mpasta
JF-Expert Member
- Jan 17, 2011
- 919
- 2,007
RIWAYA: MSAKO WA MWEHU
SEHEMU YA KUMI NA NANE
SURA YA KUMI
Ijumaa ya mkono wa Tanzia nchi nzima
Kachero Manu na Kachero Yasmine walikuwa wapo kwenye viwanja vya Bunge Dodoma tokea jogoo la kwanza. Siku hiyo walilala usingizi wa mang'amung'amu wakifikiria usalama wa viongozi wao wa nchi wanaokutana leo kwenye hitimisho la maombolezo ya kitaifa yaliyodumu kwa muda wa wiki nzima. Walikatika maini juu ya usalama wa viongozi hao hasa baada ya kushindwa kumtia mbaroni "Maso Maso" usiku ule wa Jumatano pale hotelini.
"Maso Maso" aliwaporonyoka katika mazingira ya kutatanisha ya kimiujiza. Mpaka baadhi ya wanausalama wakafikia hatua ya kukufuru kuwa "Maso Maso" ni Jini la Kisomali lina uwezo wa kujigeuza upepo na kutokomea au likajigeuza mwanamke au hata mnyama kama mbwa au paka. Hawakuamini kwa ulinzi ule wa siku ile angeweza vipi kuwapotea kimaajabu kama angekuwa ni binadamu wa kawaida.
Wasichofahamu ni kuwa "Maso Maso" aliwazidi kete kwa kutorokea kupitia mfumo wa bomba la maji taka lililounganisha na hoteli hiyo na nyumba kadhaa za jirani. Bomba hilo lilikuwa linakwenda kuibukia Msalato, nje ya Jiji la Dodoma kando na barabara ya kuelekea Wilaya ya Kondoa.
Kabla hajafika eneo lolote "Maso Maso" alikuwa ni msomaji mzuri wa ramani nzima ya eneo analokwenda na namna atakavyotoroka mambo yakienda segemnege. Alhamisi yote walishinda wanamsaka kila mahali na vizuizi vya barabarani vikazidi kuimarishwa ili wamkamate lakini wakaambulia patupu.
Hitimisho likawa ni kuzuia madhara yake yasitokee hivyo walijihimu kufika eneo la tukio siku hiyo ya Ijumaa kuhakikisha mambo yanaenda vizuri kabisa. Walichokuwa hawakifahamu ni kuwa nae "Maso Maso" alikuwa yupo jirani tu jengo la Bunge, nae akiandaa shambulizi lingine la kishindo. Shambulio ambalo litasababisha kilio kingine cha kusaga na meno cha nchi nzima.
Wageni Waheshimiwa kutoka ndani na nje ya Tanzania walikusanyika ndani ukumbi maarufu kwa jina la "Pius Msekwa" kwa ajili ya kuhitimisha maombolezo ya kitaifa kwa ajili ya kuwapa heshima za mwisho wahanga wasio na hatia, Wabunge, na Mabalozi wa Nchi za Ng'ambo kutoka Marekani na Canada, waliouawa juma moja lililopita. Wingu la huzuni na majonzi lilitanda na kutamalaki katika nyuso za miongoni mwa waombolezaji.
Huku wengine wakilia kwa kwikwi hasa baada ya kuyaona majeneza ya Waheshimiwa Wabunge yanaingizwa Bungeni na kupangwa safusafu. Waombolezaji ambao walionekana nadhifu kwa mavazi yao ya suti nyeusi kuashiria wapo kwenye msiba mzito wa Kitaifa. Maafisa Usalama nao hawakuachwa nyuma walikuwa wametingwa kuhakikisha mambo yote yanaenda sawa bila kuharibika.
Ilipotimu saa nne asubuhi juu ya alama mgeni rasmi wa maombolezo hayo kutoka serikalini, Makamu wa Rais aliyekuwa anasubiriwa kwa pashau kubwa na waombolezaji aliwasili katika viunga hivyo vya Bunge. Alilakiwa na viongozi wa Mkoa wa Dodoma na wa Kitaifa kisha akasindikizwa moja kwa moja kwenda kuweka saini kwenye daftari la kumbukumbu za wageni.
Baada ya hapo akapitiliza moja kwa moja ukumbini kuchukua nafasi yake aliyoandaliwa. Mshehereshaji wa shughuli hiyo alifungua hitimisho la tanzia hiyo kwa sala ya kuwaombea marehemu kutoka kwa wawakilishi toka makundi mbalimbali ya dini, anuwai mbalimbali za madhehebu yote yaliyopo Tanzania. Kisha zikasomwa historia za marehemu kutoka mwakilishi mmoja mmoja kutoka kila familia.
Baada ya hapo wakateuliwa Wabunge wawili wa kutoa neno la shukrani kwa wageni waliohudhuria kwa niaba ya Wabunge wote. Hotuba zao Wabunge hao wawili ziliwaliza waombolezaji na kuwatonesha upya simanzi ya moyo.
Makamu wa Rais nae akatoa neno lake la faraja kwa Watanzania na kuwahakikishia msako mkali wa magaidi bado unaendelea wavute subira na wawe na imani na vyombo vyao vya usalama. Shughuli ikahitimishwa kwa kupanga mistari mirefu na kuanza kuaga maiti zikiwa kwenye majeneza yao. Mpaka kufikia saa tisa mchana shughuli zikawa zimehitimishwa na kila mmoja na wao anatawanyikia anapokujua yeye. Haikuwa shughuli ya maneno chekwachekwa kama ilivyozoeleka katika mikutano ya wanasiasa, hivyo ilihitimishwa kwa wakati. Nyuso za Kachero Manu na Yasmine zilianza kuchanua furaha kwa kubeba tabasamu hasa baada ya kushuhudia shughuli nzima imehitimishwa kwa amani na usalama bila kuchafuliwa na magaidi kama walivyoahidi kuichafua shughuli hiyo.
Lakini ilikuwa ni furaha ya muda mfupi tu, wakiwa wameshapanda kwenye gari lao wanataka kuondoka simu ya Kachero Manu ikaanza kuita. Akashtuka, mapigo ya moyo yanaanza kwenda kasi, akarukwa roho yake kwa sababu alijua ni ya Mudiru wake, Mkuu wa Usalama wa Taifa Bwana Omega Mtanika kutokana na mlio maalumu kwa ajili yake. Alipoitoa kiunoni kwa ajili ya kuipokea akaona ni kweli namba ya simu ya Bosi wake.
Akajua chuma kimeshalia huko maana simu ya Bwana mkubwa huyu ikipigwa ujue kuna lamgambo maalumu kwake la taarifa ya kazi. "Hellow...Kiongozi habari yako", alibonyeza kitufe cha kupokelea simu na kuanza kusalimia Kachero Manu. "Habari mbaya sana, nimepata taarifa sasa hivi kuwa Wabunge wengine 5 na madereva wao wote inasadikiwa kwa pamoja wamefariki wakiwa njiani kurejea Dar es Salaam muda huu, kama nusu saa iliyopita" alijibu salamu Bwana Omega Mtanika kwa kuleta taarifa mpya na mbaya kwa Kachero Manu.
Kachero Manu taarifa hiyo kwake ilipenya kwa kasi kwenye ngoma ya masikio yake na kumsababishia ahisi kama yupo kwenye njozi, tena ndoto yenyewe ni ya mchana kweupe. "Sasa kama mtahitaji msaada wa majasusi wa kigeni toka F.B.I mnijulishe haraka tujipange kuwaalika, kazi njema" akamaliza maongezi yake na kukata simu. Kachero Manu alibaki sekunde kadhaa ameshikilia simu sikioni bila kuiachia haamini kama wamepigwa tobo tena na magaidi.
"Bosi nini zaidi kimekusibu mbona kama unaweweseka sikuelewi" Kachero Yasmine alimzindua mkuu wake wa kazi ambaye alikuwa amerushwa akili na simu ile aliyopigiwa yenye taarifa kabihu isiyovutia kwa msikilizaji. "Aah..acha tu, Wabunge 5 na madereva wao kwa pamoja wamefariki dunia barabarani maeneo kati ya Ihumwe na Pandambili wakiwa njiani kuelekea Dar es Salaam" alijibiwa Kachero Yasmine kwa sauti ya unyonge.
"Huyu atakuwa mwana halula "Maso Maso" kashafanya yake, mshenzi sana" alisema Kachero Yasmine kwa sauti ya hamaki. Kachero Manu hakujibu kitu, alikuwa anaona Mkuu wake wa kazi ameshaanza kupoteza imani naye.
"Anasema anataka alete F. B. I waje kuwasaka magaidi, ni kama mshenga kumwambia mume aliyeshindwa kumpa ujauzito mkewe kuwa atamletea mume mwenza wachuane" aliendelea kuwaza Kachero Manu kiunyonge."Tuelekee hospitali ya Mkoa, tukacheki maiti zilizoletwa afu tutajua ya kufanya", alitoa amri Kachero Manu. Kachero Yasmine akatii amri ya mkubwa wake wa kazi, wakatoka mbio mbio kama watu waliopagawa.














SEHEMU YA KUMI NA NANE
SURA YA KUMI
Ijumaa ya mkono wa Tanzia nchi nzima
Kachero Manu na Kachero Yasmine walikuwa wapo kwenye viwanja vya Bunge Dodoma tokea jogoo la kwanza. Siku hiyo walilala usingizi wa mang'amung'amu wakifikiria usalama wa viongozi wao wa nchi wanaokutana leo kwenye hitimisho la maombolezo ya kitaifa yaliyodumu kwa muda wa wiki nzima. Walikatika maini juu ya usalama wa viongozi hao hasa baada ya kushindwa kumtia mbaroni "Maso Maso" usiku ule wa Jumatano pale hotelini.
"Maso Maso" aliwaporonyoka katika mazingira ya kutatanisha ya kimiujiza. Mpaka baadhi ya wanausalama wakafikia hatua ya kukufuru kuwa "Maso Maso" ni Jini la Kisomali lina uwezo wa kujigeuza upepo na kutokomea au likajigeuza mwanamke au hata mnyama kama mbwa au paka. Hawakuamini kwa ulinzi ule wa siku ile angeweza vipi kuwapotea kimaajabu kama angekuwa ni binadamu wa kawaida.
Wasichofahamu ni kuwa "Maso Maso" aliwazidi kete kwa kutorokea kupitia mfumo wa bomba la maji taka lililounganisha na hoteli hiyo na nyumba kadhaa za jirani. Bomba hilo lilikuwa linakwenda kuibukia Msalato, nje ya Jiji la Dodoma kando na barabara ya kuelekea Wilaya ya Kondoa.
Kabla hajafika eneo lolote "Maso Maso" alikuwa ni msomaji mzuri wa ramani nzima ya eneo analokwenda na namna atakavyotoroka mambo yakienda segemnege. Alhamisi yote walishinda wanamsaka kila mahali na vizuizi vya barabarani vikazidi kuimarishwa ili wamkamate lakini wakaambulia patupu.
Hitimisho likawa ni kuzuia madhara yake yasitokee hivyo walijihimu kufika eneo la tukio siku hiyo ya Ijumaa kuhakikisha mambo yanaenda vizuri kabisa. Walichokuwa hawakifahamu ni kuwa nae "Maso Maso" alikuwa yupo jirani tu jengo la Bunge, nae akiandaa shambulizi lingine la kishindo. Shambulio ambalo litasababisha kilio kingine cha kusaga na meno cha nchi nzima.
Wageni Waheshimiwa kutoka ndani na nje ya Tanzania walikusanyika ndani ukumbi maarufu kwa jina la "Pius Msekwa" kwa ajili ya kuhitimisha maombolezo ya kitaifa kwa ajili ya kuwapa heshima za mwisho wahanga wasio na hatia, Wabunge, na Mabalozi wa Nchi za Ng'ambo kutoka Marekani na Canada, waliouawa juma moja lililopita. Wingu la huzuni na majonzi lilitanda na kutamalaki katika nyuso za miongoni mwa waombolezaji.
Huku wengine wakilia kwa kwikwi hasa baada ya kuyaona majeneza ya Waheshimiwa Wabunge yanaingizwa Bungeni na kupangwa safusafu. Waombolezaji ambao walionekana nadhifu kwa mavazi yao ya suti nyeusi kuashiria wapo kwenye msiba mzito wa Kitaifa. Maafisa Usalama nao hawakuachwa nyuma walikuwa wametingwa kuhakikisha mambo yote yanaenda sawa bila kuharibika.
Ilipotimu saa nne asubuhi juu ya alama mgeni rasmi wa maombolezo hayo kutoka serikalini, Makamu wa Rais aliyekuwa anasubiriwa kwa pashau kubwa na waombolezaji aliwasili katika viunga hivyo vya Bunge. Alilakiwa na viongozi wa Mkoa wa Dodoma na wa Kitaifa kisha akasindikizwa moja kwa moja kwenda kuweka saini kwenye daftari la kumbukumbu za wageni.
Baada ya hapo akapitiliza moja kwa moja ukumbini kuchukua nafasi yake aliyoandaliwa. Mshehereshaji wa shughuli hiyo alifungua hitimisho la tanzia hiyo kwa sala ya kuwaombea marehemu kutoka kwa wawakilishi toka makundi mbalimbali ya dini, anuwai mbalimbali za madhehebu yote yaliyopo Tanzania. Kisha zikasomwa historia za marehemu kutoka mwakilishi mmoja mmoja kutoka kila familia.
Baada ya hapo wakateuliwa Wabunge wawili wa kutoa neno la shukrani kwa wageni waliohudhuria kwa niaba ya Wabunge wote. Hotuba zao Wabunge hao wawili ziliwaliza waombolezaji na kuwatonesha upya simanzi ya moyo.
Makamu wa Rais nae akatoa neno lake la faraja kwa Watanzania na kuwahakikishia msako mkali wa magaidi bado unaendelea wavute subira na wawe na imani na vyombo vyao vya usalama. Shughuli ikahitimishwa kwa kupanga mistari mirefu na kuanza kuaga maiti zikiwa kwenye majeneza yao. Mpaka kufikia saa tisa mchana shughuli zikawa zimehitimishwa na kila mmoja na wao anatawanyikia anapokujua yeye. Haikuwa shughuli ya maneno chekwachekwa kama ilivyozoeleka katika mikutano ya wanasiasa, hivyo ilihitimishwa kwa wakati. Nyuso za Kachero Manu na Yasmine zilianza kuchanua furaha kwa kubeba tabasamu hasa baada ya kushuhudia shughuli nzima imehitimishwa kwa amani na usalama bila kuchafuliwa na magaidi kama walivyoahidi kuichafua shughuli hiyo.
Lakini ilikuwa ni furaha ya muda mfupi tu, wakiwa wameshapanda kwenye gari lao wanataka kuondoka simu ya Kachero Manu ikaanza kuita. Akashtuka, mapigo ya moyo yanaanza kwenda kasi, akarukwa roho yake kwa sababu alijua ni ya Mudiru wake, Mkuu wa Usalama wa Taifa Bwana Omega Mtanika kutokana na mlio maalumu kwa ajili yake. Alipoitoa kiunoni kwa ajili ya kuipokea akaona ni kweli namba ya simu ya Bosi wake.
Akajua chuma kimeshalia huko maana simu ya Bwana mkubwa huyu ikipigwa ujue kuna lamgambo maalumu kwake la taarifa ya kazi. "Hellow...Kiongozi habari yako", alibonyeza kitufe cha kupokelea simu na kuanza kusalimia Kachero Manu. "Habari mbaya sana, nimepata taarifa sasa hivi kuwa Wabunge wengine 5 na madereva wao wote inasadikiwa kwa pamoja wamefariki wakiwa njiani kurejea Dar es Salaam muda huu, kama nusu saa iliyopita" alijibu salamu Bwana Omega Mtanika kwa kuleta taarifa mpya na mbaya kwa Kachero Manu.
Kachero Manu taarifa hiyo kwake ilipenya kwa kasi kwenye ngoma ya masikio yake na kumsababishia ahisi kama yupo kwenye njozi, tena ndoto yenyewe ni ya mchana kweupe. "Sasa kama mtahitaji msaada wa majasusi wa kigeni toka F.B.I mnijulishe haraka tujipange kuwaalika, kazi njema" akamaliza maongezi yake na kukata simu. Kachero Manu alibaki sekunde kadhaa ameshikilia simu sikioni bila kuiachia haamini kama wamepigwa tobo tena na magaidi.
"Bosi nini zaidi kimekusibu mbona kama unaweweseka sikuelewi" Kachero Yasmine alimzindua mkuu wake wa kazi ambaye alikuwa amerushwa akili na simu ile aliyopigiwa yenye taarifa kabihu isiyovutia kwa msikilizaji. "Aah..acha tu, Wabunge 5 na madereva wao kwa pamoja wamefariki dunia barabarani maeneo kati ya Ihumwe na Pandambili wakiwa njiani kuelekea Dar es Salaam" alijibiwa Kachero Yasmine kwa sauti ya unyonge.
"Huyu atakuwa mwana halula "Maso Maso" kashafanya yake, mshenzi sana" alisema Kachero Yasmine kwa sauti ya hamaki. Kachero Manu hakujibu kitu, alikuwa anaona Mkuu wake wa kazi ameshaanza kupoteza imani naye.
"Anasema anataka alete F. B. I waje kuwasaka magaidi, ni kama mshenga kumwambia mume aliyeshindwa kumpa ujauzito mkewe kuwa atamletea mume mwenza wachuane" aliendelea kuwaza Kachero Manu kiunyonge."Tuelekee hospitali ya Mkoa, tukacheki maiti zilizoletwa afu tutajua ya kufanya", alitoa amri Kachero Manu. Kachero Yasmine akatii amri ya mkubwa wake wa kazi, wakatoka mbio mbio kama watu waliopagawa.















