NITAKUPATA TU
SEHEMU YA 035
Akapewa kitu mfano wa picha, akaikunjua kutoka kwenye kitu kama gazeti na kuitupia macho. Akakutana na picha ya Mpenzi wake akiwa sambamba na mtu ambaye alimfahamu sana. Mtu ambaye alimkuza katika fani hadi kufikia hapo. Aliitizama picha kwa muda kisha akairudisha mikononi kwa Dee plus. "Hakikisha hawakupotei au hakikisha unakijua kile ambacho wamekizungumzia." Aliongea masimba akiunyoosha mkono. Dee plus aliichukua ile picha na kuondoka akimuacha masimba akiendelea kuburudika. Bado alihitaji kujua kile ambacho teddy na ben walikuzungumza pale ufukweni. Dee plus akaondoka safari hii akielekea katikati ya mji. Alitaka kuanza na ben kwanza. Kwa kuwa alikuwa na hisia kuhusu kikao cha pale ufukweni mwa bahari. Bastola mbili zilikuwa sehemu tofauti mwilini. Alimjua teddy na pia ben, licha ya kuwajua huko lakini hakuhofia kwa kuwa hata yeye alikuwa mmoja kati yao.
Picha ya teddy na ben wakiwa ufukweni mwa bahari ni kitu ambacho kilimjengea maswali masimba katika kichwa chake. Muonekano wa watu hawa katika picha aliyoitazama muda mfupi uliopita hapakuonekana ishara ya mapenzi juu yao. Ukaaji na jinsi walivyokuwa wakitizamana ilionyesha uwepo wa kitu nyeti kilichokuwa kikijadiliwa na watu hawa wawili. Hisia kwamba teddy anapanga mipango ovu juu yake ilikuwa akikigonga kichwa chake. Haikuwahi kutokea teddy na ben kuwa na ukaribu huu.. hilo likampa mashaka na wasiwasi. Hisia kwamba teddy bado hajabadilika bado ziliendelea kumsumbua. Akatamani kumfuata na kwenda kumuuliza kwa kuwa bado alimpenda sana. Hata alipokumbuka usaliti aliotendewa na watu wake, akahisi labda alimtafuta ben kwa ajili ya kumpa kazi ya kuwafutilia mbali jimmy na washirika wake. Vifo vya watu sita katika nyumba fulani ni ishara kuwa yupo mtu anayetembea naye kila sehemu. Kwa mara ya kwanza akawaza kuitumbukiza risasi kichwani kwa mwanamke huyu. Ni dhahiri kuwa mapenzi kwake tayari yalishakwisha. Akaendekea kuuvuta muda tena na tena. Wakati wa kuianza hii kazi hakuwaza kama angefika huku. Hakuwaza kama yangetokea haya. Kwa mara ya kwanza akakumbuka wito wa DG wa idara ya Ujasusi. Wito ambao kidogo ulionyesha kumtatiza katika kuukubali. Sekunde hii alikuwa amekaa akiwaza, sekunde ya pili alikuwa akiukaribia mlango wa kutokea tayari kwa safari ya kuelekea kwa Chief. Alitembea kwa miguu mpaka maeneo ya bamaga, hapo akachukua tax tayari kwa safari ya kuelekea masaki nyumbani kwa mkurugenzi. Muda wote alikuwa kimya wakati tax akisonga kuelekea masaki. Mara moja moja alikuwa akiangalia kwenye vioo vya pembeni kuona kama anafuatiliwa, lakini haikuwa hivyo. Hapakuwa na gari wala usafiri wa aina yoyote. Wakati tax inafika kwenye mataa ya Morocco, akaiona gari nyeupe kupitia kioo cha pembeni akiwafuatilia. Ingawa gari ile ilikuwa katikati ya magari mawili, lakini hilo halikumfanya asigundue kuwa inamfuatilia yeye kwa kuwa, wakati anatoka pale afrika sana, -hii gari aliipita ikiwa imeegeshwa pembezoni mwa barabara. Hakuongea kitu wala kuonyesha mabadiliko yoyote, dereva naye akaendelea kuendesha pasipokugundua kitu. Wakavuka mataa sasa wakielekea maeneo ya oysterbey. Alipoiangalia ile gari, akaiona nayo ikiendelea kusogea tena ikiwa katikati ya yale magari matatu . Hapo kengele za hatari zikaendelea kugonga kichwani mwake. Hisia kwamba yale magari matatu yalikuwa katika safari moja ikamjia. Kwa mara ya kwanza akajipapasa sehemu alipoihifadhi bastola yake. Baada ya kuhakikisha ipo akatabasu huku akimuomba dereva aelekee ulipo ubalozi wa ufaransa. Dereva akatii na kuuongeza mwendo, huku nyuma magari yale nayo yakaongeza.
Muda mfupi dereva akasimamisha gari pembeni mwa barabara. Masimba na dereva wote wakashuka, masimba akatia mkono wake mfukoni na kutoq noti mbili za elfu kumi kumi na kumpa yule dereva. Wakati dereva akijipapasa kutafuta chenji ya kumrudishia masimba. Muda ule ule gari zile zikawapita kwa mwendo ule ule, lakini kufika mbele kidogo zikaacha barabara inayokwenda posta, mbili zikaingia kushoto kwenye barabara inayokwenda Masaki nyingine moja ikapita kama inaelekea daraja la salenda. Kila kitu kilichokuwa kikitendeka pale kilimsisimua na kumfurahisha masimba. Kila kitu kilichokuwa kikitendeka ulikuwa ni mpango uliosukwa na DG wa Tiss. Alizijua gari na vile vile alizitambua mbinu husika. Hakuogopa tena.. dakika ile ile akaliacha eneo lile akiwa juu ya usafiri wa pikipiki.
*******
Ukimya ulikuwa umechukua nafasi yake kama kawaida katika eneo lote la masaki. Walinzi wa idara zote walikuwa wakizunguka kila kona kuwalinda viongozi wote. Makachero walikuwa kila sehemu wakinusa hiki na kufanya kile. Masimba alishuka umbali wa hatua hamsini kutoka yalipo makazi ya chief. Akatembea taratibu macho yake ya kitizama kila sehemu. Maafisa usalama na jeshi maalum la usalama wa taifa walikuwa wamezagaa kila upande wakiangalia usalama. Masimba akatembea kanakwamba hakuwa akiwaona walinzi na hata maafisa wengine. Akalikaribia geti, hapo akasimamishwa huku mitutu ya bunduki ikielekezwa kwake. Mtu mmoja alieonekana kama mkuu wa ulinzi akamsogelea masimba kwa ukaribu. Alipomfikia na kugundua alikuwa nani alimpa heshima kisha kumuongoza kuelekea ndani tayari kwa kukutana na Chief. Geti likafunguliwa masimba akaongozwa mpaka ndani pembeni kukiwa na watu maalum kutoka kikosi cha walinzi wa viongozi yaani VIP PROTECTION UNIT. Kufika ndani akaongozwa mpaka ndani ya jumba. Kuingia tu akukatana na macho ya chief mr godliving kimaro akimtizama. Hayakuwa macho ya kutisha machoni mwake, yalikuwa macho ya kawaida na macho ambayo hayakuwa na chochote. Wakaangaliana tena na tena, kila mmoja akimtizama mwenzake. "Shikamoo Mzee." Hatimaye masimba asabahi. Chief akaitika kwa kichwa kisha akampa ishara ya kukaa katika moja ya viti pale ndani. Masimba akakaa pasipo kubisha. Macho yake yalikuwa yakimuangalia Chief. Hata chief naye akawa ana muangalia usoni. "Bila shaka nadhani unajua kuhusu hiki kilichotokea hapa nchini. Mambo yamekuwa magumu sana, mashinikizo kutoka mamlaka za juu yamezidi. Mkuu wa nchi anataka kupata taarifa kuhusu hiki kifo. Lakini bado wenzako wameshindwa kupata chanzo cha kilicho nyuma ya hili tukio. Wote ambao tulidhani wangeweza kutufumbua katika hili nao huuawa katika mazingira ambayo nadhani ni kutaka kuuficha ukweli. Nimekuita hapa kukupa hii kazi, kushindwa kwa idara zetu za ujasusi ni aibu kwa nchi na kwa dunia. Mheshimiwa rais ametishia kuwaomba CIA NA MOSSAD katika kumgundua muuaji huyu ama chanzo mauaji hayo. Fanya ufanyavyo na kwa njia zako zote ili tufahamu hili. Unaruhusiwa kutumia chochote katika hili."aliongea chief akionekana kukerwa na hiki ambacho kinaendelea kutokea. "Masimba hakutaka kuongea kwa muda ule. Kichwa chake kilikuwa kikiifikiria kazi hii aliyopewa. Kazi ya kumtafuta muuaji wa waziri mkuu, muuaji ambaye alikuwa ni yeye mwenyewe. Akatamani kumjibu kwamba mimi ndiye muuaji, lakini akauacha huo mpango. Angejichunguzaje wakati muuaji alikuwa yeye? Hapo akauona umuhimu wa kuwawahi Jimmy, suresh na mwamvita. Alitambua watu hawa ndio watakuwa mashahidi juu ya maovu ya Hayati. "Unadhani mtuhumiwa wa mauaji aliyenusurika kufa kwa amri yako anaweza kuifanya kazi nzito kama hiyo tena akitumwa na watu wale wale wali0mtuhumu? Akauliza masimba masimba. . Safari hii akibadilika.
"Najua kwa nini nimekuita hapa, hayo mengine achana nayo, nimeunusa ukweli ndio maana kama mkuu wa idara nikakuita." Akajibu Chief.
"Sawa nitafanya naomba muda wa wiki mbili nitarudi hapa nikiwa na ushahidi ama mtuhumiwa mwenyewe. Ninachoomba ni ruhusa kutoka mamlaka za juu kuipekua nyumba zote zinazomilikiwa na marehemu." Lilikuwa ombi ambalo lilimduwaza chief. Hakulitegemea hilo. Akakaa kimya kama sekunde ishirini kisha kwa sauti yake akasema. "Sawa nitazingatia ombi lako." Baaada ya jibu hilo la chief, masimba akainuka na kutoka tayari kwa kuondoka huku akicheka kimoyomoyo.