RIWAYA-MSAKO WA MWEHU
SEHEMU YA KUMI NA SABA
Kachero Manu baada ya kutua mezani kile chakula akaingiza mkono wake wa kulia kiunoni upande wa kulia ili achomoe bastola yake awaweke chini ya ulinzi. Akashtukia tayari amewahiwa yeye kwa kufyatuliwa risasi ya mkono wake wa kulia iliyopiga kwenye kidole gumba chake na kuitupa bastola yake mita kadhaa. "Tumevamiwa kiongozi changamkaaaaa....tusepe mshenzi mbele yetu!" zilikuwa ni kelele za "Maso Maso" zilizomzindua Inspekta Haroub Farouq na kufahamu kuwa hali sio shwari tena mle chumbani.
Akaziachia zile nyaraka kisha akaruka kama samaki mkizi kumrukia Kachero Manu ambaye alikuwa anajiandaa kuifuata bastola yake. Wakaanguka wote kwa pamoja chini ya sakafu pwatwaa. Wakaanza mbiringembiringe za kufirigisana, kupapatuana na kuviringishana mieleka pale ardhini chumbani, wakawa wanapinduana kwa zamu juu chini chini juu, wanapimana ugali.
Ndio nafasi aliyokuwa anaitafuta "Maso Maso", hakutaka kupambana na vyombo vya dola muda huu, wakati kazi aliyotumwa bado mbichi hata robo hajaimaliza. Akapiga risasi moja taa ya chumbani ikamuitikia kwa mlio wa paaah...!!. Giza likatawala chumbani totorooo..!!. Kama nyani vile anavyodaka ndizi akarukia kibegi chake kitandani na kuanza kuparamia ukutani kama chui akafanikisha kutoboa dari la "gypsum" na kuingia juu ya kenchi la hoteli.
Alipoangaza chini kwa kwa tabu, macho yake yalianza kuzoea giza akaona bado Inspekta Haroub na Kachero Manu wanachuana, lakini Inspekta Haroub anaelekea kutepeta hawezi kupambana na kijana kama yule. Mara ikasikika sauti nyingine ya paaaaah...!!paaaah....!! "Aaaaaah mamaaaa naku....f...a...aaa!", ilikuwa sauti ya Inspekta Haroub akilalamikia maumivu baada ya kulambwa shaba mbili takatifu za kichwani na shingoni, zilizomfanya apoteze maisha pale pale.
"Maso Maso" aliamua kumtwanga risasi Inspekta Haroub kupoteza ushahidi, alifahamu fika akiwa hai mateso atakayopewa ataropoka kila kitu, harafu ataharibu mipango yote. Akaanza kukwava kwa kutumia msaada wa mwangaza wa tochi ya simu akiwa juu ya dari. Mpaka akafika kwenye boksi mbalimbali za kuunganisha waya toka sehemu mbalimbali za hoteli. Akawa anakata na kufumua hizo nyaya kwa kutumia koleo. Baada ya zoezi hilo hoteli nzima ikawa giza na kusababisha mlipuko ulitikisa mtaa mzima.
Kachero Manu alipowasha taa ya simu yake akapigwa na butwa baada ya kuona dari juu ya chumba limefumuliwa. Akabaki amebung'aa tu, akajiongeza tu ukiona manyoya jua ameliwa, alishatorokwa zamani. Alikuwa hajawahi kushuhudia binadamu mwenye kufanya mambo yake kwa kasi ya haraka kama alivyofanya "Maso Maso".
Akafungua mlango na kuchomoka kasi nje ya chumba huku akiwa na bastola yake mkono mmoja na mwingine kashikia tochi ya simu. Akajikuta wamekumbana mzima mzima wenyewe kwa wenyewe na Kachero Yasmine ambaye nae alikuwa anakuja wanguwangu chumbani kwa Inspekta Haroub, maana ilishapita nusu saa walioahidiana, akajua fika mambo huko yamechacha chumbani kwa Inspekta Haroub. Wakanyanyuka wote haraka haraka wakiharakisha kutoka nje ya hoteli kuzidi kuimarisha ulinzi ili asiwatoroke. Mambo yalikuwa mpwitompwito yamenoga tayari.














Alishatambaa kama dakika 12 na ushee akiwa juu ya kenchi huku jasho linamtiririka kama maji kwa joto lake lenye kushitadi haswa. Akaamua sasa liwalo na liwe lazima atoboe tundu tena hapo hapo alipo. Akaanza kupapachua tundu kwa vidole vyake. Tundu lilipokuwa kubwa lenye uwezo wa kupitisha kiwiliwili cha mwanadamu akaanza kunusa harufu ya vyakula, hisia zikamtuma huenda ikawa ni jikoni. Alipochungulia vizuri akamkuta babu mpishi kala chumvi kiasi chake akiwa kwenye sare zake za kazi anahangaika huku na kule na kutekeleza majukumu yake ya kazi. Ametingwa na kusokotwa na jukumu la kuchoma nyama huku amewasha taa za kuchaji zinazomsaidia kuona vizuri ili asiunguze nyama za wateja ikawa kesi.
Bila kufanya ajizi akateremka jumlajumla kwa kushtukiza na kutua juu ya sinki ya kuoshea vyombo. Babu wa jikoni alishtukia baada ya kuona vyombo vichafu kwenye sinki vimetoa mlio wa kuvunjika baada ya kudondoka chini. Akashindwa hata kukimbia kwa kihoro alichonacho, akaanguka ndengu chini na kuzimia kwa uoga hasa alivyoona mtu aliyeshuka kavaa nguo nyeupe, fikra zake zikamtuma huenda mzuka umemshukia.
Bila kuchelewa, akaanza kumburuza taratibu yule mpishi mpaka akamfikisha kwenye stoo ya vyakula, akamuingiza na kujifungia nae. Akatoa zana za kazi kwenye kibegi chake hima hima, akajinyoa ndevu zake haraka kwa kutumia mwangaza wa tochi ya simu, kisha akavaa sura ya bandia. Akawa amevua nusu kanzu na pajama la chini yake.
Akawa juu amebakia na singilendi nyeupe na bukta la ndani tu akavaa nguo za babu mpishi. Muda wa rakaateni usiozidi hata dakika 2 tokea amzimishe, ghafla wakaja askari njagu kama 3 kule jikoni wakiwa na tochi zao mikononi na bastola. "Aisee...lipishi hujaliona lijitu limepita huku kavaa kanzu nyeupe kama Osama?" aliuliza mmoja wa njagu wale kwa lafudhi zao za kinoko, akionekana ni mpya katika kazi ndio kwanza ametoka chuoni CCP-Moshi karibuni hivyo ana usongo wa kazi. "Maso Maso" akazuga kuchomoka na gunia la viazi jikoni anakuja nalo usoni mwa askari wanguwangu na kulibwaga kwa kishindo mbele yao.
"Hapana mkuu sijamuona kabisaaa huku nipo peke yangu" akajibu "Maso Maso" kwa kujiamini huku akijitia anakimbilia kuchukua jalo la kubebea samaki na kuwaweka samaki kwenye mafuta yaliyokuwa tayari yamepata moto yanatoa ule moshi wa kuonyesha yameshapashika moto vilivyo. Wale askari kwa pupa huku bastola zipo mkononi mwao wakaondoka jikoni mbio mbio kuelekea kusikojulikana, wakijiridhisha yule ni mpishi kutokana na nguo nyeupe aliyovaa na kigiza giza kilichopo.
Laiti wangemulika tochi zao tu darini, ndipo "Maso Maso" angetambua hamna bamvua lisilo na usubi, lakini wapi hawakupata mawazo hayo, na arobaini yake ilikuwa bado kutimu. Uamuzi wa Mungu hushinda mizungu, ahadi yake ya kukamatwa ilikuwa bado kutimu. Daima ubaya hatima yake mbaya tu. Chapuchapu kwa mwendo wa mateka, "Maso Maso" akabeba kibegi chake akatoka nje ya jiko akatembea kwenye veranda mpaka akatoka kwenye bustani ya nje iliyopo ndani ya ukuta wa hoteli.
Akakuta makundi ya wafanyakazi na baadhi ya wateja wamejikusanya vikundi vikundi wanazogoa kwa uwoga, macho yao yamepigwa na taharuki hawajui cha kufanya. Maswahibu yamewakumba Wallahi wanasubiria kudura ya Manani na nusra yake, mithili ya ng'ombe aliyeingia kwenye kumi na nane za mchinjaji anasubiria tu shingo yake itenganishwe na mwili wake watu wakajisosomole kwenye supu. Akawapuuza na kuachana nao, alipotupa jicho kwenye uwazi wa vidirisha vya ukuta akaona kuna polisi kibao na mbwa wametanda.
Akakata tamaa ya kuokoka kirahisi bila kutumia akili ya kuzaliwa,"natakiwa nicheze kama Pelle wa Brazili na timu yake ya Santos nikibugi tu wataniletea ukuda". Akiwa kwenye lindi zito la mawazo ya kujiokoa, akaanza kusikia ving'ora nje ya Hoteli vimeongezeka, akajua hapa leo hatumwi mtoto dukani. Wana usalama walikuwa wanaongezeka idadi yao, sasa walikuwa wanajeshi ndugu zao akina Marwa na Chacha ndio wanatia timu.
"Maso Maso" kwa tahadhari kubwa akaanza kurudi nyuma nyuma kwa tahadhari kubwa kwa mwendo wa kunyata huku akielekea usawa wa nje wa jiko. Akawa kama kuna kitu anakitafuta kilichopotea. Utafutaji wake ulikuwa wa umakini mkubwa utasema mgonjwa aliyeenda kutafuta tiba, kisha akaagizwa na kalumanzila wake amtafute sisimizi mjamzito aweze kupona.
Utafutaji wake alikuwa huku anamulika na mwangaza wa tochi yake ya simu. Akajawa na furaha ya ghafla baada ya kuona alichokuwa anakitafuta. Akaanza kujipiga mangumi mfululizo kifuani mwake kujipongeza kwa ushujaa wake. Kifua chake kila anapokuwa anakipiga kikawa kinatoa sauti kama taruma la reli, kuonyesha kimekubali shuruba za mazoezi magumu. Akasimama katikati na kitu alichokuwa anakitafua akatoa zana za kazi kwenye kibegi chake na kuzima simu yake. Akawa anasikia kwa mbali inatoka amri kwenye spika sasa watu waliopo kwenye jengo la Hoteli wajisalimishe, waanze kutoka nje ya jengo.
Walielekezwa kupitia magetini huku wakiwa na vitambulisho vyao rasmi vinavyowatambulisha. Taa kubwa maalumu zikiwa kwenye magari zikawashwa kuangaza eneo zima pale. Msururu wa foleni ukapangwa kwa ajili ya ukaguzi wa uso kwa uso. Huku wanajeshi waliowasili punde tu wakiamua kuanza msako wa ndani ya jengo wa chumba mpaka chumba.
Leo kwa mara ya kwanza wanajeshi na polisi walikuwa wanashirikiana kwa pamoja. Mara nyingi hawa wawili walikuwa hawapaliani moto. Akajisemea "Maso Maso" "sasa ugali moto, mboga moto, wanajiapiza lazima atiwe mbaroni "Maso Maso" mtoto wa Bi.Mwantumu, kishindo changu hawaniwezi, mpaka wataniimba jina langu usiku na mchana Bara na Visiwani nchi nzima. Kishindo changu hawakiwezi" aliwazaKkisha akatabasamu. Tabasamu la kuwazidi akili wana usalama lukuki.













ITAENDELEA
Maso Maso Mwehu kawaacha kwenye mataa Makachero,kawachomokaje??Kwa mbinu gani??