Riwaya: Msako wa mwehu

Riwaya: Msako wa mwehu

Haya haya masomaso ananendelea kuwa win makachero big up kwako mwandishi
 
SEHEMU-21


Ilipofika saa mbili asubuhi akaletwa mbele ya Kachero Yasmine kwa ajili ya mahojiano. "Swali langu ni moja tu, yuko wapi mfanyakazi wako wa gereji aliyefanya kazi siku ya Ijumaa na kutokomea kusipojulikana"? aliuliza Kachero Yasmine mara baada ya Meneja huyo mhalifu kuletwa mbele yake. "Simfahamu mie ni Meneja tu, kila kitu mhusika ni mmiliki, nadhani mkimpata yeye mtapata majibu kamili" alijibu kiujeuri akionekana kuwa ni mnyonge kuonyesha amechoshwa na mateso ya usiku.
Akawa hana jinsi ya kumlazimisha kwa sababu wanachunga haki za binadamu hakupenda wazidi kumpa mateso zaidi bila sababu. Jukumu lao ni kupepeleza ushahidi utakaomtia hatiani wakimpelekea mbele ya vyombo vya sheria. Akaamrisha arudishwe selo huku wakihakikisha wamempatia chakula cha kushiba.
Kachero Yasmine baada ya mahojiano na yule Meneja mtuhumiwa, akawasha kompyuta yake mpakato na kujiunga na kifurushi cha mtandao. Akatuma moja ya barua pepe. Akawa amebaki kusubiria majibu, baada ya dakika 5 akajibiwa. Muda wote alikuwa anatabasamu pana la ushindi kisha akafungua akaunti feki ya mtandao wa kijamii wa "Facebook". Kisha akatuma picha zake alizopiga katika mapozi mbalimbali. Akiwa bado yupo kwenye mtandao hajatoka, akaona akaunti moja yenye picha ya msichana yenye jina la "NUSRA COMMITTEE" inamuomba urafiki.
Haraka haraka akakubali urafiki huo aliomuomba. Akaanza kutumiwa kwenye akaunti yake feki mada mbalimbali za umuhimu wa ndoa kwa mwanamke wa kiislamu. Akafunga kompyuta yake huku akishukuru kwa hatua aliyoifikia sio haba. Kachero Yasmine alikuwa anakifanyia kazi kikadi alichodondoshewa na "Maso Square The Duduman" pale hotelini.
Kikadi kilikuwa na anuani ya barua pepe. Ambayo Kachero Yasmine aliitumia kutuma taarifa zake. Ndipo mpaka alipokutanishwa na "NUSRA COMMITTEE" sasa alikuwa anasubiria nini kitakachojiri. Alishakisia kuwa "NUSRA COMMITTEE" inahusika na kutafutia wachumba wanawake kwa wanaume. Alipoichunguza alikuta ni akaunti maarufu sana kwa wadada wa kiislamu kwa wakaka wenye kusaka wenza wao wenye maadili ya Kiislamu. Umaarufu wa "NUSRA COMMITTEE" ulivuma zaidi baada ya kuwa wenza wakikubaliana inagharamia gharama zote za sherehe ya ndoa kwa kiwango walichoweka cha bajeti. kisha kama mume hana kazi wanamjaribu kama anafaa wanamtafutia shughuli maalumu ambayo ni siri yao na mhusika.
Kachero Yasmine jina lake tayari lilishawekwa kwenye orodha ya wanaotafuta wachumba, lengo akitaka kuleta ufukunyuku wa kufahamu hao wasichana mamia kwa mamia wanapelekwa wapi baada ya ndoa, wao na waume zao.

Kachero Manu alikuwa ameshafika kwenye kituo kidogo cha kuwashikilia magaidi katika jengo la "NMC" ya zamani kama saa mbili yaliyopita akitokea Hospitali ya Mkoa. Ambapo hakupata taarifa yoyote kuhusiana na mkewe pamoja na kupewa maneno matamu ya ahadi ya kupewa taarifa pindi atakapofikishwa hapo.
Hakutaka kwanza kuwahusisha polisi wasije kuvuruga mambo, mkewe akapata matatizo. Ikabidi sasa hana jinsi zaidi ya kumsimulia Kachero Yasmine juu ya kutoweka kwa mkewe. "Sasa tunafanyaje Bosi,?" aliuliza Kachero Yasmine akionekana ameshachanganyikiwa baada ya kupewa penyenye hizo.
"Hatuna njia yoyote zaidi ya kwanza tusubirie kama ametekwa tuone masharti yao wanataka nini!" alijibu kiunyonge Kachero Manu. Kweli kisu kilikita kwenye mfupa alikuwa ameshikwa pabaya. Wakiwa bado wapo kwenye taharuki hiyo iliyowakumba simu ya Kachero Manu ikaanza kuita. Akaitoa kiunoni mwake, kucheki ni namba mpya, akaanza kutetemeka anagitagita kuipokea kama anavyotetema mlevi wa pombe kali iliyomkolea mwilini.
Akawa hana jinsi zaidi ya kuipokea, "Hello....Hello..nani mwenzangu?" aliuliza Kachero Manu baada ya kubonyeza kitufe cha kupokelea simu. "Hamna cha mwenzangu hapa, fungua "Whatsapp" yako uone utamu utamuni, tunavyojipocholea teh.. teh.. teh.." kisha akakata simu huyo mpigaji. Kachero Manu akawa bado amepigwa bumbuwazi. Alikuwa kwenye dimbwi la mawazo Kachero Manu, kijasho chembamba kikaanza kumvuja licha ya kuwa kiyoyozi mle ofisini kilikuwa kinatema baridi ya kutosha.
Ikabidi haraka haraka awashe data kwenye simu yake, na Kuingia kwenye mtandao wa "Whatsapp" akaona kuna video imetumwa kwa namba ngeni asiyoifahamu ambayo haipo kwenye orodha ya namba za watu wenye mawasiliano na yeye. Akaanza kutetemeka vidole vyake kubonyeza ile video ili aone inahusiana nae nini mpaka atumiwe yeye na asisitiziwe kabisa kuwa aangalie!. Akavaa vazi la ujasiri, wa liwalo na liwe yeye ni mtoto wa kiume, na matatizo ni sehemu ya maumbile ya maisha ya mwanadamu akaifungua.
Hamadi...! Simu ikamponyoka mpaka chini ikaenda kuangukia karibu kabisa na miguu ya Kachero Yasmine kwa mshtuko wa yale aliyoyaona kwenye simu yake. Kachero Yasmine muda wote alikuwa anamuangalia tu namna Bosi wake anavyopitia kipindi kigumu ambacho hajawahi kumuona anakipitia tokea waanze kufanya kazi pamoja. Alikuwa anaonekana kama mtu bozibozi tofauti na jinsi anavyomfahamu kuwa ni mtu jasiri na shupavu. Akamsaidia kuiokota simu na kumrejesha mwenyewe. Kachero Manu akaichukua simu na kuingia tena "Whatsapp" akaipunguza sauti ya spika ya simu yake, na kuruhusu video ianze kucheza tena.
Maskini weeeh..Masalale! ilikuwa ni video ya ngono, mkewe Kachero Manu amerekodiwa anaingiliwa kwa nguvu, mtungo na mijitu miwili mishababi iliyoshibiana, sumsum haswa miili yao ukiitazama na imejaaliwa dhakari kubwa mithili ya punda kilongwe. Mijitu ambayo kwa juu imefunika nyuso zao kwa maski nyeusi, ili isijulikane uhalisia wao. Ilikuwa inaonyesha mkewe Kachero Manu amefungwa kwenye kingo za kitanda na kamba madhubuti akiwa hana nguo yoyote kaachwa uchi kitandani. Wakawa wanamsukasuka kwa zamu huku analalamika kwa sauti ya juu maumivu ya vitendo vya kifedhuli vya kuingiliwa kinguvu anavyofanyiwa.
Alivyoimaliza kuiangalia video hiyo fupi ya dakika 3, Kachero Manu machozi yakaanza kumtiririka kama maji mashavuni mwake, huku akichomoa hanchifu chake na kuanza kujifuta machozi. "Vipi Bosi sikuelewi ni msiba, maana unagogoteza maneno yasiyoeleweka kama umepandwa na ruhani kichwani?, Faith amepona kweli jamani..!" aliuliza Kachero Yasmine. Akawa Kachero Manu hana nguvu ya kumjibu mwenzake zaidi ya kumpa simu ajionee unyama anaofanyiwa mkewe na watekaji.
Kachero Yasmine nae hakuwa na hali kwa jinsi alivyoiona hiyo video, ilikuwa ni unyama usiomithilika kutazama kwa mwenye akili iliyosalimika labda mwenye akili hamuma ndio atafurahia unyama huo. Wakawa wameshang'amua kuwa mkewe Kachero Manu ametekwa na watekaji hawajatoa kitu wanachokitaka kutokana na utekaji huo. "Kama watekaji watahitaji mshumbi wa pesa nipo tayari kukwangua akaunti zangu zote kwa ajili ya mke wangu hata ikibidi kukopa pesa benki nipo tayari ili mahabubu wangu awe huru" alisema Kachero Manu kumwambia mwenzake Yasmine wakati wanatafakari nini cha kufanya na kubadilishana mawazo.
Ghafla wakiwa kwenye majadiliano hayo, simu ya Kachero Manu ikaanza kuita, sasa halahala bila kuchelewa akabonyeza kitufe cha kuruhusu mpigaji wa simu asikike anachotaka kusema.
"Haya Baba nadhani umeona mwenyewe, kwanza nikupongeze memsapu wako ni fundi sana kitandani vijana wangu mahabithi wa tabia wameniambia wamefurahi sana, tena furaha isiyo kifani yaani ile fokofoko kustarehe na memsapu wako, haya tuyaache uamuzi ni wako, kama unamtaka mkeo akiwa salama tunaomba saa sita usiku leo hii umlete mateka mnayemshikilia Bwana 'Kareem Abdallah', Meneja wa "Chops Carwash & Garage" katika uwanda wa bonde la Mzakwe karibia na mashamba ya zazibu ya Mjerumani-DODEP, maelezo zaidi utayapata huko huko, kinyume chake hautompata tena.
Wale vijana wa kazi, waliompa shughuli mkeo hainehaine! nimewazuia mimi tu wasiendelee kujilia uroda, walishambeba juu juu sasa hivi wakamfanyie radidi tena.
Vinginevyo watakesha nae kitandani. Tunakupa hadhari usijaribu katu kuleta ujanja wowote, ukihalafa tu utampoteza mkeo, kwanza ongea nae mkeo akusalimie.." baada ya kupita kitambo kifupi akaanza kusikia sauti ya mkewe iliyojaa majonzi na simanzi, "Pliiiz Beeebiii...help me pliiiz i'm in great trouble" akanyang'anywa simu alipoanza kukatwa hapo hapo simu hiyo kabla hajaendelea kuzungumza zaidi na mumewe.
Kachero Manu akabaki amenyong'onyea hajui cha kufanya bado ameishikilia simu yake sikioni. Akapata nguvu za kujaribu kuipiga tena ile namba ya wale watekaji ikawa haipatikani kuonyesha imezimwa tayari. Akajaribu kupiga maradufu lakini jibu likawa ni lile lile linalokera masikio yake asilotaka kulisikia.
Ikabidi Kachero Manu ampe mchapo mzima Kachero Yasmine na namna watakavyoweza kufanya maneva ya kivita ya kumuokoa mke wake na bado adui agonge mwamba asiweze kuwatoroka.
 
SEHEMU-22


Kachero Manu, alivyotoka ofisini kwa Meneja Bwana Kareem Abdallah tayari alikuwa kwenye rada za magaidi. Kuna vijana kama wanne walikuwa wanashinda pale gereji kama mafundi lakini wapo pale kwa kazi maalumu. Wakapewa jukumu la kumfuatilia nyendo zake. Hasa baada ya kuuliza maswali yanayohusisha kampuni ya 'Chops Carwash & Garage' na vifo vya Wabunge watano na madereva wao.
"Nimewaiteni kikao kifupi, naomba mfuatilie yule jamaa mtu aliyeingia ofisini kwangu sasa hivi. Namba zake za gari nakukabidhi wewe Jimmy mhakikishe hapotei kwenye rada zetu, mpaka tutakapopata maelekezo toka kambi kuu Jijini Tanga nini tumfanye" alifungua mazungumzo kwenye kikao kifupi Bwana Kareem Abdallah kilichofanyika ofisini kwake punde tu baada ya kutoka kwa Kachero Manu.
"Vipi tunaruhusiwa kuondosha uhai wake kama atatushtukia na kuamua kupambana na sisi?". Aliuliza Jimmy ambaye ndio alikuwa kiongozi wao huku akionekana umri wake ni takribani kijana wa makamo ya miaka 45, anayeikimbilia miaka ya rushudi. "Ikibidi hamna jinsi ila sitegemei iwe hivyo, wewe Jimmy achana na fikira tasa, wewe ni mzoefu wa mambo ya uhalifu tokea utoto wako, kumbuka wewe ukiwa na miaka 10 tu mwaka 1991 ulikuwa unawafanya watu wa Jiji la Dar es Salaam wanalala saa 12 jioni, kwa kuogopa kundi lako la watoto wenzako enzi hizo la 'Komando Yosso', hivyo sitegemei ushindwe kumfuatilia kwa umakini Mlugaluga kama yule" aliongea Bwana Kareem Abdallah, huku Jimmy akitikisa kichwa chake kuonyesha anakubali kile kinachoongewa na Bosi wake kuwa yeye alikuwa ni jambazi sugu kwa zaidi ya miaka 34.
Bila kuchelewa Jimmy akagawa majukumu kwa wenzake na kuanza kazi mara moja, kila mmoja akatawanyikia upande wake kutimiza majukumu yake. Wawili kati yao ndio wale aliopambana nao Kachero Manu kule chooni pale "Chako ni Chako bar" baada ya kuzuka suitafahamu baina yao.
Jimmy na mwenzake ndio waliomsindikiza Kachero Manu mpaka wakapajua nyumbani kwake bila ya yeye mwenyewe kutanabahi chochote. Hakuwahi kuwazia kama anaweza kufuatiliwa nyendo zake. Maana magaidi ni waoga sana ndio maana wanafanya matukio yao kwa kuvizia. Jimmy ambaye mwenyewe akipenda sana kujiita "Komando Yosso Veterani" alipopewa taarifa za kutekwa kwa Bosi wao Bwana Kareem, moja kwa moja akamtuhumu Kachero Manu kuhusika na figisufigisu zilizompata Bosi wao.
Nae akapanga mipango ya kulipiza kisasi kwa kumteka mkewe, ili wamtumie kama chambo cha kumrejesha Bosi wao kutoka mafichoni. Ili kuleta tashiwishi ya kufanya maamuzi ya haraka ya kumrejesha Bwana Kareem bila kusita wakawatumia wataalamu wao katika uhalifu wa kucheza na kompyuta wanaojua kuchezesha video. Wakampiga picha ya sehemu ya juu ya memsapu wake Kachero Manu, kuanzia chini ya kifua kuja juu, kisha wakaichanganya kiutaalamu mkubwa na mojawapo ya video za mcheza filamu za ngono nguli.
Ikawa ukiiangalia hiyo video utaamini moja kwa moja kuwa mke wa Kachero ndio anafanyiwa vitendo hivyo vya kifedhuli. Kwa sababu chini ya titi la kushoto la mke wa Kachero Manu kulikuwa na kovu dogo ambalo lilikuwa linaonekana dhahiri shahiri kwenye ile video feki.
Mbinu ambayo ilishafanikiwa tayari Kachero Manu alisharudisha mpira kwa golikipa, alishakubali yaishie. Hata siku moja usicheze na nguvu ya mapenzi, hamna boflo ngumu mbele ya chai ya mkandaa. Ilikuwa inasubiriwa muda tu Bwana 'Kareem Abdallah' akombolewe na washirika wake. Alijutia sana kwa uzembe wake laiti angekuwa ameongeza umakini angeshagundua kuwa kuna watu wanamwinda. Hamna mtu wa kawaida alikuwa anafahamu kama yeye ataenda kulala kwa mkewe hata Kachero Yasmine hakufamu wapi Bosi wake amelala usiku ule.
Ila alijiapiza "kwa vitendo hivi hobelahobela walivyomfanyia mke wangu nitahakikisha ninawatia adabu kwa mikono yangu mwenyewe mpaka wajutie uhuni walionifanyia" machozi yakawa yanamtiritika kama mtu mdogo, usicheze na maumivu ya kuchapiwa mke tena fauka ya kuchapiwa tena kwa mtindo wa mtungo na wahuni. Ambao afya zao hazijulikani kama wamesalimika na UKIMWI au magonjwa mengine ya zinaa.
Maumivu yake ni zaidi ya msiba. Aliona wamemfanyia unyama wa hali ya juu. Alikuwa anajijutia mkewe amemuingiza kwenye matatizo yasiyomhusu. Maana yeye mkewe alikuwa ni mtu rahimu na matendo yake ni hasanati hajawahi kumfanyia mtu yoyote matendo hasaisi yasiyoendana na utu.
"Wamenivua nguo hadhari, siwezi kuficha aibu hii, kujaribu kuficha ni sawa na kujikinga jua kwa kutumia ungo, nitauweka wapi uso wangu pindi wakiamua kuzirusha hizi video chafu kwenye mitandao ya kijamii kama Instagram, Facebook, Jamiiforums na hata Utube" alizidi kuwaza huku machozi yanazidi kutiririka kutoka kwenye mboni za macho bila kizuizi. Maji yalimfika shingoni Kachero Manu, magaidi walijua kulenga kunako.

Serikali ilipitisha maamuzi ya kuwa msako wa "Maso Square The Duduman" na genge lake la magaidi uwe ni wa kimya kimya. Ila picha za "Maso Square The Duduman" zikawa zimetawanywa kila kona ya nchi kuwa anatafutwa kwa udi na uvumba. Yeyote atayefanikisha kupatikana kwake aliahidiwa donge nono la milioni 100, na kuhakikishiwa ulinzi wa vyombo vya dola maisha yake yote.
Hata kwa misiba iliyotokea ya waheshimiwa wabunge na madereva wao, serikali iliamua maombolezo yawe kimya kimya, kusiwe na hashuo na kila mtu azikwe bila kutangaza kwa upana habari hizo kwenye vyombo vya habari. Lengo likiwa ni kumfanya adui asijue nini kinachopangwa na pia kuondosha hofu ya usalama kwa wananchi hivyo kuzorotesha uchumi wa nchi.
Ilipofika saa 12:00 jioni Kachero Yasmine alipowasha data tu ya simu yake ili apate kurambaza habari kwa njia ya mtandao, akaona meseji zimetiririka kwenye akaunti yake feki ya "Facebook". Kufungua tu alipoisoma tu akaanza kutabasamu, "Vipi Yasmine mbona furaha kama zote kulikoni unanipa jaka moyo" alichombeza Kachero Manu, kidogo kidogo alishaanza kuizoea hali ya kutekwa kwa mkewe. "Nimependwa na gaidi "Maso Maso" mwenzio anataka kunioa na picha yake kanitumia teh teh teh" alijibu kwa kujigamba Kachero Yasmine kuonyesha tayari ameshamuingiza kwenye mtego wa mapenzi. "Nilijua tu ile siku namna alivyokuwa anakuangalia alionyesha kabisa amekuzimikia vibaya sana, hongera sana Mrs. Maso Square keki ya harusi itakatwa kwa mtutu wa mtutu wa bunduki" aliongea Kachero Manu, utani ambao ulimuacha Kachero Yasmine akiwa hana hali kwa kicheko huku akimueleza Bosi wake alichowasiliana na "Maso Maso".
Nimeshampa masharti yangu kama anataka kunioa ndio nasubiria majibu yake". "Ila ukiangalia hii picha iliyotumwa ni ya kwake pasina shaka yoyote ila ni kama imechezewa kiutaalamu mkubwa ili usimgundue kuwa ni yeye anayetafutwa kwa hali na mali na vyombo vya dola, angalia sana sana haya masharubu hasa kwenye ncha hii inayogusa mashavu ni ya kuweka kabisa sio yake" alichangia mawazo yake Kachero Manu wakati anaiangalia kwa makini picha aliyotumiwa Kachero Yasmine na "Maso Maso" huku akionyesha masharubu hayo kwa ncha ya kidole chake cha shahada.
Wakaachana na habari za "Maso Maso", wakajisahaulisha kwa muda habari zake na kuchukua sasa ramani ya bonde la maji la Mzakwe ili waangalie wapi wataweza kutega mtego wao wa kuwafanya magaidi wasiwatoroke. Hilo ndio jukumu kubwa lililokuwa linawakabili mbele yao.
"Ehee...unaona hili bonde la Mzakwe lipo ndani ya bonde la Makutupora, na hiki ndio chanzo cha maji cha Jiji la Dodoma, sasa yumkini kuna ulinzi wa kutosha wa kulinda eneo hili la chanzo cha maji cha jiji. Pia kambi ya jeshi la kujenga taifa ya Makutupora ipo jirani na shamba la zabibu la DODEP, hawa wakijileta hawawezi kutoka kamwe" aligutuka kwa sauti kubwa Kachero Yasmine huku anasoza kidole kwenye ramani iliyokuwa imetandikwa mbele yao, baada ya kuitafakari ramani hiyo.
"Upo sahihi mia kwa mia hapa ramani inaonyesha kabisa njia za kuingilia kwenye shamba la zabibu ni mbili tu, unaweza kupitia njia ya Makutupora jeshini au ukapitia kijijini Veyula ukiliacha shamba la zabibu la kanisa unakata kulia, sasa hawa nadhani wamechagua hili eneo kututisha kuwa wana nguvu kubwa mpaka mateka wanampokelea karibu na kambi ya jeshi lakini ni mikwara tu, ni kama kelele za chura tu haziwezi kumzuia tembo kunywa maji" alizidi kuichambua Kachero Manu ramani ya bonde la Mzakwa.
"Kizuri zaidi ukiangalia kuanzia hapa tembea uwanda huu wote mpaka unakatiza hapa kijiji cha Mchemu wote hawa wamehamishwa wasije kuharibu chanzo cha mazingira, hivyo hapa ni pori hata tukilianzisha sokomoko hamna madhara yoyote kwa wananchi, bibi harusi wa gaidi mikono inawasha kabla sijaenda kuolewa na "Maso Maso", huko itakuwa ni mwendo wa majuba tu na kuswali tu saa zote sitopata muda tena wa kuipigania nchi yangu" aliendelea kuwekea tashdidi tafsiri ya ramani huku akichomekea utani Kachero Yasmine, utani ambao ulimchekesha Kachero Manu na kuzidi kumuondolea uchungu wa kutekwa kwa mkewe.
Wakaendelea kuisasambua ramani vilivyo, nje ndani mpaka wakakubaliana kuwa Kachero Yasmine atakuwa upande wa barabara inayotokea kijijini Veyula na Kachero Manu ataingilia barabara kuu ya kupitia jeshini, ili kama wakikimbia kwa kupitia njia ya kijijini Kachero Yasmine awazushie tifu. Somo la usomaji ramani ya dunia nzima ilikuwa ni moja ya somo la mtaala wao wa kikachero. Walikuwa wanafundishwa kitabu kimoja kinaitwa "The Red Atlas" kilichoandikwa na Bwana John Davies na Alexandaer Kent kikielezea namna Muungano wa Kisovieti ulivyofanikiwa kutengeneza ramani ya dunia nzima kwa mbinu mbalimbali.
Hivyo kuisoma ramani ya kijpande cha Mkoa ilikuwa kama kumsukuma mlevi kwenye utelezi. Hiyo ramani ya bonde la Mzakwe kwao ilikuwa maarifa tu ya somo la Jiografia kidato cha nne. Walichukua kama nusu saa tu kupata muwafaka wa pamoja baada ya kuhitalifiana hapa na pale katika namna ya kuwakabili maadui. Lakini mwishowe wakapata suluhisho la pamoja watakalolifuata. Wakawa tayari wameshapandwa na raghba ya kupambana na adui.
Wakaanza kutayarisha silaha zao na vifaa vingine wanavyohitaji kwa ajili ya usiku wa rabsha rabsha unaokuja. Walikuwa wamekaramka kwa furaha utasema wanaenda kuhudhuria harusi kumbe wanaenda kuziweka rehani roho zao kwenye usiku wa kufa au kupona.
 
hapo bonde la mzakwe ndo pazuri magaidi watabanwa na hivi kuna kambi ya makutopora cjui kama watachomoka poti all of all asante sana
 
SEHEMU-23



Usiku wa sokomoko katika Bonde la Mzakwe
Majira ya saa tano na nusu usiku, giza likiwa limetanda huku anga ikiwa imepambwa na idadi sufufu ya nyota na kipande kiduchu cha mwezi kilichojikata kuashiria tumeshaingia katika mwanzo wa mwezi mwandamo kwa mahesabu ya mzunguko wa mwezi.
Kachero Manu akiwa peke yake na mateka wake ndani ya gari yake aina ya "Subaru Forester" alikuwa ndio anaiacha taratibu barabara ya lami ya Arusha na kukata kona ya barabara ya kulia kuelekea barabara ya vumbi, yenye mashimo kochokocho yaliyojaza maji tobi kuonyesha mvua kubwa ilinyesha siku za karibuni. Pia njia hiyo inayoelekea kwenye shamba la mizabibu la DODEP ilikuwa na makorongo ya kutosha. Alikuwa anaendesha kwa kufuata maelezo toka kwa watekaji wa mkewe. Ambapo walimtaka asifuatane na mtu yoyote zaidi ya mateka wao Bwana 'Kareem Abdallah' peke yake.
"Simamisha gari hapo hapo ulipo kisha ushuke chini na Bwana Kareem" ilikuwa ni maelezo anayopewa Kachero Manu kupitia kwenye simu yake. Kila amri aliyopewa jibu likawa ni hewala! tu kwa Kachero Manu.
Maadui walikuwa wameshika mpini na yeye kakamata makali, hivyo wangeweza kumgeuza wanavyotaka. Alikuwa hawaoni walipojificha maadui zake. "Itakuwa wamejificha humu porini mapema sana, hivyo wamenichora mpaka namna nilivyoingia humu ndani ya eneo" aliwaza Kachero Manu huku akiwa amezima gari na kushuka na mateka wake ambaye bado alikuwa kwenye hali nzuri ya kiafya.
"Tembea mpaka kwenye ule mti wa mwarobaini uliopo mbele yako ukiwa na Bwana Kareem, hakikisha hauna simu wala silaha yoyote ile mfukoni". Kachero Manu akawa anatii kwa kufuata maelekezo aliyopewa. Alipotembea kwa mwendo wa kama dakika 3 akiwa hana hili wala lile, ghafla bin vuu likajitokeza gari linakuja kutokea pembezoni mwake upande wa kushoto kwa kasi huku limewasha taa zote kwa mwanga mkali.
Akiwa hajajua nini cha kufanya gari likawa tayari limeshafika likiwa limefungua mlango tayari, huku likiwa bado halijazimwa wakamdaka Bwana Kareem na kumtupia nyuma ya gari huku mkewe Kachero Manu nae akitupwa chini kama mzigo. Kisha gari likaondoka kwa mchepuko wa kasi kama gari za mashindano ya mbio kuelekea njia ile ile aliyoweka mtego Kachero Yasmine.
Mara moja bila kuzubaa Kachero Manu akambeba mgongoni mkewe akawa anakimbia nae kurudi kwenye gari yake aliyoiacha meta kadhaa aweze kwenda kumsaidia kachero Yasmine. "Pole sana baby, ndio matatizo ya dunia uliyoyapata hayana mwenyewe, haya uliyoyaonja ni thumuni tu yale ninayoonja mumeo kila siku katika kazi zangu" alisema huku anamuweka sawa kwenye kiti mkewe. Ambaye alijibu kwa ishara ya kutikisa kichwa tu kuashiria wapo pamoja katika shida na raha.
Alikuwa amevishwa vazi la kiislamu la baibui nyeusi lilisitiri mwili wake wote. Akawa analalamika baridi kali, ikabidi akilaze kiti na kuchukua koti lake na kumvika yeye kisha akamlaza kwa upole.
Wakati anajiandaa kuwasha swichi ya gari lake, ghafla akaanza kusikia mirindimo ya risasi mfululizo kutokea upande ule ule walioelekea wale magaidi. "Kazi imeanza Ustaadhati Yasmine anawabatiza magaidi kwa mtutu wa bunduki" alijisemea pole pole Kachero Manu.
Akaanza kulitoa gari taratibu kuelekea upande ule ule walioelekea magaidi. Akaendesha mpaka sehemu fulani yenye kichaka akaiegesha. Kisha akabeba mtutu wake kukimbilia eneo la tukio bila kuaga kwa mkewe, akimuacha anakoroma akiwa ameshonwa na usingizi mzito unaotokana na uchovu wa sulubu za watekaji zilizomkosesha mapumziko ya raha.

Kachero Yasmine akiwa amejificha kwenye fukutu la nyasi, akiwa amejitandazia nyasi mwili mzima ulikuwa huwezi kudhani kama amejificha mtu kwenye kichaka hicho. Mwili wake ukiwa umevikwa kombati maalumu zilizokuwa zimechafuka matope kutokana na kutuama kwa maji kwenye eneo alilokuwepo.
Alikuwa ameshajichimbia hapo kwenye kichaka kwa karibia saa tatu timilifu, huku akiomba Mungu magaidi wapite njia hiyo. Walijua fika hawawezi kupita njia kuu ya jirani na kambi ya jeshi watapewa kichapo cha mbwa koko. Kuna wakati bonge la joka lenye urefu zaidi ya futi 8 lilimtambaa mwilini kuanzia kwenye buti miguuni, na kutambaa mpaka kuja kutokezea kichwani kwa kupanda kwenye kofia yake na kutokomea zake kwenye kichaka, likiwa kwenye harakati zake za kuwinda mawindo yake. Kwa ujasiri mkubwa bila kujitikisa aliliacha limfanye linavyotaka.
Mbu nao hawakubaki nyuma kumletea kero ya udungaji wa maumivu, lakini hawakuwa kikwazo kwake kutimiza lengo lake. Kuna wakati upepo ulivyokuwa unapuliza na miti kutingishika, huku sauti ya vyura ikirindima kwenye vifereji vidogo vidogo. Popo nao walikuwa katika harakati zao za kujitafutia maisha usiku huo wanahama mti mmoja na kuhamia mwingine. Ulikuwa ni msitu wenye kuogofya hasa nyakati za usiku kwa mtu mwenye roho nyepesi. Ukichanganya sauti ya mvumo wa upepo, kelele za vyura, na mtikiso wa matawi ya miti kulikuwa kunapatikana burudani fulani ya sauti yenye kuvutia inayobembeleza kwa msikilizaji na mwili kupata raha. Hiyo hali ikawa inataka kupelekea kope za macho yake ziwe nzito, usingizi ulikuwa unataka kuanza kumnyemeleza na kumpiga dafrau kipindi cha hatari.
Lakini akikumbuka ukubwa wa nguvu za adui ambaye ana nguvu ya kiuchumi, askari watiifu wanaopiga kwa malengo ya kusimamisha utawala wa kiislamu na waliofuzu mafunzo, usingizi wote ukayeyuka kama samli ndani ya moto. Akashtukizwa na kelele za gari linalokuja kasi huku limewasha taa zote kuashiria kuna hatari. Likiwa kwenye umbali wa kama mita kumi akaikoki vizuri silaha yake aina ya "Submachine Gun" aliyoifanyia utundu kuongeza manjonjo yake.
Bila kujiuliza mara mbili mbili akaanza kuzifyatua risasi kama njugu mfululizo, huku akilenga usawa wa kiti cha dereva na abiria. Kachero Yasmine alikuwa ni mtaalamu wa matumizi ya mkono wa kushoto, hakukosi shabaha kijinga akikuwinda risasi. Lengo la kupiga mfululizo ilikuwa ni kuwachanganya maadui wajue kama wamezingirwa na wapiganaji wengi. Mbinu ilijibu vyema, magaidi walipigwa na taharuki, lilikuwa ni shambulizi la kushtukiza kwao hawakutegemea kuzingirwa kirahisi.
Walianza kupiga risasi mfululizo bila mpangilio wowote. Kachero Yasmine kuzima mzizi wa fitina, akabahatisha kubutua matairi ya mbele yote ya gari lao, kwa kuwa lilikuwa kwenye kasi kubwa likayumba na kwenda kujibamiza kwenye mti mkubwa na kuzalisha kishindo kikubwa, na kupelekea gari kupinduka vibaya zaidi ya mara nne, kisha likatulia tuli.
Akasubirishia kama robo saa kuona labda kuna mtego wametegewa akaona kimya. Akawa anachomoka porini huku anakuja wanguwangu kwa kujiamini, akashtukia risasi mbili zinapigwa uelekeo ule ule anakokwenda, akajitupa chini haraka haraka na kuanza kutambaa. Kachero Manu akaanza kuita kwa sauti ya kupaliza iliyokuwa inasikia vizuri "Yasmiiiinee... njoo game is over...!".
Kachero Yasmine alivyosikia hivyo akasita kujitokeza mpaka alivyoisikia tena na kuhakikisha ni sauti ya Kachero Manu akajitokeza mbele ya gari la maadui na kulakiwa na Kachero Manu ambaye nae ndio alikuwa anafika, wakakutana ndindaninda.
“Kazi zuri Kachero Yasmine, nilivyokuwa nazisikia njugu zinatemwa nikajisemea kazi ipo leo Mpemba kashapandisha maruhani yake, maana anuwai yako ya ufyatuaji wa risasi imejipambanua kwangu, wakasalimu magaidi wenzao huko kuzimu" alitoa pongezi Kachero Manu huku akamkumbatia akisifu umahiri uliomfanya awe kama mtazamaji mpira uwanjani, ambaye anashangilia magoli yaliyofungwa na wachezaji.
"Na wewe ahsante kwa kuokoa uhai wangu nilijua nimewamaliza wote kumbe kuna mmoja alikuwa ananivizia nije anidokoe vizuri" Kachero Yasmine alitoa shukrani kwa mwenzake. Ni ukweli tungerudisha jina tu Pemba maana alikuwa pale pembeni ya mti anakuvizia tu ujilete" alijibu Kachero Manu kiufahari. Mara moja bega kwa bega wakaanza upekuzi mle ndani ya gari aina "Jeep kibanda wazi" la maadui.
Wakakuta kulikuwa na magaidi wapambanaji wa kiume 4 pamoja na dereva wao, na mateka wao waliyemkomboa Bwana Kareem Abdallah wakiwa wote wamepoteza maisha. Huku tafrija ya damu ikiwa imetapakaa kwenye gari. Damu ambayo ilitokana na mipigo ya risasi kutoka kwenye silaha ya Kachero Yasmine na kutokana na majeraha ya ajali mbaya ya gari lao. Wakamkuta pia mwanamke mmoja akiwa bado anapigania roho yake amezimia anapumua kwa mbali lakini ana majeraha makubwa kichwani.
"Huyu tumkimbize hospitalini hapo jeshini, tuombe gari la wagonjwa wampeleke Hospitali ya Mkoa" alitoa ushauri wenye mbolea Kachero Yasmine. "Upo sahihi feli bilahi kupona au kutokupona ni majaliwa ya Mwenyezi Mungu" aliongea Kachero Manu kuonyesha kukubaliana na ushauri wa mwenzake. Wakati wanamuweka nguo zake vizuri ikaonekana bahasha nzito ngumu ya kaki imechimbiwa kwenye nguo ya ndani inachungulia. Ikabidi Kachero Yasmine aitoe, na kuanza kuifungua kwa kuchana gundi yake ngumu iliyogandishwa. Alipofanikiwa kuifungua zikajitokeza pesa za kigeni dola za kimarekani kitita kisichopungua dola $10,000 baada ya kuhesabiwa kwa haraka haraka. Kisha wakakuta na barua imevirigiwa kwenye bahasha ndogo. Akapatwa na udadisi wa kuifungua, alipoifungua tu, Kachero Manu kwa msaada wa tochi akaanza kummulikia Kachero Yasmine asome
IMG-20200618-WA0012.jpg
 
Back
Top Bottom