Shupavu
JF-Expert Member
- Apr 23, 2015
- 371
- 525
RIWAYA: MSAKO WA MWEHU
MTUNZI: Badi .M. Bao
MWASILIANO. 0625920847, ( whatsap )
E- mail: badi.bao11@gmail.com
Dar es Salaam
SEHEMU YA KWANZA
SURA YA KWANZA
Idara ya magonjwa ya akili, Hospitali ya Taifa Muhimbili
Gangaganga ya mganga humwacha mgonjwa na matumaini, jitihada ya kutatua tatizo humpa mwenye tatizo tumaini. Bi Mwantumu Haji alikuwa amepatwa na maswahibu ya ulimwengu. Tatizo lililompata alijiona kama kaibeba dunia nzima mgongoni mwake. Ilikuwa ni majira ya saa tatu za asubuhi tulivu, iliyopambwa na mwangaza usioumiza wa jua ambalo lilikuwa tayari limeshachomoza upande wake wa mashariki, Bibi huyo alikuwa amekaa kwenye kiti na baadhi ya watu wengine akisubiria kuingia kwenye chumba cha daktari kilichopo kwenye bloku la hospitali ya Muhimbili, idara ya magonjwa ya akili.
Uso wake tu ukimuangalia ulionyesha ana jambo limemsibu, kwani daima dumu barua ya moyo husomwa juu ya panda la uso la mtu. Mtu akiwa na hali ya furaha au huzuni yote husomeka kwenye uso wake. Alikuwa amewasili katika hospitali ya taifa ya Muhimbili tokea muda wa jogoo la kwanza kuwika akimleta mtoto wake wa kiume anayeitwa "Masoud Masoud" maarufu kwa jina la Maso Maso” aliyerukwa na akili usiku huo wa manane uliopita.
Naam "Maso Maso" sasa kawa kichaa, mwehu, mwendawazimu, majinuni, akili zake zimetadathali, vyovyote utakavyopenda kutamka, lakini "Maso Maso" sasa akili zake ni maji kupwa na maji kujaa. Mgonjwa huyo alilazwa katika wodi ya wagonjwa wa afya ya akili katika Hospitali Taifa ya Muhimbili.
Mara ikasikika sauti toka kwenye kipaza sauti cha mhudumu wa zamu, mgonjwa mwenye kadi namba 10 aelekee kwa daktari chumba namba 02. Lilikuwa ni tangazo lililoleta faraja kwenye moyo wa Bi Mwantumu hasa ukichukulia yupo hapo hospitalini kwa zaidi ya saa sita tokea saa tisa za usiku na sasa saa tatu na dakika saba za asubuhi ndio anapata nafasi ya dhahabu aliyokuwa anaisubiria kwa hamu ya kuonana na daktari.
Bila simile, Bi. Mwantumu na uzee wake wa miaka 65 akajinyanyua kwa tabu pale kitini pake alipokuwa amejipweteka na kuingia kwenye chumba cha daktari bingwa wa Afya na Magonjwa ya Akili wa Hospitali ya Taifa Muhimbili. Alipokelewa kwa uso wa bashasha na tabasamu toka kwa Dokta "Alshad Mpenumbe". Alikuwa ni daktari wa hospitali hiyo mwenye uzoefu wa zaidi ya miaka 20 sasa, na umri wake alikuwa ndio anaingia kwenye rika la uzee wa makamo, wa miaka 55.
Karibu sana mama yangu, na pole na matatizo yalikuwa ni makaribisho ya Dokta Mpenumbe kwa Bi Mwantumu. Ahsante mwanangu nimeshapoa, matatizo tumeumbiwa wanadamu hatuna budi kuyapokea na kuyakabili kwa subira na stahamala kubwa alijibu kwa unyenyekevu Bi Mwantumu huku akijiweka vizuri kitini. Samahani naomba hiyo kadi yako alisema Dokta Mpenumbe. Bi Mwantumu akajibu kwa vitendo kwa kunyoosha mkono wake wa kulia kuikabidhi kadi kwa daktari apate kuisoma.
Ukapita muda kama wa rakaateni, muda ambao Dokta Mpenumbe alikuwa ametingwa na kuandika andika kwenye kompyuta yake ya mezani kisha, akamaliza akavua miwani yake akaiweka pembezoni mwa kompyuta yake, akaitoa hanchifu yake nyeupe kutoka kwenye koti lake jeupe alilovaa, akajifuta kwenye macho akajikohoza kidogo kulisafisha koo lake na kuanza mazungumzo na Bi Mwantumu.
Daktari: “Eheemwanao Masoud hili tatizo lake la akili limemuanza lini"?. Lilikuwa ni swali lililovunja ukimya uliopita baina yao kwa dakika kadhaa.
Bi Mwantumu: "Jana kuanzia saa mbili usiku alikuwa anazungumza mambo mchafukoge mara anasema kuna watu wapo nje ya nyumba wamekuja kumchukua. Wakati mwingine anasema amepigiwa simu na Rais kuwa ameteuliwa kuwa Mkuu wa Mkoa. Ila ilipofika saa sita usiku, ndio akaanza kufanya fujo na kuvunja vitu vya ndani anataka tumruhusu atoke nje ya nyumba."
Daktari: "Kwenye ukoo wenu au familia yenu ameshawahi kutokea mgonjwa wa afya ya akili"? Bi Mwantumu: "Billahi wa Rasuli hakuna mtu huyo kwenye ukoo wetu, sio upande wangu wala upande wa marehemu mume wangu." alitoa kiapo kwa kutumia kidole chake cha shahada kukwangua juu ya koo lake kuweka msisitizo wa maneno yake.
Daktari: "Mwanao, ni Mwanachuo au Muajiriwa?"
Bi Mwantumu: "Mwanangu amemaliza Chuo mwaka juzi, Shahada ya Uhandisi huko nchini Uingereza, na mwaka huo huo akapata kismati cha kazi nchini Saudi-Arabia, lakini akaacha ghafla kazi, sasa ana miezi kama 6 yupo tu nyumbani, na wala hajatuambia kilichomsibu huko alipokuwa mpaka akaacha kazi."
Daktari: "Je mwanao, ni mtu wa kujichanganya na marafiki na je ameoa au kuwa na rafiki wa kike?"
Bi Mwantumu: "Zamani kabla hajasafiri kwenda masomoni Uingereza alikuwa mtu wa watu, mpenda marafiki. Nyumbani kwangu walikuwa hawakauki marafiki zake kama maji ya kisima, lakini tokea arejee masomoni akawa ni mtu wa kujitenga tu, hana marafiki na hata sijawahi kusikia wala kumuona yupo na rafiki wa kike tokea amebaleghe. Na nimemzaa akiwa ni mzima wa afya jogoo linapanda mtungi"
Daktari: (Akatabasamu kwa jibu la Bi Mwantumu akifurahishwa na msisitizo aliouonyesha kuthibitisha mtoto wake sio hanithi). "Sasa mama yangu, vipimo vya maabara vimerudi, mtoto wako hana malaria wala ugonjwa wowote ule. Maana mwanzoni nilihisi huenda malaria yamepanda kichwani, lakini hana malaria. Kutokana na maelezo yako, mtoto wako ana ugonjwa wa akili kitaalamu tunauita Schizophrenia. Huu ni miongoni mwa magonjwa makubwa ya akili. Jina hilo limetoholewa kutoka katika lugha ya Kilatini ambayo ni maneno mawili "Schizo" na "Phrenia". Mgonjwa anayeugua ugonjwa huo anakosa muunganiko kati yake na akili yake", akaweka kituo kidogo cha maelezo yake Dokta Mpenumbe kwa kumeza mate kisha akaendelea kuelezea.
"Kwa kawaida binadamu huwa na hisia tano muhimu, ambazo ni za kuona, kugusa, kuonja, kusikia na kunusa. Mtu aliyechanganyikiwa kutokana na ugonjwa huu anaweza kuona, kuhisi, kunusa, kugusa au kusikia vitu ambavyo wengine hawaoni, kuhisi wala kusikia. Mgonjwa anaweza kusema anaona simba anapita eneo ambalo mmekaa naye, lakini nyie msimuone au anasikia sauti na watu wanazungumza habari zake, wanamshurutisha au wanamtisha lakini nyie hamuoni wala hamsikii chochote". Machozi yalikuwa yanamchuruzika churururu bila kikomo Bi Mwantumu pindi alipokuwa anasikiliza maelezo ya daktari kwa umakini mkubwa.
Bi Mwantumu: "Sasa kitinda mimba wangu kweli atapona daktari"? Nieleze ukweli usinifiche kitu kabisa" alikatisha mazungumzo ya daktari kwa kuuliza swali kisha akaanza kutoa kilio cha sauti ya uchungu.
Daktari: "Mama, huwa tunatumia njia tatu kuwatibu wagonjwa wa akili ambazo ni za kibaiolojia, kisaikolojia na kijamii. Hivyo shaka ondoa mama yangu"
Bi Mwantumu: "Nashukuru sana Daktari, Mwenyezi Mungu akubariki na kukupa afya uendelee kutupa huduma wahitaji".
Daktari: "Sawa, mama yangu, tutajuzana kinachoendelea. Tutamlaza kwa siku kadhaa ili tuzidi kuangalia maendeleo yake".
Bi Mwatumu akanyanyuka na kutoka nje ya ofisi ya Daktari. Akaelekea kwa keshia kwenda kufuatilia bili yake ya matibabu ya mwana wake ili apate kufanya malipo.
"Mimi ndio "Maso Maso" msela toka Sinza kwa wajanja. Nyie Watanzania maboya tu, unakuta Mbunge anakuhonga buku tano umpigie kura, halafu unamchagua kwa miaka mitano, maana yake kila mwaka mmoja amekununua kwa buku". Ha..... Ha.....Ha.....Ha.......mazwazwa sana nyie watu tembeeni duniani mfunguke akili. Kutwa mnashindia "chips-dume" na maji, maziwa kwa watoto wenu hawanywi mpaka wanywe sumu, tokea wakiwa shule ya vidudu akili za kugundua ndege na magari kama wazungu mtapata wapi sasa, wakati watoto wa wenzenu Ulaya wanashiba baga kwa maziwa. Viongozi wenu nao ni janga la kitaifa, watoto wao wanawasomesha shule za kuzungumza "Yes... Yes.. Mzungu kala mafenesi" mpaka anamaliza chuo kikuu huko Ulaya mtoto kagharimu milioni mia tatu.
Afu anarudi 'Bongoland' kugombania ajira na watoto wa akina yahe waliosoma shule za kata. Ambao gharama zao mpaka chuo kikuu haifiki hata milioni moja. Hizo akili au matope!. Ukiwekeza kwa mtoto wako milioni mia tatu, basi muandalie mazingira ya kuja kuendeleza kampuni zako za mabilioni na sio kuja kuajiriwa kwa kamshahara cha laki nne na watoto wa walalahoi". Ha.... ha.... ha... ha.... sogeeni hapa mpate elimu kitaa bure, mupate rai tumbitumbi zenye mafundisho.
Wakulima wenu nao majanga tupu, shamba lake, mbegu za kwake, kupanda, palizi zote kwa gharama zake lakini akivuna mazao yake, serikali inaanza kumpangia sijui Ooh...usiuze nje ya nchi, huo ni unyonyaji mbona Wafanyabiashara hamuwazuii kuuza bidhaa zao nje ya nchi, mbona watumishi wa umma hamuwapangii matumizi ya ndururu zao za mwezi!.
Ningekuwa Rais wa nchi wagonjwa nyie mngekula bata tu, sio viporo mnavyoletewa na ndugu zenu. Dripu zingekuwa za juisi na sio za maji kwani nyie mmekuwa samaki... Ha...Ha..Ha....Ha....! "
Wakati Masoud anaendelea kubwabwaja mbovu, akasikika nesi mmoja anamuongelesha mwenzake, "Huyo ndio Masoud bana akianza kumwaga sera hapo ni usiku kucha mtakesha nae na kuna wakati anaongea vitu vya msingi hata sisi wenye akili timamu hatuwezi kuviwaza".
"Afu nasikia kasomea Uingereza ana Shahada ya Uhandisi, labda karogwa maana familia zetu za kiswahili nazo ni shida, wana roho ya tukose wote. Wanapenda wote tufanane hali zetu za maisha, wote tuwe wali deni mchuzi karadha. Babu dobi, Baba muuza kahawa, Mjomba fundi seremala, Shangazi kazi yake mchambaji kwenye "kitchen party", Mama mchoma vitumbua, hivyo ndivyo wanavyotaka. Akitokea mmoja tu anataka kujifanya msomi msomi wataanza kumpiga tunguri mpaka atakoma", nesi mwenzake nae alichangia kusherehesha mazungumzo yao.
"Madame Neesi eeh....Madame Neeesi....!, Nataka kwenda chooni kujisaidia, au nijisaidie hapa hapa wodini, mie sioni noma fumbeni macho tu nimtoe nyoka pangoni hadharani" ilikuwa ni sauti ya Masoud, alikatiza mazungumzo yao waliyokuwa wanateta wale manesi mawili.
"Aaaah.... hapana rafiki yangu Masoud usifanye hivyo, nenda chooni bana, tena leo simuiti mlinzi akusindikize nenda mwenyewe na urudi haraka rafiki" alisema nesi yule akimrai Masoud asijisaidie ndani ya wodi hiyo ya wagonjwa akili. Masoud alikuwa tayari ameanza kufungua mkanda wa suruali yake akitishia kujisaidia tayari.
Masoud akaondoka zake wodini kuelekea chooni kwa mwendo wa chapuchapu. Muda ulikuwa ni saa nne za usiku. Hiyo ndio ikawa ni kwaheri ya kuonana, kama vile kawapa mkono wa buriani, hawakumuona tena. Kwa ufupi Masoud alikuwa ametorokea mtaani kusikojulikana, alichoka maisha ya kufungiwa wodini kama ndege tunduni.
ITAENDELEA
MTUNZI: Badi .M. Bao
MWASILIANO. 0625920847, ( whatsap )
E- mail: badi.bao11@gmail.com
Dar es Salaam
SEHEMU YA KWANZA
SURA YA KWANZA
Idara ya magonjwa ya akili, Hospitali ya Taifa Muhimbili
Gangaganga ya mganga humwacha mgonjwa na matumaini, jitihada ya kutatua tatizo humpa mwenye tatizo tumaini. Bi Mwantumu Haji alikuwa amepatwa na maswahibu ya ulimwengu. Tatizo lililompata alijiona kama kaibeba dunia nzima mgongoni mwake. Ilikuwa ni majira ya saa tatu za asubuhi tulivu, iliyopambwa na mwangaza usioumiza wa jua ambalo lilikuwa tayari limeshachomoza upande wake wa mashariki, Bibi huyo alikuwa amekaa kwenye kiti na baadhi ya watu wengine akisubiria kuingia kwenye chumba cha daktari kilichopo kwenye bloku la hospitali ya Muhimbili, idara ya magonjwa ya akili.
Uso wake tu ukimuangalia ulionyesha ana jambo limemsibu, kwani daima dumu barua ya moyo husomwa juu ya panda la uso la mtu. Mtu akiwa na hali ya furaha au huzuni yote husomeka kwenye uso wake. Alikuwa amewasili katika hospitali ya taifa ya Muhimbili tokea muda wa jogoo la kwanza kuwika akimleta mtoto wake wa kiume anayeitwa "Masoud Masoud" maarufu kwa jina la Maso Maso” aliyerukwa na akili usiku huo wa manane uliopita.
Naam "Maso Maso" sasa kawa kichaa, mwehu, mwendawazimu, majinuni, akili zake zimetadathali, vyovyote utakavyopenda kutamka, lakini "Maso Maso" sasa akili zake ni maji kupwa na maji kujaa. Mgonjwa huyo alilazwa katika wodi ya wagonjwa wa afya ya akili katika Hospitali Taifa ya Muhimbili.
Mara ikasikika sauti toka kwenye kipaza sauti cha mhudumu wa zamu, mgonjwa mwenye kadi namba 10 aelekee kwa daktari chumba namba 02. Lilikuwa ni tangazo lililoleta faraja kwenye moyo wa Bi Mwantumu hasa ukichukulia yupo hapo hospitalini kwa zaidi ya saa sita tokea saa tisa za usiku na sasa saa tatu na dakika saba za asubuhi ndio anapata nafasi ya dhahabu aliyokuwa anaisubiria kwa hamu ya kuonana na daktari.
Bila simile, Bi. Mwantumu na uzee wake wa miaka 65 akajinyanyua kwa tabu pale kitini pake alipokuwa amejipweteka na kuingia kwenye chumba cha daktari bingwa wa Afya na Magonjwa ya Akili wa Hospitali ya Taifa Muhimbili. Alipokelewa kwa uso wa bashasha na tabasamu toka kwa Dokta "Alshad Mpenumbe". Alikuwa ni daktari wa hospitali hiyo mwenye uzoefu wa zaidi ya miaka 20 sasa, na umri wake alikuwa ndio anaingia kwenye rika la uzee wa makamo, wa miaka 55.
Karibu sana mama yangu, na pole na matatizo yalikuwa ni makaribisho ya Dokta Mpenumbe kwa Bi Mwantumu. Ahsante mwanangu nimeshapoa, matatizo tumeumbiwa wanadamu hatuna budi kuyapokea na kuyakabili kwa subira na stahamala kubwa alijibu kwa unyenyekevu Bi Mwantumu huku akijiweka vizuri kitini. Samahani naomba hiyo kadi yako alisema Dokta Mpenumbe. Bi Mwantumu akajibu kwa vitendo kwa kunyoosha mkono wake wa kulia kuikabidhi kadi kwa daktari apate kuisoma.
Ukapita muda kama wa rakaateni, muda ambao Dokta Mpenumbe alikuwa ametingwa na kuandika andika kwenye kompyuta yake ya mezani kisha, akamaliza akavua miwani yake akaiweka pembezoni mwa kompyuta yake, akaitoa hanchifu yake nyeupe kutoka kwenye koti lake jeupe alilovaa, akajifuta kwenye macho akajikohoza kidogo kulisafisha koo lake na kuanza mazungumzo na Bi Mwantumu.
Daktari: “Eheemwanao Masoud hili tatizo lake la akili limemuanza lini"?. Lilikuwa ni swali lililovunja ukimya uliopita baina yao kwa dakika kadhaa.
Bi Mwantumu: "Jana kuanzia saa mbili usiku alikuwa anazungumza mambo mchafukoge mara anasema kuna watu wapo nje ya nyumba wamekuja kumchukua. Wakati mwingine anasema amepigiwa simu na Rais kuwa ameteuliwa kuwa Mkuu wa Mkoa. Ila ilipofika saa sita usiku, ndio akaanza kufanya fujo na kuvunja vitu vya ndani anataka tumruhusu atoke nje ya nyumba."
Daktari: "Kwenye ukoo wenu au familia yenu ameshawahi kutokea mgonjwa wa afya ya akili"? Bi Mwantumu: "Billahi wa Rasuli hakuna mtu huyo kwenye ukoo wetu, sio upande wangu wala upande wa marehemu mume wangu." alitoa kiapo kwa kutumia kidole chake cha shahada kukwangua juu ya koo lake kuweka msisitizo wa maneno yake.
Daktari: "Mwanao, ni Mwanachuo au Muajiriwa?"
Bi Mwantumu: "Mwanangu amemaliza Chuo mwaka juzi, Shahada ya Uhandisi huko nchini Uingereza, na mwaka huo huo akapata kismati cha kazi nchini Saudi-Arabia, lakini akaacha ghafla kazi, sasa ana miezi kama 6 yupo tu nyumbani, na wala hajatuambia kilichomsibu huko alipokuwa mpaka akaacha kazi."
Daktari: "Je mwanao, ni mtu wa kujichanganya na marafiki na je ameoa au kuwa na rafiki wa kike?"
Bi Mwantumu: "Zamani kabla hajasafiri kwenda masomoni Uingereza alikuwa mtu wa watu, mpenda marafiki. Nyumbani kwangu walikuwa hawakauki marafiki zake kama maji ya kisima, lakini tokea arejee masomoni akawa ni mtu wa kujitenga tu, hana marafiki na hata sijawahi kusikia wala kumuona yupo na rafiki wa kike tokea amebaleghe. Na nimemzaa akiwa ni mzima wa afya jogoo linapanda mtungi"
Daktari: (Akatabasamu kwa jibu la Bi Mwantumu akifurahishwa na msisitizo aliouonyesha kuthibitisha mtoto wake sio hanithi). "Sasa mama yangu, vipimo vya maabara vimerudi, mtoto wako hana malaria wala ugonjwa wowote ule. Maana mwanzoni nilihisi huenda malaria yamepanda kichwani, lakini hana malaria. Kutokana na maelezo yako, mtoto wako ana ugonjwa wa akili kitaalamu tunauita Schizophrenia. Huu ni miongoni mwa magonjwa makubwa ya akili. Jina hilo limetoholewa kutoka katika lugha ya Kilatini ambayo ni maneno mawili "Schizo" na "Phrenia". Mgonjwa anayeugua ugonjwa huo anakosa muunganiko kati yake na akili yake", akaweka kituo kidogo cha maelezo yake Dokta Mpenumbe kwa kumeza mate kisha akaendelea kuelezea.
"Kwa kawaida binadamu huwa na hisia tano muhimu, ambazo ni za kuona, kugusa, kuonja, kusikia na kunusa. Mtu aliyechanganyikiwa kutokana na ugonjwa huu anaweza kuona, kuhisi, kunusa, kugusa au kusikia vitu ambavyo wengine hawaoni, kuhisi wala kusikia. Mgonjwa anaweza kusema anaona simba anapita eneo ambalo mmekaa naye, lakini nyie msimuone au anasikia sauti na watu wanazungumza habari zake, wanamshurutisha au wanamtisha lakini nyie hamuoni wala hamsikii chochote". Machozi yalikuwa yanamchuruzika churururu bila kikomo Bi Mwantumu pindi alipokuwa anasikiliza maelezo ya daktari kwa umakini mkubwa.
Bi Mwantumu: "Sasa kitinda mimba wangu kweli atapona daktari"? Nieleze ukweli usinifiche kitu kabisa" alikatisha mazungumzo ya daktari kwa kuuliza swali kisha akaanza kutoa kilio cha sauti ya uchungu.
Daktari: "Mama, huwa tunatumia njia tatu kuwatibu wagonjwa wa akili ambazo ni za kibaiolojia, kisaikolojia na kijamii. Hivyo shaka ondoa mama yangu"
Bi Mwantumu: "Nashukuru sana Daktari, Mwenyezi Mungu akubariki na kukupa afya uendelee kutupa huduma wahitaji".
Daktari: "Sawa, mama yangu, tutajuzana kinachoendelea. Tutamlaza kwa siku kadhaa ili tuzidi kuangalia maendeleo yake".
Bi Mwatumu akanyanyuka na kutoka nje ya ofisi ya Daktari. Akaelekea kwa keshia kwenda kufuatilia bili yake ya matibabu ya mwana wake ili apate kufanya malipo.
"Mimi ndio "Maso Maso" msela toka Sinza kwa wajanja. Nyie Watanzania maboya tu, unakuta Mbunge anakuhonga buku tano umpigie kura, halafu unamchagua kwa miaka mitano, maana yake kila mwaka mmoja amekununua kwa buku". Ha..... Ha.....Ha.....Ha.......mazwazwa sana nyie watu tembeeni duniani mfunguke akili. Kutwa mnashindia "chips-dume" na maji, maziwa kwa watoto wenu hawanywi mpaka wanywe sumu, tokea wakiwa shule ya vidudu akili za kugundua ndege na magari kama wazungu mtapata wapi sasa, wakati watoto wa wenzenu Ulaya wanashiba baga kwa maziwa. Viongozi wenu nao ni janga la kitaifa, watoto wao wanawasomesha shule za kuzungumza "Yes... Yes.. Mzungu kala mafenesi" mpaka anamaliza chuo kikuu huko Ulaya mtoto kagharimu milioni mia tatu.
Afu anarudi 'Bongoland' kugombania ajira na watoto wa akina yahe waliosoma shule za kata. Ambao gharama zao mpaka chuo kikuu haifiki hata milioni moja. Hizo akili au matope!. Ukiwekeza kwa mtoto wako milioni mia tatu, basi muandalie mazingira ya kuja kuendeleza kampuni zako za mabilioni na sio kuja kuajiriwa kwa kamshahara cha laki nne na watoto wa walalahoi". Ha.... ha.... ha... ha.... sogeeni hapa mpate elimu kitaa bure, mupate rai tumbitumbi zenye mafundisho.
Wakulima wenu nao majanga tupu, shamba lake, mbegu za kwake, kupanda, palizi zote kwa gharama zake lakini akivuna mazao yake, serikali inaanza kumpangia sijui Ooh...usiuze nje ya nchi, huo ni unyonyaji mbona Wafanyabiashara hamuwazuii kuuza bidhaa zao nje ya nchi, mbona watumishi wa umma hamuwapangii matumizi ya ndururu zao za mwezi!.
Ningekuwa Rais wa nchi wagonjwa nyie mngekula bata tu, sio viporo mnavyoletewa na ndugu zenu. Dripu zingekuwa za juisi na sio za maji kwani nyie mmekuwa samaki... Ha...Ha..Ha....Ha....! "
Wakati Masoud anaendelea kubwabwaja mbovu, akasikika nesi mmoja anamuongelesha mwenzake, "Huyo ndio Masoud bana akianza kumwaga sera hapo ni usiku kucha mtakesha nae na kuna wakati anaongea vitu vya msingi hata sisi wenye akili timamu hatuwezi kuviwaza".
"Afu nasikia kasomea Uingereza ana Shahada ya Uhandisi, labda karogwa maana familia zetu za kiswahili nazo ni shida, wana roho ya tukose wote. Wanapenda wote tufanane hali zetu za maisha, wote tuwe wali deni mchuzi karadha. Babu dobi, Baba muuza kahawa, Mjomba fundi seremala, Shangazi kazi yake mchambaji kwenye "kitchen party", Mama mchoma vitumbua, hivyo ndivyo wanavyotaka. Akitokea mmoja tu anataka kujifanya msomi msomi wataanza kumpiga tunguri mpaka atakoma", nesi mwenzake nae alichangia kusherehesha mazungumzo yao.
"Madame Neesi eeh....Madame Neeesi....!, Nataka kwenda chooni kujisaidia, au nijisaidie hapa hapa wodini, mie sioni noma fumbeni macho tu nimtoe nyoka pangoni hadharani" ilikuwa ni sauti ya Masoud, alikatiza mazungumzo yao waliyokuwa wanateta wale manesi mawili.
"Aaaah.... hapana rafiki yangu Masoud usifanye hivyo, nenda chooni bana, tena leo simuiti mlinzi akusindikize nenda mwenyewe na urudi haraka rafiki" alisema nesi yule akimrai Masoud asijisaidie ndani ya wodi hiyo ya wagonjwa akili. Masoud alikuwa tayari ameanza kufungua mkanda wa suruali yake akitishia kujisaidia tayari.
Masoud akaondoka zake wodini kuelekea chooni kwa mwendo wa chapuchapu. Muda ulikuwa ni saa nne za usiku. Hiyo ndio ikawa ni kwaheri ya kuonana, kama vile kawapa mkono wa buriani, hawakumuona tena. Kwa ufupi Masoud alikuwa ametorokea mtaani kusikojulikana, alichoka maisha ya kufungiwa wodini kama ndege tunduni.
ITAENDELEA