SEHEMU-22












Kachero Manu, alivyotoka ofisini kwa Meneja Bwana Kareem Abdallah tayari alikuwa kwenye rada za magaidi. Kuna vijana kama wanne walikuwa wanashinda pale gereji kama mafundi lakini wapo pale kwa kazi maalumu. Wakapewa jukumu la kumfuatilia nyendo zake. Hasa baada ya kuuliza maswali yanayohusisha kampuni ya 'Chops Carwash & Garage' na vifo vya Wabunge watano na madereva wao.
"Nimewaiteni kikao kifupi, naomba mfuatilie yule jamaa mtu aliyeingia ofisini kwangu sasa hivi. Namba zake za gari nakukabidhi wewe Jimmy mhakikishe hapotei kwenye rada zetu, mpaka tutakapopata maelekezo toka kambi kuu Jijini Tanga nini tumfanye" alifungua mazungumzo kwenye kikao kifupi Bwana Kareem Abdallah kilichofanyika ofisini kwake punde tu baada ya kutoka kwa Kachero Manu.
"Vipi tunaruhusiwa kuondosha uhai wake kama atatushtukia na kuamua kupambana na sisi?". Aliuliza Jimmy ambaye ndio alikuwa kiongozi wao huku akionekana umri wake ni takribani kijana wa makamo ya miaka 45, anayeikimbilia miaka ya rushudi. "Ikibidi hamna jinsi ila sitegemei iwe hivyo, wewe Jimmy achana na fikira tasa, wewe ni mzoefu wa mambo ya uhalifu tokea utoto wako, kumbuka wewe ukiwa na miaka 10 tu mwaka 1991 ulikuwa unawafanya watu wa Jiji la Dar es Salaam wanalala saa 12 jioni, kwa kuogopa kundi lako la watoto wenzako enzi hizo la 'Komando Yosso', hivyo sitegemei ushindwe kumfuatilia kwa umakini Mlugaluga kama yule" aliongea Bwana Kareem Abdallah, huku Jimmy akitikisa kichwa chake kuonyesha anakubali kile kinachoongewa na Bosi wake kuwa yeye alikuwa ni jambazi sugu kwa zaidi ya miaka 34.
Bila kuchelewa Jimmy akagawa majukumu kwa wenzake na kuanza kazi mara moja, kila mmoja akatawanyikia upande wake kutimiza majukumu yake. Wawili kati yao ndio wale aliopambana nao Kachero Manu kule chooni pale "Chako ni Chako bar" baada ya kuzuka suitafahamu baina yao.
Jimmy na mwenzake ndio waliomsindikiza Kachero Manu mpaka wakapajua nyumbani kwake bila ya yeye mwenyewe kutanabahi chochote. Hakuwahi kuwazia kama anaweza kufuatiliwa nyendo zake. Maana magaidi ni waoga sana ndio maana wanafanya matukio yao kwa kuvizia. Jimmy ambaye mwenyewe akipenda sana kujiita "Komando Yosso Veterani" alipopewa taarifa za kutekwa kwa Bosi wao Bwana Kareem, moja kwa moja akamtuhumu Kachero Manu kuhusika na figisufigisu zilizompata Bosi wao.
Nae akapanga mipango ya kulipiza kisasi kwa kumteka mkewe, ili wamtumie kama chambo cha kumrejesha Bosi wao kutoka mafichoni. Ili kuleta tashiwishi ya kufanya maamuzi ya haraka ya kumrejesha Bwana Kareem bila kusita wakawatumia wataalamu wao katika uhalifu wa kucheza na kompyuta wanaojua kuchezesha video. Wakampiga picha ya sehemu ya juu ya memsapu wake Kachero Manu, kuanzia chini ya kifua kuja juu, kisha wakaichanganya kiutaalamu mkubwa na mojawapo ya video za mcheza filamu za ngono nguli.
Ikawa ukiiangalia hiyo video utaamini moja kwa moja kuwa mke wa Kachero ndio anafanyiwa vitendo hivyo vya kifedhuli. Kwa sababu chini ya titi la kushoto la mke wa Kachero Manu kulikuwa na kovu dogo ambalo lilikuwa linaonekana dhahiri shahiri kwenye ile video feki.
Mbinu ambayo ilishafanikiwa tayari Kachero Manu alisharudisha mpira kwa golikipa, alishakubali yaishie. Hata siku moja usicheze na nguvu ya mapenzi, hamna boflo ngumu mbele ya chai ya mkandaa. Ilikuwa inasubiriwa muda tu Bwana 'Kareem Abdallah' akombolewe na washirika wake. Alijutia sana kwa uzembe wake laiti angekuwa ameongeza umakini angeshagundua kuwa kuna watu wanamwinda. Hamna mtu wa kawaida alikuwa anafahamu kama yeye ataenda kulala kwa mkewe hata Kachero Yasmine hakufamu wapi Bosi wake amelala usiku ule.
Ila alijiapiza "kwa vitendo hivi hobelahobela walivyomfanyia mke wangu nitahakikisha ninawatia adabu kwa mikono yangu mwenyewe mpaka wajutie uhuni walionifanyia" machozi yakawa yanamtiritika kama mtu mdogo, usicheze na maumivu ya kuchapiwa mke tena fauka ya kuchapiwa tena kwa mtindo wa mtungo na wahuni. Ambao afya zao hazijulikani kama wamesalimika na UKIMWI au magonjwa mengine ya zinaa.
Maumivu yake ni zaidi ya msiba. Aliona wamemfanyia unyama wa hali ya juu. Alikuwa anajijutia mkewe amemuingiza kwenye matatizo yasiyomhusu. Maana yeye mkewe alikuwa ni mtu rahimu na matendo yake ni hasanati hajawahi kumfanyia mtu yoyote matendo hasaisi yasiyoendana na utu.
"Wamenivua nguo hadhari, siwezi kuficha aibu hii, kujaribu kuficha ni sawa na kujikinga jua kwa kutumia ungo, nitauweka wapi uso wangu pindi wakiamua kuzirusha hizi video chafu kwenye mitandao ya kijamii kama Instagram, Facebook, Jamiiforums na hata Utube" alizidi kuwaza huku machozi yanazidi kutiririka kutoka kwenye mboni za macho bila kizuizi. Maji yalimfika shingoni Kachero Manu, magaidi walijua kulenga kunako.












Serikali ilipitisha maamuzi ya kuwa msako wa "Maso Square The Duduman" na genge lake la magaidi uwe ni wa kimya kimya. Ila picha za "Maso Square The Duduman" zikawa zimetawanywa kila kona ya nchi kuwa anatafutwa kwa udi na uvumba. Yeyote atayefanikisha kupatikana kwake aliahidiwa donge nono la milioni 100, na kuhakikishiwa ulinzi wa vyombo vya dola maisha yake yote.
Hata kwa misiba iliyotokea ya waheshimiwa wabunge na madereva wao, serikali iliamua maombolezo yawe kimya kimya, kusiwe na hashuo na kila mtu azikwe bila kutangaza kwa upana habari hizo kwenye vyombo vya habari. Lengo likiwa ni kumfanya adui asijue nini kinachopangwa na pia kuondosha hofu ya usalama kwa wananchi hivyo kuzorotesha uchumi wa nchi.
Ilipofika saa 12:00 jioni Kachero Yasmine alipowasha data tu ya simu yake ili apate kurambaza habari kwa njia ya mtandao, akaona meseji zimetiririka kwenye akaunti yake feki ya "Facebook". Kufungua tu alipoisoma tu akaanza kutabasamu, "Vipi Yasmine mbona furaha kama zote kulikoni unanipa jaka moyo" alichombeza Kachero Manu, kidogo kidogo alishaanza kuizoea hali ya kutekwa kwa mkewe. "Nimependwa na gaidi "Maso Maso" mwenzio anataka kunioa na picha yake kanitumia teh teh teh" alijibu kwa kujigamba Kachero Yasmine kuonyesha tayari ameshamuingiza kwenye mtego wa mapenzi. "Nilijua tu ile siku namna alivyokuwa anakuangalia alionyesha kabisa amekuzimikia vibaya sana, hongera sana Mrs. Maso Square keki ya harusi itakatwa kwa mtutu wa mtutu wa bunduki" aliongea Kachero Manu, utani ambao ulimuacha Kachero Yasmine akiwa hana hali kwa kicheko huku akimueleza Bosi wake alichowasiliana na "Maso Maso".
Nimeshampa masharti yangu kama anataka kunioa ndio nasubiria majibu yake". "Ila ukiangalia hii picha iliyotumwa ni ya kwake pasina shaka yoyote ila ni kama imechezewa kiutaalamu mkubwa ili usimgundue kuwa ni yeye anayetafutwa kwa hali na mali na vyombo vya dola, angalia sana sana haya masharubu hasa kwenye ncha hii inayogusa mashavu ni ya kuweka kabisa sio yake" alichangia mawazo yake Kachero Manu wakati anaiangalia kwa makini picha aliyotumiwa Kachero Yasmine na "Maso Maso" huku akionyesha masharubu hayo kwa ncha ya kidole chake cha shahada.
Wakaachana na habari za "Maso Maso", wakajisahaulisha kwa muda habari zake na kuchukua sasa ramani ya bonde la maji la Mzakwe ili waangalie wapi wataweza kutega mtego wao wa kuwafanya magaidi wasiwatoroke. Hilo ndio jukumu kubwa lililokuwa linawakabili mbele yao.
"Ehee...unaona hili bonde la Mzakwe lipo ndani ya bonde la Makutupora, na hiki ndio chanzo cha maji cha Jiji la Dodoma, sasa yumkini kuna ulinzi wa kutosha wa kulinda eneo hili la chanzo cha maji cha jiji. Pia kambi ya jeshi la kujenga taifa ya Makutupora ipo jirani na shamba la zabibu la DODEP, hawa wakijileta hawawezi kutoka kamwe" aligutuka kwa sauti kubwa Kachero Yasmine huku anasoza kidole kwenye ramani iliyokuwa imetandikwa mbele yao, baada ya kuitafakari ramani hiyo.
"Upo sahihi mia kwa mia hapa ramani inaonyesha kabisa njia za kuingilia kwenye shamba la zabibu ni mbili tu, unaweza kupitia njia ya Makutupora jeshini au ukapitia kijijini Veyula ukiliacha shamba la zabibu la kanisa unakata kulia, sasa hawa nadhani wamechagua hili eneo kututisha kuwa wana nguvu kubwa mpaka mateka wanampokelea karibu na kambi ya jeshi lakini ni mikwara tu, ni kama kelele za chura tu haziwezi kumzuia tembo kunywa maji" alizidi kuichambua Kachero Manu ramani ya bonde la Mzakwa.
"Kizuri zaidi ukiangalia kuanzia hapa tembea uwanda huu wote mpaka unakatiza hapa kijiji cha Mchemu wote hawa wamehamishwa wasije kuharibu chanzo cha mazingira, hivyo hapa ni pori hata tukilianzisha sokomoko hamna madhara yoyote kwa wananchi, bibi harusi wa gaidi mikono inawasha kabla sijaenda kuolewa na "Maso Maso", huko itakuwa ni mwendo wa majuba tu na kuswali tu saa zote sitopata muda tena wa kuipigania nchi yangu" aliendelea kuwekea tashdidi tafsiri ya ramani huku akichomekea utani Kachero Yasmine, utani ambao ulimchekesha Kachero Manu na kuzidi kumuondolea uchungu wa kutekwa kwa mkewe.
Wakaendelea kuisasambua ramani vilivyo, nje ndani mpaka wakakubaliana kuwa Kachero Yasmine atakuwa upande wa barabara inayotokea kijijini Veyula na Kachero Manu ataingilia barabara kuu ya kupitia jeshini, ili kama wakikimbia kwa kupitia njia ya kijijini Kachero Yasmine awazushie tifu. Somo la usomaji ramani ya dunia nzima ilikuwa ni moja ya somo la mtaala wao wa kikachero. Walikuwa wanafundishwa kitabu kimoja kinaitwa "The Red Atlas" kilichoandikwa na Bwana John Davies na Alexandaer Kent kikielezea namna Muungano wa Kisovieti ulivyofanikiwa kutengeneza ramani ya dunia nzima kwa mbinu mbalimbali.
Hivyo kuisoma ramani ya kijpande cha Mkoa ilikuwa kama kumsukuma mlevi kwenye utelezi. Hiyo ramani ya bonde la Mzakwe kwao ilikuwa maarifa tu ya somo la Jiografia kidato cha nne. Walichukua kama nusu saa tu kupata muwafaka wa pamoja baada ya kuhitalifiana hapa na pale katika namna ya kuwakabili maadui. Lakini mwishowe wakapata suluhisho la pamoja watakalolifuata. Wakawa tayari wameshapandwa na raghba ya kupambana na adui.
Wakaanza kutayarisha silaha zao na vifaa vingine wanavyohitaji kwa ajili ya usiku wa rabsha rabsha unaokuja. Walikuwa wamekaramka kwa furaha utasema wanaenda kuhudhuria harusi kumbe wanaenda kuziweka rehani roho zao kwenye usiku wa kufa au kupona.











