SEHEMU-29














Muadhini akatoa wito wa ikama, akazungumza maneno ya kiarabu yanayowataka Waumini wasimame kwa ajili ya kuanza kuswali. Waumini waliposikia hayo maneno wakasimama na wakajipanga safusafu. Imamu akafanya juhudi za kuhimiza waumini wanyooshe vizuri safu zao.
Alivyomaliza msisitizo wake akaelekea kibla na kuifungua swala yake kwa takbira. Swala haikuwa ndefu sana, imamu alisoma sura za Kurani fupi fupi ili asiwachoshe waumini waliowasili msikitini tokea saa 6:00 mchana. Ambao wengi wao walikuwa bado hawajapata mlo wa mchana na pia wanarejea kwenye shughuli zao za kujitafutia tonge la siku.
Baada ya swala kwisha tu, Imamu akasimama akiwa na uso wa bashasha na kutoa tangazo, "Salamu Aleikum Warahmatullah Wabarakatuhu, awali ya yote tunamshukuru Allah kwa kutuwezesha kutekeleza ibada hii ya swala ya Ijumaa. Tunaomba swala yetu hii mbele ya Mola iwe ni yenye kukubaliwa". Msikiti mzima ukaitikia "Ameen".
Kisha Imamu akaendelea "leo hatuna mawaidha hotuba yetu imejitosheleza kikubwa ni kuifanyia kazi, ila tuna matangazo matatu tu, tangazo la kwanza ni kuhusu michango yetu ya upanuzi wa msikiti bado inaendelea likipita kapu mbele yako usisite kutia chochote kitu, Allah atakulipa. Tangazo la pili hapa msikitini sasa hivi tutapitisha Nikaha, muumini mwenzetu anaozesha dada yake hivyo wale wenye wasaa wa wasubirie kushuhudia ndoa hiyo. Nawaomba wale waoaji toka Tanga wasogee mbele tayari kwa kuanza kwa shughuli hiyo. Na tangazo la tatu baada ya ndoa kutakuwa na swala ya maiti, tubakie kuswalia kuna mlundi wa thawabu unapatikana mithili ya mlima Uhudi uliopo nchini 'Saudi-Arabia' kwenye kuswalia maiti, wabillahi tawfiq" Imamu akawa amemaliza matangazo yake.
Waumini wenye haraka zao wakawa kwenye hekaheka za kutoka milangoni wanapigana vikumbo na wale wenye kuhitaji fadhila za kushuhudia ndoa wakawa wanajivuta mbele ili kusubiria shughuli ianze. Kaka feki wa Yasmine ambaye wakati wote wa swala alikuwa na furaha akijua wanakuja kumtia mbaroni "Maso Maso" uso wake ghafla ulipigwa na taghayari ukapoteza uchangamfu wake. Alikumbwa na bumbuwazi baada ya kuona hamuoni mlengwa wake "Maso Maso'". Shekhe akaitisha ubani na chetezo cha moto na kuanza hotuba ya ndoa mpaka akamaliza. Akamuita muoaji na muozeshaji wamsogelee karibu ili ahitimishe shughuli.
Uzalendo ukamshinda kaka feki wa Yasmine ikabidi aulize, "yupo wapi Bwana harusi, kutuma mwakilishi hayakuwa makubaliano. Nimemuona kabisa yupo ndani ya msikiti na tumeswali nae nashangaa ameyeyuka. Hii ni dharau kubwa anatuonyesha shemeji yetu mtarajiwa". Rafiki wa "Maso Maso" huku anachekea tumboni ikabidi ajitutumue kumjibu "kapatwa na udhuru tumbo la ghafla la kuharisha ameshindwa kuhudhuria, kanituma nimuwakilishe".
Shekhe ikabidi aingilie kati kuleta suluhu baina yao kutetea mpunga wake anaolipwa kwa kufungisha ndoa. "Inajuzu ndoa kufungwa kwa kutumia muwakilishi haina shaka kabisa". Kishingo upande ikawa hana budi bali kukubaliana na hali halisi.
Ndoa ikapitishwa, muwakilishi wa Bwana harusi na mwenzake wakapelekwa upande wanaoswalia wanawake wakambeba mke wao Yasmine na kutokomea nae kutoka viwanja vya pale msikitini. Ukiona manyoya, jua ameliwa tayari. "Maso Maso" alishawatimulia vumbi tayari wana usalama kama kawaida yake, gaidi maluhuni kabisa.














"Tukamate tu hawa washirika wake, halafu tunawabinya na kuwaswaga kisawasawa kwa vipigo takariri watatuekeza yupo wapi huyo mshenzi" aliropoka kwa hasira mmoja wa wana usalama. "Hiyo njia ni kama vile kuitaka asali kwa kupiga manati kwenye mzinga wa nyuki, unaweza kula asali lakini ujiandae kwa manundu usoni. Vita dhidi ya ugaidi inahitaji akili na maarifa na sio nguvu tupu. Usiwe na wasiwasi Kachero Manu yupo Tanga tayari na hata huyu Bibi harusi waliyembeba leo wamepeleka maafa wasiyoyatarajia" alizungumza mmoja wa Maofisa ambaye alionekana ana busara zaidi kushinda wenzake.
Wakakubaliana wafanye msako wa haraka haraka huenda akawa amejichomeka miongoni mwa makundi ya waumini wanaotoka msikitini. Zaidi ya nusu saa za msako hakukuwa na dalili yoyote ya kumnasa "Maso Maso". Wakafunguliwa na mmoja wa viongozi wa msikiti kila chumba cha ofisi, mpaka chooni walipita kote wakaambulia patupu.
Walipoingizwa kwenye chumba cha kuoshea maiti, wakazikuta maiti kama tatu zimelazwa kwenye meza kubwa. Wakaanza kupekenyua sanda ya kila maiti wakitarajia huenda ameleta ujanja wa kujigeuza marehemu, wakaambulia patupu. Wakati baadhi ya Maofisa wameshatangulia kutoka nje ya chumba, mmoja wao akasita kutoka nje. Akawa anaangaza mule ndani akaona kuna hitilafu kwenye dirisha dogo la juu. Aliliona kama vile limetegeshwa halijajishikiza kisawa sawa. Alivyowaita wenzake wakakagua wakakuta kweli limenyofolewa.
Wakathibitisha ushahidi wa kimazingira ametorokea kupitia dirishani. Haraka haraka wakatoka nje kwenda hospitalini kumsaka huenda amejisweka humo akisubiria mambo yatulie ndio achomoke. Kikosi kikaanza kukimbizana hospitali.














Maarufu mtaani akijulikana kama "Dr.Jembe", lakini jina lake halisi alilopewa na wazazi wake ni Juma Chembea. Aliajiriwa zaidi ya miaka 8 iliyopita na sasa alikuwa na Cheo cha Daktari Msaidizi "Advance Medical Officer". Alihamishiwa hospitali ya Sinza miezi kama 9 iliyopita akitokea hospitali ya Tuangoma, Kigamboni. Muda mfupi tu aliohudumu Sinza umaarufu wake ulisambaa kama moshi, Sinza yote utasema ni mzoefu hapo miaka kadhaa. Mbwembwe na mikogo yake ya kutembea ni katika vitu vilimfanya avume kila kona. Kama ni ugonjwa wa pumu basi ulimpata mgonjwa, udaktari ulifika mahali pake.
Kwanza popote utakapomkuta "Dr.Jembe" lazima awe amevaa koti lake jeupe, hata akija kula kwa mama lishe kitaa. Bila kusahau kifaa cha kidaktari, stethoskopu shingoni mwake lazima ining'inie kama wale wacheza ngoma za kisukuma, wanavyojining'iniza nyoka shingoni. Pia umaarufu wake ulivuma kwa vichenchede vya mashuleni kwa kuchoropoa mimba. Hao vichenchede ndio waliompachika jina la "Dr.Jembe". Wasichana wa shule walikuwa wakinasa mimba, sasa hawana hofu ya kufukuzwa shule wanapeana taarifa za kumsaka Dr.Jembe arekebishe mambo. Lakini toka wiki iliyopita "Dr.Jembe" hakuwa na furaha kabisa, alikuwa kwenye msongo mkubwa wa mawazo. Sio "Dr.Jembe" yule aliyezoeleka wakati wote ni mcheshi na tabasamu fokofoko lisilokauka usoni mwake.
Alikuwa amebakiza wiki mbili tu afunge ndoa yake, lakini michango ya harusi toka kwa ndugu, jamaa na marafiki ilikuwa bado inasuasua. Kwa kupenda sifa kwake alitaka iwe bonge la sherehe ya kufutu ada, na kuacha gumzo. Bajeti ya kamati ya harusi ilipangwa kuwa milioni 50, lakini mpaka Ijumaa hii ya leo makusanyo ya michango kwa mweka hazina ilikuwa inasoma milioni 5 tu. Kila aliyekuwa anaguswa achangie anaruka kimanga na jibu pendwa katika zama hizi, la "vyuma vimebana". Alikuwa ofisini kwake kimwili tu, lakini kimawazo hakuwepo kabisa. Aliziona dalili kabisa za kwenda kufungia ndoa kijijini kwao, huko Mlembule Wilayani Mpwapwa, Dodoma. Ambapo huko bajeti ya milioni 5 ingetosheleza na chenji kubaki na kuacha gumzo la miaka kadhaa kwa uzuri wa sherehe hiyo.
Huko kijijini kwao, pombe ya kienyeji ya laki 5, watu wangelewa mpaka kutambaa kwa magoti. Disko Joka (DJ) wa kule kijijini elfu 30 tu ingetosha kuporomosha segedansi la nguvu usiku kucha na maspika yake yanayokoroma kama kishindo cha radi. Wasiwasi wake mkubwa ulikuwa kwa mkewe mtarajiwa, Bi Chausiku. Alikuwa nae mpenda ufahari na mbwembwe kama mumewe. Chausiku alipania awanyooshe mashosti zake wa Tandale kuwa ameolewa na mlalaheri. Mashoga zake ambao nao walimkoga kwenye ndoa zao. Hivyo kama "Dr.Jembe" angeleta wazo la ndoa yao kwenda kufungwa kijijini Mlembule, Chausiku angeweza kuzusha varangati na tifu lisilo na ukomo baina yao.
Sasa akiwa kwenye dimbwi hilo la mawazo mbagombago, akasikia mlango wake unagongwa kisha ukafunguliwa. "Samahani daktari kuna mgeni wako" ilikuwa ni sauti ya unyenyekevu ya mmoja wa manesi aliyelambishwa mwekundu wa msimbazi na gaidi "Maso Maso" ili amtafutie daktari mjanja mjanja wa haraka. Yule nesi bila kufanya ajizi akampeleka kwa "Dr.Jembe" akiwa na uhakika mia kwa mia hawezi kumuangusha. "Dr.Jembe" alionyesha kutaka kusitasita maana hakuwa na miadi ya kukutana na mtu yoyote siku hiyo.
"Njagu nini wanataka kuniotea wanitulie mchanga kitumbua changu kutokana na kuchoropoa mimba za mabinti wa watu!" alikuwa anawaza nafsini mwake. Akaamua kuvaa ujasiri wa kiume na kumwambia amruhusu apite. "Habari yako Bwana daktari naomba msaada wako nimenasa" aliongea gaidi "Maso Maso" huku anavuta kiti na kuketi. "Dr.Jembe" aliingiwa na hofu huenda ni majinuni kaingia ofisini mwake, maana "Maso Maso" aliingia anapekua bila viatu. Halafu kanzu yake ilichafuka vumbi katika harakati za kuparamia ukuta.
"Eleza shida yako" alijibu kwa ukali kuonyesha hataki utani kazini na watu wehu. "Maso Maso" akakohoa kidogo kuiweka sauti sawa, kisha akajieleza. "Nataka unisaidie kutoroka maeneo haya ya hospitali kwa kutumia gari la wagonjwa mahututi 'ambulance'". "Dr.Jembe" akaona yale yale ya ukichaa asiyoyataka ndio analetewa na huyu mgeni ofisini mwake.
"Toka toka toka shenzi wahidi nanusu wewe huu muda wa kazi unakuja kuleta masihara" alifoka "Dr.Jembe" mpaka povu jeupe la hasira mdomoni mwake likaonekana huku akisimama kuashiria anataka kwenda kufungua mlango amfurushe nje ya ofisi.
Msongo wa mawazo wa ukosefu wa pesa za kufanya harusi alitaka kuhamishia kwa gaidi "Maso Maso". "Maso Square The Duduman" hakuwa na muda wa kupoteza tena, alikuwa anakimbizana na muda. Alitambua wakati ni upanga, uchezee ukukate au uutumie vizuri kukata mambo yako unayotaka kuyatekeleza ndani ya wakati. Wakati "Dr.Jembe" tayari ameshasimama, "Maso Maso" akamuwahi haraka haraka akavuta kiti na kufika mlangoni kabla ya daktari na akafanikiwa kufunga mlango. Akachomoa funguo mlangoni kisha akatoa bastola yake ndogo na kumnyooshea mdomo wake "Dr.Jembe".
"Ukitaka ukubali kutekeleza matakwa yangu kwa hiari yako nikupe chauchau, au ukatae nikudonyoe shaba za kichwani uende kuzimu sasa hivi, memsapu wako abatizwe jina jipya na kuitwa mjane wa marehemu" alitamka "Maso Maso" maneno yaliyoonyesha hatanii anachoongea na ana maanisha kwa vitendo atafanya faya kun fayaa kama atabisha kutekeleza. "Dr.Jembe" alikuwa anacheza tetemo mwili mzima huku jasho jekejeke lile la uoga likimtiririka, taharuki imemkamata. Usifanye mchezo hata kidogo na kifo. Kifo hakimjui kwamba huyu ni mfalme au shamba boi, kila mtu kitamfika, na kila mmoja anakikwepa. Kifo hakina kinga, kusema utafanya hili na lile ili ukiepuke.
"Kama unaogopa kifo namna hiyo usingekuwa unachoropoa mimba za wasichana wetu mashuleni ha ha ha" 'Maso Maso" alizidi kumchokonoa zaidi ili kumfanya atoe maamuzi ya haraka