmoja ukiwa bado upo kwenye mfuko wa ndani wa koti lake la suti. Haraka nikagundua kuwa alikuwa akiipapasa bastola yake mfukoni tayari kukabiliana na chochote.
Hofu ikiwa imeanza kuniingia nikapiga moyo konde na kumeza funda kubwa la mate kuitowesha hofu iliyoanza kujengeka nafsini mwangu na katika harakati za kurudisha hali ya kujiamini wakati nikipishana na yule mtu nikamuuliza huku nikilazimisha tabasamu la kirafiki usoni mwangu.
“Y at-il quelque chose de mal patron?”. Kuna tatizo lolote bosi?.
“Occupe toi de tes affaires”. Fuata mambo yako. Yule mtu akanijibu kwa jeuri huku taratibu akiutoa mkono wake mfukoni na kunipiga kumbo hafifu huku akiendelea na safari yake. Kwa sekunde kadhaa moyo wangu ukawa ni kama ulioshika ganzi huku baridi nyepesi ikisambaa mwilini mwangu. Hata hivyo nilijitahidi kwa kila namna kuimeza hofu yangu huku nikiendelea mbele na safari yangu pasipo kugeuka nyuma.
Wakati nikikifikia kile chumba cha lifti nikagundua kuwa kilikuwa kimepanda ghorofa ya juu kumpeleka mtu mwingine hivyo nikabonyeza kitufe cha kushuka chini kuiita ile lifti. Ile lifti iliposhuka na mlango wake kufunguka haraka nikaingia mle ndani na kubonyeza kitufe cha kushuka ghorofa ya chini kabisa ya lile jengo.
Wakati nikishuka chini ya lile jengo la ile hoteli mawazo mengi yakawa yakipita kichwani mwangu. Kupitia wale wanaume wawili niliopishana nao wakati nikishuka zile ngazi kuelekea ghorofa ya nne ya lile jengo na yule mtu matata niliyepishana naye muda mfupi uliopita kwenye ile korido. Sasa nilikuwa na hakika kuwa uwepo wangu kwenye lile jengo la hoteli ulikuwa ukifahamika na adui zangu lakini vilevile nilipokumbuka juu ya vile vifaa vya kijasusi nilivyovigundua kwenye miili ya wale watu niliopambana nao kule ofisini. Ilikuwa ni ishara tosha kuwa nilikuwa nimejitumbukiza kwenye mkasa hatari wa mapambano dhidi ya watu wenye ujuzi wa hali ya juu katika masuala ya kijasusi. Hivyo nafsi yangu ikazidi kunionya kuwa niwe makini sana na nyendo zangu.
Ndani ya muda mfupi kile chumba cha lifti kikawa kimefika ghorofa ya chini kabisa ya lile jengo la ile hoteli New Parador Residence. Mlango wa kile chumba cha lifti ulipofunguka nikatoka nje na kupishana na wanaume wengine wawili ambao haraka waligeuka na kunitazama kabla hawajaingia kwenye ile lifti. Mara tu nilipotoka kwenye kile chumba cha lifti sikutaka kutoka nje ya lile jengo kwa kupitia ule mlango mkubwa uliokuwa sehemu ya mbele ya ile hoteli. Hivyo haraka nikashika uelekeo wa upande wa kushoto nikipotelea gizani nyuma ya ile sehemu ya mapokezi ya ile hoteli huku nikijitahidi kutoyavuta macho ya mtu yeyote ambaye angekuwa akinitazama.
Sikuwa mwenyeji wa mazingira yale hivyo kwa kila namna nilijitahidi kuwa mwangalifu. Nyuma ya ile sehemu ya mapokezi nikatokezea kwenye korido pana yenye mwanga hafifu. Nikaanza kuufuata uelekeo wa korido ile pasipo kutambua ilikuwa ikielekea wapi huku mara kwa mara nikigeuka nyuma kutazama kama kulikuwa na mtu yoyote ambaye angekuwa akinifuatilia. Sikumuona mtu yoyote hivyo hali bado ilikuwa shwari. Nilipofika kule mbele nikagundua kuwa ile korido ilikuwa imebadili uelekeo na kufuata upande wa kulia na niliposoma kibao elekezi kwenye ile korido nikagundua kuwa ule uelekeo ulikuwa ni wa kwenda kwenye sehemu za maliwato ya wahudumu wa ile hoteli. Hivyo nikauacha ule uelekeo na kuanza kushuka ngazi zilizokuwa mbele ya kona ya ile korido sehemu yenye giza. Niliporidhika kuwa nimetokomea kabisa gizani sehemu ile nikalitelekeza chini lile sinia kisha nikazivua zile sare za mhudumu wa ile hoteli na kulivaa vyema lile koti langu jeusi la mvua. Ile chupa ya mvinyo mwekundu wa gharama wa kifaransa Château Lascombes nikaitia kwenye mfuko wa koti langu na kuzidi kushuka zile ngazi gizani.
Nilipofika chini kabisa ya zile ngazi nikashika uelekeo wa upande wa kushoto nikitembea katika uchochoro mwembamba wenye giza nene. Nilitamani kuwasha kurunzi yangu mkononi hata hivyo nilijikuta nikisita kufanya vile baada ya kuhisi kuwa mwanga wake ungeweza kumvuta mtu yeyote ambaye angekuwa eneo lile.
Baada ya safari fupi hatimaye nikaanza kuuona mwanga hafifu wa taa kabla ya kusikia maongezi ya watu eneo lile. Nilipochunguza nikagundua kuwa nilikuwa nimetokezea kwenye sehemu ya jiko la ile hoteli na wakati nikiendelea kutembea nikahisi kuwa nilikuwa nikilikaribia zaidi lile eneo la jiko la ile hoteli. Kwa mbali niliweza kuwaona wapishi katika sare zao za kazi wakiendelea na shughuli zao kwenye jiko lile. Hewa ya mle ndani ilikuwa nzito kidogo kutokana na moshi mwingi na joto kali ambalo lilikuwa likitoka kwenye ile sehemu ya lile jiko.
Niliendelea kutembea kwa utulivu na nilipokaribia lile jiko upande wa kulia nikaiona korido nyingine ambayo chini yake ilikuwa imetandazwa mabomba mengi ya maji, gesi na nyaya za umeme huku eneo lile likitawaliwa na harufu ya mnuko wa mafuta ya vyakula.
Hatimaye nikauacha ule uelekeo wa lile jiko la ile hoteli na kuanza kuifuata ile korido ya upande wa kulia kwa tahadhari huku mara kwa mara nikigeuka na kutazama nyuma kama kungekuwa na mtu yeyote akinifuatilia. Baada ya umbali mfupi wa safari yangu mara nikauona mlango mmoja wa chumba cha stoo. Nilipochunguza vizuri nikagundua ule mlango ulikuwa wazi na ndani yake kulikuwa na watu kutokana na minongʾono hafifu iliyokuwa ikisikika. Kwa tahadhari nikaupita mlango wa kile chumba na kuendelea mbele na safari yangu na baada ya hatua chache nikakutana na korido nyingine inayokatisha mbele yangu. Nilipofika kwenye ile korido nikasimama na kuanza kulichunguza eneo lile kwa makini.
Kulikuwa na giza zito eneo lile ingawa kupitia mwanga hafifu uliopenya kutoka lile eneo la jiko niliweza kuona kwa shida mandhari yale. Ile korido kwa upande wa kulia ilikuwa ikielekea kwenye tenki kubwa la maji ya akiba ya ile hoteli na nilipochunguza vizuri nikagundua kuwa hakukuwa na uelekeo mwingine baada ya ile sehemu yenye lile tenki la maji. Hivyo nikaamua kushika uelekeo wa upande wa kushoto nikitembea katikati ya korido nyembamba inayotazamana na vyumba vyenye mitambo ya umeme huku bastola yangu ikiwa imetuama vyema mkononi.
Baada ya muda mfupi nikawa nimetokezea kwenye sehemu kubwa ya wazi yenye mitambo mingine mikubwa ya umeme wa lile jengo likiwemo jenereta kubwa umeme wa dharura. Nilipofika pale nikasimama tena nikiyapeleleza vizuri mazingira yale na kwa kufanya vile upande wa kulia nikauona mlango mkubwa wa wavu na nondo za chuma kuelekea sehemu ya nyuma ya ile hoteli. Hisia zangu zikanieleza kuwa angalau nilikuwa kwenye eneo salama lenye unafuu wa kutoroka kwangu ingawa kwa namna moja au nyingine nilikuwa nikiamini kuwa mpaka kufikia wakati ule lile jengo la ile hoteli New Parador Residence lingekuwa chini ya uangalizi mkali wa watu waliokuwa wakifanya mawasiliano na wale watu niliopambana nao kule juu kwenye ile ofisi ya meneja wa ile hoteli ghorofani.
Nilipoitazama saa yangu ya mkononi nikagundua kuwa muda ulikuwa umeenda sana hata hivyo nilihisi mafanikio kidogo katika kazi yangu. Hatimaye nikaikamata vyema bastola yangu mkononi na kuanza kulitoroka taratibu eneo lile lakini mara moja nikiwa katika harakati zile mara nikajikuta nikimezwa na mshtuko wa aina yake. Moyo wangu ukapiga kite kwa nguvu na kupoteza utulivu huku nywele kichwani zikinicheza.
Hatua chache kutoka pale lilipokuwa lile jenereta la umeme wa dharura wa lile jengo la hoteli kulikuwa na mtu aliyesimama na sikuweza kuelewa ni kwa namna gani mtu yule hakuweza kushtukia uwepo wangu eneo lile. Ingawa kulikuwa na giza zito lakini miali hafifu ya mwanga wa taa uliopenya kutoka nje ya lile jengo uliniwezesha kumuona kwa shida kidogo yule mtu. Alikuwa mrefu zaidi yangu mwenye umbo lenye afya njema na alikuwa amevaa suti nadhifu ambayo sikuitambua haraka rangi yake kutokana na giza la ile sehemu na nilipomchunguza vizuri yule mtu nikagundua kuwa mkononi alikuwa ameshika bastola.
Yule mtu alikuwa akitazama upande mwingine wa lile eneo huku akiyatembeza macho yake huku na kule kama atafutaye kitu na hapo nikawaza kuwa huwenda yule mtu alikuwa mbali na lile eneo muda mfupi uliopita kabla ya kufika pale. Niliwahi haraka kurudi nyuma na kujibanza kwenye kona moja ya ukuta wa eneo lile huku kwa makini macho yangu yakimtazama yule mtu.
Kitambo kifupi cha ukimya kikaumeza mshtuko wangu huku nikiendelea kumtazama yule mtu kwa makini na bastola yangu mkononi. Baada ya kitambo kifupi mara nikamuona yule mtu akianza kuzitupa hatua zake kwa tahadhari kuja pale nilipojibanza huku akionekana kama aliyehisi jambo fulani. Macho yangu yakiwa makini kumtazama yule mtu nikaanza kujiandaa kumkabili. Hata hivyo kabla hajanifikia mara nikaona taa ndogo ya kijani ikiwaka kwenye sehemu ya ukosi wa koti lake la suti shingoni. Tukio lile likampelekea yule mtu asite kuendelea mbele na safari yake badala yake haraka akaupeleka mkono wake shingoni kurekebisha kifaa chake cha mawasiliano. Uzoefu wangu ukanitanabaisha kuwa kulikuwa na mtu mwingine mbali na eneo lile aliyekuwa akitaka kuwasiliana na yule mtu bahati mbaya sana maneno machache ya lugha waliotumia kuwasiliana watu wale sikuielewa ingawa nilikuwa na kila hakika kuwa ilikuwa ni lugha ya kirundi.
Muda mfupi baada ya mawasiliano kwenye kile kifaa cha mawasiliano cha yule mtu kukatika hewani mara nikamuona yule mtu akisitisha kuja pale nilipokuwa nimejibanza na badala yake haraka akabadili uelekeo akikatisha kwenye ile korido niliyotoka na kutokomea gizani. Kwa sekunde kadhaa nikaendelea kujibanza eneo lile huku nikiupisha utulivu nafsini mwangu. Ile sauti ya hatua hafifu za yule mtu taratibu ikaendelea kutokomea mbali na eneo lile na hatimaye kukoma kabisa. Sasa nilikuwa na kila hakika kuwa yule mtu alikuwa shirika moja pamoja na wale watu hatari waliokuwa wakiisaka roho yangu kwa udi na uvumba.
Kitambo kifupi cha ukimya kikapita wakati nikiendelea kufanya tathmini ya hali ya usalama wa eneo lile. Nilipojiridhisha kuwa hapakuwa na mtu mwingine eneo lile taratibu nikayaacha maficho yale kwa tahadhari na kuelekea kwenye ule mlango mkubwa wa nondo na wavu. Nilipofika na kuuchunguza vizuri ule mlango nikagundua kuwa lile geti lilikuwa limefungwa kwa mnyororo mkubwa na kufuli moja imara hata hivyo sikupata upinzani wowote kwani mfukoni nilikuwa na funguo zangu maalum kwa ajili ya kushughulika na maeneo korofi kama yale. Hivyo kwa tahadhari nikaifungua ile kufuli na kisha kuufungua na ule mnyororo. Nilipotoka nje nikaurudishia vizuri ule mlango na kulifunga lile geti kama nilivyolikuta.
Sasa nilikuwa nimetokezea sehemu ya nyuma ya lile jengo la New Parador Residence na mbele yangu niliweza kuona mabwawa matatu makubwa ya kupigia mbizi katika uwanja mkubwa wenye nyasi nzuri za kijani kibichi. Mabwawa yale yalikuwa yamezungukwa na viti maalum vya kupumzika chini ya miavuli mikubwa yenye rangi za kupendeza. Umbali mfupi baada ya ile sehemu yenye yale mabwawa ya kupigia mbizi kulikuwa na viwanja vitatu vikubwa vya michezo. Kiwanja kimoja cha mpira wa kikapu, kingine cha mpira wa mikono na kiwanja cha mwisho kilikuwa cha mazoezi ya viungo ya kawaida.
Eneo kubwa lililosalia lilikuwa ni la kiwanja cha mpira wa golf hata hivyo kiwanja kile kilizungukwa na sehemu nzuri zenye viti visivyohamishika vya kupumzika vilivyokuwa chini ya miti mirefu ya vivuli. Mandhari ile ilikuwa ni ya kupendeza sana hata hivyo nilipoendelea kulichunguza lile eneo sikuweza kumuona mtu yeyote ingawa hali ile haikuwa kigezo tosha cha kunihakikishia kuwa eneo lile halikuwa chini ya ulinzi.
Nikiwa bado nayatathmini vizuri mazingira yale kando ya ule mlango mkubwa wa wavu na nondo mara ghafla nikauona mwanga mkali wa kurunzi ikimulika mulika mle ndani kwenye lile eneo la chini la lile jengo nilipotoka muda mfupi iliopita. Haraka nikawahi kusogea kando na kujibanza huku nikichungulia na kutazama mle ndani. Kwa kufanya vile nikawaona wanaume wawili wakiwa na bastola zao mikononi huku mmoja akiwa ameshika kurunzi mkononi mwake.
Kulikuwa na mabishano hafifu baina yao ingawaje sikuweza kuambulia kitu kupitia ile lugha waliyokuwa wakiizungumza ambayo niliihisi kuwa ilikuwa ni lugha ya kirundi. Hata hivyo kupitia vitendo niliweza kuhisi kiini cha mabishano yale baina ya wale watu wawili.
Yule mtu aliyeshika ile kurunzi mkono wake mwingine ulikuwa umezishika zile sare za mhudumu wa ile hoteli ambazo muda mfupi uliopita nilikuwa nimetoka kuzivua na kuzitelekeza mle ndani gizani. Yule mtu alikuwa akimuonesha mwenzake zile nguo huku akimfokea kwa jazba dhahiri akionekana kushikwa na hasira. Kupitia tukio lile nikafahamu kuwa mpango wangu wa kutoroka kwenye lile jengo haukuwa siri tena kwani wale watu hatari tayari walikuwa wameingʾamua vyema hila yangu...ITAENDELEA