Riwaya: Ufukwe wa Madagascar

Riwaya: Ufukwe wa Madagascar

RIWAYA: UFUKWE WA MADAGASCAR
SEHEMU: 52

"Bonjour”. Habari. Nikamsalimia yule askofu huku nikiupuuza mshangao wake.
“Quʾest-ce que a besoin dʾici?”. Unataka nini hapa?. Yule askofu akaniuliza kwa jazba.
“Une brève conversation, sʾil vous plaît, puis-je rester?”. Maongezi mafupi tu na wewe, tafadhali ninaweza kuketi?. Taratibu nikaongea huku nikikisogelea kiti kimoja kilichokuwa mkabala na ile meza ya yule askofu. Chuki sasa ilikuwa dhahiri machoni kwa yule askofu hata hivyo nilikuwa tayari kukabiliana naye ingawa kwa namna nyingine nilishindwa kuelewa chuki kwa mtumishi wa Mungu kama yule ingetokana na nini. Hatimaye nikavuta kiti na kuketi baada ya kuchoka kusubiri ukaribisho rasmi kwani nilimuona yule askofu akiinama na kuendelea na hamsini zake kana kwamba uwepo wangu haukuwa na maana yoyote mle ndani. Nikachukizwa sana na aina ile ya dharau vinginevyo ningeweza kumtia adabu yule askofu hata hivyo lile halikuwa suala lililonifikisha pale hivyo nikaishia kujipa utulivu wa nafsi. Yule askofu akaondoa miwani yake usoni na kuiweka pale mezani kisha akayafikicha macho yake kivivu na kupiga mwayo hafifu kisha akaiegemeza mikono yake mezani katika uso wa chuki na ghadhabu kabla ya kuongea.
“Jʾai beaucoup de travail à faire, ce nʾest pas temps pour rencontrer de gens. Qui vous a permis dʾentrer dans mon bureau”. Nina kazi nyingi za kufanya, huu siyo muda wa kuonana na watu. Nani aliyekuruhusu uingie ofisini kwangu?.
“Jʾai besoin de parler avec toi”. Nahitaji kuongea na wewe. Uso wangu ukiwa mbali na mzaha nikaongea kwa utulivu huku nikimtazama yule askofu. Yule askofu akanitazama kwa mshangao kisha nikamuona akitabasamu kwa dharau kabla ya kuniambia.
“Dʾaccord, vous pouves parler”. Okay, zungumza.
Hata hivyo wakati nilipokuwa nikijiandaa kutoa hoja yangu yule askofu akaniuliza.
“Qui est-tu?” Wewe ni nani?.
Swali la yule askofu likanipelekea niketi vizuri na kuiegemeza mikono yangu pale mezani na nilipomtazama machoni nikavunja ukimya.
“Désolé pour le travail de Dieu. Je mʾapelle Géorge Ntahimana”. Kwanza pole sana na kazi ya Mungu. Mimi naitwa Géorges Ntahimana. Wakati nikimaliza kujitambulisha mara nikashangaa kumuona yule askofu akitabasamu na muda mfupi uliofuata tabasamu lake likageuka kicheko kikubwa kilichoniacha na mduwao wa aina yake ingawa sikutia neno lolote. Yule askofu akaendelea kucheka kama mwehu na kicheko chake kilipokuwa ukingoni akavunja ukimya.
“Utilise to nom de Tibba Ganza, tu sera bien éntendu”. Tumia jina lako la Tibba Ganza utaeleweka vizuri. Maneno ya yule askofu yakanifanya nishtuke huku nikishangazwa na kulijua jina langu. Kwa kweli nilistaajabu sana, sasa nilifahamu kuwa taarifa zangu nchini Burundi zilikuwa zimezagaa kila kona. Nimefahamika vipi na nani anayesambaza taarifa zangu?. Nikajiuliza bila kupata majibu hata hivyo sikuonesha tashwishi yoyote usoni.
“Appelle-moi de toute façon”. Unaweza kuniita upendavyo.
“Et pourquoi tu me menteque tu est Géorges Ntahimana alors que tu tʾapelle Tibba Ganza?”. Sasa kwa nini unidanganye kuwa wewe ni Gèorges Ntahimana wakati unaitwa Tibba Ganza?” Yule askofu akaongea huku akiendelea kucheka.
“Je ne tʾai pas menti, cʾest toi quia voul de mʾapelle ça”. Sijakudanganya ila ni wewe ndiye umeniita hivyo. Nikaongea kwa hasira kidogo huku nikianza kuchoshwa na tabia ile ya dharau.
“Dʾaccord, tu as quel probléme?”. Okay, una shida gani?. Yule askofu akaniuliza huku akinikazia macho.
“Jʾai bésoin de voir du prêtre Aloysius Kanyameza”. Nahitaji kuonana na padri Aloysius Kanyameza. Nikaongea kwa utulivu na hapo yule askofu akanikata jicho kama mtu anayetafuta hakika ya maneno yangu kisha akavunja ukimya.
“Pourquoi?”. Unamuhitaji wa nini?.
“Son amie proche”. Mimi ni rafiki yake wa karibu. Nikadanganya na hapo yule Askofu akaangua tena kicheko cha dhihaka.
“Mais le prêtre Aloysius Kanyameza nest jamais dit nous àpropos de toi?”. Mbona padri Aloysius Kanyameza hakuwahi kutuambia juu ya habari zako?.
“Peut être nʾa fait cela pour ses propres raisons”. Huwenda alifanya hivyo kwa sababu zake binafsi. Maelezo yangu yakampelekea tena yule askofu aangue kicheko cha dhihaka kisha akavunja ukimya akinipuuza.
“Ne mentes-moi parce-que je conais chaque chose à propos de toi. Est-ce-que tu pense que je ne conais pas que cʾest toi qui lui a tue’?. S’il vous plais leve-toi et partir. Dieu te jugera à son”. Usinidanganye kwani nafahamu kila kitu kuhusu wewe. Unadhani sifahamu kuwa wewe ndiye uliyemuua?. Tafadhali simama uende zako. Mungu atakuhukumu kwa muda wake.
“Vous ne saves pas de quoi vous parlez”. Hujui unachozungumza. Nikaongea kwa msisitizo na hapo yule askofu akanitazama kwa dhihaka kisha akavuta mtoto wa meza yake ya ofisini na kutoa picha nne ambazo alizitupia pale mezani mbele yangu bila kutia neno. Haraka nikasogea pale mezani na kuzitazama vizuri zile picha na mara moja nilipoziona nikashtuka sana. Zilikuwa ni picha nilizopigwa na kamera za usalama wakati nilipokuwa ndani ya kile chumba 403 cha Le Tulip Hôtel Africaine wakati nikiupekuwa ule mwili wa yule padri wa kizungu aliyenyongwa.
Mara moja nikagundua kuwa huwenda picha zile zingekuwa zimenaswa na kamera maalum ya siri iliyokuwa imepandwa mle ndani. Nikaanza kujilaumu kwa kutokuwa makini kiasi cha kupigwa picha zile bila kushtukia. Lakini jambo moja lilikuwa limenishangaza sana. Picha zile ziliwezaje kumfikia yule askofu tena mapema kiasi kile?. Nani alifahamu kuwa ningefika pale hadi akatanguliza picha zile kuniwekea ukuta katika kupata taarifa muhimu za upelelezi wangu?. Maswali meni yakaanza kupita kichwani mwangu na nilipomtazama yule askofu nikaanza kuhisi kuwa alikuwa miongoni mwa watu wale hatari waliokuwa wakinisaka usiku na mchana.
“Ce nʾest pas moi qui là tué prêtre Aloysius Kanyameza”. Mimi siyo niliyemuua padri Aloysius Kanyameza. Nikaongea kwa utulivu huku nikiendelea kuzitazama zile picha kwa makini.
“Je te conceille jeûne hôme di être loi de cette casse parce-que ton âme sera en danger”. Nakushauri kijana kaa mbali na hili suala vinginevyo uhai wako utauweka matatani. Yule askofu akaongea kwa hadhari huku akiviminyaminya vidole vyake pale mezani.
“Je suis ici pour aider atraper celui qui là tue”. Nipo hapa kusaidia kumnasa yeyote aliyehusika na kifo chake.
“Qui est mort?”. Kifo cha nani?. Yule askofu akaniuliza huku akiyafikicha macho yake na kisha kuitia miwani yake machoni na hapo akanitazama kwa utulivu.
“Prêtre Aloysius Kanyameza”. Padri Aloysius Kanyameza. Nikaongea kwa msisitizo huku mawazo mengi yakipita kichwani mwangu kisha baada ya kukohoa kidogo nikaendelea.
“Que-ce que tu pense come la cause de sa mort?”. Unadhani ni sababu ipi iliyopelekea kifo chake?. Swali langu likampelekea yule askofu taratibu aangue tabasamu la dharau huku akinitazama kisha akaegemea kiti chake cha ofini baada ya kuyabetua mabega yake.
“Coment puis je connaitre?”. Mimi nitajuaje?. Lilikuwa jibu lililonikatisha tamaa sana na kunipelekea kwa sekunde kadhaa nimtazame yule askofu pasipo kutia neno ingawa akili yangu ilikuwa imezama katika kufikiri juu ya nini kilichokuwa kikiendelea. Taratibu nikayahamisha macho yangu na kuanza kuyatembeza mle ndani nikiichunguza tena ile ofisi kana kwamba ndiyo nilikuwa nimeingia mle ndani muda mfupi uliopita. Hisia za kushindwa katika harakati zangu zilikuwa zimeanza kunisimanga kiasi cha kunipelekea nishindwe kufahamu kama nilikuwa nikipiga hatua au nilikuwa nimejitumbukiza kwenye mkasa usiyonihusu. Taswira mbaya ya yule padri wa kizungu aliyenyongwa vibaya kwa waya na kutundikwa katikati ya chumba 403 cha Le Tulip Hôtel Africaine haraka ikaumbika tena akilini mwangu na kuibua hoja ambazo majibu yake yangehitaji mazingira rafiki.
“Prêtre Aloysius Kanyameza a un amie qui sapelle Pierre Opango?”. Padri Aloysius Kanyameza amewahi kuwa na rafiki yeyote anayeitwa Pierre Opango?. Hatimaye nikavunja ukimya na kumuuliza yule askofu huku nikirejesha macho yangu kwake. Yule askofu akanitazama na mara ile hakutaka kutumia kifaransa tena katika maongezi yetu.
“Nadhani swali hilo ni yeye mwenyewe ndiye anayeweza kukujibu”.
“Ningekuwa na uwezo wa kuongea na marehemu huwenda wewe ungekuwa mtu wa mwisho kukufikia”. Maelezo yangu yakampelekea yule askofu anikate jicho lenye kila kaishiria cha kuchoshwa na maongezi yale kabla ya kuongea kwa utulivu huku akinitazama.
“Muda siyo mrefu utapata nafasi nzuri ya kufanya mahojiano naye huko kuzimu”. Yule askofu akaongea kwa kujiamini kisha akasogeza nyuma kiti chake cha ofisini na kusimama huku akiendelea kunitazama. Maneno ya yule askofu yakawa yameniacha njia panda na hapo nikaanza kuhisi jambo la hatari. Hatimaye akavunja tena ukimya na kuendelea.
“Najua kwanini upo hapa nchini Burundi, najua nini kilichokuleta hapa hivyo hakuna namna unayoweza kunificha Tibba”. Yule askofu akaweka kituo akikohoa kidogo kisha akaendelea tena.
“Kwa miaka mingi nchi yako Tanzania imekuwa ikijizolea sifa nyingi kutoka kwa mabwana wakubwa wa nchi za magharibi eti kuwa ni kisiwa cha amani. Sifa hizo zimekuwa zikiwavimbisha kichwa na kuwapelekea mjione kuwa kweli mna amani kiasi cha kuingilia taratibu za nchi nyingine na kujipa nafasi za usuruhishi wa migogoro kana kwamba kweli mna amani wakati chaguzi zenu zinatawaliwa na mizengwe ya uibaji wa kura na ubadilishwaji wa matokeo. Tanzania haina amani labda niseme kuwa ina idadi kubwa ya wanaume wengi waoga kama wanawake”. Yule askofu akaweka kituo akinitazama ingawa nilipomchunguza nikagundua kuwa alikuwa akijipa utulivu katika kufikiri jambo fulani. Kisha akaendelea tena
“Tanzania ndiyo nchi pekee ambayo waziri wake anaweza kutumia shilingi milioni kumi, pesa za wananchi walipa kodi kununulia mboga ya kula na familia yake, na bado wananchi wakamchagua tena ili aendelee kuwatumikia. Tanzania ndiyo nchi pekee ambayo waziri wake anatafuna pesa za walipokodi shilingi bilioni moja na kujinadi mbele ya waandishi wa habari kuwa eti pesa hiyo ni vijisenti tu, na bado raia wake wakakaa kimya bila kufanya chochote. Tanzania ndiyo nchi pekee ambayo kiongozi wa nchi anafanya safari zaidi ya 360 nje ya nchi kwa pesa za walipakodi huku raia wake wamekaa kimya bila kuchukua hatua yoyote.
Tanzania ndiyo nchi pekee duniani ambayo wanyapori wake wanatoroshwa kwa ndege ya jeshi ya nchi nyingine kwenda ughaibuni huku viongozi wa nchi wakijitia kutofahamu chochote huku raia wake wakiishilia kulalamika majumbani mwao bila kuchukua hatua yoyote. Wapinzani wa vyama vyenu vya siasa wanakamatwa, wanapigwa, wanadhalilishwa na kusekwa rumande wakifunguliwa mashtaka ya kipuuzi huku raia wenu wamekaa kimya tu wasione tatizo lolote. Sisi siyo waoga kama nyinyi na tumeikataa hali hiyo. Tunataka kuona nchi ya Burundi yenye umoja na usawa na hatutaki katu kuingiliwa mambo yetu”. Yule askofu akaweka kituo na hivyo kunipa nafasi nzuri ya kuyatafakari vizuri maneno yake.
Katika baadhi ya hoja zake niliona kuwa huwenda alikuwa sahihi kabisa lakini sikuona kama pale palikuwa mahala pake. Ni dhahiri kuwa askofu yule alikuwa ameshikwa na jazba na mara moja nilipomchunguza nikagundua kuwa alikuwa akifahamu mengi yaliyojificha nyuma ya kifo cha padri Aloysius Kanyameza kuliko nilivyodhani. Nikameza funda kubwa la mate kujipa utulivu nafsini mwangu huku macho yangu yakiendelea kumtazama yule askofu kwa makini na sasa alikuwa ametia mikono yake katika mifuko ya joho lake.
“Nani aliyekupa habari zangu?”. Hatimaye nikavunja ukimya kwa kumuuliza yule askofu na hapo nikajikuta nikishtushwa na kicheko chake. Kicheko chenye kila mikogo ya dhihaka na kejeli.
“Ningekueleza lakini nadhani hilo siyo suala lililokuleta hapa”. Hatimaye yule askofu akaongea huku akitabasamu na kwa mara ya kwanza nikajikuta nikikabiliana na msongo mkubwa wa mawazo. Nikahisi kuwa taarifa zangu zote sasa zilikuwa kiganjani kwa adui. Nani aliyewapasha watu wale habari zangu?. Nikajiuliza pasipo kupata majibu hata hivyo nilipomtazama yule askofu nikamuona kuwa ndiye angekuwa chanzo cha kwanza cha taarifa muhimu nilizokuwa nikizihitaji. Hivyo kichwani nikaanza kupanga mahesabu namna nitavyoitupa vyema karata yangu.
“Nahitaji msaada wako tafadhali”. Nikaongea kwa sauti ya utulivu.
“Chochote kuhusu masuala ya kiimani na kanisa…?”
“Hapana, ni kuhusu padri Aloysius Kanyameza, chochote unachofahamu kuhusu kifo chake”
“Unahitaji vipi taarifa za kifo chake wakati mshukiwa wa kwanza wa kifo chake ni wewe?. Unapoteza muda wangu bure hapa. Simama utoke ofisini kwangu”. Yule askofu akafoka kwa jazba na hapo nikasogeza kiti nyuma na kusimama.
“Kama utapata nafasi ya kurudi nchini kwako salama nenda ukamueleze bosi wako kuwa kazi aliyokutuma imekushinda”. Yalikuwa maneno ya karaha na yenye kufedhehesha na mimi sikuwa tayari kamwe kukubaliana nayo. Hivyo nikapanga namna ya kumkabili yule askofu kibabe huku nikiamini kuwa angekuwa na majibu ya kuridhisha. Hata hivyo sikufanikiwa kwani wakati nikijiandaa kumkabili yule askofu nikajikuta nikitazamana na mdomo wa bastola yenye uchu mikononi mwa yule askofu. Koo likanikauka ghafla, baridi nyepesi ikaanza kusambaa mwilini mwangu huku mapigo ya moyo yakipoteza kabisa utulivu.
“Huwendi kokote tulia hapohapo, huu ndiyo mwisho wako”. Yule askofu akanionya huku akiwa makini na nyendo zangu. Kwa kweli nilistaajabu sana kwa vile sikuwahi kufikiria kuwa kiongozi wa kiroho kama yule angeweza kuwa muumini namba moja wa mtutu wa bunduki na hapo nikashusha pumzi na kumtazama kwa utulivu.
“Ni watu wangapi umefanikiwa kuwauwa kwa mkono wako hadi sasa?”. Nikamuuliza yule askofu kwa utulivu huku nikimtazama, lengo langu likiwa ni kuununua muda zaidi.
“Wengi sana sikumbuki hata hivyo nafurahi sana kuua mtu kwa manufaa ya taifa langu”
“Ni manufaa yapi unayoyazungumzia?”. Nikamuuliza kwa udadisi.
“Wewe siyo raia wa nchi hii hivyo siyo rahisi ukanielewa”
“Kwa hiyo kwa kuniua mimi unadhani kuwa utatimiza hiyo nadharia ya uzalendo dhidi ya nchi yako?”
“Hilo halikuhusu, toa bastola yako na uiweke mezani. Nakusihi usithubutu kufanya hila kwani risasi yangu moja tu inaweza kubadili jina lako” Yule askofu akanionya na maneno yake yalikuwa dhahiri na hali ile ikanitia mashaka.
“Nadhani hujui unachokifanya”. Nikaongea kwa utulivu huku akili yangu ikipiga mahesabu namna ya kujinasua kwenye hatari ile.
Mdomo wa ile bastola ya yule askofu sasa ulikuwa umbali mfupi mbele yangu. Utayari wa kidole chake kwenye kile kilimi cha bastola ukanitahadharisha kuwa mtikisiko hafifu ungeweza kuruhusu risasi kupenya kichwani mwangu na kuacha tundu dogo linalovuja damu na huo ndiyo ungekuwa mwisho wangu. Hivyo sikutaka kupuuza hata hivyo wakati nikiendelea kufikiria namna ya kukabiliana na tukio lile ghafla mlango wa ile ofisi nyuma yangu ukafunguliwa kwa kasi ya ajabu na kabla sijageuka vizuri kutazama nyuma yangu nikazabwa kofi zito la shingoni. Haraka nikaupeleka mkono wangu mafichoni kuifikia bastola yangu. Bahati mbaya mko wangu ukaishia njiani kwani kwa mtindo hatari wa judo ule mkono ukadakwa njiani na kuzungushwa kwa kasi ya ajabu na kufungashwa mgongoni kwangu kisha nikachezea kichapo cha ngumi mbili makini za mbavuni. Mwili ukatengeneza mitetemo dhaifu, maumivu makali yakasambaa mwilini, mbavu zikabana na hapo kichomi dhaifu kikanipelekea niachame mdomo wazi na kuhema taratibu kama bata aliyemeza gololi ya moto.
“Tulia hivyo hivyo kenge weh!”. Sauti kavu ya kiume kutoka nyuma yangu ikanionya. Muda uleule nikapigwa kabari matata shingoni iliyoniruhusu kuhema kwa shida na nguvu iliyotumika ilikuwa kubwa mno kana kwamba nilikuwa nimekaidi agizo. Sikuweza kufurukuta kwani kabari ile ilikuwa kama pingu kiasi kwamba kadili nilivyokuwa nikijitahidi kujinasua ndivyo kipenyo cha koo langu kilivyozidi kupungua. Wakati nikiwa katika harakati za kujipanga mara nikaanza kufanyiwa upekuzi wa haraka na mikono miwili makini iliyokuwa ikifanya kazi ile ikanitanabaisha kuwa nyuma yangu kulikuwa na wanaume wawili makini.
Zoezi la upekuzi hatimaye likafika ukomo huku bastola yangu na vitambulisho vyangu vikichuliwa na adui. Yule mtu alipomaliza kunipekua akageuka na kunizaba makofi mawili ya nguvu usoni na hivyo kunipelekea nione taswira tofauti za nyota kubwa na ndogo kabla ya kamasi nyepesi za damu kuanza kuchuruzika puani na maumivu niliyasikia ni kama niliyepigwa na kipande cha ubao wa mninga. Kiganja cha mkono wa yule mtu kilikuwa kimekomaa kama simenti.
“Safi sana mwanaharakati wetu, tulikuwa na wasiwasi kuwa pengine ungeshindwa kumdhibiti huyu kunguni”. Yule mtu aliyenipiga kabari nyuma yangu nikamsikia akizungumza kwa sauti kavu ya kibabe. Nikashindwa kuelewa nani alikuwa akiambiwa maneno yale. Lakini kitendo cha kumuona yule askofu akitabasamu nikajua maneno yale yalimhusu yeye.
“Kazi imekuwa rahisi sana kama mnavyoona. Hivi mlijuaje kuwa angekuja hapa?”. Yule askofu akawauliza wale watu huku bastola yake bado amielekezea kwangu.
“Imekuwa kama bahati kwani tulipewa habari na François”. Yule mtu nyuma yangu akafafanua.
“François ndiyo nani?”
“Mwanaharakati mwenzetu dereva wa teksi tuliyempandikiza katikati ya jiji la Bujumbura”. Maneno ya yule mtu alitenipiga kabari nyuma yangu yakanipelekea nishtuke. Haraka nikawa nimemkumbuka yule dereva wa teksi aliyenitoroka kule barabarani msituni na kupitia maelezo yake sikuwa na shaka yoyote kuwa ndiye aliyesemekana kuwapasha habari zangu wale watu hatari. Loh! kwa kweli sikuwa nimemfikiria kabisa yule dereva wa teksi hata chembe kuwa angekuwa miongoni mwao.
“Nini mnachokitaka kwangu?”. Nikawauliza wale watu kwa hasira wakati yule mtu aliyekuwa akinipekuwa mifukoni alipokuwa akiendelea kuvipitia vitambulisho vyangu...ITAENDELEA
 
RIWAYA; UFUKWE WA MADAGASCAR
SEHEMU:53

“Tunataka uhai wako lakini kabla ya kufanya kazi yetu kuna mambo machache tungependa kuyafahamu”. Yule mtu aliyenipiga kabali nyuma yangu akafoka kibabe.
“Mnataka kuniua kwa kosa gani?”. Nikawauliza wale watu huku akili yangu ikifanya kazi na wakati nikiwa katika hali mara nikamuona yule mtu wa pili aliyekuwa akivipitia vitambulisho vyangu akiachia tabasamu hafifu la kifedhuri kisha akasogea karibu yangu na kunichapa kofi la nguvu usoni.
“Unaweza kutueleza hizi pasipoti tatu, zenye picha yako na majina matatu tofauti na uraia wa nchi tatu zina maana gani?”. Yule mtu aliyekuwa akinipekuwa akaniuliza na sasa niliweza kumuona vizuri. Alikuwa mwanaume mrefu mno na mweusi kama lami. Sura yake mbaya haikuvutia kuitazama mara mbili. Alikuwa miongoni mwa wale watu walioingia kule kanisani muda mfupi uliopita.
“Jibu swali uliloulizwa wewe ngedere”. Yule mtu nyuma yangu akafoka huku akizidi kunikwida kabali na kwa kweli nilisikia maumivu makali sana huku nikihema kwa taabu. Yule askofu mbele yangu nikamuona akinikenulia meno kama fisi kwa furaha.
“Sina jibu lolote”. Nikaongea kwa shida huku nikijitahidi kujinasua kwenye ile kabali bila mafanikio.
“Tunakufahamu vizuri wewe ngedere usijitie hufahamu chochote”. Yule mtu nyuma yangu akafoka kwa hasira.
“Sasa kama mnanijua vizuri kwanini mnaniuliza au mnapenda kusikia sauti yangu?”. Nikaongea kwa hasira.
“Kwanini unafanya ujasusi wakati unafahamu kuwa ukikamatwa adhabu yake ni kifo?”. Yule mtu aliyenichapa kofi akaniuliza huku akinishika taya langu la nchini na kunikodolea macho yenye kila dalili za roho mbaya iliyopindukia.
“Nani aliyewaambia kuwa mimi ni jasusi”. Nikawauliza wale watu hata hivyo kabla sijajibiwa yule mtu mwenye sura mbaya akanichapa ngumi mbili kavu za tumbo zilizonipelekea nianze kuhisi kichefuchefu.
“Tangu lini swali likajibiwa kwa swali. Hatutaki malumbano ya kipuuzi hapa”. Yule mtu nyuma yangu akafoka huku akizi kunikwida hali iliyonipelekea nining’inie juu juu.
“Umefikia wapi hapa jijini Bujumbura?”. Yule mtu mwenye sura mbaya akaniuliza huku akinikodolea macho kwa hasira.
“Nimefikia Le Tulip Hôtel Africaine kwenye chumba kinachotazama na chumba 403”
“Muongo mkubwa wewe”
“Kama hamniamini si muende mkahakikishe”. Nikaongea kwa msisitizo huku nikijiweka sawa na wakati nikifanya vile nikamsikia yule mtu nyuma yangu akicheka.
“Usijidanganye, unadhani tutakupa nafasi nyingine ya kufanya hila?. Huwendi popote, tuambie umekuja hapa kufanya nini?”. Yule mtu nyuma yangu akaniuliza kwa ghadhabu.
“Wapi?, hapa kanisani au hapa nchini Burundi?”. Nikawauliza wale watu huku lengo langu kuununua muda. Hata hivyo sikuweza kuendelea kuongea kwani nilianza kushushiwa kipigo cha ngumi za kila mahali na yule mtu mwenye sura mbaya utadhani amepiga chafya kali iliyogomea njiani. Nikapiga yowe kali la maumivu nikimsihi yule mtu aniache hata hivyo haikusaidia kitu kwani yule mtu aliendelea kunishushia kipigo cha mbwa mwizi.
“Hebu muache kidogo huwenda sasa akayajibu maswali yetu vizuri”. Yule mtu alinipiga kabali nyuma akamwambia yule mtu mwenye sura mbaya aliyekuwa akinishushia kipigo. Kufuatia kipigo kile halia yangu ilikuwa imeanza kuwa mbaya. Kipigo kile kilikuwa ni cha ufundi wa hali ya juu huku yule mpigaji akionekana kutumia nguvu nyingi isivyokawaida. Maumivu makali yakasambaa mwilini na sasa nilianza kuhisi kizunguzungu huku nikihema hovyo.
“Tuambie umekuja hapa kufanya nini?”. Yule mtu akaniuliza tena.
“Nimekuja hapa Burundi kutembea na vilevile kutafuta fursa za uwekezaji kwenye soko la Afrika Mashariki”. Nikadanganya na hapo wale watu wakaniangalia kwa ghadhabu kisha wakapeana ishara fulani na hapo nikaanza tena kushushiwa kichapo. Kwa kweli maumivu ya kipigo kile yalikuwa makali mno hata hivyo macho yangu yalikuwa makini kuutazama ule mdomo wa bastola ya yule Askofu kwa namna ulivyokuwa ukinitazama kwa uchu. Kipigo kile kikaendelea kwa ufundi wa hali ya juu na kwa namna ile hali yangu ikazidi kuwa mbaya.
Sasa nilianza kuona hatari ya kuendelelea kutuhusu kipigo cha aina ile hivyo mara moja nikayatembeza macho yangu nikimtazama yule Askofu kisha nikayahamishia kwa yule mtu mwenye sura mbaya aliyekuwa akinishushia kipigo. Tathmini yangu ikanitanabaisha kuwa wale watu walikuwa wameanza kupoteza umakini. Sikutaka kusubiri zaidi hivyo muda uleule nikakusanya nguvu kisha nikampiga kichwa matata cha kinyumenyume yule mtu aliyenipiga kabari nyuma yangu na kuuvunja vibaya mwamba wa pua yake huku akipiga yowe kali la maumivu. Yule mtu akaniachia bila kupenda huku damu nyingi ikimtoka puani.
Yule Askofu mbele yangu kuona vile akavuta kilimi cha bastola yake mkononi kunilenga lakini shabaha yake ilikuwa dhaifu kwani haraka nikawahi kuinama, ile risasi iliyofyatuliwa ikanipalaza kidogo begani na kuchubua koti langu kisha ikasafari na kuuvunja mfupa wa bega la yule mtu nyuma yangu na hapo nikamsikia yule mtu nyuma yangu akipiga yowe kali la maumivu lililosindikizwa na tusi zito mle ndani. Yule mtu mwenye sura mbaya kuona vile akawa ni kama aliyepigwa na butwaa na lile likawa kosa kubwa kuwahi kufanya na binadamu yule kwani niliwahi kumchapa pigo moja la nguvu makini la kareti shingoni mwake kwa kutumia mikono yangu yote miwili. Lile pigo lilikuwa na athari kubwa dhidi ya mtu yule kwani muda uleule nikamuona akianza kulegea na iile ikawa nafasi nzuri ya kumrukia na kumchapa kabala huku nijizungusha pale mezani kama pia na kufanikiwa kumnasa kwa kabali makini ya miguu yangu yule Askofu na hapo ile bastola mkononi ikamuanguka chini hivyo akabaki akifurukuta kwa nguvu zake zote kujinasua kwenye ile kabali yangu makini bila mafanikio.
Yule mtu mwenye sura mbaya sasa nilikuwa nimemdhibi kikamilifu kwa kabali yangu hivyo kuona vile akaingiza mkono kwenye mfuko wa koti lake la suti kuchomoa bastola. Risasi ya kwanza aliyoifyatua kunilenga kichwani nyuma yake nikawahi kuikwepa na hapo ikachana dari ya ile ofisi na kupasua taa ya mle ndani na hapo sauti mbaya ya mlio wa risasi na mpasuko wa ile taa ukasikika mle ndani. Risasi ya pili wakati inafyatuliwa nikawahi kuusukuma mkono wake hivyo yule mtu akapoteza tena shabaha yake hivyo ile risasi ikachimba chini sakafuni. Yule mtu alipotaka kufyatua risasi ya tatu hakufanikiwa kwani nilikaza zaidi misuli imara ya mikono yangu na kumpelekea yule mtu ashindwe kuhema vizuri na hivyo kuishiwa nguvu kisha nikaivunja shingo yake. Yule mtu akapiga yowe kali la maumivu huku amajishika koo na hapo nikamuachia na kumsukumia chini huku akiwa hoi hajitambui.
Yule Askofu alikuwa bado aking’ang’ana kujinasua kwenye ile kabala yangu matata ya miguu lakini kamwe halikuwa jambo rahisi hata kidogo kwani kabala yangu ilikuwa imemnasa shingoni kikamilifu kama nyororo ngumu ya kuvutia magogo. Macho yalikuwa yamemtoka pima huku mishipa ya shingoni imemtutumka kama mizizi. Mara moja nilipoyatupa macho yangu kule mbele nikamuona yule mtu aliyekuwa akinipiga kabala pale awali akijizoazoa pale chini sakafuni, mkono wake mmoja akiwa amalishika lile jeraha lake la risasi linalovuja damu begani huku mkono wake mwingine ukiwa umeshika bastola na kuilekezea kwangu. Kuona vile nikawahi kuifungua ile kabala yangu shingoni kwa yule Askofu kisha nikamchapa teke maridadi la kifua lenye uzito sawa na tofali moja la zege nikimbamiza ukutani.
Nilipogeuka kumtazama yule mtu pale mlangoni nikamuona akininyooshea bastola kisha akavuta kilimi cha bastola yake kunilenga. Nikiwa tayari nimeiona hatari ile haraka nikajirusha na kuteleza kwa tumbo juu ya ile meza na hatimaye kuangukia upande wa pili. Ile risasi ikanikosa na hapo yule mtu akaanza kufyatua risasi hovyo kunilenga name nikawa nijitahidi kuzikwepa zile rasasi kwa kuhamahama kwa kujificha nyuma ya ile meza ofisini. Hali ilikuwa tete hata hivyo nilijitahidi kwa kila namna risasi zile zisinifikie. Kwa kufanya vile hatimaye nikaifikia ile bastola ya yule Askofu kule ilipoangukia. Haraka nikaizoa na kuitia mikononi kisha nikawahi kujitupa chini na nikiwa pale chini nikafanikiwa kuiona miguu ya yule mtu aliyekuwa upande wa pili wa ile meza. Bila kujishauri nikavuta kilimi cha bastola yangu mkononi na hapo risasi moja ikavunja mfupa wa mguu wa yule mtu na kumsababishia maumivu makali yaliyompelekea apige yowe kali la maumivu na kuanza kurukaruka kama ndama. Risasi yangu ya pili ikamalizia ule mguu wa yule mtu uliosalia na hapo yule mtu akaanguka chini sakafuni hivyo kichwa chake nikawa nikikiona vizuri. Risasi yangu ya tatu ikafunga kazi kichwani mwake na kusababisha tundu dogo kwenye fuvu linalovuja damu.
Nikiwa katikati ya furaha ile mara kufumba na kufumbua yule Askofu kutoka kule alipokuwa kuwa akajizoa na kunirukia shingoni akinipiga kabali ya nguvu. Nilipomuelekezea yule Askofu bastola ile nimtulize akawahi kuupiga mkono wangu na kwa kuwa sikuwa nimejiandaa vizuri kwa tukio lile ile bastola yangu mkononi ikaniponyoka na kuteleza hadi kwenye uvungu wa kabati la mle ndani. Yule Askofu kuona vile akazidi kuikaza vizuri kabali yake shingoni kwangu na hivyo kunipelekea nishindwe kuhema vizuri. Nikajitahidi kufurukuta kwenye kabala ile bila mafanikio. Ile kabali ilikuwa na madhara ya haraka sana kwa binadamu hivyo nilipoona hali yangu ya kiafya inazidi kuwa mbaya nikaamua kupiga mikono sakafuni kama mwanamieleka aliyekubali kushindwa nikimsihi yule Askofu aniachie lakini ilikuwa kazi bure kwani ndiyo kwanza lile tukio lilionekana kumfurahisha sana yule Askofu na hivyo kuongeza nguvu za kutosha kunikaba shingoni. Hali yangu ikazidi kuwa mbaya zaidi kwani ni kama mzunguko wa damu kuja kichwani mwangu ulikuwa umezimika kwa muda, hewa nikawa naitafuta kwa udi na uvumba huku nikijihisi kutaka kulia na kutapika kwa wakati mmoja.
Nilipoona kuwa hapakuwa na mazingira yoyote ya msamaha nikakusanya nguvu za kutosha na kunyanyuka ju na yule yule Askofu kisha nikambeba mzegamzega nikirudi kinyumenyume na kwenda kumbwaga juu ya ile meza ya ofisini kama gunia la viazi. Ilikuwa hila nzuri kwani nilimsikia yule Askofu akipiga yowe kali la maumivu na kuniachia bila kupenda na hapo nikageuka kwa wepesi wa hali ya juu na kumzima teke la tumbo. Hata hivyo yule Askofu alikuwa mpiganaji hodari na mwepesi hivyo akalipangua lile teke langu kama mzaha kisha haraka akajibetua pale mezani na kunichapa teke la kichwani lililoniyumbisha na kunisababishia maumivu makali yaliyoambatana na kizunguzungu kibaya. Nikapepesuka kama mlevi huku nikirudi kinyumenyume.
Yule Askofu kuona vile akaniwahi akiruka hewani na kunizaba mateke mawili ya kifuani ya flying kicks. Loh! sikuwa na ujanja tena kwani nguvu ya mapigo yale ya ufundi ilitosha kabisa kunirusha na kunibamiza kwenye rafu ya vitabu ilikuwa ukutani mle ndani. Ile rafu ya vitabu ikachanguka na vile vitabu vikatawanyika hovyo sakafuni. Maumivu makali yakiwa yameanza kunishambulia mwilini nikahisi hatari kubwa ilikuwa mbioni kunifikia hivyo nikaamua kujidhatiti vizuri.
Pigo linguine la teke la yule Askofu liliponijia nikawahi kuliona hivyo nikainama kidogo kulikwepa huku likisababisha mvumo wa upepo masikioni mwangu hivyo pigo lile likakata upepo bila mafanikio. Pigo lingine la teke la yule Askofu liliponijia nalo nikawahi kulikwepa hivyo likaenda kukita ukutani na kuacha alama. Mtindo ule wa urushaji wa mateke ya ufundi yule Askofu alionekana kuumudu vyema bila kuweka angalizo na hilo lilikuwa kosa lake kubwa kwani wakati pigo lake la tatu la teke likinijia nikawahi kulikwepa kwa kuinama chini kidogo huku nikiwekeza nuvu za kutosha kisha nikamshona ngumi moja makini ya korodani. Pigo lile likampelekea yule Askofu abweke kama mbwa mwizi aliyepigwa na tofali huku akizishika malighafi zake.
Sikutaka kumchelewesha yule Askofu hivyo nikamzaba teke makini la shingoni. Yule Askofu akawahi kuliona lakini hakufanikiwa kulipangua vizuri hivyo likamvunja vidole viwili vya mkono wake. Pigo la pili nikampiga kifuani na kichwani. Pigo langu la tatu la teke yule Askofu akalidaka lakini wakati akiwa katikati ya furaha nikajibetua hewani na kuchapa teke moja makini la kichwani huku nikiangua upande wa pili. Kama bondia aliyetupiwa sumbwi zito yule Askofu akapiga yowe kali huku pigo langu likionekana kumlevya hivyo akapepesuka kabla ya kupiga mweleka wa nguvu na hatimaye kuangukia kwenye ile meza ya ofisini.
Nikawahi kumfikia yule Askofu pale chini ili nimuongezee dozi kamili lakini bahati mbaya alikuwa hajiwezi kwa hali. Damu nyingi ilikuwa ikimtoka puani na masikioni, mdomo wake ulikuwa umepasuka na kuanza kuvimba kama aliyeumwa na nyigu. Jicho lake moja lilikuwa likitokwa na damu...ITAENDELEA
 
RIWAYA: UFUKWE WA MADAGASCAR
SEHEMU; 54

Jicho lake moja lilikuwa likitokwa na damu huku lile lingine limevimba likiona kwa shida na alikuwa akihema hovyo kutafuta hewa safi kama mhanga wa mgodini. Hata alipojitahidi kusimama hakufanikiwa kwani kipigo changu kilikuwa kimemlevya vibaya.
“Pole sana mtu wa Mungu, sikujua kuwa u hodari wa mapambano ya ana kwa ana kwa kiwango hiki”. Nikamwambia yule Askofu baada ya kumsogelea na kuinama huku nikiitazama saa yangu ya mkononi.
“Go to hell you bastard!”. Yule Askofu akaongea kwa shida huku maneno yake yakisikika kwa taabu kama kibogoyo. Nikamkwida shingoni na kumchapa makofi mawili ya nguvu usoni ili kumweka sawa.
“Niambie, balozi Adam Mwambapa mmempeleka wapi?”. Nikamuuliza kwa hasira hata hivyo nilishangaa kumuona yule Askofu akiangua kicheko cha dharau na nilipomtazama usoni haraka nikagundua kuwa hakuwa tayari kunijibu.
“Unadhani nitakwambia?”. Yule Askofu akaongea kwa shida huku damu nyingi ikimtoka mdomoni kisha akakohoa kidogo na kuendelea.
“Unapoteza muda wako bure na tambua kuwa huwezi katu kuizuia mipango yetu”
“Mipango gani?”. Nikamuuliza yule Askofu huku nikimtazama kwa udadisi hata hivyo hakunijibu tena badala yake nikamuona ni kama anayetaka kuongea jambo fulani kiasi cha kupelekea kinywa chake kufunguka kwa shida huku damu nyingi ikimtoka. Muda mfupi uliofuata nikayaona macho yake yakipoteza nuru na kuanza kufumba taratibu, mwili wake ukalegea na hatimaye akakata roho.
Kwa sekunde kadhaa nikabaki nikimkodolea macho yule Askofu huku maswali mengi yakipita kichwani mwangu. Maneno ya yule Askofu wakati aliponiambia ‘Unapoteza muda wako bure na tambua kuwa huwezi katu kuizuia mipango yetu’ yalikuwa yameniacha njia panda huku nikishindwa kabisa kuelewa kuwa watu wale ni akina nani na hiyo mipango yao ilihusu nini. Nilipoitazama saa yangu ya mkononi nikashtushwa na mwenendo wa majira yake. Muda ulikuwa umesonga sana huku nikihisi kuwa sikuwa nimepata fununu zozote za kunisaidia katika harakati zangu.
Sikutaka kupoteza muda zaidi mle ndani hivyo haraka nikasimama na kuanza kuipeleleza vizuri ile ofisi. Nilianza kwa kuchukua vitambulisho vyangu kutoka kwa mmoja wa wale watu niliopambana nao mle ndani ambao sasa walikuwa marehemu. Bastola yangu nikaitia kibindoni na kuanza kuichunguza ile ofisi kila sehemu. Nilianza kwa kupekuwa vitabu vilivyokuwa kwenye ile rafu ukutani kisha nikahamia kwenye kabati la mle ndani nikipekua mafaili. Sikupata chochote cha maana katika upekuzi wangu hivyo hatimaye nikahamia kwenye ile meza ya ofisini nikifungua droo moja baada ya nyingine. Mle namo sikuambulia kitu chochote cha maana bali vitabu vichache vya dini, mihutasari ya vikao vya kanisa vilivyofanyika siku za nyuma na kitabu kimoja chenye rekodi za matoleo ya ibada. Bado sikupata chochote cha maana cha kunisaidia hivyo nikahamia kuifanyia upekuzi miili ya wale watu niliopambana nao mle ndani.
Kitendo cha kuifanyia ile miili upekuzi wa kina kikanipelekea nigundue kitu kimoja muhimu. Katika mfuko mdogo wa koti la suti la yule mtu wa kwanza kunipiga kabali nikakuta kipande kidogo cha karatasi kichochanwa hovyo pasipo kuzingatia ustaarabu kikiwa kimekunjwa na kufinyangwa. Nilipokichukua kile kikaratasi na kukifungua juu yake nikaona maandishi madogo ya hati mbovu yakisomeka “Maison numéro 27,Rue de la Ruvubu”-Nyumba namba 27, Mtaa wa Ruvubu. Mara nilipomaliza kuyasoma maelezo yale akili yangu ikachangamka na kupata afya njema.
Nikakitia kile kikaratasi mfukoni huku nikiendelea kufanya upekuzi. Wakati nikiendelea na upekuzi ule nikajikuta nikikumbuka kuwa wale watu niliotoka kupambana nao mle ndani muda mfupi uliopita walikuwa watatu kwa idadi yao wakati walipokuwa wakiingia kule kanisani. Hivyo nikawaza kuwa mmoja wao huwenda alikuwa amebaki kule nje kama mtu wa mwisho kumalizia kazi endapo ingetokea nimewazidi ujanja wale wenzake.
Sikuona sababu ya kuendelea kupoteza muda zaidi mle ndani hivyo nikawa nimepanga kuondoka haraka na kurudi jijini Bujumbura kuitafuta nyumba namba 27 ya mtaa wa Ruvubu. Hata hivyo wakati nikiendelea kujishauri nini cha kufanya mara mlango wa ile ofisi ukafunguliwa taratibu kisha mtutu wa bastola ukatangulia mbele. Haraka nikawahi kuchepuka na kujibanza nyuma ya ule mlango huku mkono wangu mmoja tayari ukiwa umeifikia bastola yangu mafichoni. Yule mtu aliyefungua ule mlango akawa ni kama aliyesita kuingia mle ndani badala yake akasimama pale mlangoni kama anayefanya tathmini ya mazingira ya mle ndani.
Kupitia uwazi mdogo uliokuwa nyuma ya ule mlango niliweza kumuona yule mtu. Alikuwa ni miongoni mwa wale watu watatu walioingia kule kanisani muda mfupi uliopita wakiniwinda. Nikahisi kuwa yule mtu alikuwa ameshtuka baada ya kuiona maiti ya mwenzake ikiwa imelala pale mlangoni sakafuni huku ikivuja damu.
Yule mtu akasita kuingia mle ndani badala yake nikamuona akirudi nyuma kidogo na kuchungulia kwenye uwazi mdogo nyuma ya ule mlango. Sikumchelewesha, risasi moja makini ya bastola yangu mkononi ikamega kibanzi kidogo cha ubao wa mlango na kupenya kwenye moyo wake huku ikiacha tundu dogo linalovuja damu. Maumivu makali yakasambaa mwilini na kumpelekea yule mtu aachame mdomo wazi huku ameshikwa na mshangao usioelezeka. Hatimaye yule mtu akaanguka chini pale mlangoni kama mti mkubwa uliopigwa shoka la mwisho.
Taratibu nikanyata hadi pale mlangoni na kuanza kumpekua yule mtu mifukoni. Sikupata kitu chochote cha maana hivyo nikamshika miguu na kuanza kumburuta nikimwingiza mle ndani ya ile ofisi kisha nikaufunga ule mlango kwa ndani. Upande wa kushoto wa ile ofisi kulikuwa na dirisha kubwa la kioo. Dirisha lile lilikuwa wazi hivyo sikutaka kupoteza muda mle ndani badala yake nikaliendea lile dirisha na kuchungulia nje. Sikumuona mtu yoyote upande ule hivyo nikapenya pale dirishani na kutoka nje huku bastola yangu tayari nikiwa nimeitia kwenye mfuko wa koti langu.
Manyunyu ya mvua yalikuwa yameanza kuanguka kutoka angani wakati nilipokuwa nikifika nje kwenye ule mlango mkubwa wa kuingilia kanisani. Kulikuwa na watu wachache waliokuwa wamesimama eneo lile wakisalimiana na kujuliana hali baada ya ukomo wa ibada na nilipowatazama nikagundua kuwa hakuna aliyekuwa ameisikia ile milio ya risasi wakati mapambano yalipokuwa yakiendelea kwenye ile ofisi ya Askofu. Baadhi ya wale watu wakageuka na kunitazama hata hivyo sikuwatilia maanani kwani akili yangu sasa ilikuwa imejikita kwenye nyumba namba 27 iliyokuwa mtaa wa Ruvubu jijini Bujumbura. Hata hivyo mshangao ulinijia haraka wakati nilipoitazama ile sehemu ya maegesho ya magari ya lile kanisa na kutoiona ile teksi niliyokuja nayo badala yake nikaliona gari jeupe aina ya Toyota Hilux double cabin ikiwa imeegesha upande wa pili wa maegesho yale. Kumbukumbu zangu zikanitanabaisha kuwa lile gari halikuwepo wakati nilipofika pale kanisani muda ule hivyo nikajua kuwa huwenda lile gari lilikuja na wale watu niliotoka kupambana nao na kuwaangamiza baada ya kupewa habari zangu na yule dereva wa teksi aliyenitoroka kule msituni.
Hapakuwa na usafiri mwingine ambao ungenifikisha jijini Bujumbura zaidi ya lile gari kwani yale magari mengine yote niliyoyakuta eneo lile wakati nikifika sasa hayakuwepo na sikujua yalielekea wapi.
Mlango wa lile gari Toyota Hilux double cabin nyeupe ulinishangaza kuukuta wazi. Kwangu ilikuwa afadhali hivyo sikujiuliza mara mbili nikaufungua na kuingia ndani. Niliikuta funguo ya gari ikiwa mahala pake hivyo nikawasha gari na kuitoa kwenye yale maegesho kwa utulivu wa hali ya juu kukwepa kuyavuta macho ya watu.
Muda mfupi baadaye nilikuwa katikati ya barabara mbovu ya kidongo chekundu kwenye inayokatisha katika msitu mnene kurudi jijini Bujumbura. Mshale wa mafuta kwenye dashibodi ya lile gari ukanitoa hofu kuwa safari yangu isingekuwa na kelele wala mikwaruzo yoyote. Mvua kubwa ilikuwa imeanza kunyesha na mwendo wangu ulikuwa wa kasi mno.

_____
Maison numéro 27,Rue de la Ruvubu ama nyumba namba 27 mtaa wa Ruvubu jijini Bujumbura ilikuwa kwenye ghorofa ya pili katika jengo la ghorofa tano la shirika la nyumba la taifa. Barabara ya mtaa ule haikusongwa na magari mengi wala pilika nyingi za kibinadamu na hivyo kuufanya mtaa ule umezwe na ukimya wa aina yake.
Kwa muda wa masaa manne yaliyopita mvua kubwa ya masika ilikuwa imenyesha na ingawa mvua hiyo sasa ilikuwa imepungua lakini ni watu wachache sana walioonekana kujitokeza barabarani wakitembea kwa miguu. Kufuatia jaribio la mapinduzi ya kijeshi lililofanyika jijini Bujumbura niliweza kugundua kuwa askari jeshi waaminifu kwa serikali ya rais Pierre Nkurunziza walikuwa wamesambaa mitaani kila kona katika harakati za kuhakikisha wanazima kabisa jaribio lile la mapinduzi ya kijeshi nan chi inarudi kwenye utulivu wake.
Nikiwa na hakika kuwa uwepo wangu jijini Bujumbura lilikuwa ni jambo hatari na lenye kutishia usalama wangu dhidi ya kikundi fulani hatari chenye malengo nisiyoyafahamu, lile gari Toyota Hilux double cabin nilikuwa nimeamua kulitelekeza kwenye kichaka kimoja cha ufukwe wa ziwa Tanganyika umbali wa kilometa chache kabla ya kufika jijini Bujumbura kisha kwa msaada wa ramani yangu ndogo ya kukunja ya kijasusi nikaamua kutembea kwa miguu hadi ulipo mtaa wa Ruvubu huku nikionekana raia mwema kabisa nisiyepaswa kutiliwa mashaka.
Ingawa hatua zangu zilipishana kwa utulivu huku macho yangu yakisafiri huku na kule katika kuchunguza magari, pikipiki na sura za watu niliopishana nao jioni ile lakini akili yangu ilikuwa imezama katika tafakuri nzito. Tukio la kutekwa kwa Balozi Adam Mwambapa jijini Bujumbura bado lilikuwa geni kabisa katika harakati zangu za kijasusi hivyo lilikuwa limeniweka katika wakati mgumu juu ya kufahamu sababu iliyopelekea tukio lenyewe. Kama watekaji walidhamiria kulipwa kiasi kikubwa cha pesa ili wamuachie kamanda huyo basi ilipaswa kuwa hadi kufikia muda ule watekaji hao tayari wangekuwa wameshajitokeza kwa njia yoyote na kuwasilisha madai yao kwa serikali ya Tanzania. Lakini hadi kufikia sasa jambo hilo lilikuwa halijajitokeza hivyo sikuona kama lengo la utekaji ule lilikuwa ni kujipatia pesa kwa watekaji hao.
Nilihisi kuwa kulikuwa na sababu nyingine nyeti ya kupelekea tukio la kutekwa kwa balozi Adam Mwambapa, sababu ambayo bado sikuifahamu. Kwa upande mwingine nilihisi kuwa kulikuwa na haja ya kuyapeleleza vizuri maisha ya balozi Adam Mwambapa jijini Bujumbura kwani huwenda kwa kufanya vile ningepata walau fununu juu ya sababu ya kutekwa kwake. Hata hivyo nilitambua kuwa hilo nalo lisingewezekana kwani mtu wa mwisho kunipa taarifa alikuwa ni Sundi Masele, kijana aliyekuwa akifanya kazi za uhudumu nyumbani kwa balozi Adam Mwambapa ambaye sasa na yeye alikuwa marehemu.
Jambo lingine lililonishangaza ni kuwa watu wale hatari waliokuwa wakinitafuta usiku na mchana jijini Bujumbura walionekana kuwa na taarifa zangu zote tangu siku ya kwanza nilipotoka jijini Dar es Salaam. Swali likawa taarifa zangu ziliwafikia vipi watu wale na ni nani aliyekuwa akizivujisha kwao?. Jibu sikulipata hivyo mawazo mengi yakaendelea kupita kichwani mwangu.
Giza tayari lilikuwa limeanza kuingia wakati nilipouinua mkono na kutazama majira kwenye saa yangu ya mkononi. Dakika chache zilikuwa zimesalia kabla ya kutimia saa moja usiku. Mwanga wa taa za magari machache yaliyokuwa yakikatisha katika barabara ya mtaa ule ukanipelekea nitembee kandokando ya barabara. Mara kwa mara niliweza kusikia majibizano ya risasi kutoka maeneo tofauti mitaani na hivyo kunifanya nitembee kwa tahadhari.
Baada ya kulipita jengo la Bank of Belgo-African mbele kidogo nikavuka barabara upande wa pili ambapo nilitembea kwa tahadhari huku mara kwa mara nikigeuka nyuma kutazama kama kungekuwa na mtu yeyote aliyekuwa akinifuatilia. Sikumuona mtu yeyote hivyo hali bado ilikuwa shwari.
Mara baada ya kulipita duka la kubadilishia fedha za kigeni na Supermarket ndogo ya mtaa nikaingia upande wa kushoto. Hatua chache zikanifikisha kwenye ngazi za jengo la ghorofa la shirika la nyumba la taifa. Uchunguzi wangu ukaniridhisha kuwa sikuwa nimepotea niendako hivyo nikaamua kuzipanda ngazi zile kwa utulivu.
Nyumba namba 27 ilikuwa upande wa kulia kwenye ghorofa ya pili ikitazamana na korido pana yenye uzio wa ukuta mfupi unaotazamana na barabara mara baada ya kumaliza kupanda zile ngazi. Nilipofika juu ya zile ngazi nikashika uelekeo wa upande wa kulia nikitembea kwa tahadhari kuikagua milango iliyokuwa ikitazamana na korido ile. Jambo moja lililonishangaza ni kuwa nyumba zote katika ghorofa ile zilikuwa gizani kana kwamba wenyeji wake hawakuwepo mle ndani.
Hatua zangu zikapungua na hatimaye kukoma wakati macho yangu yalipotua juu ya mlango mmoja wa korido ile na kuiona namba 27. Kwa sekunde kadhaa nikasimama nje ya mlango ule nikiupima utulivu wa mle ndani. Hapakuwa na kiashiria chochote cha uwepo wa kiumbe hai mle ndani zaidi ya makelele ya muungurumo wa hafifu wa magari machache yaliyokuwa yakipita barabarani chini ya lile jengo la ghorofa ambayo nikiwa pale juu niliweza kuyaona vizuri.
Mtu yeyote ambaye alikuwa akiishi mle ndni kwa namna moja au nyingine alipaswa kuwa na taarifa fulani za siri zenye mahusiano ya moja kwa moja na wale watu niliopambana nao kule kanisani Bubanza. Taarifa ambazo niliamini kuwa endapo ningezipata ningeweza kunipa walau uelekeo mzuri wa kile nilichokuwa nikikipeleleza. Baada ya kujiridhisha na hali ya usalama wa eneo lile nikausogelea ule mlango na kuanza kugonga hodi. Hakuna aliyeniitikia wala ule mlango kufunguliwa na hali ile ilinitia tumbo joto. Nikarudia kugonga hodi mara kadhaa lakini majibu yalikuwa yale yale.
Nikiwa nimeanza kuhisi kuwa nilikuwa nikipoteza muda nikashika kitasa cha ule mlango na kujaribu kuufungua. Ule mlango ulikuwa umefungwa hivyo bila kupoteza muda nikachukua funguo zangu malaya kutoka mfukoni na baada ya kukolokochoa kidogo ule mlango ukafunguka. Bila kupoteza muda nikaichomoa ile funguo mlangoni na kuusukuma ule mlango taratibu huku tayari mkono wangu ukiwa umeifikia bastola yangu mafichoni.
Mara baada ya kuingia mle ndani na kuufunga ule mlango nikasimama pale mlangoni nikiupima utulivu wa mle ndani. Kulikuwa na sauti hafifu ya mshale wa saa ya ukutani na muungurumo wa jokofu lililokuwa kwenye kona fulani mle ndani, zaidi ya pale sikusikia sauti ya kitu chochote kingine. Hisia zangu zikanitanabaisha kuwa huwenda mwenyeji wa ile nyumba hakuwepo mle ndani.
Ingawa nilikuwa siifahamu vizuri ramani ya ile nyumba lakini ujenzi wa nyumba nyingi za barani Afrika nilikuwa nikiufahamu. Hivyo taratibu nikapapasa ukutani na kuipata swichi ya taa ya mle ndani. Lakini kabla sijaiwasha ile taa nikahisi kuwa tukio la namna ile lingeweza kuyavuta macho ya mtu yeyote ambaye angekuwa jirani na ile nyumba. Hivyo nikaamua kuachana na mpango ule badala yake nikatumbukiza mkono kwenye mfuko wa koti langu na kuchukua kurunzi yangu ndogo ya kijasusi yenye mwanga mkali.
Bastola yangu ikiwa mkononi nikaiwasha ile kurunzi na kuanza kumulika mle ndani. Ilikuwa ni sebule kubwa yenye samani za kisasa. Kulikuwa na seti moja nzuri ya makochi ya sofa ya rangi nyeupe yaliyopangwa katika mtindo wa kuizunguka ile sebule. Katikati ya sebule ile kulikuwa na meza fupi ya mti wa msandarusi iliyochongwa kwa ustadi wa hali ya juu na kuwekwa nakshi za kupendeza juu ya sakafu nzuri ya malumalu nyeupe zenye maua mazuri ya kuchorwa. Taratibu nikautembeza ule mwanga wa kurunzi yangu mkononi kumulika upande wa kushoto.....ITAENDELEA
 
RIWAYA: UFUKWE WA MADAGASCAR
SEHEMU:55

...wa kushoto. Kwa kufanya vile nikaiona runinga kubwa flat screen ya inchi 52 aina ya Sony bravia ikiwa imefungwa ukutani. Chini ya runinga ile kulikuwa na sistimu nzuri ya muziki ya Jvc. Havikuwa vitu vilivyonivutia katika upelelezi wangu hivyo nikauhamisha ule mwanga wa tochi kumulika sehemu nyingine mle ndani.
Pembeni ya dirisha kubwa lililofunikwa na mapazia mawili marefu yasiyoruhusu mtu aliyeko nje kuona mle ndani kulikuwa na saa kubwa ya ukutani na kupitia majira ya saa ile nikagundua kuwa ilikuwa ikielekea kutimia saa moja na dakika ishirini usiku. Jokofu lililokuwa likiunguruma mle ndani lilikuwa kwenye kona ya sebule ile mara baada ya kuipita meza ndogo ya ofisini yenye kiti kimoja na kompyuta desktop juu yake na taa ndogo ya kusomea Lampshade. Upande wa kulia kulikuwa na rafu ndogo ya vitabu. Mandhari ya sebule ile yakanitanabaisha kuwa mwenyeji wa ile nyumba alikuwa mtu msomi.
Taratibu nikaisogelea ile rafu ya vitabu na kuanza kuichunguza. Upande wa kushoto kulikuwa na vitabu vichache vya novels za lugha ya kifaransa na kiingereza za waandishi mabingwa duniani kama James Hadley Chase, John Grisham, Joe Nesbo, Dan Brown, Danielle Steel na wengineo. Upande wa kulia kulikuwa na vitabu vya ujuzi na nilipoinama na kuvichunguza nikagundua kuwa vitabu vile vingi vilikuwa vinavyohusu masuala ya elimu ya uhasibu katika benki.
Pembeni ya vitabu vile nikaona mafaili yaliyopangwa vizuri yenye nyaraka muhimu za kiofisi. Mafaili yale yalikuwa na lebo maalum za vipande vya karatasi nyeupe vilivyoandikwa kwa marker pen nyeusi kama Annual financial report, Cashflow analysis report, Balance sheet and Bank reconciliation report na kadharika. Sasa sikuwa na shaka yoyote kuwa mwenyeji wa nyumba ile alikuwa ni mfanyakazi katika taasisi ya kifedha kama benki au shirika fulani la mikopo. Nikajikuta nikivutika zaidi na utafiti wangu hivyo nikachomoa faili moja kutoka kwenye rafu ile na kuanza kusoma nyaraka zilizokuwa mle ndani.
Mara moja nilipofungua ukurasa wa kwanza wa lile faili na kuanza kupitia maelelezo yake nikajikuta nikishtuka. Moyo wangu ukapoteza kabisa utulivu huku baridi nyepesi ikisambaa mwilini. Kumbukumbu za haraka zilikuwa zimenijia akilini. Moja ya nyaraka zile ilikuwa ni barua ya ofisi iliyoandikwa na meneja mkuu wa Banque de la République du Burundi, ndugu Jean Aristide Wamba kwenda kwa mkuu wa idara ya mikopo ya benki hiyo. Ndugu Léon Dingo ili kuidhinisha kiasi fulani cha pesa kutolewa na benki hiyo kama mkopo kwenda kwa chama cha walimu nchini Burundi kwa ajili ya ujenzi wa jengo la ofisi kuu ya chama hicho. Chini ya barua ile kulikuwa na sahihi ya meneja yule wa benki.
Jina la Jean Aristide Wamba lilikuwa limeushtua sana moyo wangu. Haraka kumbukumbu zangu zikanirudisha kwenye ule msitu mkubwa uliokuwa nyuma ya jengo la Le Tulip Hôtel Africaine usiku wa jana. Taswira ya watu sita wafu waliofungwa kwenye miti na kuuwawa kinyama ikapita mbele ya macho yangu na kuibua hisia mbaya zilizopelekea mikono yangu kuanza kutetemeka. Jina la Jean Aristide Wamba lilikuwa miongoni mwa wale watu waliouwawa kule msituni. Haraka nikatumbukiza mkono wangu katika kipenyo cha mfuko mdogo wa siri wa koti langu na kuichukua kadi ndogo ya utambulisho wa kazi niliyoipata kule msituni. Jina la mhusika wa kadi ile lilishabihiana kila kitu na lile jina la meneja wa benki katika ile barua ya kikazi.
Lilikuwa jambo la kushtua na lenye kuvuta hisia zangu. Kwa namna moja au nyingine niliamini kuwa mwenyeji wa nyumba ile alifahamika kwa jina la Léon Dingo, mfanyakazi wa Banque de la République du Burundi mwenye cheo cha afisa mikopo. Kwa maana nyingine ni kuwa Jean Aristide Wamba na ndugu Léon Dingo walikuwa na unasaba mkubwa wa kikazi kwani wote walikuwa wafanyakazi wa Banque de la Republique du Burundi.
Kwa mara ya kwanza tangu niingie jijini Bujumbura nikaanza kuhisi ukweli fulani juu ya hisia zangu dhidi ya kile nilichokuwa nikikipeleleza. Mwili wangu ukapigwa na baridi nyepesi huku nywele zangu zikinicheza. Nikatumbukiza tena mkono kwenye vipenyo vya mifuko ya siri ya koti langu kuuchukua ule ufunguo niliouokota kule msituni na kuanza kuuchunguza upya kwa makini. Ulikuwa ni ufunguo wenye umbo la kipekee sana ambao akili yangu ilishindwa kabisa kuufananisha na kumbukumbu za funguo nyingi za maeneo tofauti zilizijihifadhi vyema kichwani mwangu. Nikaamua tena kuutembeza ule mwanga wa tochi pale sebuleni nikitafuta kitu chochote kilichofungwa ambacho kingeweza kufunguliwa na ufunguo ule lakini sikupata hivyo nikautazama tena ule ufunguo kwa udadisi huku nikiugeuzageuza kabla ya kuurudisha mfukoni.
Kupitia ile kurunzi yangu mkononi nikaanza kuyapekua yale mafaili mengine yaliyosalia huku nikitarajia kupata ziada nyingine katika uchunguzi wangu. Bahati mbaya sana nilimaliza upekuzi wangu bila ziada yoyote ya taarifa nilizozihitaji kwani ndani ya mafaili yale taarifa nyingi zilikuwa za kiofisi ambazo hazikuwa na mrengo wowote na harakati zangu.
Ndani ya jokofu lililokuwa kwenye kona moja ya sebule ile nilipofungua na kuchunguza sikuona kitu chochote cha kuvuta macho yangu zaidi ya pakiti za maziwa ya mgando, matunda na kipolo cha wali. Hivyo nikaliacha lile jokofu na kulisogelea pazia refu lililokuwa kando yake. Kwa kufanya vile nikajikuta nikitazamana na korido fupi iliyofunikwa na zulia jepesi la manyoya sakafuni. Kando ya korido ile kulikuwa na rafu ndogo ya mbao juu yake kukiwa kumepangwa viatu vya ngozi vya kiume na makubazi za ngozi. Sikuona viatu vya kike au vya mtoto mdogo hivyo hisia zangu zikanitanabaisha kuwa huwenda mwenyeji wa ile nyumba alikuwa mwanaume mseja.
Taratibu nikatembea kuifuata korido ile huku nikimulikamulika huku na kule. Kulikuwa na milango mitatu iliyokuwa ikitazamana na korido ile. Milango miwili ya kwanza ilikuwa upande wa kulia na mlango mmoja uliosalia ulikuwa mwishoni kabisa ukutazamana na ile korido. Nikatembea taratibu nikiichunguza kwa makini milango ile. Ile milango miwili ya upande wa kulia ilikuwa nusu wazi na niliposogea karibu kuchungulia mle ndani nikagundua kuwa ule mlango wa chumba cha kwanza ulikuwa wa chumba cha stoo na ndani yake hapakuwa na kitu. Mlango wa chumba cha pili ulikuwa ni wa chumba cha jiko dogo la kisasa lenye meza ya fomeka ukutani, masinki mawili ya kuoshea vyombo na sistimu ya gesi ya kupikia. Sakafu ya chumba kile lifunikwa kwa malumalu nzuri za kupendeza. Hapakuwa na kitu kingine cha ziada kinachoweza kunivutia hivyo nikaamua kuelekea kwenye kile chumba cha mwisho kilichokuwa kikitazamana na ile korido. Mlango wake ulikuwa umefungwa.
Nilipofika pale mlangoni nikasimama nikiupima utulivu wa mle ndani. Sikuweza kusikia kitu chochote, mle ndani kulikuwa kimya sana kama pango lisilokuwa na mkazi. Bastola yangu ikiwa mkononi taratibu nikakishika kitasa na kujaribu kuufungua ule mlango. Ule mlango ulikuwa umefungwa na hivyo bila kupoteza muda nikapachika funguo zangu za kazi na kuanza utundu wangu. Jaribio la pili likazaa matunda hivyo nikausukuma ule mlango taratibu na kuingia mle ndani na kisha kuufunga ule mlango nyuma yangu.
Kwa msaada wa mwanga mkali wa kurunzi yangu mkononi niliweza kuyaelewa vizuri mandhari yake. Nilikuwa ndani ya chumba kikubwa chenye madirisha mawili makubwa yenye uwezo wa kupitisha mwanga na hewa ya kutosha kwa upande wa kushoto na kulia. Katikati ya chumba kile kulikuwa na kutanda cha kisasa kikubwa cha futi sita kwa sita kilichofunikwa kwa shuka na blanketi laini na mito miwili ya kuegemea. Pembeni ya kitanda kile kulikuwa na meza fupi ya taa ya mwanga hafifu wa chumbani Lampshade. Kando ya taa ile niliona pakiti moja ya sigara iliyofunguliwa, kibakuli cha kuwekea majivu ya sigara, kibiriti cha gesi na mzinga mmoja wa pombe kali aina ya Goldons.
Mwisho wa kile kitanda upande wa kushoto ukutani kulikuwa na makabati mawili makubwa ya nguo pembeni ya kochi moja kubwa la sofa laini. Nikaendelea kumulika mle ndani kwa utulivu nikichunguza. Chini ya makabati yale kulikuwa na droo nyingi. Nikajikuta nikishawishika kwenda kupitisha upekuzi kwenye zile droo lakini baada ya kutazama upande wa kulia na kuiona selfu ndogo ya chuma nikajikuta nikighaili na kutembea taratibu kuifuata ile selfu. Hata hivyo kabla sijaifikia ile selfu hatua zangu zikakoma na hapo nikageuka nyuma na kuyatega vizuri masikio yangu. Kwa mbali niliweza kusikia ule mlango wa kule sebuleni ukigunguliwa na kufungwa kisha nikaanza kusikia sauti za watu wawili wakizungumza, mmoja alikuwa mwanamke na mwingine mwanaume. Maongezi yao yalikuwa katikati ya furaha huku mwanamke akicheka kwa sauti hafifu.
Ukimya kidogo ukafuatia kisha nikaanza kusikia sauti ya hatua hafifu za watu wale wakitembea kwenye ile korido kuja kwenye kile chumba. Haraka nikazima ile kurunzi yangu mkononi huku nikitafuta sehemu ya kujificha mle ndani. Mwisho wa kile chumba upande wa kulia kulikuwa na mlango wa kuelekea chumba cha bafu na maliwato. Sikuona kama mle ndani ingekuwa sehemu salama ya kujificha hivyo haraka nikarudi kwenye yale makabati na kuchunguza mle ndani. Yale makabati yalikuwa yamejaa nguo zilizopangwa vizuri hivyo utundu wangu wowote wa kujificha ungeweza kuniumbua. Niliacha yale makabati na kukisogelea kile kitanda cha mle ndani huku nikipiga mahesabu ya kujificha uvunguni na wakati nikifanya vile nikasikia kitasa cha ule mlango wa kile chumba kikichokolewa kwa funguo. Kile kitanda kilikuwa na matendegu marefu kiasi kwamba uvungu wake ulikuwa wazi sana kwa mtu kujificha bila kuonekana.
Wakati ule mlango ukifunguliwa na wale watu kuingia mle ndani mimi tayari maficho yangu yalikuwa nyuma ya pazia zito na refu la dirisha la upande wa kushoto wa kile chumba. Bastola yangu ikiwa imetuama vyema mkononi jicho langu moja lilikuwa tayari limejificha katika ya uwazi mdogo uliotengenezwa na mpishano wa kipande kimoja cha pazia na kingine kwenye dirisha lile kuwatazama wale watu waliokuwa wakiingia mle chumbani. Ule mlango wa kile chumba ilipofunguliwa mwanaume na mwanamke wakaingia mle ndani huku wakiwa wameshikana mikono. Tathmini yangu ikanitanabaisha kuwa walikuwa ni wapenzi walioshibana sana.
Mwanaume alikuwa mrefu na mwenye umbo kubwa linalopendeza. Alikuwa amevaa suti nadhifu ya rangi ya kijivu ya single button na shati jeusi lililomkaa vyema na kumpendeza. Miguuni alikuwa amevaa viatu vya ngozi na saa ya mkononi. Sikuweza kuiona vizuri sura yake kwani mara tu walipoingia mle ndani yule mwanaume akautupa mkoba wake ngozi aliokuwa ameushika pale kitandani kisha akageuka na kumshika yule mwanamke kiunoni ambapo alimvuta karibu yake na hapo wakaanza kunyonyana ndimi kama waliowehuka na mzuka wa ngono.
Nikiwa nyuma ya pazia pale dirishani nikajikuta nikivutiwa kuitazama sinema ile ya kusisimua ya aina yake. Yule mwanamke alikuwa amevaa suruali ya jeans iliyombana na hivyo kulichora vizuri umbo lake matata lenye mzigo wa makalio ya wastani na mapaja yaliyonona. Juu alikuwa amevaa kofia nyeusi ya kapelo iliyouficha uso wake. Shati lake zito la kadeti na fulana yake nyekundu vilichangia muonekano wa kupendeza wa msichana yule mrefu.
Wakati wapenzi wale wakiendelea kunyonyana ndimi mara nikamuona yule mwanaume akiharakisha kuvua koti lake la suti na kulitupia sakafuni kisha akaanza kufungua vifungo vya shati lake huku mara kwa mara mkono wake mmoja ukihama na kuyatomasa makalio ya yule mwanamke kwa papara. Ndimi zao zikiwa bado zimeng’ang’ania mara nikamuona yule mwanamke na yeye akianza kufungua vifungo vya shati lake lakini si kwa papara sana kama ilivyokuwa kwa yule mwanaume. Alipomaliza akavua shati lake na kulitundika kwenye vishikizo maalum vilivyokuwa nyuma ya ule mlango wa chumbani kisha akavua fulana yake na kuyaacha matiti yake makubwa ya wastani yenye chuchu zilizosimama yakiwa yameshikiliwa vyema na sidiria yake ya rangi nyeusi. Yule mwanamke alipomaliza akamsogelea tena yule mwanaume kisha akapitisha mikono yake nyuma shingoni kwa yule mwanaume na hapo wakaanza tena kunyonyana ndimi. Mara hii niliweza kusikia sauti ya miguno hafifu ya wapenzi wale huku kila mmoja akijitahidi kumpapasa mwenzake maungoni. Hisia zikionekana kuwa mbioni kuwazidi wapenzi wale mara nikamuona yule mwanaume akivua viatu kwa miguu yake kisha akavipiga teke pembeni na hapo akalegeza mkanda wa suruali yake na kuivua. Sasa yule mwanaume amebakiwa na nguo yake ya ndani tu mwilini huku uchu wa ngono ukionekana kumnasa vilivyo kisha akambeba yule mwanamke na kumtupia pale kitandani huku wote wakiangua vicheko hafifu vya mahaba.
Wale wapenzi wakiwa pale kitandani yule mwanaume akafungua kifungo na zipu ya suruali ya yule mwanamke kwa papara alipomaliza akamvua viatu yule mwanamke na kunitupilia mbali kisha akanza kumvua ile suruali akiivuta kwa juu. Suruali ile ilipomvuka yule mwanamke nikaweza kuliona umbo zuri la mlimbwende yule, hakika mwili wangu ulisisimka sana. Kiuno chake maridhawa kilizunguka taratibu upande huu na ule wakati mikono ya mwanaume yule mwenye uchu ilipokuwa ikishughulika vilivyo kuivua nguo yake ya ndani. Ingawa yule mwanamke pale kitandani alijitahidi kuzuia kitendo kile kisifanikiwe kwa kuizuia mikono ya yule mwanaume. Lakini ilikuwa kazi bure kwani yule mwanaume hakuonekana kuwa tayari kucheleweshewa adhma yake. Yule mwanaume uchu wa ngono ulikuwa umemnasa vilivyo huku macho yamemwiva. Sikuwa na shaka yoyote kuwa alikuwa akiisubiri nafasi ile kwa muda mrefu. Bada ya kukurukakara za hapa na pale hatimaye yule mwanaume akafanikiwa kumvua yule mwanamke nguo yake ya ndani na kuitupilia mbali huku na yeye akijivua nguo yake ya ndani kwa kasi isiyoelezeka.
Muda mfupi uliofuata nilikuwa nikishuhudia sinema ya mapenzi yenye kila kionjo cha kumtoa nyoka pangoni. Nikiwa nyuma ya lile pazia nikajikuta nikipambana vikali na hisia zangu. Pale kitandani mapenzi yalinoga kwa namna yake, miguno ya mahaba ikahanikiza kila mahali mle ndani. Ile mito ya kujiegemeza pale kitandani ikaangukia sakafuni, mmoja huku na mwingine kule lakini hakuna aliyejishughulisha kuiokota. Shuka likavurugwa hovyo wakati wapenzi wale walipokuwa wakivingirishana sarakasi pale kitandani. Kwangu ilikuwa ni adhabu kubwa dhidi ya hisia zangu, labda kama ningekuwa nafahamu mambo yale kuwa yangejiri mle ndani basi ningejipa subira kwanza kule nje kuliko kuteseka namna ile. Hata hivyo sikuwa na namna badala yake nikabaki nikimeza mate tu na kupambana na hisia zangu. Kule nje nilipotazama pale dirishani giza lilikuwa limeshamili huku mvua kubwa ikiendelea kunyesha.
Takribani muda wa saa moja ulipoyeyuka wapenzi wale walikuwa hoi huku kila mmoja akionekana kutosheka na mwenzake. Yule mwanamke alikuwa wa kwanza kuamka na kuketi kwenye ukingo wa kile kitanda huku akiwa uchi kama alivyozaliwa. Mara nikamuona akigeuka na kutazama pale dirishani nilipojibanza kama ambaye amehisi jambo. Moyo wangu ukapiga kite huku kijasho chepesi kikianza kunitoka. Hata hivyo macho yangu yaliweka kituo vizuri na kumtazama yule mwanamke na kwa kufanya vile nikajikuta nikishikwa na mshangao.
Yule mwanamke alikuwa Amanda kwani kwa kadiri nilivyoendelea kumtazama ndivyo nilivyozidi kumkumbuka sura yake. Alikuwa Amanda haswaa, yule msichana mrembo niliyesafiri naye kutoka jijini Kigali nchini Rwanda siku ile ya kwanza nilipotoka jijini Dar es Salaam na hatimaye kunisaliti kwa wale wanajeshi watatu waliokuja kunichukua kule nyumbani kwake. Ingawa nakiri kuwa nilikuwa nimetokea kumpenda sana Amanda kwa mara ya kwanza tu nilipomuona siku ile kabla ya kuanza safari yangu ya kuja jijini Bujumbura kutoka Kigali nchi Rwanda lakini sasa nilikuwa namchukia Amanda kama kirusi hatari kabisa katika harakati zangu za kijasusi. Siyo tu kwamba Amanda alikuwa amenisaliti pamoja na fadhila zangu zote za kumuokoa kutoka kwenye mikono ya wale watekaji hatari kule barabarani msituni siku ile tulipokuwa tukisafiri kutoka jijini Kigali nchini Rwanda. Lakini pia alionekana kushirikiana vyema na wale watu hatari waliokuwa wakiniwinda pale jijini Bujumbura. Amanda alikuwa msichana hatari mwenye hila kama nyoka. Msichana aliyefahamu kuutumia vizuri uzuri wake kuzinasa roho za nyepesi za wanaume wakware na hatimaye kutimiza adhma yake.
Amanda akaendelea kutazama pale dirishani nilipojibanza kwa muda mrefu kiasi cha kuyavuta macho ya yule mwanaume pale kitandani na yeye ageuke na kutazama pale dirishani. Bastola yangu ikiwa imetulia vyema mkononi nikaganda kama sanamu huku nikizipima vizuri hisia zao.
“Kuna nini mpenzi?”. Yule mwanaume akamuuliza Amanda huku akizifikicha chuchu za Amanda, tukio ambao lilionekana kuamsha upya hisia za Amanda na hapo Amanda akageuka na kumtazama yule mwanaume pale kitandani huku akitabasamu.
“Hakuna chochote mpenzi, nilikuwa nafikiria namna ya kupata usafiri wa kunifikisha nyumbani kwangu mara baada ya kutoka hapa”. Amanda akaongea huku akikipapasa kifua cha yule mwanaume pale kitandani.
“Kwanini leo usilale hapa mpenzi halafu kutakapopambazuka nitakupeleka nyumbani kwako kwa gari langu?”
“Kama ungekuwa umeniambia mapema ningejiandaa mpenzi”. Amanda akaongea kwa utulivu na kutabasamu huku taratibu akikipasa kifua cha yule mwanaume.
“Mh! kujiandaa kwa lipi?”
“Usiku huu rafiki yangu anakuja kunitembelea na tulishakubaliana kuwa leo atalala kwangu. Sasa akifika na kunikosa nahofia kuwa atahisi kuwa sijapendezwa na ugeni wake na hivyo nikaamua kumkwepa”. Amanda akaongea kwa sauti nyororo ya kubembeleza huku akiyachua mapaja ya yule mwanume.
“Mgeni wa kike au wa kiume?”. Yule mwanaume akauliza pale kitandani huku usoni akionesha wivu wa dhahiri.
“Mh! punguza wivu mpenzi, ni mgeni wangu wa kike, rafiki na mfanyakazi mwenzangu”
“Afadhali awe mwanamke maana wivu ulishaanza kuniingia”. Yule mwanaume akaongea kwa utulivu huku akionekana kuzama kwenye tafakuri fupi. Amanda akabaki akimtazama kwa utulivu kisha akavunja ukimya akimuuliza yule mwanaume.
“Umenifanyia kazi yangu?”
“Halikuwa jambo rahisi mpenzi”. Yule mwanaume akaongea huku akimtazama Amanda usoni.
“Una maana gani?. Kazi umeifanya au hujaifanya?”. Amanda akauliza huku sauti yake ikionekana kuingiwa na kitetemeshi.
“Kazi yako nimeifanya mpenzi”. Hatimaye yule mwanaume akaongea kwa utulivu huku taratibu akikipapa kiuno cha Amanda.
“Iko wapi?”. Amanda akauliza huku akionekana kuwa na shauku. Yule mwanaume pale kitandani hakutia neno badala yake taratibu akageuza kichwa kuutazama ule mkoba wa ngozi uliokuwa pembeni ya kile kitanda. Kitendo kile kikampelekea Amanda na yeye ageuke na kuutazama ule mkoba huku tabasamu jepesi likichanua usoni mwake.
“Una maanisha ipo ndani ya huo mkoba?”. Amanda akauliza huku akionekana kutafuta hakika ya jibu.
“Ndiyo”. Yule mwanaume akajibu. Amanda akautazama ule mkoba kwa hamasa kama wenye kito cha thamani ya juu sana hata hivyo hakuupeleka mkono wake kuuchukua ule mkoba badala yake akawa ni kama anayetaka kushuka pale kitandani ili aelekee kule bafuni. Lakini yule mwanaume aliwahi kumzuia kwa kumshika mkono huku uso wake ukiwa mbali na mzaha kisha akamuuliza Amanda.
“Mipango inaendeleaje?”
“Kila kitu kipo safi”. Amanda akajibu kwa mkato. Yule mwanaume akamtazama Amanda kwa udadisi kabla ya kumuuliza tena.
“Nani anayeratibu mipango yote?”
“Meja jenerali Godfroid Niyombare akishirikiana na makamanda wengine wa jeshi”. Amanda akajibu kwa kifupi huku akionekana kutopendezwa sana na maswali ya aina ile.
“Una hakika kuwa mpango mzima utafanikiwa?”
“Huu siyo mkakati wa mtu mmoja. Tuna mtaji wa mkubwa wa viongozi wa serikali na makamanda wa jeshi na wahisani waliopo nje ya nchi hivyo hatuwezi kushindwa”
“Nahitaji kuonana na kiongozi wenu”. Yule mwanaume akaongea kwa utulivu huku akimaanisha na hapo Amanda akamtazama yule mwanaume huku akiangua tabasamu hafifu la hila.
“Hakuna mtu yeyote anayeruhusiwa kuonana naye kwa sasa mpaka mpango utakapokamilika”. Jibu la Amanda lilikuwa kavu mno kiasi cha kumpelekea yule mwanaume ashikwe na mshangao hata hivyo Amanda alionekana kumpuuza.
“Mpango wenu ukifanikiwa mimi nitakuwa na nafasi gani?”
“Gavana wa benki kuu ya Burundi”. Amanda akaongea huku akitabasamu kisha akainama na kumbusu yule mwanaume mdomoni halafu taratibu akajitoa pale kitandani akielekea kule bafuni.
Akiwa na hakika kuwa macho ya yule mwanaume pale kitandani yalikuwa nyuma yake yakisimsindikiza Amanda akaendelea kutembea kwa maringo kama twiga anayekatisha barabara ya mbugani huku mtikisiko wa umbo lake lisilositiriwa na nguo yoyote ukitengeneza taswira nzuri ya kuvutia machoni. Yule mwanaume akaendelea kumtazama Amanda kwa hamasa huku akionekana kupendezwa na mjongeo ule hadi pale Amanda alipoingia bafuni kisha haraka akageuka na kuuchukua ule mkoba wake wa ngozi pale kitandani ambapo aliufungua haraka na kutoa bahasha ndogo mbili za kaki. Nikamuona akizichunguza zile bahasha kwa makini na baada ya pale akairudisha bahasha moja kwenye ule mkoba na kuufunga. Ile bahasha nyingine iliyosalia haraka akafunua godoro na kuificha. Lile tukio lilikuwa limezivuta sana hisia zangu na sasa nilianza kuhisi kuwa kulikuwa na jambo fulani ambalo yule mtu alikuwa amekusudia kumficha Amanda.
Dakika chache baadaye mara nikamuona Amanda akirudi kutoka kule bafuni. Mara alipofika pale ndani akachukua nguo zake na kuanza kuzivaa huku akionekana mwenye haraka. Yule mwanaume akiwa pale kitandani akamtazama Amanda kwa utulivu huku akitabasamu kisha akajisogeza pembeni na kuupeleka mkono wake kuchukua ile pakiti ya sigara mezani kando ya kile kitanda ambapo aliichomoa moja na kujiwashia akianza kuvuta kwa utulivu huku akitazama kwenye dari ya kile chumba. Amanda hakuonekana sana kumtilia maanani yule mwanaume badala yake akaendelea kutia viwalo vyake mwilini na alipomaliza akasogea kwenye kioo kikubwa cha kabati la mle ndani na kuanza kujiweka sawa kisha akavaa kofia yake na kujitengeneza vizuri.
Akiwa bado amesimama kwenye kioo cha lile kabati mara nikamuona Amanda akimtazama kwa hila yule mwanaume pale kitandani na hapo jambo moja likanishtua. Muda uleule nikamuona Amanda akiingiza mkono kwenye mfuko wa shati lake na kutoa bastola yenye kiwambo maalum cha kuzuia sauti kisha haraka akageuka na kumsogelea yule mwanaume pale kitandani huku uso wake ukiwa umebadilika na kujawa na ufedhuri. Yule mwanaume pale kitandani alipogeuka na kumuona Amanda akiwa ameshika bastola mkononi akaingiwa na hofu kiasi cha sigara yake kumuanguka mdomoni.
“Unataka kufanya nini Lucia?”
“I am very sorry Léon”
“What…?”
Yule mwanaume hakumalizia kuongea kile alichokusudia kwani muda uleule Amanda akavuta kilimi cha bastola yake yenye kiwambo maalum cha kuzuia sauti...ITAENDELEA
 
RIWAYA: UFUKWE WA MADAGASCAR
SEHEMU: 55

...taswira nzuri ya kuvutia machoni. Yule mwanaume akaendelea kumtazama Amanda kwa hamasa huku akionekana kupendezwa na mjongeo ule hadi pale Amanda alipoingia bafuni kisha haraka akageuka na kuuchukua ule mkoba wake wa ngozi pale kitandani ambapo aliufungua haraka na kutoa bahasha ndogo mbili za kaki. Nikamuona akizichunguza zile bahasha kwa makini na baada ya pale akairudisha bahasha moja kwenye ule mkoba na kuufunga. Ile bahasha nyingine iliyosalia haraka akafunua godoro na kuificha. Lile tukio lilikuwa limezivuta sana hisia zangu na sasa nilianza kuhisi kuwa kulikuwa na jambo fulani ambalo yule mtu alikuwa amekusudia kumficha Amanda.
Dakika chache baadaye mara nikamuona Amanda akirudi kutoka kule bafuni. Mara alipofika pale ndani akachukua nguo zake na kuanza kuzivaa huku akionekana mwenye haraka. Yule mwanaume akiwa pale kitandani akamtazama Amanda kwa utulivu huku akitabasamu kisha akajisogeza pembeni na kuupeleka mkono wake kuchukua ile pakiti ya sigara mezani kando ya kile kitanda ambapo aliichomoa moja na kujiwashia akianza kuvuta kwa utulivu huku akitazama kwenye dari ya kile chumba. Amanda hakuonekana sana kumtilia maanani yule mwanaume badala yake akaendelea kutia viwalo vyake mwilini na alipomaliza akasogea kwenye kioo kikubwa cha kabati la mle ndani na kuanza kujiweka sawa kisha akavaa kofia yake na kujitengeneza vizuri.
Akiwa bado amesimama kwenye kioo cha lile kabati mara nikamuona Amanda akimtazama kwa hila yule mwanaume pale kitandani na hapo jambo moja likanishtua. Muda uleule nikamuona Amanda akiingiza mkono kwenye mfuko wa shati lake na kutoa bastola yenye kiwambo maalum cha kuzuia sauti kisha haraka akageuka na kumsogelea yule mwanaume pale kitandani huku uso wake ukiwa umebadilika na kujawa na ufedhuri. Yule mwanaume pale kitandani alipogeuka na kumuona Amanda akiwa ameshika bastola mkononi akaingiwa na hofu kiasi cha sigara yake kumuanguka mdomoni.
“Unataka kufanya nini Lucia?”
“I am very sorry Léon”
“What…?”
Yule mwanaume hakumalizia kuongea kile alichokusudia kwani muda uleule Amanda akavuta kilimi cha bastola yake yenye kiwambo maalum cha kuzuia sauti. Risasi moja ikapenya kwenye shingo ya yule mwanaume pale kitandani na nyingine ikaacha tundu dogo linalovuja damu kifuani pake. Yule mwanaume akapiga yowe huku macho yamemtoka kwa hofu. Amanda akatabasamu kidogo huku akimtazama kisha akafungua kiwambo cha kuzuia sauti kwenye bastola yake na kuitia ile bastola kwenye mfuko wa ndani wa shati lake. Alipomaliza akamsogelea yule mwanaume pale kitandani na kumchunguza kwa makini kama muuaji anayetafuta hakika na matunda ya kazi yake.
Kulikuwa na kila dalili kuwa yule mwanaume pale kitandani asingechukua muda mrefu kabla ya kukata roho. Hivyo Amanda akamuacha na kuuchukua ule mkoba wa ngozi uliokuwa kando pale kitandani. Haraka akaufungua ule mkoba na kumimina kila kila kitu kilichokuwa ndani yake pale kitandani na baada ya upekuzi mfupi hatimaye akaifikia ile bahasha ndogo ya kaki. Nilimuona Amanda akiichukua ile bahasha na kuanza kuichunguzachunguza kupitia ule mwanga wa taa ya mle ndani kisha akaichana na kutoa karatasi nyeupe yenye maandishi. Hatimaye akayatuliza macho yake akiyasoma maelezo kwenye ile karatasi na kadiri alivyokuwa akiyapitia maelezo yale ndivyo tabasamu lake lilivyokuwa likichanua usoni. Ni kama alikuwa amepata kile alichokuwa akikihitaji.
Hasira zikanipanda, nikatamani kutoka pale mafichoni na kumshikisha adabu Amanda hata hivyo nilichelelewa kwani muda uleule Amanda akairudisha ile karatasi kwenye bahasha na kuitia ile bahasha mfukoni. Kisha akaelekea pale mlangoni ambapo aliufungua ule mlango haraka na kutoka nje. Nikiwa nimeanza kuhisi majibu ya maswali yangu mengi kichwani yalikuwa mbioni kupatikana sikutaka Amanda anitoroke mle ndani kwani kwa namna moja au nyingine nilikuwa na kila sababu ya kuamini kuwa Amanda alikuwa akifahamu juu ya wapi alipokuwa balozi Adam Mwambapa au wati waliohusika kumteka. Hivyo wakati Amanda akitoka mle ndani mimi tayari nilikuwa hatua chache nyuma yake bila yeye kujua. Hata hivyo niseme kuwa sikufanikiwa kwani wakati nikikaribia kuufikia ule mlango wa kile chumba Amanda alikuwa tayari ameshatoka na kuufunga ule mlango kwa nje. Hivyo sikufanikiwa kutoka badala yake nikasikia sauti hafifu ya hatua za Amanda zikiyoyoma kwenye ile korido. Muda mfupi uliofuata nikausikia ule mlango wa kule sebuleni ukifunguliwa na kufungwa kisha baada ya pale mle ndani kukawa kimya.
Nilijaribu mara kadhaa kuufungua ule mlango wa kile chumba ili nitoke nje lakini hilo halikuwezekana kwa haraka kwani ule mlango ulikuwa umefungwa kwa nje hivyo nikabaki nimeganda kama nyamafu huku donge la hasira likiwa limeninasa kooni. Matumaini ya kumpata Amanda taratibu nikaanza kuyaona yakiyeyuka moyoni mwangu. Siyo kwamba ningeshindwa kuufungua ule mlango na kutoka nje la hasha!, lakini nilijua kuwa lingekuwa zoezi ambalo lingenichukua muda kidogo na pale ambapo ningefanikiwa kuufungua ule mlango Amanda tayari angekuwa amekwishatoweka kusikojulikana. Hivyo nikabaki nimeshikwa na hasira nisijue la kufanya.
Nikiwa katika hali ile mara nikajikuta nikishawishika kukimbilia kwenye dirisha la upande wa kulia wa kile chumba ili niweze kutazama nje chini ya lile jengo. Nilipofika pale dirishani nikasogeza pazia na kutazama upande wa pili wa ile barabara iliyokuwa ikikatisha chini mbele ya lile jengo. Kwa kufanya vile mara nikaliona gari dogo jeupe aina ya Nissan Patrol likiacha maegesho kando ya barabara ile na kushika uelekeo wa upande wa kulia na hapo nikahisi kuwa Amanda angewa ndani ya gari lile akiondoka.
Kwa mara ya kwanza nikajikuta nikijilaumu kwa kutokufanya maamuzi ya haraka ambayo yangepelekea nimtie Amanda mikononi wakati alipokuwa akijivinjari mle ndani. Hata hivyo nilijifariji kuwa kwa namna moja au nyingine uvumilivu wangu nyuma ya pazia mle ndani mafichoni ulikuwa na manufaa wakati nilipoikumbuka ile bahasha ndogo ya kaki iliyofichwa chini ya godoro na yule mwanaume aliyeuwawa na Amanda mle ndani muda mfupi uliopita.
Niliporudi pale kitandani nikamkuta yule mwanaume aliyeuwawa kwa kupigwa risasi na Amanda akiendele kuhema taratibu huku mapafu yake yakipambana kuvuta hewa kwa shida. Mara moja nilipomchunguza yule mtu nikatambua kuwa utaalam wowote wa daktari bingwa mbobezi usingeweza kurudisha matumaini ya uhai kwa mtu yule. Pumzi ilikuwa ukingoni na roho yake ni kama ilikuwa imeshikiliwa na uzi mwembamba na dhaifu. Macho yake yalikuwa wazi yakitazama darini huku mdomo wake ameuachama wazi kwa mshangao. Yale matundu mawili ya risasi yalikuwa yakivuja damu na damu ile nyingi sasa ilikuwa ikielekea kutotesha foronya za kile kitanda. Sikuwa na mashaka yoyote kuwa mwanaume yule pale kitandani ndiye angekuwa Léon Dingo, mwenyeji wa ile nyumba.
Nilitamani kutoweka haraka mle ndani hivyo sikuona sababu ya kuendelea kupoteza muda. Akili yangu yote sasa ilikuwa kwenye ile bahasha ndogo ya kaki iliyofichwa na yule mtu chini ya godoro wakati ule Amanda alipokuwa bafuni. Hivyo nikamsogeza kando yule mtu na kufunua lile gadoro na kwa kufanya vile macho yangu yakajikuta yakiitazama bahasha ndogo ya kaki juu ya chaga za kile kitanda. Kwa sekunde kadha macho yangu yakaweka kituo kuitazama ile bahasha huku mawazo mengi yakipita kichwani mwangu. Hatimaye nikaichukua ile bahasha na kuifungua. Ndani ya ile bahasha kulikuwa na karatasi nyeupe iliyokunjwa vizuri hivyo nikaitoa ile karatasi mle ndani na kuifungua. Nilipoyatuliza macho yangu kwenye ile karatasi nikauona mchoro mdogo mfano wa ramani ilichorwa kwa kalamu ya wino.
Ramani ile isiyoeleweka ilikuwa imewekwa alama fulani za mkazo katika baadhi ya maeneo, ingawa mchoraji wa ramani ile hakuwa amezingatia vigezo vya kitaalam lakini alifanikiwa vizuri kuwasilisha kile alichokusudia. Jambo lililonishangaza ni kuwa ile ramani haikuwa na utambulisho wa eneo lolote la jijini Bujumbura au nchini Burundi badala yake katika zile sehemu zilizowekwa mkazo kuliandikwa namba fulani na herufi. Ilikuwa ramani ngeni kabisa na isiyoeleweka machoni mwangu. Hata hivyo nilihisi kuwa ramani ile ilikuwa imehifadhi siri nzito juu ya jambo fulani nisilolifahamu.
Kuendelea kuzubaa mle ndani nikahisi kuwa lingekuwa ni jambo la hatari kwangu hivyo sikuona sababu ya kuendelea kupoteza muda mle ndani. Niliirudisha ile ramani kwenye ile bahasha kisha ile bahasha nikaitia mfukoni mwangu. Niliendelea kufanya upekuzi mle ndani nikianzia kwenye droo za yale makabati na kuelekea kwenye ile selfu ya chuma iliyokuwa kando ya dirisha upande wa kulia wa kile chumba. Nilipoifikia ile selfu na kujaribu kuifungua nikagundua kuwa ilikuwa imefungwa. Bila kupoteza muda nikachukua funguo zangu malaya na kuanza utundu. Haikuwa kazi rahisi lakini baada ya muda nikafanikiwa kuifungua ile selfu ya chuma. Ile selfu ilipofunguka na kutazama mle ndani nikajikuta nikipigwa na mduwao.
Vibunda vya pesa safi, dola za kimarekani vilikuwa vimepangwa na kuhifadhiwa vyema ndani ya ile selfu. Ilikuwa pesa nyingi sana ambayo thamani yake nisingeweza kuifahamu kwa haraka. Nikachomoa noti moja na kuichunguza vizuri nikitumia mwanga mkali wa kurunzi yangu mkononi. Zilikuwa fedha halali na siyo feki kama nilivyokuwa nimeanza kuhisi. Kiasi kile kingi cha pesa kikanitia wazimu katika fikra zangu huku nikishindwa kuamini. Sikuona kama fedha ile ingefanana na kipato halali cha mfanyakazi wa cheo chochote cha benki vilevile niliona kuwa lilikuwa ni jambo la hatari kwa mtu kukaa na kiasi kile kingi cha fedha nyumbani badala ya kuhifadhi benki. Léon Dingo mwenyeji wa ile nyumba hakuelekea hata kidogo kufanana na kiasi kile cha pesa hivyo kwa namna moja au nyingine nilihisi kuwa zile fedha zilikuwa haramu zilizoibwa kutoka sehemu fulani na kuhifadhiwa mle ndani wakati zikipangiwa mkakati wa kutakatishwa.
Nikachomoa kibunda cha kwanza kisha cha pili halafu cha tatu na cha nne na kuvitupia kwenye mifuko ya koti langu. Kibunda cha tano nilipokitia mfukoni, muonekano wangu ukaanza kunisuta, mifuko ilikuwa imetuna na hapo nikajua kuwa isingekuwa rahisi kuondoka na ile pesa yote mle ndani. Nikatamani kutafuta mfuko mkubwa ambao ningetumbukiza pesa ile yote na kupotelea nayo mitaani hata hivyo baada ya kufikiri kidogo nikajikuta nikiachana na mpango ule kwani ile pesa ilikuwa nyingi sana kutembea nayo mitaani bila ulinzi wa kuaminika na endapo ningekutana na purukushani yoyote mbele ya safari nisingekuwa huru kujitetea. Akili yangu ikachangamka na kuanza kufanya kazi kwa kasi ya ajabu.
Muda mfupi baada ya zunguka zunguka ya hapa na pale mle ndani nikawa nimefanikiwa kupata wazo. Kwenye kona moja ya kile chumba upande wa kushoto kulikuwa na kifuniko kidogo cha tundu la kuingilia darini. Nikaona kuwa ingekuwa salama kuzificha zile fedha juu ya dari ya kile chumba hadi hapo baadaye nitakapoamua nini cha kufanya. Hivyo bila kupoteza muda nikachukua zile fedha na kuzifunga kwa pamoja kwenye shuka moja nililolipata kwenye moja ya yale makabati ya mle ndani. Kisha nikadandia mlango wa kabati na kukiondoa kile kifuniko cha darini ambapo niitupia ile pesa darini na kufunika vizuri.
Sasa sikuwa na muda wa kuondelea kupoteza zaidi mle ndani. Lucia, yule msichana hatari niliyemfahamu kwa jina la Amanda nilitambua kuwa alikuwa mbioni kuifikia sehemu fulani katika ramani feki aliyoikuta ndani ya ile bahasha aliyoichukua kwenye ule mkoba mle ndani. Nikajaribu kuvuta picha ni kwa namna gani atakavyochezeshwa shere kama mtoto mdogo. Bado sikupata picha namna atavyochanganyikiwa kabla ya risasi zangu hazijamfumania. Hatimaye nikatoka nje ya kile chumba na kufunga mlango. Muda mfupi uliofuata nilikuwa nje ya ile nyumba nikikatisha kwenye korido kuzifuata ngazi za kushuka chini ya lile jengo.
Mvua kubwa ya radi sasa ilikuwa ikinyesha, giza nalo lilikuwa limetanda kila mahali huku kwa mbali nikisikia milio ya majibizano ya risasi mbali kidogo na eneo lile. Ni dhahiri kuwa hali ya usalama jijini Bujumbura bado ilikuwa kizungumkuti.
Mawazo juu ya Veronica yalikuwa yamenijia akilini kama hisia za mapenzi ziutekavyo ubungo wa binadamu. Kitendo cha kuwa mbali na Veronica kwa muda wa kutwa nzima kilikuwa kimenipelekea nianze kuhisi hali ya upweke. Hivyo mawazo yangu yakahamia Havana Club. Nikawaza kuwa nikiwa huko ningeweza kupata mlo mzuri wa wali wa samaki na juisi ya miwa na kisha kuonana na Veronica huku tukijadili hili na lile kabla ya kumuaga na kuendelea na harakati zangu, tukiahidiana kuonana tena baadaye usiku ule kule nyumbani kwa Veronica.
Nilimaliza kushuka zile ngazi na kushika uelekeo wa upande wa kushoto nikiifuata barabara ya Rue du Ruvubu huku mawazo mengi yakipita kichwani mwangu. Tukio la kuuwawa kwa Léon Dingo kwenye ile nyumba niliyotoka lilikuwa limeibua mjadala mkubwa kichwani mwangu.
Barabara ya Rue du Ruvubu usiku huu ilikuwa pweke sana na yenye ukimya wa kutisha, siyo watu, bodaboda wala magari yalioonekana kukatisha na hali ile ilinipa hadhari na hofu kidogo.
Upande wa kushoto mwisho wa lile jengo la ghorofa kulikuwa na barabara nyingine ya lami iliyokuja na kuungana na ile barabara ya Rue du Ruvubu ambayo sikuifahamu jina lake. Hivyo nilipofika mwisho wa lile jengo la ghorofa nikaingia upande wa kushoto nikiifuata ile barabara iliyokuwa ikikatisha katikati ya majengo marefu ya ghorofa. Lengo langu lilikuwa ni kutafuta kituo cha teksi cha karibu na eneo lile ambapo ningekodi teksi hadi Havana Club.
Hata hivyo kabla sijafika mbali zaidi nikakumbuka kutimiza wajibu wangu wa kujilinda kwa kugeuka nyuma kuchunguza mara kwa mara katika kuhakikisha kuwa hakuna mtu anayenifuatilia. Nikiwa naamini kuwa mambo bado yalikuwa shwari kama kawaida hisia zangu zikaniambia kuwa nilikuwa nikijidanganya.
Kiasi cha umbali usiopungua mita hamsini nyuma yangu nikawaona watu watatu wakiwa katika mavazi ya makoti marefu ya mvua wakiharakisha kuja uelekeo wangu. Moyo wangu wangu ukaingiwa na baridi ya ghafla ingawa sikuwa na hakika kuwa watu wale walikuwa wakinifuata mimi lakini miguu yangu ilikuwa ni kama iliyotiwa mshawasha wa kuharakisha zaidi safari yangu. Hivyo nikaanza kuharakisha huku mara kwa mara nikigeuka nyuma kuwachunguza wale watu. Mashaka yalikuwa yameanza kuniingia, wasiwasi juu ya jambo la hatari ukazidi kuzitekenya fikra zangu, nywele zikanicheza na kijasho chembamba kikaanza kunitoka.
Ingawa sikuwa mgeni na namna ile ya ufuatiliwaji katika harakati zangu nyingi za kijasusi nilizowahi kupitia lakini nilitaka kutafuta hakika juu ya hisia zangu. Hivyo haraka nikavuka ile barabara na kuhamia upande wa pili huku tayari mkono wangu ukiwa umepenya kwenye mfuko wa koti langu kuifikia bastola yangu mafichoni.
Wakati nikivuka ile barabara nikageuka tena nyuma kuwapiga ukope wale watu na hapo moyo wangu ukapoteza utulivu kabisa. Niliwaona wanaume wawili miongoni mwa wale wanaume watatu nyuma yangu wakivuka ile barabara kunifuata. Mashaka yakiwa yameanza kuniingia sasa nilikuwa na hakika kuwa nilikuwa nimefungiwa mkia. Akili ya haraka ikanijia kichwani, sikumaliza kuvuka ile barabara badala yake nikarudia njiani ule upande niliotoka na safari hii macho yangu yalikuwa makini zaidi kuzitazama nyendo za wale watu. Wale watu ni kama walikuwa wameishtukia hila yangu hivyo na wao pia wakavuka barabara wakihamia upande wangu. Kufikia pale sikuona tena sababu ya kuendelea kuzipuuza hisia zangu hivyo taratibu nikaanza kuchanganya miguu kuelekea mbele. Wale watu na wao kuona vile wakaanza kukimbia taratibu wakinifuata na nilipogeuka nyuma kuwatazama nikagundua kuwa endapo ningeendelea kuzembea basi muda siyo mrefu wangenifikia. Sasa nilianza kutimua mbio za hakika...ITAENDELEA
 
RIWAYA: UFUKWE WA MADAGASCAR
SEHEMU: 56

Sasa nilikuwa makini sana na nyendo za wale watu huku nikifahamu kuwa uzembe wowote ambao ningeufanya ingekuwa ni sawa na kucheza maisha yangu kamari hivyo mbio zangu zilikuwa za mwanariadha wa medani za kimataifa.
Kwa mara nyingine nilipogeuka na kutazama nyuma yangu nikajikuta nikishikwa na taharuki baada ya kugundua kuwa idadi ya wale watu waliokuwa wakinifukuza nyuma yangu ilikuwa imeongezeka. Tathmini yangu ikanitanabaisha kuwa jumla yao sasa walikuwa watu watano, nikashindwa kuelewa wale watu wawili walioongezeka walikuwa wametokea wapi. Hata hivyo sikusimama, nikaendelea kutimua mbio lakini kwa tahadhari zaidi kwa vile nilikuwa mgeni wa maeneo yale.
Wale wale walionekana kuwa makini sana na nyendo zangu kiasi cha kutonipa nafasi ya kuwatoroka na badala yake wakajigawa. Wawili upande wa kushoto, mmoja nyuma yangu na wawili wengine upande wa kulia na mbio zao zilikuwa za kuaminika huku makoti yao yakipepea kama vishada.
Hatua chache mbele yangu kulikuwa na kona ya kuelekea upande wa kushoto, hivyo nikapiga mahesabu kuwa mara baada ya kuifikia ila kona ningepata nafasi nzuri ya kupambana na wale watu kwa vile kulikuwa na sehemu nzuri ya kujibanza. Yule mtu aliyekuwa nyuma yangu mbio zake zilikuwa matata sana, hatua zake miguuni zilisafiri kama kiberenge chenye hitilafu ya mfumo wake wa breki huku koti lake likipepea kama bendera chakavu, hivyo alikuwa wa kwanza kunikaribia.
Wakati nikiifikia ile kona ya upande wa kushoto wa ile barabara wale watu nyuma yangu wakawa ni kama walioshtukia dhamira yangu ya kutaka kuwatoroka kupitia ile kona hivyo wakaanza kunifyatulia risasi. Hata hivyo walikwishachelewa kwani niliwahi kujitupa chini haraka na kujiviringisha kama gurudumu la gari nikipotelea kwenye ile kona hivyo risasi zao zikaambulia kunipunyua punyua lakini hakuna iliyonipata. Hatimaye nikajibanza kwenye ile kona huku nikitweta hovyo, moyo wangu ukipiga kite kwa nguvu huku kijasho chepesi kikinitoka puani.
Nikiwa na hakika kuwa wale watu walikuwa mbioni kunifikia nikaikamata vyema bastola yangu mkononi na kugeuka nikichungulia kwenye ile kona huku nikiwa nimeegemea ukuta. Kwa kufanya vile mara nikamuona mtu mmoja miongoni mwa wale watu akiambaa ambaa na ule ukuta kuja kwenye ile kona kunifuata. Sikumkawiza nikamchapa risasi mbili kifuani na kumlaza chali na ule ndiyo ukawa mwisho wake. Wale wenzake kuona vile wakasita kunifuata badala yake nikawaona wakipanga mkakati fulani juu ya vita ile halafu muda mfupi uliofuata nikawaona wakipotelea gizani kama misukule. Tukio lile likanishangaza sana hata hivyo kwangu ilikuwa ni afadhali.
Kitambo kifupi cha ukimya kikapita huku nikiwa bado nimejibanza kwenye ile kona na kuendelea kuchungulia kule nyuma. Sikumuona mtu yeyote wala kuhisi kitu chochote na hali ile ilizidi kunishangaza. Nikiwa nimeipa utulivu milango yangu ya fahamu sikusikia sauti ya kitu chochote isipokuwa sauti za njiwa zilizokuwa zikihanikiza kutokea kwenye vipenyo vya juu vya paa la lile jengo la ghorofa lililokuwa likipakana na ile barabara. Nikajiuliza wale watu wangekuwa wamepotelea wapi na kwanini waliamua kuniacha huru namna ile bila kuendelea na jitihada zozote za kunidhibiti. Jibu sikulipata lakini vilevile sikutaka kuamini kuwa hali ilikuwa shwari hivyo haraka nikasimama na kuanza kutimua mbio nikiifuata ile barabara ya upande wa kushoto. Bado sikuweza kusikia sauti ya kitu chochote cha kunishtua zaidi ya mitupo ya mapigo yangu ya moyo na vishindo vya hatua zangu ardhini.
Sikujua ni wapi nilikuwa nikielekea lakini sasa nilikuwa nikikimbia kuifuata ile barabara iliyokuwa imekatisha katikati ya yale majengo marefu ya ghorofa. Hakukuwa na umeme eneo lile hivyo ile barabara ilikuwa katikati ya giza nene na mvua nayo ilikuwa ikinyesha. Mwendo wangu ulikuwa wa matiti hasa, koti langu likipepea huku bastola yangu nimeikamata vyema mkononi.
Loh! nilikuwa sijafika mbali sana katika mbio zangu pale hisia mbaya ziliponijia akilini kuwa miguu yangu ilikuwa ikinipeleka mautini na hapo nikapunguza mwendo huku nikianza kuziogopa hisia zangu. Nilipogeuka kutazama nyuma sikumuona mtu yeyote na hapo nikajiona kama niliyemezwa na hisia za woga. Hivi mimi nakimbia nini kama mwehu wakati hakuna chochote kinachonifukuza?. Nikajiuliza lakini kabla sijaanza kujipongeza kwa maamuzi yangu mara nikasikia sauti kali ya mluzi mwepesi kutoka sehemu jirani na eneo lile, kisha nikasikia sauti ya mvumo wa kitu fulani kikija kwa kasi eneo lile. Haraka nikaikumbuka sauti ile hatari ya mvumo niliyowahi kuisikia mara kadhaa katika harakati zangu za kijasusi hivyo nikawahi kuchumpa nikijitupia kwenye mtaro uliokuwa kando ya ile barabara.
Kombora zito la silaha kali aina ya LPG lilikuwa limetumwa pale nilipo na kunikosa badala yake likachimbua kipande kikubwa cha ardhi na masalia ya kifusi kile yakanifunika baada ya sauti kali ya mlipuko wa lile bomu kusikika. Nikiwa pale mtaroni mara nikaanza kusikia mvua ya risasi ikianza kurindima eneo lile kwa mipigo ya ufundi tofauti na nilipoyatuliza masikio yangu na kuyatega vizuri, tathmini yangu ikaniambia kuwa bunduki ya mrusi aina ya AK-47 ilikuwa kazini.
Nikiwa pale mtaroni nikaendelea kuyatega vizuri masikio yangu ili kufahamu kuwa milio ile ya risasi ilikuwa ikitokea upande gani eneo lile. Mbele ya ile barabara upande wa kushoto juu ya jengo moja la ghorofa risasi zile ndiyo zilipokuwa zikitokea. Niligundua haraka baada ya kuuona mtutu wa bunduki namna ulivyokuwa ukitema cheche. Muda mfupi uliofuata shambulizi lile la risasi likakoma kisha nikasikia kelele za watu zikihanikiza eneo lile. Sikuwa na shaka yoyote kuwa kile kingekuwa kikundi cha watu na nilipoyatega vizuri masikio yangu mara nikasikia vishindo watu wale wakitimua mbio kuja eneo lile. Nilikuwa nimekumbuka kuwa kufuatia jaribio la mapinduzi ya kijeshi nchini Burundi hadi kufikia wakati ule baadhi ya maeneo ya jiji la Bujumbura yalikuwa yakishikiliwa na vikundi vya waasi na hivyo huwenda pia kikundi kile kingekuwa miongoni mwavyo.
Hivyo sikutaka kusubiri badala yake haraka nikajitoa kwenye mabaki ya kile kifusi mtaroni kisha nikasimama na kuanza kutimua mbio nikirudi kule nilipotoka. Hata hivyo sikufika mbali katika harakati zangu kwani dhamira yangu ni kama ilikuwa imeshutukiwa na wale watu na hapo wakaanza kunikimbiza huku wakianza kunifyatulia risasi nyuma yangu. Niliendelea kukimbia huku nikijitahidi kuzikwepa zile risasi kwa kila namna kwa kutoka upande mmoja wa barabara na kuhamia upande mwingine huku nikijitupa chini na kusimama. Hata hivyo hatari ikazidi kunikaribia kwani wale watu walikuwa wengi na suala la kufyatua risasi halikuonekana kuwa na pingamizi lolote katika kuhakikisha kuwa wananitia mikononi. Baadhi ya risasi zikawa zikinipita juu, kuchimba ardhini na kupukutisha kuta za majengo ya jirani na eneo lile.
Kuona vile nikachepuka na kuingia upande wa kushoto nikilifuata jengo moja la ghorofa la siku nyingi ambalo lilikuwa halijamaliziwa kujengwa kwa sababu nisizozifahamu. Ni dhahiri kuwa hatari ya kifo ilikuwa hatua chache nyuma yangu hivyo moyo wangu ulikuwa ukienda mbio isivyokawaida. Haraka nilikuwa nimetambua kuwa mbio zangu zisingeweza kufua dafu mbele ya risasi zile.
Nilipolifikia lile pagale jengo la ghorofa nikaanza kuparamia ngazi za zege za lile jengo kupanda juu huku risasi zikinikosakosa nyuma yangu. Sikusimama na hatimaye nikafika ghorofa ya pili ya lile jengo na wakati ule nikawa nikisikia sauti ya vishindo vya watu wakikazana kukwea zile ngazi kwa papara kunifuata kule juu. Kuona vile nikageuka na kuanza kuwafyatulia risasi wale watu, mara mbili tatu nikasikia sauti za watu miongoni mwao wakipiga mayowe lakini haikusaidia kitu kwani ni kama nilikuwa nimeutibua mzinga wa nyuki na kunipelekea nijute kwa kitendo kile kwani muda uleule wale watu wakaanza kunifyatulia mvua ya risasi, na hapo eneo lile lote likasambaa moshi wa risasi.
Hatari ikiwa imenikaribia ile sehemu haikuwa salama tena kwangu, hivyo kuona vile haraka nikaanza kukwea ngazi nyingine kuelekea ghorofa ya tatu ya lile jengo nikitafuta sehemu nzuri ya kuificha roho yangu. Hofu ya kukamatwa mzimamzima tayari ilikuwa imeanza kuniingia kwani niliamini kuwa kuwa mara baada ya kufika juu kabisa ya lile jengo nisingekuwa na sehemu nyingine zaidi ya kukimbilia. Bahati mbaya sana lile jengo la ghorofa lilikuwa limeishia ghorofa ya tatu. Hivyo sikuwa na sehemu nyingine ya kukimbilia.
Mara baada ya kuifikia ile ghorofa ya tatu haraka nikaanza kuzunguka pande za lile jengo kuchunguza kama kungekuwa na upenyo wowote wa kutoroka. Nyuma ya lile jengo sehemu ya chini nikaiona barabara moja ya lami. Roho ya ujasiri ikaniambia nijirushe kule chini barabarani na endapo ningetua salama ningeanza tena kutimua mbio nikipotelea mitaani. Katika mafunzo magumu ya ujasusi na ukomandoo umbali ule usingekuwa kikwazo kikubwa hususani pale linapokuja suala la usalama wa roho yangu. Wale watu waliokuwa wakinifukuza sasa walikuwa mbioni kuifikia ile ghorofa ya tatu ya lile jengo na kwa kweli sikutaka wanifikie huku kazi yangu nikiwa bado sijaimaliza. Lakini pia sikuwa tayari kukabiliana na kifo cha aibu na cha mateso makali.
Bahati ilikuwa kwangu kwani wakati nilipokuwa nikijiandaa kujirusha chini ya lile jengo mara nikasikia muungurumo wa gari likiingia na kukatisha kwenye ile barabara chini ya lile jengo. Nilipochungulia vizuri chini ya lile jengo nikaliona roli la jeshi lililofunikwa na turubai kwa nyuma. Loh! nikapata matumaini ya kutoroka salama hivyo nikasubiri lile roli lifike chini kwenye usawa wa lile jengo na hapo nikajirusha hewani kulifuata lile lori. Mahesabu yangu yalikuwa sawia kwani muda mfupi uliofuata nikatua nyuma ya lile lori kama paka na hivyo kusababisha mtikisiko hafifu. Kisha baada ya hangaika hangaika ya hapa na pale nikafanikiwa kupata sehemu ya kujishikilia na hapo nikajilaza chali kwa utulivu.
Dereva wa lile roli akapunguza mwendo kidogo kama aliyehisi kishindo changu huku akitazama nyuma kupitia vioo vya ubavuni vya lile lori. Hakuona kitu chochote hivyo akapuuza na kuongeza mwendo wa lori. Bastola yangu ikiwa mkononi nikageuka na kutazama kule juu ya lile jengo la ghrofa nilikojirusha na hapo nikauona mwanga wa kurunzi ukimulika mulika huku na kule. Tabasamu hafifu likachipua taratibu usoni mwangu, ule mwanga wa kurunzi ukawa ukitokomea taratibu machoni mwangu kadiri lile roli lilivyokuwa likitokomea mbali na eneo lile.
_____
Mwendo wa lile lori la jeshi ulikuwa wa kasi sana na nikiwa juu ya lile lori kule nyuma niliweza kuitathmini vizuri safari ile wakati lile lori lile lilipokuwa likiingia barabara ya mtaa mmoja na kutokea barabara ya mtaa mwingine. Taratibu moyo wangu ulikuwa umeanza kurejewa na utulivu huku nikiwa bado siamini vizuri kuwa nimefanikiwa kutoroka kifo.
Mvua kubwa ilikuwa ikiendelea kunyesha na kufuatia jaribio lile la mapinduzi ya kijeshi nchini Burundi watu wengi walikuwa wameyakimbia makazi yao na hivyo kupelekea mitaa ile kubaki na ukiwa. Magari ya jeshi barabarani sasa yalikuwa mengi kuliko ya raia na vile vikwazo vya barabarani vyenye askari navyo vilikuwa vimeongezeka.
Nilipousogeza mkono wangu karibu kutazama majira kwenye saa yangu ya mokononi nikagundua kuwa muda wa Veronica kutoka kazini kwake tayari ulikwishafika. Nilikuwa tayari nimechelewa hivyo suala la kuonana tena na Veronica kule Havana club ni dhahiri kuwa lisingewezekana tena kwa wakati ule. Njaa ilikuwa ikiniuma na safari ya harakati zangu bado ilikuwa ndefu. Hivyo nikajikuta nikitamania kushukia sehemu yoyote kwenye mgahawa wa karibu ambapo ningeweza kupata mlo mzuri kabla ya kuamua nielekee wapi. Wazo lile likanipelekea nijisogeze pembeni ili niweze kuona vizuri kwenye ile mitaa lile lori lilipokuwa likipita.
Hali ilikuwa tofauti na matumaini yangu ya kutaka kuuona mgahawa wowote wa karibu na eneo lile yakafutika. Lile lori lilikuwa likielekea nje ya jiji la Bujumbura na sasa tulikuwa tukiliacha nyuma eneo la makazi ya watu na kuifuata barabara ya vumbi iliyokuwa ikilekea msituni. Tukio lile likanishtua sana, starehe ya kule juu ilikuwa imenilaghai na kunipelekea nijisahau hadi kupelekwa sehemu nisiyoitaka. Sikuweza kufahamu kuwa lile lori lilikuwa likielekea wapi kwani lengo langu lilikuwa ni kufika kwanza katikati ya jiji la Bujumbura na baada ya mlo katika mgahawa wowote wa kisasa ningepata akili kuwa nishike uelekeo upi kabla ya baadaye kurudi kule nyumbani kwa Veronica.
Hivyo sikuona sababu ya kufuata uelekeo wa lile lori hasa kwa kuzingatia kuwa lile lori lilikuwa likishika uelekeo wa nje ya jiji la Bujumbura. Kuona vile taratibu nikaanza kujisogeza kurudi nyuma ya lile lori ambapo hatimaye ningeshuka na kushika uelekeo wangu.
Loh! sikufanikiwa kwani wakati nilipokuwa katika harakati za kushuka mara kwa mbali nyuma ya lile lori nikauona mwanga mkali wa taa za mbele za gari likitufuata. Haraka nikajilaza na kurudi kule mbele nilipotoka ambapo niliwahi kujibanza, lengo langu likiwa nisiweze kuonekana na watu waliokuwa kwenye lile gari lililokuwa nyuma yetu. Lile gari nyuma yetu lilikuwa katika mwendo wa kasi mno na dereva wake alikuwa amewasha full light kulimulika lile lori nililokuwa. Nikaanza kuingiwa na wasiwasi huku nikijiuliza nini kilichokuwa kikiendelea. Jibu sikulipata hivyo nikaendelea kujibanza juu ya lile lori huku nikilitazama lile gari kule nyuma namna lilivyokuwa likifukua mbio kutukaribia.
Tulikuwa tayari tumetembea umbali mrefu na sasa lile lori lilikuwa limekunja kona kuingia upande wa kulia kuifuata barabara nyingi ya nyasi iliyokuwa ikikatisha msituni mbali na mji na makazi ya watu. Lile gari sasa lilikuwa umbali mfupi nyuma yetu na dereva wa lile gari hakuonesha jitihada zozote za kutaka kulipita lile lori. Nilipolichunguza vizuri lile gari nikagundua kuwa lilikuwa ni gari dogo la jeshi aina ya Tdi-Discover. Sikuwa na mashaka yoyote kuwa dereva wa lile lori alikuwa tayari ameliona lile gari dogo nyuma yetu hata hivyo nilishangaa kuona yule dereva wa lile lori hafanyi jitihada zozote za kutaka kusimama au kuzidi kukimbia. Hivyo nikaanza kuhisi huwenda watu wale walikuwa kitu kimoja na walikuwa wakifahamiana.
Bila shaka tulikuwa tumesafiri katika umbali usiopungua maili thelathini na ushei katika barabara mbovu yenye madimbwi ya maji, makorongo na mawe katika msitu mzito pale nilipoliona lile lori likipunguza mwendo na kuanza kuingia msituni zaidi sehemu kusikokuwa na barabara katikati ya nyasi ndefu na miti mikubwa. Lile gari dogo nalo nikafanya vilevile likilifuata lile lori taratibu kwa nyuma. Tukazidi kuzama kwenye ule msitu hadi tulipofika katikati ya msitu mnene ambapo lile lori lilisimama. Kuona vile kwa tahadhari nikajisogeza vizuri na kutazama kule mbele ya lile lori.
Kupitia mwanga wa taa za mbele za lile lori niliweza kuona vizuri kule mbele ya ule msitu. Kulikuwa na shimo kubwa lililochimbwa na kifusi cha shimo lile kilikuwa kando yake kama mlima mdogo. Nikashtuka huku nikishindwa kuelewa ni nani aliyechimba shimo lile katikati ya msitu mnene kama ule sehemu kusikokuwa na dalili ya makazi ya watu. Shimo lile lilikuwa la nini na mchimbaji alilichimba kwa makusudi gani?. Nikajiuliza huku nisipate majibu hivyo nikabaki na mashaka.
Muda mfupi baada ya lile lori kusimama na lile gari dogo la jeshi Tdi-Discover nalo likasimama huku limewasha taa za mbele kisha muda uleule milango ya lile gari dogo ikafunguliwa na hapo nikawaona wanaume sita katika sare za jeshi wakishuka na bunduki zao mkononi. Miongoni mwao walikuwepo Koplo watatu, Luteni mmoja, na Meja wawili ambao niliwatambua vizuri kutokana na vyeo katika sare zao za jeshi.
Wale watu waliposhuka wakaanza kutembea taratibu na kwa tahadhari ya hali ya juu kuja nyuma ya lile lori. Kwa kweli niliingiwa na wasiwasi hivyo nikaanza kujiandaa kukabiliana hali yoyote ambayo ingejitokeza. Wakati wale watu wakizidi kuikaribia sehemu ya nyuma ya lile lori mara nikaiona milango ya mbele ya lile lori nayo ikifunguliwa kisha wakashuka wanajeshi wengine watatu mmoja wao akiwa ni dereva wa lile lori ambapo nao wakaanza kutembea wakija kule nyuma ya lile lori. Sikuweza kufahamu vyeo vya wale askari walioshuka kwenye lile lori kwa vile walikuwa wamevaa suruali na fulana za jeshi huku kichwani wakiwa wamevaa kofia za jeshi aina ya bereti. Nilipozidi kuwachunguza vizuri wale wanajeshi nikagundua kuwa wawili miongoni mwao walikuwa na bunduki aina ya SMG mikononi mwao isipokuwa yule dereva ambaye alikuwa ameshika bastola mkononi. Mashaka yakiwa yameanza kuniingia nikaanza kunusa harufu ya jambo la hatari eneo lile.
Wale watu wote wakakusanyika nyuma ya lile lori kisha wale askari watatu wenye cheo cha Koplo wakapanda kule nyuma ya lile lori na kufungua lile turubai kisha wakaingia ile sehemu nyuma. Moyo wangu ulikuwa ukidunda isivyo kawaida, hofu ilikuwa imeniingia na sasa nilianza kuhisi jambo fulani la hatari lililokuwa mbioni kutokea. Nikatamani nishuke chini ya lile lori na kuanza kutimua mbio lakini roho yangu ilisita huku nikihisi kuwa nisingefika mbali kabla ya risasi za watu wale hazijanilaza chali. Hivyo nikaendelea kujibanza juu ya lile lori huku nikitazama kilichokuwa kikiendelea.
Mara baada ya wale wanajeshi wenye cheo cha Koplo kuingia nyuma ya lile lori nikaanza kusikia mburuto wa vitu fulani na wakati nikiwa natafakari juu ya sauti ile ya mburuto mara nikawaona watu wakishushwa chini nyuma ya lile lori kwa kusukumwa na hapo nikasogea karibu na kuchungulia kule nyuma. Kwa sekunde kadhaa moyo wangu ukasimama baada ya kuona kile kilichokuwa kikiendelea nyuma ya lile lori.
Jumla ya watu ishirini na mbili wakashushwa kutoka nyuma ya lile lori, watu wale walikuwa wanaume na wote walikuwa wamefungwa kwa kamba miguu na mikononi kama ng’ombe wa machinjioni na vichwani walikuwa wamevalishwa mifuko myeusi huku wakiwa uchi wa mnyama. Watu wale wakashushwa chini kama mizigo wakiangukiana hovyo na miili yao ilikuwa na majeraha mabaya ikiashiria kuwa walikuwa wamepitia mateso makali kabla ya kufikishwa pale msituni. Kwa kweli nilikuwa nimeshangazwa sana kwani muda wote ule niliokuwa juu ya lile lori sikuwa nimeshtukia kuwa mle ndani kulikuwa na watu.
Wale watu waliposhushwa chini ya lile lori wakaanza kuburutwa kuelekea kando ya lile shimo lililochimbwa mbele ya lile lori ambalo sasa lilikuwa limeanza kujaa maji kutokana na mvua kubwa iliyokuwa ikeendelea kunyesha. Walipofika kando ya lile shimo wale watu wakaketisha chini katika mstari mmoja mnyoofu na hapo nikawasikia wale watu wakianza kuomba msamaha huku wengine wakiangua kilio cha majuto lakini hakuna aliyeonekana kuwasikiliza badala yake nikawaona wale askari waliokuwa wakiwaburuta wakijipanga mbele yao na bunduki zao mkononi. Hofu ikaniingia baada ya kuhisi nini ambacho kingefuatia baada ya pale.
Mara nikamuona mwanajeshi mmoja mwenye cheo cha Meja miongoni mwa wale wanajeshi akiwaonesha wenzake ishara fulani kwa kichwa na hapo mwili wangu ukaingiwa na baridi ya ghafla huku nikishindwa kuamini macho yangu.
Muda uleule pale msituni pakaanza kurindima sauti ya risasi zisizo na idadi, risasi zile zikielekezwa kwa wale watu waliofungwa kamba miguuni na mikononi na kufunikwa kwa mifuko myeusi kichwani. Sauti za wale watu wakipiga mayowe ya hofu na maumivu zikahanikiza mle msituni kisha baada ya pale kukafuatiwa na ukimya baada ya wale watu kuanguka chini na hapo wale wanajeshi wakasitisha kufyatua risasi. Lilikuwa tukio la kinyama sana kuwahi kulishuhudia hata hivyo sikuwa namna ya kufanya kuzuia unyama ule.
Baada ya wale wanajeshi kusitisha kufyatua risasi nikamuona yule mwanajeshi mwenye cheo cha Luteni akiwasogelea wale watu waliofyatuliwa risasi na kuwageuza geuza kwa buti lake mguuni akiwakagua mmoja baada ya mwingine na aliporidhika akawafanyia ishara ya kichwa wale wanajeshi wenzake kuwa kazi ilikuwa imekamilika na hapo wote wakaanza kuondoka eneo lile. Nikaendelea kuwatazama wale watu huku nikiwa bado juu ya lile lori. Mtu mmoja miongoni mwa wale watu waliofyatuliwa risasi akaanza kusota taratibu kutoka lile eneo na kuelekea kwenye kichaka kimoja kilichokuwa kando ya lile eneo huku akiwa hajiwezi kwa hali baada ya kuchakazwa vibaya na risasi.
Haukupita muda mrefu mara nikawaona wale askari wenye cheo cha Koplo wakirudi eneo lile huku wakiwa wameshika machepe mikononi. Walipofika lile eneo lile bila kupoteza muda wakaishika miili ya wale watu na kuanza kuwatupia kwenye lile shimo. Zoezi lile likafanyika haraka na wale watu walipoamaliza kuwatupia wale watu shimoni wakaanza kulifukia lile shimo kwa kutumia yale machepe mikononi. Mambo yote yalifanyika haraka na wale wanajeshi walipomaliza kufukia lile shimo wakaondoka lile eneo na kurudi kwenye lile gari dogo kule nyuma na kupanda na hapo lile gari likageuza na hapo safari ya kuondoka eneo lile ikaanza.
Nilikuwa nimemkumbuka yule mtu mmoja miongoni mwa wale watu waliouwawa kwa kufyatuliwa risasi eneo lile ambaye alikuwa amejificha kwenye kile kichaka cha jirani na lile shimo. Nilihisi kuwa kulikuwa na jambo muhimu nililopaswa kulifahamu kabla ya kuondoka eneo lile hivyo wakati lile lori likigeuza mimi nikawahi kudandia tawi la moja la mti juu ya lile lori na kuliacha lile lori la jeshi likitokomea. Nilipohakikisha kuwa hali ilikuwa shwari taratibu nikashuka chini ya ule mti huku bastola yangu ikiwa mikononi na hapo nikaanza kunyata kwa tahadhari nikielekea kwenye kile kichaka alipokuwa amejificha yule mtu.
Sauti ya yule mtu aliyekimbilia kule kichakani sasa ilikuwa dhahiri ikisikika masikioni mwangu, alikuwa akihema kwa shida, mapafu yake yalikuwa yakihangaika kutafuta hewa baada ya mzunguko wake wa damu mwilini kuingia hitilafu kupitia majeraha mabaya ya risasi kifuani mwake. Haraka nikachukua kurunzi yangu kutoka mfukoni kisha nikaiwasha na kummulika yule mtu mbele yangu.
Loh! yule mtu alikuwa amelala chali kwenye nyasi dhaifu, miguuni na mikono yake ilikuwa imefungwa kikamilifu na kichwani alikuwa amevikwa mfuko mweusi wa nguo. Zile risasi zilikuwa zimeacha majeraha mabaya mwilini mwake yasiyo na matumaini ya uhai na majeraha yale yalikuwa yakivuja damu nyingi.
Taratibu nikamsogele yule mtu pale chini, ule mwanga wa kurunzi yangu mkononi bila shaka ulikuwa umemshtua kiasi cha kumpelekea aanze tena kujisotesha taratibu kuingia ndani zaidi ya kile kichaka. Nikawahi kumzuia kwa kumshika mguu na hapo yule mtu akajitahidi kupingana na kitendo kile lakini mwili wake haukuwa na nguvu tena, hatimaye nikamvua ule mfuko mweusi kichwani...ITAENDELEA
 
RIWAYA: UFUKWE WA MADAGASCAR
SEHEMU: 57

Loh! yule mtu alikuwa amelala chali kwenye nyasi dhaifu, miguuni na mikono yake ilikuwa imefungwa kikamilifu na kichwani alikuwa amevikwa mfuko mweusi wa nguo. Zile risasi zilikuwa zimeacha majeraha mabaya mwilini mwake yasiyo na matumaini ya uhai na majeraha yale yalikuwa yakivuja damu nyingi.
Taratibu nikamsogelea yule mtu pale chini, ule mwanga wa kurunzi yangu mkononi bila shaka ulikuwa umemshtua kiasi cha kumpelekea aanze tena kujisotesha taratibu kuingia ndani zaidi ya kile kichaka. Nikawahi kumzuia kwa kumshika mguu na hapo yule mtu akajitahidi kupingana na kitendo kile lakini mwili wake haukuwa na nguvu tena na hatimaye nikamvua ule mfuko mweusi kichwani.
“Tafadhali nakuomba usiniue”.Yule mtu akanisihi huku majeraha yake yakiniogopesha kwa namna alivyochakazwa vibaya na risasi za wale watu. Hata kama nisingemuua basi dakika kumi za uhai wake hapa duniani ingelikuwa ni muujiza wa kwanza kuwahi kuushuhudia kwa karibu.
“Ondoa shaka, nahitaji kukusaidia”. Nikamwambia yule mtu huku nikimtazama kwa makini usoni. Umri wake ungelingana na wangu, muenekano wake ukanitanabaisha kuwa alikuwa askari jeshi na cheo chake nisingeweza kukifahamu. Mtu mwembamba, mrefu na mwenye macho makali yaliyohifadhi siri na hila nyingi.
“Wewe ni nani?”. Yule mtu akaniuliza huku akihema kwa taabu.
“Mimi ni mwindaji katika msitu huu, nimeshuhudia yote uliyofanyiwa wewe na wale wenzako muda mfupi uliyopita wakati nikiwa nimejificha humu msituni”. Nikamdanganya yule mtu huku nikimsogeza na kumuegemeza vizuri kwenye shina la mti mmoja mkubwa uliokuwa eneo lile.
“Tafadhali naomba unipeleke hospitali kabla sijafia hapa”. Yule mtu akanisihi huku mkono wake unaotetemeka ukinishika begani.
“Wewe ni nani?”
“Askari wa jeshi la wananchi wa Burundi, Staff Sajenti Evariste Habonimana.
“Na wale watu waliowafyatulia risasi ni akina nani?”. Nikamuuliza kwa shauku.
“Wanajeshi walioasi jeshi letu na kupanga jaribio la mapinduzi ya kijeshi hapa Burundi”
“Sasa imekuwaje hadi wakaja kuwaulia huku msituni?”. Nikauliza kwa udadisi.
“Tafadhali naomba uniwahishe hospitali hali yangu ni mbaya sana”. Yule mtu akanisihi zaidi huku akionekana kulipuuza swali langu.
“Sawa lakini nitalazimika kukubeba maana hakuna usafiri wa haraka eneo hili”. Nikamtia moyo huku nikijitia kumuweka sawa kwanza kabla ya kuanza kwa safari yetu.
“Tulikuwa miongoni mwao kabla hawajagundua kuwa tunawasaliti kwa kuvujisha siri za mipango yote ya mapinduzi ya kijeshi kwa viongozi wetu watiifu kwa serikali”
“Kwanini mmewasaliti wenzenu?”
“Tumechoshwa sana na vita vya wenyewe kwa wenyewe visivyoisha katika nchi hii”. Maelezo ya yule mtu yakanipelekea nitulie kidogo na kumtazama huku tafakuri fupi ikipita kichwani mwangu.
“Kiongozi wa mapinduzi haya ya kijeshi ni nani?”. Hatimaye nikamuuliza yule mtu.
“Simfahamu, inasemekana kuwa ni watu wachache wanaomfahamu na mimi siyo miongoni mwao”. Yule mtu akaongea kwa tabu huku akikihangaisha kichwa chake kutafuta unafuu.
“Ni siri gani za mapinduzi hayo ya kijeshi mlizokuwa mkizivujisha?”. Nikamuuliza yule mtu kwa udadisi.
“Mipango yote ya jaribio la mapinduzi ya kijeshi yaliyofanyika hapa nchini”. Yule mtu akaongea kwa taabu huku akikohoa damu.
“Wahusika wa jaribio hilo la mapinduzi ya kijeshi ni akina nani?”
“Baadhi ni makamanda wa jeshi, viongozi wenye nyadhifa muhimu serikalini, baadhi ya nchi marafiki na mamluki kutoka nchi wahisani”
“Vikao vya jaribio hili la mapinduzi ya kijeshi vilikuwa vikifanyika wapi?”
“Nyumba namba 42 mtaa wa Boulevard Mwezi Gisabo”. Yule mtu akaongea kwa tabu kisha akaweka kituo kidogo akikohoa kabla ya kunisihi tena.
“Tafadhali naomba uniwahishe hospitali hali yangu ni mbaya sana”. Yule mtu akazidi kunisihi huku akinikamata shingoni kwa nguvu zake zote. Macho yake yalikuwa yameanza kupoteza nuru na mwili wake ulikuwa ukipoa kwa haraka, mdomo wake ulikuwa ukimchezacheza kwa hofu na roho yake ni kama ilikuwa imeshikiliwa na uzi mwembamba na dhaifu. Sikuwa na shaka yoyote kuwa muda si mrefu angekata roho. Hatimaye macho yangu yakaweka kituo kumtazama huku nikifikiria swali jingine la kumuuliza. Lakini ni kama nilikuwa nikipoteza muda kwani muda uleule nilimuona yule mtu akianza kuhangaika kisha muda mfupi baadaye akatulia huku roho yake ikiwa mbali na mwili. Muda haukuwa rafiki tena hivyo nikasimama na kulichunguza vizuri eneo lile, niliporidhika kuwa hali ilikuwa shwari nikaanza kuondoka.
_____
Kitendo cha teksi kusimama ghafla kikayarudisha tena mawazo yangu mle ndani na hapo nikageuka upande wa kulia nikishusha kioo cha mlangoni na haraka kuyapeleka nje macho yangu. Au Bon Prix, taswira ya Supermarket ndogo ya kisasa ikaumbika machoni mwangu na kunitanabaisha kuwa tayari tulikuwa tumefika barabara ya Avenue Burambi jijini Bujumbura. Kabla dereva wa teksi hajanisemesha nikatumbukiza mkono wangu mfukoni kuchukua Wallet, nilipoifungua nikachomoa noti mbili za faranga za Kirundi na kumpa yule dereva aliyeonekana kushangazwa sana ziara yangu ile ya usiku kisha nikafungua mlango na kushuka nikiiacha ile teksi ikichochea mwendo na kutokomea mitaani.
Baada ya safari ndefu ya kutembea kwa miguu tangu nilipotoka kule msituni niliposhuhudia mauaji ya wale watu ishirini na mbili wakipigwa risasi, hatimaye nilikuwa nimepata usafiri wa teksi katika barabara ya Chaussée d’uvira huku nikiwa mbioni kukata tamaa baada ya magari mengi niliyoyasimamisha kuomba lifti kunipita kama mti bila kusimama. Ramani yangu ndogo ya kijasusi ilikuwa imenielekeza kuwa barabara ya Avenue Burambi na barabara ya Boulevard Mwezi Gisabo zilikuwa jirani na kwa vile sikutaka dereva yule wa teksi afahamu nilipokuwa nikielekea hivyo nikawa nimemuomba anishushie nje ya Supermarket ya Au Bon Prix.
Ile teksi ilipotokomea nikavuka barabara upande wa pili nikiipa mgongo ile Supermarket ya Au Bon Prix na hapo nikaanza kutembea kwa miguu huku mkono wangu mmoja nimeutumbukiza kwenye mfuko wa koti langu kuikamata bastola yangu vyema. Sikuona gari, bodaboda wala mtembea kwa miguu na majengo yote yaliyokuwa yamepakana na ile barabara yalikuwa gizani isipokuwa ile Supermarket ya Au Bon Prix ambayo juu yake kulikuwa na bango lenye maandishi makubwa yanayowaka taa yakisomeka Au Bon Prix. Mandhari yale yalitawaliwa na utulivu wa kifo na japokuwa mvua ilikuwa ikinyesha niliweza kuisikia vizuri mitetemo ya hatua zangu ardhini sambamba na mapigo ya moyo hata hivyo sikuacha kugeuka nyuma katika kila hatua tano nilizosafiri.
Mwisho wa barabara ile ya Avenue Burambi nikaingia upande wa kushoto na hapo nikajikuta nimetokezea kwenye barabara ya Boulevard Mwezi Gisabo. Barabara ya Boulevard Mwezi Gisabo ilikuwa barabara pana ya lami kama zilivyokuwa barabara nyingi kuu zinazokatisha katikati ya miji mikubwa. Barabara ile ilikuwa ikipakana na majengo mengi ya ghorofa ya shirika la nyumba la taifa. Hata hivyo barabara ile haikuwa na taa na hivyo kutawaliwa na giza zito. Niliyaona magari machache yakikatisha katika barabara ile hata hivyo kulikuwa na utulivu wa kupita kiasi.
NIliendelea kutembea kandokando ya barabara ile huku nikichunguza mandhari yale na niliporidhika na utafiti wangu nikavuka barabara upande wa pili. Sasa nikawa natembea karibu na majengo yale ya ghorofa, sikumuona mtu yeyote akitembea barabarani kama mimi na hali ile ikanipelekea nizidi kuwa makini. Kulikuwa na maelekezo mazuri yanayoweza kumsaidia mgeni kufika nyumba anayoitaka katika kila jengo la ghorofa.
Nyumba namba 42 ilikuwa katika jengo la ghorofa ya tano katika majengo mengi ya ghorofa yaliyoongozana yakitazamana na ile barabara. Taa za jengo lile zilikuwa zimezimwa na katika sehemu ya maegesho sikuona gari lolote na hapo nikaanza kupata mashaka huku nikijiuliza kama kweli nilikuwa sehemu sahihi. Nilipofika mbele ya jengo lile nikasimama huku nikiyatathmini vizuri mandhari yake chini ya mti mmoja katika miti mingi iliyokuwa eneo lile. Hapakuwa na dalili za uwepo wa mtu au watu eneo lile ingawa hali ile isingetosha kuniridhisha kuwa nilikuwa mahali salama. Hali bado ilikuwa shwari hivyo hatimaye nikaayacha maficho yale na kuanza kuambaa ambaa na ukuta wa lile jengo na nilipozifikia ngazi za lile jengo nikaanza kupanda kuelekea juu.
Kwa mujibu wa maelekezo yaliyokuwa chini ya lile jengo ni kuwa nyumba namba 42 ilikuwa katika floo ya tatu upande wa kushoto. Niliendelea kupanda zile ngazi na nilipofika katika floo ya kwanza nikasimama kwenye korido ndefu inayotazamana na milango mingi na baada ya kupeleleza vizuri mandhari yale tathmini yangu ikanieleza kuwa lile jengo lilikuwa halitumiki, huwenda kwa miezi kadhaa kama siyo miaka. Mamlaka ya shirika la nyumba la Burundi ilikuwa imetoa amri ya kuwataka wakazi wote waliokuwa wakiishi kwenye jengo lile kuhama kutokana na uchakavu mkubwa wa jengo lile ili kupisha ukarabati kwani uchakavu na ubovu wa jengo lile ulikuwa ukitishia uhai wa wakazi wake. Nilifahamu vile baada ya kusoma maelezo katika karatasi moja iliyobandikwa kwenye korido ile kwa muda mrefu kiasi cha maandishi yake kufifia na hivyo kusomeka kwa shida.
Vioo vya jengo lile vingi vilikuwa vimepasuka, baadhi ya madirisha yalikuwa wazi, milango yake mingi ilikuwa imeliwa na mchwa na vitasa vyake baadhi vilikuwa vimeng’olewa. Rangi ya kuta zile ilikuwa imezeeka na ya muda mrefu na sasa ilikuwa imemezwa na uchafu wa mikono. Nilipochunguza katika baadhi ya maeneo nikaona nyufa kubwa zilizosambaa kila mahali kama mizizi ya mti mkubwa uliokula chimvi nyingi.
Hapakuwa na mkazi yeyote katika floo ile hivyo nikaamua kupanda ngazi nyingine za kuelekea ghorofa ya pili na wakati nikifanya vile kwa mbali nikasikia baadhi ya bawaba za milango zikilalamika baada ya baadhi ya milango kupigwa kumbo na mvumo wa upepo. Nikasita kidogo na kuyatega vizuri masikio yangu, bado hakukuwa na dalili zote za uwepo wa binadamu eneo lile hivyo nikaendelea na safari yangu.
Madhari ya ile floo ya pili haikutofautiana sana na yale mandhari ya floo ya kwanza hivyo sikutaka kupoteza muda badala yake nikapanda ngazi zaidi kuelekea ghorofa ya tatu. Mara hii nilikuwa makini zaidi ingawa hisia za kuwa nilikuwa nimedanganywa zilikuwa zimeanza kuchipua taratibu moyoni mwangu.
Mara tu nilipomaliza kupanda ngazi na kuingia kwenye korido ya ghorofa ya tatu nikasimama na kuanza kuchunguza mandhari yale. Yale mandhari hayakutofautiana na yale ya floo ya kwanza na yale ya floo ya pili lakini kulikuwa na vitu vichache vilivyoamsha upya hisia zangu. Milango yote iliyokuwa kwenye ile korido ilikuwa wazi na chakavu isipokuwa mlango mmoja tu uliokuwa umefungwa. Mlango ule ulikuwa wa rangi ya samawati na haukuwa chakavu kama ile milango mingine. Nilipochunguza nikagundua kuwa juu ya mlango ule kulikuwa na uwazi mdogo uliofanywa kwa papi nyembamba za mbao zilizolazwa mshazari ili kuruhusu hewa kupita. Kupitia uwazi ule niliweza kuona mwanga wa taa kutoka mle ndani. Mwanga ule hafifu pia ukaniwezesha kuona sehemu kidogo ya ukuta uliokuwa ukitazama na ule mlango ambao ulikuwa na matundu kadhaa ya risasi.
Hisia zangu zikaniambia kuwa nilikuwa sehemu sahihi hivyo nikaikamata vyema bastola yangu mkononi na kuanza kunyata taratibu kuelekea kwenye ule mlango kwa kuambaa ambaa na ukuta. Hata hivyo kabla sijaufikia ule mlango nikaona kuwa ingekuwa vyema kwanza endepo ningevikagua vile vyumba vingine ambavyo milango yake ilikuwa wazi na mingine imeng’olewa kwa uchakavu. Zoezi lile nikalifanya kwa muda mfupi na nilipomaliza sikuona kitu chochote cha kutilia mashaka hivyo hatimaye nikaufikia ule mlango wenye taa inayowaka kwa ndani. Nilipofika nikajibanza kando na kusikilizia kama kungekuwa na chochote ambacho kingesikika mle ndani. Sikusikia chochote na kabla sijakishika kitasa cha ule mlango nilipochunguza vizuri nikaona kuwa sehemu fulani juu ya ule mlango kulikuwa na matundu mawili makubwa kiasi. Nilipozidi kuchunguza nikagundua kuwa matundu yale yalikuwa ni matundu ya risasi za bunduki hatari ya kudungulia kama Sniper Rifle 338 Lapua Magnum au M18. Mashaka yakaniingia hivyo nikaachana kwanza na kile kitasa na kuchungulia mle ndani kupitia yale matundu. Sikufanikiwa kuona vizuri mle ndani kwa vile kulikuwa na pazia ambalo bila shaka lilikuwa pia limezuia mwanga wa taa ya mle ndani kuweza kupenya kwenye yale matundu moja kwa moja na kuangaza kwenye ile korido.
Hapakuwa na namna hivyo nikashika kile kitasa kwa tahadhari kisha taratibu nikakizungusha kuufungua ule mlango. Moyo wangu ukazidi kuingiwa na mashaka baada ya kugundua kuwa ule mlango ulikuwa haujafungwa. Nikaikamata vyema bastola yangu mkononi kisha taratibu nikausukuma kidogo ule mlango na kuchungulia mle ndani. Sikumuona mtu yeyote lakini uchunguzi wangu pia haukukamilika hivyo nikausukuma zaidi ule mlango ili niingie ndani. Haikuwa rahisi kabla ya kushtukia kuwa kulikuwa na kitu kilichokuwa kikiuzuia ule mlango usifunguke vizuri kwa ndani. Ikabidi niingize kichwa kwa uangalifu kwenye uwazi mdogo baina ya ule mlango na ukuta ili kuchungulia nyuma ya ule mlango. Kwa kufanya vile nikashikwa na mshtuko.
Nyuma ya ule mlango kulikuwa na mwili wa mwanajeshi mmoja uliyeuwawa kwa kupigwa risasi ya kichwa. Ubongo wake ulikuwa umetawanyika hovyo sakafuni katikati ya dimbwi la damu na kichwa chake kilikuwa na tundu kubwa sawa na ukubwa wa risasi hatari iliyotumika kuupora uhai wake. Alikuwa mwanaume mweusi wa haja, jitu la miraba minne na kupitia cheo kilichokuwa kwenye gwanda zake za kijeshi begani na kifuani nikagundua kuwa yule mwanajeshi alikuwa na cheo cha Luteni Kanali Luade Ngouma. Nikausogeza ule mlango vizuri na kuingia mle ndani. Sikupiga hatua yoyote zaidi badala yake taratibu nikayatembeza macho yangu kuyasahili vizuri yale mazingira na nilipoona kuwa hakukuwa na dalili yoyote ya hatari nikainama kidogo na kuibana mishipa ya damu ya yule kamanda shingoni mwake. Majibu yakaniambia kuwa muda usiopungua saa moja iliyopita roho yake ilikuwa imefunga safari kuuacha mwili kwani damu yake ilikuwa mbioni kupoteza joto la uhai.
Hatimaye nikaikamata vyema bastola yangu na kusimama. Sebule ya ile nyumba ilikuwa kubwa iliyozungukwa na makochi ya sofa, sakafuni kulifunikwa zulia jekundu na katikati ya sebule ile palikuwa na meza fupi ya mti wa msobari. Juu ya meza ile kulikuwa na kibakuli kidogo cha dongo cha kuwekea majivu ya sigara kilichojaa majivu na vipisi vya sigara. Kando ya meza ile niliona kreti tatu za bia zilizonywewa tayari na chupa zake kutelekezwa shaghala baghala sakafuni. Juu ya dari ya sebule ile feni la pangaboi lilikuwa likizunguka taratibu na upepo wake haukuwa na madhara yoyote mle ndani. Kulikuwa na dirisha kubwa nyuma ya sebule ile na zaidi ya pale sikuona kitu kingine chochote. Nikazidi kusonga mbele zaidi nikiichunguza vizuri ile sebule na kwa kufanya vile nikaiona miili mingine miwili ya wanajeshi sakafuni.
Mmoja alikuwa Sajenti Jonas Bilindwa, mwili wake ukiwa umelala sakafuni hatua chache kabla ya kuufikia mlango wa kuelekea jikoni. Risasi moja tu ilikuwa imeacha tundu kubwa linalovuja damu kwenye sehemu ya moyo wake kifuani. Alikuwa amelala chali sakafuni kama mtu anayefanya mapenzi huku mdomo na macho yake vikiwa wazi. Yule mwanajeshi mwingine alikuwa na cheo cha Meja mwenye jina la Pasteur Kazarama, mkononi alikuwa ameshika bastola ambayo haikumsaidia kitu kwani risasi mbili hatari zilikuwa zimeuvunja vibaya uti wake wa mgongo huku zikiacha majeraha yaliyofumuka vibaya kifuani kwake. Mwili wake ulikuwa umeangukia pembeni ya kochi na nilipomchunguza nikagundua kuwa ni kama alikuwa kwenye harakati za kuongea jambo fulani wakati risasi zile zilipomfuania.
Bastola yangu ikiwa mkononi nikasimama kwa tahadhari nikiitazama ile miili kwa utulivu huku nikishindwa kuelewa ni nani aliyetekeleza mauaji yale na sababu gani iliyomlekea afanye vile. Kulikuwa na kila dalili kuwa kulikuwa na kikao kizito kilichofanyika mle ndani kabla ya lile timbwili kutokea. Taratibu nikaanza kupiga hatua zangu kuelekea vyumbani kufanya ukaguzi wa kina zaidi. Vyumba vyote vilikuwa wazi na hapakuwa na dalili zozote kuwa vyumba vile vilikuwa vikitumika na hapo nikahisi kuwa huwenda ile nyumba ilikuwa imeandaliwa haraka kwa ajili ya kufanikisha vikao vya haraka vya mapinduzi ya kijeshi nchini Burundi. Akina nani walikuwa wahusika wakuu wa kikao kile?...ITAENDELEA
 
RIWAYA: UFUKWE WA MADAGASCAR
SEHEMU: 58

...damu kwenye sehemu ya moyo wake kifuani. Alikuwa amelala chali sakafuni kama mtu anayefanya mapenzi huku mdomo na macho yake vikiwa wazi. Yule mwanajeshi mwingine alikuwa na cheo cha Meja mwenye jina la Pasteur Kazarama, mkononi alikuwa ameshika bastola ambayo haikumsaidia kitu kwani risasi mbili hatari zilikuwa zimeuvunja vibaya uti wake wa mgongo huku zikiacha majeraha yaliyofumuka vibaya kifuani kwake. Mwili wake ulikuwa umeangukia pembeni ya kochi na nilipomchunguza nikagundua kuwa ni kama alikuwa kwenye harakati za kuongea jambo fulani wakati risasi zile zilipomfuania.
Bastola yangu ikiwa mkononi nikasimama kwa tahadhari nikiitazama ile miili kwa utulivu huku nikishindwa kuelewa ni nani aliyetekeleza mauaji yale na sababu gani iliyomlekea afanye vile. Kulikuwa na kila dalili kuwa kulikuwa na kikao kizito kilichofanyika mle ndani kabla ya lile timbwili kutokea. Taratibu nikaanza kupiga hatua zangu kuelekea vyumbani kufanya ukaguzi wa kina zaidi. Vyumba vyote vilikuwa wazi na hapakuwa na dalili zozote kuwa vyumba vile vilikuwa vikitumika na hapo nikahisi kuwa huwenda ile nyumba ilikuwa imeandaliwa haraka kwa ajili ya kufanikisha vikao vya haraka vya mapinduzi ya kijeshi nchini Burundi. Akina nani walikuwa wahusika wakuu wa kikao kile?. Nikajiuliza bila kupata majibu.
Baada ya kumaliza ziara yangu makini ya ukaguzi vyumbani, stoo na sehemu ya bafu na maliwato hatimaye nikahitimisha ukaguzi wangu kwenye chumba cha jiko cha ile nyumba. Hakukuwa na dalili zozote kuwa chumba kile kiliwahi kutumika kwa shughuli zozote za mapishi kwa siku za hivi karibuni kwani hapakuwa na kitu chochote mle ndani zaidi ya makabati chakavu ya kuhifadhia vyombo ukutani yalikuwa wazi bila kitu chochote ndani yake. Masinki mabovu ya kuoshea vyombo na mabomba yasiyotoa maji baada ya koki zake kung’olewa. Kulikuwa pia na utandu mkubwa wa buibui kwenye dari ya kile chumba mbali na vumbi jingi lililotanda kila kona. Kwa msaada wa mwanga wa kurunzi yangu mkononi nikajiridhisha kuwa kusingekuwa na ziada nyingine katika chumba kile cha jikoni. Hata hivyo wakati nilipokuwa katika harakati za kutaka kutoka kwenye kile chumba cha jiko nikahitimisha kwa kumulika sakafuni.
Macho yangu yakajikuta yakivutiwa na lundo la majivu lililokuwa kando ya mlango wa kuingilia mle ndani hivyo taratibu nikainama na kumulika sehemu ile. Yalikuwa majivu mengi yaliyotokana na kuchomwa kwa karatasi nyingi. Kwa msaada wa mwanga mkali wa kurunzi yangu mkononi nikamulika kwa karibu kuyachunguza yale majivu huku nikipeleleza kama ningeweza kupata kitu chochote cha kunisaidia. Zile karatasi zilikuwa zimeungua zote hata hivyo kwa kuwa majivu yake yalikuwa hayajachanguliwa wino mweusi juu ya jivu jeupe la karatasi zile uliweza kusomeka kwa shida kidogo.
Yalikuwa maelezo yaliyohusu uratibu wote wa mkakati wa jaribio la mapinduzi ya kijeshi yaliyofanyika nchini Burundi. Kupitia maelezo yale yaliyosomeka kwa shida nikaona baadhi ya vipaumbele vya mapinduzi yale vilivyoainishwa kama hatua ya awali kabisa ya utekelezaji wa mapinduzi hayo. Vipaumbele hivyo vikiwa ni pamoja na wanajeshi waasi kuelekezwa kuteka na kuyaweka kizuizini maeneo nyeti ya nchi kama kituo cha kurushia matangazo cha idhaa ya redio ya taifa ya Burundi, kiwanja cha ndege na kuzuia ndege yoyote kuingia na kutoka, vituo vyote vya kurushia matangazo ya redio na runinga. Vituo vya kuzalisha umeme vya gridi ya taifa, kufunga mipaka ya nchi na barabara zote muhimu za kuingia na kutoka nchini Burundi na kisha kuwakamata watu wete hususani viongozi wa jeshi watakaoonekana kupinga mapinduzi yale.
Maelezo ya chini hayakusomeka vizuri kwani baadhi ya yale majivu yalikuwa yamehama kufuatia upepo uliokuwa ukivuma mle ndani kupitia madirishani. Hata hivyo kwa shida niliweza kuyasoma na kuyaelewa vizuri maelezo yake. Yalikuwa ni maelezo yanayoainisha vizuri ni kwa namna gani kila eneo la kimkakati lililotajwa kwenye karatasi lingewekwa kizuizini kwa haraka katika kufanyika mapinduzi yale. Yale majivu ya zile karatasi za chini maandishi yake hayakuweza kusomeka asilani kwa vile yalikuwa yametawanywa hovyo na upepo. Nilitamani sana kujua kilichokuwa kimeandikwa kwenye karatasi zile lakini nafasi ile sikuipata kwani majivu ya chini yalikuwa yamechanganyikana hovyo. Hatimaye nikazima kurunzi na kusimama huku nikilaani hali ile hata hivyo kabla ya kuondoka mle ndani nikatibua yale majivu kwa buti langu mguuni kuangalia kama kungekuwa na chochote kilichofichika, Sukiuona chochote.
Sikuwa nimepata chochote cha kunisaidia na hapo nikajihisi mgonjwa wa hisia. Hatimaye nikaikamata vyema bastola yangu mkononi na kurudi kule sebuleni. Nilipofika nikasimama katikati ya ile sebule nikitafakari huku mikono nimeiweka kiunoni. Nikayatembeza tena macho yangu kuitazama ile miili ya wale wanajeshi waliouwawa mle ndani na kwa kufanya vile wazo jipya likanijia kichwani. Nilianza kuhisi kuwa mtu yeyote aliyehusika na mauaji yale alipaswa kuwa ni mtu asiyekuwa na unasaba wowote na wale watu waliokuwa mle ndani wakiendelea na kikao kwani vinginevyo kama vile vingekuwa vimetokana na kutokuwa na maelewano baina ya wale watu waliokuwa mle ndani basi ni dhahiri kuwa idadi ya vifo mle ndani ingestahili kuwa kubwa zaidi. Lakini vilevile kulipaswa kuwa na dalili za majibishano ya risasi baina ya pande pinzani katika mgogolo ulioibuka kwenye kikao kile. Hivyo pale sebuleni palitakiwa kuonekana maganda kadhaa ya risasi sakafuni pamoja na matundu ya risasi katika baadhi ya maeneo. Hatimaye nikahitimisha kuwa muuaji alikuwa ni mtu aliyekuwa nje na eneo lile lakini akifahamu kila kitu kilichokuwa kikiendelea mle ndani katika mkutano ule wa siri. Lazima kulikuwa na mtu mwingine ambaye angefaa kuitwa msaliti au mtu wa kutoka upande tiifu wa serikali iliyokuwa madarakani ya Rais Pierre Nkurunziza. Labda mtu au watu kutoka kikosi maalum cha ulinzi wa rais au kutoka kada ya intelijensia na usalama wa nchi ya Burundi. Nikameza funda kubwa la mate na kuikamata vyema bastola yangu mkononi. Shuguli bado ilikuwa mbichi kabisa huku shauku ya kutaka kumjua mtu aliyehusika na mauaji yale ikizidi kunawiri moyoni.
Taswira ya Amanda ilikuja na kutoweka haraka katika mboni za macho yangu na kuichemsha hasira mbaya kifuani mwangu. Amanda alikuwa miongoni mwa wajumbe muhimu wa mkakati wa mapinduzi yale ya kijeshi. Kwa tafsiri nyingine ni kuwa Amanda alikuwa akifahamu kila kitu kilichokuwa kikiendelea na hivyo sasa nilianza kuona umuhimu wa kumsaka popote alipo kwa udi na uvumba. Sasa nikawa nafikiria kutoka nje ya ile nyumba na kuingia mitaani kumsaka Amanda. Lakini kabla sijafanya vile nikashtushwa na mlio wa simu ya mkononi iliyoanza kuita mle ndani. Moyo wangu ukapiga kite kwa nguvu ya mshtuko na hapo nikageuka na kuyatembeza macho yangu mle ndani. Ule mlio wa simu ukasikika kutoka katika mfuko wa suruali wa yule mwanajeshi aliyeuwawa nyuma ya mlango wa kuingilia mle ndani akifahamika kama Luteni Kanali Luade Nguoma. Nilikuwa karibu na ule mwili wa yule mwanajeshi hivyo haraka nikainama ili kuichukua ile simu kutoka kwenye mfuko wa suruali wa yule kamanda.
Loh! hadi leo nalikumbuka vizuri tukio lile, ilikuwa ni simu muhimu sana katika kipindi chote cha maisha yangu ukiachilia mbali ile simu ya mchumba wangu wakati aliponipigia siku ya kwanza kuniambia kuwa alikuwa amekubali ombi langu la kumtaka tuwe wapenzi baada ya kupigwa dana dana kwa muda mrefu wakati nikiwa mwanafunzi wa sekondari kabla ya kupoteana kwenye harakati za maisha.
Hofu ya kifo ilikuwa imeniingia haraka na kusambaa mwili kama maumivu ya sindano ya sumu. Nywele zikanicheza kichwani kisha kijasho chepesi kikaanza ziara fupi maungoni mwangu. Sauti mbaya ya mpasuko mkubwa wa kioo cha dirishani nyuma ya ile sebule ilikuwa ni ishara muhimu kuwa bado nilikuwa hai nikipumua vizuri bila kulipia hata senti tano ya pumzi yangu. Kitendo kile cha kuinama ili niichukue ile simu kilikuwa kimeniokoa mbali na risasi hatari ya mdunguaji iliyonipunyua kidogo kisogoni na kuacha tundu kubwa mlangoni huku ile rasasi ikitokezea upande wa pili na kuacha tundu ukutani.
Nikawahi kujitupa chini kando ua ule mwili wa yule mwanajeshi huku bado nikiwa siamini macho yangu. Risasi ya pili ikatua kando ya goti langu na kuchimba sakafu ya ile sebule baada ya sauti nyingine mbaya ya mpasuko wa kioo cha dirisha kubwa la nyuma ya ile sebule husika. Zilikuwa risasi za mdunguaji ambaye sikuwa na shaka yoyote kuwa kwa muda mrefu alikuwa akinitazama mle ndani kupitia lile dirisha kubwa la ile sebule.
Loh! risasi nyingine ya tatu ikanipunyua begani na hapo nikaanza kuona kasi hatari ile kunikaribia hivyo nikawahi kujitupa kando ya eneo lile na kujiviringisha sakafuni hadi kwenye pembe ya kochi moja lililokuwa jirani na eneo lile nikitafuta sehemu ya kujikinga dhidi ya risasi za yule mdunguaji kisha nikaikamata vyema bastola yangu mkononi. Risasi moja yenye shabaha makini ikaichangua na kuisambaratisha vibaya taa ya pale sebuleni na hapo giza zito likachukua nafasi yake mle ndani.
Ile simu ilikuwa bado ikiendelea kuita hivyo haraka nikajiviringisha sakafuni hadi kwenye mwili wa yule mwanajeshi ambapo nilimpekua haraka mifukoni na kufanikiwa kuipata ile simu iliyokuwa ikiita. Namba ya simu iliyokuwa ikiita kwenye ile simu ya mkononi ilikuwa ni Private number na tuki lile likavuta sana hisia zangu hata hivyo nikabofya kitufe cha kupokelea pasipo kuzungumza neno lolote na hapo sauti ya kike ikasika huku mzungumzaji akionekana kuwa na haraka na wasiwasi mwingi katika mazungumzo yake.
“Mambo siyo shwari, saa nane kamili usiku huu, Jardin Public!”
Ilikuwa sauti ya kike yenye kitetemeshi na hakika lakini haikuwa halisi. Mzungumzaji upande wa pili nikahisi alikuwa ameweka kitambaa cha leso kwenye receiver ya simu akinuia kuificha sauti yake halisi kusikika vizuri, kisha ile simu upande wa pili ikakata.
Jasho jepesi lilikuwa likinitoka puani, moyo wangu ilikuwa umepoteza utulivu kabisa. Sikuwa na muda wa kutafakari zaidi hivyo nikaizima ile simu na kuitia kwenye mfuko wa koti langu la kazi. Kwa kweli pamoja na utundu wangu wote nilikuwa nimeshindwa kabisa kuitambua sauti ile. Nilipomfikiria Amanda nikajikuta nikimeza funda kubwa la mate kuupoza mtima wangu.
Mawazo juu ya yule mdunguaji aliyetoka kunichachafya mle ndani muda mfupi uliopita yakanijia haraka akilini kama maumivu makali yasambaavyo mwilini baada ya unyayo peku wa mguu kukanyaga kiwembe mchangani. Kwa tahadhari nikasimama na kunyata nikikatisha katikati ya ile sebule kuelekea dirisha huku bastola yangu ikiwa mkononi. Nilipofika nikajibanza pembeni ya lile dirisha na kutazama kule nje ya lile dirisha risasi zile za mdunguaji zilipokuwa zikitokea.
Upande wa pili wa lile jengo baada ya kulipita eneo la maegesho ya magari ya magari nyuma ya lile jengo kulikuwa na majengo mengine ya ghorofa yalioongozana katika mstari mnyoofu. Katika mlolongo ule wa majengo ya ghorofa kulikuwa na jengo moja la ghorofa lililokuwa likitazamana na lile jengo la ghorofa nililokuwa. Vyumba vyote katika lile jengo vilikuwa gizani ingawa taa za nje zilikuwa zikiwaka. Nikayatuliza vyema macho yangu kuchunguza vizuri vyumba vya lile jengo na kwa kufanya vile nikagundua kuwa kulikuwa na chumba kimoja ambacho dirisha lake lilikuwa wazi. Macho yangu yakazidi kuvutika kwa ukaribu zaidi na kuweka kituo nikikichunguza vizuri kile chumba kupitia lile dirisha wazi. Kwa sekunde kadhaa moyo wangu ukasimama. Kivuli cha mtu aliyevaa kofia ya pama kikatulia vyema katikati ya mboni ya macho yangu........ITAENDELEA
 
RIWAYA: UFUKWE WA MADAGASCAR
SEHEMU: 59

Niliendelea kumtazama yule mtu pale dirishani na kwa kufanya vile nikagundua kuwa hata yeye alikuwa makini sana kutazama sebule ya ile nyumba niliyokuwa, pengine alikuwa akijiuliza nini kilichokuwa kimetokea hadi kupelekea taa ya mle ndani kuzimika. Alikuwa mdunguaji, sikuwa na shaka yoyote kuwa alikuwa ni yeye na mara moja nilipoyakumbuka yale matundu ya risasi juu ya mlango wa ile sebule wakati nilipokuwa nikiingia mle ndani nikahitimisha kuwa ile ilikuwa kazi yake. Risasi zake chakaramu zilikuwa zimefanikiwa kuilaza miili ya wanajeshi watatu mle ndani na sasa alikuwa katika harakati za kufunga hesabu zake na mimi.
Tusi zito likaniponyoka mdomoni kisha kwa tahadhari nikaayacha maficho yale nikinyata taratibu kuelekea kwenye ule mlango wa kutokea nje ya ile sebule. Kurunzi yangu nikaitia mfukoni huku bastola yangu nikiwa nimeikamata vyema mkonboni. Nikiwa na hakika kuwa mdunguaji alikuwa makini sana kuchunguza mjongeo wowote mle ndani. Sikutaka kumpa nafasi ile hivyo hatua zangu makini zikawa zikielea juujuu kama mnajimu Neil Armstrong mwezini. Nilipoufikia ule mlango nikaufungua taratibu na kutoka nje.
Muda mfupi baadaye nilikuwa chini ya lile jengo la ghorofa. Nilipofika chini nikasimama kwenye kiunga kimoja cha maua nikichunguza kama kungekuwa na mtu yeyote eneo lile. Sikumuona mtu yeyote hivyo nikaikamata vyema bastola yangu mkononi na kukatisha eneo lile kwa tahadhari nikielekea kwenye lile jengo la ghorofa alikuwa yule mdunguaji. Mvua ilikuwa ikinyesha na hali ile ilinipa faraja kwa vile kelele za mjongeo wangu zingeweza kumezwa na kelele za mvua ile. Macho yangu yalikuwa makini na milango yangu ya fahamu isingemruhusu adui kunifikia kabla sijamtia risasi.
Mbele ya lile jengo nilipofika nikaanza kupanda ngazi kwa tahadhari kuelekea floo ya tatu huku akili yangu ikisumbuka katika kutaka kufahamu mdunguaji angekuwa akiwaza nini juu yangu. Lile jengo lilikuwa likitumika kwani kuta na floo yake vilikuwa safi, milango yake ilikuwa imefungwa na madirisha yake yalikuwa na vioo timilifu. Hata hivyo hapakuwa na dalili zozote kuwa wakazi wa lile jengo walikuwa mle ndani kwa wakati ule. Hofu ya nchi kuingia kwenye machafuko makubwa ya kisiasa yenye kupelekea umwagaji mkubwa wa damu ilikuwa imewafurusha raia wengi wa Burundi kukimbilia nchi za jirani kusalimisha maisha yao hivyo lile jengo lilikuwa limeachwa ukiwa.
Hatimaye nikafika floo ya tatu ya lile jengo na hapo kwa tahadhari nikaanza kutembea kwenye ile korido nikiichunguza milango iliyokuwa ikitazamana na ile korido. Milango yote ilikuwa imefungwa na hapakuwa na dalili za uwepo wa kiumbe hai chochote katika zile nyumba. Safari ya hatua zangu hatimaye ikatia nanga kwenye mlango wa nyumba namba 101 upande wa kushoto wa floo ya tatu ya lile jengo. Sasa nikawa nikiutazama ule mlango kama mlango wa mwisho wa kuingia kuzimu. Macho yangu yakawa ni kama yanayomuona mdunguaji mle ndani huku akiwa ameutega vyema mtutu wa bunduki yake hatari katika upenyo wa dirisha moja la kioo lililofunguliwa na kuachwa wazi katika pembe ya nyuzi arobaini na tano. Jicho lake moja likiwa katika lenzi kali ya darubini maalum ya kutazamia windo lake. Sikuwa na shaka yoyote kuwa mdunguaji yule alikuwa bado hajaondoka mle ndani kwa vile hapakuwa na sababu ya haraka ya kumpelekea afanye vile.
Kwa tahadhari nikakishika kitasa cha ule mlango na kukizungusha, mrejesho ukanitanabaisha kuwa ule mlango ulikuwa umefungwa. Mdunguaji alikuwa ameufunga kwa ndani kama mkakati wa kujihakikishia usalama wake na vilevile kuifanya kazi yake kwa utulivu zaidi. Nikainama na kuchungulia mle ndani kupitia tundu la kile kitasa, sikuona kitu chochote kwa vile mle ndani kulikuwa na giza. Hivyo nikachukua funguo zangu malaya kutoka katika mfuko wa koti langu na kuzipachika kwenye lile tundu la kitasa. Sikutaka zile funguo zisababishe rabsha yoyote ambayo ingemshutua mdunguaji hivyo nilikiwa makini sana. Funguo ya pili tu kile kitasa kikatoa majibu hivyo nikausukuma ule mlango taratibu na kuzama mle ndani huku bastola yangu ikiwa mkononi tayari kumkemea msumbufu yeyote kisha ule mlango nikaurudishia taratibu nyuma yangu.
Mara baada ya kuingia mle ndani sikupiga hatua yoyote badala yake nikasimama huku nikiyastadi vizuri mazingira yale na kwa kufanya vile nikagundua kuwa ramani ya ile nyumba haikuwa tofauti na ramani ya ile nyumba niliyotoka upande wa pili wa lile jengo muda mfupi uliopita. Nikaitazama ile sebule kwa makini hata hivyo sikumuona mtu yeyote mahali pale hivyo nikaamua kushika uelekea wa upande wa kushoto nikiifuata korido inayotazamana na milango mitatu. Mlango wa chumba cha kwanza ulikuwa wazi na mle ndani nilipochungulia sikuona kitu chochote wala mtu yeyote. Chumba cha pili kilitumika kama bafu na sehemu ya maliwato, mlango wake nao ulikuwa wazi na hapakuwa na mtu yeyote ndani yake. Chumba cha tatu nilipochungulia katika uwazi mdogo baina ya bawaba na mlango. Mdunguaji alikuwa mle ndani ametulia juu ya stuli ndefu dirishani, bunduki yake hatari ya kupokonya roho za watu aina ya M24 SWS ikiwa imetuama vyema kwenye ukingo wa dirisha juu ya kitako maalum cha miguu miwili kama Twiga anayekunywa maji mtoni.
Yule mdunguaji alikuwa makini kutazama kwenye ile sebule ya upande wa pili wa lile jengo, kichwani alikuwa amevaa kofia ya pama. Alikuwa mwanaume mrefu na mwenye mwili ulioshiba misuli. Sehemu nyingine ya mwili wake sikuweza kuiona vizuri kwa vile alikuwa amevaa koti kubwa la kujikinga na baridi na mvua ya usiku ule.
Mlango wa kile chumba cha mdunguaji ulikuwa umefunguliwa kidogo na kuachwa wazi hata hivyo uwazi ule usingeniruhusu kuingia mle ndani pasipo kuufungua zaidi ule mlango. Sikuwa na shaka yoyote kuwa mdunguaji hakuwa na taarifa yoyote juu ya ile ziara yangu ya kushtukiza mle ndani. Hivyo ni dhahiri kuwa maandalizi yake ya kujihami yalikuwa hafifu na hapo nikajishauri nimshindilie risasi kwanza halafu mahojiano baadaye au nimkabili mzima mzima. Hata hivyo uamuzi wowote ambao ningeuchukua ulikuwa na walakini kwani endapo ningemshindilia risasi upo uwezekano kuwa angeweza kupoteza maisha kabla ya lengo langu halijafanikiwa na endapo ningeamua kumkabili upo uwezekano kuwa hakuwa peke yake eneo lile hivyo kukuru kakara zingeweza kuwavuta wenzake eneo lile na hapo shughuli ingekuwa kubwa.
Baada ya kujishauri sana nikaona kuwa ingekuwa vyema endapo ningetumia mitindo yote mwili yaani kumkabili ana kwa ana na kumtia risasi. Hivyo nikakishika kitasa cha ule mlango na kuusukuma ndani taratibu na hapo ndipo nilipofanya makosa bila kutarajia kwani bawaba za ule mlango zilikuwa kavu mno hivyo wakati nikiusukuma ule mlango taratibu ili niingie mle ndani zile bawaba za ule mlango zikapiga kelele na hivyo kumshtua yule mdunguaji. Mdunguaji akaondoa haraka jicho lake kwenye lenzi ya darubini pandikizi juu ya ile bunduki na kugeuka nyuma haraka akitazama pale mlangoni. Alikuwa mwepesi sana kuishtukia hila yangu, kisu cha kwanza alichokitupa nikawahi kuinama hivyo kikakata upepo na kwenda kukita ukutani. Kisu cha pili nikawahi kukizuia kwa ule mlango hivyo kikakita mlangoni na kunasa.
Nilimuona yule mdunguaji akisogeza koti lake kiunoni ili achomoe bastola yake, sikumruhusu atimize adhma yake, nikampunguza kasi kwa kumchapa risasi ya bega hivyo mkono wake haukuifikia ile bastola badala yake akapiga yowe kali la maumivu na hapo akasimama haraka na kuibetua ile stuli ndefu aliyoikalia kwa mguu wake akinitupia pale nilipokuwa. Kuona vile nikaruka hewani na kuirudisha ile stuli ilipotokea kwa pigo moja maridadi la teke la angani. Mdunguaji akawahi kuliona pigo lile na kuinama hivyo ile stuli ikajipiza dirishani na kusambaratisha vioo vya lile dirisha. Nilipokuwa katika harakati za kutaka kumchapa risasi nyingine, akawahi kujitupa hewani katika mtindo ambao kwa kweli ulinishangaza sana. Nikajipanga nimzuie lakini namna ya alivyokuwa akijizungusha akanizuga na kunipotezea umakini juu ya wapi pa kuanzia mashambulizi yangu. Mara moja akawa amenifikia na kunichapa mapigo mawili ya kungu-fu kifuani yaliyonipelekea nijisikie kutaka kutapika na hatimaye akanichapa na teke la kichwa nililojaribu kulizuia bila mafanikio. Pigo lile hatari likanitia kizunguzungu na hapo nikapepesuka huku nikirudi kinyumenyume kama bondia aliyepigwa sumbwi zito la kichwa lililomlevya na hatimaye bastola yangu ikaniponyoka mkononi.
Mdunguaji akazidi kunifuata akinichanganyia mapigo tofauti ya kung-fu ambayo nilijitahidi kuyapangua kama mzaha na hivyo hakuna pigo lililonifikia. Hatimaye nikajitupa kando kisha haraka nikatembea hewani kwenye pembe za kile chumba kutafuta nguvu ya pigo la miguu. Mdunguaji akawa akizunguka kunivizia bila mafanikio na kabla hajabadili mbinu teke langu makini likatia nanga kifuani mwake na kukita vibaya, likamtupa nyuma huku akipiga chafya kama aliyenusa ugolo. Hatimaye yule mdunguaji akapiga mwereka hadi chini na sikutaka kumpa nafasi ya kuzidi kunisumbua hivyo haraka nikamfikia pale chini na kumzaba teke la tumbo. Lakini alikuwa mwerevu dhidi ya mbinu yangu ile hivyo akawahi kunikwepa kwa kujiviringisha kando hivyo pigo langu likakata upepo bila mafanikio na kabla sijaushusha chini mguu wangu nikashtukia nikichotwa matama hatari wa ufundi wa hali ya juu. Nikarushwa hewani kama furushi lakini nilipotua chini nikatua kama paka bila athari zozote kisha nikajibetua na kumkabili yule mdunguaji. Pigo lake la ngumi ya uso nikalipangua kwa wepesi kisha nikamchapa pigo moja la shingo na ingawa alijitahidi kulipangua lakini lilimpata na kumlevya vibaya hivyo akarudi kinyumenyume huku akipiga yowe kali. Kuona vile nikamzaba mateke mawili ya chapchap, teke la kwanza akalipangua hata hivyo lililofuatia hakuweza kulihimili hivyo likamtupa hadi kwenye mlango wa kile chumba. Akauangukia ule mlango na hapo ule mlango ukavunjika vipande vipande na kutawanyika kila mbao sehemu yake. Nilimuona akigaagaa pale chini kufuatia maumivu makali mwilini mwake hata hivyo aliwahi kusimama kabla sijamfikia na hapo akapangua vipande vya mbao za ule mlango na kusimama kama mjeruhi wa mbogo akijipanga upya kisha akaanza kunifuata kwa ghadhabu ili kunikabili. Kwa kweli yule mdunguaji alikuwa mpiganaji nunda asiyekolea kipigo kwa urahisi. Wakati akinijia kwa kasi nikajipanga kumkwepa lakini alikuwa makini akafanikiwa kunichapa kofi zito la uso lililoniduwaza na kunipelekea nione maluweluwe mbele yangu na hapo nikawa nikizunguka mle ndani huku na kule kumkwepa.
Hatimaye akanifikiwa kiulaini na kunitandika teke la mgongo na maumivu yake yakanipelekea nigune kama mchawi aliyefumaniwa. Kwa kuwa nilikuwa sioni vizuri mbele yangu nikatupa mapigo kadhaa yaliyokosa shabaha na mwishowe nikajikuta nimeenea vizuri kwenye kabali ya mtukutu yule.
Sasa kukawa patashika ya aina yake mle ndani, yule mdunguaji alikuwa akizidi kunikaba kwa mkono wake mgumu kama mbao ya mpingo nyuma yangu. Kwa kweli alikuwa na nguvu zisizoelezeka, macho yakanitoka kwa hofu huku mishipa ya shingo imenituna kama mizizi ya mti ardhini. Sasa tukaanza kukokotana huku na kule mle ndani nikitafuta namna ya kujinasua kwenye kabali ile ya kifo bila mafanikio. Hatimaye nikaufikia ukuta mmoja wa kile chumba ambapo niliikita miguu yangu kwenye ule ukuta kisha kwa nguvu zangu zote nikajisukuma nyuma na hapo wote tukajibwaga chini kama mizigo, nikawahi kuinuka na kumpiga yule mmdunguaji kiwiko cha mbavu. Nikasikia mvunjiko wa mbavu na hapo yule mdunguaji akapiga yowe kali la maumivu. Nikawahi kujiviringisha kando kisha nikasimama, mdunguaji naye kuona vile akawahi kusimama huku amejipinda kidogo na kujishika mbavuni maumivu makali yakionekana kumtafuna. Sikumchelewesha nikawahi kujitupa karibu naye na kumchapa teke la tumbo lililomtupa dirishani. Nilipomtazama yule mdunguaji nikagundua kuwa tayari alikuwa amelainika, nikawahi kumfikia, akajaribu kutupa ngumi lakini niliwahi kuudaka mkono wake kisha kwa pigo maridhawa nikaupigiza kwenye kingo moja ya dirisha na hapo nikasikia sauti nyingine ya mvunjiko wa kitu kama kijiti kikavu. Mkono wake ukavunjika na hapo mdunguaji akaangua kilio kama mtoto mdogo. Nikamkwida na kumzoa kisha nikamuweka pale dirishani, kiwiliwili chake kikawa nusu kinaning’inia nje ya lile dirisha na nusu nyingine ndani ya kile chumba kisha mahojiano yakaanza.
“Wewe ni nani?”. Nikamuuliza huku nikimtishia kumsukuma chini ya lile jengo kupitia pale dirishani.
“Nakuomba tafadhali usiniue…”. Mdunguaji akalalama kwa hofu.
“Wewe ni nani?”. Nikamuuliza tena.
“Kwanini unataka kunifahamu?”. Yule mdunguaji akaniuliza huku hali yake ikizidi kuwa mbaya na hapo nikatishia tena kumsukuma.
“Niache tafadhali nitakueleza”. Mdunguaji akanisihi.
“Haya niambie wewe ni nani?”
“Meja Denise wa jeshi la wananchi wa Burundi”
“Unafanya nini hapa?”. Swali langu likampelekea yule mtu abaki kimya kama ambaye hajanisikia vizuri. Hatimaye akavunja ukimya.
“Kazi yangu ni mwanausalama hivyo nipo hapa kutekekeleza majukumu yangu”
“Majukumu gani?”
“Kuhakikisha usalama wa nchi yangu. Wewe ni nani?”. Yule mdunguaji akaniuliza na hapo nikamtazama kwa uyakinifu kabla ya kuvunja ukimya.
“Namtafuta balozi Adam Mwambapa”. Nikamwambia kwa utulivu na hapo nikauona mshtuko mkubwa machoni mwake.
“Balozi wa Tanzania…?”. Yule mtu akaniuliza kwa mshtuko.
“Ninaweza kumpata wapi?”. Nikamuuliza mdunguaji kwa udadisi. Yule mdunguaji akanitazama kwa utulivu kisha nikamuona akitikisa kichwa taratibu kukata na hatimaye akaniambia.
“Sifahamu alipo”. Macho ya mdunguaji yalikuwa yakizungumza ukweli, taarifa zile zilionekana kuwa ngeni kabisa masikioni mwake. Ukimya kidogo ukapita wakati nikifikiria nini cha kufanya. Hatimaye sikuona sababu kumuangamiza mwanausalama yule hivyo nikamvuta na kumrudisha mle ndani huku nikimpigapiga kifuani kumtia moyo. Alikuwa hoi hajiwezi lakini kitendo cha kumrudisha mle ndani kikampa faraja ya uzima.
“Hutaweza kukaa hapa kwa muda mrefu kabla ya kifo hakijakuotea. Jiokoe mwenyewe kamanda”. Nikamwambia Meja Denise huku nikimuegemeza vizuri ukutani kisha nikaiokota bastola yangu na kuishika mkononi.
“Usiku mwema komredi”. Nikamwambia Meja Denise kisha taratibu nikaanza kuzitupa hatua zangu kutoka nje ya kile chumba.
_____

Jardin public au bustani ya umma ilikuwa katikati ya jiji la Bujumbura. Kupitia ramani yangu ndogo ya kijasusi sikusumbuka sana kuivumbua sehemu ile. Maongezi ya mwisho kwenye simu ya mkononi ya Luteni Kanali Luade Ngouma wakati nikiwa kwenye ile nyumba namba 42 nilipoikuta ile miili ya wanajeshi watatu yalikuwa yamenipelekea nifike mapema sehemu ile. Mvua kubwa iliyokuwa ikiendelea kunyesha sasa ilikuwa imepungua na sehemu yake kuchukuliwa na upepo wa hapa na pale.
Wakati nilipoitupia macho saa yangu ya mkononi nikagundua kuwa dakika ishirini zilikuwa zimesalia kabla ya kutimia saa nane usiku, muda ambao mzungumzaji katika ile simu ya mkononi alikuwa amemtaka Luteni Kanali Luade Ngouma kuwa waonane mahali pale.
Sauti ya mzungumzaji yule kwenye simu sasa ilikuwa ikinijia akilini na hivyo kuibua maswali chungumzima. Mtu yule alikuwa nani na kwanini alitaka kuonana na Luteni Kanali Luade Ngouma usiku wa manane kama ule?. Nikakumbuka pia mzungumzaji alisema kuwa “Mambo siyo shwari…” na hapo nikajiuliza kuwa ni mambo gani hayo yasiyokuwa shwari?. Majibu sikupata hivyo nikaendelea kujipa subira na kwa vile bado nilikuwa ndani ya muda kulikuwa na muda mzuri wa kujipanga.
Mandhari ya Jardin Public yalikuwa yametawaliwa na hisia za hofu. Ingawa eneo lile lilionekana kuwa na tija sana hasa kwa nyakati za mchana watu wakilitumia kujipumzisha dhidi ya jua kali huku biashara ndogondogo zikiendelea. Lakini usiku huu bustani ile ilionekana kama kichaka hatari ambacho kingeweza kutumika na maharamia katika kupanga mipango yao ya uvunjifu wa amani.
Bustani ile ilipambwa kwa miti mizuri ya kivuli na maua aina ya bougavillea. Chini ya miti ile ya kivuli kulikuwa na viti maalum vya zege, mahali ambapo watu wangeketi na kujipumzisha nyakati za mchana wakisubiri machweo ya jua ili waendelea na shughuli zao na hatimaye kuelekea majumbani mwao. Miti ile sasa ilikuwa mikubwa sana na hivyo kutengeneza kipande cha msitu katikati ya jiji la Bujumbura.
Barabara ya Avenue Pierre Ngendandumwe ilikuwa imenifikisha katika bustani ile iliyozungukwa na barabara za lami pande zote. Sikumuona mtu yeyote wala gari lililoegeshwa eneo lile. Eneo lote la ile bustani lilikuwa kimya bila kiashiria chochote cha uhai. Barabara za mtaa mingi ya jiji la Bujumbura usiku ule zilikuwa tulivu kama mtuhumiwa wa kesi ya mauaji anayesubiri hukumu ya mwisho kwenye kizimba cha mahakama.
Baada ya kuhakikisha kuwa hakuna mtu yeyote aliyekuwa akinifuatilia nikavuka barabara na kupotelea ndani ya bustani ile kisha nikafanya uchunguzi wa kina kwenye ile bustani ili kupeleleza kama kungekuwa na mtu yeyote aliyejificha kwa hila eneo lile. Hapakuwa na mtu yeyote hivyo hatimaye nikatafuta kiti kimoja cha zege na kuketi halafu baada ya kufikiria kidogo nikaona kuwa ingekuwa vyema kuiandaa kabisa bastola yangu. Hivyo nikaondoa magazini kwenye ile bastola na kuichungulia. Loh! ile magazini ilikuwa imesaliwa na risasi moja tu hivyo nikaitupa kando na kupachika magazini nyingine iliyojaa risasi.
Nilipoitazama tena saa yangu ya mkononi nikagundua kuwa zilikuwa zimesalia dakika tano kabla ya kutimia saa nane usiku, muda wa miadi na hapo nikasimama na kuanza kutembeza macho yangu huku na kule.
Haikuwa hadi ilipotimia saa nane kamili usiku mara ile simu kwenye mfuko wa koti langu ikaanza kuita tena. Kabla ya kuipokea ile simu nikageuka tena nikiyatembeza macho yangu kutazama huku na kule. Sikumuona mtu yeyote hivyo nikaichukua ile simu kutoka mfukoni na kubonyeza kitufe cha kupokelea. Ile sauti ya awali niliyoisikia kwenye ile simu wakati nikiwa kwenye ile nyumba namba 42 ikarudi tena hewani na mara hii ilisikika kwa utulivu zaidi. Mzungumzaji alikuwa mwanamke ingawa sauti yake bado ilikuwa ngeni kabisa machoni mwangu.
“Luteni…?”
“Naam…”. Nikaitikia kwa utulivu nikijaribu kuiga sauti nisiyoifahamu huku nikiwaza kuwa huwenda sauti ile ingekuwa ikifanana na ile sauti Luteni Kanali Luade Nguoma ingawa sikuwahi kumuona akiwa hai sembuse kuzungumza naye. Ukimya kidogo ukapita labda mzungumzaji alionekana kuingiwa na mashaka na mimi na hapo kelele za muungurumo wa injini ya gari likija eneo lile ukanishtua. Haukupita muda mrefu mara nikauona mwanga wa gari...ITAENDELEA
 
RIWAYA: UFUKWE WA MADAGASCAR
SEHEMU: 60

“Uko wapi?”. Sauti ya yule mtu upande wa pili ikaniuliza kwa mashaka kidogo.
“Jardin Public kama tulivyokubaliana”. Nikaongea kwa kujiamini kisha kitambo kifupi cha ukimya kikafuatia na wakati ule upande wa pili wa ile simu kwa mbali nikasikia mazungumzo mafupi katika lugha ya Kirundi ambayo sikuyaelewa. Hatimaye ile sauti ikarejea tena hewani.
“Wewe ni Luteni?”. Ile sauti ikaniuliza kwa mashaka.
“Luteni kanali Luade Ngouma, nimeshafika Jardin Public, wewe uko wapi?”. Nikamuuliza yule mtu kwa kujiamini na wakati nikiendelea na yale maongezi kwenye ile simu mara nikaliona gari fulani likiingia kwenye barabara ya mzunguko wa ile bustani huku likitembea taratibu kiasi cha mtu yeyote mtembea kwa miguu kuweza kulipita pasipo jitihada kubwa. Dereva wa lile gari alikuwa amewasha taa za mbele zenye mwanga dhaifu au dimlight. Nikaendelea kulitazama lile gari kwa makini huku damu ikianza kunichemka mwilini.
“Tazama gari ndogo inayoingia kwenye mzunguko wa barabara ya hiyo bustani. Mimi nipo ndani ya hili gari”. Ile sauti ikazidi kusisitiza.
“Ndiyo nimeliona”. Nikaongea kwa hakika huku nikiendelea kulitazama lile gari namna lilivyokuwa likitembea taratibu kwenye barabara ya mzunguko wa ile bustani.
Ilikuwa gari ndogo aina ya Volkswagen Comb nyeupe, vioo vya ile gari vilikuwa vimewekwa tinted nyeusi hivyo sikuweza kuwaona watu waliokuwa mle ndani kwa urahisi.
“Ifuate hii gari hadi kwenye kona ndogo ya kuchepukia barabara ya Avenue Janvier. Tafadhali harakisha Luteni kabla mambo hayajaharibika zaidi”. Ile sauti ikasisitiza.
“Mko wangapi ndani hiyo gari?”. Nikauliza
“Tupo wawili, mimi na dereva”
“Tunaelekea wapi?”. Nikauliza kwa udadisi.
“Com on!, punguza maswali mengi Luteni. Laiti ungeijua hatari iliyopo mbele yetu usingepoteza muda hata sekunde”
“Kwa hatua tuliyofikia ni muhimu kufahamu kila kinachoendelea”. Nikaongea katika namna ya ushawishi huku kwa tahadhari nikitoka kwenye ile bustani na kuanza kulifuata lile gari kwenye mzunguko wa ile barabara huku mkono wangu wa kushoto ukiwa tayari umezama kwenye mfuko wa koti langu kuikamata vyema bastola yangu.
“Nakupa dakika tatu Luteni kama hutofika tutaondoka kwani hili eneo si salama”. Ile sauti ya upande wa pili kwenye simu ikasisitiza huku mzungumzaji akionekana kuwa ni mtu mwenye mashaka.
“Punguza dakika moja ya muda wako nitakuwa tayari nimefika hapo”. Nikaongea kwa msisitizo na kujiamini kisha nikakata ile simu na kuizima nikiitia mfukoni.
Muda mfupi uliofuata nikawa nimetoka kwenye ile bustani ya Jardin Public na kuingia kwenye ule mzunguko wa barabara, nikitembea kando kando ya ile barabara kwa tahadhari ya hali ya juu.
Kona ndogo ya barabara ya Avenue Janvier ilikuwa upande wa kushoto wa mashariki mwa ile bustani. Hivyo nikaona kuwa ingekuwa vyema endapo ningeshika uelekeo ambao ungenipelekea nitokezee nyuma ya lile gari na siyo mbele ambapo muonekano wangu pasina shaka yoyote ungeweza kuwatia mashaka wale watu waliokuwa ndani ya lile gari kuwa sikuwa Luteni Kanali Luade Ngouma waliokuwa wakimtarajia.
Mara moja nikageuka kutazama nyuma yangu, sikumuona mtu yeyote akinifuatilia na hali ile ikanitia faraja kuwa bado nilikuwa salama. Hata hivyo nilikuwa makini sana na mjongeo wa hatua zangu huku nikiyatembeza macho yangu kutazama huku na kule.
Hatimaye nikaiona ile gari Volkswagen Comb ikiwa imeegesha kwenye kona ndogo ya barabara ya Avenue Janvier, mwisho wa ule mzunguko wa bustani. Moyo wangu ulikuwa ukienda mbio isivyo kawaida huku kijasho chepesi kikianza kunitoka maungoni. Kwa tahadhari ya hali ya juu nikaendelea kutembea nikilifuata lile gari pale lilipokuwa limeegesha na kwa kweli moyo wangu ulikuwa umepoteza utulivu kabisa. Mishipa yangu mwilini ilikuwa ikisukuma damu katika presha ya hali ya juu, mikono yangu ilikuwa ikitetemeka na hatua zangu miguuni sasa zilianza kupwaya. Nilifahamu kuwa nilikuwa nikiikaribia hatari ambayo ingeweza kuugharimu uhai wangu lakini kamwe sikuwa tayari kurudi nyuma kwani wakati huu kila tukio mbele yangu lilikuwa na taarifa muhimu za kuelekea kukamilisha uchunguzi wangu.
Kupitia yale maongezi kwenye simu nilikuwa nimeanza kuhisi kuwa kulikuwa na jambo hatari na la siri lililokuwa limefichika baina ya Luteni Kanali Luade Ngouma na watu waliokuwa kwenye lile gari mbele yangu. Hatimaye nikalifikia lile gari na kupitia giza nene lililokuwa eneo lile nikafahamu fika kuwa isingekuwa rahisi kwa wale watu waliokuwa ndani ya lile gari kuweza kunishtukia kwa haraka kuwa sikuwa Luteni Kanali Luade Ngouma waliyekuwa wakimtarajia.
Nilipolifikia lile gari nikashika kitasa cha mlango wa nyuma na kujaribu kuufungua ule mlango huku tayari nikiwa nimeichomoa bastola yangu kutoka kwenye mfuko wa koti na kuikamata vyema mkononi. Mlango wa nyuma wa lile gari haukufunguka kwa urahisi kama nilivyotarajia na hapo hofu dhidi ya kushtukiwa hila yangu ikaanza kuniingia. Vioo vyeusi vya lile gari havikuniwezesha kuona mle ndani hivyo nikauacha ule mlango na kusogea dirishani kwa dereva na kuanza kugonga. Hata hivyo dereva wa lile gari hakufungua mlango wala kushusha kioo. Sekunde chache zikapita nikiwa nimesimama pale mlangoni kama sanamu na wakati nikiwa mbioni kukata tamaa mara dereva wa lile gari akawasha taa za mbele za gari. Kufuatia tukio lile nikahisi wale watu ndani ya lile gari walikuwa katika mkakati wa kutaka kujiridhisha kuwa nilikuwa Luteni Kanali Luade Ngouma na si vinginevyo. Taratibu nikaanza kuhisi jambo la hatari.
Loh! ule mwanga wa taa za mbele za lile gari ukanisaidia walau kuona kwa shida idadi ya watu waliokuwa ndani ya lile gari. Mzungumzaji kwenye ile simu alikuwa sahihi. Mle ndani kulikuwa na watu wawili tu na wote walikuwa wameketi sehemu ya mbele ya lile gari na ghafla wakati nikiendelea kutafakari mara nikaona kioo cha dirishani cha ule mlango wa dereva kikishushwa taratibu kisha nikaisikia vizuri ile sauti ya kike iliyokuwa ikizungumza na mimi kwa njia ya simu. Loh! moyo wangu ukalipuka hata hivyo nikajitahidi kuumeza mshtuko wangu.
“Fungua mlango wa nyuma uingie Luteni, tunatakiwa kuondoka haraka eneo hili”. Yule mwanamke alikuwa ameketi kando ya dereva na aliongea kwa kujiamini pasipo kugeuka na kunitazama dirishani. Sauti yake ikafufua vizuri kumbukumbu zangu akilini na hapo moyo wangu ukashtuka. Yule mwanamke alikwa Amanda kwani sauti yake nilikuwa nikiikumbuka vyema. Kwa kweli sikuwa nimetarajia kabisa kuwa yule mwanamke niliyekuwa nikuzungumza naye kwenye simu angekuwa yeye. Kukutana kwa mara nyingine na mwanaharamu yule kwangu ilikuwa ni zaidi ya bahati niliyokuwa nikiisubiri katika maisha yangu.
Bila kupoteza muda nikasogea nyuma na kufungua mlango, mara hii mlango ule ulifunguka bila pingamizi na hapo nikaingia mle ndani kama zombi. Amanda na yule dereva wakageuka nyuma haraka kunitazama, nikagundua kuwa wasingeweza kunitambua kwa urahisi kwa vile kichwani nilikuwa nimejifunika kofia ya koti langu la mvua. Hatimaye wakanipigia saluti za kijeshi na tukio lile likanipelekea nijisikie kuuvaa vizuri uhusika wa Luteni Kanali Luade Ngouma. Nikazijibu salamu zile za kijeshi kwa weledi wa hali ya juu bila kuzungumza neno lolote na kwa kuwa kule nyuma nilikuwa nimeketi peke yangu hali ile ikanipa faraja. Bastola yangu nikaikamata vyema mkononi. Amanda alipogeuka kutazama mbele akamwambia yule dereva aendeshe gari ili tuondoke eneo lile na hapo safari ikaanza.
“Mambo yameharibika Luteni. Tunahitaji kutoroka nchi hii haraka iwezekanavyo”. Amanda akavunja ukimya.
“Una maanisha nini?”. Nikamuuliza Amanda kwa udadisi huku taratibu nikiiruhusu risasi moja kuingia kwenye chemba ya bastola yangu mkononi sambamba na kikohozi cha kujifanyisha. Amanda akageuka tena nyuma kunitazama na namna ya utazamaji wake ukanitia shaka. Lakini kwa kuwa nilikuwa nimejifunika kofia ya koti langu ingelimchukua muda mrefu kunitambua. Sikuoneshwa wasiwasi wowote hivyo hatimaye Amanda akageuka tena kutazama kule mbele na kuendelea kuongea.
“Baadhi ya wenzetu wametusaliti kwa kuvujisha siri za mipamgo yetu ya mapinduzi ya kijeshi kwa wanajeshi watiifu kwa serikali. Taarifa zinaonesha miongoni mwa makomredi wetu wapo waliokamatwa na wengine kuuwawa kinyama”
“Nani aliyekupasha habari hizo?”. Nikauliza kwa shauku.
“Watu wetu tuliowapandikiza kwenye vitengo vya usalama”. Amanda akaongea huku akiitazama saa yake ya mkononi.
“Tunatoroka kuelekea wapi?”. Yule dereva akauliza kwa shauku.
“Nchi yoyote tutakapokubaliwa kupata hati ya ukimbizi wa kisiasa”. Amanda akafafanua huku akigeuka na kumtazama yule dereva.
“Vipi kuhusu mgao wa pesa?”. Wasiwasi ukiwa mbioni kumvaa yule dereva nikamsikia akiuliza kwa sauti iliyopwaya.
“Huu siyo wakati wa kufikiria pesa. Tunachotakiwa sasa ni kutafuta namna ya kutoroka kwanza kabla hatujakamatwa”. Amanda akasisitiza hata hivyo maneno yale hayakuonekana kumuingia vizuri yule dereva.
“Tunahitaji kwanza pesa. Bila pesa hatuwezi kuvuka mipaka ya nchi hii. Tutakamatwa kama panya kwenye tenga na baada ya hapo tutateswa kinyama kabla ya kupigwa risasi za kichwa. Loh! laiti ningelijua nisingejiingiza kwenye mpango huu…”. Yule dereva hakumaliza kuongea akakatishwa na mguso wa mdomo wa bastola ya Amanda kichwani mwake.
“Acha kulalamika wewe muoga”. Amanda akamfokea yule dereva.
“Pesa ziko wapi?”. Nikauliza kwa udadisi na hivyo kuuzima mjadala baina ya Amanda na yule dereva.
“Maelezo niliyapata kuhusu sehemu ilipofichwa fedha ni ya uongo. Nimejaribu kupeleleza sehemu hiyo bila mafanikio”. Amanda akajitetea.
“Maelekezo hayo uliyapata wapi?”. Nikauliza.
“Niliyapata kutoka kwa mmoja wa watu wetu wa benki lakini mtu huyo kwa sasa ni marehemu”. Maelezo ya Amanda yakanipelekea nilikumbuke vizuri lile tukio la kwenye kile chumba Amanda alipomuua yule mwanaume baada ya kumalizia kufanya naye mapenzi. Sasa nilianza kupata picha juu ya nini kilichokuwa kikiendelea. Amanda na wenziwe walikuwa wakitarajia kupata kiasi fulani cha fedha pengine kwa ajili ya kufanikisha jaribio lile la mapinduzi ya kijeshi huku yule mtu aliyeuwawa na Amanda kwenye ile nyumba akiwa ndiye kiungo muhimu katika ufanikishaji wa upatikanaji wa fedha hizo. Huku yule mtu aliyeuwawa akiwa ameahidiwa nafasi ya kuwa gavana wa benki kuu ya Burundi mara baada ya mapinduzi hayo kufanikiwa.
Nikaanza kuwaza kiasi cha pesa ambacho kingeweza kugawanywa kwa watu muhimu katika mapinduzi yale. Kwa vyovyote kilitakiwa kiwe kiasi kikubwa cha pesa za kuhamasisha, pesa ambayo kwa vyovyote ingekuwa ya magendo. Maelezo ya Amanda pia yakanipelekea niikumbuke vizuri ile bahasha ndogo niliyoichukua chini ya godoro kule chumbani kwenye ile nyumba. Nikakumbuka kuwa ndani ya ile bahasha kulikuwa na ramani ndogo isiyoeleweka. Mara moja nilipokumbuka vile akili yangu ikachangamka kwani kupitia ile ramani ningeweza kuyafikia maficho ya fedha hizo na hakuna mtu mwingine ambaye angeifahamu vizuri siri ile.
“Ni lazima tufikirie namna ya kufanikisha kutoroka kwetu kwani kwa sasa suala la kupata fedha tuliyokuwa tukiitarajia halipo tena”. Amanda akaendelea kujitetea kisha akaingiza mkono mfukoni na kuchukua bahasha ndogo ya kaki. Nilipoitazama ile bahasha haraka nikaikumbuka kuwa ilikuwa ni ile bahasha ambayo Amanda aliichukua chumbani kwenye ile nyumba baada ya kumuua yule mwanaume kitandani.
Amanda alipoifungua ile bahasha akatoa karatasi fulani kutoka kwenye ile bahasha na kwa kuwa kulikuwa na giza akataka kuwasha taa iliyokuwa kwenye paa ya lile gari ili sote tuweze kuona kilichokuwa kwenye ile karatasi. Haraka nikashtuka kuwa ile taa endapo ingewashwa ingeweza kunifichua hivyo nikawahi kutumbukiza mkono mfukoni kuchukua kurunzi yangu kisha nikaiwasha na kumulika kwenye ile karatasi.
Tukiwa tumezama katika kuichunguza ile karatasi ndiyo lilipotokea tukio ambalo kamwe sikulitarajia katika fikra zangu. Ghafla tukasikia mshindo mkubwa uzioelezeka masikioni, kisha nikasikia sauti fulani zisizoeleweka kama za watu wanaopiga mayowe ndani ya kisima kirefu kisichokuwa na maji. Kelele kama za mazimwi katika masimulizi ya kale, na hapo nikajihisi kama niliyerushwa kwa wepesi wa hali ya juu kwa nguvu isiyoelezeka kutokea nyuma yangu. Kisha kichwa changu kikapigwa na dhoruba kali wakati niliposikia kelele za mpasuko mbaya masikioni mwangu. Kichwa changu kikavamiwa na ulevi mkali nisioujua chanzo chake, wingu zito jeusi likatanda kwenye mboni za macho yangu kisha maumivu makali yakaanza kusambaa mwilini kama niliyepigwa shoti ya umeme mkubwa.
Mara nikajiona nikididimia taratibu kwenye shimo refu lenye kiza kinene na jitihada zangu za kujinasua hazikuweza kufua dafu. Nikataka kupiga yowe ili niombe msaada lakini mdomo wangu ulinisaliti. Hatimaye taratibu nikafumba macho yangu, fahamu zangu zikitekwa na kupelekwa katika sayari nyingine na hapo sikuweza tena kufahamu kinachoendelea.
_____

Niliyafumbua macho yangu taratibu kisha pasipo kufanya mjongeo wowote masikio yangu nikayatega vyema nikijaribu kusikiliza sauti ya kitu chochote mle ndani. Sikusikia sauti yoyote, lile eneo lilikuwa na utulivu wa kupita kiasi. Nikajiuliza hapa ni wapi?, jibu sikulipata lakini maumivu makali yaliyosambaa haraka mwilini mwangu yakazirejesha kumbukumbu zangu.
Mara ya mwisho nikakumbuka kuwa nilikuwa kwenye gari Volkswagen Comb na mle ndani ya gari tulikuwa watatu, yaani mimi, Amanda na kijana mwingine dereva ambaye sikuweza kulifahamu jina lake. Tulikuwa tukielekea wapi?. Hapana sikufahamu tulipokuwa tukielekea, labda Amanda na yule kijana dereva wangeweza kulijibu swali lile kwa usahihi. Nikakumbuka kuwa tulikuwa kwenye mpango wa kutoroka, niseme walikuwa kwenye mpango wa kutoroka mahaini wale baada ya jaribio la mapinduzi ya kijeshi chini Burundi kugonga mwamba.
Walikuwa wamepanga kutorokea wapi vile?. Oh!, ndiyo Amanda alisema kuwa wangetorokea kwenye nchi yoyote ambayo wangeweza kupata hati ya ukimbizi wa kisiasa. Kha! Amanda atoroke?, kwanini anitoroke kirahisi wakati ana majibu mengi ya maswali yangu?. Kwanini anitoroke bila kulipa gharama ya ufedhuli alionifanyia?. Halafu nikakumbuka kuwa wasingeweza kutoroka kwa kuwa hawakuwa na fedha za kufanikisha kutoroka kwao.
Sasa tabasamu jepesi likachanua usoni mwangu pale nilipoikumbuka ile bahasha yenye mchoro kamili wa pesa ilipofichwa. Bahasha ambayo niliichukua kutoka kwenye ile nyuma ya yule mwanaume aliyeuwawa kwa kupigwa risasi na Amanda.
Tabasamu langu halikufika mbali, nikaliyeyusha taratibu kama kipande cha siagi kwenye kikaango cha moto kwani mishipa ya kichwa changu ilikuwa ni kama imeshtuka na hivyo kusambaza maumivu makali mwilini. Hata hivyo furaha ile haikutoweka, sasa nikataka niupeleke mkono wangu kwenye mfuko wa siri wa kipenyo cha koti langu kuipapasa ile bahasha. Loh! sikufanikiwa kwani kicheko cha mtu aliyekuwa pembeni yangu kikanishtua na hapo taratibu nikageuka kutazama upande wa kulia.
Niliona kitanda cha hospitali na juu ya kitanda kile alikuwa amelala mtu mmoja ambaye kamwe sikumfahamu. Taswira ya mtu yule hakika ilinitisha, alikuwa mtu mrefu sana na mweusi ti, alikuwa amevaa bukta nyeupe lakini bukta ile ilikuwa imelowa damu chapachapa, majeraha yaliyokuwa mwilini hayakufaa kutazamwa mara mbili, ni kama alikuwa amchomwa na kukatwa na kitu chenye ncha kali kama kisu, bikari au bisbisi. Mikono na miguu yake ilikuwa imefungwa kwa nyaya ngumu zilizopelekea mvilio wa damu sehemu zile. Kichwani alikuwa na majeraha mabichi sana yaliyovuja damu kwa muda refu na damu ile kuganda. Jicho lake moja lilikuwa limeng’olewa, sikio lake moja limekatwa na kutupwa kusikojulikana na mdomo wake ulikuwa umechanika hovyo kama sikio la mmasai. Loh! sikuwahi kumuona mtu aliyesulubiwa kinyama namna ile na hata alipocheka alionekana kama anayelia. Maumivu makali yalikuwa yamepita mwilini mwake na kiwango kile cha maumivu kilimfanya aonekane kama punguani kidogo, nati chache za kushikilia akili yake huwenda zilikuwa zimeanza kulegea.
“Unataka kufanya nini wewe?”. Yule mtu akaniuliza.
“Nataka kukaa”. Nikaongea huku nikitabasamu na hapo yule mtu akaendelea kucheka, kicheko chake kilipokoma akaniambia.
“Sasa utakaa vipi wakati umefungwa mikono na miguu?. Hii siyo sehemu ya starehe komredi”
“Kwani hapa ni wapi?”. Nikamuuliza yule mtu kwa shauku huku nikayafumbua vizuri macho yangu kutazama huku na kule na kwa kufanya vile nikamuelewa vizuri yule mtu aliyekuwa kando yangu akinisemesha. Mikono na miguu yangu vilikuwa vimefungwa na zaidi ya nguo yangu ya ndani sikuwa na nguo nyingine ya kunisitiri mwilini.
Nilikuwa nimelala juu ya kitanda chakavu cha hospitali chenye godoro chakavu la foronya ya mpira. Hatukuwa watu wawili tu mle ndani, tulikuwa zaidi ya watu ishirini na sita. Watu wale walikuwa wamefungwa kama mimi huku baadhi yao wakiwa watundikiwa dripu. Hali ya afya za watu wale zilikuwa mbaya sana. Baadhi walikuwa wamefunikwa kwa mashuka yaliyolowa damu ya muda mrefu na hivyo kuvunda. Wengine walikuwa uchi wa mnyama hawajafunikwa chochote na majaraha yao mwilini yalitisha mno kuyatazama. Wote walikuwa wamelala mle ndani isipokuwa mimi na yule jirani yangu ambaye nilipozinduka nilimkuta akiwa macho.
“Tupo sehemu ya mangojeo kabla ya kupelekwa kwenye chumba cha mahojiano”. Yule mtu akaniambia huku akiendelea kutabasamu kama mwehu na hapo nikahisi akili yake ilikuwa mbioni kufyatuka kutokana na kupitia mateso makali.
“Mahojiano ya nini?”. Nikamuuliza yule mtu kwa mshangao huku nikiendelea kukisahili vizuri kile chumba kikubwa. Kulikuwa na mlango mkubwa wa chuma upande wa kushoto hata hivyo mlango ule ulikuwa umefungwa. Upande wa kulia ukutani kulikuwa na matundu madogo mawili ambayo yasingeweza kuruhusu hata mkono wa binadamu kupenya na kupelekea hewa ya mle ndani iwe nzito mno. Kulikuwa na taa mbili za tubelight kwenye dari ya kile chumba zilizokuwa zikiangaza mle ndani na kupitia mwanga wa zile taa nikaweza kubaini kuwa ule ulikuwa usiku wa manane.
“Mahojiano ya kawaida tu, mfano wewe ni nani, umeoa au hujaolewa, unatokea wapi, kazi yako ni ipi na unafanya nini hapa Burundi”. Yule mtu akaendelea kunifafanulia na nilipomtazama nikagundua kuwa akili yake haikuwa sawa kabisa na wala hakuonekana kujuta kuwa mle ndani. Hata hivyo nikaendelea kuyatafakari maelezo yake kwa utulivu huku nikivuta picha. Loh! jasho likaanza kunitoka baada ya kugundua kuwa nilikuwa nimekamatwa na kuwekwa kizuizini, jasusi aliyeko kwenye tundu la kifo. Hofu ikaniingia na hapo nikageuka na kumuuliza yule mtu.
“Nimefikaje fikaje hapa?”
“Leo ni siku yako ya sita humu ndani. Ulipoletwa siku ile nikajua tayari umekufa kumbe una roho ngumu kama ya paka. Daktari akikuona atakusifu kwa kuzinduka mapema. Mimi ananilaumu sana kwa kutolala usiku kucha, mimi huwa namcheka tu”. Yule mtu akaendelea kuongea huku akitabasamu.
“Daktari yupi?”
“Daktari wa humu ndani”. Maelezo ya yule mtu yakanipeleke nimtazame kwa kutafakari kabla ya kumuuliza.
“Nililetwa peke yangu humu ndani?”. Nikamuuliza yule mtu kwa udadisi huku taswira ya Amanda ikijengeka kwa hasira kichwani mwangu.
“Uliletwa na mwenzako mmoja, wakadhani kuwa ni mzima kumbe keshajifia zamani”
“Wa kike au wa kiume?”
“Wa kiume, alilazwa kitanda kile kwa siku moja asubuhi kulipopambazuka wakashtukia kuwa tayari amekufa, wakamtoa na kumpeleka wanakokujua”.
“Una hakika kuwa alikuwa wa kiume?”. Nikamuuliza.
“Unaelekea unapenda sana wanawake wewe,eti eh?”. Yule mtu akaniambia huku akicheka na hapo nikatabasamu.
“Tuliletwa na nani humu ndani?”
“Mliletwa na wanajeshi nane wenye roho mbaya kama shetani”. Maelezo ya yule mtu yakanipelekea nitabasamu kidogo huku nikianza kuvuta picha ya hatari iliyoko mbele yangu. Yule mtu akaendelea.
“Nasikia waliwaokota kwenye ajali mbaya ya gari mkiwa hamjitambui”
“Nani aliyekwambia?”
“Niliwasikia wale wanajeshi waliowaleta humu ndani wakizungumza”
Mara moja kupitia maongezi ya yule mtu nikalikumbuka lile tukio la mwisho ambalo sikuwa nimelielewa kabisa. Tukio lililonipelekea kupoteza fahamu zangu na hapo ndiyo nikatambua kuwa tulikuwa tumepata ajali mbaya baada ya watu wote kwenye lile gari kuzama katika kuichunguza ile karatasi ya Amanda.
“Wewe ni nani?”. Nikamuuliza yule mtu nikijaribu kumpeleleza.
“Kepteni Amadou Coulibary Sidibe”. Yule mtu akajitambulisha huku akionekana kufurahishwa na jina lake, na hapo nikageuka na kumtazama vizuri. Jina lake lingefaa kufananishwa na majina ya watu wa nchi za Afrika magharibi, nchi kama Senegal, Burkinafaso, Gambia, Mali au Ivory coast.
“Unatokea nchi gani?”. Nikamuuliza yule mtu huku nikianza kufurahishwa na urafiki wetu.
“Natokea Mali”. Yule mtu akanijibu kwa kujiamini.
“Nchi ya Mali?”
“Ndiyo, natokea kaskazini mwa nchi ya Mali katika jimbo la Azawad. Umewahi kulisikia?”. Yule mtu akaniuliza mara hii akiacha kutabasamu na kunitazama kwa uyakinifu. Tukatazamana kwa sekunde chache huku akili yangu ikifanya kazi na kwa kufanya vile nikaikumbuka vizuri nchi ya Mali hususani jimbo lililoko upande wa kaskazini mwa nchi hiyo liitwalo Azawad. Ni katika jimbo hilo la Azawad ndiyo lilipochipukia kundi hatari la waasi wa Tuareg mapema mwaka 2012. Kundi hilo hatari la waasi likipigana kufa na kupona kuing’oa mdarakani serikali ya rais Amadou Toumani Toure. Lengo la kundi hilo likiwa ni kujipatia uhuru wake binafsi kama nchi nyingine za Afrika na kuliongoza jimbo la Azawad chini ya chama cha MNLA-Mouvement national de liberation de lʾAzawad kinachoongozwa na Bilal Ag Acherif.
“Mbali na kulisikia pia nalifahamu vizuri”. Nikamwambia yule mtu huku nikianza kuvutiwa na wasifu wake. Kisha ukimya kidogo ukapita nikiuma meno yangu baada ya maumivu makali kupita kichwani mwangu. Maumivu yale yalipopungua nikamuuliza yule mtu.
“Wewe ni mwanajeshi wa Tuareg?”
“Ndiyo wala hujakosea, nimefurahi umeniita vizuri sana komredi. Mwanajeshi wa Tuareg siyo muasi wa Tuareg kama vyombo vya habari vya magharibi vinavyojitosa kuunadi ubaya wetu. Sisi ni watu wema kabisa tunapigania uhuru wetu”
“Imekuwaje ukafika humu ndani?”. Nikamuuliza yule mtu kwa udadisi na hapo akasita kidogo.
“Tumekuja kusaidia mapinduzi ya kijeshi hapa Burundi”
“Mmekuja…?, wewe na nani?”
“Wenzangu, baadhi wametoroka na wengine ndiyo sisi humu ndani tuliokamatwa”. Nikamtazama yule na mara moja nikamuelewa vizuri. Alikuwa askari wa kukodiwa, yeye na wenzake.
“Nyinyi ni mamluki?”
“Tumekuja tu kusaidia mapinduzi ya kijeshi ya wenzetu wapenda haki kama sisi”. Yule mtu akijitetea.
“Mlikuwa wangapi?”......ITAENDELEA
 
RIWAYA: UFUKWE WA MADAGASCAR
SEHEMU: 61

“Tulikuwa arobaini na mbili”. Yule mtu akaongea huku akionekana kufikiria jambo fulani na kwa mara nyingine nilipomtazama mawazo yangu yakasafiri mbali zaidi. Nani alipaswa kulaumiwa?, uongozi wa serikali ya Burundi au waasi waliopanga jaribio lile la mapinduzi ya kijeshi?. Binafsi nikaona kuwa kila mmoja alistahili kubebeshwa lawama lakini serikali ilikuwa na nafasi kubwa zaidi ya kulaumiwa.
Viongozi wengi barani Afrika wanaugua maradhi ya kansa ya kupenda madaraka, kansa hiyo hutokana na ubinafsi mkubwa walionao, ubabe, kujiamini kupita kiasi kuwa wao ndiyo wanaojua kila kitu na hivyo kutokutoa nafasi kwa wengine wenye maono mazuri kwa mustakabari wa maendeleo ya mataifa yao. Baadhi ya viongozi hao wamekuwa wakiandaa sinema tofauti tofauti kila unapokaribia wakati wao wa kuachia madaraka. Mathalani huamua kubadili katiba iliyopo na kusimika katiba nyingine mpya itakayowaruhusu kuendelea na madaraka. Wengine huzuia vyombo vya habari vinavyokosoa tawala zao kwa mantiki au kuwakamata waandishi wa habari walioko mstari wa mbele wanaoikosoa serikali. Wengine huweka zuio kwa vyama pinzani vya siasa visiendeshe shughuli zao kwa mujibu wa sharia, kuwakamata viongozi wa vyama hivyo na kuwafungulia mashtaka ya uhaini ya kubambikiziwa na hatimaye kuwafunga gerezani kama siyo kuwaua kwa mipango ya siri. Bahati mbaya matokeo ya vitendo hivi huibua hasira na chuki kwa raia dhidi ya serikali zao, chuki hiyo ikisha kukomaa huzaa uasi dhidi ya serikali husika iliyoko madarakani na hapo ustaarabu wote wa mwanadamu uharibika na nchi kutumbukia kwenye machafuko.
Kwa namna nyingine waasi pia wamekuwa na sehemu yao ya kulaumiwa kwani pamoja na baadhi ya vikundi vya waasi kuwa na ajenda muhimu za kutaka kuzing’oa serikali zilizopa madarakani kama kukithiri kwa rushwa, madaraka ya upendeleo, udini, ukabila, ufujaji wa mali za umma na uonevu dhidi ya raia. Lakini vikundi hivyo vya uasi harakati zao zimejikuta zikigharimu maisha ya watu wengi raia wasio na hatia, vitendo vya ubakaji kwa wanawake, watoto wadogo kuingizwa kibabe katika mapambano ya mtutu wa bunduki kinyume na haki zao, uharibifu mkubwa wa rasilimali, vifo na maradhi. Haya yote hufanyika zaidi barani Afrika yalipo makazi ya mtu mweusi.
Ni dhahiri kuwa Kepteni Amadou Coulibary Sidibe na washirika wake walikuwa ni askari wa kukodiwa au mamluki walioingilia ugomvi usio wahusu. Ingawa kimsingi walionekana kama watu wenye nia njema lakini kwa namna moja au nyingine walikuwa ni kama wanaochochea ugomvi badala ya kusuluhisha. Kwa vipi watoke mbali kote huko tena kwenye nchi yenye matatizo makubwa ya kisiasa na kujitia kimbembele kutatua matatizo ya nchi nyingine?. Kwa kweli sikuona mantiki yoyote ya kuwaita mashujaa na sasa nilianza kuwahurumia juu ya hatima yao kwani vyombo vya usalama vya nchini Burundi vilikuwa vimewakamata mapema hata kabla hawajatimiza adhma yao. Kimya kilikuwa mbioni kushika hatamu hivyo nikavunja ule ukimya.
“Nani aliyewaalika kushiriki karamu hii ya mapinduzi ya kijeshi?”. Swali langu likampelekea Kepteni Amadou Coulibary Sidibe ageuke na kunitazama huku akitabasamu.
“Mapinduzi haya yalipangwa muda mrefu lakini wakati sahihi ulikuwa haujafika. Miezi minne iliyopita ofisi yetu ya sera na mipango ilipokea faksi kutoka hapa nchini Burundi. Faksi hiyo ikituomba msaada wa kijeshi ili kufanikisha mapinduzi ya kijeshi hapa Burundi. Baada ya kikao kizito chenye majadiliano ya kina tukaijibu faksi ile kwa kuonesha kukubali lile ombi lakini kwa masharti fulani”. Yule mtu akaweka kituo kama mtu anayefikiri jambo.
“Masharti yepi hayo?”. Nikauliza kwa shauku.
“Kabla ya kuanza safari nusu ya malipo ya kazi yenyewe ilitakiwa iwe tayari imetumbukizwa kwenye akaunti yetu ya siri jijini Bamako. Baada ya hapo askari wetu wangegharamiwa huduma zote muhimu kama malazi, chakula,usafiri na matibabu kuanzia mwanzo wa safari hadi mwisho wa oparesheni”
“Hayo yote yalifanyika?”
“Ndiyo, mambo yote yalienda sawa lakini baada ya kufika hapa Burundi tukagundua kuwa waratibu wa mapinduzi haya ya kijeshi walikuwa hawajajiandaa vizuri pengine kutokana na kukosekana kwa ushawishi toshelevu na taarifa za kutosha. Yaani ni kama walikuwa wamekurupuka tu baada ya kutamanishwa na mazingira ya ghafla”
“Una maanisha nini kusema hivyo?”. Nikamuuliza yule mtu kwa udadisi huku nikimtazama.
“Msukumo wa mapinduzi haya unaonekana ulitokana na kujitokeza kwa ziara ya ghafla ya rais Pierre Nkurunziza kuelekea nchini Tanzania. Hivyo niseme kuwa hapakuwa na maandalizi ya kutosha kama washirika wetu walivyotuaminisha”. Yule mtu akaongea kwa utulivu kisha kama mwenye msongo wa mawazo nikamuona akiangua kicheko lakini kicheko chake kiliambatana na machozi. Kwa kweli nilimuonea huruma huku nikihisi kuwa alikuwa akiwaza mambo magumu yaliyokuwa mbioni kumkabili baada ya kukamatwa.
“Faksi mliyotumiwa ilitoka kwa nani?”
“Ilitoka kwa uongozi wa juu wa uratibu wamapinduzi haya. Wiki mbili baada ya kupokea ile faksi umoja huo ulimtuma mjumbe wao kuja kuonana na sisi kwa vile mazungumzo mengine yalihitaji kuonana ana kwa ana”
“Unataka kuniambia kuwa huyo mjumbe alisafiri kutoka hapa Burundi hadi Mali?”
“Ndiyo, alikuja nchini Mali na tukafanya naye mkutano wa siku tatu ndani ya chumba chake alichokodi katika hoteli ya La Venise Malienne iliyopo barabara ya Kalaban Coura jijini Bamako”
“Unaweza kulikumbuka jina la huyo mjumbe?”. Nikamuuliza yule mtu kwa udadisi huku nikianza kuvutiwa na maelezo yale.
“Namkumbuka, anaitwa Asta ingawa siwezi kushangaa kuwa huwenda lilikuwa jina bandia kwani mambo haramu hufanyika kwa utambulisho haramu”. Yule mtu akaweka kituo akitazama juu ya dari ya kile chumba kisha nikamuona akiangua tena kicheko hafifu kama mwehu. Hata hivyo mara hii nilikabiliana vizuri na hali ile na kuungana naye katika kicheko chake na hapo hisia kuwa msichana aliyeitwa Asta angekuwa ndiyo Amanda zikaanza kuniingia taratibu.
“Sasa ilikuwaje hadi mkafika humu ndani?”. Nikamuuliza na hapo kimya kifupi kikapita huku yule mtu akiendelea kucheka, halafu ghafla akasitisha tena kicheko chake na kugeuka kunitazama.
“Kikao kile kilipomalizika tukawa tumefikia muafaka. Msichana yule niliyemtambua kwa jina la Asta akatumbukiza nusu ya pesa kwenye akaunti yetu kisha mipango ya safari ikaanza”
“Mlikuja kwa usafiri gani hadi hapa Burundi?”
“Ilibidi tuondoke kwa mafungu mafungu tukitumia ndege mbili tofauti kama watu tusiofahamiana kabisa na safari yetu ilianza usiku. Kundi la kwanza la watu ishirini liliondoka saa nne usiku kwenye uwanja wa ndege wa kimataifa wa Modibo Keita jijini Bamako Mali kwa ndege ya shirika la ndege la Chad. Kundi la pili ambalo nilikuwa mimi na wenzangu ishirini na moja tuliondoka saa sita kasoro usiku kwa ndege ya shirika la ndege la Tunisia”. Yule mtu akaweka kituo na kuzama tena kwenye tafakuri.
“Kwanini mliamua kujigawa?”
“Hatukutaka kusafiri pamoja kwa kukwepa kushtukia kwa urahisi vilevile kuongozana wote kwa pamoja kungeweza kumpa adui unafuu mkubwa wa kutukamata kwa urahisi endapo tungeshtukiwa”
“Hati za kusafiria mlipata wapi?”
“Asta, msichana tuliyeonana naye katika kile chumba cha hoteli ya La Venise Malienne jijini Bamako ndiye alitupatia hati za kusafiria siku moja kabla ya kuanza kwa safari yetu”. Yule mtu akafafanua na hapo nikaupisha utulivu nikiyatakari vizuri maelezo yake.
“Huyo Asta mliongozana naye kwenye ndege kutoka Bamako?”
“Hapana yeye alitangulia siku moja kabla na siku iliyofuata ndiyo sisi tukaanza safari”. Kupitia maelezo yale mawazo yangu yakaweka tena kituo kumtafakari Asta na hapo hisia zangu zikanitanabaisha kuwa huwenda Asta aliyekuwa akizungumzia pale ndiye angekuwa Amanda, Lucia au jina lingine lolote ambalo lingefaa kutumika katika kupoteza utambulisho halisi wa Amanda. Loh! Amanda alikuwa msichana hatari aliyepaswa kuogopwa kama ukoma.
“Mlifika saa ngapi hapa Bujumbura?”
“Siku ile hatukufika moja kwa moja hapa Burundi. Usiku ule tulifikia kwanza jijini Antananarivo kisiwani Madagascar katika nyumba moja iliyopo barabara ya Rue Docteur Joseph Raseta. Mambo yote yalifanyika kwa usiri mkubwa wa kukwepa kushtukiwa na maafisa usalama wa Madagascar”
“Mliwezaje kufika kwenye hiyo nyumba?”
“Tayari Asta alikuwa ametupa maelekezo yote muhimu ya kuifikia nyumba hiyo”
“Kwa hiyo katika hiyo nyumba mlimkuta Asta anawasubiri?”
“Ndiyo, tulimkuta Asta akiwa na mwanaume fulani ambaye baadaye Asta alitutambulisha kuwa mwanaume yule ni nani”
Safari hii maelezo ya yule mtu yakavuta zaidi hisia zangu na hapo nikageuka vizuri na kumtazama. Kupitia muonekano wake kulikuwa na kila dalili kuwa alikuwa akisema ukweli.
“Asta aliwatambulisha kuwa huyo mwanaume ni nani?”. Nikauliza kwa shauku. Swali langu likampelekea yule mtu atulie akinitazama kama anayeupisha utulivu kichwani mwake.
“Siwezi kulikumbuka jina lake lakini alikuwa mwanaume mweusi na mrefu mwenye mwili imara. Umri wake ungekuwa miaka hamsini na ushei. Asta alitueleza kuwa tusihofu kwani yule mwanaume alikuwa mwanamapinduzi mwenzetu na ndiye aliyekuwa amefanya mpango wa kupatikana kwa ile nyumba tuliyofikia. Hata hivyo baadaye tulikuja kugundua kuwa yule mwanaume alikuwa ni afisa wa jeshi mwenye uzoefu mkubwa wa mbinu za mapambano”
“Afisa wa jeshi mwenye uzoefu mkubwa wa mbinu za mapambano…moyo wangu ukashtuka kidogo wakati nikiyatafakari maneno yale na hapo akili yangu haraka ikahama nikiikumbuka ile picha ya afisa mmoja wa jeshi la wananchi wa Burundi niliyoiona kwenye sebule ya lile jumba nililotekwa na wale wanajeshi aliokujanao Amanda siku ya kwanza nilipofika jijini Bujumbura.
“Nini kilifuata baada ya hapo?”. Nikauliza na kwa kweli maelezo ya yule mtu yalikuwa yamefanikiwa walau kwa sehemu kunisahaulisha masaibu yangu. Yule mtu hakunijibu haraka badala yake nikamuona ni kama aliyekuwa mbioni kurudiwa na ule wazimu wake wa awali kisha nikamuona akigeuka na kunitazama kama mbwa mwenye njaa.
“Wewe ni nani na umefuata nini humu ndani?”. Yule mtu akang’aka huku jicho limemtoka pima kwa hasira kana kwamba alikuwa ameshtuka kutoka katika usingiza wenye ndoto mbaya.
“Mimi ni mateka kama wewe”. Nikaongea kwa utulivu huku nikihamisha macho yangu na kutazama kwenye dari ya kile chumba.
“Acha uongo wewe unafikiri sikujui?. Kwanini uniulize maswali mengi wakati sifahamu lolote kuhusu wewe?. Yule mtu akaniuliza huku akicheka kwa sauti na hapo nikaingiwa na mashaka zaidi kuwa nilikuwa nikiongea na mtu na mtu aliyekosa utulivu wa kuaminika kichwani mwake. Halafu wakati nikizama katika kusikitishwa na uharibifu ule wa akili ya binadamu kwa njia ya mateso makali yule mtu akasitisha kicheko chake kwa ghafla na kuongea kwa utulivu.
“Nahisi njaa sana ni lazima nile haraka vinginevyo nitakufa”
“Chakula utapata wapi?”. Nikamuuliza yule mtu na hapo akaangua tena kicheko kabla ya kuongea.
“Wewe ni mgeni humu ndani ndiyo maana hujui utaratibu wa humu. Muda siyo mrefu tutaletewa chakula na wale watu wenye roho mbaya”
Maelezo ya yule mtu yakapekea mvurugo mkubwa tumboni mwangu. Nilifahamu hatari kubwa iliyokuwa mbioni kunikabili, mateso yangu kama jasusi ni dhahiri yalihitaji kutekelezwa na watu wenye roho mbaya kuzidi hata ile ya shetani mwenyewe. Watu ambao ongezeko la furaha yao huwenda sambamba na kutaabika kwa mtu wanayemtesa. Watu ambao wangeweza kutumia mbinu zozote katika kunilazimisha nizungumze kile wanachohitaji kukisikia masikioni mwao. Sikuwa na shaka yoyote kuwa mateso yangu yangekuwa makali sana na hatimaye kuuwawa kinyama na huo ndiyo ungekuwa mwisho wangu.
Ni dhahiri kuwa yule mtu kando yangu pale kitandani alikuwa mbioni kugeuka mwehu kwani mara hii nilimuona akigeuka na kuanza kutafuna godoro la kitanda chake.
“Hao watu wanaoleta chakula humu ndani huja muda gani?”. Nikamuuliza yule mtu.
“Unafikiria kutoroka?”. Yule mtu akaniuliza huku akiangua kicheko cha mahoka kisha akageuka tena na kunitazama kabla ya kuendelea.
“Usipoteze muda wako komredi kwa kufikiria namna ya kutoroka kwani hutofika popote kabla hawajakukamata na kukusulubu vibaya hadi kifo”
“Sifikirii kutoroka”. Nikamjibu yule mtu kwa utulivu hata hivyo akili yangu haikuwa pale kwani mawazo mengi yalikuwa yakipita kichwani mwangu. Kwa mujibu wa maelezo ya yule mtu jirani yangu ni kuwa siku sita tayari zilikuwa zimetokomea tangu nilipofikishwa mle ndani na hapo nikajiuliza Veronica angekuwa katika hali gani baada ya kutoniona kwa muda wote ule?. Nikaendelea kujiuliza, kama mle ndani tuliletwa watu wawili, yaani mimi na yule kijana ambaye ndiye aliyekuwa dereva wa lile gari, Amanda yeye alikuwa wapi?. Halafu nikakumbuka kuwa sikuwa na lile koti langu mwilini, koti ambalolilikuwa na vitu vyangu vyote muhimu vya ujasusi. Loh! tumbo likaanza kunivuruga tena pale nilipowaza kuwa ningekuwa na machache sana ya kuzungumza wakati wa mahojiano yangu kwani vielelezo vilivyokuwa kwenye lile koti vilitosha kabisa kunitanabaisha kuwa mimi ni mtu wa namna gani. Ni dhahiri kuwa mateso makali hadi kifo yalikuwa mbioni kunikabili. Mwili wangu ulikuwa dhaifu sana kwani kitendo cha kutokula kwa siku kadhaa kilikuwa kimenimaliza nguvu mwilini na nikiwa pale kitandani ndiyo nikaanza kuyasikia vizuri maradhi ya njaa kali tumboni mwangu yaliyopeleke mikono yangu ianze kutetemeka hovyo.
Nikiwa katikati ya tafakuri yangu mara nikashtushwa na sauti za vishindo vya hatua za watu nje ya mlango wa kile chumba. Sekunde chache zilizofuata mara nikasikia kufuli za ule mlango zikifunguliwa kwa nje. Haraka nikamuona Kepteni Amadou Cuolibary Sidibe akigeuka na kunitazama na namna ya utazamaji wake ukaniondoa matumaini kabisa. Nilimuona akimeza funda kubwa la mate kwa uchungu kama mtu aliyeona tukio baya la kutisha sana katika maisha yake. Kisha kwa sauti dhaifu yenye hofu akaniambia.
“Wanakuja”
“Akina nani?”. Nikamuuliza kwa mashaka.
“Wale watu wenye roho mbaya. Najua hawatonisikiliza tena baada ya kuushtukia uongo wangu”. Kepteni Amadou Cuolibary Sidibe akaweka kituo akimeza funda lingine la mate na kuendelea.
“Niliwadanganya nikidhani kuwa ningepata nafasi ya kutoroka lakini sasa matumaini yote yamefifia. Kifo changu kimekuwa jirani sana kuliko nilivyodhani. Najua wataniua tu kwani hilo halina mjadala. Hata hivyo mimi siyo mtu wa kuogopa kifo kwani tayari nilishakufa siku nyingi zilizopita. Hata wakiniua nitakuwa ni kama ninayetangulia tu kwani hakuna aliyewahi kuletwa humu ndani halafu akatoka salama. Wakimaliza kuniua mimi atafuatia mwingine na mwingine”. Kepteni Amadou Cuolibary Sidibe akaweka kituo huku akipiga mwayo hafifu na nilipomtazama nikagundua kuwa alikuwa kwenye majuto makuu ya nafsi yake.
“Yote uliyoniambia katika maongezi yetu ni ya kweli?”. Nikamuuliza nikitafuta hakika ya maneno yake.
“Ni ya kweli lakini hayatokusaidia kitu komredi. Sisi sote humu ndani ni wafu tunaosubiri kufukiwa shimoni na baada ya hapo habari zetu zitafika ukomo hapa duniani huku dunia ikiendelea na udhalimu wake.
“Uliwadanganya nini?”. Nikamuuliza Kepteni Amadou Cuolibary Sidibe hata hivyo hakunijibu kwani mlango wa kile chumba tayari ulikwishafunguliwa kisha wanaume sita wanajeshi shupavu waliovaa sare wakaingia mle ndani lakini mmoja wao ningefaa kumuita daktari. Daktari yule alikuwa mfupi sana wa kimo au nimuite mbilikimo. Alikuwa amevaa koti jeupe kubwa la daktari na hivyo kumpelekea aonekane kama mtoto mdogo katika mavazi ya baba yake. Alikuwa amevaa miwani ya macho huku kifuani akiwa ametundika kifaa cha kutazamia mwenendo wa mapigo ya moyo ya mgonjwa, stetheskopu. Mikono na miguu ya daktari yule ilikuwa mifupi sana kama vipande vya muhogo wa kibandameno, vodole vyake vilifanana na karoti zenye afya zilizopitia kilimo cha msimu wa maji mengi kwenye ardhi yenye udongo wenye rutuba. Hata hivyo macho yake makubwa yalikuwa na viashiria vya huruma iliyofichika. Wale wanajeshi wawili miongoni mwao walikuwa na cheo cha Kanali, mmoja alikuwa Sajenti na wale wawili waliosalia walikuwa na cheo cha Koplo. Watu wale weusi urefu wao ulibakiza futi chache tu kuifikia dari ya kile chumba. Sura zao zilielekea kufurahia matendo ya kinyama kuliko hata siku zao za kuzaliwa. Mwanajeshi mmoja mwenye cheo cha Koplo mkononi alikuwa amebeba galeni ndogo ya lita tano yenye kimiminika nisichokifahamu, na hapo mashaka yakazidi kuniingia.
Wale wanajeshi wakatembea kwa mwendo wa kibabe hadi walipofika katikati ya kile chumba ambapo walisimama na kuanza kuyetembeza macho taratibu mle ndani kuwatazama watu waliokuwa wamelala juu ya vitanda vya mle ndani. Haraka nikajua kuwa kulikuwa na mtu waliyekuwa wakimtafuta mle ndani. Hisia zangu zikanipelekea nijihisi kuwa pengine mtu aliyekuwa akitafutwa ni mimi. Taratibu wasiwasi ukaanza kuniingia, hisia zangu zikiniambia jambo baya lilikuwa likielekea kutokea mle ndani na sikuwa na mashaka yoyote kuwa mhanga wa tukio hilo baya ningekuwa mimi, kwa vile wenzangu wote mle ndani walikwishapitia mateso makali. Sikuwa na namna ya kufanya zaidi ya kufumba macho yangu taratibu na kuanza kumuomba Mungu aniepushie mbali na kadhia ile. Ilikuwa sala fupi na muhimu iliyojaa ushawishi wa kila namna. Hata hivyo nilipofumbua macho nikahisi kuwa maombi yangu yalikuwa tayari yamejibiwa. Wale wanajeshi walioingia mle ndani hawakushughulika na mimi badala yake nikawaona wakiwa wamezunguka kile kitanda alicholala Kepteni Amadou Coulibary Sidibe kando yangu.
“Kepteni…”. Nilimsikia mmoja wa wale wanajeshi akiita pale kitandani na hapo Kepteni Amadou Coulibary Sidibe akageuka na kumtazama yule mtu huku akitokwa na jasho jingi la woga.
“Umepoteza muda wetu mwingi kwa kutudanganya”. Yule mtu akaendelea.
“Nimewadanganya nini?”. Kepteni Amadou Coulibary Sidibe akajitetea na kuzidi kuzichafua sura za wale watu kwa hasira. Mwanajeshi mmoja mwenye cheo cha Kanali akasogea karibu zaidi ya kile kitanda huku tabasamu la kinyama likiumbika taratibu usoni mwake kisha hatimaye akavunja ukimya mikono yake ameitia mfukoni.
“Kepten, mwisho wa ujanja wako sasa umefika. Hatuna muda wa kuendelea kusikiliza hadithi zako za sungura mjanja. Tumeshampata mtu mwingine atakayetusaidia kile tunachokitaka”. Yule Kanali wa jeshi akaweka kituo na kukohoa kidogo kabla ya kuendelea.
“Jirani yako upande wa kushoto kuna mtu anaitwa Tibba Ganza, yeye ndiye mtu atakayetuweka bayana juu ya mambo yote yanayaoendelea hapa Burundi. Hivyo wewe hauna umuhimu tena”
Kisikia vile moyo wangu ukalipuka kwa hofu wakati jina langu lilipotajwa na yule mtu, tumbo likanisokota na moyo wangu ukaanza kwenda mbio. Yule Kanali wa jeshi alipomaliza kuongea akaonesha ishara fulani ya kichwa na hapo ndiyo nikaelewa nini kilichokuwa ndani ya ile galeni ya lita tano.
Nilimuona mwanajeshi mmoja mwenye cheo cha Koplo aliyebeba ile galeni akiifungua haraka kisha akaanza kummiminia Kepteni Amadou Coulibary Sidibe pale kitandani, akianzia kichwani hadi miguuni. Tukio lile likapelekea harufu nyepesi ya mafuta ya petroli kupenya taratibu puani mwangu na hivyo kuamsha hisia za mauti. Zoezi lile lilipokamilika wale wanajeshi wakasogea kando na kumuacha yule Kanali kando ya kile kitanda.
Tofauti na matarajio yangu Kepteni Amadou Coulibary Sidibe hakuonekana kushtushwa na tukio lile hata kidogo badala yake alianza kwa kutabasamu na hatimaye akaangua kicheko cha mahoka huku akiporomosha matusi ya kila namna akiwatukana wale wanajeshi. Kepteni Amadou Coulibary Sidibe alikuwa ni mtu mwenye roho ngumu sana hata hivyo yule Kanali hakuonekana kushtushwa na zile mbwembwe zake badala yake akaingiza mkono mfukoni na kutoa kiberiti cha gesi kisha muda uleule akakiwasha na kumtupia Kepteni Amadou Coulibary Sidibe pale kitandani na hapo Kepteni Amadou Coulibary Sidibe akaanza kupiga mayowe wakati akianza kuungua. Muda uleule moto kubwa wenye wingu jeusi ukalipuka pale kitandani. Loh! Kepteni Amadou Coulibary Sidibe akaanza kukukuruka pale kitandani ili ajinasue lakini ni kama aliyekuwa akipoteza muda wake bure kwani alikuwa amefungwa kikamilifu kwa nyaya ngumu kama nguruwe pori. Tangu nizaliwe sikuwahi kuona unyama wa aina ile duniani.......ITAENDELEA
 
Hadith ya kisenge jasusi gani mzembe hivi alafu unaeleza mabarabara tu hata siimalizii wachaniendelee kuwasoma wakongwe
 
Hadith ya kisenge jasusi gani mzembe hivi alafu unaeleza mabarabara tu hata siimalizii wachaniendelee kuwasoma wakongwe
sio jukumu letu sisi kazi yetu ni kusoma na kuburudika
watu kama nyie lazima muwepo duniani kukamilisha hatua inayoitwa MAISHA
 
Hadith ya kisenge jasusi gani mzembe hivi alafu unaeleza mabarabara tu hata siimalizii wachaniendelee kuwasoma wakongwe
sio jukumu letu sisi kazi yetu ni kusoma na kuburudika
watu kama nyie lazima muwepo duniani kukamilisha hatua inayoitwa MAISHA
 
Nimependa stori ako unavypituma husubiri mpaka tukushtue ila improve uandishi wako unaelezea sana maeneo na nyumba stori ina matukio machache
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom