Riwaya: Msako wa mwehu

Riwaya: Msako wa mwehu

RIWAYA: MSAKO WA MWEHU

SEHEMU YA KUMI NA NANE

SURA YA KUMI
Ijumaa ya mkono wa Tanzia nchi nzima
Kachero Manu na Kachero Yasmine walikuwa wapo kwenye viwanja vya Bunge Dodoma tokea jogoo la kwanza. Siku hiyo walilala usingizi wa mang'amung'amu wakifikiria usalama wa viongozi wao wa nchi wanaokutana leo kwenye hitimisho la maombolezo ya kitaifa yaliyodumu kwa muda wa wiki nzima. Walikatika maini juu ya usalama wa viongozi hao hasa baada ya kushindwa kumtia mbaroni "Maso Maso" usiku ule wa Jumatano pale hotelini.
"Maso Maso" aliwaporonyoka katika mazingira ya kutatanisha ya kimiujiza. Mpaka baadhi ya wanausalama wakafikia hatua ya kukufuru kuwa "Maso Maso" ni Jini la Kisomali lina uwezo wa kujigeuza upepo na kutokomea au likajigeuza mwanamke au hata mnyama kama mbwa au paka. Hawakuamini kwa ulinzi ule wa siku ile angeweza vipi kuwapotea kimaajabu kama angekuwa ni binadamu wa kawaida.
Wasichofahamu ni kuwa "Maso Maso" aliwazidi kete kwa kutorokea kupitia mfumo wa bomba la maji taka lililounganisha na hoteli hiyo na nyumba kadhaa za jirani. Bomba hilo lilikuwa linakwenda kuibukia Msalato, nje ya Jiji la Dodoma kando na barabara ya kuelekea Wilaya ya Kondoa.
Kabla hajafika eneo lolote "Maso Maso" alikuwa ni msomaji mzuri wa ramani nzima ya eneo analokwenda na namna atakavyotoroka mambo yakienda segemnege. Alhamisi yote walishinda wanamsaka kila mahali na vizuizi vya barabarani vikazidi kuimarishwa ili wamkamate lakini wakaambulia patupu.
Hitimisho likawa ni kuzuia madhara yake yasitokee hivyo walijihimu kufika eneo la tukio siku hiyo ya Ijumaa kuhakikisha mambo yanaenda vizuri kabisa. Walichokuwa hawakifahamu ni kuwa nae "Maso Maso" alikuwa yupo jirani tu jengo la Bunge, nae akiandaa shambulizi lingine la kishindo. Shambulio ambalo litasababisha kilio kingine cha kusaga na meno cha nchi nzima.
Wageni Waheshimiwa kutoka ndani na nje ya Tanzania walikusanyika ndani ukumbi maarufu kwa jina la "Pius Msekwa" kwa ajili ya kuhitimisha maombolezo ya kitaifa kwa ajili ya kuwapa heshima za mwisho wahanga wasio na hatia, Wabunge, na Mabalozi wa Nchi za Ng'ambo kutoka Marekani na Canada, waliouawa juma moja lililopita. Wingu la huzuni na majonzi lilitanda na kutamalaki katika nyuso za miongoni mwa waombolezaji.
Huku wengine wakilia kwa kwikwi hasa baada ya kuyaona majeneza ya Waheshimiwa Wabunge yanaingizwa Bungeni na kupangwa safusafu. Waombolezaji ambao walionekana nadhifu kwa mavazi yao ya suti nyeusi kuashiria wapo kwenye msiba mzito wa Kitaifa. Maafisa Usalama nao hawakuachwa nyuma walikuwa wametingwa kuhakikisha mambo yote yanaenda sawa bila kuharibika.
Ilipotimu saa nne asubuhi juu ya alama mgeni rasmi wa maombolezo hayo kutoka serikalini, Makamu wa Rais aliyekuwa anasubiriwa kwa pashau kubwa na waombolezaji aliwasili katika viunga hivyo vya Bunge. Alilakiwa na viongozi wa Mkoa wa Dodoma na wa Kitaifa kisha akasindikizwa moja kwa moja kwenda kuweka saini kwenye daftari la kumbukumbu za wageni.
Baada ya hapo akapitiliza moja kwa moja ukumbini kuchukua nafasi yake aliyoandaliwa. Mshehereshaji wa shughuli hiyo alifungua hitimisho la tanzia hiyo kwa sala ya kuwaombea marehemu kutoka kwa wawakilishi toka makundi mbalimbali ya dini, anuwai mbalimbali za madhehebu yote yaliyopo Tanzania. Kisha zikasomwa historia za marehemu kutoka mwakilishi mmoja mmoja kutoka kila familia.
Baada ya hapo wakateuliwa Wabunge wawili wa kutoa neno la shukrani kwa wageni waliohudhuria kwa niaba ya Wabunge wote. Hotuba zao Wabunge hao wawili ziliwaliza waombolezaji na kuwatonesha upya simanzi ya moyo.
Makamu wa Rais nae akatoa neno lake la faraja kwa Watanzania na kuwahakikishia msako mkali wa magaidi bado unaendelea wavute subira na wawe na imani na vyombo vyao vya usalama. Shughuli ikahitimishwa kwa kupanga mistari mirefu na kuanza kuaga maiti zikiwa kwenye majeneza yao. Mpaka kufikia saa tisa mchana shughuli zikawa zimehitimishwa na kila mmoja na wao anatawanyikia anapokujua yeye. Haikuwa shughuli ya maneno chekwachekwa kama ilivyozoeleka katika mikutano ya wanasiasa, hivyo ilihitimishwa kwa wakati. Nyuso za Kachero Manu na Yasmine zilianza kuchanua furaha kwa kubeba tabasamu hasa baada ya kushuhudia shughuli nzima imehitimishwa kwa amani na usalama bila kuchafuliwa na magaidi kama walivyoahidi kuichafua shughuli hiyo.
Lakini ilikuwa ni furaha ya muda mfupi tu, wakiwa wameshapanda kwenye gari lao wanataka kuondoka simu ya Kachero Manu ikaanza kuita. Akashtuka, mapigo ya moyo yanaanza kwenda kasi, akarukwa roho yake kwa sababu alijua ni ya Mudiru wake, Mkuu wa Usalama wa Taifa Bwana Omega Mtanika kutokana na mlio maalumu kwa ajili yake. Alipoitoa kiunoni kwa ajili ya kuipokea akaona ni kweli namba ya simu ya Bosi wake.
Akajua chuma kimeshalia huko maana simu ya Bwana mkubwa huyu ikipigwa ujue kuna lamgambo maalumu kwake la taarifa ya kazi. "Hellow...Kiongozi habari yako", alibonyeza kitufe cha kupokelea simu na kuanza kusalimia Kachero Manu. "Habari mbaya sana, nimepata taarifa sasa hivi kuwa Wabunge wengine 5 na madereva wao wote inasadikiwa kwa pamoja wamefariki wakiwa njiani kurejea Dar es Salaam muda huu, kama nusu saa iliyopita" alijibu salamu Bwana Omega Mtanika kwa kuleta taarifa mpya na mbaya kwa Kachero Manu.
Kachero Manu taarifa hiyo kwake ilipenya kwa kasi kwenye ngoma ya masikio yake na kumsababishia ahisi kama yupo kwenye njozi, tena ndoto yenyewe ni ya mchana kweupe. "Sasa kama mtahitaji msaada wa majasusi wa kigeni toka F.B.I mnijulishe haraka tujipange kuwaalika, kazi njema" akamaliza maongezi yake na kukata simu. Kachero Manu alibaki sekunde kadhaa ameshikilia simu sikioni bila kuiachia haamini kama wamepigwa tobo tena na magaidi.
"Bosi nini zaidi kimekusibu mbona kama unaweweseka sikuelewi" Kachero Yasmine alimzindua mkuu wake wa kazi ambaye alikuwa amerushwa akili na simu ile aliyopigiwa yenye taarifa kabihu isiyovutia kwa msikilizaji. "Aah..acha tu, Wabunge 5 na madereva wao kwa pamoja wamefariki dunia barabarani maeneo kati ya Ihumwe na Pandambili wakiwa njiani kuelekea Dar es Salaam" alijibiwa Kachero Yasmine kwa sauti ya unyonge.
"Huyu atakuwa mwana halula "Maso Maso" kashafanya yake, mshenzi sana" alisema Kachero Yasmine kwa sauti ya hamaki. Kachero Manu hakujibu kitu, alikuwa anaona Mkuu wake wa kazi ameshaanza kupoteza imani naye.
"Anasema anataka alete F. B. I waje kuwasaka magaidi, ni kama mshenga kumwambia mume aliyeshindwa kumpa ujauzito mkewe kuwa atamletea mume mwenza wachuane" aliendelea kuwaza Kachero Manu kiunyonge."Tuelekee hospitali ya Mkoa, tukacheki maiti zilizoletwa afu tutajua ya kufanya", alitoa amri Kachero Manu. Kachero Yasmine akatii amri ya mkubwa wake wa kazi, wakatoka mbio mbio kama watu waliopagawa.
 
Riwaya mpya ya "Msako wa Mwehu" inapatikana sehemu zifuatazo kwa gharama ya Tsh.10,000/=
(1)DAR ES SALAAM
(i)Ununio- Come and Read Bookstore
0717 978 899
(ii)Ubungo Stendi-Opposite na TBS gate
0784 033 820
(iii)Posta Mpya Sanamu la Askari
0713 454 152-Nje ya JD Pharmacy
(iv)Kariakoo-Benki ya Posta Msimbazi
0652055555
(2)MOSHI-
+255 713 082 140
(3)ARUSHA-
+255 757 690 302 (Nje ya KIMAHAMA Bookshop)
(4)LINDI STENDI
+255 757 461 516
(5) MTWARA
+255 626 065 669
(6)KIBAHA
0625920847
(7)MWANZA-MAKOROBOI
0735 475 112
(8)TANGA-Madaraka Street
0655 173 115
(9)ZANZIBAR
Darajani-Opposite Masomo Bookshop
0777027207
(10) MOROGORO
0719226293
NB:
Unaweza kuwasiliana na Mwandishi moja kwa moja kupitia
Barua Pepe:
Badi Mwalimu Bao
badi.bao11@gmail.com
Simu:0625920847
 
Jipatie nakala yako
IMG-20200614-WA0046.jpg
 
Riwaya: MSAKO WA MWEHU
SEHEMU YA KUMI NA.TISA


Kachero Manu aibukia "Chops Modern Car Wash & Garage"
Ilikuwa ni kiota kipya cha kuoshea magari kilichozinduliwa jirani kabisa na Bunge, mkabala na Chuo cha Biashara "College of Business Education" (C. B. E), Dodoma. Ilikuwa ni majira ya Alasiri ya siku ya Jumapili Kachero Manu alikuwa anashuka kwenye gari yake aliloliegesha mbele ya sehemu maalumu ya kuoshea magari maarufu kwa jina la "Chops Modern Car Wash".
Lilikuwa ni eneo nadhifu linaloosha magari kwa kutumia mashine, likiwa kwa mbele yake limeungana na grereji kubwa ya kisasa ya kukarabati magari inaitwa "Chops Garage". Huku mteja akipatiwa huduma anayotaka ya kinywaji kama chai, kahawa au soda yoyote anayoihitaji wakati anasubiria gari yake.
"Bosi karibu, huduma zetu ni nzuri na nafuu sana, kuosha gari ni Tsh. 15,000/= tu" alikuwa ni kijana nadhifu mhusika wa eneo hilo akitoa makaribisho. "Ahsante sana, naomba kuonana na mhusika wa kituo" aliomba Kachero Manu. "Mhusika pita hapa ukatokezee kule mbele utaona kibao kimeandiwa kwa kimombo "Garage Manager" hapo utamkuta" alijibu kwa unyenyekevu.
"Sawa basi nioshee hilo gari yangu usichelewe sana, nitatoka ndani ya robo saa" alitoa maagizo Kachero Manu huku akimuachia funguo wake wa gari kijana huyo na kutokomea kuelekea ofisi ya Meneja wa gereji. Ilimchukua dakika 3 tu kufika mpaka mlango wa Meneja huyo. Kabla hajabisha hodi, akashtukia anafunguliwa mlango."Karibu sana ndugu" alisema yule mwarabu aliyeonekana kuwa na mwili wa kushupaa kuonyesha ni mtu wa mazoezi.
"Ahsante sana, nimekaribia" yalikuwa ndio majibu ya Kachero Manu huku anapitiliza na kwenda kukaa kwenye kiti. "Sijui nikusaidie nini rafiki yangu" aliuliza yule Mwarabu, akionekana ni mtu mkorofi. Kabla ya kujibu Kachero Manu akang'ariza macho kwenye kiofisi kie kwa haraka haraka.
Akagundua kuna CCTV-Kamera inayorekodi matukio ya eneo zima la gereji. Pia ofisi ilikuwa ni ndogo ila samani zake ni za gharama toka nchi za ng'ambo. Ukutani kulikuwa na picha kubwa ya Rais wa nchi ya Tanzania, na pembeni yake kulikuwa na mabango ya picha za maandishi ya Q'uran kitabu kitakatifu kwa Waislamu.
"Hawa wanajitia kumshiriki Mwenyezi Mungu lakini kumbe wanamshiriki Shetani" alijiwazia moyoni mwake. Kisha akavunja ukimya, "mimi naitwa Kachero Manu, nimekuja kuna maswali ningependa nikuhoji ili nipate majibu yake ya kina". Yule Meneja alikuwa anakunywa soda yake iliyokuwa mezani, ghafla baada ya kusikia maelezo ya Kachero Manu, soda ikampalia kooni akaanza kukohoa mfululizo. "Ok.....Ok...verry sorry ehee nakusikiliza, ila kwanza naomba kitambulisho chako" alijieleza yule Meneja akionyesha kujiamini. Kachero Manu akajibu kwa vitendo kwa kuonyesha kitambulisho, yule Meneja akajiridhisha, mahojiano yakaanza;
Kachero Manu: "Jina lako kamili ni nani? "
Meneja: "Naitwa Kareem Abdallah"
Kachero Manu: "Nani mmiliki wa hili eneo? "
Meneja: "Hili eneo la familia"
Kachero Manu: "Nafahamu ila nataka kujua ambaye jina lake lipo kwenye usajili kule BRELA".
Meneja: "Ni Baba yangu mzazi Mzee Hafeedh Abdallah"
Kachero Manu: "Mnazo rekodi ya magari yanayoingia kupata huduma zenu kwa siku"?
Meneja: "Tunazo rekodi na ukitaka nitakupatia bila shida yoyote"
Kachero Manu: "Ninaomba unipatie ya wiki iliyopita mpaka kufikia siku ya Jumapili"
Meneja: "Subirisha kidogo nikudurufie". Kikapita kitambo kifupi mara kompyuta yake mezani ikaanza kutoa karatasi kupitia printa yake. Akamkabidhi Kachero Manu. Akazipokea na kuanza kuzipitia, baada ya kuzipitia zile karatasi, mahojiano yakaendelea upya.
Kachero Manu: "Sioni rekodi ya siku ya Ijumaa" (akauliza huku anamkazia macho)
Meneja: "Ijumaa siku yetu kubwa ya ibada huwa hatufanyi kazi, tunamwabudu Allah tu, au nyie Jumapili mnaenda kazini?" (akauliza kichokozi kujitafutia kichaka cha kufichia uwongo wake). Kachero Manu akapotezea kujibu swali hilo la kizushi.
Kachero Manu: "Kuna magari yoyote ya Waheshimiwa huwa yanakuja hapa kupata huduma?"
Meneja: "Siwezi kufahamu kama hili ni gari la Mlalaheri au Mlalahoi, sie kazi yetu ni kuhudumia watu wote kwa usawa. Mimi nakaa tu ofisini sihusiki kazi za nje".
Kachero Manu: "Una habari kuwa Wabunge 5 na madereva wao wamefariki? "
Meneja: "Msalie Mtumee...ndio kwanza unanipasha hizo taarifa sijasikia bado". Kachero Manu alipomuangalia machoni mwake alijua fika kuna uwongo anauficha.
Kachero Manu: "Ahsante kwa ushirikiano wako, nikikuhitaji tena sitosita kukutafuta".
Meneja: "Ahsante sana, karibu tena Afande". Wakapeana mikono na kuagana. Kachero Manu akaelekea mpaka alipoaliacha gari lake. "Bosi tayari gari na risiti yako ya malipo ya EFD tayari hii hapa" alisema yule kijana huku anakabidhi risiti kwa Kachero Manu. "Ahsante sana umeosha vizuri gari yangu, kamata hii bahashishi yako" alisema Kachero Manu huku anamkabidhi mkono wa ahsante wa Sh.10,000/= yule kijana.
"Ahsante sana Bosi Mungu akubariki sana" alijibu yule kijana huku anapokea ile pesa huku akiwa na furaha fokofoko isiyo na kifani. Kachero Manu akawasha gari yake akawa anarudi kinyumenyume ili aweze kuondoka akasimamisha ghafla huku yule kijana yupo pembezoni mwa dirisha la dereva.
Akashusha kioo chake kidogo "kijana chukua hii kadi yangu ya anuani yangu na namba ya simu tuonane leo ukitoka tu uje 'Chako ni Chako Bar' saa mbili na nusu usiku tuongee nina mpango wa kufungua sehemu ya kuoshea magari kama hii hapa, uje unipe ushauri rafiki" akamrushia ile kadi huku anatimka bila kusubiri jibu toka kwa yule kijana. Alijua tu piga ua lazima aje kwenye udhia penyenza rupia, sasa kashampa kilainishi atashindwa vipi kutokea eneo la miadi.

Mauaji ya kutisha ndani ya Chako ni Chako Bar
Kachero Manu alifika muda saa mbili na dakika kadhaa huku akikuta watu wameshonana ile mbaya. Alikuwa anasikia tu "Chako ni Chako Bar" ndio mara yake ya kwanza kukanyaga. Licha ya kwamba mkewe anafanya kazi Ndani ya Jiji hili la Dodoma.
Alichoshangazwa ni kuwa jina la Baa na mandhari ya muonekano wa nje ni mbingu na ardhi. Akifananiza na kiota kama "Rose garden" ya jijini Dar es Salaam ambayo ina jina kubwa kuliko yenyewe ilivyo. Baa hiyo ya "Chako ni Chako" inapatikana maeneo ya barabara ya kuelekea uwanja wa ndege "Airport Road", eneo ambalo ni maarufu sana Jijini Dodoma.
Alikuta wateja pomoni wamejiachia ile mbaya, mambo ya nyama choma, kuku choma, mishikaki, chipsi kavu kwa mayai, supu za kongoro ndio mahali pake. Bila kusahau wanawake viruka njia hapo pia ndio eneo lao la kusaka mawindo toka kwa wanaume viruka mito. Kila mtu na lake, wengine wanakula na kunywa na baadhi yao wanacheza muziki unaopigwa kwenye santuri. Ila kuna meza moja tu yenye viti vitatu kimekaliwa kimoja tu.
Akaenda kuketi palepale, wakasalimiana na mteja aliyemkuta amekaa hapo anapiga vyombo vyake hana habari na mtu. Mara mhudumu wa kike aliyevali sare maalumu akaja kwa haraka. "Karibu sana Nakusikiliza kaka yangu!" ilikuwa ni sauti ya mhudumu ikimtaka Kachero Manu atoe oda yake. "Naomba uniletee kuku wa kuchoma wa kienyeji mzima, akauke vizuri tafadhali, bila kusahau maji ya moto aina ya 'Usambara Soft' chupa kubwa, Yale maji toka Tanga" alitoa oda yake kwa msisitizo huku anaperuzi simu yake kuangalia arafa zozote zilizoingia kwenye simu kwa muda huo.
Yule mhudumu akawa anaondoka anaondoka kwa mwendo wa njiwa, Kachero Manu akawa anamsindikiza kwa macho ya huba kuangalia miondoko ya yule dada wa Kinyaturu. Kitendo ambacho yule mteja mwenzake alishuhudia namna anavyokula kwa macho.
"Brother ni mgeni Dodoma Eeeh... Brother...?" aliulizwa na yule jirani yake kwa sauti ya kilevi. "Hapana Dodoma ni mwenyeji kiasi chake maana mke wangu anaishi hapa hapa Dodoma, ila viwanja hivi ndio mara yangu ya kwanza kutia maguu yangu alimjibu Kachero Manu jamaa yule ambaye ulevi ulishaanza kumchukua vilivyo.
"Basi Brother hapa ndio umefika kuna mabinti wengi sana 'visu' toka Singida, Babati, Mbulu, Kateshi na Arusha. Hao mabinti kwenye viunga vya 'kula bata' ndani ya Jiji hili hawakosekani. Wametamalaki kwenye lounges, clubs, pubs, local bars, restaurants, massage points na saloons za kike' hao ndio wana hati miliki hapa Dodoma. Hapa nazungumzia 15 - 23 yrs old chicks!" alizungumza kwa mbwembwe za kilevi yule jamaa huku akitia kimombo, akionekana ni mtu wa kuendekeza starehe vilivyo.
"Nashukuru kwa kunitoa tongo tongo za macho nilikuwa siyajui hayo" alimjibu kwa kumvika kilemba cha ukoka. Basi ikawa ndio kama amechochea kuni kwenye moto, wacha jamaa aendelee kubwabwaja. "Ikifika jioni watu taratibu wanaanza kujisogeza viwanja kama' Platinumz, Rainbow, Rose Garden, Maisha Club, Morena, Chako ni Chako hapa kama unavyojionea mwenyewe, African Dreams, hapa tunakuja kufuata kuku na hili giza giza la hapa ukiiba mke wa mtu, sisi wanaume virukamito unakuja kujisunda nae huku hata huonekani na kadamnasi ya watu" aliendeleza hadithi zake yule mlevi. Ikabidi Kachero Manu abakie anachekea tumboni hakutaka mazoea nae sana kwa sababu hamfahamu, huku anakunywa maji aliyoagiza wakati anasubiria oda yake ya kuku.
Haikuchukua muda akaaga yule mlevi akaondoka zake kwa mwendo wa kilevi, anapepesuka njia nzima, mezani akabakia Kachero Manu pekee anabung'aa tu. Baada ya nusu saa kuku akawa tayari ameletwa mezani, akaagiza na "Sprite" baridi akaanza kumshambulia kuku kama ana njaa ya ndovu kumla mwanawe. Kila alipokuwa akitazama saa muda ulikuwa unayoyoma kijana anayemsubiria hatokei. Mpaka saa tatu kamili alikuwa hajatokeza bado.
Akiwa bado amezama kwenye mawazo ya yule kijana waliyewekeana nae miadi akashtukia anaguswa begani. "Bosi habari yako, samahani kwa kuchelewa majukumu yaliongezeka pale kazini hata nyumbani sijafika nimeona bora tuonane na wewe kwanza ndio nichome zangu maskani" alijitetea kiustaarabu yule kijana ili asionekane mswahili, mwenye ahadi za mkahawani akiwa na mavazi yake ya kazi.
Kachero akamtoa mashaka, kisha akamkaribisha kitini. Akamuitia mhudumu na kumpa wasaa kijana yule wa kuagiza chochote anachokitaka katika maakuli na mashrabu, mazungumzo yakaanza yao yakafunguliwa rasmi.
Kachero Manu: "Kama nilivyokuambia nina mpango wa kufungua sehemu ya kisasa kama ile yenu pale, hivyo nahitaji kukufahamu kwa undani, huenda nikakupa Umeneja". Alidanganya Kachero Manu apate analolikusudia.
Kijana: "Hamna shida, tena mie nitashukuru ukinipa ajira maana wale hata siwaelewi kuhusu mustakabali wangu".
Kachero Manu: "Kivipi huwaelewi?"
Kijana: "Mfano juzi Ijumaa, waliniambia hawatofungua kwa ajili ni siku ya ibada lakini cha ajabu nina mshikaji wangu yupo jirani pale akanishtua Ijumaa hiyo wamefungua na wanafanya kazi. Ikabidi nije kisirisiri nikathibitisha kweli pamefunguliwa na nikamuona mtu anayaosha magari, nikashangaa sasa kuna nini kinaendelea nyuma yangu".
Kachero Manu: "Inaelekea watakufukuza siku za usoni, sasa huyo mtu aliyefanya Ijumaa bado upo nae au hajaja tena? "
Kijana: "Hajafika tena, ila nilishangaa sana kwa sababu ni rafiki wa Babu mmiliki wa ile "car wash" Mzee Hafeedh Abdallah, ameshawahi kuja nae pale ile wiki iliyopita zaidi ya mara tatu. Hivyo hana hadhi kabisa ya kuosha magari katu".
Kachero Manu: "Labda waliona siku hiyo kuna wageni wengi wa heshima wanaokuja kwenye maombolezo ya msiba, hivyo wanahitaji mtu makini anayejua hata kukicharaza kimombo..!"
Kijana: "Labda maana mie kwa haraka niliyaona magari ya Wabunge si chini ya saba yanaoshwa pale, achilia mbali vigogo wengine"
Mhudumu mara akafika kumletea chakula chake yule kijana. "Bosi nakuja ngoja niende msalani kwanza kibofu kitapasuka, nilindie usalama wa zege langu wasitue inzi maana nina ubao kinyama aisee... " akanyanyuka zake yule kijana kuelekea kuutafuta ulipo msala. Kachero Manu alikuwa na furaha isiyo kifani. Sasa ameshapata mtu wa kumbinya nae ni Meneja wa 'Chops carwash' mpaka watamtoa "Maso Maso" .
"Ananidanganya Ijumaa siku ya ibada hakufanya kazi kumbe hata kijana wao amethibitisha kwa macho yake palifunguliwa" alijisemea Kachero Manu nafsini mwake. Macho yake Kachero yakiwa uelekeo wa msala akimsubiria kwa hamu kijana arejee, ghafla akaona vijana wawili wanaelekea msalani kwa mwendo wa kasi. Akasisimkwa na malaika, hisia zikamtuma hao ni watu wabaya, kama ni kubanwa na haja haiwezekani wote kwa pamoja tena muwe mnakaribia kuingia chooni ndio wajifanye wamezidiwa.
Akaamua kutii hisia zake, Kachero Manu akachomoka nae kwa mwendo wa kupega huku mkono upo kiunoni tayari kwa kuchomoa bastola. Alipokata kupinda korido ya kuelekea vyooni, akamkuta mmoja wao amesimama nje ya mlango wa choo uliofungwa. Yule jamaa alipomwona tu Kachero Manu akaanza kumrushia mvua ya risasi. Lakini alikuwa anapiga ovyo kuonyesha sio mzoefu, hakuna hata moja iliyolenga shabaha. Na hata kama ingelenga shabaha, Kachero Manu daima dawamu, layla wa nahara anavaa fulana maalumu ya kuzuia risasi kupenya mwilini.
Jamaa yule baada ya kuona Kachero Manu ameshachomoa bastola yake akaona isiwe tabu akaruka ukuta na kukimbia zake, akimtelekeza yule mwenzake aliyekuja nae. Mjuba mwingine mle chooni alibaki ameduwaa baada ya kusikia shaba zinarindima nje ya choo akajua kimenuka tayari. Akatoka mkukumkuku nje ya choo huku mkononi ameshika bastola yake.
 
Riwaya mpya ya "Msako wa Mwehu" inapatikana sehemu zifuatazo kwa gharama ya Tsh.10,000/=
(1)DAR ES SALAAM
(i)Ununio- Come and Read Bookstore
0717 978 899
(ii)Ubungo Stendi-Opposite na TBS gate
0784 033 820
(iii)Posta Mpya Sanamu la Askari
0713 454 152-Nje ya JD Pharmacy
(iv)Kariakoo-Benki ya Posta Msimbazi
0652055555
(2)MOSHI-
+255 713 082 140
(3)ARUSHA-
+255 757 690 302 (Nje ya KIMAHAMA Bookshop)
(4)LINDI STENDI
+255 757 461 516
(5) MTWARA
+255 626 065 669
(6)KIBAHA
0625920847
(7)MWANZA-MAKOROBOI
0735 475 112
(8)TANGA-Madaraka Street
0655 173 115
(9)ZANZIBAR
Darajani-Opposite Masomo Bookshop
0777027207
(10) MOROGORO
0719226293
NB:
Unaweza kuwasiliana na Mwandishi moja kwa moja kupitia
Barua Pepe:
Badi Mwalimu Bao
badi.bao11@gmail.com
Simu:0625920847
Tutafika kukuunga mkono
 
RIWAUA: MSAKO WA MWEHU

SEHEMU YA-20


Jamaa yule baada ya kuona Kachero Manu ameshachomoa bastola yake akaona isiwe tabu akaruka ukuta na kukimbia zake, akimtelekeza yule mwenzake aliyekuja nae. Mjuba mwingine mle chooni alibaki ameduwaa baada ya kusikia shaba zinarindima nje ya choo akajua kimenuka tayari. Akatoka mkukumkuku nje ya choo huku mkononi ameshika bastola yake.
Ile kutokeza tu nje akakutana na mdomo wa bastola, "tupa chini bastola yako, la sivyo nitasambaratisha ubongo wako sasa hivi" alisema kwa ukali Kachero Manu akiwa amemnyooshea mdomo wa bastola. Yule jamaa akaitupa chini bila ubishi na akanyoosha mikono juu. Kosa alilofanya Kachero Manu ni kutaka kuchungulia chooni kuangalia usalama wa kijana wa 'Chops CarWash'. Jamaa alionekana mzoefu wa kazi, akamshambulia kwa kurusha teke na kufanikiwa kudondosha bastola ile wakapanga mikono sasa watifuane vilivyo.
Kachero Manu alitaka pambano liishe raundi ya kwanza, akarusha teke moja la ubavuni ambalo uzito wake kama Mwalimu Kashasha yule mchambuzi wa Michezo "TBC-FM" angeliona kasi yake angethibitisha kuwa lina uwezo wa kuchana mifupa ya mbavu vipande vidogo vidogo. Tahamaki jamaa alichofanya ni kukaza mifupa ya mbavuni teke likadunda kama kitenesi.
Haraka haraka akabadili mbinu, akaamua sasa atakuwa anampiga kwa kumdokoa kwa lengo la kumchosha kama mbinu ya bondia bingwa nguli duniani kupata kutokea katika historia ya masumbwi, Mohamedi Alli. Mbinu hiyo ilifanya kazi na kuleta tija haraka baada ya muda mfupi jicho la kushoto na la kulia la yule mjuba yakaanza kuvuja damu, huku midomo yake yote miwili imepasuka haina hali. Jamaa akawa amepandwa na hasira akaja kumvamia Kachero Manu na kumbeba jumla jumla na kumtupa chini, mtupo ambao Kachero Manu alianguka kichwangomba kwa kugongeshwa kwenye ukuta.
Haraka haraka akajizoa pale sakafuni na kusimama. Yule adui akawa anacheka kicheko cha dharau cha kikwakwa huku meno yake ya susa yenye uchafu wa moshi wa sigara ukijionyesha dhahiri shahiri. Kachero Manu akameza mate machungu ingawa alikuwa kwenye maumivu makali. Akaamua ambadilishie mbinu za mapigano, jamaa ikawa akirusha ngumi anazikwepa halafu anamtandika chembe kidevu mbili za dabodabo.
Jamaa akaishiwa mbinu akabaki kutegemea maguvu yake, akaja kwa kasi na kumzoa tena Kachero Manu kwa kuikamata miguu yake kwa pamoja na kumnyanyua tena akiwa na lengo la kwenda kumbamiza kwenye ukuta. Alichofanya Kachero Manu nikukusanya nguvu na kumpiga kichwa cha katikati ya kichwa kwenye kidazi. Mbinu ambayo ilisaidia sana damu zikaanza kumchuruzika kwenye upara wake yule adui akaanza kuyumba kama mlevi, huku anaona kisunzi.
Usifanye mchezo na kichwa cha Komandoo wewe, kina nguvu zaidi ya jiwe fatuma. Kachero Manu kila akiona damu ndio mori wake unapanda, marshimarshi akaanza kumshambulia kwa kasi kwa mateke na mangumi baada ya sekunde kama 40 adui akawa ameshapiga dafrao yupo chini anatapatapa, huku kwenye suruali yake ameshajiachia ngama na mkojo. Akaifuata bastola yake na kumuwekea mtutu wake sikioni huku amemkandamiza goti lake kifuani mwake.
"Chiiifu Chiiifu nisamehee Chiifu..." aliomba msamaha yule adui. "Nani kakutuma uje umteke huyu kijana"?, tamaa Chiiifu, imeniponza nisamehe... Chiifu" alikuwa anaongea kwa takilifu mjuba yule. Gari za polisi zikawa zinasikika kwa mbali zinakuja eneo la tukio, maana ile milio ya risasi kule chooni ilisababisha mkukumkuku miongoni mwa wahudumu na wateja wao. Paka wa baa kwao ikawa ganda la muwa la jana chungu kaona kivuno, wanajisosomola kuku choma na mishikaki iliyotelekezwa na wateja mezani wanaokikwepa kifo.
Kachero Manu akakimbilia chooni na kumkuta yule kijana anatapatapa kwenye dimbwi la damu, huku kisu kimechomekwa ubavuni mwake, kisu ambacho kiliroromoa donda kubwa ubavuni mwake. Yule kijana alipomuona tu Kachero Manu akaanza kuongea kwa tabu huku analalamika,"Menejaaa.....ana...niuaaa....ana.... sem....aaa nime.....ku.... paa siriiiii". Haraka haraka Kachero Manu akapiga simu ya dharura waje wamchukue wamkimbize hospitalini kuokoa maisha yake.
Alipotoka nje ya choo tu akamkuta yule jamaa aliyepambana nae amezimia. Akapishana nao wana usalama wanaingia yeye ndio anaondoka na gari yake, huku akimpigia simu Kachero Yasmine kuhakikisha usiku huu wanamtia mbaroni mmiliki wa "Chops CarWash & Garage" na Meneja wake, ambao ni Baba na Mwana, ili wasaidie upelelezi wa kubaini wahusika wa mauaji ya Wabunge na dereva wao.

Mipango ya mauaji ya Wabunge namna ilivyotekelezwa ndani ya "Chops Carwash & Garage"
Mzee Hafeedh Abdullah mmiliki wa "Chops Carwash & Garage" akiwa ni mkandarasi mwenye vitega uchumi mbalimbali Afrika Mashariki na Kati, alikuwa pia ndio mfadhili mkuu wa ugaidi kwenye ukanda huo. Baada ya kutungwa kwa sheria ya ugaidi mwaka 2002 Bungeni, alichukizwa na sheria hiyo akiita kuwa ni ya ukandamizaji. Akaweka nia ya dhati ya kulipiza kisasi kwa Wabunge, waliopitisha sheria hiyo. Hivyo akanunua baadhi ya maeneo jirani na hapo Bungeni kwa kutumia majina tofauti tofauti.
Ilivyokuja mipango hii mipya kutoka "Al-shabaab" ya kuipa shinikizo serikali ya Tanzania wafunge balozi yao nchini Kenya ndio akaanzisha gereji na sehemu ya kuoshea magari inayoendana na hadhi ya Waheshimiwa. Mbaya zaidi viongozi wetu wengi hawapo makini kwenye kuchunga usalama wao. Dereva anapewa jukumu la kupeleka gereji anayoijua yeye na sehemu ya kuoshea magari anapopataka dereva, wanakula katika migahawa ya mitaani bila kuchunga usalama wao.
Mpango wa kwanza wa kutekeleza mauaji ya Wabunge kupitia kemikali ya kwenye vibomba vya kutawadhia hotelini ulivyobumburushwa na Kachero Manu, haraka haraka ukapangwa mkakati namba mbili wa kuwaua kupitia magari yao. Mauaji yalipangwa yafanyike siku ya ijumaa, siku hiyo hiyo ya hitimisho la maombolezo ya kitaifa hasa baada ya Tanzania kupuuza vitisho vya Al-shabaab" vya kupewa wiki moja watekeleze vinginevyo wataleta maafa tena.
"Maso Maso" baada ya kufanikiwa kuwapiga chenga ya mwili wana usalama kule hotelini, Dodoma akapata hifadhi nyumbani kwa Bwana Hafeedh Abdallah, ambaye ndio mfadhili wake wa masomoni kule Uingereza. Miaka ya karibuni Bwana Hafeedh Abdallah alikuwa anapatikana sana Jijini Dodoma hasa baada ya serikali kuhamia huko. Yeye shughuli zake za ukandarasi asilimia 85% zilikuwa zinategemea tenda za magumashi toka kwa watumishi wala rushwa wa serikalini.
"Sasa utatekelezaje hayo mauaji kijana wangu "Maso Maso" maana si unajua sasa Wabunge wanalindwa ile mbaya baada ya siri zetu kuvuja kwenye vyombo vya usalama? " alikuwa Mzee Hafeedh Abdallah anamsaili 'Maso Square The Duduman' ili asije kufanya kosa litakalowagharimu. "Unajua nimepanga kuwawekea sumu kwenye magari yao, sumu ambayo baada ya kuanzia nusu saa mpaka lisaa limoja baada ya kuvuta hiyo sumu inaleta madhara unakufa mara moja", alieleza "Maso Maso". "Utawekaje sasa hizo sumu si unajua magari ya vigogo hao yanachungwa sana" alizidi kudadisi Mzee Hafeedh, alitaka atolewe wasiwasi usioacha mashaka.
"Teh teh teh teh..labda nchi zingine sio Tanzania, nchi hii unakuta Hakimu kawahukumu majambazi kifungo cha miaka 30 jela halafu bado anaishi uswahilini, na jioni atakuja baa kupata kilaji. Ndio maana zamani enzi za mkoloni viongozi walikuwa wana maeneo yao maalumu ya kuishi yanayolindwa, wana sehemu zao maalumu za kustarehe ndio maana kulikuwa na ile 'Leaders Club' pale Dar es Salaam, lakini sasa mambo yanaenda shaghalabagala ukitaka kuleta madhara kwa kiongozi ni dakika sifuri tu" alizungumza "Maso Maso" kwa majigambo na kujitapa kuonyesha anaijua kazi yake ya ugaidi nje ndani.
"Sasa nimepanga kuweka sumu kupitia mfumo wa kipoza hewa wa gari. Nitakachofanya magari ya waheshimiwa yakifika kuoshwa nitafungua A/C Filter kisha naweka kemikali yangu ambayo wakiwasha kiyoyozi tu baada ya lisaa limoja dereva na kigogo wake wanapokelewa akhera leo hii, wataivuta hiyo kemikali sumu wakati hewa baridi inapuliza kiyoyozi ndani ya gari lao" alimaliza maelezo yake marefu yaliyomkinaisha na kukata kiu yake kibopa Hafeedh Abdallah, hivyo akapitisha mkakati huu.
Ndio ikapangwa siku ya Ijumaa wafanyakazi wa gereji na wote wanaohusika na 'Carwash' waambiwe wasije kazini, ili kumpa fursa "Maso Maso" apige kazi yake ya mwisho kuiadabisha Tanzania kisha wote watoroke kwenda kujificha huko mafichoni. Mzee Hafeedh Abdallah tayari alishaacha vitega uchumi vya siri vingi kwa majina ya watu tofauti tofauti ili kuificha serikali isikamate mali zake. Hivyo alikuwa na uhakika wa kuishi mafichoni mpaka kifo chake bila shida yoyote ya pesa.
Baada ya Kachero Manu na Kachero Yasmine kupewa taarifa ya msiba wa Wabunge hao, na Mkuu wao wa kazi, Bwana Omega Mtanika, ikawabidi wakimbilie hospitali ya mkoa ya Dodoma "General" kuangalia miili ya wahanga. Walikuta umati wa wakazi wa Jiji la Dodoma wamefurika mochwari ya Dodoma. Uvumi mitaani ulienea magari zaidi ya magari 10 yamegongana na kusababisha vifo vya mamia ya watu. Hawakujua kama kuna ugaidi ndani ya tukio hilo.
Bahati na ngekewa ilikuwa upande wake Kachero Manu, kuna dereva mmoja wa mmoja wa Wabunge wale alikuwa bado yupo hai ila yupo kwenye hali mbaya, anapitia sakaratu mauti. Hizo taarifa alizipata toka kwa Mganga Mkuu Mfawidhi wa hospitali walipoenda kuhojiana nae.
Kachero Manu alikesha chumba cha wagonjwa mahututi, "Intensive Care Unit"- (I. C. U) akimsubiria dereva huyo apate nafuu huenda akaambulia chochote kitu. Mishale ya saa tisa usiku uvumilivu wake ulilipa, kama wanavyosema mvumilivu hula mbivu, yule dereva alipata nafuu kidogo na alifanikiwa kueleza sehemu ya mwisho waliyopitia kabla ya tukio ni 'Chops Carwash'. Lakini baadae hali ilibadilika akaaga dunia. Ila alichoshukuru Kachero Manu ni kupata sehemu ya kuanzia upelelezi wake.

SURA YA KUMI NA MOJA
Mke wa Kachero Manu mikononi mwa magaidi
Siku ya Jumatatu, Kachero Manu aliamka majira ya saa tatu asubuhi akiwa buheri wa afya. Kwa wiki nzima iliyopita alikuwa hajapata utulivu wa maana wa kupumzisha mwili na nafsi, mpaka Jumapili usiku akaamua akalale nyumbani kwa mkewe Bi.Faith Magayane. Mamsapu wake alikuwa anaishi maeneo ya karibu na Viwanja vya Maonyesho ya Nane Nane-Nzuguni katika nyumba ya kupangisha yenye chumba tatu, jiko na sebule. Ilikuwa ni nyumba inayoendana na hadhi yake kama mtumishi wa umma katika sekta binafsi.
Alipoamka usingizini Kachero Manu alikuta tayari mkewe kashang'oa nanga kuelekea kibaruani kwake. Usiku walikesha na mkewe wanapeana michapo ya hapa na pale ya matukio mbalimbali, mpaka mechi za Wanandoa wakacheza, mwishowe wakajikuta wamelala mishale mibaya. Alipoamka kitandani alikwenda kwanza kunawa uso na kusafisha meno yake, kisha akafanya mazoezi binafsi ya viungo kama muda wa robo saa, kisha akaenda kuoga, akavaa vizuri na kuelekea mesini.
Hapo alikuta tayari kashatayarishiwa kifungua kinywa na mkewe. Alikuta kuna sahani ya matunda mchanganyiko iliyofunikwa na kawa yenye maandishi ya kimahaba. Pia akakuta hotipoti limejaa kande za mahindi mabichi na chai nzito ya maziwa kwenye chupa kubwa. Bila kufanya ajizi akaanza kujichana vilivyo, alimaliza akaenda kuosha vyombo jikoni kisha akawa anajiandaa kuondoka zake.
Akiwa anajiandaa kufunga mlango wa nyumba simu yake ya mkononi ikaanza kuita. Akaichomoa simu kuangalia akaona ni namba ngeni kwake akaipokea. "Hellow....unazungumza na Afisa Rasilimali Watu kutoka Benki ya KCB-Dodoma naitwa 'Martin Hoseah', nadhani nazungumza na mume wa mfanyakazi mwenzetu 'Faith Magayane'?". Mapigo ya moyo ya Kachero Manu yakalipuka na kupatwa na ususuavu wa moyo. Akaanza kujiuliza, "mke wangu kafariki, katekwa au kapata ajali,? mbona sijawahi kupigiwa simu toka kazini kwake hata siku moja,?" aliwaza Kachero Manu mpaka akajisahau hajatoa majibu ya swali aliloulizwa.
"Hellow.. Hellow.." yule Afisa alipoona hamna majibu akakata simu yake. Baada ya sekunde kadhaa kupita akaanza kupiga upya, Kachero Manu akakurupuka kama katoka ndotoni na kuipokea. Yule Afisa akaeleza anachokikusudia. "Samahani mkeo hajafika kazini mpaka sasa na hapatikani kwenye simu yake ya mkononi na hatuna taarifa zake zozote mpaka sasa hivi tunavyoongea". "My God, amepatwa na maswahibu gani tena, maana nyumbani kadamka asubuhi na mapema kuja huko kazini! labda tusubirie Kwanza tutaendelea kujuzana" alijibu Kachero Manu, wakaagana kwa maafikiano ya kupeana taarifa ya juu kinachoendelea katika sakata hilo la kupotea kwa mkewe.
Baada ya simu kukatwa ikabidi arudi kukaa sebuleni kwenye sofa na kuanza kutafakari kitu cha kufanya. "Nini kimempata mahabubu wangu Faith!, mbona tumelala raha mustarehe na asali tumelambishana mpaka usiku wa manane, tena mechi ya patashika nguo kuchanika!. Hajaniambia lolote kama kuna mbaya wake labda anamuwinda kwa kisasi. Itakuwa labda amepata ajali au kifo inabidi sasa hivi nielekee hospitali ya Mkoa kabla sijaendelea na chochote mkururu wa fikra ulikuwa unasafiri katika kichwa cha Kachero Manu.
Akaamua na yeye kujaribu kuipiga simu ya mkewe kupitia namba zake mbalimbali alizo nazo kwenye simu yake zote zikawa hazileti majibu yoyote zaidi ya lile jibu pendwa la simu iliyozimwa la kuwa “mtumiaji wa simu uliyempigia hapatikani jaribu tena baadae. Akajaribu kupiga kwa baadhi ya marafiki zake, nao hawakuwa na majibu ya kueleweka zaidi ya paukwa pakawa. Hakutaka kabisa kuwapigia ndugu na wazazi wa mkewe kuogopa wasijepatwa na taharuki juu ya uhai wa mtoto wao, na kuharibu uchunguzi wote.
"Lazima nipite Hospitali ya Mkoa kwanza kuulizia, vinginevyo nitaharibu kazi za watu bure kama sitofahamu usalama wa mke wangu kwanza" alijisemea mwenyewe wakati anajiandaa kutoka nyumbani. Akafunga mlango wa nyumba yao na kisha kupanda ndani ya gari lake ili aondoke zake kwenda hospitali ya Mkoa, akaanze kuhemea taarifa za mkewe kama zipo. Akiwa ameshaweka funguo kwenye swichi ya gari ili awashe aondoke zake, akaisikia simu yake inaita tena. Sasa hivi akafanya pupa kuichomoa kiunoni alijua labda ni mkewe Faith anapiga kumtoa wasiwasi juu ya usalama wake au labda ni yule Afisa Uajiri wa Benki ya KCB amepata taarifa mpya. Kuangalia akaona ni namba ya kachero Yasmine, akaipokea.
"Hellow...Bosi habari yako natumaini umeamka salama salimini wa afya, huyu Kareem Abdallah Meneja wa "Chops Carwash & Garage" tayari nilishamtia mbaroni toka saa sita usiku kama ulivyoagiza nifanye hivyo ila baba yake mzazi ametuachia manyoya hajulikani alipo, na vijana wangu wa kazi wanasema kuna dalili ameshatoroka maana hajaonekana popote pale kwenye viwanja vyake vya kujivinjari. Huyu mtoto wake tutazaa nae tupo nae huku chimbo letu kijiji cha Zuzu hapa hapa Dodoma mpaka sasa hajatoa ushirikiano wowote" alimaliza maelezo yake Kachero Yasmine kwa mkuu wake wa kazi.
"Good job..sasa mie nitakuja huko baada ya saa mbili kuona tunafanyaje, maana huyo ndio kabeba ramani nzima ya magaidi wa "Al-shabaab" yaliyosababishwa na gereji yake" akamalizia maongezi Kachero Manu wakaagana zao.
Hakutaka kumpa hiyo taarifa ya kupotea mkewe Kachero Yasmine aliogopa atamchanganya na kumpotezea umakini. Saa tano kamili asubuhi akawa ndio anawasili kwenye maegesho ya Hospitali ya Mkoa ya Dodoma kuangalia uwezekano wa kumpata mkewe akiwa mgonjwa au marehemu.

Kareem Abdullah, Meneja wa kampuni ya "Chops Carwash & Garage" mpaka sasa alikuwa ametumikia saa 12 akiwa ametimbika na kupigika vilivyo katika kituo cha siri cha kuwahoji watuhumiwa wa ugaidi. Baba yake mzazi alishatorokea mafichoni kwenda kujichimbia kusikojulikana.
Kituo hiko kilikuwa kipo katika barabara ya kuelekea kijiji cha Zuzu, katika jengo la zamani la NMC "National Milling Company" Kufika kilipo hiko kituo ilitakiwa uifuate barabara ya kuelekea Arusha (Arusha Road) kama unatokea katikati ya Jiji la Dodoma kisha unakata kushoto kuifuata barabara ya Kizota. Utatakiwa uende barabara ya vumbi na changarawe kwa zaidi ya kilometa 35 ndipo utakapokikuta kituo hicho kikiwa kipo pembezoni kabisa mwa reli.
Kachero Yasmine na vijana wake wa kazi walimuwekea mtego nje ya nyumba yake Bwana Kareem Abdallah. Kwenye muda ya saa 6:15 usiku wakati anarejea nyumbani kwake. Wakamteka juu kwa juu na wala hakuleta ubishi wowote, hivyo wakamsafirisha usiku kwa usiku mpaka kwenye kituo chao walichokiteua kwa kazi hiyo maalumu.
Kituo kilikuwa na watu maalumu wa utesaji wanne wanaopokezana zamu masaa 12, wakiingia wawili wawili. Ukiwaona walikuwa ni kama mapacha jinsi wanavyofanana majumbile yao. Walikuwa warefu, weusi tii, wamejazia mwili wa kimazoezi huku vifua vyao vikiwa ni vipana vimetengeneza mikato mikato kutokana na ubebaji wa vitu vizito na milo bora inayonawirisha miji yao hiyo. Sura zao zilikuwa zinatisha hazina chembe ya upendo wala huruma hata kidogo, huku macho yao daima yakiwa ni mekundu. Meno yao makubwa huku yakiwa yamejivika ukungu kutokana na uwingi wa idadi ya sigara wanazovuta kwa siku.
Kareem Abdallah Meneja na mtoto wa mmiliki wa 'Chops Carwash & Garage' alivyobwagwa kituoni hapo na Kachero Yasmine alipokelewa na hao wazee wa kazi. Ambao kwanza walimgombania kama mpira wa kona unavyogombaniwa na wachezaji wote wa timu mbili pinzani. Tahamaki baada ya dakika kama 10 tu alikuwa hatamaniki usoni kwa idadi ya manundu na mipasuko. Ghafla akapata umbile la macho ya chawa kama ya Wachina. Kisha baada ya hapo akawekwa kwenye kiti cha umeme halafu unawashwa umeme anapigwa shoti za umeme mpaka akazimia.
Akapewa huduma ya kwanza alipozinduka akawekwa kwenye chumba kilichofunguliwa muziki kama wa disko la mitaani, muziki ambao umefunguliwa mpaka sauti ya juu, wakamfungia humo. Hapo tena akakesha mkesha wa lazima bila kupenda mpaka kulipokucha.
Ilipofika saa mbili asubuhi akaletwa mbele ya Kachero Yasmine kwa ajili ya mahojiano. "Swali langu ni moja tu, yuko wapi mfanyakazi wako wa gereji aliyefanya kazi siku ya Ijumaa na kutokomea kusipojulikana"? aliuliza Kachero Yasmine mara baada ya Meneja huyo mhalifu kuletwa mbele yake. "Simfahamu mie ni Meneja tu, kila kitu mhusika ni mmiliki, nadhani mkimpata yeye mtapata majibu kamili" alijibu kiujeuri akionekana kuwa ni mnyonge kuonyesha amechoshwa na mateso ya usiku.
 
Back
Top Bottom