RIWAYA: UFUKWE WA MADAGASCAR
SEHEMU: 35
shwari. Ile barabara ilikuwa ikikatisha moja kwa moja mbele ya ile suparmaket niliyoegesha gari langu hivyo nilinyoosha moja kwa moja.
Wakati nikilifikia lile gari langu nikachepuka kidogo na kujibanza kwenye kona moja ya ukuta katika namna ya kuchunguza hali ya usalama wa eneo lile na niliporidhika kuwa hali bado ilikuwa shwari nikavuka barabara na kuelekea kwenye gari langu kwa tahadhari huku mkono wangu wa kushoto ukiwa umekikamata vyema kilimi cha bastola yangu kwenye mfuko wa koti langu tayari kukabiliana na rabsha yoyote ambayo ingejitokeza eneo lile. Hatimaye nikalifikia gari langu na baada ya kulizunguka kidogo kukagua usalama wake na kuridhishwa nikafungua mlango wa dereva na kuingia mle ndani. Koti langu la mvua nikalivua na kulitupia siti ya nyuma kasha bila kupoteza muda nikawasha gari na kuondoka eneo lile huku mawazo mengi yakipita kichwani mwangu.
Kwa namna moja au nyingine nilianza kuamini kuwa tukio la kutekwa kwa balozi Adam Mwambapa lilikuwa limetekelezwa na kikundi cha wanajeshi wachache wa jeshi la wananchi wa Burundi ingawa bado sikuweza kufahamu dhamira ya watekaji hao. Nilikuwa nimeanza kushawishika kwenda kuripoti juu ya tukio lile kwa maafisa usalama waandamizi wa nchini Burundi hata hivyo hali ile ya machafuko ya kisiasa iliyokuwa ikiendelea nchini Burundi ilinionya kuwa kwa kufanya vile huwenda ningejitumbukiza kwenye hatari ya kugharimu uhai wangu badala ya kutatua tatizo kama ilivyokuwa lengo langu.
Mvua kubwa bado ilikuwa ikiendelea kunyesha na wakati nikiendelea na safari yangu mbali na kile kitongoji cha Chaussée P.L. Rwagasore nikagundua kuwa mifereji mingi ya maji iliyokuwa ikipakana na barabara za kitongoji kile ilikuwa mbioni kufurika kwa maji ya mvua kubwa iliyokuwa ikiendelea kunyesha. Nikaendelea kuendesha gari kwa kasi nikikitoroka kitongoji kile huku mara kwa mara nikiyapeleka macho yangu kutazama vioo vya ubavuni vya lile gari kuona kama kungekuwa na gari lolote lililokuwa likinifungia mkia kwa nyuma. Sikuona gari lolote hivyo hali bado ilikuwa shwari.
Baada ya mwendo mrefu wa safari yangu nikivizunguka vichuguu kushuka mabonde na kupanda milima hatimaye nikapita mbele ya jengo refu la ghorofa la Vaya residence apartments services. Nilipolipita lile jengo upande wa kushoto baada ya safari fupi nikakunja kona upande wa kulia nikipanda mlima mfupi katika barabara ya Chaussée P.L. Rwagasore. Mwendo wangu ulikuwa wa kasi mno hivyo baada ya muda mfupi nikawa nimeyafikia makutano ya barabara ya Chaussée P.L. Rwagasore na barabara ya Avenue Belvedere. Nilipoyafikia yale makutano nikapunguza mwendo na kuingia barabara ya Avenue Belvedere nikianza kushuka mteremko mkali wa barabara ile kuelekea mjini.
_____
Saa tano na dakika kumi usiku niliegesha gari langu katika viunga vya maegesho ya magari vya jengo la New Parador Residence kando ya barabara ya Boulevard du 28 Novembre. Mvua bado ilikuwa ikiendelea kunyesha na nje ya jengo ile kulikuwa na magari machache yaliyoegeshwa.
Nilikuwa nimeyakumbuka vyema maelezo ya Hidaya kuwa siku ile ambayo hakuhudhuria kazini Balozi Adam Mwambapa alikuwa amealikwa na maafisa waandamizi wa serikali ya Burundi kuhudhuria kikao juu ya hali tete ya machafuko ya kisiasa iliyokuwa imeanza kutokea nchini Burundi. Kwa mujibu wa maelezo ya Hidaya aliyoyapata kutoka kwa Balozi Adam Mwambapa ni kuwa mkutano ule ungefanyikia katika ukumbi wa lile jengo la New Parador Residence ndiyo kisa nikawa nimefika pale.
Kabla ya kushuka kwenye gari nikatulia kwa dakika chache nikitathmini vizuri mandhari yale. Eneo la mbele la maegesho ya magari ya lile jengo kulipandwa miti mirefu ya kivuli aina ya Quercus virginiana katikati ya bustani nzuri ya maua baina ya sehemu moja ya maegesho ya gari na sehemu nyingine. Kulikuwa na taa hafifu za ardhini zilizokuwa zikimulika eneo lile na hivyo kulifanya lile eneo lipendeze.
Nilipozidi kuchunguza nikagundua kuwa kulikuwa na magari machache madogo yaliyokuwa yameegeshwa eneo lile. Mbali na magari yale madogo pia kulikuwa na basi moja la wanafunzi wa shule ya sekondari ya Eldoret ya nchini Kenya, lori moja kubwa la kubebea watalii wa masafa marefu na gari moja jeusi aina ya Nissan Caravan lililokuwa limeegeshwa upande wa kushoto mwisho wa lile jengo.
Upande wa kulia wa eneo lile kulikuwa na kibanda kidogo chenye mashine mbili za ATM za benki. Mashine moja ya ATM ya Banque de Crédit de Bujumbura na mashine nyingine ya ATM ya Banque de la République du Burundi. Kulikuwa na watu wachache katika foleni za wahitaji huduma kuelekea kwenye zile mashine za ATM na wengi wao walikuwa ya wazungu wa kutoka nje ya bara la Afrika. Pembeni ya mashine zile za ATM kulikuwa na bustani ya nyasi laini zilizokatiwa vizuri na kupendeza na katika bustani ile kulikuwa na sehemu za kupumzika zenye viti na meza chini ya miamvuli mikubwa yenye rangi za kupendeza. Nilipoyatembeza macho yangu kwa utulivu nikagundua kuwa hapakuwa na mtu yeyote eneo lile labda kutokana na mvua kubwa iliyokuwa ikiendelea kunyesha.
Jengo la New Parador Residence lilijengwa kwa ufanisi wa hali ya juu kiasi kwamba taa nzuri zilizokuwa zikiwaka kwenye ghorofa zake zililipelekea jengo lile lionekane kama meli kubwa ya kupendeza iliyotia nanga kwenye bandari ya nchi kavu. Chini ya lile jengo kulikuwa na supermarket moja kubwa, maduka ya nguo za kisasa, ofisi za mashirika ya simu, ofisi za Dstv, Dhl na maduka mawili ya kubadilishia fedha za kigeni.
Hatimaye nikalichukua lile koti langu jeusi la mvua na kulivaa kisha nikafungua mlango wa gari na kushuka. Taratibu nikaanza kukatisha kwenye viunga vile vya maegesho taratibu nikielekea mbele wa lile jengo sehemu kulipokuwa na mlango mkubwa wa kioo na varanda pana yenye ngazi iliyofunikwa kwa kofia nzuri ya zege.
Wakati nikiendelea kutembea nikawa nikiyatembeza macho yangu kwa utulivu kutazama huku na kule kuchunguza kama kungekuwa na mtu yeyote ambaye angekuwa akizifuatilia nyendo zangu. Sikumuona mtu yeyote wa kumtilia mashaka hivyo hatimaye nikazifikia zile ngazi na kuanza kuzipanda tatatibu kisha nilipoufikia ule mlango wa kioo nikausukuma na kupotelea ndani.
Kulikuwa na vijana wawili wahudumu wa ile hoteli waliokuwa wamesimama kando ya ule mlango wa kuingilia kwa ndani. Vijana wale waliovaa sare za kazi, suruali nyeusi, makoti ya suti ya rangi nyekundu na kofia nyeupe kichwani wakanipokea kwa bashasha zote huku wakinionesha tabasamu la kirafiki kwenye nyuso zao. Nikawashukuru vijana wale kwa ukaribisho wao na kuendelea na safari yangu nikitembea juu ya kipande mstatili cha zulia jekundu kuelekea sehemu ya mapokezi ya hoteli ile huku nikiendelea kuyatembeza macho yangu kupeleleza mandhari ya mle ndani.
Upande wa kushoto mara baada ya kushuka ngazi chache chini kulikuwa na ukumbi mkubwa wenye meza nyingi za kulia chakula zenye umbo duara zilizozungukwa kwa viti nadhifu vyenye foronya laini. Meza zile zilikuwa zikimefunikwa kwa vitambaa visafi vya rangi nyeupe na juu yake kuliwekwa kadi ngumu za kupendeza zenye orodha ya vyakula na vinywaji vinavyopatika katika hoteli ile. Karatasi laini nyeupe za tishu za kufutia mikono na vifaa vyote muhimu vya kujipatia maakuli kama uma, visu na vijiko. Vikasha wiwili vidogo kimoja cha kuwekea chumvi ya mezani na kingine cha vijiti vya kuchokolea meno. Pembeni ya meza zile kulikuwa na makochi mazuri ya sofa yaliyopangwa kuzizunguka meza fupi za vioo katika mpangilio mmoja unaovutia. Nilipozidi kuchunguza mwisho wa ukumbi ule nikaiona kaunta kubwa ya vinywaji.
Madirisha makubwa ya vioo ya ukumbi ule yalikuwa yamefunikwa kwa mapazia marefu yenye rangi nzuri za kupendeza. Ukutani kulikuwa na runinga pana za flat screen zilizokuwa zikiendelea kurusha taarifa kutoka sehemu mbalimbali za jiji la Bujumbura zikielezea juu ya hali ya machafuko ya kisiasa iliyokuwa ikiendelea kufuka moshi nchini Burundi.
Nilipotazama vizuri ndani ya ule ukumbi nikaona kuwa kulikuwa na watu wachache waliokuwa wameketi mle ndani wakijipatia mlo na vinywaji huku kwa makini wakiendelea kufuatilia taarifa zilizokuwa zikirushwa kupitia zile runinga. Ukumbi ule mkubwa ulikuwa umetenganishwa na ile sehemu ya mapokezi kwa ukuta mkubwa wa kioo unaomruhusu mtu yeyote kuweza kuona mle ndani bila usumbufu wowote.
Nilipogeuka kutazama upande wa kulia nikauona ukumbi mwingine mdogo wenye nguzo mbili kubwa katikati yake. Kulikuwa na watu wachache kwenye ukumbi ule, wazungu kwa waafrika wakiendelea na maongezi yao ya hapa na pale katika makochi mazuri ya sofa yenye meza fupi za mbao. Watu wale wakijipatia vinywaji, wengine wakivuta sigara na kutazama mechi za mpira wa miguu za ligi za ulaya zilizokuwa zikioneshwa kwenye runinga tofauti zilizotundikwa ukutani. Wahudumu wa hoteli ile walikuwa wakiendelea na taratibu zao za kutoa huduma kwa wateja kama ilivyo ada.
Wakati nilipokuwa nikiifikia kaunta ya mapokezi ya ile hoteli mle ndani nikawaona vijana wawili waliovaa sare za kazi zinazofanana na za wale vijana wengine walionikaribisha kule mlangoni na wote walikuwa warefu na weusi wenye maumbo imara na miili iliyojengeka vizuri. Mhudumu mmoja alikuwa akizifuta bilauri ndefu za vinywaji kwa kitaulo kidogo kilichokuwa begani mwake na kuzipanga vizuri katika rafu ya mbao iliyokuwa ukutani eneo lile. Mwenzake alikuwa akiandika taarifa fulani kwenye kitabu kidogo kilichokuwa juu ya meza ya ile kaunta na aliponiona haraka akaacha kile alichokuwa akikifanya na kunikaribisha kwa tabasamu zuri la kibiashara na mimi bila ajizi nikawahi kumsalimia.
“Comment va le travail?’’. Habari za kazi?.
“Bien frère, je peus tʾaider?”. Salama kaka sijui nikusaidie nini?. Yule kijana akanijibu kwa bashasha zote za kirafiki huku akinitazama kwa makini huku akikunja vizuri mikono ya shati lake.
“Je suis Iʾofficien de Iʾambassade de Tanzanie ici à Bujumbura. Je veus savoir sʾil y a eu une reunion de dirigents qui a eu lieu dans votre”. Mimi ni afisa wa ubalozi wa Tanzania hapa Bujumbura. Nataka kufahamu kama kulikuwa na mkutano wowote wa viongozi wa serikali uliofanyikia hapa siku ya juzi. Nikaongea kwa utulivu huku nikiwatazama wale vijana kwa makini. Swali langu bila shaka lilimshtua kidogo yule kijana na hapo nikamuona akinikata jicho la udadisi kabla ya kugeuka na kumtazama mwenzake pale kaunta. Nikahisi jambo fulani nisilolielewa hata hivyo sikutia neno lolote. Yule kijana akageuka na kunitazama tena.
“Pardon!, nous ne sommes pas permis de donner auquʾune information, peut être allez voir notre directeur’’. Samahani!, haturuhusiwi kutoa taarifa zozote za kiofisi labda ukamuone meneja wetu.
Yule kijana akaniambia kwa utulivu huku akinitazama na kwa kweli sikuona tashwishwi yoyote usoni mwake. Kitambo kifupi cha ukimya kikapita huku nikigeuka nyuma na kuyatembeza macho yangu taratibu katika namna ya kupeleleza sura za watu zinazostahili kutiliwa mashaka mle ndani. Sikumuona mtu yoyote akinitazama hivyo nikayarudisha macho yangu kwa yule kijana na kuweka kituo.
“Où est le bureau de votre directeur?”. Ofisi ya meneja wenu iko wapi?. Nikamuuliza yule kijana mhudumu na mara ile tena nikamuona akigeuka na kumtazama mwenzake pasipo kusema neno lolote kisha akayarudisha macho yake tena kunitazama.
“Au cinquieme niveau dans la chambre numero 302”. Ghorofa ya tano chumba namba 302. Yule kijana akaniambia kwa utulivu huku akinitazama na hapo nikakumbuka kutumbukiza ombi langu.
“Fais un coup de téléphone et dis lui quʾil ya qulquʾun qui veut le voir”. Piga simu mueleze kuwa kuna mtu anahitaji kumuona. Nikamwambia yule kijana na baada ya kusita kidogo nikamuona akinyanyua kiwambo cha simu ya mezani iliyokuwa pale juu kwenye meza ya kaunta na kukiweka sikioni kisha nikamuona akibonyeza tarakimu kadhaa. Muda mfupi uliofuata ile simu ilikuwa hewani na hapo nikajua kuwa yule kijana alikuwa akiwasiliana na meneja wa ile hoteli ingawa mazungumzo ya simu yalipoanza sikuambulia kitu chochote kwani lugha ya mawasiliano iliyokuwa ikitumika baina ya yule kijana mhudumu na meneja wa ile hoteli ilikuwa ni kirundi ambayo mimi sikuifahamu. Yale mazungumzo ya simu yaliposimama nikamuona yule kijana akigeuka na kuniuliza.
“II demande qui etes vous?’’. Anauliza kuwa wewe ni nani?.
“Dis lui que cʾest Iʾofficié de Iʾembassade de Tanzanie ici au Burundi”. Mwambie kuwa mimi ni afisa kutoka ubalozi wa Tanzania hapa nchini Burundi. Nikamwambia yule kijana huku taratibu nikivigongesha vidole vyangu juu ya sakafu ya ubao wa ile kaunta. Yule kijana akayahamishia maongezi yake tena kwenye ile simu kisha baada ya maongezi mafupi akaikata ile simu na kukirudishia kile kiwambo mahala pake. Muda uleule akageuka tena na kunitazama akivunja ukimya.
“Allez maintenant, il est dans la chambre numero 302, il vous ettend”. Nenda sasa hivi yupo chumba namba 302 anakusubiri. Yule kijana akaniambia.
“A la fin de ce comptoire du côté droit tu vas voir Iʾassacaire. Ça sera bien si vous partez vite, parcequʾil reste avec un peu de temps avant quʾil ferme son bureau cette nuit’’. Mwisho wa hii kaunta upande wa kulia utaona lifti. Itakuwa vizuri ukiwahi maana amebakiwa na muda mfupi kabla ya kufunga ofisi yake usiku huu. Yule mwenzake akasisitiza.
“Je vous remercis beaucoup”. Ahsanteni sana.
Nikawashukuru wale vijana na kuanza kuondoka eneo lile. Niliiacha ile kaunta ya mapokezi na kushika uelekeo wa upande kulia nikitembea kwa utulivu na baada ya kuipita nguzo moja kubwa ya ule ukumbi upande wa kushoto nikaiona lifti ya lile jengo. Nilipochunguza vizuri nikagundua kuwa ile lifti ilikuwa ikishuka hivyo nikasimama na kusubiri mtu aliyekuwa...ITAENDELEA