RIWAYA: UFUKWE WA MADAGASCAR
SEHEMU: 26
Mtunzi:Kelvin Mponda
“Hapana sikurudi nyumbani kwani hata kama ningerudi nyumbani bado nisingeweza kupata usingizi kutokana na hali yenyewe ya mambo ilivyokuwa. Kutoka nyumbani kwangu hadi hapa ofisini umbali wake siyo mrefu sana hivyo nikawa nimepata wazo la kupenyapenya mitaani na kuja hapa.
“Walinzi wa hapa ofisini waliponiona waliingiwa na wasiwasi hata hivyo niliwatoa hofu kwa kuwaambia kuwa kulikuwa na jambo la dharura lililokuwa limejitokeza na hivyo nilikuwa nimelazimika kufika hapa usiku ili kulifanyia kazi. Sikukabiliana na upinzani wowote hivyo nikafungua ofisi na kuingia ndani ndiyo nikaketi na kuandika ile Fax na hatimaye kuituma makao makuu ya idara yetu ya ujasusi jijini Dar es Salaam”
Maelezo ya Hidaya yakawa yameniingia vizuri na kwa mara nyingine nikajikuta nikimpongeza kwa kuwa msichana jasiri, mzalendo na mwenye kujali.
“Ulitoa taarifa kwa vyombo vya usalama vya hapa Burundi?”. Nikamuuliza Hidaya kwa udadisi.
“Hapana! kwani baada ya kufikiri sana niliona kuwa hilo lisingekuwa jambo jema”
“Kwa nini?”
“Jaribio hili la mapinduzi ya kijeshi hapa nchini Burundi limepelekea hali ya kutoaminiana sana tena kwa baadhi ya maafisa katika vyombo vya usalama. Hivyo niliona kuwa taarifa kama hii ya kutekwa kwa Balozi Adam Mwambapa huwenda kwa baadhi ya maafisa usalama wa hapa wangeipa uzito unaostahili huku wengine wakihisi kuwa ni kama niliyekuwa nimeenda kutoa taarifa za uchochezi baina ya nchi na nchi au baina ya makundi hasimu. Vilevile sikutaka serikali ya Burundi ijihusishe kwa namna yeyote katika suala hili kwa kigezo kuwa katika mazingira nisiyoyaelewa huwenda ushahidi wa tukio hili la kutekwa kwa Balozi Adam Mwambapa ungetoweshwa na vyanzo vyake vyote muhimu vya upelelezi kufutiliwa mbali na hivyo kazi yote kuwa ngumu”. Hidaya akaweka kituo baada ya kumaliza kutoa maelezo yake na kwa kweli alikuwa amenifurahisha sana kiasi cha kulipelekea tabasamu langu jepesi lichomoze usoni taratibu kama miale ya jua la asubuhi.
“Niseme kuwa umefanya uamuzi mzuri wa busara kwa kuto kutoa taarifa hizi kwa chombo chochote cha usalama cha hapa nchini Burundi kwani hata Chifu amesisitiza kuwa jambo hili lifanyike kwa weledi na usiri wa hali ya juu. Vinginevyo serikali yetu inaweza kulaumiwa kwa kutokuwa makini na usalama wa maafisa wake”. Nikasisitiza kisha baada ya kufikicha macho kidogo nikamuuliza Hidaya.
“Kuna mtu mwingine yeyote anayefahamu habari hizi za kutekwa kwa Balozi Adam Mwambapa katika ofisi yenu?”
“Hapana nimelazimika kutengeneza taarifa ya uongo inayotanabaisha kuwa Balozi Adam Mwambapa amepata dharura ya kikazi hivyo hatokuwepo hapa ofisini kwa siku kadhaa. Sikupenda mtu yeyote wa hapa ofisini afahamu juu ya suala hili katika hatua ya awali kama hii”. Hidaya akaniambia kwa hakika pasina kuujutia uamuzi wake na kwa kweli hata mimi nilikuwa nimependezwa na uamuzi wake.
“Chifu analifahamu hilo?”. Nikamuuliza Hidaya katika namna ya kutafuta uhalali
“Wazo hili limetoka kwake na nimekuwa nikimfahamisha kwa ukaribu kila kitu kinachoendelea hapa nchini Burundi tangu kutokea kwa jaribio hili la mapinduzi ya kijeshi”
“Umefanya vyema sana”. Nikamwambia Hidaya kisha nikakohoa kidogo kusafisha koo kabla ya kuendelea.
“Niseme tukio la kutekwa kwa Balozi wetu Adam Mwambapa limenishtua na kunishangaza sana kwani hadi sasa nikifikiria bado sioni sababu yoyote walau ya kuhisi tu inayoweza kuhalalisha tukio la kinyama kama hili”
“Hata mimi nimeshindwa kuelewa kinachoendelea Tibba”. Hidaya akasisitiza huku akitikisa kichwa chake katika namna ya kuonesha kusikitishwa na tukio lile.
“Nitajitahidi kufanya kila liwezekanalo katika kuhakikisha kuwa Balozi wetu Adam Mwambapa anapatikana na yeyote aliyehusika na kitendo hiki cha kiharamia ataijutia nafsi yake”. Maelezo yangu yalikuwa ya hakika na kwa namna moja au nyingine yalionekana kumfurahisha sana Hidaya kiasi cha kumpelekea atabasamu na uzuri wake kujidhihirisha vizuri usoni mwake.
“Kuwa mwangalifu sana Tibba kwani huwenda hali ikawa tofauti kabisa na vile unavyofikiria”. Hidaya akaniambia na kupitia sauti yake tulivu ya kike niliweza kuhisi huruma aliyokuwa nayo juu yangu. Hata hivyo nilimtoa wasiwasi kwa kumwambia.
“Ondoa shaka Hidaya naamini kuwa Mungu atanisaidia”. Kitambo kifupi cha ukimya kikapita huku kila mmoja akionekana kuzama kwenye tafakuri na wakati hali ile ikiendelea mara nikakumbuka kumuuliza Hidaya.
“Kuna mtu yeyote aliyefanikiwa kufika nyumbani kwa Balozi Adam Mwambapa baada ya tukio la kutekwa kwake?”
“Hakuna mtu yeyote aliyefika kwani ni kama nilivyokueleza kuwa hakuna mtu mwingine anayefahamu juu ya tukio hili hapa ofisini isipokuwa mimi peke yangu na Balozi Adam Mwambapa huko alipo. Hidaya akaongea kwa msisitizo na kwa hakika nilimuelewa vizuri. Ukimya kiasi ukapita baina yetu huku kila mmoja akionekana kuzama tena katika fikra zake na kwa kweli tukio la kutekwa kwa Balozi Adam Mwambapa lilikuwa limenishangaza sana.
Kwa namna moja au nyingine niliamini kuwa watu hao ambao walihusika katika kumteka Balozi Adam Mwambapa walikuwa ni watu wenye uwezo na maarifa ya juu ya medani za kijeshi kwa vile Balozi Adam Mwambapa alikuwa ni kiongozi mstaafu wa jeshi mwenye maarifa ya juu sana ya mapambano. Ingawa bado sikuweza kuhisi lengo la watekaji hao.
Mwanzoni nilihisi kuwa huwenda watekaji hao walikuwa na lengo la kujiingizia fedha haramu endapo wangejitokeza na kudai malipo kwa ajili ya kumwachia Balozi Adam Mwambapa. Lakini ni kitendo cha kuona kuwa muda unaenda pasipo watekaji hao kujitokeza na kudai fedha kilizidi kunitia mashaka. Ukimya ule ulipokuwa mbioni kushika hatamu Hidaya akaibua hoja.
“Umefikia kwenye hoteli gani hapa jijini Bujumbura?’. Swali la Hidaya likanipelekea nitabasamu kidogo kabla ya kuvunja ukimya.
“Mwenyeji wangu ameniambia kuwa anakaa nyumba namba 37 kwenye jengo la shirika la nyumba la taifa kando ya barabara ya Boulevard de Iʾndependence. Nyuma ya uwanja wa mpira wa miguu wa Prince Rwegasore Stadium hapa jijini Bujumbura”
“Mh! mara hii tu ushapata mwenyeji wa kufikia kwenye jiji usilolijua?”. Hidaya akaniuliza huku akiangua kicheko cha kimbea na kuubinua mdomo wake.
“Mwenyeji wangu anaitwa Veronica. Toto zuri la kirundi lenye vigezo vyote vya kuupoza vyema mtima wangu”. Nikaongea kwa utulivu huku nikiliruhusu tabasamu hafifu kuchanua usoni mwangu. Hidaya akaangua kicheko hafifu cha udaku huku akipiga makofi dhaifu ya kimbea.
“Mh! Tibba kwa mambo hayo tu mimi sikuwezi. Najua mtoto wa watu atakuwa amebabaishwa na uzuri wako tu vinginevyo huna lolote zaidi ya kumdanganya”
“Sasa Hidaya nifanyeje wakati mzabuni wa kunipikia chakula kitamu cha kirundi na kunipa huduma nyingine za kimwili na za kiroho keshashinda tenda hiyo moyoni mwangu tena kwa kiwango cha juu”. Nikaongea kwa utulivu huku nikiangua kicheko hafifu na bila shaka Hidaya nilikuwa nimemfikisha mahala pake kwani suala la utani ilikuwa hulka yake hali iliyompelekea azidishe kicheko huku mkono wake mmoja shavuni na mdomo wake kuachama kwa mshangao.
“Mh! Tibba kweli umeshindikana bora utafute mmoja wa kuoa utakayetulia naye kama mimi ya kaka yako. Tambua kuwa umri unaenda huo!”. Hidaya akaniambia huku machozi ya kicheko yakikaribia kubisha hodi machoni mwake.
“Kwani kuoa mwisho miaka mingapi wenzangu mliopo kwenye ndoa?”. Nikamchombeza tena utani.
“Shauri yako!. Wewe kazi yako kuwachezea warembo na kuwaacha kwenye mataa. Yaani kama ndiyo ningekuwa mimi wala nisingekubaliana na huo upuuzi wako”. Hidaya akaongea huku akiyabetua mabega yake.
“Mh! jamani kwani nimemdanganya au tumekubaliana. Kama atanifaa basi huwenda nikatangaza nia kabisa na wewe ukiwa kama wifi yake mwandamizi basi naamini kuwa hapata haribika jambo”. Maneno yangu yakamuacha Hidaya akiendelea kuangua kicheko cha udaku huku kichwani nikianza kupanga namna ya kuanza rasmi harakati zangu pale jijini Bujumbura. Kile kicheko cha Hidaya kilipokuwa mbioni kukoma akageuka na kuniambia.
“Chifu aliniambia nikuandalie sehemu nzuri ya malazi pamoja na silaha”
“Wala usisumbuke Hidaya mimi nitalala kwa mrembo Veronica na kuhusu silaha tayari nimekwishaipata moja ya kuanzia kazi”. Maelezo yangu yakapeleka mshangao wa aina yake usoni kwa Hidaya na hapo kile kicheko chake kikakoma kabisa.
“Khe! Hiyo silaha umeipata wapi?”. Hidaya akaniuliza huku kanitumbulia macho kwa mshangao.
“Nimeipata huko njiani nilipotoka”. Jibu langu likatosha kabisa kumfahamisha Hidaya nini nilichokuwa nikimaanisha hivyo haraka akamezea na kubadili mada.
“Sasa ungependa nikusaidie nini kwa sasa?”
“Nahitaji usafiri wa uhakika usiokuwa na rekodi ya kesi yoyote ya barabarani”. Nikaongea kwa utulivu huku nikimtazama Hidaya usoni.
“Kuhusu hilo ondoa shaka. Nyuma ya hili jengo kuna gari moja jeusi aina ya Peugeot 504. Utalitumia kwa muda wote utakao kuwa hapa jijini Bujumbura. Chifu alinifahamisha juu ya hilo mapema wakati tulipozungumza kwa simu hivyo tayari nilikuwa nimekuandalia gari”. Hidaya akaongea kwa utulivu.
“Nashukuru sana Hidaya”
“Sema kingine” Hidaya akaniambia huku akinitazama kwa shauku.
“Ofisi ya Balozi Adam Mwambapa ipo wapi katika hili jengo?’’. Nikamuuliza Hidaya huku nikiitazama saa yangu ya mkononi.
“Nje ya chumba hiki kuna korido. Ukitoka nje upande wa kushoto mwisho wa korido hiyo utaziona ngazi. Panda hizo ngazi kuelekea ghorofa ya pili na utakapomaliza kupanda hizo ngazi utajikuta ukitazamana na korido pana inayotazamana na milango ya vyumba vya ofisi mbalimbali. Wewe nyoosha moja kwa moja hadi mwisho wa hiyo korido utauona mlango mkubwa wa kijivu. Mlango huo ndiyo wa kuelekea ofisi ya Balozi Adam Mwambapa na juu yake kuna kibao kidogo cheusi chenye maandishi meupe kinachotanabaisha cheo chake”. Maelezo ya Hidaya nikayashika vyema hivyo nikasogeza kiti changu nyuma na kusimama.
“Ofisi yake ipo wazi?”. Nikamuuliza na hapo nikamuona Hidaya haraka akijipapasa mifukoni na baada ya muda mfupi akawa amepata funguo moja na kunikabidhi mkononi. Nikaipokea ile funguo na kuitia mfukoni kabla ya kumuuliza.
“Maafisa wenzako hawawezi kunisumbua?”
“Usijali nitawataarifu kuwa wewe ni fundi wa mashine ya kudurufu iliyopata hitilafu ofisini kwa Balozi”. Uongo wa Hidaya ukanifanya niliruhusu tabasamu hafifu kuchomoza usoni mwangu kwani Hidaya alikuwa msichana mjanja sana na mwerevu.
“Ngoja nikachunguze huwenda nikapata chochote cha kunisaidia”. Hatimaye nikamwambia Hidaya huku nikimkonyeza kichokozi tukio lililompelekea aangue kicheko kama ilivyokuwa kawaida yake.
“Usijali Tibba uwanja sasa ni wako unaweza kucheza utakavyo. Ukihitaji msaada wowote usisite kunijulisha mimi nitakuwa pale mapokezi nikisaidiana na wenzangu kuhudumia watu”. Hidaya akaniambia huku na yeye akisogeza kiti chake nyuma na kusimama. Nilipousukuma ule mlango na kutoka nje Hidaya tayari alikuwa nyuma yangu akanipiga ngumi hafifu ya kichokozi mgongoni kisha akashika uelekeo wa upande wa kulia kuelekea ile sehemu ya mapokezi. Nikasimama kidogo nikitabasamu huku nikimtazama Hidaya namna alivyokuwa akitembea kwa mikogo kisha nikaanza kuzitupa hatua zangu taratibu kuelekea mwisho wa ile korido sehemu kulipokuwa na ngazi za kupanda kuelekea ghorofa ya juu ya lile jengo.
Nilitembea kwa utulivu huku mawazo mengi yakipita kichwani mwangu na nilipozifikia zile ngazi nikaanza kuzipanda na kwa kuwa nilikuwa mgeni wa mazingira yale mara kwa mara nilijikuta nikisimama na kuweka kituo nikitazama huku na kule. Baada ya muda mfupi hatimaye nikamaliza kuzipanda zile ngazi na hapo nikajikuta nikitazamana na korido pana yenye sakafu imara ya tarazo inayotazamana na milango minne. Milango miwili ilikuwa upande wa kushoto na milango miwili mingine ilikuwa upande wa kulia na mwisho wa korido ile kulikuwa na mlango mkubwa wa rangi ya kijivu.
Kabla ya kukatisha katika korido ile nikageuka na kutazama mwisho wa ngazi zile upande wa kushoto. Kupitia dirisha jembamba la kioo lililokuwa upande ule niliweza kuona mandhari tulivu ya lile jengo yaliyozungukwa na miti mirefu ya kuvutia na bustani nzuri ya maua. Vyote vikiwa ndani ya uzio wa ukuta wenye sistimu maalum ya umeme wa kuzuia wezi. Nje ya ukuta ule niliyaona majengo mengine ya ghorofa yenye nyungo za runinga na minara ya mawasiliano juu yake.
Nikiwa nimeridhika na uchunguzi wangu wa awali nikaanza kutembea taratibu nikikatisha katikati ya korido ile kuelekea kwenye ule mlango mkubwa wa kijivu uliokuwa mwisho wa ile korido. Kwa kufanya vile nikapata wasaha mzuri wa kuitazama ile milango iliyopakana na ile korido kwa upande wa kulia na kushoto. Kwa kufanya vile nikaweza kuiona ofisi ya afisa mahusiano, ofisi za afisa mkuu anayeshughulika na masuala ya vibali vya ukaaji na pasi za kusafiria pamoja na ofisi ya afisa mkaguzi kupitia utambulisho uliokuwa juu ya milango ile. Hatimaye nikaufikia ule mlango wa kijivu uliokuwa mwisho wa ile korido na kupitia kibao cheusi juu ya mlango ule chenye maandishi meupe nikatambua kuwa ile ilikuwa ni ofisi ya Balozi Adam Mwambapa kama Hidaya alivyokuwa amenielekeza hapo awali.
Nilipoufikia ule mlango nikakishika kitasa chake na kujaribu kuufungua. Ule mlango ulikuwa umefungwa hivyo sikutaka kutia ufundi mwingine badala yake nikaingiza mkono mfukoni na kuchukua ile funguo niliyopewa na Hidaya. Nilipoupachika ule ufunguo kwenye lile tundu la kitasa na kuuzungusha kabari yake ikafyatuka na hapo nikakizungusha kidogo kile kitasa na kuusukuma ule mlango kwa ndani. Ule mlango ukafunguka na hapo kwa tahadhari nikausukuma na kuingia mle ndani kabla ya kuurudishia nyuma yangu.
Taswira iliyojengeka machoni mwangu ilikuwa ni ya mandhari tulivu ya ofisi ya kisasa yenye vitu vyote muhimu. Upande wa kushoto kulikuwa na dirisha pana la kioo dirisha hilo lilikuwa limefunikwa kwa mapazia mawili marefu ya rangi ya kijivu. Nilipoyatembeza macho yangu kwa utulivu juu ya lile dirisha nikaziona picha mbili zilizotundikwa ukutani. Picha moja ilikuwa ni ya Rais wa jamhuri ya muungano wa Tanzania na picha nyingine ilikuwa ni ya Balozi Adam Mwambapa akiwa katika suti nadhifu nyeusi, shati la kijivu na tai nyeusi. Macho yake tulivu katika sura yake ya umbo duara, pua pana ya kibantu na mdomo uliozungukwa na ndevu zilizokatiwa vizuri vikiongeza ziada nyingine katika wajihi wake.
Kando ya dirisha lile kulikuwa na meza kubwa ya ofisini yenye majalada mengi juu yake. Bendera ndogo mbili, moja ya taifa la Tanzania na nyingine ya taifa la Burundi. Kitabu kidogo cha katiba ya nchi ya Tanzania. Kidau cha wino, mhuri na kichupa kidogo chenye wino mweupe wa kufutia maandishi.
Nyuma ya meza ile kulikuwa na kiti kikubwa cha ofisini yenye foronya laini na kiti kile kilikuwa kimetundikwa koti jeusi la suti. Niliendelea kuyatembeza macho yangu kwa utulivu mle ndani na upande wa kulia wa ile meza nikaliona kabati kubwa nadhifu la mbao lenye droo sita. Sakafu ya ofisi ile ilifunikwa kwa zulia maridadi jekundu huku katikati likiwa na mstari mpana wenye rangi za bendera ya taifa la Tanzania.
Upande wa kushoto kulitundikwa saa kubwa ya ukutani ya mshale na pembeni ya saa ile kulikuwa kalenda moja kubwa. Kando ya dirisha lile mle ndani kulipangwa seti moja ya makochi mazuri ya ngozi laini ya sofa yaliyoizunguka meza ya kioo yenye umbo duara na chini ya meza ile kulikuwa na magazeti na majarida kadhaa tofauti ya huko siku za nyuma. Kando ya makochi yale kulikuwa na rafu kubwa ya vitabu na majalada yaliyopangwa kwa ustadi wa hali ya juu. Kiyoyozi makini kilichokuwa mle ndani kiliendea kusambaza hewa safi.
Ofisi ilikuwa ya kistaarabu sana yenye samani za kisasa na iliyopangiliwa vizuri ama kwa hakika muonekano wake uliendana kabisa na ule wa hadhi ya ofisi ya balozi. Runinga kubwa ya ukutani iliyounganishwa na chaneli tofauti za kimataifa iliyokuwa ukutani mle ndani ilikuwa imezimwa na katika kona mbili za ile ofisi kulikuwa na maua mazuri ya asili katika vyungu vyake maalum vya udongo, kazi nzuri ya mfinyanzi.
Nikiwa nimeridhishwa na mandhari nzuri ya ofisi ile yenye hadhi ya juu taratibu nikaanza kutupa hatua zangu nikianza uchunguzi kwenye yale magazeti na majarida yaliyokuwa chini ya ile meza ya kioo mle ndani iliyozungukwa na ile seti ya makochi ya sofa. Nilipofika kwenye ile meza nikaanza kufanya upekuzi. Hata hivyo nilipomaliza upekuzi wangu sikuambulia chochote cha maana kwani yale magazeti na majarida yalikuwa ni ya kawaida kabisa tena matoleo ya siku za nyuma. Hatimaye nikaiacha sehemu ile na kuhamia kwenye ile rafu ya mbao yenye vitabu na majalada chungu mzima nikaanza kufanya upekuzi wangu kwa makini huku nikipekua kila kitabu na jalada na maeneo yote muhimu katika rafu ile. Hata hivyo nilimaliza zoezi lile pasipo kuambulia chochote cha maana kwani vile vitabu na yale majalada vilikuwa ni nyaraka za wazi za sera za mahusiano ya kimataifa. Ajenda za vikao na mikutano iliyofanyika huko siku za nyuma pamoja na masuala ya sheria za kimataifa sera na mipango.
Hatimaye nikaiacha ile rafu na kuelekea kwenye lile kabati lenye droo sita lililokuwa upande wa kushoto wa ile ofisi. Nilipofika nikaanza kuzifungua zile droo moja baada ya nyingine na kuanza kufanya upekuzi makini na kwa vile droo zile hazikuwa na vizuizi vyovyote kazi ilikuwa rahisi tu. Hata hivyo ndani ya droo zile hapakuwa na kitu chochote cha maana zaidi ya picha za Balozi Adam Mwambapa akiwa na viongozi mbalimbali wa kitaifa wa Burundi. Picha zile zilikuwa zimepigwa katika maeneo tofauti yenye hadhi ya juu baadhi kwenye hoteli za kifahari na nyingine Ikulu ya Burundi. Hatimaye nikazifunga zile droo na kuhamishia upekuzi wangu kwenye ile meza ya ofisini.
Nilianza upekuzi kwa kupekua jalada moja baada ya jingine juu ya meza ile lakini pia sikuambulia kitu chochote katika ukomo wa upekuzi wangu hivyo nikahamishia upekuzi wangu kwenye droo tatu za meza ile ya ofisini. Mle ndani ya droo sikuambulia kitu chochote cha maana zaidi ya pini za majalada, gundi ya maji, kalamu mbalimbali za wino na karatasi mbili za kaboni zilizokuwa zimekunjwa vizuri na kuhifadhiwa vyema ndani ya bahasha ya kaki. Hakukuwa na kitu kingine cha maana ambacho kingeweza kunisaidia katika harakati zangu hivyo hatimaye nikazifunga zile droo kama nilivyozikuta. Kisha kwa makini nikayapanga vyema yale majalada pale juu ya meza huku akili yangu ikifikiria upya juu ya nini cha kufanya.
Nikiwa katika hali ile mara nikapata wazo fulani wakati nilipolitazama lile koti la suti lililotundikwa kwenye kile kiti cha ofisini. Nikasogea karibu na kulichukua lile koti na kuanza kulipekua mifukoni na wakati nikifanya vile pua yangu ikajikuta ikisumbuliwa kidogo na harufu nzuri ya manukato ya gharama yaliyopuliziwa kwenye koti lile. Lilikuwa ni koti zuri la suti lenye vifungo vinne la brandi ya daraja la kwanza kwa ubora na sikuwa na mashaka yoyote kuwa koti lile la suti lilikuwa ni la Balozi Adam Mwambapa. Hata hivyo nilipomaliza upekuzi wangu sikuambulia kitu chochote cha maana zaidi ya pakiti moja ya sigara aina ya Marlboro iliyokuwa na sigara mbili ndani yake pamoja na kibiriti kimoja cha gesi na hapo nikahitimisha kuwa Balozi Adam Mwambapa alikuwa mvutaji wa sigara. Hatimaye nikalirudishia lile koti la suti mahala pake huku akili yangu ikianza kuhisi kushindwa.
Mwishowe nikasimama na kuitia mikono yangu mifukoni kwa utulivu huku nikianza upya kuishughulisha akili yangu. Pembeni ya ile meza ya ofisini chini yake kulikuwa na mashine ndogo ya digital ya kurudufu, printer, scanner na mashine moja ya fax. Nilijaribu kuifanyia upekuzi mashine moja baada ya nyingine nikijaribu kupekua karatasi zilizokuwa ndani yake nikichunguza kama ningeweza kupata kitu chochote muhimu cha kunisaidia. Sikupata kitu chochote cha kunisaidia na kwa kutaka kujiridhisha zaidi nikaiwasha ile kompyuta ya pale mezani ili kuchunguza kama kungekuwa na nyaraka zozote zilizokuwa zimefanyiwa kazi kupitia ile mashine ya kurudufu, printer, scanner na ile mashine ya fax. Hata hivyo jitihada zangu ziligonga mwamba kwani ile kompyuta ilikuwa imefungwa kwa password inayofahamika na mtumiaji pekee wa ile kompyuta ambaye bila shaka alikuwa ni Balozi Adam Mwambapa. Nikaanza kuhisi kuwa upekuzi wangu ulikuwa hauelekei kuniletea manufaa yoyote hivyo nikaizima ile kompyuta na kuanza kutembeatembea mle ndani katika namna ya kufikiri zaidi nini cha kufanya.
Nikiwa katika hali ile mara wazo fulani likawa limenijia kichwani baada ya kuikumbuka ile simu ya mezani iliyokuwa pale juu ya ile meza ya ofisini mle ndani. Nilipoikaribia ile meza na kuichunguza ile simu kwa utulivu nikagundua kuwa mfumo wa mawasiliano wa ile simu ulikuwa ni ule wa kizamani unaotumia sistimu ya Landline. Hali ile ikanipa matumaini hivyo nikakichukua kiwambo cha ile simu na kukiweka sikioni katika namna ya kujaribu kama ile simu ilikuwa ikitumika au lah!. Kwa kufanya vile nikagundua kuwa ile simu bado ilikuwa ikitumika.
Wakati nilipokuwa nikikirudisha kile kiwambo cha simu mahala pake ghafla nikashtuka baada ya kuuona ule mlango wa ile ofisi ukifunguliwa. Tukio lile likapelekea haraka niupeleke mkono wangu mafichoni kuikamata bastola yangu lakini kitendo cha kumuona Hidaya akiingia mle ndani kikabadili dhamira yangu na hapo nikahitimisha kwa kuweka kile kiwambo cha simu mahala pake huku uso wangu ukitengeneza tabasamu la kirafiki...ITAENDELEA IJUMAA.