NITAKUPATA TU
SEHEMU YA 028
******
Kunachangudoa mmoja ambaye inasemekana alionekana akiwa na mwanaume ambaye begani alimbeba mtu, walichukua tax lakini walipofika magomeni mwembechai mwanamke yule alishuka na haukupita muda na huyo mwanaume naye akatelemka akimuaga mtoa taarifa kuwa kuna maagizo amesahau kumpa yule mwanamke. Alikwenda huko kwa muda wa dakika tano, kisha kurejea na kuomba apelekwe kimara. Yalikuwa maelezo kutoka kwa dereva wa tax aliyekodiwa usiku wa jana hotelini pale. Kikundi cha wanausalama kikatumwa huko na kingine kimara,wengine wakabaki pale hotelini wakihangaika na camera za usalama sambamba na mhudumu ambaye alikuwa zamu siku ya mauaji. Barabara zikafungwa kwa muda huku magari yakipekuliwa na madereva kutiwa kashkash. Mhudum Hakuwepo hotelini ama hakuonekana kabisa. Wanausalama walipekua hata chini ya mazuria. Kila kitu kilikuwa kikitiliwa shaka. Wengine ambao walielekea chumba cha kuongozea camera, nao wakapigwa na butwaa. Hapakuwa na chochote katika camera zile. Hapakuonekana mtu wala kikundi cha watu. Hapakuonekana mtu wa kutilia mashaka katika hilo. Bado wataalam wakahangaika huku na huko lakini hapakuonekana chochote. Hata wakati Waziri Mkuu akiingia haikuonekana kwenye camera. Hilo likawafanya wachoke. Kitu kwamba mpango huo ulipangwa mapema kama ya ujio wa mheshimiwa waziri likatawala akilini mwa wanausalama. "Nani amelifanya hili? Nani ameingia na kutekeleza mauaji haya ya waziri mkuu? Je kuna kisasi hapa? Kipi kilimtoa waziri nyumbani kwake mpaka kuja hapa? Ni mtu gani alimbeba mtu? Na ni nani aliyebebwa? Yalikuwa maswali yaliovisumbua vichwa vya wanausalama. Maswali ambayo hayakuwa rahisi kujibiwa kwa wakati ule. Wakatamani hata kumhoji marehemu mwenyewe awaambie. Walitamani waziri ainuke na kukitegua kitendawili kile. Lakini kilikuwa kitu kigumu kama kulazimisha jua kuwaka usiku na mbalamwezi kuangaza mchana. Vichwa vyao vilichoka na kuchokeana. Wakatafakari sana huku wakitamani zingekuwa zama zile, zama za kina Joram Kiango na Willy Gamba. Wasingesubiri waambiwe katika hili bali wangeamua wenyewe. Wasingesubiri muuaji apotee bali wangemtafuta na kumrudisha ama kumsafirisha. Zilikuwa Nuru na Tunu pekee katika nchi ya Tanzania. Nuru iliyong'ara kama Madini ya TANZANITE. Lakini hapakuwepo na Willy Gamba wala Joram Kiango, alikuwepo mtu mmoja aitwaye Masimba, alikuwepo mtu huyu ambaye uwezo wake ulijulikana katika mipaka na mataifa yote. Lakini wana usalama wengine hawakujua kilichopo nyuma. Ni hapo walipokuwa wakiliwaza hilo, wakapewa taarifa kuonekana kwa matone ya damu katika chumba fulani. Wote wakaelekea huko. Hata walipofika hapo ni kweli waliyaona matone ya damu. Damu ilikuwa imeganda kuonyesha haikuwa ya muda ule. Hatua kumi mbele ndani ya pipa ndani ya chunba kile wakauona mwili wa mwanamke ukiwa hauna uhai. Kila mmoja kengele ya hatari ikagonga kichwani. Hawakuamini kama hata huyo changudoa alikuwa salama. Kwa mara ya kwanza wakakili kuwa walikutqna na mtu anayeijua kazi yake. Mtu aliyewajua na kuwatambua.
*****
Baada ya Dee plus kupokea maelezo kutoka kwa masimba, alichokifanya ni kuondoka usiku ule akiamua kuanzia pale hotelini. Alitambua kazi ya kumpata changudoa yule ilikuwa rahisi kuliko kwenda kuharibu camera za usalama. Hakutaka kuchukua gari yake kwa kuhofia kujulikana. Bali alichofanya ni kuchukua usafiri wa pikipiki ambao ulimpeleka mpaka magomeni. Akashuka kama mtu wa kawaida, kisha akaongoza mpaka hotelini. Alipanda ngazi kama mteja, lakini wakati anatokea mapokezi akapokelewa na mhudumu anayeonekana ni mwenye wasiwasi. Uso wake ulikuwa ukiongea hofu tu. Alionyesha woga wawaziwazi. Dee plus akatabasamu ili kuitoa hofu kwa mwanamke yule. Lakini hilo halikufanikiwa, mwanadada yule alikuwa na hofu. Kuna wakati alijaribu kuongea vitu lakini hayakusika masikioni kwa dee plus.
"Habari yako mrembo? Dee plus aliamua kujizungumzisha ili kujaribu kumvuta mwanamke yule. Lakini bado salamu haikujibiwa.
"Kaka naomba nikwambie kitu lakini sio hapa." Akaropoka mwanamke yule akionyesha kupagawa. Dee plus akatingisha kichwa, kwa mara ya kwanza alikubaliana na masimba suala la kutaka kuwasafirisha watu hawa. Kwa muonekano wa huyu mhudumu asingeweza kuufumba mdomo wake kama angekutana na wanausalama. Hakuchelewa kumvuta mpaka sehemu aliyotakiwa. Binti naye bila kujua ameletewa tiketi ya kifo, akaufumbua mdomo na kutaka kuongea... hakupewa hiyo nafasi, tayari basi lilimfika tayari kwa kumchukua. Risasi mbili kutoka kwenye bastola yenye kuzuia mlio zilipenya upande wa kushoto wa kifua chake. Hakuweza kupiga ukelele wowote. Alitupwa umbali wa hatua tatu akaanguka chini. Alikuwa maiti tayari. Baada ya kuhakikisha mwanamke yule hatafumbua mdomo tena, akamuinua na kumtupia ndani ya pipa. Sasa alikuwa akihamia kwenye chumba cha camera za usalama katika hoteli ile. Aliwapita wana usalama akiwa amevaa kitamburisho kama mfanyakazi wa hoteli ile. Akaingia pasipokuonyesha wasiwasi. Muda wa dakika kumi akatoka ndani akiwa ameshaimaliza kazi na sasa ilikuwa safari ya kuelekea nyumbani kwa changudoa yule. Akawapita wanq usalama kwa mara ya pili bila kushtukiwa na yoyote yule.
*******
Ni nyumba yenye watu wengi, nyumba ambayo asubuhi hii iliwakuta watu wakiwa kwenye vikundi vidogo vidogo wakijadili na kuongea kuhusu kifo cha waziri mkuu wa nchi. Kila mmoja alikuwa akiongea kile ambacho ana uhakika nacho. Huku wengine wakiongelee kuuawa kwa waziri kunatokana na mwanamke, wengine walikuwa wakilihusisha hili suala na mtifuano wa kisiasa unaoendelea nchini. Watu kutekwa na watu wasiofahamika ni kitu ambacho kiliufanya mjadala juu ya kifo cha kiongozi mkuu wa nchi upambe moto. Wakati wakijadiliana hilo, wakashtushwa na gari jeusi likisimama mbele ya uwanja wa nyuma ile. Kabla hawajakaa vizuri, wakashtushwa na kuwaona watu wanne wakishuka. Ushukaji wa watu wale ulikuwa ukitia fora na kuogopesha miongoni mwa watu wachache waliokuwepo pale. Kila mmoja akaliacha alilokuwa anaongea, macho yao sasa yalikuwa kwa watu ambao tayari walishaufikia mlango wa nyumba ile. Hakuna aliyeinua mdomo kuongea chochote. Sura za watu hawa hazikuwa sura za kawaida. Punde mmiliki wa nyumba ile akafika naye akionekana ni mwenye wasiwasi. Macho ya watu waliokuwa wakimtizama yalimfanya atetemeke. Hakuna aliyeongea chochote zaidi kutoa kitu mfano wa picha na kumuonyesha. Mama yule akaipokea na kuitizama. Bila kuongea chochote akawaongoza watu wale kuingia ndani. Hatua mbili tatu akawaonyesha kwa kidole chumba anachoishi msichana yule. Sekunde moja wanausalama walikuwa mlangoni mwa chumba kile. Kila mmoja bastola ilikuwa ikitizama ndani. Ukagongwa kidogo, lakini cha kushangaza mlango ukafunguka kuonyesha haukuwa umefungwa.
Wanausalama wakaangaliana huku kengele za tahadhari zikigonga kichwani. Mmoja akaukamata mlango na kuufungua taratibu. Wote macho yao yakatizama ndani... wakaushuhudia mwili wa mwanamke ukiwa mtupu umelala kitandani pembeni kidogo kukiwa na dimbwi kubwa la damu. Wote wakaangaliana. Simu za upepo zikatembea kona zote za nchi. Sasa kila kitu kilikuwa kigumu. Wanausalama wakaingia na kuuanza kuuchunguza. Risasi mbili za kifua upande wa kushoto zilitosha kuuchukua uhai wa mwanamke huyu. Licha kupekuwa kila sehemu, lakini wanausalama wale hawakufanikiwa kugundua ama kupata chochote. Wakatoka nje na kumuita tena mama mwenye nyumba, safari hii wakamuomba awaitie wapangaji waliokuwepo hapo usiku uliopita.
Mama yule akawaita wote, kisha akawatambulisha kwa wana usalama. Kila mmoja akanyamaza kimyq huku wengine presha ikianza kupanda.
"Sisi ni wanausalama tumekuja hapa kufuatilia kuhusu mauaji yaliyotokea usiku wa jana." Alijitambulisha mmoja huku akionyesha kitambulisho chake. Wapangaji wote wakatizamana. Wakatizamana huku sura zao zikishindwa kuuficha mshangao. Mshangao ambao hata wana usalama wenyewe waliligundua hilo. Haiwezekani kifo cha mtu mkubwa nchini uchungizi uje ufanyike pale. Kama kawaida ya wanawake wa magomeni walivyo na midomo mirefu, hawakuchelewa kuuliza hilo.
"Sasa kipi mmetuitia hapa? Ina maana mauaji ya waziri yamefanywa na mtu wa nyumba? Alihoji mama chausiku huku akiwaangalia wana usalama kwa zamu.
Hawakumuangalia yeye bali walitoa ishara wapangaji wa sogee. Wakafanya hivyo, mmoja ya wana usalama akaufungua mlango na kuwataka wote waangalie ndani. Kila mmoja akafanya hivyo.