Riwaya: Msako wa mwehu

Riwaya: Msako wa mwehu

SEHEMU-26

Kwa umbile lake alikuwa ni kibushuti mfupi haswa, pandikizi la mtu akiwa ni mweusi tii kama pipa la lami huku uso wake ukiwa una makovu ya kutosha kuonyesha amepitia mikiriti na mikutuo mbalimbali ya mapigano. Huku macho yake yakiwa na makengeza, macho kumberu. Alikuwa amefuga ndevu lakini zilikuwa zimemkataa hazijanawiri vilivyo, hazina rutuba zikawa kuna sehemu kidevuni zimejikusanya kama mkutano wa inzi. Kichwani alikuwa amejifunga kilemba cha rangi nyeupe kilichokuwa kinang'ara vilivyo. Alikuwa anatisha ukimuangalia mwonekano wake hakuwa na uso wa jamala wala wenye haiba ya mvuto. Uso wake haukuvaa hata chembe la tabasamu, ulimvimba kama mvua ya masika. Alikuwa akiongea anaunguruma kama radi, sauti ya punda. Akaanza hotuba yake fupi iliyojaa amri na vitisho. "Salaam Aleikum Jamiiia, ama baada ya salamu sina mengi, kwanza nimeletewa taarifa tumepata 'Mujaahidu' mmoja amesilimu na moja kwa moja amekuja kwenye viwanja vya jihadi" akavuta pumzi kidogo kabla akaendelea. Zikaanza kulipuka kelele za vishindo vya sauti za maneno ya kiarabu "Takbiiiiiir......Allahu Akbaru, Takbiiiiiir.......Allahu Akbar" wakionyesha wamefurahia kwa huyo mgeni aliyeamua kuachana na maisha ya anasa za kidunia na kuamua kujiunga nao maporini kuja kupigania vita vya jihadi. Hapo alikusudia kuwapa taarifa za ujio wa Kachero Manu pale msikitini kwao.
Kisha baada ya vishindo hivyo akaendelea, "kizuri zaidi nimepata taarifa aliwahi kupitia jeshini lakini akashindwana nao hao madhalimu akaacha kazi miaka kama mitano iliyopita, kwa hiyo msisite kumtumia kwenye baadhi ya mambo" akakoma kuzungumza huku macho ameyakazia alipo Kachero Manu.
"Asalaaam Aleikuuum ndugu zangu katika imani ya haki, mimi ndugu yenu nilikuwa naitwa 'Raphael Kitokambali' lakini baada ya kuiona taa ya Uislamu sasa naitwa Abubakari" akasimama kuendelea kujitambulisha Kachero Manu baada ya vishindo vizito tena vya takbira vilivyokuwa vinakaribia kutaka kuezua paa la msikiti huo wa matofali ya kuchoma. "Nimechagua jina la Aboubakr kwa sababu nimesikia alikuwa rafiki wa karibu sana wa Mtume Muhammad (S.A.W). Na mimi nitafanya bidii mpaka niwe karibu na kiongozi wa harakati hizi za jihadi. Hivyo mimi ni ndugu yenu katika imani, wazazi wangu wamenitenga baada ya kusikia nimeingia kwenye imani hii mpya, ahsanteni sana" akamaliza na kukaa chini, akiongea maneno aliyokaririshwa vilivyo na Kachero Yasmine.
Wakawa wanamfuata na kumkumbatia kwa kumpa pongezi juu ya tukio lake hilo adhimu. Kisha yule mgeni mhashamu akaendelea na hotuba yake."Lakini pia kuna jambo tusha, baya la usaliti limetokea hapa kambini" akapumzika kidogo. Kila mmoja akawa ameshikwa na wasiwasi wanatazamana wenyewe kwa wenyewe. Walijua tayari pepo mchafu anataka kupita wajiandae. Kila mmoja kiroho kikawa kinamdunda kama saa mbovu, maana walijua adhabu ya msaliti ni kifo.
"Mke wa ikhwa mwenzetu mmoja katoroka na amana yetu ya Dola za Kimarekani $10,000 alizopewa afikishe sehemu yapata miezi miwili iliyopita. Kawauza wenzake, wakauliwa kinyama huko bonde la Mzakwe, Dodoma yeye katokomea na pesa zetu. Sasa tumechunguza tumegundua mumewe nae ni mhusika wa njama hiyo. Mleteni hapa haraka sana laanatu-llah ziwe juu yake maluuni mkubwa huyu" alizungumza kwa jazba na raghba kubwa ya kumuadabisha msaliti. Baada ya kutoka hiyo amri ikawa ni mikikimikiki ya kumuingiza ndani ya msikiti kupitia mlango wa katikati ya msikiti aliyehisiwa kuwa ni msaliti huku akiwa amefungwa kamba za miguuni na mikononi, kamba zilizokazwa ndindindi zilizomfanya asiweze kufurukuta.
Kachero Manu alikuwa anashuhudia mubashara tukio hilo, ambalo chanzo chake anakijua nje ndani, mwanzo mwisho. Yeye na Kachero Yasmine ndio waliokoa maisha ya 'Ukhti Rayhaan' ambaye anatuhumiwa kutoroka na Dola $10,000 za magaidi. Walimkuta amezimia na kujeruhiwa vibaya kwenye ajali siku magaidi walipojileta kwenye bonde la Mzakwe, na kuchakazwa vibaya na Kachero Yasmine. Baada ya ambushi hiyo, wenzake waliuawa kinyama na yeye kuponea chupuchupu huku akikutwa na kitita cha Dola za Kimarekani $10,000 kwenye nguo zake za ndani na barua zikiwa njiani kuelekea kwa mama yake "Maso Maso", Bi Mwantumu.
Alipozinduka hospitalini baada ya kukataa katakata kutoa ushirikiano mwishowe alikubali kuuza siri za magaidi waliomtuma, hii ilikuwa ni baada ya kuhakikishiwa usalama wake. Alijieleza yeye akiwa binti anayesomea fani ya Udaktari ngazi ya Chuo Kikuu alishawishiwa kuacha chuo na kwenda kujiunga kwenye kikundi cha ugaidi cha "Al-shabaab" nchini Somalia. Waliporejea Tanzania moja kwa moja wakatua Wilayani Kilindi yeye na mumewe aliyekutana nao huko huko Somalia. Kutokana na kujitolea kwao katika jihadi yeye akachaguliwa kuwa ni mmoja wa wana baraza la shura, wasiri wa ndani wa "Maso Square The Duduman" .
Mpaka akaaminika kufanywa tarishi wake wa kupeleka barua huku na kule. Hivyo mara ya mwisho alitumwa kupeleka pesa na barua kwa mama mzazi wa "Maso Maso", Bi Mwantumu lakini pia alitakiwa kupitia Dodoma kwa Bwana Kareem Abdallah achukue barua ya siri ya kuileta kwa "Maso Maso" yenye kuelezea namna serikali walivyochukua hatua baada ya shambulizi dhidi ya wabunge wake. Ndipo akakutana na sokomoko la kukuta mwenyeji wake Bwana Kareem Abdallah meneja wa Chops Carwash & Garage ametekwa.
Hivyo kwanza akasaidia kumtorosha baba yake mzazi Bwana Kareem Abdallah kumpeleka mafichoni Tanga, kisha akatia nia ya kushiriki ukombozi wa Bwana Kareem ili apewe hiyo barua kisha ndio aelekee Dar es Salaam kwa Bi. Mwantumu. Ndipo yakamkuta yaliyomkuta mpaka akanaswa mikononi mwa Makachero mahiri wanaopambana na magaidi.
'Ukhti Rayhaan' ndio aliyetoa maelekezo kuwa mzigo wa pesa na barua alikuwa anaupeleka kwa 'Shekhe Jamsheed' wa Sinza ambaye yeye ndio angeufikisha siku ya dua Alhamisi ya mwishoni mwa mwezi. Ndio ukachezwa mchezo wa pata potea wa Kachero Manu akajifanye amesilimu katika msikiti unaoongozwa na Shekhe Jamsheed.
Kisha baada ya hapo ajenge nae Shekhe Jamsheed mazoea mpaka amuingize kwenye harakati za "Al-shabaab" huko Kilindi, Tanga. Pata potea ikajibu vizuri, Shekhe Jamsheed ndani ya mwezi mmoja tu akamshiba Kachero Manu na kumfanya mwandani wake mpaka kuanza kumtapikia sumu za "Al-shabaab" kuwa ni kundi lililo katika haki, ila vyombo vya habari vya nchi za kimagharibi ndio vinawachafua kwa kusambaza propaganda chafu dhidi yao. Kachero Manu akaanza kuigiza anapendezwa sana na zile shemere za hadithi za Al-shabaab. Ndipo Shekhe Jamsheed akampa mchongo wa Kilindi Kachero Manu bila kujua anampeleka adui mwenye nia ya kuisambaratisha "Al-shabaab" itoweke Afrika Mashariki, watu waanze kuishi kwa amani na usalama kama zamani.
Mikono yake Kachero Manu ilikuwa inamsisimuka akawa anatamani anyanyuke aende akalianzishe tifu, awadunde kumuokoa mumewe 'Ukhty Rayhaan' lakini nafsi yake ikamuambia vuta subira, daima mwisho mwema ulio mzuri huwafikia wenye subira.
Kwa mkululu huu wa watu zaidi ya 200 ndani ya msikiti tena wakiwa na silaha za kivita hata uwe Komandoo wa dunia ukianzisha ugomvi utegemee tu kunyakuliwa kama mwewe anavyomnyakua kifaranga cha kuku.
Yule anayetuhumiwa kuwa msaliti akatupwa miguuni mwa 'Mullah', akawa anamuangalia 'Mullah' kwa macho ya huruma huku machozi ya huzuni yanamtiririka akitaraji shufaa yake huku jasho jekejeke limetotesha kanzu yake.
Ilikuwa ni siku yake ya mashaka fundo katika siku yake ya mwisho maishani. 'Mullah' akawa anamsinzilia kwa macho yake makali yule msaliti. 'Mullah' alikuwa akipitisha maamuzi ndio yamepita hivyo, alikuwa na tabia ya kisonoko mtamba na ukoko, haambiliki kamwe. Akaletewa jambia kubwa lile la kuchinjia ngamia aliyefutwa kodi huko Arabuni.
Akaanza kulizungushazungusha hewani kwa madaha na mbwembwe, halafu anatishia kama ndio anaanza kuchinjia, umati wote macho yanawatoka juu juu kwa hofu. Alivyolizungusha mara ya tatu na kulitua chini jambia halikurudi bure likatua kwa kasi shingoni na kutenganisha kichwa na kiwiliwili vipande viwili kwa kuikata mishipa ya damu na neva ya shingoni. Damu zilikuwa zinachuruzika kwa kasi mithili ya bomba chakavu la "DAWASA" lililopasuka mtaani.
Wakajitokeza watu wamevaa makoti meupe kama madaktari wakiwa na machela yao wakaibeba maiti na kuondoka nayo kwenda kuizika kusikojulikana. Biashara siku hiyo ikawa imeishia hapo mmoja, kila akatawanyikia upande wake kichwa chini, huku wengine wanashtakia njia kama kuku mwenye mdondo huku Kachero Manu akipewa rafiki atakayekuwa anaishi nae chumba kimoja hapo kambini.
received_580110482929074.jpg
 
HARAMBEE YA "MSAKO WA MWEHU"
Wakazi wa Dar es Salaam wenye moyo wa kushiriki kumsaka "MWEHU" mpaka apatikane, wakapate nakala zao kwa bei elekezi ya Tshs.10,000/= tu, sehemu zifuatazo;
(1)UNUNIO, MBWENI, BOKO, BUNJU, TEGETA, MADALE, GOBA, SALASALA, N.K
Waende COME & READ BOOKSTORE lililopo UNUNIO-0717978899
(2)KARIAKOO Nenda kituo cha Mwendokasi-Msimbazi "B"- 0653799999
(3) UBUNGO STENDI- 0784033820
(4) POSTA MPYA- 0713453152

Wale wa Mikoani piga namba 0625920847 uweze kuelekezwa wapi utapata kopi yako.
AHSANTENI SANA WAPENDWA WANGU.
 
SEHEMU-27



Ilimchukua takribani miezi miwili tu, kila mmoja kambini kumfahamu Kachero Manu kwa jina la 'Komandoo Aboubakr' ni mtu wa shoka. Hii ilitokana na bidii na kujituma kwake kwenye mazoezi. Alikuwa pia anawapa mbinu na maneva mpya mpya za kivita ambazo ni ngeni kwa ufahamu wao.
Aliwafundisha kuanzia mbinu mpya za upigaji wa risasi, namna ya utegaji wa mabomu, na mbinu za utekaji. Sifa zake zilipaa mpaka zikafika mapango ya Amboni anakoishi "Maso Square The Duduman" na wateule wake. Sifa pia zikamrudia Shekhe Jamsheed kwa kuwaletea namba moja ya hatari sana kama 'Komandoo Aboubakr'. Na hayo yote ndio aliyokuwa anayatarajia Kachero Manu.
Wakati mwingine alipopata nafasi ya kuchokonoa mwenendo wa mambo pale kambini alifanya hivyo kwa utaalamu mkubwa. Ili yule mwenye ufahamu mkubwa azinduke mwenyewe kuwa kundi hili alilojiunga haliko katika njia ya sawa. "Swaahibu wangu 'Abuu-Fadhli' hivi haya matukio tunafanyaga tunaenda kutega mabomu sokoni au kwenye umati wa watu tunawaua watu wasio na hatia na sisi wenyewe tunajiua ni sahihi kweli?, mie naona ilibidi tukamlipue adui na sio hawa madhaifu akina mama, vikongwe na watoto ambao hawana hatia na hata kutushambulia kwa jiwe hawawezi, vipi mtazamo wako maana mie ni mgeni katika dini ya uislamu nisije kuonekana nakufuru imani yetu tukufu ya uislamu" alijitia kuuliza Kachero Manu kwa heshima na taadhima kubwa kumuuliza sanjari wake baada kutoka kupewa mpango kazi wa miezi sita ijayo usiku katika kikao cha wanamgambo wote.
Ambapo ilipangwa yakalipuliwe mabomu kwenye mechi za mpira wa miguu na mengine masokoni ili kuwashtua watawala kuwa "Al-shabaab" bado ina nguvu Afrika Mashariki. Wakiwa katika kitanda chao cha dabodeka Kachero Manu akiwa amening'iniza miguu yake chini huku mwenzake amejilaza kitanda cha chini, yule sanjari wake hakujibu swali aliloulizwa bali alinyanyuka na kuelekea mpaka mlangoni. Kachero Manu akaingiwa na wasiwasi huenda swali limemkera mwenzake na kumfanya amuone yeye sio mfia dini kama wao. Akawa amesisimkwa na malaika mwilini, akakaa vizuri mkao wa kazi hisia zilimtuma huenda mwenzake ameenda kubeba silaha amshindilie risasi za kutosha hivyo asibweteke kibwegebwege. Alipofika mlangoni akafunga mlango kwa funguo, kisha akazima taa ya chumbani na kurudi kitandani pake, kisha akatulia kama kuna kitu anatafakari.
Kisha akaanza kumjibu, "Komandoo Aboubakr leo umeleta hoja yenye mashiko ambayo sikutegemea mtu mgeni kwenye dini kama wewe uweze kuileta. Wengi wetu tunafuata mambo kama nyumbu tu, Shekhe au Kiongozi wa dini akisema sisi tunafuata tu kibubusa bila kuhoji hicho alichozungumza Shekhe ni maneno ya Mwenyezi Mungu toka kwenye Q'urani au maneno yake yanayotokana na hawaa ya nafsi yake! " alizungumza Abuu-fadhli kwa hisia za ndani, kisha akaendelea. "Hilo jambo ulilolichokonoa hata mimi nilikuwa ninalitafakari sipati majibu sahihi na ya kina. Kwa mfano kuua mtu asiye na makosa ya kuua mtu tumekatazwa kwenye Q'urani".
Wakaendelea na mazungumzo yao yaliyowaweka macho kodo mpaka manane ya usiku, yakipaza usingizi wao. Kutokea hapo wakazidi kuwa marafiki wa chanda na pete, kila alipokuwa 'Komandoo Aboubakr' (Kachero Manu) habanduki Abuu-fadhli, amejibandika nae. Huku Kachero Manu akimfunda rafiki yake mbinu madhubuti za kivita, ambazo ni adimu akiwa na malengo ya kumtumia kama msaada kwake wa kuisambaratisha hii kambi siku za usoni.
Baada ya kupita miezi kadhaa tena yakatoka maagizo toka kambi kuu, mapango ya Amboni, ambapo ndipo anapoishi gaidi mkuu "Maso Square The Duduman", ya kumteua 'Komandoo Aboubakr' kuwa ni Kiongozi Msaidizi wa kambi ya Dibungo. Kila mwanamgambo wa "Al-Shabaab" kambini hapo alipopata taarifa hizo alikubaliana moja kwa moja uteuzi huo bila kuleta ukaidi. Ikaandaliwa hafla ya kumpa mkono wa baia wa kukubaliana na uteuzi wake.
Hapo sasa akawa na uwezo wa kuingia bohari kuu ya silaha na vifaa vya kijeshi bila kikwazo chochote. Fursa ambayo kwake ilikuwa ni kama nafasi ya dhahabu, aliitumia ipasavyo kukamilisha nia yake ya undumilakuwili (Double Agent). Mchana alikuwa anafanya majukumu ya Al-qaeeda kama 'Komandoo Aboubakr' na nyakati za usiku anajigeuza kuwa Kachero Manu anaenda kutega mabomu ya ardhini kuzunguka kambi nzima, mpaka alipokamilisha zoezi lake. Na hakutiliwa mashaka hata chembe na walinzi wa usiku wa kambi kutokana na cheo chake.
Nyota yake ikazidi kung'ara zaidi sasa akapewa barua ya kupandishwa cheo, akatakiwa ahamie kambi kuu ya mapango ya Amboni. Barua ilimtaka akaripoti kambini haraka iwezekanavyo. Gaidi mkuu "Maso Square The Duduman" alikuwa anaondoka kwa muda na baadhi ya Makomandoo wazoefu hivyo kambi kuu ilitakiwa iongezewe nguvu na watu makini kama Kachero Manu ambaye wenyewe wakimfahamu kama 'Komandoo Aboubakr'.
Siku ya siku, majira ya saa tatu usiku wakiwa wamejifungia chumbani kwao, Kachero Manu akampa taarifa rafiki yake. "Swaahibu wangu mie ndio naelekea Amboni, safari yangu imeiva hivyo huku tena nakata mguu, kesho asubuhi na mapema jua litakapoanza kupasua matlai natakiwa niwe Amboni. nasikitika kutengana na wewe lakini nitafanya juu chini tuungane tena hata kwa kuwashawishi viongozi wetu" yalikuwa ni maneno ya Kachero Manu kwa rafiki yake kipenzi Abuu-fadhli. " Nikutakie kazi njema, ila ninachokuonya ni kuwa makini sana yale mapango ni balaa unaweza kujikuta unatoweka usipofuata masharti yake" alipewa nasaha za tahadhari na rafiki yake, maana alimjua Kachero Manu mtundu mtundu muda mfupi tu aliokaa nae ameona shughuli yake.
"Unaonyesha kama unayafahamu vizuri sana hayo mapango swaahibu wangu eeh?" aliuliza Kachero Manu swali la kudodosa. "Nayajua vizuri sana na kila kichochoro na kijia chake, marehemu Baba yangu alikuwa ni mmoja wa wahifadhi wa yale mapango akiwa muajiriwa wa serikali hivyo tumecheza sana mapangoni" alijibu kwa kujiamini. Ndipo zikaanza stori za mapango hayo, yenye hadithi za kusisimua zilizomuacha Kachero Manu mdomo wazi lakini zikimpa mwangaza wa makazi mapya anayoenda kuishi.

SURA YA KUMI NA TATU
Mipango ya ndoa ya Maso Maso na Kachero Yasmine inapangwa
Ni saa 2:30 usiku kwa majira ya saa za Afrika Mashariki na Kati, Kachero Yasmine alikuwa ameegesha gari yake ya kisasa yenye rangi nyeusi aina ya "2017 Nissan Murrano" pembezoni mwa barabara ya 'Survey' inayoelekea Chuo Kikuu cha Ardhi "Ardhi University". Ndani ya gari kiti cha nyuma alikuwepo mwanaume aliyevalia kanzu nyeupe na kofia, akiwa amepindua kiti na kujilaza.
Walikuwa wameshakaa kuwasubiria wageni wao wanaotarajia kuonana nao kwa zaidi ya nusu saa. Tayari alishaanza kuvuta hisia za watu wanaopita njia hiyo kutaka kufahamu kilichomuweka hapo. "Dada habari yako samahani umepatwa na shida yoyote unahitaji msaada? nimekuona umesimama hapa muda mrefu..!" ilikuwa ni kauli ya mlinzi wa kampuni binafsi anayelinda eneo la Chuo Kikuu. "Hapana kuna mtu namsubirishia amenipa ahadi tukutane hapa" akajibu Kachero Yasmine huku tayari gari alilokuwa analisubiria lilikuwa limeshapiga taa za ishara na kwenda kwa mbele yake kisha linasimama.
Kisha lile gari la mbele aina ya "Land cruiser GX-R" rangi nyeupe likawa linaongoza njia huku Kachero Yasmine analifuata kwa nyuma. Wakauzunguka uwanja wa mpira wa miguu na kushika njia ya darajani inayoelekea kota za wanajeshi wa kambi ya Lugalo kisha wakashika njia ya kuelekea Makongo juu. Wakatembea kama mwendo wa kilometa moja gari ya mbele ikawasha indiketa kuingia barabara ndogo ya upande wa kushoto wa barabara. Wakaenda kama meta 600 wakakutana na nyumba moja ya roshani iliyojengwa kifahari imezungushiwa ukuta nyumba yote.
Gari likapiga honi, punde si punde mlinzi wa nyumba akawa analisukuma geti ili magari yaingie. Moja kwa moja magari yakaegeshwa kwenye eneo la maegesho ambapo kulikuwa na magari mengine ya kifahari zaidi ya matatu yameegeshwa. Haraka haraka wakashuka watu watatu waliokuwa kwenye gari la mbele na kuwalaki akina Kachero Manu. Walikuwa wanaume wawili na mwanamke mmoja. "Salaamu aleikum karibuni sana wageni wetu jisikieni mpo nyumbani" yalikuwa ni makaribisho toka kwa mume wa yule dada aliyekuwa anaendesha gari. "Waleikum salaam tumeshakaribia shukrani sana" akajibu mwanaume aliyefuatana na Kachero Yasmine.
Wakaongoza msafara kuelekea ndani ya nyumba hiyo ya roshani tatu. Wakati wote wanatembea kuingia ndani Kachero Yasmine alikuwa anaithaminisha nyumba hiyo gharama yake. "Kuisimika nyumba kama hii si chini ya bilioni 1.5, hawa watu wanaishi kwenye ukwasi wa hatari" alikuwa anajisemea moyoni mwake. Mpaka wakafika kwenye sebule maalumu iliyotengwa kwa ajili ya mazungumzo yao. Kulikuwa na masofa ya chini kwa chini huku yakizungukwa na zulia zito lenye marembo marembo yaliyonakshiwa vizuri. Pia kulikuwa na mito midogo midogo iliyozagaa. Mmoja wa watumishi wa kike wa kwenye ile nyumba akiwa amevaa vazi la stara lililofunika mwili wote akaleta mchapalo wa visheti vikavu vya sukari, tende nyeusi na chupa ya kahawa na vikombe vyake.
Akawakaribisha na kuondoka zake. Kachero Yasmine na yule mwanamke mwingine wakanyanyua kahawa yao na kubeba mchapalo wao kwenye visosi viwili vidogo wakaomba ruhusa na kujitenga kando, huku wakiwaacha wale wanaume watatu sasa wanazungumza wenyewe soga zao. "Ukhty Yasmine mie naitwa Ukhty Ranilah ndio muongozaji wa NUSRA COMMETTE akaunti ya Facebook" wakapeana mikono kwa nyuso za bashasha.
 
SEHEMU YA-28


Kisha akaendelea na maongezi yake Ukhty Ranilah, huku Kachero Yasmine anamsikiliza na kusukumizia visheti kwa kahawa. "Ile akaunti nimeifungua feesabil-llah hakuna anayenilipa, nataraji thawabu kwa Allah kesho yaumu kiyama" akaweka kituo na kuchota tende kwenye kisosi akamung'unya na kutema kokwa za tende kiganjani kisha akateremshia tarumbeta la kahawa kavu kama mafundo matatu, akaendelea na mazungumzo yake.
"Huwa napokea maombi kutoka pande zote wanaume kwa wanawake, wanaotafuta wachumba. Kisha tunafanya uhakiki wa taarifa za muombaji nikijiridhisha ndio nawaunganisha hao wachumba. Sasa wewe nilipata taarifa zako toka kwa mfanyabiashara mmoja mkubwa sana nchini Sudani, na hapa Tanzania ana vitega uchumi vyake kadhaa mkoani Tanga, anaitwa 'Akhu Nufeil'. Alinipa taarifa zako kuwa kakupa anuani ya barua pepe yangu. Ni mtu Mchamungu sana, ndio maana hakutaka aongee na wewe moja kwa moja kwa sababu anajua angepata madhambi mbele ya Allah kuongea na mwanamke ambaye sio maharimu wake wakiwa faragha. Hivyo akanipa kazi pindi ukishanitumia meseji nikufanyie usaili nikijiridhisha kuwa unamfaa ndio tupange mipango ya ndoa. Je wewe huyo mchumba ni kweli mlionana ana kwa ana?" baada ya kuzungumza kwa dakika kadhaa Kachero Yasmine akatupiwa swali na mwenyeji wake Ukhty Ranilah. Kachero Yasmine akajifanya kuinama chini kama kisichana kidogo tena bikira kisichoelewa mambo ya kikubwa huku anajifanya kutafuna kucha. Baada ya kitambo kifupi akatoa jibu.
"Ni kweli tulionana Simba Hoteli, Jijini Dodoma, lakini hakunieleza lolote kutoka moyoni mwake ila lugha ya vitendo ilinijulisha kuna kitu kitaendelea baina yetu" alijibu kwa unyenyekevu huku anajifanya hawezi kumuangalia machoni mshenga wa "Maso Maso" .
"Sasa ile mahari yako uliyoitaja ya Dola za Kimarekani $5,000 nimeshamwambia na amekubaliana nayo ni wewe tu utuelekeze kwa wazazi wako tulete tuje kuoa haraka iwezekanavyo" alisema Ukhty Ranilah huku anamkazia macho Kachero Yasmine. "Bahati nzuri nimekuja na kaka yangu wa damu makusudi ili aweze kupokea posa na mahari, baba yangu kampa idhini na mamlaka ya kumaliza kila kitu, kama unavyojua dini yetu haipendi uchumba sugu" akajibu Kachero Yasminie kwa sauti ya upole yenye kuonyesha yupo tayari kwa ndoa.
Baada ya kupata muafaka wa pamoja kati ya Ukhty Ranilah na Kachero Yasmine, wakarejesha mrejesho wa waliyoafikiana kwenye baraza la wale wanaume watatu kwa majadiliano zaidi. Mpaka kufikia saa 4:00 usiku wakawa wamefikia muafaka wa ndoa kufanyika baada ya wiki moja siku ya Ijumaa baada ya swala. Ndoa ilipangwa kufungwa katika msikiti wa Sinza-Palestina, "Masjid Noor". Hapo ndio ilisemekana ndio jirani na nyumba ya kaka yake Kachero Yasmine.
Kiuhalisia yule hakuwa kaka wa damu wa Kachero Yasmine, bali alikuwa ni Afisa Usalama ambaye alipangwa katika mbinu za kumtia mbaroni gaidi "Maso Maso". Walichagua eneo la Sinza, kwa kuwa ni jirani na nyumbani kwao "Maso Maso" wakahisi huenda akashawishika kulala nyumbani kwao wamtie mbaroni kirahisi. Ikishindikana kumkamata siku moja kabla ya ndoa, watamkamata ndani ya msikiti wakati anafungishwa ndoa na Shekhe.

"Masjid Noor" ni moja ya misikiti mikubwa sana iliyopo Sinza. Upo pembezoni mwa barabara ya Shekilango, barabara ambayo inaunganisha barabara ya Mwai Kibaki na barabara ya Morogoro. Upande wa kusini msikiti huo umepakana na ukuta wa Hospitali ya serikali ya Sinza Palestina.
Siku hiyo ilikuwa ni Ijumaa, siku maalumu kwa ibada ya pamoja kwa waislamu wa sehemu mbalimbali. Waumini walikuwa wamefurika kuanzia ndani mpaka nje ya msikiti. Magari pia yalikuwa yameshonana pande zote mbili za magharibi na mashariki ya msikiti. Waumini wengi wao wakiwa wamevaa mufti, vazi la kanzu nyeupe na barakashia na tasbihi zao mikononi walikuwa wametulizana kwenye mazulia ya rangi ya kijani yaliyotandikwa msikiti mzima wanamsabihi Mola wao.
Wanausalama nao walikuwa wametanda ndani na nje ya msikiti kuhakikisha wanamtia mbaroni "Maso Maso". Walikuwa katika hekaheka za kutaka kumlengesha wamtie nyavuni. Walimvizia nyumbani kwa mama yake maeneo ya Sinza-A walidhania huenda katika harakati za harusi atateleza kidogo kwenda nyumbani kwao kuweka mambo sawa, lakini haikuwa hivyo abadan. Karata yao ya mwisho ilikuwa ni kumkamatia ndani ya msikiti.
"Maso Maso" alikuwa tayari yupo ndani ya msikiti na rafiki zake watatu. Wakiwa wamevalia mavazi sare ya kanzu nyeupe na kilemba kichwani kilichozungushiwa hegali nyeusi. Kiunoni wakiwa wamejining'iniza majambia ya urembo ya kutoka Omani. kwa "Maso Maso" halikuwa jambia la kawaida kama zinazojulikana, bali ilikuwa ni silaha maalumu. Silaha ambayo kama ukimuendea kibwege atakuchakaza nayo. Kipindi cha hotuba ya swala ya Ijumaa wakati inaendelea, gaidi "Maso Maso" alikuwa alikuwa hana utulivu. Alishahisi ameingia choo cha kike kukubali kuja Jijini Dar es Salaam kuja kufunga ndoa yeye mwenyewe. Mwanzoni alipopewa taarifa sio salama kwake kuja mwenyewe alipinga sana wazo hilo. Alitamani usiku wa kwanza wa ndoa aufaidi na mkewe huyo aliyetokea kumpenda kuliko maelezo. Licha ya kutambua anasakwa kwa udi na uvumba kwa utundu wake alifanikiwa kutoka mafichoni na mpaka kuingia msikitini bila kushitukiwa. Alipokuwa msikitini kuna sura alikuwa kila akizutupia macho haziamini kabisa. Akili yake ikafanya kazi haraka sana zaidi ya kompyuta, akamnong'oneza kitu rafiki yake, wakaelewana.
Msomaji hotuba ya swala ya Ijumaa msikitini alipomaliza hotuba zake mbili, aliashiria muda wa kusimama kwa ajili ya swala kuu ya Ijumaa umetimia. Waumini walipokuwa katika harakati za kusimama ili imamu wa msikiti aanzishe swala, "Maso Maso" akavua kilemba chake na hegali yake akamkabidhi mwenzake na kuanza kuzipasua safu za watu waliojipanga anarudi nyuma kuelekea mlango wa chooni. Hakuna aliyemjali walijua ni muumini ambaye ametengukwa na udhu hivyo anaenda kutia udhu bombani. Hata baadhi ya wana usalama aliwapita bila kumtambua hasa kwa kuwa sasa alikuwa kichwa wazi na wao walimuona akiingia amejifunika kichwa chake. Alikuwa amejibadilisha muonekano wake alinyoa kabisa ndevu zake, kidevu kilikuwa kinang'aa kama balbu. Alipofika maeneo ya mabomba ya kutilia udhu akapitiliza chooni moja kwa moja, akakuta vimefungwa kuashiria kuna watu wanakidhi haja zao, huku wengine wamesimama kusubiria toka ingia ya chooni.
Akaunga foleni ya kutaka kusubiri, lakini Imamu alivyoanza kisomo chake cha swala machale yakamcheza. Akaanza kuondoka maeneo yale ya chooni na kuelekea chumba kingine kilichojitenga. Hamna aliyemjali kumfuatilia kila mmoja alibanwa na haja akili zao zilikuwa ni kupata nafasi ya kuingia chooni wakatoe chenye kuupa udhia mwili. Mpaka alipofika kwenye chumba hicho akasimama na kusoma maandishi makubwa yaliyobandikwa mlangoni hapo ya lugha ya kiarabu yalisomeka "GHURFAT LIGHASIL ALJUTHATH". Alivyoyasoma akatabasamu akajaribu kunyonga kitasa kikakubali, hakikuwa kimefungwa na ufunguo. Akaingia mpaka ndani, kilikuwa ni chumba maalumu cha kuoshea maiti.
Chumba ambacho siku zote kilikuwa hakikosi maiti za kuoshwa kuanza za watoto wachanga wanaozaliwa wamefariki hadi za watu wazima kutokana na ujirani na hospitali ya Sinza Palestina. Kwa haraka haraka alikuta kuna maiti tatu zikiwa tayari zimeshavikwa sanda na kupambwa zinasubiria kuingizwa kwenye jeneza, ziswaliwe zikazikwe. Pembezoni kulikuwa na mabaki ya kitambaa kikubwa cha sanda na pamba zake zinazotumika kuziba kwenye matundu yote ya mwili wa maiti kuanzia sehemu ya haja kubwa, masikioni mpaka puani. Akaanza kujiweka pamba za puani akiwa na lengo ajiviringishie sanda nae wamuhesabie kuwa ni marehemu iwapo wataingia chumba hicho. Alipoanza kujiweka pamba za masikioni, akasita kidogo. Akaamua aghairishe zoezi hilo la kujifanya maiti.
"Mhudumu wa hiki chumba akija akakuta maiti zipo nne badala ya tatu atapagawa na kupiga kelele za uwoga ndio nitakaposhikwa" aliwaza kimoyomoyo "Maso Maso". Akaangazaangaza mule chumbani akaona kidirisha kidogo, ambacho kinaweza kumpitisha mtu. Akafanya bidii kukikwea mpaka akafanikiwa kupapachua kidirisha kidogo cha Aluminiamu na kufanikiwa kutoka nje ya msikiti. Akaruka mfereji mwembamba unaotenganisha ukuta wa msikiti na ukuta wa hospitali. Akapanda ukuta wa hospitali na kurukia ukuta wa ndani ya hospitali ya Sinza Palestina.
Ni kitendo alichokifanya ndani ya dakika chache sana tena kwa umahiri wa hali ya juu. Alipojitupa chini akajikuta yupo ndani ya uzio wa hospitali. Akakuta mbele yake kuna tanuri, kizimba cha kuchomea taka za hospitali kinafanya kazi na hamna mtu yoyote. Akaenda mbele kwa kulipita tanuri hilo, mpaka akajitokeza kwenye korido la hospitali. Akakutana na mmoja wa wahudumu, akamsalimia na kunong'ona nae baadhi ya mambo. Akaelekezwa anachotaka, akaagana nae na kuelekea kwa huyo mtu aliyekuwa anamhitaji akiwa katika mwendo wa haraka. Yule mtumishi alikuwa anamsindikiza kwa macho hasa baada ya kumuona hata viatu hajavaa anatembea peku peku
 
SEHEMU-29




Muadhini akatoa wito wa ikama, akazungumza maneno ya kiarabu yanayowataka Waumini wasimame kwa ajili ya kuanza kuswali. Waumini waliposikia hayo maneno wakasimama na wakajipanga safusafu. Imamu akafanya juhudi za kuhimiza waumini wanyooshe vizuri safu zao.
Alivyomaliza msisitizo wake akaelekea kibla na kuifungua swala yake kwa takbira. Swala haikuwa ndefu sana, imamu alisoma sura za Kurani fupi fupi ili asiwachoshe waumini waliowasili msikitini tokea saa 6:00 mchana. Ambao wengi wao walikuwa bado hawajapata mlo wa mchana na pia wanarejea kwenye shughuli zao za kujitafutia tonge la siku.
Baada ya swala kwisha tu, Imamu akasimama akiwa na uso wa bashasha na kutoa tangazo, "Salamu Aleikum Warahmatullah Wabarakatuhu, awali ya yote tunamshukuru Allah kwa kutuwezesha kutekeleza ibada hii ya swala ya Ijumaa. Tunaomba swala yetu hii mbele ya Mola iwe ni yenye kukubaliwa". Msikiti mzima ukaitikia "Ameen".
Kisha Imamu akaendelea "leo hatuna mawaidha hotuba yetu imejitosheleza kikubwa ni kuifanyia kazi, ila tuna matangazo matatu tu, tangazo la kwanza ni kuhusu michango yetu ya upanuzi wa msikiti bado inaendelea likipita kapu mbele yako usisite kutia chochote kitu, Allah atakulipa. Tangazo la pili hapa msikitini sasa hivi tutapitisha Nikaha, muumini mwenzetu anaozesha dada yake hivyo wale wenye wasaa wa wasubirie kushuhudia ndoa hiyo. Nawaomba wale waoaji toka Tanga wasogee mbele tayari kwa kuanza kwa shughuli hiyo. Na tangazo la tatu baada ya ndoa kutakuwa na swala ya maiti, tubakie kuswalia kuna mlundi wa thawabu unapatikana mithili ya mlima Uhudi uliopo nchini 'Saudi-Arabia' kwenye kuswalia maiti, wabillahi tawfiq" Imamu akawa amemaliza matangazo yake.
Waumini wenye haraka zao wakawa kwenye hekaheka za kutoka milangoni wanapigana vikumbo na wale wenye kuhitaji fadhila za kushuhudia ndoa wakawa wanajivuta mbele ili kusubiria shughuli ianze. Kaka feki wa Yasmine ambaye wakati wote wa swala alikuwa na furaha akijua wanakuja kumtia mbaroni "Maso Maso" uso wake ghafla ulipigwa na taghayari ukapoteza uchangamfu wake. Alikumbwa na bumbuwazi baada ya kuona hamuoni mlengwa wake "Maso Maso'". Shekhe akaitisha ubani na chetezo cha moto na kuanza hotuba ya ndoa mpaka akamaliza. Akamuita muoaji na muozeshaji wamsogelee karibu ili ahitimishe shughuli.
Uzalendo ukamshinda kaka feki wa Yasmine ikabidi aulize, "yupo wapi Bwana harusi, kutuma mwakilishi hayakuwa makubaliano. Nimemuona kabisa yupo ndani ya msikiti na tumeswali nae nashangaa ameyeyuka. Hii ni dharau kubwa anatuonyesha shemeji yetu mtarajiwa". Rafiki wa "Maso Maso" huku anachekea tumboni ikabidi ajitutumue kumjibu "kapatwa na udhuru tumbo la ghafla la kuharisha ameshindwa kuhudhuria, kanituma nimuwakilishe".
Shekhe ikabidi aingilie kati kuleta suluhu baina yao kutetea mpunga wake anaolipwa kwa kufungisha ndoa. "Inajuzu ndoa kufungwa kwa kutumia muwakilishi haina shaka kabisa". Kishingo upande ikawa hana budi bali kukubaliana na hali halisi.
Ndoa ikapitishwa, muwakilishi wa Bwana harusi na mwenzake wakapelekwa upande wanaoswalia wanawake wakambeba mke wao Yasmine na kutokomea nae kutoka viwanja vya pale msikitini. Ukiona manyoya, jua ameliwa tayari. "Maso Maso" alishawatimulia vumbi tayari wana usalama kama kawaida yake, gaidi maluhuni kabisa.

"Tukamate tu hawa washirika wake, halafu tunawabinya na kuwaswaga kisawasawa kwa vipigo takariri watatuekeza yupo wapi huyo mshenzi" aliropoka kwa hasira mmoja wa wana usalama. "Hiyo njia ni kama vile kuitaka asali kwa kupiga manati kwenye mzinga wa nyuki, unaweza kula asali lakini ujiandae kwa manundu usoni. Vita dhidi ya ugaidi inahitaji akili na maarifa na sio nguvu tupu. Usiwe na wasiwasi Kachero Manu yupo Tanga tayari na hata huyu Bibi harusi waliyembeba leo wamepeleka maafa wasiyoyatarajia" alizungumza mmoja wa Maofisa ambaye alionekana ana busara zaidi kushinda wenzake.
Wakakubaliana wafanye msako wa haraka haraka huenda akawa amejichomeka miongoni mwa makundi ya waumini wanaotoka msikitini. Zaidi ya nusu saa za msako hakukuwa na dalili yoyote ya kumnasa "Maso Maso". Wakafunguliwa na mmoja wa viongozi wa msikiti kila chumba cha ofisi, mpaka chooni walipita kote wakaambulia patupu.
Walipoingizwa kwenye chumba cha kuoshea maiti, wakazikuta maiti kama tatu zimelazwa kwenye meza kubwa. Wakaanza kupekenyua sanda ya kila maiti wakitarajia huenda ameleta ujanja wa kujigeuza marehemu, wakaambulia patupu. Wakati baadhi ya Maofisa wameshatangulia kutoka nje ya chumba, mmoja wao akasita kutoka nje. Akawa anaangaza mule ndani akaona kuna hitilafu kwenye dirisha dogo la juu. Aliliona kama vile limetegeshwa halijajishikiza kisawa sawa. Alivyowaita wenzake wakakagua wakakuta kweli limenyofolewa.
Wakathibitisha ushahidi wa kimazingira ametorokea kupitia dirishani. Haraka haraka wakatoka nje kwenda hospitalini kumsaka huenda amejisweka humo akisubiria mambo yatulie ndio achomoke. Kikosi kikaanza kukimbizana hospitali.

Maarufu mtaani akijulikana kama "Dr.Jembe", lakini jina lake halisi alilopewa na wazazi wake ni Juma Chembea. Aliajiriwa zaidi ya miaka 8 iliyopita na sasa alikuwa na Cheo cha Daktari Msaidizi "Advance Medical Officer". Alihamishiwa hospitali ya Sinza miezi kama 9 iliyopita akitokea hospitali ya Tuangoma, Kigamboni. Muda mfupi tu aliohudumu Sinza umaarufu wake ulisambaa kama moshi, Sinza yote utasema ni mzoefu hapo miaka kadhaa. Mbwembwe na mikogo yake ya kutembea ni katika vitu vilimfanya avume kila kona. Kama ni ugonjwa wa pumu basi ulimpata mgonjwa, udaktari ulifika mahali pake.
Kwanza popote utakapomkuta "Dr.Jembe" lazima awe amevaa koti lake jeupe, hata akija kula kwa mama lishe kitaa. Bila kusahau kifaa cha kidaktari, stethoskopu shingoni mwake lazima ining'inie kama wale wacheza ngoma za kisukuma, wanavyojining'iniza nyoka shingoni. Pia umaarufu wake ulivuma kwa vichenchede vya mashuleni kwa kuchoropoa mimba. Hao vichenchede ndio waliompachika jina la "Dr.Jembe". Wasichana wa shule walikuwa wakinasa mimba, sasa hawana hofu ya kufukuzwa shule wanapeana taarifa za kumsaka Dr.Jembe arekebishe mambo. Lakini toka wiki iliyopita "Dr.Jembe" hakuwa na furaha kabisa, alikuwa kwenye msongo mkubwa wa mawazo. Sio "Dr.Jembe" yule aliyezoeleka wakati wote ni mcheshi na tabasamu fokofoko lisilokauka usoni mwake.
Alikuwa amebakiza wiki mbili tu afunge ndoa yake, lakini michango ya harusi toka kwa ndugu, jamaa na marafiki ilikuwa bado inasuasua. Kwa kupenda sifa kwake alitaka iwe bonge la sherehe ya kufutu ada, na kuacha gumzo. Bajeti ya kamati ya harusi ilipangwa kuwa milioni 50, lakini mpaka Ijumaa hii ya leo makusanyo ya michango kwa mweka hazina ilikuwa inasoma milioni 5 tu. Kila aliyekuwa anaguswa achangie anaruka kimanga na jibu pendwa katika zama hizi, la "vyuma vimebana". Alikuwa ofisini kwake kimwili tu, lakini kimawazo hakuwepo kabisa. Aliziona dalili kabisa za kwenda kufungia ndoa kijijini kwao, huko Mlembule Wilayani Mpwapwa, Dodoma. Ambapo huko bajeti ya milioni 5 ingetosheleza na chenji kubaki na kuacha gumzo la miaka kadhaa kwa uzuri wa sherehe hiyo.
Huko kijijini kwao, pombe ya kienyeji ya laki 5, watu wangelewa mpaka kutambaa kwa magoti. Disko Joka (DJ) wa kule kijijini elfu 30 tu ingetosha kuporomosha segedansi la nguvu usiku kucha na maspika yake yanayokoroma kama kishindo cha radi. Wasiwasi wake mkubwa ulikuwa kwa mkewe mtarajiwa, Bi Chausiku. Alikuwa nae mpenda ufahari na mbwembwe kama mumewe. Chausiku alipania awanyooshe mashosti zake wa Tandale kuwa ameolewa na mlalaheri. Mashoga zake ambao nao walimkoga kwenye ndoa zao. Hivyo kama "Dr.Jembe" angeleta wazo la ndoa yao kwenda kufungwa kijijini Mlembule, Chausiku angeweza kuzusha varangati na tifu lisilo na ukomo baina yao.
Sasa akiwa kwenye dimbwi hilo la mawazo mbagombago, akasikia mlango wake unagongwa kisha ukafunguliwa. "Samahani daktari kuna mgeni wako" ilikuwa ni sauti ya unyenyekevu ya mmoja wa manesi aliyelambishwa mwekundu wa msimbazi na gaidi "Maso Maso" ili amtafutie daktari mjanja mjanja wa haraka. Yule nesi bila kufanya ajizi akampeleka kwa "Dr.Jembe" akiwa na uhakika mia kwa mia hawezi kumuangusha. "Dr.Jembe" alionyesha kutaka kusitasita maana hakuwa na miadi ya kukutana na mtu yoyote siku hiyo.
"Njagu nini wanataka kuniotea wanitulie mchanga kitumbua changu kutokana na kuchoropoa mimba za mabinti wa watu!" alikuwa anawaza nafsini mwake. Akaamua kuvaa ujasiri wa kiume na kumwambia amruhusu apite. "Habari yako Bwana daktari naomba msaada wako nimenasa" aliongea gaidi "Maso Maso" huku anavuta kiti na kuketi. "Dr.Jembe" aliingiwa na hofu huenda ni majinuni kaingia ofisini mwake, maana "Maso Maso" aliingia anapekua bila viatu. Halafu kanzu yake ilichafuka vumbi katika harakati za kuparamia ukuta.
"Eleza shida yako" alijibu kwa ukali kuonyesha hataki utani kazini na watu wehu. "Maso Maso" akakohoa kidogo kuiweka sauti sawa, kisha akajieleza. "Nataka unisaidie kutoroka maeneo haya ya hospitali kwa kutumia gari la wagonjwa mahututi 'ambulance'". "Dr.Jembe" akaona yale yale ya ukichaa asiyoyataka ndio analetewa na huyu mgeni ofisini mwake.
"Toka toka toka shenzi wahidi nanusu wewe huu muda wa kazi unakuja kuleta masihara" alifoka "Dr.Jembe" mpaka povu jeupe la hasira mdomoni mwake likaonekana huku akisimama kuashiria anataka kwenda kufungua mlango amfurushe nje ya ofisi.
Msongo wa mawazo wa ukosefu wa pesa za kufanya harusi alitaka kuhamishia kwa gaidi "Maso Maso". "Maso Square The Duduman" hakuwa na muda wa kupoteza tena, alikuwa anakimbizana na muda. Alitambua wakati ni upanga, uchezee ukukate au uutumie vizuri kukata mambo yako unayotaka kuyatekeleza ndani ya wakati. Wakati "Dr.Jembe" tayari ameshasimama, "Maso Maso" akamuwahi haraka haraka akavuta kiti na kufika mlangoni kabla ya daktari na akafanikiwa kufunga mlango. Akachomoa funguo mlangoni kisha akatoa bastola yake ndogo na kumnyooshea mdomo wake "Dr.Jembe".
"Ukitaka ukubali kutekeleza matakwa yangu kwa hiari yako nikupe chauchau, au ukatae nikudonyoe shaba za kichwani uende kuzimu sasa hivi, memsapu wako abatizwe jina jipya na kuitwa mjane wa marehemu" alitamka "Maso Maso" maneno yaliyoonyesha hatanii anachoongea na ana maanisha kwa vitendo atafanya faya kun fayaa kama atabisha kutekeleza. "Dr.Jembe" alikuwa anacheza tetemo mwili mzima huku jasho jekejeke lile la uoga likimtiririka, taharuki imemkamata. Usifanye mchezo hata kidogo na kifo. Kifo hakimjui kwamba huyu ni mfalme au shamba boi, kila mtu kitamfika, na kila mmoja anakikwepa. Kifo hakina kinga, kusema utafanya hili na lile ili ukiepuke.
"Kama unaogopa kifo namna hiyo usingekuwa unachoropoa mimba za wasichana wetu mashuleni ha ha ha" 'Maso Maso" alizidi kumchokonoa zaidi ili kumfanya atoe maamuzi ya haraka
 
Back
Top Bottom