RIWAYA; UFUKWE WA MADAGASCAR
SEHEMU; 16
Mtunzi:Kelvin Mponda
... na Burundi. Mbali na kadi zile pia kulikuwa na ramani ndogo ya kukunja ya kijasusi niliyokuwa nimepewa na mratibu wangu wa safari za kijasusi Brigedia Jenerali Ibrahim Gambari. Muda mfupi kabla ya kuanza safari yangu jijini Dar es Salaam, Tanzania. Kwa kweli nilijikuta nikiishiwa nguvu pale nilipohisi kuwa kulikuwa na uwezekano mkubwa wa nyaraka zile muhimu za kijasusi kuwa tayari zingekuwa zimeonwa pale ambapo Amanda angeamua kufanya upekuzi kwenye begi langu wakati fahamu zikiwa zimenitoka.
Hata hivyo sikuwa na namna ya kufanya kwani chochote ambacho kingetokea nilipaswa kujipanga kukabiliana nacho ingawa uzima wa afya yangu kilikuwa ni kipaumbele cha kwanza. Hatimaye nikameza funda kubwa la mate nikijitahidi kuyatowesha mawazo yale kichwani mwangu huku zile dawa za kutuliza maumivu zikiendelea kufanya kazi mwilini.
_____
Sikuweza kufahamu ni wakati gani lepe hafifu la usingizi lilikuwa limefanikiwa kuziteka fikra zangu pale kitandani wakati nilipokuwa nikiendelea kuwaza hili na lile juu ya safari yangu ile ya kijasusi, pale niliposhtuka kutoka usingizini baada ya kitasa cha mlango wa kile chumba kusikika kikizungushwa taratibu na ule mlango kufunguliwa ukisukumwa kwa ndani.
Hisia zangu zikanitanabaisha kuwa yule alikuwa Amanda na alikuwa akija mle ndani kuniletea chakula. Hivyo nikageuka taratibu nikitabasamu na kuyapeleka macho yangu kuutazama ule mlango wa kile chumba huku nikitarajia kumuona Amanda akiwa na sinia kubwa lenye maakuli. Hata hivyo hilo halikutokea na badala yake mbele yangu nikajikuta nikikabiliana na mshtuko usioelezeka.
Ule mlango ulipofunguliwa Amanda akaingia mle ndani huku akiwa ameongozana na wanaume watatu, warefu na weusi wenye miili iliyojengeka imara. Huku wote wakiwa wamevaa sare za jeshi la wananchi wa Burundi na kofia za bereti vichwani mwao. Jamaa walikuwa wamepanda hewani kisawasawa na namna ya mikono ya gwanda zao ilivyokuwa imekunjwa niliweza kuiona misuli yao imara ya mikononi namna ilivyotuna kikamilifu kwa mazoezi ya nguvu yasiyokuwa na kikomo. Haraka nilipowachunguza nikagundua kuwa walikuwa ni makomandoo waliofuzu vizuri katika medani za masuala ya kijeshi na hapo koo langu likanikauka ghafla kwa hofu. Mapigo ya moyo wangu yakaanza kunienda mbio huku baridi nyepesi ikisafiri katika maungo yangu. Hali ile ikanipelekea nijihisi kuwa nimepona kabisa yale maradhi yangu na kuanza kujilaumu kuwa nilikuwa nikipoteza muda wangu pale kitandani.
Sasa nilikuwa na hakika kuwa Amanda alikuwa ameniuza tena kwa bei ya rejareja isiyokuwa na majuto yoyote katika nafsi yake na kwa kweli sikutaka haraka kuamini vile. Wale wanajeshi huku wakiwa wameongozana na Amanda wakazitupa hatua zao kwa tahadhari huku wakitembea kikakamavu katika namna iliyonipelekea niweze kuzisikia vizuri buti zao ngumu miguuni namna zilivyofanikiwa kwa kiasi kikubwa kuitetemesha sakafu ya kile chumba. Nilitamani nilitupe kando lile blanketi nililojifunika kisha nikurupuke na kuanza kutimua mbio. Lakini hilo halikuwezekana kwa kuwa muda haukuniruhusu kufanya vile na wale watu walikuwa ni kama tayari wameshanifikia pale kitandani nilipolala. Mbali na vile pale kitandani sikuwa na nguo hata moja ya kunisitiri, hali iliyonipelekea sasa niamini kuwa Amanda alikuwa amenifanyia hila kwa kunivua nguo ili hata zikitokea purukushani zozote nisiweze kukimbia loh!.
Wale wanajeshi walipofika pale kitandani nilipolala wakajigawa katika mtindo wa kukizunguka kile kitanda. Mmoja akaja na kusimama nyuma yangu, mwingine upande wa kushoto na mwingine upande wa kulia. Amanda yeye akasimama mbele ya kile kitanda huku akinitazama kwa tabasamu la kinafiki lenye tafsiri ya ushindi. Nikiwa nimeshikwa na mshtuko wa hali ya juu, nikayatembeza macho yangu taratibu nikizikagua vizuri sura za wale watu kisha nikaweka kituo nikimtazama Amanda huku nikijitahidi kuumeza mshtuko niliokuwa nao moyoni. Amanda akanitazama na baada ya kitambo kifupi akavunja ukimya akiniambia.
“Jean ne tʼenfait pas cʼest sont mes amis, ils vont tˊaider”. Jean, hawa ni marafiki zangu, watakusaidia. Maelezo ya Amanda yenye kila namna ya chuki na usaliti yakanipelekea nitabasamu kidogo kujifariji na kuitowesha hasira iliyokuwa imeanza kuchemka moyoni mwangu na hapo nikamuona yule mwanajeshi wa upande wa kulia akisogea kidogo pale kitandani huku tabasamu la kifidhuli likijitokeza taratibu usoni mwake na mikono yake ameishikamanisha mbele yake. Kwa heshima akajitambulisha.
“Je mʼappelle Major Pascal Karibwami, je suis contant de te voir ici”. Naitwa Meja Pascal Karibwami, nafurahi sana kukuona hapa. Yule mwanajeshi akaongea kwa kujiamini huku akinipa heshima zote utasema mimi nilikuwa mkuu wake wa kazi. Alikuwa mwanaume mrefu na mweusi kama mjaruo. Hali iliyonipelekea niyaone vizuri macho na meno yake meupe wakati alipokuwa akitabasamu. Alipomaliza kujitambulisha mwenzake naye akasogea na kujitambulisha kwa nidhamu zote hali iliyonipelekea nishikwe na mduwao.
“Staff Surgent Anatole Nkunda”
Wakati yule mwanajeshi mwingine akijitambulisha nikageuka na kumtazama na sura yake ikanitia mashaka. Macho yake yalikuwa makubwa yenye uchovu lakini yanayoonya. Uso wake mrefu ulikuwa umetulia kama maji ya kisima na ijapokuwa alikuwa amevaa kofia ya bereti lakini kofia ile ya kiafande ilikuwa imetuama vizuri kwenye upara wake unaowaka na usiokuwa na unywele hata mmoja. Isipokuwa mishipa ya damu iliyotuna na kusambaa kichwani kama mizizi ya mmea wa mhindi. Yule afande akakaza sura akinitazama utasema alikuwa akivishwa medani ya heshima na amiri jeshi mkuu. Alipomaliza kijitambulisha yule askari mwenzake aliyekuwa nyuma yangu nikamsikia naye akijitambulisha. Hata hivyo sikuweza kumuona kutokana na namna nilivyokuwa nimelala pale kitandani isipokuwa sauti yake ilikuwa nzito mno.
“Corporal Adolphe Sahinguvu”
“Je ne, veux pas lʼaide de qui que ça sole”. Sihitaji msaada wa mtu yeyote. Nikaongea kwa jazba hata hivyo wale maafande wakaishia kuangua kicheko cha dharau ambacho kilinishangaza sana na kunitia hasira. Kicheko kile kilipokoma nikamsikia yule mwanajeshi mkubwa kwa cheo aliyejitambulisha kwangu kama Major Pascal Karibwami akiniuliza kwa utulivu.
“Comment ça va camarade?”. Vipi komredi unajisikiaje?.
“Je ne me sens pas bien, et je suis trés enfamé”. Sijisikii vizuri na nasikia njaa sana. Nikaongea kwa utulivu huku nikianza kuhisi usalama wangu ulikuwa ukielekea kudorora mbele ya uwepo wa watu wale. Ingawa taratibu za kijasusi zilikuwa zikinionya kutomuamini mtu yeyote katika mazingira yoyote lakini kwa kweli sikuwa nimetarajia kabisa kuwa Amanda angekuja kunisaliti tena katika mazingira kama yale. Hata hivyo nilijionya kuwa ukorofi wowote ambao ningeamua kuuleta katika mazingira yale usingenisaidia kitu kwani afya yangu bado ilikuwa dhaifu. Hivyo nikaishia kumeza funda kubwa la mate kuipoza hasira yangu kifuani.
“On ne tʼa pas encore donner à manger?”. Hujapewa chakula?. Major Pascal Karibwami akaniuliza kwa utulivu huku akitabasamu. Ingawa nilikuwa na hakika kuwa alikuwa akinidhihaki hata hivyo ilinibidi nimjibu.
“Oui”. Ndiyo.
“Ne tʼenfaite pas, nous allons te donner à manger”. Usijali sisi tutakupa chakula kingi na utashiba vizuri. Meja Pascal Karibwami akaniambia huku akiendelea kutabasamu na nilipomtazama usoni nikashtushwa na tabasamu lake la kinyama. Hali iliyonipelekea nizidi kushikwa na mashaka juu ya hatima yangu.
“Qui etes des qui?”. Nyinyi ni akina nani?. Nikawauliza wale watu huku nikifoka kwa kitendo kile cha kuchezewa akili yangu kama mtoto mdogo.
“Ne te derange pas, dans peu de temps tu vas nous connaître”. Ondoa shaka, muda siyo mrefu utatufahamu vizuri sisi ni akina nani. Meja Pascal Karibwami akaniambia huku akikenua meno yake na kunitazama kwa furaha. Alipoyatoa macho yake kwangu akayatembeza taratibu akimtazama Amanda pamoja na wale askari wenzake kisha akayarudisha tena pale kitandani nilipolala na kuniambia kwa sauti tulivu lakini yenye kumaanisha.
“Nous venons te prendre camarade”. Tumekuja kukuchukua komredi. Maelezo ya Meja Pascal Karibwami yakanipelekea nishikwe na mshangao huku nikishindwa kuelewa kuwa alikuwa amenuia nini. Hatimaye nikamuuliza huku nikiwa nimeanza kushikwa na wasiwasi juu ya kauli ile.
“Vous mʼamainer où?”. Mnanipeleka wapi?. Swali langu likawapelekea wale maafande wote mle ndani waangue kicheko kana kwamba nilikuwa nimeongea kitu cha kipuuzi na cha kuchekesha sana. Wakati wale watu wakiendelea kucheka nikiwa pale kitandani nikamtazama Amanda na kitendo cha kumuona akiungana na wale watu kunicheka kikanitia gadhabu. Kile kicheko chao kilipofika kikomo Meja Pascal Karibwami akaniambia kwa hadhari huku akinitazama.
“Nous tʼamainons à lʼhospitale parceque votre santé ne pas bonne”. Tunakupeleka hospitali kwani afya yako siyo nzuri.
“Qui vous a dit que je veux lʼaide dʼaller à lʼhospitale?”. Nani aliyewaambia kuwa nahitaji msaada wa kupelekwa hospitali?. Nikamuuliza kwa jazba yule mtu huku nimeshikwa na hasira kwa kudhihakiwa.
“Si tu es bien, pourquoi maintenant tu dors ice de dans comme une femme aceinte?”. Sasa kama wewe ni mzima kwanini unalala lala humu ndani kama mama mjamzito?. Meja Pascal Karibwami akaniuliza na kuwapelekea wale watu wote mle ndani waangue kicheko.
Kwa kweli nilishikwa na hasira hasa nilipokumbuka namna nilivyomuokoa Amanda kutoka katika ile mikono ya wale watekaji kule njiani msituni.
“Je ne veux pas lʼaide de qui que ça sole”. Sihitaji msaada wa mtu yoyote. Nikaongea kwa msisitizo na hapo nikamsikia yule mwanajeshi aliyekuwa nyuma yangu akiniambia kwa kufoka.
“Arreter de sʼopposer toi singe!”. Acha ubishi wewe tumbili!. Hali ile ikanipelekea nimuulize Amanda kwa hasira.
“Amanda, quʼest-ce quʼevolue ici de dans, je nʼarrive pas à te comprendre?”. Amanda, nini kinachoendelea humu ndani, mbona sikuelewi?.
“Sans doute tu es troublé Jean, qui est Amanda?”. Bila shaka umechanganyikiwa Jean, Amanda ndiyo nani?. Amanda akanimbia huku akiangua kicheko cha dhihaka.
“Cʼest toi!”. Si ni wewe!. Nikamwambia Amanda kwa mshangao huku nikijihisi kuchanganyikiwa kwa kutumbukia katika mkasa ule wa hatari. Meja Pascal Karibwami akaangua kicheko hafifu kabla ya kuniambia.
“Cʼest pour quoi je te dis que nous venons tʼamainer à lʼhopital, votre inteligence nʼest pas bonne, tu vois tu es entré de baptiser les gents le noms qui ne sont pas les leur!”. Ndiyo maana nikamwambia kuwa tumekuja kukuchukua tukupeleke hospitali. Akili yako siyo nzuri, huoni unavyowabatiza watu majina yasiyo yao?.
“Je ne vous comprend pas?”. Mbona siwaelewi?. Nikawauliza wale watu kwa hasira hata hivyo swali langu likawapelekea wale watu waangue tena kicheko wakinidhihaki. Kisha Meja Pascal Karibwami akaniambia kwa utulivu huku akitabasamu.
“Ne tʼenfait pas camarade, nous allons te faire comprendre”. Usihofu komredi, tutakuelewesha. Kisha nikamuona Meja Pascal Karibwami akiwafanyia ishara fulani ya kichwa wale askari wake hali iliyonipelekea nihisi jambo baya lilikuwa likielekeza kutekelezwa juu yangu.
Muda uleule lile blanketi nililokuwa nimefunikwa pale kitandani likaondoshwa kwa kasi na yule mwanajeshi aliyekuwa amesimama kushoto kwangu. Nilijitahidi kulizuia lakini kutokana na udhaifu wa mwili wangu sikufanikiwa. Hivyo nikajikuta nimebaki uchi kama nilivyozaliwa pale kitandani. Muda siyo mrefu mara nikamuona yule mwanajeshi mwenye cheo cha Koplo ambaye hapo awali alikuwa amejitambulisha kwangu kama Koplo Adolphe Sahinguvu, akizunguka kwenye kile kitanda na kunishika miguu. Kisha akanivuta chini kwa nguvu zake zote hali iliyonipelekea nitue pale chini sakafuni kwa matako na hivyo kupelekea maumivu makali yanisambae mwili mzima. Nilijitahidi kujitetea lakini ilikuwa kazi bure kwani mapigo ya mateke mgongoni na mabegani mwangu yakazidi kunipelekea niishiwe na nguvu kizunguzungu kikanishika na kunipelekea nijihisi kutaka kutapika.
Wale watu waliporidhika kuwa kile kipigo kilikuwa kimenilegeza kiasi cha kutosha, wakaamua kuniacha huku nikihema ovyo. Damu sasa ilikuwa ikinitoka puani, sehemu ya juu ya jicho langu la kulia ilikuwa imevimba na kuchanika huku ikivuja damu taratibu. Mdomo wangu nao ulikuwa umechanika sehemu yake ya chini na hivyo kunipelekea nihisi ladha nyepesi ya chumvi ya damu iliyokuwa ikivuja kwenye jeraha lile. Ikafikia hatua nikawa siwezi kuona vizuri mbele yangu. Nikiwa pale chini sijielewi vizuri baada ya kuleweshwa na ule mkong’oto wa nguvu kutoka kwa wale watu mara kwa shida nikamuona yule askari mwenye cheo cha chini kabisa kuliko wenzake akanisogelea pale nilipokuwa na kuanza kunifunga kamba mikononi na miguuni. Sikuweza kuleta upinzani wowote kutokana na hali yangu ya kiafya kuzidi kuzorota. Yule askari alipomaliza kunifunga zile kamba akaambiwa neno fulani la kirundi na yule Meja Pascal Karibwami ambalo muda mfupi baadaye nilifahamu vizuri maana ya neno lile kupitia vitendo. Kwani muda uleule yule mwanajeshi aliyenifunga zile kamba akanizoa pale chini sakafuni mzegamzega na kujitwisha begani huku nikiwa uchi wa mnyama bila nguo yoyote ya kujisitiri mwilini.
Huku nikiwa ninaning’inia begani kwa yule askari muda uleule safari ya kutoka mle ndani ikaanza huku yule askari aliyenibeba akitangulia mbele. Nyuma akafuatia Amanda na wale wanajeshi wengine. Hali yangu kiafya ilikuwa mbaya sana hata hivyo nilijitahidi kuituliza akili yangu na kuyachunguza vizuri mazingira yale.
Mara tu tulipotoka kwenye kile chumba tukajikuta kwenye korido pana kiasi iliyokuwa ikitazamana na milango mitatu upande wa kushoto ambayo kwa wakati ule yote ilikuwa imefungwa. Upande wa kulia wa ile korido kulikuwa na dirisha kubwa la kioo lililofunikwa kwa pazia refu na mwisho wa dirisha lile kulikuwa na mlango uliofungwa...ITAENDELEA