Riwaya: Nitakupata tu

Riwaya: Nitakupata tu

NITAKUPATA TU

SEHEMU YA 036

ILIPOISHIA.. alikuwa akicheka kimoyomoyo. Akicheka baada ya kupewa kazi ya kumtafuta muuaji, huku muuaji akiwa ni yeye mwenyewe. Je nini kitaendelea? Shuka nayo.

******

Alitembea sasa akitaka kufanya haraka katiks kulimaliza hili. Suresh, Jimmy na Mwamvita kisha teddy sambamba na Beni Bomphe wote lazima waondoke katika uso wa dunia. Sasa alikuwa huru kuifanyakazi yake. Sasa alikuwa huru kufanya kile ambacho alikuwa akikifanya kwa kificho. Mbinu ya kuwasafirisha wasichana wale watatu kilikuwa kitu sawa kabisa. Hii ili saidia kulificha hili suala mpaka sasa. Idara ya ujasusi kushindwa kupata fununu za nani muuaji lilikuwa jambo muhimu sana katika kazi yake. Rais akitaka kuyaomba mashirika ya kijasusi kuja kusaidia katika sakati hili, hilo pia lilimpa tabasamu, tabasamu la pongezi kwa kuwa ameifanya kazi hii katika weledi mkubwa. Kufanikiwa kuizidi maarifa idara ya kijasusi Tanzania halikuwa jambo dogo. Kwani hakuna ambaye hawajui hawa watu. Akaliacha eneo la masaki katika namna ya kufurahi. Kwa mara ya kwanza akaona kuna umuhimu wa kurudi nyumbani kwake. Nyumba ambayo aliisusa katika kipindi chote alichokuwa akitafutwa. Leo alitaka akauangalie mzigo wake, mzigo ambao ndio unasababisha teddy kuufanya usaliti. Muda wote alitembea akiomba Mungu aipate ruhusa ya kupekua nyumba zote ambazo zilimilikiwa na waziri mkuu. Kuipata ruhusa hiyo itamfanya kukamilisha kazi aliyopewa katika wakati ule alioomba kupewa.

******

Baada ya kutoka pale coco beach, teddy alienda moja kwa moja mpaka nyumbani kwake kinondoni. Aliikuta nyumba ikiwa kwenye mabadiliko makubwa. Ilionyesha wana usalama walipiga kambi hapo na kuipekuwa nyumba yao nje ndani. Kila kitu kilikuwa katika mpangili0 wake ule ule lakini vikionyesha kupekuliwa katika umakini wa hali ya juu. Teddy akasimama hapo kwa muda akitizama hiki na kile. Akili yake ilikuwa akiufikiria mzigo uliopotea. Licha ya kujua umechukuliwa na Masimba lakini hakuwahi kujua ni wapi ambapo masimba aliuficha mzigo ule wa mamilioni ya shilingi. Tamaa ya pesa ikamuingia, akaona ulikuwa ni wakati wa kuutafuta ule mzigo. Alikuwa na uhakika wa kuwepo mle ndani ama kule ambako alipelekwa wakati alipopoteza fahamu. Akairuhusu miguu yake kuingia kila chumba na kila sehemu za siri ambazo huwa wanatumia kuhifadhi vitu vyao. Tamaa ya pesa ilikuwa imeshamuingia mtoto huyu wa kipare. Hakuwaza tena mapenzi wala pesa, hakuwaza mipango yao ya baadae alichokiwaza ni ule mzigo. Mzigo ambao ulimfanya au na yeye kunusurika kuuawa mara kadhaa. Alipekuwa na kutafuta kila sehemu lakini hakupata kitu, hakupata mzigo wala kitu chochote. Akarudi chumbani akionyesha kuwaza hili na lile. Mishipa ya hasira bado haikuondoka usoni mwake. Chuki dhidi ya masimba ikaongezeka zaidi na zaidi. Alitamani kuiruhusu risasi kukipasua kichwa chake pale ambapo angefanikiwa kumuona. Baada ya kuwaza sana akaona ajimwagie maji kwanza ili akitoka aelekee kule alipoamkia akaendelee kuutafuta mzigo. Yote hayo aliyawaza akiwa anajua masimba bado ni anarafutwa. Hakujua kile kilichotokea muda mfupi uliopita. Akayatoa mavazi yake na kubaki kama alivyozaliwa. Akapiga hatua mpaka bafuni. Akafungulia maji na kuyaacha yamwagikie mwilini. Wakati maji ya kizidi kumpa uhueni kumbukumbu juu ya kilichotokea usiku wa jana ikaanza kujirudia. Mauaji ya mama wa Asteria kwa kutega bomu kwenye nyumba yake, ulikuwa mpango ambao ulipangwa afe pamoja na Masimba. Ni yeye aliyetoa taarifa kwa Jimmy kuhusu safari ya masimba nyumbani kwa mama wa Asteria. Kilichotokea mpaka masimba kupona hakukijua. Alipowaza tukio la kusalitiwa na wenzake kisha kupigwa kichwani na kupoteza fahamu, alihisi moyo ukizizima. Masimba alimuokoa na kumtoa mikononi mwa kifo. Lakini leo alitaka kumuua masimba kwa sababu ya pesa. Hilo likaonyesha kumtuliza kwa muda lakini bado mawazo yake yalikuwa kwenye pesa. Akayaondoa mawazo yale kwa kuichukua sabuni na kuanza kujipaka mwilini. Ni wakati akilifanya hilo akausikia mlango ukifunguliwa kisha nyayo za mtu zikasikika kuingia pale ndani. Akayafunga maji kisha kutulia mle mle bafuni. Miguu bado iliendelea kutembea pale chumbani. Akaangalia pembeni kidogo sehemu ya kuwekea vifaa vyake, lakini hakuiona bastola yake, alikuwa ameisahau pale chumbani sambamba na mavazi yake. Akaendelea kutulia huku bado mtu yule akionekana kuhangaika hapo chumbani. Akatamani kutoka mle bafuni lakini hakuweza kwa kuwa kulikuwa na ugumu, pia alikuwa uchi na bastola yake ilikuwa chumbani. WakAti akifikiria nini cha kufanya, mtu yule akasikika akitoka mle chumbani kisha kupotelea. Teddy akaufungua mlango na kuchungulia kwa nje, macho yake yakamuona mtu akimalizikia kwenye kiza. Kwa kuwa alikuwa uchi huku akiwa bado na povu la sabuni, teddy alitoka mpaka ndani na kuingia chumbani. Cha kwanza kukiangalia ilikuwa bastola yake. Akaiona ikiwa pale pale alipoiacha. Akaangalia na vitu vingine. kitu alikikuta kikiwa kipo pale pale. Yule ni nani? Na alikuja hapa kufanya nini? Yalikuwa maswali ambayo hayakuwa na majibu.

******

Wana usalama walikuwa mtaani wakiendelea kuwafuatilia Jimmy na Suresh. Kila sehemu walikuwepo na hata kwenye makazi yake ya siri yalikuwa yakichunguzwa kwa umakini wa hali ya juu. Muda wote walioanza kumchunguza bado hapakuwa na chochote walichokipata kutoka kwenye uchunguzi wao. Mawasiliano yao yalikuwa yameingiliwa na kufuatiliwa kwa kila hatua. Hakukuwa na mawasiliano ya kutia shaka. Licha ya hilo wanausalama bado walikuwa wakiendelea kufuatilia. Katika kufuatilia huko wakagundua kuwa Jimmy huwasiliana na namba karibu tano kwa kila siku. Namba hizo huwa haipiti dakika mbili mpaka tano pasipokuwasiliana. Hilo likawatia shaka wana usalama wale. Kwani hata walipoifuatilia mawasiliano ya Suresh walikutana na namba zile zile na mawasiliano yale yale na muda ni ule ule kama yale ambayo hufanyika kwa Jimmy. Wote wakahisi uwepo wa mawasiliano yasiofaa kati ya watu wale... leo hii vijana wawili walikuwa wamekaa maeneo buguruni kwa mnyamani wakibishana sambamba na vijana kuhusu sakata linaloendelea hapa nchini kuhusu kutekwa kwa watu na kupotea kwa mwanaharakati na mkosoaji mkuu wa serikali ya Tanzania Ben John Saatisa. Wakati wengine wakiilaumu serikali hasa Idara ya Ujasusi, wengine walikuwa wakikihoji chama chake kwa kukaa kimya muda wote mpaka pale mitandao ya kijamii kuibua suala hilo. Licha ya ubishi huo, lakini walikuwa hapo kwa kazi maalum. Kazi aliowaleta hapo ilitokana na kugundua kuwa mmoja kati ya watu wanaowasiliana na Jimmy pamoja na Suresh alikuwa akiishia katika viunga hivyo vya buguruni. Walibishana hapo lakini macho na mawazo yao yalikuws mbele ya jumba fulani kubwa. Hapo ndipo anapoishi mtu wao waliokuwa wakimfuatilia. Wakati mabishano yakiendelea, wakaiona ikiingia taratibu katika eneo la jumba hilo. Punde lango likafunguliwa na ile gari kupita ndani moja kwa moja. Vijana wale hawakuonyesha chochote bado waliendelea kubishana. Ikiwa hazikupita hata sekunde kumi tokea kuingia kwa hari hilo. Wakamuona mwanadada mrefu na mrembo sana akichungulia kutoka ndani kisha kuufunga mlango. Haukupita muda tena wakamuona muokota makopo akipita akielekea pale kwenye lango la jumba lile. Macho yao yakahamia kwa muokota makopo yule. Muokota makopo ambaye aliwashangaza na kuwaduwaza. Hakuwa muokota makopo kama anavyoonekama.. bali huyu alikuwa mtu kama wao.. Yaani hata yeye alikuwa ni kachero, lakini hawakujua kwa nini yuko pale na imekuaje Akajibadili na kuwa muokota makopo.

ITAENDELEA
 
NITAKUPATA TU

SEHEMU YA 037

Alikuwa muokota makopo, muokota makopo ambaye hakuonekana kufanana na kazi hiyo. Bado wakaendelea kumtizama. Hata wakati analifikia geti na kuligonga bado walikuwa wametulia wakimtizama. Suruali iliyochanika, kofia chakavu na fulana ya hovyo haikuwafanya wapelelezi hawa waamini kile walichotakiwa kuaminishwa. Kuaminishwa kuwa huyu alikuwa mchafu tena muokota makopo. Kila mmoja akaendelea kumtizama safari hii kwa umakini. Wakataka kuaminishwa kuwa hakuwa mtu kama wao, lakini hilo halikutokea kwao kuamini. Kuamini kuwa yule ni mwenda wazimu. Walijua na kutambua kuwa yule alikuwa mwenzao. Geti likafunguliwa na mwanadada yule yule aliyelifunga mwanzo, hakuna aliyetegemea kutokea kwa kilichotokea. Kwani muda mfupi walikuwa wakimuangalia yule mtu kama muuza machupa. Hata wakati akiliendea geti walilijua hilo. Lakini kitendo cha geti kufunguliwa na kushuhudia ule upigaji wa muokota makopo yule, wakabaki wameduwaa. Mwanadada aliyefungua geti alikuwa chini nje kidogo ya geti akiwa hana fahamu. Mtu yule muokota makopo akageuka na kuwapa ishara ya kumchukua mwanamke yule. Hapo ndipo walipomtambua na kumjua muokota makopo. Huyu alikuwa Dee plus, huyu alikuwa kijana wao. Baada ya kuitoa ile ishara Dee plus akalifungua geti taaratibu na kuzama ndani. Macho yake yakakumbana na giza, giza ambalo ilikuwa ishara kuwa jumba lile halikuwa linaishi watu wa kawaida. Kingine kilichomstaajabisha ulikuwa ni ukimya. Ukimya ambao hapo mwanzo haukuwepo. Bastola ilikuwa mkononi wakati akiuendea mlango wa jumba lile kwa kupitia chini ya magari ambayo yalikuwa pale ndani. Bado ukimya uliendelea kutanda na kumfanya Dee plus a0ngeze umakini. Alipoufingia mlango kwa upande wa nyuma akasimama kwanza kusikiliza kama atasikia kitu chochote. Lakini bado hakuisikia sauti ya tv wala sauti ya redio. Jumba lilikuwa kimya kabisaa. Akaendelea kusonga mbele. Baada ya kutembea hatua kadhaa, akaukuta mlango ukiwa wazi, hapo akasita kwanza. Akasimama upenuni mwa jumba lile. Mbele yake akiutizama mlango ambao ulikuwa wazi. Licha ya kusubiri kwa muda wa dakika moja, lakini hakuweza kumuona mtu yoyote akitoka ama kuingia. Hapo akaamua kusogea mbele zaidi kuufuata mlango. Alipoufikia akatembeza macho yake ndani kwa sekunde moja akitegemea kuona chochote lakini hakuliona hilo. Sasa akaamua kuingia ndani kabisa. Bado ukimya na giza viliendelea kuwepo hata ndani. Bastola mkononi, macho yakitembea huku na huko akafanikiwa kuingia mpaka sitting room. Bado ukimya haukuondoka hapa. Akatulia hapo akiangalia kama mtu wake atakuwepo hapo, lakini bado hakumuona mwenyeji wake. Sebule haikuonyesha dalili ya uwepo wa watu hapo. Hilo pia likamshangaza kama sio kumduwaza.

Akainuka akipanga kuitafuta switch ili awashe taa aangalie. Wakati anafika karibu na swichi akaisikia sauti ya mtu akigugumia kwa maumivu. Akaacha kwanza alichotaka kukifanya alatulia ilikusikiliza kwa makini. Bado sauti dhaifu ya mtu aliye0nyesha yupo kwenye hatua za mwisho aliendelea kuisikia safari hii kwa karibu. Dee plus asogea mdomo wa bastola ukiwa mbele. Mbele kidogo akakanyaga kitu mfano wa maji. Kabla hajajua ni kitu gani, harufu ya damu ikasikika puani. Akatambua kuwa ilikuwa damu tena inawezekana ni damu ya mtu yule anayegumia kwa maumivu. Hapo akaliacha hilo la damu na kuanza kumsaka majeruhi. Kengele za tahadhari zikilia kichwani kwake. Haikuwa sawa na hapukuwa na usalama tena. Alishawahiwa na mtu. Kitendo cha kuukuta mlango uko wazi kisha kulikuta hili la dimbwi la damu ilikuwa ishara kuwa tayari kuna mtu amemuwahi katika hili. Hii ilikuwa ile ile staili ya fumbana midomo. Hata huyu naye alikuwa amezibwa mdomo kutotakiwa kuongea chochote. Nani atakuwa amelifanya hili wakati hii ilikuwa ni siri ya idara ya ujasusi? Nani anavujisha hili kutoka ndani ya idara ya usalama wa Taifa? Tuna wanaotusaliti? Tuna wanaovujisha hili? Nani amejua nani atakuja huku ndani? Yalikuwa mawazo yaliyomsogeza mpaka chini ya sakafu alipolala mtu yule. Bado alikuwa akiugulia maumivu. Akainama kumuangalia mtu huyu kama anaweza kupata lolote, lakini haikuwa hivyo, mtu yule akampa ishara ya kuwasha taa.. Dee plus akainuka huku bado bastola iko usawa wa mtu huyu. Akarudi nyuma na kuiwasha taa.. sebule yote ikawa nyeupe. Hapo akashtuka baada ya kukutana na watu watatu wakimtizama. Teddy, Ben na Mwamvita. Wote walikuwa wakitabasamu huku teddy akipiga makofi. Dee plus hakushtuka na hukuwajali, bado macho yake yalikuwa yakiutizama mwili wa mtu yule aliyelala katikati ya dimbwi la damu. Akili yake ikafanya kazi kwa haraka. Akageuka kuwaangalia watu wale watatu, hakuamini macho yake pale alipokutana na midomo mitatu ya bastola ikimtizama huku sakafuni kukiwa na miili ya wale vijana wawili ikiwa haina uhai. Hakuacha kuuonyesha mshangao wake. Watu watatu ambao alikuwa akiwatizama hawakuuonyesha utani wala masihara. Hata pale walipokuwa wakimsogelea hakujua nini cha kufanya. Ilikuwa miujiza tu kutoka mikononi mwa viumbe hawa watatu. Viumbe ambao hawakuwahi kuwa na roho kibinadamu. Akasimama akimuangalia zaidi teddy. Kwa mara ya kwanza alikuwa akiushuhudia unyama wa teddy. Hakuonyesha kama hata yeye ni kachero. Hapa aliubeba unyama unyama. Wote wakamfikia katika muda ule ule. Midomo ya bastola zao iliugusa mwili wa Dee plus. Wakimtizama katika kila aina ya vitendo na ishara. Nadhani hawakuwa wakimjua vizuri dee plus, nadhani hawakuwa wakimjua kwa kuwa hawakuweza kusimama kwa muda ule. Mapigo fulani ya kijapani yalisababisha bastola zao kuanguka chini pasipo wao kutaraji. Sasa walikuwa wakitizamana, wakiangaliana na hata kusogeleana. Dee plus alikuwa akiwatizama jinsi walivyokuwa wanakuja. Ni wakati hilo likifanyika mlango ukafunguliwa kwa kasi huku risasi zikivurumishwa ndani ya sebule. Hakuna aliyesimama hapo bali kila mmoja akachupa kwa upande wake. Moshi wa baruti pekee ndio uliyesikika ndani ya chumba kile. Dee plus alikuwa amebana nyuma ya meza kubwa macho yake yakitizama kila upande. Ukimya ulikuwa umechukua nafasi kubwa ndani ya jumba. Hakuna hata mmoja ambaye alikuwa akipumua. Pale alipojibanza Dee plus nyuma yake kulikuwa na mlango mdogo ambao mwanzo hakuwa ameuona. Hata mtu ambaye alikuwa akimimina risasi naye alikuwa amejibanza kimya. Sebule bado ilikuwa giza kutokana na risasi zilizokuwa zikivurumishwa kuipasua taa. Dee akaufungua mlango taraatibu na kuingia ndani ya Chumba kile kisha kuufunga tena. Wakati akitaka kugeuka nyuma aondoke, akamuona mtu mle ndani. Huyu alikuwa mwanadada. Alikuwa akitetemeka huku akiwa hana hata vazi maungoni mwake. Alikuwa akitetemeka sana na licha ya kutetemeka huko pia alikuwa akivuja damu maeneo mbali mbali ya Mwili wake. DEE PLUS AKATULIA AKIMTIZAMA HUKU MDOMO WA BASTOLA UKIMLENGA MWANAMKE YULE. Hakutaka kumuamini kwa asilimia zote. Hata katika kazi zao za kijasusi hakutakiwa kumuamini mtu yoyote. Kitendo cha teddy kutaka kumuua ni kuonyesha ni jinsi gani binadamu hawaaminiki. Akaichukua khanga ambayo ilikuwa juu ya meza akamtupia na kumtaka watoke mle ndani. Kwa kuwa mwanamke yule alikuwa mwenyeji wa jumba lile akamuongoza Dee plus kutoka katika jumba lile wakiacha milindimo ya risasi ikiendelea.

*******

Alihitaji kuupata ujumbe kutoka kwa Dee plus kutoka sehemu fulani aliyomtuma. Lakini muda ulikuwa umekwenda sana na bado hakuwa amepata ujumbe huo pia Dee plus hakuwa amefika. Hilo likampa wasiwasi kidogo. Akaamua kumpigia, lakini simu yake ilikuwa ikiita tu pasipokupokelewa. Hata hilo hakulitegemea. Akili yake ikamwambia dee plus alikuwa msambweni. Wakati akitaka kuinuka tayari kwa safari ya kumfuatilia.. mlango ukafunguliwa akaingia dee plus, hakuwa mwenyewe bali alikuwa na mwanamke aliyeonyesha kulowa damu. Hapo akagundua kuwa mawazo yake kwamba Dee alikuwa msambweni yalikuwa sahihi. Akawaangalia wote kwa pamoja, lakini kabla hajazungumza chochote simu ya Masimba ikaita. Akaichomoa simu mfukoni na kuangalia Jina la mpigaji. Alikuta simu inatoka kwa mama yake mzazi. Machale yakamcheza.. akahisi hatari kwa mzazi wake sambamba na wanawe France na Yaseer. "Hallow Mamaaa!!!!! Akaita masimba..

"Tunahitaji mzigo wetu!! La sivyo utakuta maiti za wanao na mama yako mzazi." Haikuwa sauti ya mama yake, bali ilikuwa sauti ya mtu mwingine ambaye hakuweza kumgundua.
 
NITAKUPATA TU

SEHEMU YA 038

Mtunzi: Ibrahim Masimba

Whatsap: 0675191162

ILIPOISHIA
Tunaomba mzigo wetu la sivyo utakuta maiti za wanao pamoja na mama yako mzazi.
ENDELEA NAYO.

Kwa muda masimba akapigwa na bumbuwazi, butwaa la kutokuamini alichokisikia. Simu ilishakatwa na haikuwa ikipatikana tena. Mama yake na watoto wake Yaseer na France walikuwa chini ya himaya ya watu asio wajua. Hasira zikaendelea kuchemka ndani kwa ndani. Aliwapenda sana wanawe na hata mama yake. Hakupenda waguswe na kubughuziwa na mtu yoyote. Lakini leo kuna watu ambao wamekwenda kuugusa moyo wake na roho yake. Walikwenda kumtingisha na kumtia hofu. Walikwenda kuonyesha kuutaka mzigo kwa njia nyingine. Ni nani hawa wanacheza na watoto wangu? Ni nani hawa wanacheza na mama yangu? Yalikuwa mawazo yaliyomuondoa pale ndani. Alitaka kuondoka katika muda ule kuelekea kwao Handeni. Alitaka kuwahi kukabiliana na watu hawa. Mzigo ni wa nini kwangu? Watu wangu wanathamani kuliko hata huu mzigo. Wakati anaukaribia mlango wa kutokea akaisikia sauti ya Dee plus ikimuita. Hapo ndipo alipogutuka na kugundua kuwa Dee plus alikuwa pale ndani tena akiwa na mwanamke aliyeliwana damu. Akageuka na kumtizama Dee plus, macho yao yakaongea kwa sekunde mbili, sekunde ya tatu masimba alikuwa akiufungua mlango akiondoka pale kwa safari ya Tanga. Safari ya kuupeleka mzigo sababu ya kuwaokoa watu wake. Alitembea hasira ikichemka, alitembea kana kwamba ni kichaa. Bastola mbili zikiwa mwilini katika sehemu tofauti. Alikuwa ameingiq vitani rasmi, alikuwa ameingia kwenye mapambano. Teddy, mwamvita, suresh na jimmy ilikuwa ni lazima wafe. Ilikuwa ni lazima waondoke. Muda mfupi alikuwa sehemu moja katika nyumba yake ya Siri maeneo ya kijitonyama. Alikuwa ndani ya chumba akiuchukua ule mzigo tayari kwa kuupeleka sehemu husika. Alikuwa tayari kufanya kila kitu kwa sababu ya watoto na mama yake. Baada ya kuweka kila kitu katika hali nzuri, safari ya kuelekea Handeni ikaanza. Alikuwa katika kiwango kikubwa cha hasira, alimtoa teddy moyoni na hata rohoni. Alikuwa tayari kumuua kwa mikono yake mwenyewe. Alikuwa tayari kuufumua ubongo wa mwanamke huyu mpuuzi. Alitambua ni yeye ambaye alikuwa nyuma ya hili suala la kushikiliwa mateka kwa wazazi wake. Hakutaka kumwambia mtu yoyote zaidi ya Dee plus. Hata Chief hakutaka kumwambia kwa kuwa anaweza kuongea na wasaidizi wake wakaivujisha. Alitaka kupambana mwenyewe, alitaka hili suala liishe mikononi mwake. Suala la kifo cha waziri mkuu akaliweka pembeni kwanza. Mawazo yalikuwa kwa watoto wake na bibi yao. Wakati akipita kwenye daraja la wami akaliona gari likimpita kwa kasi sana. Mwendo wa gari lile ulimshangaza sana lakini kwa kuwa halikumhudu akaamua kuachana na mawazo kuhusu hilo. Akaendelea kuendesha gari kwa mwendo wa wastani. Wakati anafika mkata ili aingie kwenye barabara iendayo Handeni, mlio wa sms ukaingia kwenye simu yake. Akaitoa simu mfukoni, akakutana na Jina la My love juu ya kioo cha simu. Sms kutoka kwa Teddy hiyo ilimshtua. Akaufungua ujumbe ule huku moyo wake ukiwa na wasiwasi mkubwa. "Najua ushajua mpaka sasa mimi ni nani. Naomba upeleke mzigo ukiwa pekee yako, ujanja wowote utakaoufanya utakuja kuokota maiti za hawa vifaranga vyako." Ulisomeka ujumbe ule. Akaurudia kuusoma tena na tena. Hakutaka kuamini kama ulikuwa ukitoka kwa teddy mwanamke aliyekuwa akiimba mapenzi kila siku. Mwanamke aliyekuwa akimwambia Nakupenda kila siku. Akaurudia tena na Tena ulitumwa kweli na Teddy. "Nitakupata tu na Nitakuua kwa mkono wangu." Akajisemea mwenyewe huku akiirudisha simu mfukoni. Teddy alikuwa ameonyesha yeye ni nani katika hili. Aliamua kujiweka wazi. Akaipita mazingara na kuitafuta SUA. Gari ikatembea na kutembea katika mwendo wa kawaida.

******

Mji wa Vibaoni ulikuwa umepoa kwa ukimya, wakazi karibia wote walikuwa wamelala huku mbwa tu wakisikika wakibweka. Alitembea kwa miguu baada ya kuiacha gari sehemu ya mbali kidogo. Alitembea usiku ule akiwa na mavazi maalum ya kutembelea usiku. Kutoka kijiji cha kwambwembwele alipoiacha gari, akapitia barabara iendayo arusha eneo maarufu liitwalo kwa kadenge. Akatembea usiku ule pasipokukutana na kitu chochote mpaka alipotokea maeneo ya Shule ya Msingi mlimani (zamani alijulikana kama vibaoni) baada ya kufika hapo akatulia kwanza akiangalia nyumba yao. Macho yake yakawaona watu wawili ambao walikuwa wamesimama Nje ya nyumba yao. Aliendelea kuangalia mara akauona mwanga wa taa za gari ukisogea taratibu. Masimba akaendelea kidogo akitizama kwa makini. Akamuona mtu mwingine akitokea nyuma ya nyumba ya mzee Mauya. Baba mzazi wa Rukia Mauya. Baada ya kutoka mtu yule akaonekana akiisogelea gari ambayo ilikuwa tayari imesimama karibu na nyumba yao. Akaondoka pale na kupitia nyuma nyuma mpaka pembeni mwa uwanja wa shule ya msingi. Wakati huo watu wale bado walikuwa wamesimama huku mmoja wao akiongea na simu. Punde akauona mlango wa gari ile ukifunguliwa, wakashuka watu wawili ambao aliwatambua kwa haraka. Alikuwa mwamvita na Ben. Hata alipoiangalia gari ile vizuri aliitambua kuwa ni ile gari iliyompita kule wami. Baada ya watu wale kushuka akawaona wakiingia ndani ya nyumba yao kisha wakatoka wakiwa wanawasukuma watoto wake na mama yake. Wakati hilo likifanyika mlango mwingine wa gari ile ukafunguliwa. Safari hii alishuka teddy mkononi akiwa ameshikilia bastola. Kwa kuwa watoto na hata mama wa masimba walikuwa wakimjua,wakamkimbilia na kutaka kumkunbatia. Haikuwa hivyo, haikuwa hivyo kwa kuwa Teddy hakulitaka hilo. Akashudia wanawe wakipaa angani baada kupokea mapigo kutoka kwa teddy. Hakuvumilia hilo, muda huo huo alikuwa amechupa hewani na kuwadaka watoto wake kabla ya kufika chini. Akatua nao chini katikati ya watu wale huku mdomo wa bastola ukiwa kichwani kwa Teddy. Kilikuwa kitendo ambacho hakikutarajiwa na watu wale, kitendo ambacho kiliwaacha kwenye hamaniko. Wakati hilo likiendelea mama yake masimba akachoropoka na kutaka kukimbilia pale alipokuwa mwanawe. Hakumfikia wala kusogea.. Bastola ya Mwamvita Ikakohoa na wakati ule ule Masimba akamshuhudia mama yake akipaa juu na kuanguka chini. Damu zilikuwa zikivuja kifuani. Masimba hakuamini hilo, hakuamini kama chini pale amelala mama yake. Akakurupuka kukimbilia ulipolala mwili wa mama yake mzazi. Wakati huo huo wanakujiji nao walikuwa wakiinuka kutokana na kuusikia mlio wa bunduki. Baada ya kuona watu wameanza kuamka majumbani mwao, wakambeba mtoto mmoja na kuingia naye kwenye gari kisha kui0ndosha gari kwa mwendo wa kasi wakimuacha masimba akilia juu ya mwili wa mama yake.

Alikuwa haamini kama mama yake ndiyo yule aliyekuwa amelala pale chini damu ikivuja kama maji. "Mnala inuka chilonge. Usekunasa mnala wezi ukuluwo na walonge na yuhi? Inuka mnala." ( inuka mama tuongee, usiniache mama, wajukuu zako wataongea na nani? Inuka mama) alilalamika masimba huku akimtingisha mama yake. Lakini haikusaidia kitu, mama yake hakuwa na kauli tena. Alikuwa katika hatua za mwisho za uhai wake. Pale pale akashuhudia mama yake akikata kauli na kugeuza shingo. Muda mfupi akaacha kupumua. Mama yake alikuwa amekufa mikononi mwake. Mama yake alikuwa amekufa kwa ajili yake. Mwamvita alikuwa amemuua mama yake. Akashindwa kuongea kwa muda. Mama yake alikuwa amenyamaza kimya. Akainuka na kusimama pembeni akiuangalia mwili wa mama yake. Lakini alipoangalia pembeni hata mwanawe Yaseer alikuwa ameanguka akitokwa na damu puani, mdomoni na masikioni. Alikuwa amepoteza fahamu. Muda ule ule difenda ya polisi yenye askari kumi wenye silaha nzito ikawasili. Wakashuka na kuanza kupiga picha za tukio lile. Muda ule ule gari aina ya wagonjwa ikafika na kumchukua yaseer. Kila kitu kilitokea kwenye kipindi kifupi sana. Muda ambao ulibadilisha maisha ya masimba. Hakujua kama mwanawe atapona kutokana na pigo la Tedd na pia hata france naye hakujua kama atakuwa salama. Watu walikuwa wengi wameuzunguka mwili wa mama wa masimba. Mama ambaye alikuwa ni maarufu sana pale vibaoni na Handeni yote kwa ujumla. Vilio vikatawala huku watoto wa kike wa marehemu wa kipoteza fahamu kwa taarifa hiyo. Muda wote Masimba hakuwa akiongea taswira ya mwamvita akimshuti mama yake ilikuwa ikijirudia. Matundu matano ya risasi kifuani yaliuondoa uhai wa mama yake. Akaitamani iwe ndoto, aliitamani iwe kama hadithi ya kusadikika. Lakini mwamvita aliutoa uhai wa mama yake. Mbele ya macho yake ulilala mwili wa mwanamke mwenye thamani kuliko mwanamke yoyote duniani. Akainuka akipiga hatua kwa mara nyingine akielekea ulipolala mwili wa mama yake. Hakuufikia kama mwanzo, kizunguzungu kikali kikamfanya aanguke chini, macho yakaingiwa na Giza na hakuona kilichoendelea.

******

Alijifungia chumbani akilia kwa uchungu. Pembeni aliuweka mzinga wa pombe kali. Macho yake yalikuwa yamevimba kwa kilio na majuto. Mbele kidogo kwenye kitanda kidogo alikuwa amelala france mtoto wa masimba akitibiwa na Daktari binafsi. Taswira yake ikalikumbuka tukio la mwamvita kuruhusu risasi kumuua mama wa masimba. Akakumbuka kumuona mama yule akiinguka. Chozi likashuka na kushuka Zaidi. "Hukustahili Kufa mama yangu. Umenitendea mema sana tokea nilipokujua . Nisamehe mama yangu ni samehe kwa ujinga wangu. Aliongea Teddy akilia. Kichwani akavuta taswira ni hali gani alionayo masimba kwa muda ule. Akainuka na kutoka nje ya kile chumba. Safari yake ikaishia chumba kingine mle ndani. Akaichomoa bastola yake na kuinyanyua juu mdomo wa bastola ukagusa kichwani mwake. Teddy alitaka kujiua. Hakuweza kulivumilia lile. Kidole kikashuka mpaka kwenye kitufe cha kufyatulia risasi.

KESHO
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom