Riwaya: Matanga ya rohoni

Riwaya: Matanga ya rohoni

Sehemu-37


Ujio wa Mr.Lorenzo ukawa ni neema kwa Mr.Martin Tenga, kutokana na Mr.Lorenzo kuletewa chakula kila wiki cha kupika toka nyumbani kwao. Hivyo wakawa wanashirikiana katika kupika kwa pamoja na kila kitu wakifanya kwa pamoja. Jambo usilolijua ni kama usiku wa giza, hawa maswahiba wapya wawili, Mr.Martin Tenga na Mr.Lorenzo walikuwa ni mtu na shemeji yake, kwa maana ya kwamba Mr.Martin amezaa mtoto na Recho ambaye ni dada wa damu wa Mr.Lorenzo. Mtoto mwenyewe wa Mr.Martin na Recho ndio huyu Pesambili ambaye anaishi nyumbani kwa Mr.Lorenzo.

Wakati Pesambili anasubiria kujiunga na masomo ya Chuo Kikuu baada ya kumaliza elimu ya kidato cha sita, akakabidhiwa na babu yake jukumu rasmi la kupeleka mahitaji ya baba mlezi wake, Mr.Lorenzo. Hapo ndio kwa mara ya kwanza tokea kuzaliwa kwake, Pesambili akaanza kuonana na baba yake mzazi uso kwa uso bila kutambuana.
[emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586]
Pesambili, tayari majibu yake ya mitihani ya kidato cha sita yalishatoka. Alifaulu kujiunga na masomo Utabibu katika Chuo Kikuu cha Turin, 'University of Turin', alikuwa anasubiria tu muhula mpya wa masomo uanze2 akaanze maisha mapya ya Chuo Kikuu. Alichaguliwa kujiunga na kitivo cha 'Medicine and Surgery' akiwa mmoja wa wanafunzi waliofanya vizuri zaidi katika mitihani ya kumaliza kidato cha 6. Pesambili alikuwa na furaha sana kufanikiwa lengo lake la kusomea Udaktari likiwa linakaribia kutimia.

Pesambili alikuwa na ndoto kubwa ya kuwa Daktari Bingwa wa Upasuaji, kutokana na huduma aliyopewa yeye utotoni ya upasuaji mpaka akaweza kutembea. Akaweka adhima na nia ya kuwa akiwa mkubwa nae atasomea Udaktari wa Binadamu ili nae aje kutoa huduma kwa wahitaji mbalimbali kama alivyosaidiwa yeye. Alipanga akimaliza Chuo Kikuu akafanye kazi katika nchi yoyote ya Afrika, hiyo ndio iwe sadaka yake kwa Mungu, aliyemtoa kwenye kituo cha watoto yatima na kumleta Ulaya. Nchi aliyoipanga kwenda kujitolea kufanya kazi, ni ile ambayo itakuwa ni ya ni ya asili ya wazazi wako. Kitu ambacho kilikuwa kinamuumiza kichwa ni kuwafahamu ndugu zake kwa upande wa baba na mama.

Taarifa aliyowahi kupewa na Babu yake wa kuasili, baba mzazi wa Mr. Lorenzo ni kuwa alichukuliwa kwenye kituo cha yatima katika moja ya nchi za Afrika, hivyo moja kwa moja mawazo yake yakampa kuwa wazazi wake wameaga dunia ndio maana alipelekwa kwenye kituo cha yatima. Bahati mbaya zaidi, Pesambili alikuwa hajijui jina lake hilo la Pesambili alilopewa na Bibi yake mzaa mama. Mr.Lorenzo alipomuasili tu, akambatiza tena upya na kumpa jina jipya la 'Trezguet Lorenzo', na hilo ndio jina alilolitumia kusomea shule. Hakuwa analipenda kabisa jina hilo la kizungu kwa asilimia 100%, ila hakuwa na jinsi. Alizidi kuchukia kuishi nchini Italia hasa kutokana na kuibuka wimbi jipya la ubaguzi wa rangi lililoanza kuibuka kwa kasi. Kuna wakati alikuwa akiingia kwenye Daladala, abiria wazungu wanampisha siti aketi peke yake.

Akikatisha mitaa ya wahuni wanambwekea sauti za nyani. Hali ambayo haikumkatisha tamaa bali ilimjenga kisaikolojia na kumshajiisha afanye bidii katika masomo ili akaungane na Waafrika wenzake kujiletea maendeleo yao binafsi hasa katika uboreshaji wa sekta ya Afya.
Kitendo cha kwenda mara kwa mara kule gerezani kumtembelea baba mlezi wake Mr.Lorenzo, Pesambili akajikuta anajenga mazoea na Mr.Martin Tenga pia. Kama waswahili wasemavyo damu ni nzito kuliko maji, alijikuta tu katokea kumpenda kwa kumsafishia nia bila kufahamu kuwa huyo ndio baba yake mzazi, huku yeye akijua ni rafiki wa Mr.Lorenzo.

Lakini kabla hawajazoeana vya kutosha na baba yake kidudu mtu kikaingilia kati. Wafungwa wote wa gereza lile la 'Museo del Carcere "Le Nuove' wakasambaratishwa kwa kutawanywa magereza mbalimbali ya nchini Italia. Hiyo ilitokana na taarifa za kiintelijinsia toka kwa mashushushu wa serikali kunusa harufu ya mpango wa kundi la Kimafia 'Ndrangheta' kutaka kutorosha gerezani baadhi ya washirika wao. Na kwa kuwa Mr.Martin Tenga alikuwa ni mshirika wao, akahisiwa nae alikuwa kwenye orodha ya wafungwa waliokuwa wanahitaji kutoroshwa gerezani, hivyo akahamishiwa gereza la siri lenye ulinzi mkali saa 24.

Pesambili nae kwa upande wake muda wa kujiiunga na Chuo Kikuu tayari kwa kuanza masomo yake ya Udaktari ukatimu. Ndio ikawa kimoja haonekani tena mitaani Jijini Turin, ametingwa na shule huku mwenyewe akitaka asijiingize kwenye jambo lolote litakalomtoa nje ya masomo. Darasa lao wanaosomea fani ya Utabibu lilikuwa lina wanafunzi 100, huku ngozi nyeusi ni Pesambili peke yake. Mwanzoni wanafunzi wenzake na baadhi ya Wahadhiri walikuwa wanamdharau wakichukulia kuwa mtu mweusi hana anachokiweza zaidi ya kupenda ngoma na starehe. Hakuwajali yeye akawa anajipanga kuwaonyesha kazi darasani.

Masomo yalivyoanza kuchanganya vizuri na kuanza Mitihani kila Mwanachuo alimheshimu na kumhusudu Pesambili. Kila Mtihani alikuwa anapata maksi kuanzia asilimia 90% kwenda juu kwenye masomo yote muhimu kwa daktari kama Anatomia 'Anatomy', Fiziolojia 'Physiology' na mengineyo. Umahiri wake kwenye masomo ukamfanya awe maarufu Chuo kizima kuanzia Wanachuo mpaka Wahadhiri wote.

Chuo tayari kilishaanza kumtongoza Pesambili kwa kumpa ahadi za mshahara mnono na marupurupu ya kutosha kama atakubali kubakia Chuoni hapo awe Mhadhiri pindi akimaliza masomo yake. Pia hospitali mbalimbali kubwa barani Ulaya walishaanza kusikia sifa zake nao wakaingia kwenye mkumbo wa kumgombea Pesambili. Wote hao Pesambili aliwaruka kimanga na kuwakatalia kuwa hayupo tayari kuingia makubaliano na mtu yoyote mpaka atakapomaliza masomo yake.

Maajabu ya kipekee kwa Pesambili ni kuwa usiku alikuwa kwa baadhi ya siku lazima amuote usingizi baba yake mzazi Mr. Martin Tenga, huku akilini akijiaminisha kabisa kuwa sio sura ngeni kabisa machoni mwake. Alikuwa kila akijaribu kuvuta hisia za kumbukumbu zake kuwa wapi alishawahi kuonana na mfungwa mwenzake wa baba yake mlezi, akili ilikuwa inagoma kabisa kukumbuka. Lakini pia bado suala la kutokujua asili yake na ya wazazi bado lilikuwa linamtafuna Pesambili. Siku alikuwa anaona zinachelewa za yeye kumaliza Chuo ili alishughulikie rasmi suala la kuitafuta asili yake na pia kuulizia ni gereza gani Mr.Martin Tenga amefungwa akamtembelee na kumdadisi vyema, huenda akafahamu walionana wapi kwa mara ya mwisho kabla ya kukutana tena gerezani.

Chambilecho siku hazigandi, miaka 5 ya kumaliza masomo kwa Pesambili ikawa imetimu, akachaguwa kwenda kufanya mazoezi vitendo katika Jiji la 'Barletta', moja ya Jiji lenye wakazi masikini nchini Italia. Hayo ndio yalikuwa mapenzi ya Dr. Pesambili au ukipenda Dr.Trezguet Lorenzo kwenda kutoa huduma kwa watu masikini, ambao shukrani yao kwake itakuwa ni kumuombea dua kwa Mungu.
[emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586]

Gandhi Square, eneo maarufu hapa mitaa ya Carlton Centre ndani ya Jiji la Johanesburg ndio ulikuwa moja ya mtaa maarufu sana kwa Mbweku Jr akiwa ameshakata miaka ndani ya Jiji hilo tokea atue nchini Afrika ya Kusini. Ulikuwa ni mtaa ambao Watanzania wengi utawaona wanazurura mitaani. Si ajabu ukakuta kwenye mtaa mzima watu wote wanaongea kiswahili. Haya yalikua maeneo duni sana, machafu, yananuka kila aina ya harufu. Wabongo wengi walikua ni vibaka, wanategeshea barabarani kwenye alama za pundamilia 'zebra cross' ambapo msongamano wa watu ni mkubwa sana. Kisha wanawazonga watu, na kuwakwapulia mali zao. Wadada na wamama walikua wanalizwa sana vitu vyao vya thamani kama simu za mkononi, fedha na vipochi vyao. Wengi wa hawa wabongo walikua kama mateja, wamechoka sana wanapolala ndio hapo hapo wanapokojoa.


Mbweku Jr alikuwa ameshatua nchini Afrika ya Kusini kiwepesi kabisa kuliko matarajio yake. Aliponea kifo kwenye tundu la sindano yeye na Deborah kwenye mlipuko wa mabomu katika jumba la Recho kule Sinza Kijiweni. Pia wakafanikiwa kuruka viunzi vya walinda usalama ambao walikuwa wanamsaka Deborah kwa kosa la kumuibia mfadhili wake Koplo Marieta. Usiku ule walikuwa wanawapita bila kusimamishwa barabarani tena wakiwa wanatembea mashimashi bila usafiri wowote tena kifua mbele bila kuogopa kitu. Deborah alikuwa anashangazwa sana kwanini watu wengine wanasimamishwa na kuhojiwa ila wao wanapita bila kuulizwa kitu chochote. Mbweku Jr alikuwa anatabasamu tu hana hata chembe cha hofu wala uoga wowote. Moyoni mwake mwake alikuwa anajua kila kitu kwanini inatokea vile hawakamatwi na wana usalama, mpaka akafanikisha mpango wake kabambe wa kutorokea nchini Afrika ya Kusini salama salimini huku akimuacha Deborah mikononi mwa rafiki yake kipenzi Timammy kwa ajili ya uangalizi wake wa kila kitu.

Mbweku Jr nae alikuwa ni miongoni mwa vijana hao vibaka wa mitaani, akiishi maisha ya kuungaunga na kubangaiza yasiyo na mbele wala nyuma. Nyumba ya kuishi alikuwa anakaa gheto na vijana wenzake kwenye chumba walichopangisha katika mtaa wa 'Polly Street', kulikuwa na jengo moja limechakaa kiasi, ndipo hapo maskamoni pake. Maamuzi yake ya kuja nchini Afrika ya Kusini licha ya ugumu wa maisha anayoishi hakuyajutia sana hasa kutokana na taarifa zake za msako kusambaa mpaka Afrika ya Kusini. Habari zilimfikia kuwa anasakwa kama nyara ya taifa na wana usalama kutokana na mlipuko wa jengo kule Sinza, na picha zake zimesambaa kila kona ya nchi kuanzia kwenye magazeti na mitaani, akituhumiwa kuwa ni mmoja wa walipuaji wa hilo jengo.

Aliishia kusononeka moyoni kutokana na kusingiziwa kitu asichohusika nacho kabisa hali ya kuwa ukweli wote alikuwa anaujua kinagaubaga kuwa sio mhusika wa tukio hilo. Moyoni alikuwa anahuzunika kuhusu yule daktari aliyemshushia kipigo, hakuwa na taarifa zake kama alisalimika au alipoteza uhai. Pia alikuwa hajui kama Bosi wake Recho aliokoka kwenye milipuko ile au nae alikuwa ni mhanga wa tukio hilo. Alichokuwa anajutia sana ni kitendo chake cha kukubali kuziacha pesa zote sufufu alizopora kwenye gari la Bosi wake Recho kwa rafiki yake aliyekuwa nae kijiwe kule Kigamboni, Timmamy.

Huyu ndio alimlaghai na kumtia ndimu vilivyo Mbweku Jr kuwa aache pesa zote atoroke yeye kama yeye bila kitu chochote huku akimtisha kuwa mpakani mwa Tanzania na Msumbiji, askari wa uhamiaji wa Msumbiji ni wakatili na wababe, watampora kila kitu chake na kumuacha patupu. Wakaweka makubaliano ya mdomo na Timmamy kuwa hizo pesa awekeze kwenye biashara ya pamoja, na mwaka wowote atakaorudi salama watagawa mali nusu kwa nusu. Pia katika makubaliano alimuomba Timmamy kila akipata muda asikose kumtembea baba yake mzazi gerezani na kumpelekea mahitaji mbalimbali hasa ukichukulia ni mgonjwa hivyo anahitaji uangalizi wa karibu.

Timmamy ndio aliyemuelekeza Mbweku Jr afikie 'Polly Street' Jijini Johanesburg. Kwa jinsi Timmamy alivyokuwa anajinadi kijiweni na kujimwambafai kuwa anaishi maisha mazuri huko nchini Afrika ya Kusini, alichokikuta Mbweku Jr ni tofauti kabisa, ni kama mbingu na ardhi. Gheto moja walikuwa wanaishi watu 15 chumba kimoja, wakiwa wamepanga magodoro chini utasema wanalala matanga msibani. Alichokuwa hafahamu Mbweku Jr ni kuwa kuna ujanja na udanganyifu hali ya juu sana, katika uwanda huu wa kidigitari unaofanywa na Watanzania wanaoishi Ughaibuni. Kwa mfano kijana anayeishi nchi za Ulaya au Afrika ya Kusini anaweka picha zake nyingi kwenye mitandao kama Facebook, Instagram au Twitter akijionyesha mwenye tabasamu, afya murua, mavazi ya kisasa na vilevile mazingira safi na mandhari za kuvutia, akiwa ameegemea gari la kisasa ili tu kuwakoga vijana wenzake ambao kwa bahati nzuri kwake wapo nchini Tanzania, ambako mazingira ya Ughaibuni wanayaona kama mazingaombwe kwao. Mpaka wengine wanafikia hatua ya kujutia kuzaliwa nchini Tanzania na kutamani hata kama wangekuwa mbwa huko Ughaibuni lakini sio kuishi Tanzania. Lakini, ndani ya picha hizo kuna matatizo makubwa ambayo hakuna anayeweza kuyajua bila kusafiri na kwenda kuishi huko japo kwa muda mfupi.

Hayo ndio yaliyomkuta Mbweku Jr kwa jinsi alivyokuwa anatamani maisha ya Ughaibuni kutokana na hadithi za paukwa pakawa za kijiweni kule Kigamboni sasa zilikuwa hadithi hizo zinamtokea puani, anaula wa chuya. Akakuta maisha ya Ughaibuni yamejaa msongo wa mawazo ambao siyo wa kawaida na kuna wakati hasa wageni wanaingia katika majaribu mbalimbali hata ya kutaka kujinyonga kwa msongo wa mawazo. Ndipo alipojikuta Mbweku Jr na vijana wenzake toka Mataifa mbalimbali ya Afrika ambao wamezamia nchini Afrika ya Kusini na maisha kukuta yanakwenda mchafukoge na kujikuta wakijiingiza katika biashara hatari ya kuuza dawa za kulevya katika mitaa mbalimbalimbali ya nchi hiyo ili wapate kipato cha kujikimu.

Kwa wanaopenda maisha ya bwerere ili kukabiliana na ugumu wa maisha ya huko Ughaibuni haishangazi kumkuta kijana wa kiume wa Kitanzania akijivinjari na mke wake mwenye umri ambao ni sawa na bibi wa kumzaa mama au baba yake, hivyohivyo kwa msichana kumkuta akiwa na babu yake ukiuliza utaambiwa maisha na makaratasi. Makaratasi ni nyaraka za kukuwezesha kuishi kama raia wa ukiwa katika nchi za Ughaibuni na kupata mahitaji yote ambayo ni ya lazima kwa raia wa nchi hiyo, hasa unapokosa kazi kwa hiyo wengi huona kama wamepata aina fulani ya ushindi.
 
SEHEMU-38


katika majaribu mbalimbali hata ya kutaka kujinyonga kwa msongo wa mawazo. Ndipo alipojikuta Mbweku Jr na vijana wenzake toka Mataifa mbalimbali ya Afrika ambao wamezamia nchini Afrika ya Kusini na maisha kukuta yanakwenda mchafukoge na kujikuta wakijiingiza katika biashara hatari ya kuuza dawa za kulevya katika mitaa mbalimbalimbali ya nchi hiyo ili wapate kipato cha kujikimu. Kwa wanaopenda maisha ya bwerere ili kukabiliana na ugumu wa maisha ya huko Ughaibuni haishangazi kumkuta kijana wa kiume wa Kitanzania akijivinjari na mke wake mwenye umri ambao ni sawa na bibi wa kumzaa mama au baba yake, hivyohivyo kwa msichana kumkuta akiwa na babu yake ukiuliza utaambiwa maisha na makaratasi.

Makaratasi ni nyaraka za kukuwezesha kuishi kama raia wa ukiwa katika nchi za Ughaibuni na kupata mahitaji yote ambayo ni ya lazima kwa raia wa nchi hiyo, hasa unapokosa kazi kwa hiyo wengi huona kama wamepata aina fulani ya ushindi.


Siku, wiki, miezi na miaka ikawa imekatika, sasa ilitimu miaka 10 taslimu, sawa na muongo mmoja tokea Mbweku Jr atoroke nyumbani, Tanzania. Sasa hamu ya kurudi nyumbani ikawa inamsonga kila wakati hasa ukichukulia maisha kila siku zinavyosonga yalikuwa yanakuwa magumu sana. Kulianza kuibuka vitendo vya chuki na ubaguzi 'Xenophobia' dhidi ya wageni nchini Afrika ya Kusini na kutikisa dunia. Vitendo ambavyo havikuweza kuvumiliwa na wapenda haki, amani, ustawi na maendeleo ya wengi duniani. Wageni walikuwa wanawindwa kwa ajili ya kuuliwa na kuharibiwa mali zao na raia wa nchi ya Afrika ya Kusini, wakiwatuhumu wamekuja nchini kwao kuziba ajira zao, hivyo kuwataka warejee nchini mwao.

"Masela wangu safari ya kurudi nyumbani Tanzania kwa upande wangu imeiva, siwezi kuvumilia kuishi maisha ya kujificha kama popo" aliongea kiunyonge Mbweku Jr akionekana kukata tamaa kabisa ya kuendelea kuishi maisha ya tabu na mashaka ugenini. Walikuwa wapo chumbani usiku wanabadilishana mawazo namna ya kukabiliana kikamilifu na vita dhidi yao inayofanywa na wenyeji. "Mwana acha kutuzingua, kila mtu ataondoka kwa namna alivyokuja, mimi binafsi yangu nitazikwa kwenye ardhi ya Mzee Madiba, maisha ya nyumbani Tanzania siyawezi tena, nimeondoka kwa zaidi ya miaka 20 halafu nirudi mikono mitupu hamna atakayenielewa. Hivyo hapa hamna mtoto mdogo wa kumpa ushauri, wewe si ulikuja kichawi huku Bondeni basi rudi kichawi vilevile" aliongea kwa jazba na hasira jamaa aliyekuwa anajulikana kwa jina la 'RAS' na wenzake akionekana kukerwa na maneno Mbweku Jr ya kukata tamaa ya kutaka kurudi nyumbani Tanzania.

Maneno ya kebehi toka kwa RAS kuwa Mbweku Jr amekuja kichawi nchini Afrika ya Kusini yaliamsha vicheko ndani ya chumba kile huku Mbweku Jr akiwa amejiinamia tu kichwani amejawa na mkururu wa mawazo, huku nae ameshikwa na hasira kama mbogo anatamani wachapane ndondi ili heshima irudi mahali pake. Wengi wao walikuwa hawaamini hadithi ya ujio wa Mbweku Jr nchini Afrika ya Kusini wa kimiujiza. Alivyowasimulia waliona kama ni ndoto za Alianacha, anawaongopea tu. Hasa wakijiangalia wao namna walivyoisotea kuitafuta Afrika ya Kusini. Mbweku Jr hakutilia maanani kebehi zao hasa akichukulia ukweli halisi alikuwa anao yeye. Kebehi hizo zikamkumbusha Mbweku Jr namna alivyosafiri ndani ya siku 3 mfululizo bila kikwazo chochote mpaka nchini Afrika ya Kusini, akajenga tabasamu la furaha usoni mwake. Akakumbukia tukio zima kwa mtiririko sahihi kabisa akiwa kijana mdogo wa miaka 17 mwenye umbo lililojengeka, wakati anafanya kibarua cha ulinzi katika danguro la Bosi Recho alipomtembelea baba yake gerezani. "Baba mie nasafiri kwenda nchini Afrika ya Kusini saa na wakati wowote kuanzia sasa, hii ni taarifa tu nakupa sihitaji ushauri wako !" aliongea Mbweku Jr akiwa ameshasimama lakini anachemka kwa hasira dhidi ya Recho, amekunja ndita mpaka akajikuta machozi yanamlengalenga. "Safari njema, wewe sasa ni mkubwa upo katika utawala wako binafsi, nakujua wewe ukilazimisha jambo lako lazima liwe unavyotaka ndio tabia yako toka utotoni. Ila kikubwa ni kama nilivyokupa nasaha, usijaribu kufanya chochote cha kulipiza kisasi kwa Recho. Kwanza hatuna ushahidi wa asilimia 100% kuwa yeye ndio mporaji wa pesa zilizoibwa ofisini, pili ana nguvu ya kipesa atakupoteza wewe na kizazi chako chote akikugundua umeijua siri yake kuwa yeye ndio muuaji wa Bosi Minja. Pia nakuomba kabla hujasafiri kwenda huko unakotaka kwenda upite Bagamoyo kwa Sheikh Maarifa akufanyie dua ya safari, wakati tupo kazini enzi zetu watumishi wengi tulikuwa tungongana kwake kunyoosha mambo yetu" aliongea Mzee Mbweku huku akisimama na kuvichukua vitu vya zawadi alivyoletewa na mtoto wake.


Siku hiyo Mbweku Jr alivyotoka hapo gerezani mchana huo, baada ya kuuliza uliza kwa watu, akaelekezwa kuwa kufika kwa Sheikh Maarifa apande gari za kuelekea Bagamoyo kisha ashuke maeneo ya mbele ya Kiromo. Akifika hapo dereva bodaboda yoyote atakayemuuliza kuwa anataka kufika kwa Sheikh Maarifa atamfikisha. Mbweni hakujivunga, na asiyesikia la mkuu huvunjika guu, huo ndio ushauri wa baba yake alikuwa hana budi lazima aende kwa Sheikh Maarifa akapate dua na baraka za safari ya Afrika ya Kusini. Mpaka kufika majira ya saa 9:30 alasiri alikuwa tayari yupo katika viunga vya Sheikh Maarifa, akikutana na wateja wengine wanaosubiria huduma.

"Sheikh kaenda kuswali msikitini, baada ya swala ndio ataendelea na huduma tena" aliongea mmoja wa wahitaji wa huduma ya Sheikh akimpasha Mbweku Jr alipoulizia. Mbweku Jr akawa hana budi kufanya subira, huku akitafuta nafasi kwenye jamvi maalumu la wateja na kuketi chini baada ya kuvua viatu vyake. Pale zikaanza soga mbili tatu juu ya umahiri wa Sheikh Maarifa namna alivyotabahari katika fani ya falaki na uaguzi wake. "Huyu Babu ni kiboko sana, akitaka kuchuma nazi, wala haitaji mkwezi yeye anachofanya ni kuomba dua zake tu basi ule mnazi unajipinda mpaka kwenye usawa wa mikono yake, anachuma kisha anauombea unarudi kama zamani" aliongea mteja wa Sheikh wa lugha ya tashiwishi na hamasa kuonyesha Sheikh ni gwiji kwelikweli katika fani yake.

"Huyu Sheikh anatisha sana katika fani, akitaka kusafiri hana haja ya kupanda gari, huwa anakaa kwenye jamvi lake anafanya kisomo tu anapaa, kwa kweli amepewa makarama sana na Mwenyezi Mungu" mwingine nae alichangia maongezi pale jamvini. Maongezi ambayo yalimtia nguvu na kumshajiisha Mbweku Jr kuwa kweli hajafunga safari bure, amekuja kwa kigogo haswa kama alivyoelekezwa na baba yake. Wakati maongezi yanaendelea baina yao, akajidhihirisha mbele yao, mtu shaibu kiumri, mrefu wa wastani, rangi ya maji ya kunde, amevaa libasi aina ya kanzu nyeupe pee isiyo na chembe ya doa kwa umaridadi wake, mkononi kabeba tasbihi na miguuni kavalia makubazi ya rangi ya hudhurungi. Alikuwa anakuja mbele yao akitokea msikitini huku midomo yake na ulimi wake unaonekana kutikisika na vidole vyake vikihesabu tasbihi kuonyesha alikuwa anamdhukuru Mwenyezi Mungu. Kila mmoja pale kwenye jamvi akazidisha kukaa mkao wa heshima na taadhima.

"Asalamu Aleikum Warahmatullah Wabarakatuhu jamia" alitoa salamu kwa sauti nzito yenye kuonyesha ni mtu mwenye kujiamini, huku akielekea moja kwa moja kuketi kwenye kiti tupu kilichokuwa kimetengwa mbele yao. "Waleikum Salaam" waliitikia watu wote kwa pamoja waliokuwa wamekaa pale jamvini. Huku kila mmoja akiwa amesinyaa kama magome ya miti, akitega masikio yake kama antena kusubiria maelekezo maridhawa toka kwa yule mtu mahashumu kwao. "Sheikh ametingwa na ugeni mzito toka Uarabuni hivyo kwa leo mimi ndio nitatoa huduma kwenu, nianze na wewe kijana Mbweku unaonekana una safari nzito ya haraka, elekea kwenye kilinge kile pale" alifungua maongezi kwa kutoa maelezo mafupi lakini safi kama msahafu yenye kuonyesha yeye sio Sheikh Maarifa mlengwa wao. Mbweku aliposikia utambulisho ule alipatwa na unyonge kidogo wa moyo juu ya uwezo wa huyu msaidizi wa Sheikh. Lakini mashaka na wahaka wake moyoni ulikuja kuondoshwa mara moja baada ya kutajwa kwa jina lake na kuelezwa sababu iliyomleta Bagamoyo hata kabla hajafungua mdomo wake kujieleza. Alichokuwa hafahamu Mbweku Jr ni kuwa mbabe huyo wa fani ya falaki alikuwa anatumia kitabu kinachoitwa 'Majmu Saatul Khabar', kitabu ambacho kwa imani zao waganga hao kilikuwa kina kanuni za kufuatwa za kujua matukio ya kila saa kwa kila mtu.

Mbweku Jr alipopewa maelekezo yale akasimama na kuelekea kwenye kilinge hicho cha kibanda cha miti kilichoezekwa kwa makuti ya mnazi na kuzungushiwa bendera nyekundu na nyeupe zilizochorwa herufi mbalimbali za lugha za maruhani. Mbweku Jr akaelekezwa akae juu ya kinu cha kutwangia huku akiwa amefumba macho yake asione kinachoendelea ndani ya Kilinge kile. Akaanza kuzisikia sauti mbalimbali za kuogofya zilizomfanya ashtuke kama mtu aliyekanyaga kaa la moto. Yule msaidizi wa Sheikh alipoingia hapo Kilingeni tu sauti zile zikakoma. Akaamrishwa afumbue macho, alipofumbua tu, ghafla bin vuu likapita bonge la paka jeusi lina shingo nene kama mbuyu amevikwa lundo la hirizi zilizoshonana kama ushanga. Paka lile likaenda kutulizana katikati ya miguu ya mtaalamu akazunguruka mara 7 mfululizo kisha akatoka nduki kukimbilia kusipojulikana. Kipindi chote hicho Mbweku Jr alikuwa roho juu juu, jasho jekejeke la uoga linamtiririka chini ya makwapa.

Mtaalamu yule hakumjali Mbweku Jr akaanza kumsomea kisomo kirefu cha zaidi ya saa moja. Baada ya hapo akaelekezwa akakae chini ya mti wa Mkungu kusubiria jani litakalo dondoka wenyewe kisha alipeleke kwa mtaalamu. Alisubiria chini ya mti kwa takribani dakika 29 ndipo jani hilo alilokuwa analisubiria kwa hamu likaanguka. Haraka haraka akaliokota hilo jani huku akiwa na furaha sheshe mpaka akalifikisha kwa msaidizi wa Sheikh. Mbweku Jr alivyokabidhi akaachwa kwenye kilinge, huku mtaalamu yule akiingia chemba kushughulikia lile jani. Zikawa zinasikika sauti za mnyama kama kondoo kulalamika kwa maumivu ya kuchinjwa chwa, huku damu zake kondoo huyo zikichiririka chiriri chiriri. Baada ya kama nusu saa hivi Sheikh yule akatoka kule chemba huku akiwa ana uso uliojaa bashasha. "Kazi yako tayari, utasafiri salama salimini, bila shida yoyote. Utatakiwa kuanza msafara wa kuelekea nchini Afrika ya kusini saa 10:29 usiku, pale ambapo, mapambazuko ya asubuhi yanakaribishwa. Ndio maana lile jani limedondoka baada ya dakika 29. Na hii ni hirizi iliyoshonwa kwa ngozi ya kondoo na ndani yake kuna jani la mkunguu na vifaa vingine vya kazi, utaivaa kiunoni kuanzia sasa na hamna Askari yoyote atakayeweza kukukamata. Na utakapofika mpakani mwa Msumbiji na Tanzania, omba kuonana na mkubwa wao wa kazi, atakapokuja muambie shida yako atakusaidia. Tayari nimeshamvuta na kumkata ulimi hatoweza kujitetea chochote mbele yako. Nakutakia safari njema, utaweka kwenye kapu lile pesa ya vifaa na sadaka yako ya ufundi" aliongea yule mtaalamu huku akiruhusu Mbweku atoke ili aingie mtu mwingine mhitaji wa huduma ya uganga.

"Ahsante sana Sheikh, Mwenyezi Mungu akubariki, kazi njema" aliongea Mbweku Jr akitoka nje ya kilinge na ile hirizi yake. Kwa usongo tu akaamua aivalie pale pale hata kabla hajafika nyumbani. Mbweku Jr kwa furaha aliyonayo akawa anarukaruka kwa furaha kama mwanambuzi. Hiyo hirizi ndio Mbweku Jr anaamini ilimsaidia usiku wa tukio la kumuokoa Deborah kuweza kupita barabara mbele ya mapolisi bila kusemeshwa chochote. Pia imani yake ikamtuma kuwa alipofika mpakani, yule Mkuu wa Uhamiaji wa upande Wa Msumbiji alimruhusu kupita bila kumuuliza hati ya kusafiria tena akimsaidia kumuombea usafiri wa gari la kumfikisha nchini Afrika ya Kusini. Simulizi hii alivyowapa wenzake hakuna aliyemwamini walijua ni Ablakadabra za kusukuma muda tu, lakini huo ndio ukweli halisi kwake.

Baada ya mazungumzo yao mule chumbani, Mbweku Jr alipanga asubuhi na mapema ataenda kujiandikisha ubalozini kwa ajili ya kurudishwa Tanzania kuepuka machafuko. Mbweku Jr hakuwa na wasiwasi wa kuishi maisha magumu atakaporejea nchini Tanzania, kwani alijua mgao wake wa pesa atakaoupata kwa rafiki yake kipenzi waliyeshibana kama chanda na pete, Timammy utamuwezesha kuishi maisha mazuri anayoyataka yeye. Penyenye alizokuwa anazipata toka kwa Vidinga popo wa nyumbani Tanzania ni kuwa Timammy ni tajiri mkubwa anayemiliki vituo vya kuuza mafuta 'Petrol Station' kila kona ya Jiji la Dar es Salaam. Alikuwa pia anamiliki nyumba za ghorofa za kupangisha lukuki katika maeneo mbalimbali ya Jiji la Dar es Salaam.

Wazo lake la kwanza alilopanga pindi akipokea mgao wake ni kujenga mjengo wa kuishi. Kisha akaenda kijijini kuifuata familia yake waishi pamoja kama zamani. Pia alipanga kufunga ndoa haraka sana, na mwanamke wa ndoto zake kila alipokuwa anawaza alikuwa ni Deborah. Alikuwa anamuona Deborah kuwa ni mwanamke aliyetimia katika idara zote. Kuanzia uzuri wa umbo, tabia ya uvumilivu katika maisha na usomi. Deborah alimsimulia Mbweku Jr madhila na manyanyaso yote aliyowahi kupitia maishani mwake. Wasiwasi pekee aliokuwa nao Mbweku Jr ni juu ya kumkuta Deborah akiwa bado hajaolewa au kupata mchumba. Akilini alishajiandaa kisaikolojia kukubali matokeo kama akimkuta kashawekwa kwenye himaya ya mtu. Kosa alilokuwa anajijutia ni uoga wake kama fisi ni kutomueleza ukweli Deborah mapema kabisa kuwa anampenda sana na anatamani aje kuwa muhibu wake wa kufanya nae maisha ya ndoa. Hofu kubwa iliyomzuia kumtapikia Deborah hisia zake ni kwanza kuogopa ataonekana ametoa msaada wa kumuokoa kule kwenye danguro kwa lengo la kujifaidisha kimwili. Pili aliogopa asije kumchanganya kimasomo, badala ya kutili mkazo kwenye shule atageukia kuwazia mapenzi tu hivyo kusababisha afeli vibaya masomo yake, kama ujuavyo penzi ni kitovu cha uzembe. Na kwa kuwa penzi lake kwa Deborah lilikuwa ni la dhati kabisa hakutaka yeye kuwa ndio kikwazo cha kumfanya Deborah ashindwe kutimiza ndoto zake. Matumaini pekee yalibakia kwa rafiki yake Timammy ambaye alimdokezea juu ya mapenzi yake ya dhati kwa Deborah na kumuomba amsaidie kwa hali na mali kutimiza ndoto zake.
[emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586]
Mwalimu wa zamu: "Jina lako unaitwa nani? "
Mwanafunzi: "Naitwa Deborah Minja"
Mwalimu wa zamu: "Fomu yako ya kujiunga na shule ipo wapi? "
Deborah: "Imeibiwa na vitu vyangu vingine..!"
Mwalimu wa zamu: "Pole sana, umetokea Mkoa gani na umemaliza shule gani? "
Deborah: "Nimetokea Mkoa wa Morogoro, Wilaya ya Mvomero, shule ya msingi Mikongeni, "
Mwalimu wa zamu: "Haya nisubiri nikaangalie jina lako kwenye ofisi ya Mwalimu wa Taaluma" aliongea Mwalimu yule huku akinyanyuka na daftari lake mkononi akimuacha ofisini mwake Deborah peke yake. Baada ya kitambo kifupi kupita akarejea akiwa ameambatana na mwanafunzi mwengine aliyevalia sare zake nadhifu za shule.
Mwalimu wa zamu: " Sasa Deborah utafuatana na huyu mwenzako, atakupeleka bwenini kwao, atakupeleka kwa Mhasibu ukalipie ada kabisa. Pia tambua umechelewa na una bahati ya mtende, kesho kutwa kuna Mitihani ya mchujo, watakaofeli wanarudishwa shule za sekondari za kawaida tambua kuwa Msalato ni shule ya watoto wenye vipaji vya akili, hivyo ujiandae vyema na mitihani katika muda huo mfupi" aliongea Mwalimu yule kwa ukarimu na umakini mkubwa.
Deborah: "Ahsante sana Mwalimu nitafuata ushauri wako" aliongea Deborah huku akisimama na kuanza kubeba sanduku lake huku yule mwenzake akimsaidia kubeba godoro lake.
Mwalimu wa zamu: Haya usome kwa bidii si umeona kaka yako kafunga safari toka Dar es Salaam mpaka Dodoma kukuleta shule ili usome kwa bidii" alizidi kuchagiza maneno ya hamasa Mwalimu yule kwa Deborah akimkumbushia Timammy, rafiki yake Mbweku Jr ambaye alijitolea kumnunulia vifaa vya shule, kumpa pesa ya ada pamoja na matumizi na kumleta shuleni, Jijini Dodoma. Pesa yote hiyo, Deborah alidhania imetoka mfukoni mwa Timammy, kumbe ni pesa ya mfadhili wake Mbweku Jr ambaye alimuokoa kule kwenye danguro la Recho, Sinza Kijiweni.

Baada ya kumaliza mikikimikiki yote ya siku nzima ya usajili pale shuleni akawa ametulia bwenini kwake, katika bweni linalojulikana kama 'Mwongozo' akawa yupo kwenye tafakari nzito ya furaha iliyochanganyika na huzuni, hali iliyomsababisha machozi ya furaha yamtiririke kama ngamia. Kwanza alikuwa haamini macho yake kama kweli kafanikiwa kutua shuleni kutimiza ndoto zake za kielimu hasa akikumbukia vimbwanga vizito alivyopitia kuanzia kule nyumbani kwa Mjomba Kobelo, kutoroka kwake, kukamatwa na polisi, kuokolewa na mfadhili wake Koplo Matuta, kutekwa kwake na kuhifadhiwa kwenye danguro la Bosi Recho hadi kuokolewa na Mbweku Jr.
Hakuchukua muda mrefu kuzoea mazingira ya shuleni pale, ndani ya muda mfupi akawa anajulikana kama mmoja wa wanafunzi vinara wa Masomo ya Sayansi. Mazingira ya shule yakampenda akanawiri kama mti uliopata mbolea. Tatizo kubwa lililokuwa linamsumbua ni la kujikojolea kila unapofika usiku wa Jumamosi kuamkia Jumapili. Ile ndoto ya ukweli juu ya mauaji ya kinyama yaliyofanywa dhidi ya baba yake ilikuwa inajirudia mara kwa mara. Hali ambayo ilikuwa inamfanya ajikojolee kwa uoga, na akishtuka usingizini anajikuta ameshachafua kitanda kwa mikojo. Wanafunzi kama uwajuavyo hawana dogo, habari zile za umbea wa kuwa Deborah ni kikojozi licha ya urembo wake na akili zake darasani zikasambaa kwa kila mwanafunzi.

Wapo waliokuwa wanamkebehi dhahiri shahiri kwa kumuita 'Mrembo Kikojozi' na wengine 'Kipanga Kikojozi' na majina kochokocho ya dharau na kashfa. Taarifa ilipofika kwa Matroni wao ikabidi amuite Deborah na kumhoji kulikoni. Ikabidi amuelezee mkasa mzima wa namna alivyoishuhudia sura ya mmoja wa wauaji wa marehemu baba yake. Mkasa ambao ulimkumba tokea akiwa kinda wa Chekechea na namna unavyomtesa mpaka leo. Mwalimu yule akamuonea huruma sana na kumpa pole nyingi kwa mkasa huo mbaya uliomkuta. Tokea siku ile Mwalimu yule akashusha mkwara mzito sana kuwa yoyote atakayegundulika anamkebehi Deborah hatua kali dhidi yake zitachukuliwa ikiwemo hata kufukuzwa shule. Tangazo hilo likawa kidogo limesaidia kutuliza hali ya hewa na kumfanya Deborah aanze kufurahia tena maisha ya shule. Hali hiyo ya kudharauliwa ndio ikawa ni kichocheo chake cha kusoma kwa bidii. Usiku wa Jumamosi kuamkia Jumapili akauchagua uwe ni usiku wa kukesha kusoma ili kuepuka aibu ya kujikojolea kitandani. Timammy kumbe nae alikuwa amekufa na kuoza kwa Deborah. Kila inapofika Jumamosi ya mwisho wa mwezi ya kutembea wanafunzi 'Visiting Day' Timmamy akawa anahudhuria na zawadi kedekede kuanzia sabuni za kuogea, manukato, mpaka vyakula vya makopo. Ukarimu aliokuwa anafanyiwa Deborah akaanza kuingiwa na mashaka, kuwa ipo siku tu isiyo na jina atalazimika kuvilipa hivyo vitu. Alianza kumuona Timammy ni adui mpenzi kama moto ulivyo, siku yoyote utakuja kumuunguza.

Hakuna marefu yasiyo na ncha, Timammy akashindwa kuficha hisia zake, kipindi ambacho Deborah yupo kidato cha 3, siku moja Timammy alivyomtembelea akavunja ukimya. Akaamua apasue ukweli uliopo moyoni mwake kwa Deborah. "Deborah wewe sasa ni mkubwa, mwakani unatimiza miaka 18, hivyo natamani ukimaliza tu shule kidato cha nne nataka nifunge ndoa na wewe". Timammy aliamua kufunguka liwalo na liwe, tayari alishavunja ahadi ya rafiki yake Mbweku Jr ambaye alidokeza kuwa ana mipango ya muda mrefu na Recho. Deborah pale pale alipokaa alisimama bila kuagana na Timammy na kutokomea zake kuelekea kusipojulikana. Timammy akaachwa mdomo wazi haamini kama kweli Deborah kamuacha solemba kwa kumfanyia jeuri. Deborah alikuwa amechefukwa na kuvurugwa na maneno ya mkahawani ya Timammy. Alimuona kabisa kuwa ni mharibifu asiye na mapenzi ya kweli kwake. Kwa sababu alimuona hajali kabisa masomo yake bali anajali kutimiza hawaa ya nafsi yake. Timammy fedheha na soni ilimkumba, akashikwa na ubaridi wa moyo, hakuamini kama Deborah atamuonyesha dharau kiasi kile, hasa ukichukulia tayari ameshaanza kutengeneza Jijini Dar es Salaam. Wanawake walikuwa wanamgombea ili awaoe wao kutokana na utajiri wake. Deborah alipotoka pale breki ya kwanza ni kwenda kushtaki kwa Mwalimu wa nidhamu. Akamuelezea kinagaubaga bila kuficha kitu, huku akiomba Timammy afutwe kabisa kwenye orodha ya majina ya ndugu zake wanaoruhusiwa kumtembelea shuleni. Ikabidi Timammy atolewe nje ya fensi ya shule chini ya ulinzi mkali wa walinzi wa shule. Timammy aliona kuwa amekashifika vya kutosha na chokoraa aliyeokolewa kwenye mdomo wa simba na rafiki yake Mbweku Jr sasa ameota mapembe. Akawasha gari lake na kuliondosha kwa kasi akirejea Jijini Dar es Salaam, huku akijiapiza lazima amshikishe adabu vya kutosha, mpaka afanikishe kumfanya mke wake iwe kufa au kupona.
[emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586]


SURA YA KUMI NA NNE
Bosi Recho baada ya kuponea kifo kwenye tundu la sindano, kwenye mlipuko wa jingo lake la ghorofa uliofanywa na Mr.Lorenzo, akajikuta amelazwa katika Hospitali ya Taifa ya Muhimbili katika kitengo cha mifupa cha Muhimbili Orthopaedic Institute MOI. Alipopokelewa tu akapelekwa moja kwa moja katika chumba cha wagonjwa mahututi ICU. Takribani mwezi mzima alikuwa hana fahamu tokea apokelewe hospitalini hapo. Madakatari bingwa walikuwa wanakesha kufanya mdahalo wa namna ya kuokoa maisha ya Bosi Recho. Baada ya majadiliano ya kina kati ya madaktari na ndugu wa Bosi Recho, wakafikia muafaka kuwa kama wana uwezo wampeleke mgonjwa wao kwenye hospitali kubwa huko ughaibuni kama nchini Afrika ya Kusini au India, lakini hapa nchini Tanzania matibabu yake yameshindikana kufanyika kutokana na kuwa na majeruhi mabaya. Ndugu zake Recho, walikuwa ni watu hohehahe wenye kipato cha kijungu meko, hivyo hawakuwa na uwezo wa kumpeleka kokote kule kwa ajili ya matibabu. Ikabidi wafikie maamuzi ya kupiga bei mali zote za Recho zilizopo Jijini Dar es Salaam ili pesa zitakazopatikana zitumike kulipia matibabu nje ya nchi na matunzo yake muda wote wa matibabu. Hatimaye Recho akasafirishwa mpaka nchini Afrika ya Kusini kwa ajili ya kuanza matibabu.

Alipelekwa kutibiwa katika hospitali inayoitwa “Busamed Hillcrest Private Hospital iliyopo Jijini Durban. Hiyo ni moja ya hospitali bora nchini Afrika ya Kusini katika orodha ya Hospitali bora 20. Ilikuwa ni hospitali yenye vyumba vya upasuaji vya kisasa, wodi za hadhi ya juu za kulaza wagonjwa, pia ilikuwa na Madaktari na Manesi bobezi katika kazi yao ya utabibu. Gharama ya siku ya matibabu kwa matibabu ya Recho hospitalini hapo ilikuwa ni shilingi elfu 50 za Kitanzania. Recho alifanyiwa upasuaji zaidi ya mara 37 katika sehemu mbalimbali za mwili wake, mpaka akaanza kupata nafuu. Ila angalizo walilotoa ni kuwa atakuwa mlemavu wa kutembelea kiti katika maisha yake yote yaliyobakia hapa duniani. Kwa huduma murua alizokuwa anazipata hapo hospitalini, baada ya kupiita muda wa miezi 9 akaanza kuongea bila shida ila hawezi kusimama, ni mtu wa kulala kitandani tu. Pesa zote alizokwenda nazo huko nchini Afrika ya Kusini zikaisha, ikabidi zikauzwe mali zake zingine za Jijini Arusha na Kilimanjaro ili ziweze kupatikana pesa za kuendelea kumtibu. Kwa hiyo rasmi Bosi Recho akawa ni muflisi, hana senti yoyote aliyoibakiza benki wala mali yoyote. Hakuwa tena na mikogo yake, ujanja wote ulishamuisha. Baada ya kukaa hospitalini kwa muda wa mwaka mmoja na nusu, ndugu zake wakaomba rasmi warudi nae nyumbani Tanzania, kutokana na kuhofia kushindwa kufanya malipo kama ataendelea na matibabu huko. Wakarudi nae Tanzania, na kupelekwa moja kwa moja kwa mama yake mdogo, aliyekuwa anaishi katika Wilaya ya Same, Mkoani Kilimanjaro. Sasa akawa ni mtu wa kutembea na kiti cha kukokotwa na magurudumu maalumu kwa walemavu. Akaanza sasa kuhangaika kwenda kwenye Makanisa ya Kilokole kwa ajili ya maombezi, akiweka matumaini huenda akafanyiwa miujiza na Wachungaji akapona na kuanza kutembea kama zamani. Akaamua rasmi kuokoka, kwa kuachana na starehe za dunia na kujiunga na makanisa ya Kilokole akiachana na dhehebu lake la Katoliki.

Upele ukawa umempata mkunaji, akawa hataki kusikia kuitwa jina la kifupisho la Recho, akawa anataka aitwe kiukamikifu jina lake la 'Rachel Francesco Gabriele'. Wapo wanaomfahamu tokea enzi zake wakambeza kuwa ng'ombe akivunjika mguu hana jinsi tena hurejea zizini, lakini Recho akayapuuza maneno yao na kumshika Mungu kikamilifu. Akaanza kuuvaa tena mkufu wa shingoni aliopewa zawadi na bibi yake mzaa baba. Mkufu ambao ulikuwa na kidani chenye herufi ya kwanza ya jina lake 'R'. Mkufu ambao aliutelekeza kitambo kirefu tokea ahamie nchini Kenya na mpenzi wake wa zamani Martin Tenga. Nyumbani kwa mama yake mdogo pakageuka kama kanisa vile, Wachungaji wa kiroho wanapishana kumfanyia maombi. Recho akatubia dhambi zake zote, huku dhambi ya kumtelekeza mtoto wake Pesambili kwenye kituo cha watoto yatima ikiendelea kumtafuna moyoni. Akaweka nia kuwa pindi akipata nafuu atafanya ziara nchini Kenya kuulizia wapi alipo mtoto wake.

Alijua kuwa mtoto wake kama atakuwa hai, sasa atakuwa ni kijana mkubwa kabisa, ambaye amekosa mapenzi ya mama kwa asilimia 100%. Akawa anajijutia kwa kumpa uyatima usio na sababu mtoto wake hali ya kuwa ana wazazi wake waliohai. Siku zikasonga hali ya kuwa bado Recho hajaanza kutembea mwenyewe zaidi ya kuendelea kutumia kiti cha magurudumu ya kukokotwa.
[emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586]
Deborah alikuwa amebakisha mwizi miwili tu kuanza mitihani ya kumaliza elimu ya kidato cha 6. Kwa muda wa miaka 6 yote ya elimu ya Sekondari alisoma shule hiyo hiyo moja tu, ya 'Msalato Girls'. Alikuwa ni miongoni mwa wakongwe wa shule, tena mkongwe ambaye hajawahi kukanyaga likizo nyumbani hata siku moja tokea ripoti shuleni. Kama waswahili wasemavyo kuwa ukimuona nyani mzee ujue amekwepa mishale mingi, huyo ndio alikuwa Deborah, alipitia misukosuko mingi akiwa shuleni mpaka kuweza kufikia kidato cha 6. Kwanza miaka 6 yote, alikuwa hajakanyaga nyumbani akiogopa kurudi kwa Mjomba wake Kobelo. Pili Timammy baada ya kuonyeshwa utovu wa nidhamu na Deborah kwa kukataliwa ombi lake la kukubali kuolewa nae akimaliza elimu ya kidato cha 4, akakacha kulipa ada. Ikabidi Deborah aombe eneo pale shuleni la kulima bustani. Akawa analima mchicha halafu anauza mchicha kwa shule kwa ajili ya kulisha wanafunzi mboga za majani. Pesa alizokuwa analipwa akawa anapotumia kwa ajili ya ada na kujinunulia mahitaji yake mengine ya kujikimu. Sasa hamu yake ilikuwa ni kumaliza shule ili apate nafasi ya kurejea nyumbani kwao kwa Mjomba wake baada ya kupotezana nao kwa zaidi ya miaka 6.

Shauku yake kubwa ilikuwa ni kwenda kumuona mama yake mzazi amjulie hali yake. Kila alipokuwa anamuwaza mama yake machozi yalikuwa yanamtoka. Alikuwa hajui kama yupo hai au amefariki.
Siku ya sherehe ya mahafari ya wanafunzi wa kidato cha 6 ikawadia. Wanafunzi hao walikuwa wameshikwa na furaha chekwachekwa ya kumaliza elimu ya sekondari. Walijiona wameshakuwa wakubwa wakiwa wamebakiza miezi michache tu waanze ya Chuo Kikuu. Walikuwa wanajiona kama vile wameshakula ng'ombe mzima wamebakiza mkia tu. Deborah nae hakubaki nyuma, alikuwa na furaha sheshe kupita hata wanafunzi wenzake wote. Hii ni kutokana na kukaribia kufanikisha ndoto zake za kielimu. Deborah alijipara, akajikwatua na kupendeza vilivyo. Sherehe zilipoanza, Deborah ndio alikuwa kinara wa kuongoza kwaya ya shule inayotumbuiza mbele ya hadhira wakiwemo wageni waalikwa. Sauti yake nyororo na namna alivyokuwa ananengua mwili wake ilikuwa ni burudani tosha kwa kila mtu aliyehudhuria hafla ile. Mgeni rasmi alikuwa ni Mfanyabiashara mkubwa tu Jijini Dodoma, maarufu kwa jina la Mrs.Tonny. Alikuwa ni mama wa makamo ambaye alikuwa anamiliki maduka mbalimbali ya kuuza vito vya thamani. Pia alikuwa anamiliki machimbo ya madini ya Tanzanite huko Mererani, Arusha. Watu wengi walikuwa hawamfahamu mumewe mama huyo zaidi ya kumjua kwa jina la Mrs.Tonny. Ukafika wakati wa kugawa vyeti na kutoa tuzo kwa wanafunzi vinara wa masomo mbalimbali.

Deborah akageuka tena kuwa gumzo kutokana na kukomba zawadi zote za masomo ya Fizikia, Kemia na Hesabu. Walimu wake wanaofahamu undani wa maisha yake walijawa na furaha ya ajabu. Deborah wakati wote alikuwa analia machozi ya furaha kwa ushindi wa masomo hayo, akiwa amewaburuza wanafunzi wenzake wenye kupata mahitaji yote muhimu kwa wakati bila vikwazo vyovyote. "Nimefurahishwa sana na matokeo ya Bi.Deborah Kunambi, ninatoa ahadi ya kumpatia kibarua katika moja ya ofisi yangu mpya itakayofunguliwa Mjini Morogoro, pia ninatoa ahadi ya kumsomesha elimu ya Chuo Kikuu kwa kozi yoyote atakayochaguliwa" hayo yalikuwa ni sehemu ya maneno ya mgeni rasmi Mr.Tonny katika hotuba yake yaliyoibua shangwe na vigeregere katika ukumbi mzima.

Deborah ikabidi anyooshe mikono angani kumshukuru Mungu kwa baraka ya kupata kibarua Mjini Morogoro kitakachomfanya aweze kumtunza mama yake mzazi bila shida. Baada ya sherehe ile kwisha, msaidizi wa tajiri Mrs.Tonny, akampatia Deborah anuani za mawasiliano atakazozitumia kuwasiliana nao ili aweze kupangiwa kituo cha kazi mara tu akimaliza shule.
 
SEHEMU-39



Nimefurahishwa sana na matokeo ya Bi.Deborah Kunambi, ninatoa ahadi ya kumpatia kibarua katika moja ya ofisi yangu mpya itakayofunguliwa Mjini Morogoro, pia ninatoa ahadi ya kumsomesha elimu ya Chuo Kikuu kwa kozi yoyote atakayochaguliwa" hayo yalikuwa ni sehemu ya maneno ya mgeni rasmi Mr.Tonny katika hotuba yake yaliyoibua shangwe na vigeregere katika ukumbi mzima. Deborah ikabidi anyooshe mikono angani kumshukuru Mungu kwa baraka ya kupata kibarua Mjini Morogoro kitakachomfanya aweze kumtunza mama yake mzazi bila shida. Baada ya sherehe ile kwisha, msaidizi wa tajiri Mrs.Tonny, akampatia Deborah anuani za mawasiliano atakazozitumia kuwasiliana nao ili aweze kupangiwa kituo cha kazi mara tu akimaliza shule.

Baada ya siku kadhaa kupita wakaanza mitihani ya kumalizia elimu ya kidato cha 6. Walipomaliza tu mitihani Deborah himahima akaelekea zake Morogoro kwenda kuripoti kazini kisha akamuone mama yake mzazi kwa mara ya kwanza baada ya kupotezana na mama yake kwa baada ya miaka 6 kupita. Laiti angelijua madhila ya mbeleni yatakayomsibu, asilani asingethubutu kukanyaga Morogoro.

Yalimsibu matanga ya rohoni yaliyomsababishia aishie gerezani kwa muda usiojulikana. Yale yale yakajirudia, ya mbuzi masikini hazai, na kama akizaa basi atazaa tasa tu. Juhudi zote za Deborah katika masomo yake ili aje kuishi kivulini, akajikuta zinakwamishwa na mahasidi wasiomtakia heri katika maisha yake. Maisha yake kila siku yalikuwa yanazalisha idadi kubwa ya maadui kuliko marafiki.
[emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586]
Mwaka 2002, Deborah alivyoikanyaga tena Morogoro kwa mara ya pili tokea atoroke nyumbani kwa Mjomba, sasa ulikuwa ni Mji wa wajanja. Mabadiliko ya Mji yalikuwa ni makubwa mno ya kimaendeleo ndani ya kipindi kifupi tu cha takribani miaka 6. Watu wake nao walionekana kuwa wamenawiri na ni wenye kufurahia maisha. Kulikuwa na wanaume kwa wanawake wanaojua kuvaa, wapenda burudani na wanaojua kuzisaka pesa kwa hali na mali. Ni mji uliofikia viwango vya kuitwa kwa jina la 'Jiji kasoro bahari' kutokana na upatikanaji wa kila kitu kinachotakiwa kasoro uwepo wa Bahari Hindi tu.

Tajiri mwanamama Mrs.Tonny mfadhili mpya wa Deborah alikuwa ni mtu maarufu na mahashumu kwenye kila kona ya Mji wa Morogoro huku akiwa na nyumba za kifahari kwenye maeneo wanaoishi watu wazito ya Forest na Rock garden. Mitaa yote kuanzia Mafisa, Msufini, Kilakala, Ngoto, Kingo, Mlapakoro, Boma road, SUA, Vibandani, Relwe magorofani, Kigurunyembe, Madizini na kwingineko kote huko alikuwa anajulikana, usicheze na pesa sabuni ya roho, ukiwa nayo kila mtu atakunyenyekea na kukuheshimu kuanzia wakubwa kwa watoto wote watakuabudu. Deborah aliwekwa aishi kwenye moja ya nyumba yake Mrs.Tonny iliyoko maeneo ya Liti huku nyumba hiyo ikiwa na ulinzi madhubuti wa saa 24. Ndani ya nyumba hiyo aliwakuta wasichana wenzake wengine wawili ambao nao ni wafanyakazi katika shughuli za Mrs.Tonny. Walikuwa wanachukuliwa nyumbani na gari na kurudishwa toka kazini na gari. Inapofika mwishoni mwa juma, Bosi wake Mrs.Tonny anakuja kuwachukua na kwenda nao muziki kwenye viwanja mbalimbali vya starehe. Walikuwa wanabadilisha viwanja watakavyo, mara waende Shimoni Morogoro Hotel, wakati mwingine Rock Garden na maonyesho ya 'Forest Hill' ili mradi Deborah alikuwa anaishi maisha ya hali ya juu ambayo hajawahi kuyaishi tokea azaliwe.

Akamshukuru Mwenyezi Mungu kwa kumjaalia kuishi maisha ya ndoto zake mapema kabisa hata kabla hajamaliza Chuo Kikuu. Baada ya kupita muda wa wiki mbili tokea aanze kazi, akaomba ruhusa ya Siku 2 kwenda kuwasalimia ndugu na jamaa zake Kijijini Mikongeni. Mrs.Tonny akamruhusu kiroho safi kabisa huku akimtaka kuhakikisha Jumatatu asubuhi na mapema kuhakikisha anaripoti kazini. Akampatia na bakhshishi ya nakidi ya pesa za kushika mkononi kwa ajili ya matumizi ya hapa na pale. Deborah alifurahi mno, ikiwa ndio pesa yake ya kwanza kutia mkononi tokea aanze kufanya kazi kwa jasho lake mwenyewe. Deborah akapitia soko kuu la Mjini Morogoro na kununua masurufu ya kubeba nyumbani. Akanunua zake sukari, mchele, sabuni na bidhaa mbalimbali za nyumbani. Bila kusahau alinunua pia vitenge kwa ajili ya shangazi yake na binamu zake. Hakuwa tayari kulipiza ubaya kwa ubaya, bali alitaka kulipa ubaya kwa wema, ili Shangazi yake ajifunze kitu.

Deborah mawazoni mwake alitaka pindi akirudi kazini, aanze harakati za kutafuta chumba cha kupangisha ili amchukue mama yake aishi nae pamoja. Aliona kabisa kuwa wakati wa kumtunza mama yake umefika. Ingawa pia akawa anatafakari, kama akimchukua akaanza kuishi nae halafu ukifika muda wa kujiunga na Chuo Kikuu itakuwaje, nani atakaa kumtunza mama yake. Mawazo hayo yakamuingiza katika bahari ya fikra, akipanga na kupangua kichwani mwake. Baada ya kukamilisha mahitaji yake akaeleka stendi ya Daladala zinazoelekea Mzumbe kwa ajili ya kwenda nyumbani kwa Mjomba wake. Baada ya kupata nafasi kwenye Daladala hiyo, kitambo kifupi tu msafara wa kuelekea Mzumbe ukaanza. Njia nzima, Deborah alikuwa anawaza namna watakavyotazama uso kwa uso na Shangazi yake. Alipanga kuwangukia miguuni Mjomba na Shangazi yake kwa kuwaomba radhi kwa utovu wa nidhamu alioufanya wa kutoroka nyumbani. Matumaini yake ni kuwa watamsamehe na tena wakijua sasa anajitegemea mwenyewe na anashika pesa zake, heshima na adabu kwake itaongezeka maradufu. "Mikongeni Mikongeni...achia bodi, abiria piga chini mnauweka usiku...!" ilikuwa ni sauti ya kondakta wa Daladala iliyomshtua Deborah na kumfanya akurupuke hima hima kwenye kiti alichokuwa amekalia. Kondakta akamsaidia kushusha mizigo yake, kisha gari ile ikatimka zake.

Deborah akabakia amepigwa na bumbuwazi kwa muda akiwa haamini jinsi mazingira yalivyobadilika na kumbabaisha vilivyo. Akajongea pembeni ya duka moja jirani na barabara na kupumzika kwenye mti wenye kivuli kwa muda akiyasoma mazingira. Barabara yote ilikuwa imepigwa lami, huku nyumba nyingi zikiwa hazipo. Kijasho chembamba kikaanza kumvuja akiwa hayaamini macho yake kama kweli amepotea nyumbani kwao kabisa. Sehemu ambayo ameishi kwa zaidi ya miaka 10, akivijua vichochoro vyote lakini leo anarudi nyumbani haioni nyumba ya Mjomba wake wala za majirani zake.

"Habari za leo kaka, samahani, hapa zamani kulikuwa na nyumba nyingi tu sizioni imekuwaje?" aliuliza Deborah kwa yule huku akijitega kwa umakini kusubiria jibu. "Ahaaa...inaelekea dada ulipotea siku nyingi sana, kuna mradi wa barabara na bomba la maji ulipita hapa, wenye nyumba wakalipwa pesa za fidia na kuvunjiwa nyumba zao, yapata miaka 5 sasa...!" aliongea yule muuza duka huku akianza kuhudumia wateja wengine waliofika dukani pale. Jibu lile lilikuwa kama kaa la moto kwa Deborah, jasho jekejeke likaanza kumvuja mwilini, akiwa hayaamini masikio yake kwa kile alichokiita. "Kaka Unasemaje?...kwa hiyo wamekwenda wapi?" alijikuta Deborah anaropoka kwa sauti ya juu, huku akiwa anakaribia kutaka kulia machozi, alimuona kama ameongea Kichina. "Ndio hivyo hivyo ulivyosikia, sio jukumu kujua wapo wapi..!" alijibu yule muuza duka kwa hasira akionekana hapendwi kusumbuliwa tena. Deborah ikabidi asogee pembeni kiunyonge akiwa haamini anachokishuhudia na kukisikia, aliona kabisa lengo lake la kumuona mama yake mzazi limeota mbawa. Mawazo yake yakahamia kwa mama yake mzazi akianza kushikwa na hofu kama bado ni mzima wamehama nae au amefariki. Alikuwa hana be wala che kuhusu familia yake mahali ilipo hivi sasa.

Njaa ikaanza kumkamata vilivyo, ikabidi asogelee mkahawa wa eneo la jirani hapo hapo na barabara ili apate kifungua kinywa. Alipoingia akaukuta mkahawa umeshona watu kochokocho, kila mtu anapata staftahi awahi kwenye mizunguko yake ya kutwa. Deborah akaenda moja kwa moja kwenye meza iliyobakia tupu ikiwa na mtu mmoja tu mwanaume wa makamo. Alipofika Deborah akasalimiana na yule mwanaume kisha akavuta kiti na kumuita mhudumu. Mhudumu alipokuja, Deborah akaagizia vitafunwa na chai ya mkandaa. Kilichomshangaza Deborah ni kumuona yule kaka aliyekaa nae meza moja akiwa anamuangalia sana kwa kuibia, kwa kijicho upembe. Deborah hakujali sana, akajua ndio wanaume walivyo, tamaa zao zipo nje nje, alipoletewa chakula akaanza kukishambulia kama anafukuzwa kutokana na njaa aliyokuwa nayo.

Ilimchukua takribani dakika 10 kumaliza kifungua kinywa kile, akiwa ameshiba kifu kifaya. Alipokuja mhudumu kutaka kutoa vyombo na kuchukua pesa, yule kaka akavunja ukimya kwa kuongea na mhudumu. "Bili yake changanya na yangu ukate pamoja" aliongea huku akifungua pochi yake na kuchomoa noti ya shilingi elfu 5 na kumkabidhi mhudumu yule. Deborah akabakia amepigwa na butwaa, akiwa anatafakari iweje analipiwa chakula kirahisi tu na mtu asiyefahamu, hakupenda kabisa kuwa jeta, kama walivyozoea madada wa Mjini wanaopenda vya bwerere. Kengele ya tahadhari ikagonga kichwani mwake, hasa akikumbukia maneno aliyowahi kuambiwa na mama mlezi wake Koplo Marieta, ya kuwa Mjini hakuna kitu cha bure.

"Dada yangu usishtuke sana, mie nakufananisha ndio maana kila wakati nilikuwa nakukodolea macho, na ndio maana nimekulipia bili yako kuwa na amani" aliongea yule kaka kwa sauti ya kujiamini huku akisitisha maongezi kidogo na kuchomoa kijiti cha kuchokonolea meno kwenye kikopo chake cha plastiki kisha akaendelea na maelezo yake. "Wewe ulikuwa unaishi kwa Mzee Kobelo pale jirani na barabara ya sasa hivi au nakufananisha, maana jina lako nimelisahau" aliongea huku amemkazia macho Deborah, muonekano wake ulionyesha ni mtu matawi ya juu sio mwenye kipato cha kijungu jiko. "Ndio mimi wala hujakosea, wewe ni nani kwani?" alijibu Deborah kwa sura ya bashasha huku sasa akijiandaa kumfahamu yule mtu mgeni machoni mwake ambaye ameonyesha kumfahamu vilivyo, alishakubali shingo upande kulipiwa bili yake. "Mimi ni Alex mtoto wa Mwalimu Mwenda" alijitambulisha kwa ufupi huku akimpa nafasi Deborah ya kukumbuka. "Ahaaaaah...Alex kaka yake rafiki yangu Devota jamani, za masiku kaka yangu nilisha kusahau" aliongea Deborah kwa furaha sheshe akiwa sasa na shauku ya kufahamu mambo mengi yaliyopita hapo Kijijini kwao Mikongeni. "Usijali ni ngumu sana wewe kunikumbuka, mlikuwa wadogo sana kama sio wewe kuwa rafiki wa mdogo wangu Devota nisingekukumbuka kirahisi, sura yako ni ile ile kitoto wazungu wanasema una 'baby face'" aliongea huku akichomekea utani uliowafanya waangushe kicheko cha nguvu.

"Kwanza pole na msiba wa mama yako, nilisikia umefiwa na sasa mmehamia wapi baada ya nyumba yenu kuvunjwa?" alitoa taarifa ambayo iliuchanachana kabisa moyo wa Deborah, ilimjaza kimuyemuye cha nafsi na kumvuruga kabisa matumbo yake. Akaanza kuhema kimjusi kama mbwa koko aliyefukuzwa mitaani. Deborah akashindwa kujizuia, akajikuta anaangusha mchozi wa nguvu, wa kimyakimya kutokana na taarifa hiyo iliyomletea takilifu. "Pole sana, kuwa na subira ndio dunia ilivyo sisi sote ni wapita njia" aliongea kwa huzuni yule kaka akionyesha kujutia kwa maneno yake yaliyoamsha hisia hasi kwa Deborah. Deborah alitaka kukikisa maneno akawa anashindwa kuongea kitu kumuuliza nani aliyekata kamba, ikabidi ajikaze kisabuni mbele za watu mule mkahawani asije akachafua hali ya hewa, akapata nguvu sasa ya kumhoji vizuri huyo mama yake alifariki lini.

.Ikabidi ajieleze kinagaubaga kuwa alitoroka karibia miaka 6 iliyopita ndio anakanyaga tena hivi sasa, hivyo hajui hata walipohamia familia yake. Alex nae hakuwa na majibu ya kina ya nani haswa aliyefariki kati ya Shangazi mtu na mama yake mzazi, maana wengi walikuwa hawajawahi kumuona mama yake mzazi, na walikuwa wanajua Shangazi yake ndio mama yake mzazi. Kukata mzizi wa fitina, ikabidi yule kijana Alex ajitolee wafunge msafara mpaka makaburini wakaangalie kaburi. Kwa maelezo ya Alex ni kuwa huo msiba ulitokea mwaka juzi wakati yupo mwaka wa mwisho Chuo Kikuu cha SUA-Morogoro. Uzuri wake makaburini kutokea pale Mkahawani hapakuwa na umbali mrefu sana, wakaamua watembee kwa miguu tu. Mizigo yake Deborah aliamua kuomba ihifadhiwe hapo hapo mkahawani ataifuata baadae. Njia nzima Deborah alikuwa amejawa na wasiwasi usiomithilika, akiwa na hofu huenda kweli mama yake mzazi ameshatangulia jongomeo. Kijana Alex akawa anajitahidi kumnyamazisha na kumtia moyo kuwa hata kama kweli mama yake atakuwa amefariki basi huo hautakuwa ndio mwisho wa dunia, lazima agangamale.

Makaburi ya kuzikiana ukoo wa Kunambi yalikuwa upande wa kushoto karibia na Mbuyu, ukiingia tu ndani ya uzio wa kuzunguka makaburini hapo. "Hili ndio kaburi linaloonekana ni jipya, ila nashangaa hata halijajengewa" aliongea Alex wakati wanafanya speksheni ya kulitafuta kaburi alilozikwa mama yake. "Naanza kuamini aliyefariki ni mama yangu tu, ndio maana hata kujengea hawajakumbuka, hata msalaba walioupanda jina limefutika tayari" aliongea Deborah akiwa amepiga magoti mbele ya kaburi amejiinamia akiwa na huzuni furufuru nafsini mwake, mvua ya machozi inabubujika mashavuni mwake. "Deborah usilie sana, jikaze huzuni yako ndio yangu, twende turudi nyumbani tujipange namna ya kuwatafuta ndugu zako, hapo ndipo tutaupata ukweli wote" aliongea Alex kwa sauti ya kubembeleza, anampigapiga kwa upole mgongoni huku anamfuta machozi Deborah kwa kutumia hanchifu yake. Deborah akawa anajihisi faraja na raha ya ajabu, inayoupoza moyo wake kama umewekwa kwenye jokofu kutokana na maneno ya kubembelezwa toka kwa Alex. Kwa miaka 21 ya Deborah tayari alishaanza kushikwa na hisia za kupenda kwa mara ya kwanza katika maisha yake. Kwa upande wake nae Alex joto la huba nalo lilikuwa limeshamkamata vilivyo kwa Deborah akisubiria muda muafaka amfungukie.

Baada ya kitambo kifupi, wakaanza kuondoka na Alex, huku Deborah akiwa kama kondoo anafuata tu hajui anapopelekwa na Alex. Kwa hali aliyokuwa nayo Deborah kipindi hicho, alikuwa anamuona Alex ndio kama mkono wake wa kulia. Alex akaanza kumpunguzia machungu kwa kumsimulia habari za rafiki yake wa kufa na kutokana, Devota ambaye walipoteza mawasiliano na Deborah. Taratibu Deborah akaanza kurudi kwenye hali yake ya kawaida.
[emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586]
"Jisikie upo nyumbani Deborah, karibu sana..! " Alex alimkaribisha Deborah ndani ya nyumba yake anayoishi katika eneo la Chuo Kikuu Cha Mzumbe. Ilikuwa ni nyumba ndogo ya kisasa, yenye vyumba vitatu, choo na bafu, ukumbi na jiko ndani yake. Sebule hiyo ilikuwa imepambwa kwa mapambo yenye widadi yenye kumvutia mtu yoyote mwenye kubahatika kuikodolea macho. Zilikuwa ni nyumba daraja nambari wani maalumu kwa kuishi Wahadhiri wa Chuo hicho. Alex alikuwa ni mhadhiri msaidizi anayefundisha masomo ya Uchumi. Aliajiriwa Chuo hicho mara baada ya kumaliza Chuo Kikuu cha SUA akisomea mchepuo wa Uchumi Kilimo.

"Ahsante sana kaka Alex, shemeji yupo wapi aniletee maji ya kunywa" alijibu Deborah akiwa na kimuyemuye huku akichomekea swali lenye utani wa kweli akitaka kufahamu kama Alex anaishi peke yake au tayari ameshaoa. "Shemeji yako ndio amekuja leo rasmi, sasa ndio ameingia kwenye nyumba hii kwa mara ya kwanza" Alex hakulaza damu, akatumia fursa hiyo hiyo kujieleza kwa mafumbo. Deborah akaelewa Alex anachomaanisha akabakia kujing'ata vidole tu, anatafuna kucha zake anaangalia pembeni kwa aibu. Kweli Deborah alikuwa msichana mwenye maadili ya kale bado akitongozwa anakula kucha, wakati wasichana wenzake wa Mjini siku hizi hawali kucha wanakula pesa zako.

Alex hakutaka kuonyesha tamaa ya fisi, alikuwa anamuingiza taratibu kwenye mtego wake. Kabla hajamtamkia wazi nia yake ya kumfanya awe mchumba wake alitaka kwanza Kumchunguza Deborah kama kweli anafaa kuwa mke, ili akijiridhisha ndio amtamkie rasmi ombi la uchumba. Alex akanyanyuka sofani alipokuwa amekaa akaenda kuwasha runinga yake, na kuweka mkanda wa video wa sinema ya Kihindi. Kisha akarudi kwenye sofa wakaanza kuangalia kwa pamoja huku wakiwa wamekaa kwenye sofa moja, lenye uwezo wa kuwakalisha watu 3 kwa pamoja. Baada ya dakika kama 5 tu, Alex akaaga kwa Deborah. "Sasa niliacha kidogo, mie ngoja nikafue nguo zangu ili ziwahi kukauka si unajua kesho kutwa ni kazini" akazungumza Alex huku akiwa anasimama akianza kupiga hatua kuelekea bafuni. "Aaaaah...zima tu runinga yako, tutaenda kufua wote, nikakusaidie..!" aliongea Deborah nae huku akinyanyuka kumfuata Alex sako kwa bako. Alex akaanza kuchekea tumboni akiona Deborah tayari ameshafaulu mtihani namba moja, akionekana ni mke kweli anayefaa 'wife material' haonyeshi mikogo. Wakaanza kufua wote huku wakikumbushiana hadithi mbalimbali za kitambo cha nyuma, enzi wapo Kijijini.

Mpaka kufika muda wa saa 8:00 mchana, wakawa wameshamaliza kufua nguo. "Sasa twende tukajiandae tukale kule Mkahawani muda umeshakwenda tayari" Alex aliongea huku akielekea chumbani kwake. "Hapana, hatuwezi kwenda kula mkahawani kama wageni, bora tupike hapa hapa wenyewe" Deborah alipinga kwa nguvu zote, bila kufahamu kuwa anapewa majaribu na Alex. Baada ya mabishano mafupi, rai ya Deborah ikapita. Ikabidi ajiandae kuingia jikoni kukarangiza mapishi kwenye jiko la gesi. Alex kwa utundu wake tu makusudi akakorofisha mrija wa mtungi wa gesi unaoingia kwenye jiko, ili tu azidi kumpima Deborah, kama kweli anaweza kuvumilia shida. "Kama gesi imegoma ngoja niingie mtaani kuulizia mkaa tupike kwa jiko la mkaa" kuongea hivyo Deborah tayari alishadaka mfuko wa Rambo akachukua pesa juu ya kabati na kuingia mtaani. Alex akabaki na furaha sheshe akiwa amejiridhisha kuwa Deborah anafaa kuwa mke, shule haijambadilisha tabia yake.

Ndani ya dakika chache alizochomoka Deborah, Alex akaitwaa simu ya Deborah aina ya 'Twanga Pepeta' na kuanza kupekenyua meseji, akitarajia huenda akakuta meseji ya mapenzi. Lakini akajikuta anatoka hola bila kuambulia meseji yoyote ya mahaba, zaidi ya meseji za Bosi wake Mrs.Tonny na za wateja wake wa dukani. Alex kwa taftishi yake ya haraka haraka akajiridhisha kuwa Deborah ndio msichana anayefaa kuwa mchumba wake. Baada ya kama robo saa Deborah akarudi na mkaa wake, akakimbilia jikoni kwenda kupika huku akimuacha Alex anaangalia zake sinema sebuleni. Mpaka kufika saa 10 alasiri chakula kilikuwa tayari kipo mjini kinasitiriwa matumboni mwao. Walipomaliza kula, Alex akampisha Deborah chumbani kwake apumzike, yeye akabakia kujipumzisha sebuleni, huku wakipanga saa 12 jioni waingie mtaani kusaka taarifa za wapi alipohamia Mjomba Kobelo.

Deborah mawazoni mwake wakati yupo kitandani, yalijaa Alex tupu. Alimuona ni mwanaume ambaye ana elimu kubwa, ana kazi nzuri lakini hana maringo na hapendi umangimeza kama walivyo wanaume wengi wenye kipato walivyo. Akajiapiza kuwa Alex akimtamkia tu kuwa anampenda hatomzungusha kamwe, atamkubalia mara moja. Ghafla bin vuu Deborah akapitiwa na usingizi wa pono akiwa juu ya kitanda cha Alex.
[emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586]
Mr.Martin Tenga, alipotolewa gerezani kule Jijini Turin, alikuja kutupwa kwenye gereza lililopo ndani ya Mji wa Barletta. Mji ambao ni mdogo wenye wakazi wasiozidi laki moja, uliopo Kusini Mashariki mwa nchi ya Italia. Ndani ya gereza jipya, hali ya hewa ilimkataa kabisa Mr.Martin Tenga, kila siku zinavyosonga mbele afya yake ilikuwa inadorora. Vipimo vya kina vilipofanyika ikagundulika ana kansa ya ini 'Liver Cancer', hivyo sasa akawa kama Lori la kubeba mkaa, linavyokuwa tripu Shamba, tripu Gereji, na yeye akawa leo yupo gerezani kesho yupo hospitalini. Hali yake ilivyozidi kuwa mbaya akahamishiwa katika hospitali ya 'Ospedale Barletta'. Hapo ndipo alipokutana kwa mara ya pili na mtoto wake wa damu, 'Pesambili' au ukipenda 'Dr Trezguet'.

Pesambili alipangiwa kufanya mafunzo ya Udaktari kwa vitendo katika Mji wa Barletta. Lakini kutokana na umahiri wake, Wahadhiri wake wakamnyooshea mkono. Akawa anaachiwa kufanya mpaka upasuaji wa wagonjwa. Siku isiyo na jina akiwa kwenye mizunguko ya usiku wodini kuangalia maendeleo ya wagonjwa wake ndipo wakatiana machoni kwa mara ya pili. Pesambili alikuwa anapita kitanda kwa kitanda, kuangalia hali za wagonjwa wake. Alipofika kwenye kitanda cha Mr.Martin Tenga, akasita kuendelea na ziara yake kwa muda. "Amicoooo.....Amicoo....!" aliita Pesambili kumuita Mr.Martin Tenga, kwa furaha baada ya kuona chata ya mchoro wa mamba kwenye shingo ya Mr.Martin Tenga aliyojichora, alama ambayo Pesambili alikuwa anaiona mara kwa mara wakati anamsaidia kule sokoni, Turin. "Amicoooo...! " alijitahidi kujibu kwa tabu sana huku akipepesa macho kumuangalia huyo Daktari anayemuita rafiki kama anamfahamu vile. Pesambili akatabasamu na kuanza kumuongelesha huku akimkumbushia kuwa walionana gerezani kule Jijini Turin akiwa chumba kimoja na baba mlezi wake Mr.Lorenzo, pia akampasha kuwa walikuwa wanaonana sokoni, mara kwa mara Jijini Turin, akiwa kama ombaomba wa vyakula, na alikuwa yeye Pesambili anampa sana msaada. Mr.Martin Tenga akabakia anatabasamu kwa furaha baada ya kukumbuka wema wa Pesambili enzi anajifanyisha ni masikini mitaani kabla hajafungwa gerezani, akiwa haamini kama kweli yule mtoto wa shule ya msingi, mwana wa panopano, rafiki yake kipenzi leo ndio Daktari mbele yake.

Pesambili akasoma faili la mgonjwa yule ambaye ni baba yake wa damu ila tu hawajuani. Aliposoma faili lile inaonyesha ana kansa ya ini iliyotokana na unywaji wa pombe kali, hivyo anahitajika kufanyiwa upandikizaji wa ini "Liver Transplant". Haraka haraka akaagiza vipimo vya damu, mkojo na DNA vfanyike usiku huo huo. Pesambili akajiweka kwenye orodha ya watu watakaomtolea damu Mr.Martin Tenga, hivyo na yeye damu ikafanyiwa vipimo. Majibu ya vipimo vya damu na DNA ya Mr.Martin Tenga na Pesambili yalimshangaza sana, mtumishi wa maabara kwa jinsi yalivyorandana. Majibu ambayo yalithibitisha kuna nasaba ya damu baina ya Mr.Martin Tenga na Daktari Pesambili au ukipenda Dr.Trezguet. Ikabidi usiku huo huo aitwe Dr.Pesambili kule maabara afahamishwe kitu kilichogundulika kwa bahati nasibu. Pesambili akapatwa na gagaziko la moyo, akaamrisha waanze kurudia tena upya vipimo, majibu yakawa ni kama yale yale ya mwanzoni. Dr. Pesambili akawa sasa ana furaha sheshe iliyochanganyika na huzuni akiwa haamini anachokishuhudia pale hospitalini. Alikuwa anaona kinachotendeka mbele yake ni zaidi ya muujiza wa Mtume Musa kuipasua bahari ya Shamu kwa fimbo yake na kuwapitisha wana wa Israeli baharini. Vipimo vilishuhudia kabisa bila chenga kuwa Dr.Pesambili, baba yake ni huyu mgonjwa mahututi Mr.Martin Tenga.

Akaona ulikuwa ni mpango wa Mungu yeye kuamua kuchagua kufanya kazi kwenye Mji wa watu masikini wa Barletta, kumbe na baba yake yupo huku anateseka gerezani kwa ugonjwa. Mawazo mengi yalimsonga kichwani mpaka akifikiria kuwa siri ile ya kuwa Mr.Martin Tenga ni baba yake mzazi huenda baba yake mlezi Mr.Lorenzo alikuwa anaifahamu fika ila hakutaka kumwambia. Akazidi kujiuliza kuwa alikuwa anamficha kwa faida ya nani?. Na kama hawajuani kwanini walikuwa wanaishi chumba kimoja?. Je Mr.Lorenzo hakupata kusimuliwa chochote na Mr.Martin Tenga kuhusu mtoto wake aliyemtelekeza kwenye kituo cha yatima.
Kulipokucha tu, mgeni wa kwanza kumtembelea Mr.Martin Tenga alikuwa ni Pesambili. Kwa jinsi alivyomshuhudia baba yake akiwa kwenye mateso makali, alishindwa kujizuia kumwaga machozi, bila Mr.Martin kung'amua kuwa mtoto wake anamlilia. Dr.Pesambili akapata matumaini kuwa huenda mama yake mzazi nae yupo hai, ila swali jipya kichwani likaja kwanini walimtelekeza kwenye kituo cha yatima wakati yeye sio yatima?. Au walimnyanyapaa kwa sababu ya ulemavu wake wakaona atakuwa mzigo kwao?. Kadri alivyokuwa anawaza ndivyo alivyokuwa anashindwa kujizuia machozi yake yasimbubujike. Ikabidi Dr.Pesambili arudi ofisini kwake kwanza ili apate utulivu wa kujipanga namna atakavyokuja kuongea na baba yake, huku akijitambulisha rasmi kwake.

Akiwa katika hali ya huzuni na simanzi, ghafla Dr.Pesambili akaisikia kengele ya hali ya tahadhari imelia kwa zaidi ya mara tatu kuashiria kuna mgonjwa wa dharura anayehitaji huduma ya haraka kuokoa uhai wake. Ikabidi Dokta Pesambili akurupuke mbio mbio utasema swala anayemkimbia Simba nyikani, kwenda kuungana na Madaktari wenzake kwenda kutoa huduma na msaada kwa wahitaji bila kujali hali aliyo nayo. Tahamaki alichokiona baada ya kufika chumba cha dharura, kilimsababishia mapigo yake ya moyo yazidi kwenda mbio maradufu. Baba yake mzazi, Mr.Martin Tenga alikuwa yupo kwenye sakaratu mauti kitandani anapigania roho yake. Saa na wakati wowote alikuwa anaaga dunia, hakukuwa na njia yoyote ya kuokoa uhai wake. Dr.Pesambili hakuwa mtu wa kukata tamaa kirahisi akaanza kupambana, alikuwa anahangaika huku na kule kuhakikisha anajaribu kuokoa uhai wa baba yake. Lakini kama unavyo, jitihada haiwezi kushindana na kudra ya Mola, Mr.Martin Tenga akaaga dunia, akihitimisha safari yake ya uhai wa duniani. Dr.Pesambili alitoa kilio mithili ya mtoto mdogo aliyetelekezwa jangwani bila msaada wowote, ukichukulia amemjua baba yake halisi saa chache tu zilizopita halafu kabla hajajitambulisha kwa baba yake, wasameheane kiroho safi na kuelezwa asili yake baba yake ni wapi, ghafla tu bin vuu anakata kamba na kurejea jongomeo bila hata kusema kwaheri ya kuonana.

Alikuwa na uchungu mkubwa sana Madaktari na Manesi ambao tayari tetesi zilishawafikia juu ya uhusiano wa Dr.Pesambili na marehemu Mr.Martin Tenga iliwabidi wafanye kazi ya ziada kumpoza machungu ya kumpoteza baba yake mzazi. Watu wa gereza alilokuwa amefungwa Mr.Martin Tenga wakapewa taarifa juu ya msiba wa mfungwa wao, nao bila ajizi wakaja kuuchukua mwili ili wakausitiri kwa taratibu zao za kisheria. Dr.Pesambili ikabidi ajieleze kwa uongozi wa gereza kinagaubaga uhusiano wake na marehemu mpaka akaruhusiwa kushiriki mazishi ya baba yake. Baada ya mazishi kupita Dr.Pesambili akajaribu kufuatilia gerezani labda kuna mawasiliano ya ndugu wa karibu wa Mr.Martin Tenga yalihifadhiwa na marehemu ili aweze kuwasiliana nao, akaambulia patupu. Kwa kuwa muda wake wa mafunzo kwa vitendo ulikuwa umebaki miezi michache, akaona bora avumilie mpaka amalize ili awe huru kabisa kuanza uzinduzi rasmi wa kusaka ndugu zake wa damu. Msako usio na kikomo mpaka ahakikishe anawatia machoni ndugu zake wa damu. Na tumaini la pekee lililobakia ni baba yake mlezi Mr.Lorenzo. Kupitia Mr Lorenzo aliamini ataupata ukweli wa wapi alimtoa huko Afrika mpaka kumleta nchini Italia.
[emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586]
.
 
SEHEMU-39



Nimefurahishwa sana na matokeo ya Bi.Deborah Kunambi, ninatoa ahadi ya kumpatia kibarua katika moja ya ofisi yangu mpya itakayofunguliwa Mjini Morogoro, pia ninatoa ahadi ya kumsomesha elimu ya Chuo Kikuu kwa kozi yoyote atakayochaguliwa" hayo yalikuwa ni sehemu ya maneno ya mgeni rasmi Mr.Tonny katika hotuba yake yaliyoibua shangwe na vigeregere katika ukumbi mzima. Deborah ikabidi anyooshe mikono angani kumshukuru Mungu kwa baraka ya kupata kibarua Mjini Morogoro kitakachomfanya aweze kumtunza mama yake mzazi bila shida. Baada ya sherehe ile kwisha, msaidizi wa tajiri Mrs.Tonny, akampatia Deborah anuani za mawasiliano atakazozitumia kuwasiliana nao ili aweze kupangiwa kituo cha kazi mara tu akimaliza shule.

Baada ya siku kadhaa kupita wakaanza mitihani ya kumalizia elimu ya kidato cha 6. Walipomaliza tu mitihani Deborah himahima akaelekea zake Morogoro kwenda kuripoti kazini kisha akamuone mama yake mzazi kwa mara ya kwanza baada ya kupotezana na mama yake kwa baada ya miaka 6 kupita. Laiti angelijua madhila ya mbeleni yatakayomsibu, asilani asingethubutu kukanyaga Morogoro.

Yalimsibu matanga ya rohoni yaliyomsababishia aishie gerezani kwa muda usiojulikana. Yale yale yakajirudia, ya mbuzi masikini hazai, na kama akizaa basi atazaa tasa tu. Juhudi zote za Deborah katika masomo yake ili aje kuishi kivulini, akajikuta zinakwamishwa na mahasidi wasiomtakia heri katika maisha yake. Maisha yake kila siku yalikuwa yanazalisha idadi kubwa ya maadui kuliko marafiki.
[emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586]
Mwaka 2002, Deborah alivyoikanyaga tena Morogoro kwa mara ya pili tokea atoroke nyumbani kwa Mjomba, sasa ulikuwa ni Mji wa wajanja. Mabadiliko ya Mji yalikuwa ni makubwa mno ya kimaendeleo ndani ya kipindi kifupi tu cha takribani miaka 6. Watu wake nao walionekana kuwa wamenawiri na ni wenye kufurahia maisha. Kulikuwa na wanaume kwa wanawake wanaojua kuvaa, wapenda burudani na wanaojua kuzisaka pesa kwa hali na mali. Ni mji uliofikia viwango vya kuitwa kwa jina la 'Jiji kasoro bahari' kutokana na upatikanaji wa kila kitu kinachotakiwa kasoro uwepo wa Bahari Hindi tu.

Tajiri mwanamama Mrs.Tonny mfadhili mpya wa Deborah alikuwa ni mtu maarufu na mahashumu kwenye kila kona ya Mji wa Morogoro huku akiwa na nyumba za kifahari kwenye maeneo wanaoishi watu wazito ya Forest na Rock garden. Mitaa yote kuanzia Mafisa, Msufini, Kilakala, Ngoto, Kingo, Mlapakoro, Boma road, SUA, Vibandani, Relwe magorofani, Kigurunyembe, Madizini na kwingineko kote huko alikuwa anajulikana, usicheze na pesa sabuni ya roho, ukiwa nayo kila mtu atakunyenyekea na kukuheshimu kuanzia wakubwa kwa watoto wote watakuabudu. Deborah aliwekwa aishi kwenye moja ya nyumba yake Mrs.Tonny iliyoko maeneo ya Liti huku nyumba hiyo ikiwa na ulinzi madhubuti wa saa 24. Ndani ya nyumba hiyo aliwakuta wasichana wenzake wengine wawili ambao nao ni wafanyakazi katika shughuli za Mrs.Tonny. Walikuwa wanachukuliwa nyumbani na gari na kurudishwa toka kazini na gari. Inapofika mwishoni mwa juma, Bosi wake Mrs.Tonny anakuja kuwachukua na kwenda nao muziki kwenye viwanja mbalimbali vya starehe. Walikuwa wanabadilisha viwanja watakavyo, mara waende Shimoni Morogoro Hotel, wakati mwingine Rock Garden na maonyesho ya 'Forest Hill' ili mradi Deborah alikuwa anaishi maisha ya hali ya juu ambayo hajawahi kuyaishi tokea azaliwe.

Akamshukuru Mwenyezi Mungu kwa kumjaalia kuishi maisha ya ndoto zake mapema kabisa hata kabla hajamaliza Chuo Kikuu. Baada ya kupita muda wa wiki mbili tokea aanze kazi, akaomba ruhusa ya Siku 2 kwenda kuwasalimia ndugu na jamaa zake Kijijini Mikongeni. Mrs.Tonny akamruhusu kiroho safi kabisa huku akimtaka kuhakikisha Jumatatu asubuhi na mapema kuhakikisha anaripoti kazini. Akampatia na bakhshishi ya nakidi ya pesa za kushika mkononi kwa ajili ya matumizi ya hapa na pale. Deborah alifurahi mno, ikiwa ndio pesa yake ya kwanza kutia mkononi tokea aanze kufanya kazi kwa jasho lake mwenyewe. Deborah akapitia soko kuu la Mjini Morogoro na kununua masurufu ya kubeba nyumbani. Akanunua zake sukari, mchele, sabuni na bidhaa mbalimbali za nyumbani. Bila kusahau alinunua pia vitenge kwa ajili ya shangazi yake na binamu zake. Hakuwa tayari kulipiza ubaya kwa ubaya, bali alitaka kulipa ubaya kwa wema, ili Shangazi yake ajifunze kitu.

Deborah mawazoni mwake alitaka pindi akirudi kazini, aanze harakati za kutafuta chumba cha kupangisha ili amchukue mama yake aishi nae pamoja. Aliona kabisa kuwa wakati wa kumtunza mama yake umefika. Ingawa pia akawa anatafakari, kama akimchukua akaanza kuishi nae halafu ukifika muda wa kujiunga na Chuo Kikuu itakuwaje, nani atakaa kumtunza mama yake. Mawazo hayo yakamuingiza katika bahari ya fikra, akipanga na kupangua kichwani mwake. Baada ya kukamilisha mahitaji yake akaeleka stendi ya Daladala zinazoelekea Mzumbe kwa ajili ya kwenda nyumbani kwa Mjomba wake. Baada ya kupata nafasi kwenye Daladala hiyo, kitambo kifupi tu msafara wa kuelekea Mzumbe ukaanza. Njia nzima, Deborah alikuwa anawaza namna watakavyotazama uso kwa uso na Shangazi yake. Alipanga kuwangukia miguuni Mjomba na Shangazi yake kwa kuwaomba radhi kwa utovu wa nidhamu alioufanya wa kutoroka nyumbani. Matumaini yake ni kuwa watamsamehe na tena wakijua sasa anajitegemea mwenyewe na anashika pesa zake, heshima na adabu kwake itaongezeka maradufu. "Mikongeni Mikongeni...achia bodi, abiria piga chini mnauweka usiku...!" ilikuwa ni sauti ya kondakta wa Daladala iliyomshtua Deborah na kumfanya akurupuke hima hima kwenye kiti alichokuwa amekalia. Kondakta akamsaidia kushusha mizigo yake, kisha gari ile ikatimka zake.

Deborah akabakia amepigwa na bumbuwazi kwa muda akiwa haamini jinsi mazingira yalivyobadilika na kumbabaisha vilivyo. Akajongea pembeni ya duka moja jirani na barabara na kupumzika kwenye mti wenye kivuli kwa muda akiyasoma mazingira. Barabara yote ilikuwa imepigwa lami, huku nyumba nyingi zikiwa hazipo. Kijasho chembamba kikaanza kumvuja akiwa hayaamini macho yake kama kweli amepotea nyumbani kwao kabisa. Sehemu ambayo ameishi kwa zaidi ya miaka 10, akivijua vichochoro vyote lakini leo anarudi nyumbani haioni nyumba ya Mjomba wake wala za majirani zake.

"Habari za leo kaka, samahani, hapa zamani kulikuwa na nyumba nyingi tu sizioni imekuwaje?" aliuliza Deborah kwa yule huku akijitega kwa umakini kusubiria jibu. "Ahaaa...inaelekea dada ulipotea siku nyingi sana, kuna mradi wa barabara na bomba la maji ulipita hapa, wenye nyumba wakalipwa pesa za fidia na kuvunjiwa nyumba zao, yapata miaka 5 sasa...!" aliongea yule muuza duka huku akianza kuhudumia wateja wengine waliofika dukani pale. Jibu lile lilikuwa kama kaa la moto kwa Deborah, jasho jekejeke likaanza kumvuja mwilini, akiwa hayaamini masikio yake kwa kile alichokiita. "Kaka Unasemaje?...kwa hiyo wamekwenda wapi?" alijikuta Deborah anaropoka kwa sauti ya juu, huku akiwa anakaribia kutaka kulia machozi, alimuona kama ameongea Kichina. "Ndio hivyo hivyo ulivyosikia, sio jukumu kujua wapo wapi..!" alijibu yule muuza duka kwa hasira akionekana hapendwi kusumbuliwa tena. Deborah ikabidi asogee pembeni kiunyonge akiwa haamini anachokishuhudia na kukisikia, aliona kabisa lengo lake la kumuona mama yake mzazi limeota mbawa. Mawazo yake yakahamia kwa mama yake mzazi akianza kushikwa na hofu kama bado ni mzima wamehama nae au amefariki. Alikuwa hana be wala che kuhusu familia yake mahali ilipo hivi sasa.

Njaa ikaanza kumkamata vilivyo, ikabidi asogelee mkahawa wa eneo la jirani hapo hapo na barabara ili apate kifungua kinywa. Alipoingia akaukuta mkahawa umeshona watu kochokocho, kila mtu anapata staftahi awahi kwenye mizunguko yake ya kutwa. Deborah akaenda moja kwa moja kwenye meza iliyobakia tupu ikiwa na mtu mmoja tu mwanaume wa makamo. Alipofika Deborah akasalimiana na yule mwanaume kisha akavuta kiti na kumuita mhudumu. Mhudumu alipokuja, Deborah akaagizia vitafunwa na chai ya mkandaa. Kilichomshangaza Deborah ni kumuona yule kaka aliyekaa nae meza moja akiwa anamuangalia sana kwa kuibia, kwa kijicho upembe. Deborah hakujali sana, akajua ndio wanaume walivyo, tamaa zao zipo nje nje, alipoletewa chakula akaanza kukishambulia kama anafukuzwa kutokana na njaa aliyokuwa nayo.

Ilimchukua takribani dakika 10 kumaliza kifungua kinywa kile, akiwa ameshiba kifu kifaya. Alipokuja mhudumu kutaka kutoa vyombo na kuchukua pesa, yule kaka akavunja ukimya kwa kuongea na mhudumu. "Bili yake changanya na yangu ukate pamoja" aliongea huku akifungua pochi yake na kuchomoa noti ya shilingi elfu 5 na kumkabidhi mhudumu yule. Deborah akabakia amepigwa na butwaa, akiwa anatafakari iweje analipiwa chakula kirahisi tu na mtu asiyefahamu, hakupenda kabisa kuwa jeta, kama walivyozoea madada wa Mjini wanaopenda vya bwerere. Kengele ya tahadhari ikagonga kichwani mwake, hasa akikumbukia maneno aliyowahi kuambiwa na mama mlezi wake Koplo Marieta, ya kuwa Mjini hakuna kitu cha bure.

"Dada yangu usishtuke sana, mie nakufananisha ndio maana kila wakati nilikuwa nakukodolea macho, na ndio maana nimekulipia bili yako kuwa na amani" aliongea yule kaka kwa sauti ya kujiamini huku akisitisha maongezi kidogo na kuchomoa kijiti cha kuchokonolea meno kwenye kikopo chake cha plastiki kisha akaendelea na maelezo yake. "Wewe ulikuwa unaishi kwa Mzee Kobelo pale jirani na barabara ya sasa hivi au nakufananisha, maana jina lako nimelisahau" aliongea huku amemkazia macho Deborah, muonekano wake ulionyesha ni mtu matawi ya juu sio mwenye kipato cha kijungu jiko. "Ndio mimi wala hujakosea, wewe ni nani kwani?" alijibu Deborah kwa sura ya bashasha huku sasa akijiandaa kumfahamu yule mtu mgeni machoni mwake ambaye ameonyesha kumfahamu vilivyo, alishakubali shingo upande kulipiwa bili yake. "Mimi ni Alex mtoto wa Mwalimu Mwenda" alijitambulisha kwa ufupi huku akimpa nafasi Deborah ya kukumbuka. "Ahaaaaah...Alex kaka yake rafiki yangu Devota jamani, za masiku kaka yangu nilisha kusahau" aliongea Deborah kwa furaha sheshe akiwa sasa na shauku ya kufahamu mambo mengi yaliyopita hapo Kijijini kwao Mikongeni. "Usijali ni ngumu sana wewe kunikumbuka, mlikuwa wadogo sana kama sio wewe kuwa rafiki wa mdogo wangu Devota nisingekukumbuka kirahisi, sura yako ni ile ile kitoto wazungu wanasema una 'baby face'" aliongea huku akichomekea utani uliowafanya waangushe kicheko cha nguvu.

"Kwanza pole na msiba wa mama yako, nilisikia umefiwa na sasa mmehamia wapi baada ya nyumba yenu kuvunjwa?" alitoa taarifa ambayo iliuchanachana kabisa moyo wa Deborah, ilimjaza kimuyemuye cha nafsi na kumvuruga kabisa matumbo yake. Akaanza kuhema kimjusi kama mbwa koko aliyefukuzwa mitaani. Deborah akashindwa kujizuia, akajikuta anaangusha mchozi wa nguvu, wa kimyakimya kutokana na taarifa hiyo iliyomletea takilifu. "Pole sana, kuwa na subira ndio dunia ilivyo sisi sote ni wapita njia" aliongea kwa huzuni yule kaka akionyesha kujutia kwa maneno yake yaliyoamsha hisia hasi kwa Deborah. Deborah alitaka kukikisa maneno akawa anashindwa kuongea kitu kumuuliza nani aliyekata kamba, ikabidi ajikaze kisabuni mbele za watu mule mkahawani asije akachafua hali ya hewa, akapata nguvu sasa ya kumhoji vizuri huyo mama yake alifariki lini.

.Ikabidi ajieleze kinagaubaga kuwa alitoroka karibia miaka 6 iliyopita ndio anakanyaga tena hivi sasa, hivyo hajui hata walipohamia familia yake. Alex nae hakuwa na majibu ya kina ya nani haswa aliyefariki kati ya Shangazi mtu na mama yake mzazi, maana wengi walikuwa hawajawahi kumuona mama yake mzazi, na walikuwa wanajua Shangazi yake ndio mama yake mzazi. Kukata mzizi wa fitina, ikabidi yule kijana Alex ajitolee wafunge msafara mpaka makaburini wakaangalie kaburi. Kwa maelezo ya Alex ni kuwa huo msiba ulitokea mwaka juzi wakati yupo mwaka wa mwisho Chuo Kikuu cha SUA-Morogoro. Uzuri wake makaburini kutokea pale Mkahawani hapakuwa na umbali mrefu sana, wakaamua watembee kwa miguu tu. Mizigo yake Deborah aliamua kuomba ihifadhiwe hapo hapo mkahawani ataifuata baadae. Njia nzima Deborah alikuwa amejawa na wasiwasi usiomithilika, akiwa na hofu huenda kweli mama yake mzazi ameshatangulia jongomeo. Kijana Alex akawa anajitahidi kumnyamazisha na kumtia moyo kuwa hata kama kweli mama yake atakuwa amefariki basi huo hautakuwa ndio mwisho wa dunia, lazima agangamale.

Makaburi ya kuzikiana ukoo wa Kunambi yalikuwa upande wa kushoto karibia na Mbuyu, ukiingia tu ndani ya uzio wa kuzunguka makaburini hapo. "Hili ndio kaburi linaloonekana ni jipya, ila nashangaa hata halijajengewa" aliongea Alex wakati wanafanya speksheni ya kulitafuta kaburi alilozikwa mama yake. "Naanza kuamini aliyefariki ni mama yangu tu, ndio maana hata kujengea hawajakumbuka, hata msalaba walioupanda jina limefutika tayari" aliongea Deborah akiwa amepiga magoti mbele ya kaburi amejiinamia akiwa na huzuni furufuru nafsini mwake, mvua ya machozi inabubujika mashavuni mwake. "Deborah usilie sana, jikaze huzuni yako ndio yangu, twende turudi nyumbani tujipange namna ya kuwatafuta ndugu zako, hapo ndipo tutaupata ukweli wote" aliongea Alex kwa sauti ya kubembeleza, anampigapiga kwa upole mgongoni huku anamfuta machozi Deborah kwa kutumia hanchifu yake. Deborah akawa anajihisi faraja na raha ya ajabu, inayoupoza moyo wake kama umewekwa kwenye jokofu kutokana na maneno ya kubembelezwa toka kwa Alex. Kwa miaka 21 ya Deborah tayari alishaanza kushikwa na hisia za kupenda kwa mara ya kwanza katika maisha yake. Kwa upande wake nae Alex joto la huba nalo lilikuwa limeshamkamata vilivyo kwa Deborah akisubiria muda muafaka amfungukie.

Baada ya kitambo kifupi, wakaanza kuondoka na Alex, huku Deborah akiwa kama kondoo anafuata tu hajui anapopelekwa na Alex. Kwa hali aliyokuwa nayo Deborah kipindi hicho, alikuwa anamuona Alex ndio kama mkono wake wa kulia. Alex akaanza kumpunguzia machungu kwa kumsimulia habari za rafiki yake wa kufa na kutokana, Devota ambaye walipoteza mawasiliano na Deborah. Taratibu Deborah akaanza kurudi kwenye hali yake ya kawaida.
[emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586]
"Jisikie upo nyumbani Deborah, karibu sana..! " Alex alimkaribisha Deborah ndani ya nyumba yake anayoishi katika eneo la Chuo Kikuu Cha Mzumbe. Ilikuwa ni nyumba ndogo ya kisasa, yenye vyumba vitatu, choo na bafu, ukumbi na jiko ndani yake. Sebule hiyo ilikuwa imepambwa kwa mapambo yenye widadi yenye kumvutia mtu yoyote mwenye kubahatika kuikodolea macho. Zilikuwa ni nyumba daraja nambari wani maalumu kwa kuishi Wahadhiri wa Chuo hicho. Alex alikuwa ni mhadhiri msaidizi anayefundisha masomo ya Uchumi. Aliajiriwa Chuo hicho mara baada ya kumaliza Chuo Kikuu cha SUA akisomea mchepuo wa Uchumi Kilimo.

"Ahsante sana kaka Alex, shemeji yupo wapi aniletee maji ya kunywa" alijibu Deborah akiwa na kimuyemuye huku akichomekea swali lenye utani wa kweli akitaka kufahamu kama Alex anaishi peke yake au tayari ameshaoa. "Shemeji yako ndio amekuja leo rasmi, sasa ndio ameingia kwenye nyumba hii kwa mara ya kwanza" Alex hakulaza damu, akatumia fursa hiyo hiyo kujieleza kwa mafumbo. Deborah akaelewa Alex anachomaanisha akabakia kujing'ata vidole tu, anatafuna kucha zake anaangalia pembeni kwa aibu. Kweli Deborah alikuwa msichana mwenye maadili ya kale bado akitongozwa anakula kucha, wakati wasichana wenzake wa Mjini siku hizi hawali kucha wanakula pesa zako.

Alex hakutaka kuonyesha tamaa ya fisi, alikuwa anamuingiza taratibu kwenye mtego wake. Kabla hajamtamkia wazi nia yake ya kumfanya awe mchumba wake alitaka kwanza Kumchunguza Deborah kama kweli anafaa kuwa mke, ili akijiridhisha ndio amtamkie rasmi ombi la uchumba. Alex akanyanyuka sofani alipokuwa amekaa akaenda kuwasha runinga yake, na kuweka mkanda wa video wa sinema ya Kihindi. Kisha akarudi kwenye sofa wakaanza kuangalia kwa pamoja huku wakiwa wamekaa kwenye sofa moja, lenye uwezo wa kuwakalisha watu 3 kwa pamoja. Baada ya dakika kama 5 tu, Alex akaaga kwa Deborah. "Sasa niliacha kidogo, mie ngoja nikafue nguo zangu ili ziwahi kukauka si unajua kesho kutwa ni kazini" akazungumza Alex huku akiwa anasimama akianza kupiga hatua kuelekea bafuni. "Aaaaah...zima tu runinga yako, tutaenda kufua wote, nikakusaidie..!" aliongea Deborah nae huku akinyanyuka kumfuata Alex sako kwa bako. Alex akaanza kuchekea tumboni akiona Deborah tayari ameshafaulu mtihani namba moja, akionekana ni mke kweli anayefaa 'wife material' haonyeshi mikogo. Wakaanza kufua wote huku wakikumbushiana hadithi mbalimbali za kitambo cha nyuma, enzi wapo Kijijini.

Mpaka kufika muda wa saa 8:00 mchana, wakawa wameshamaliza kufua nguo. "Sasa twende tukajiandae tukale kule Mkahawani muda umeshakwenda tayari" Alex aliongea huku akielekea chumbani kwake. "Hapana, hatuwezi kwenda kula mkahawani kama wageni, bora tupike hapa hapa wenyewe" Deborah alipinga kwa nguvu zote, bila kufahamu kuwa anapewa majaribu na Alex. Baada ya mabishano mafupi, rai ya Deborah ikapita. Ikabidi ajiandae kuingia jikoni kukarangiza mapishi kwenye jiko la gesi. Alex kwa utundu wake tu makusudi akakorofisha mrija wa mtungi wa gesi unaoingia kwenye jiko, ili tu azidi kumpima Deborah, kama kweli anaweza kuvumilia shida. "Kama gesi imegoma ngoja niingie mtaani kuulizia mkaa tupike kwa jiko la mkaa" kuongea hivyo Deborah tayari alishadaka mfuko wa Rambo akachukua pesa juu ya kabati na kuingia mtaani. Alex akabaki na furaha sheshe akiwa amejiridhisha kuwa Deborah anafaa kuwa mke, shule haijambadilisha tabia yake.

Ndani ya dakika chache alizochomoka Deborah, Alex akaitwaa simu ya Deborah aina ya 'Twanga Pepeta' na kuanza kupekenyua meseji, akitarajia huenda akakuta meseji ya mapenzi. Lakini akajikuta anatoka hola bila kuambulia meseji yoyote ya mahaba, zaidi ya meseji za Bosi wake Mrs.Tonny na za wateja wake wa dukani. Alex kwa taftishi yake ya haraka haraka akajiridhisha kuwa Deborah ndio msichana anayefaa kuwa mchumba wake. Baada ya kama robo saa Deborah akarudi na mkaa wake, akakimbilia jikoni kwenda kupika huku akimuacha Alex anaangalia zake sinema sebuleni. Mpaka kufika saa 10 alasiri chakula kilikuwa tayari kipo mjini kinasitiriwa matumboni mwao. Walipomaliza kula, Alex akampisha Deborah chumbani kwake apumzike, yeye akabakia kujipumzisha sebuleni, huku wakipanga saa 12 jioni waingie mtaani kusaka taarifa za wapi alipohamia Mjomba Kobelo.

Deborah mawazoni mwake wakati yupo kitandani, yalijaa Alex tupu. Alimuona ni mwanaume ambaye ana elimu kubwa, ana kazi nzuri lakini hana maringo na hapendi umangimeza kama walivyo wanaume wengi wenye kipato walivyo. Akajiapiza kuwa Alex akimtamkia tu kuwa anampenda hatomzungusha kamwe, atamkubalia mara moja. Ghafla bin vuu Deborah akapitiwa na usingizi wa pono akiwa juu ya kitanda cha Alex.
[emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586]
Mr.Martin Tenga, alipotolewa gerezani kule Jijini Turin, alikuja kutupwa kwenye gereza lililopo ndani ya Mji wa Barletta. Mji ambao ni mdogo wenye wakazi wasiozidi laki moja, uliopo Kusini Mashariki mwa nchi ya Italia. Ndani ya gereza jipya, hali ya hewa ilimkataa kabisa Mr.Martin Tenga, kila siku zinavyosonga mbele afya yake ilikuwa inadorora. Vipimo vya kina vilipofanyika ikagundulika ana kansa ya ini 'Liver Cancer', hivyo sasa akawa kama Lori la kubeba mkaa, linavyokuwa tripu Shamba, tripu Gereji, na yeye akawa leo yupo gerezani kesho yupo hospitalini. Hali yake ilivyozidi kuwa mbaya akahamishiwa katika hospitali ya 'Ospedale Barletta'. Hapo ndipo alipokutana kwa mara ya pili na mtoto wake wa damu, 'Pesambili' au ukipenda 'Dr Trezguet'.

Pesambili alipangiwa kufanya mafunzo ya Udaktari kwa vitendo katika Mji wa Barletta. Lakini kutokana na umahiri wake, Wahadhiri wake wakamnyooshea mkono. Akawa anaachiwa kufanya mpaka upasuaji wa wagonjwa. Siku isiyo na jina akiwa kwenye mizunguko ya usiku wodini kuangalia maendeleo ya wagonjwa wake ndipo wakatiana machoni kwa mara ya pili. Pesambili alikuwa anapita kitanda kwa kitanda, kuangalia hali za wagonjwa wake. Alipofika kwenye kitanda cha Mr.Martin Tenga, akasita kuendelea na ziara yake kwa muda. "Amicoooo.....Amicoo....!" aliita Pesambili kumuita Mr.Martin Tenga, kwa furaha baada ya kuona chata ya mchoro wa mamba kwenye shingo ya Mr.Martin Tenga aliyojichora, alama ambayo Pesambili alikuwa anaiona mara kwa mara wakati anamsaidia kule sokoni, Turin. "Amicoooo...! " alijitahidi kujibu kwa tabu sana huku akipepesa macho kumuangalia huyo Daktari anayemuita rafiki kama anamfahamu vile. Pesambili akatabasamu na kuanza kumuongelesha huku akimkumbushia kuwa walionana gerezani kule Jijini Turin akiwa chumba kimoja na baba mlezi wake Mr.Lorenzo, pia akampasha kuwa walikuwa wanaonana sokoni, mara kwa mara Jijini Turin, akiwa kama ombaomba wa vyakula, na alikuwa yeye Pesambili anampa sana msaada. Mr.Martin Tenga akabakia anatabasamu kwa furaha baada ya kukumbuka wema wa Pesambili enzi anajifanyisha ni masikini mitaani kabla hajafungwa gerezani, akiwa haamini kama kweli yule mtoto wa shule ya msingi, mwana wa panopano, rafiki yake kipenzi leo ndio Daktari mbele yake.

Pesambili akasoma faili la mgonjwa yule ambaye ni baba yake wa damu ila tu hawajuani. Aliposoma faili lile inaonyesha ana kansa ya ini iliyotokana na unywaji wa pombe kali, hivyo anahitajika kufanyiwa upandikizaji wa ini "Liver Transplant". Haraka haraka akaagiza vipimo vya damu, mkojo na DNA vfanyike usiku huo huo. Pesambili akajiweka kwenye orodha ya watu watakaomtolea damu Mr.Martin Tenga, hivyo na yeye damu ikafanyiwa vipimo. Majibu ya vipimo vya damu na DNA ya Mr.Martin Tenga na Pesambili yalimshangaza sana, mtumishi wa maabara kwa jinsi yalivyorandana. Majibu ambayo yalithibitisha kuna nasaba ya damu baina ya Mr.Martin Tenga na Daktari Pesambili au ukipenda Dr.Trezguet. Ikabidi usiku huo huo aitwe Dr.Pesambili kule maabara afahamishwe kitu kilichogundulika kwa bahati nasibu. Pesambili akapatwa na gagaziko la moyo, akaamrisha waanze kurudia tena upya vipimo, majibu yakawa ni kama yale yale ya mwanzoni. Dr. Pesambili akawa sasa ana furaha sheshe iliyochanganyika na huzuni akiwa haamini anachokishuhudia pale hospitalini. Alikuwa anaona kinachotendeka mbele yake ni zaidi ya muujiza wa Mtume Musa kuipasua bahari ya Shamu kwa fimbo yake na kuwapitisha wana wa Israeli baharini. Vipimo vilishuhudia kabisa bila chenga kuwa Dr.Pesambili, baba yake ni huyu mgonjwa mahututi Mr.Martin Tenga.

Akaona ulikuwa ni mpango wa Mungu yeye kuamua kuchagua kufanya kazi kwenye Mji wa watu masikini wa Barletta, kumbe na baba yake yupo huku anateseka gerezani kwa ugonjwa. Mawazo mengi yalimsonga kichwani mpaka akifikiria kuwa siri ile ya kuwa Mr.Martin Tenga ni baba yake mzazi huenda baba yake mlezi Mr.Lorenzo alikuwa anaifahamu fika ila hakutaka kumwambia. Akazidi kujiuliza kuwa alikuwa anamficha kwa faida ya nani?. Na kama hawajuani kwanini walikuwa wanaishi chumba kimoja?. Je Mr.Lorenzo hakupata kusimuliwa chochote na Mr.Martin Tenga kuhusu mtoto wake aliyemtelekeza kwenye kituo cha yatima.
Kulipokucha tu, mgeni wa kwanza kumtembelea Mr.Martin Tenga alikuwa ni Pesambili. Kwa jinsi alivyomshuhudia baba yake akiwa kwenye mateso makali, alishindwa kujizuia kumwaga machozi, bila Mr.Martin kung'amua kuwa mtoto wake anamlilia. Dr.Pesambili akapata matumaini kuwa huenda mama yake mzazi nae yupo hai, ila swali jipya kichwani likaja kwanini walimtelekeza kwenye kituo cha yatima wakati yeye sio yatima?. Au walimnyanyapaa kwa sababu ya ulemavu wake wakaona atakuwa mzigo kwao?. Kadri alivyokuwa anawaza ndivyo alivyokuwa anashindwa kujizuia machozi yake yasimbubujike. Ikabidi Dr.Pesambili arudi ofisini kwake kwanza ili apate utulivu wa kujipanga namna atakavyokuja kuongea na baba yake, huku akijitambulisha rasmi kwake.

Akiwa katika hali ya huzuni na simanzi, ghafla Dr.Pesambili akaisikia kengele ya hali ya tahadhari imelia kwa zaidi ya mara tatu kuashiria kuna mgonjwa wa dharura anayehitaji huduma ya haraka kuokoa uhai wake. Ikabidi Dokta Pesambili akurupuke mbio mbio utasema swala anayemkimbia Simba nyikani, kwenda kuungana na Madaktari wenzake kwenda kutoa huduma na msaada kwa wahitaji bila kujali hali aliyo nayo. Tahamaki alichokiona baada ya kufika chumba cha dharura, kilimsababishia mapigo yake ya moyo yazidi kwenda mbio maradufu. Baba yake mzazi, Mr.Martin Tenga alikuwa yupo kwenye sakaratu mauti kitandani anapigania roho yake. Saa na wakati wowote alikuwa anaaga dunia, hakukuwa na njia yoyote ya kuokoa uhai wake. Dr.Pesambili hakuwa mtu wa kukata tamaa kirahisi akaanza kupambana, alikuwa anahangaika huku na kule kuhakikisha anajaribu kuokoa uhai wa baba yake. Lakini kama unavyo, jitihada haiwezi kushindana na kudra ya Mola, Mr.Martin Tenga akaaga dunia, akihitimisha safari yake ya uhai wa duniani. Dr.Pesambili alitoa kilio mithili ya mtoto mdogo aliyetelekezwa jangwani bila msaada wowote, ukichukulia amemjua baba yake halisi saa chache tu zilizopita halafu kabla hajajitambulisha kwa baba yake, wasameheane kiroho safi na kuelezwa asili yake baba yake ni wapi, ghafla tu bin vuu anakata kamba na kurejea jongomeo bila hata kusema kwaheri ya kuonana.

Alikuwa na uchungu mkubwa sana Madaktari na Manesi ambao tayari tetesi zilishawafikia juu ya uhusiano wa Dr.Pesambili na marehemu Mr.Martin Tenga iliwabidi wafanye kazi ya ziada kumpoza machungu ya kumpoteza baba yake mzazi. Watu wa gereza alilokuwa amefungwa Mr.Martin Tenga wakapewa taarifa juu ya msiba wa mfungwa wao, nao bila ajizi wakaja kuuchukua mwili ili wakausitiri kwa taratibu zao za kisheria. Dr.Pesambili ikabidi ajieleze kwa uongozi wa gereza kinagaubaga uhusiano wake na marehemu mpaka akaruhusiwa kushiriki mazishi ya baba yake. Baada ya mazishi kupita Dr.Pesambili akajaribu kufuatilia gerezani labda kuna mawasiliano ya ndugu wa karibu wa Mr.Martin Tenga yalihifadhiwa na marehemu ili aweze kuwasiliana nao, akaambulia patupu. Kwa kuwa muda wake wa mafunzo kwa vitendo ulikuwa umebaki miezi michache, akaona bora avumilie mpaka amalize ili awe huru kabisa kuanza uzinduzi rasmi wa kusaka ndugu zake wa damu. Msako usio na kikomo mpaka ahakikishe anawatia machoni ndugu zake wa damu. Na tumaini la pekee lililobakia ni baba yake mlezi Mr.Lorenzo. Kupitia Mr Lorenzo aliamini ataupata ukweli wa wapi alimtoa huko Afrika mpaka kumleta nchini Italia.
[emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586]
.
Tuko pamoja chief.
 
SEHEMU-40


️[emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586]
"Nikutakie kazi njema mpenzi wangu, mimi ngoja niwahi Kibaruani, leo nina kipindi saa 3:00 asubuhi, nakutegemea Jumamosi jioni utakuja tena nyumbani Mzumbe" aliongea Alex huku akimkumbatia kwa nguvu Deborah wakiwa tayari wameshashuka nje ya gari la Alex. "Nashukuru sana mpenzi, nikutakie kazi njema, ila nisamehe sana kwa yaliyotokea juzi usiku sio kusudi langu kabisa" aliongea Deborah huku machozi yakianza kumlengalenga akionekana kujutia tukio hilo alilolifanya nyumbani kwa Alex. "Usijali na ondoa mashaka tupo pamoja katika shida na raha, mwishoni mwa juma tutaanza kutafuta ufumbuzi wa tatizo lako, nimekusamehe kiroho safi" alijibu Alex huku akirudia kumkumbatia tena kwa mara ya pili na kuanza kumpeperushia mabusu motomoto mashavuni mwake Deborah. "Wewe malaya baridi unataka kazi kweli au umeshanogewa na mapenzi unataka ukawe kahaba tena? " ilikuwa ni sauti kali iliyojaa hasira furifuri toka kwa Bosi wa Deborah, Mrs.Tonny aliyekuwa amesimama meta chache kutoka waliposimama Deborah na Alex akiwachora mubashara namna wanavyo onyeshana mahaba hadharani. Sauti ile kutoka kwa mtu wa karibu na Deborah, anayoifahamu fika hata kama akiamshwa usiku wa manane, ilizua wahaka na mshituko mkubwa katika moyo wa Deborah, himahima akajipapatua kwa nguvu kutoka kwenye ya Alex na moja kwa moja akageuk kisha akapiga magoti na kuvikutanisha vidole vya viganja vyake vya mkono pamoja na kuviweka chini ya kidevu chake. "Samahani sana Madame...nipo chini ya miguu yako sirudii tena kuzembea kazini, nisamehe....! " aliongea Deborah kwa sauti iliyojaa uoga na majuto huku akitambaa kwa magoti kumfuata Bosi wake Mrs.Tonny pale alipokuwa amesimama. "Wewe kijana potea haraka kwenye upeo wa macho yangu kabla sijakutwanga risasi, mpumbavu wewe na kigari chako cha mkopo unataka kuniharibia binti yangu...!" aliendelea kufoka Mrs.Tonny huku kibao sasa kikimgeukia kijana Alex, akiwashiwa moto wa shari. Kwa mkwara tu, Mrs.Tonny akachomoa bastola yake kwenye pochi yake, na kutishia kama anataka kupiga risasi kwenye tairi ya upande wa kushoto wa gari akachimba chini jirani na tairi. Alex haraka haraka akaingia kwenye gari yake akaiwasha na kutokomea zake kwa kasi kubwa kusipojulikana akiwa na kiwewe akiepuka shari kamili inayomnyemelea. "Wewe mjinga unanidanganya unaenda kuangalia familia yako, kumbe unaenda kukutana na mahawara zako, hapa Mjini kuwa makini, ukimuona kijana anamiliki gari tu tayari umeshampapatikia, unataambukizwa UKIMWI shauri yako mpumbavu wewe, haya fungua duka mie naondoka zangu...! " alifoka Mrs.Tonny huku akimrushia funguo za duka hilo la vito Deborah na kuanza kupiga hatua kadhaa kuelekea kwenye gari lake kisha akasita kwenda na kugeuka nyuma. "Ebu lete hiyo simu yangu, maana hiyo simu ndio inakufanyia ukuadi na kuhangaika na viruka mito wako" aliongea huku tayari akiwa ameshafika alipo Deborah. Bila ubishi wowote akasalimisha simu kwa Mrs Tonny huku akiwa amejawa na aibu na soni hana hata ujasiri wa kumuangalia usoni mfadhili wake. Kiunyonge akajivuta na kumkabidhi funguo mlinzi amsaidie kufungua geti la dukani. Machozi yalikuwa yanambubujika usoni Deborah akiona kabisa Mrs.Tonny anamuonea na kumletea mtima nyongo kwenye penzi lake jipya ambalo ndio kwanza ameanza kupanda mbegu za upendo hata kuchipua bado. "Sasa nina miaka 21, sio mwanafunzi na nina haki ya kuwa na rafiki ninayemtaka mimi sasa iweje aniporomoshee matusi ya nguoni mimi na mpenzi wangu Alex, au ana ajenda gani ya siri dhidi yangu? Sasa Alex si anaweza kughairisha kunichumbia, na ukichanganya na kituko cha aibu nilichomfanyia Alex Jumamosi usiku ndio kabisa atatafuta mchumba mwingine" hayo yalikuwa ni baadhi tu mawazo ambayo yanapita kichwani mwa Deborah kipindi chote alichokuwa anasubiri milango ya duka ifunguliwe. Kwa ufupi siku nzima ya Deborah ilikuwa imeharibika, kwa kujawa na soni na simanzi kubwa moyoni mwake. Aliona kabisa mfadhili kaamua kumpanda kichwani kwa makusudi na kutia mchanga kwenye kitumbua cha penzi lake. Mpaka akawa anajiuliza huenda Bosi wake kaamka vibaya leo kuna kitu kinamvuruga, kwa maana tokea wameanza kufanya kazi pamoja hajawahi hata kumkemea lakini leo bila kosa lolote mpaka anafikia hatua ya kuchomoa bastola hadharani na kurusha risasi. Siku hiyo hata chakula hakuwa na hamu nacho kabisa, hisia za njaa tumboni mwako ziliyeyuka kabisa, akageuka kama mfungaji wa swaumu. Akaanza kufikiria hali ya mpenzi wake Alex huko alipo. Akaanza kumuonea huruma kwa kuingizwa kwenye matatizo yasiyo mhusu. Akakumbuka jinsi siku za Jumamosi na Jumapili Alex alivyojitoa mhanga kwake kumsaidia kuwasaka ndugu zake kwa udi na uvumba bila kuchoka. Juhudi ambazo zilikuwa tasa hazikuzaa matunda kwa maana hawakufanikiwa kufahamu wapi alipoelekea Mjomba Kobelo na familia yake. Saa za kufunga duka siku hiyo alikuwa anaziona zinaenda taratibu sana kwa mwendo wa kinyonga. Kwa amri yake alitamani afunge sasa hivi akajipumzishe zake hasa ukichukulia yupo kwenye kizungumkuti cha kutofahamu kama mama yake mzazi yu hai au amefariki, pia hajui alipo Mjomba wake na familia yake halafu Bosi wake Mrs.Tonny anamletea maswaibu mengine mapya ya kutaka kumpeperushia ndege mnana wake, Alex. Ilipofika saa 1:30 usiku gari linalotumika kuwarudisha nyumbani likawasili dukani kwa Deborah kuja kumchukua. Alikuwa tayari ameshafunga mahesabu ya siku hiyo, hivyo harakati za kufunga mlango wa duka zikaanza. Baada ya dakika 10 akawa ameshafunga duka na kumkabidhi funguo za duka dereva wa Bosi wake tayari kwa kurejea nyumbani. Kwenye gari walikuwa watu 4 kama kawaida, dereva na waliobaki ni wasichana wauzaji wa maduka ya Bosi wao Mrs.Tonny. Siku hiyo kadri walivyokuwa wanataniana Deborah alikuwa mtulivu tuli kama maji mtungini, kichwani ameshavurugwa. Walipofika nyumbani Deborah akapitiiza moja kwa moja mesini kula mlo wa chajio, usiku mbichi ulikuwa tayari umetimu. Mtumishi wa nyumba alikuwa tayari ameshapika chakula na kurejea kwao. Alipokula tu moja kwa moja akaenda kuoga na kujifungia zake chumbani kwake. Usingizi siku hiyo ulimpaa kabisa hautaki kuja, mawazo yote yapo kwa Alex. Alifahamu fika huenda hivi sasa Alex anamtafuta kupitia simu yake ya mkononi, lakini anaona kimya tu bila kufahamu kuwa simu amepokonywa na Bosi wake.
[emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3585][emoji3586]
SURA YA KUMI NA TANO
"Habari za kazi, nimekuja kumuulizia ndugu yetu anaitwa Deborah Kunambi..! " aliongea kwa kujiamini dereva wa mfanyabiashara Timammy aliyetumwa kumuulizia Deborah huku Timammy mwenyewe akiwa amebakia kwenye gari. "Hee...kumbe yule Deborah ana ndugu wenye uwezo eeh, sie tukimjua ni fukara mwenzetu tu, maana ana muda mrefu hajawahi kurudi kwao likizo....! " alijibu yule mlinzi wa getini huku macho yake akiyaelekeza kwenye kukagua daftari lake kuangalia wanafunzi ambao wameshaondoka tayari shuleni, kwa wale waliomaliza shule na wanaosafiri likizo. "Yule kiburi chake tu, ndugu anao sema mjeuri tu..! " akaongopa yule dereva kuanua ngoma juani. " Ndio kawaida ya watoto wenye akili nyingi wanakuwa na misimamo sana. Hapa inaonyesha ameshachukuliwa saa mbili zilizopita, angalia hii anuani" aliongea yule mlinzi huku akimkabidhi yule dereva kikaratasi alichokiandika jina na anuani ya mtu aliyemchukua Deborah shuleni. "Oooh....sawa huku Morogoro ni kwa ndugu zake upande wa baba akina Kunambi, lakini hatukuwasiliana nao...!" aliongopa yule dereva huku akichukua kile kikaratasi na kuagana haraka haraka na yule mlinzi. "Kaka hata ya chai huachi kidogo, maana mie nimekusaidia tu ulitakiwa uende kule kwa Mwalimu wa zamu, si unaona mnyororo wa wazazi waliowafuata watoto kule.....! " alijichekesha yule mlinzi akiomba pesa kwa dereva wa Predeshee Timammy huku akimuonyesha kwa kidole mstari wa wazazi katika ofisi ya Mwalimu wa zamu. Yule dereva bila hiana wala kutia neno akachomoa mfukoni noti ya shilingi 500/= akamkabidhi mkononi. Yule mlinzi alishukuru kweli kutokana na ukata uliokuwa unamkabili, utasema amepewa kipande cha almasi kumbe mia 5 tu. "Ngoma ishakuwa ngumu Bosi, kinda Deborah kashachurupuka...!" aliongea dereva kiunyonge huku ameegemeza kichwa chake kwenye kiti chake cha dereva, wakati anamkabidhi kikaratasi chenye anuani ya mtu aliyeondoka na Deborah pale shuleni. "Uuuuuuhhh......Shabaashi..! usimwambie, kashanizidi ujanja..! Huyu Binti piga ua ni wangu, mie siwezi oa mwanamke mwingine zaidi yake, natambua kuwa nimempita zaidi ya miaka 10 taslimu lakini yule ana mvuto fulani utakaonituliza mimi, kwa njia yoyote Deborah atakuwa mke wangu tu, siwezi kukubali mtu yoyote anizidi kete kwa Deborah" alijikuta anaropoka kwa hasira Predeshee Timammy akijiapiza kumpata Deborah. Dereva wake akabakia amepigwa na butwaa mdomo wazi, akijiuliza haswa huyu Bosi wake kapatwa na mswaibu gani haswa mpaka haoni wala hasikii kwa binti wa shule. Deborah kwa upande wake alishamsahau Timammy tokea amfurushe siku aliyomtongoza kule shuleni alipomtembelea. Alijua Timammy ameshakoma kumfuatilia na ilishapita takribani miaka 3 bila kusikia chochote toka kwake na ada alishakata mguu kumlipia akajua ameshakasirikiana nae kimoja. Kumbe mwenzake bado alikuwa yupo kichwani mwake anampigia mahesabu makali. Hesabu ya kwanza alipiga kuwa Deborah atakuwa ameishi maisha magumu sana shuleni, na matokeo ya kidato cha 4 yalivyotoka alivyoona kachaguliwa pale pale akajua sababu kubwa ni ya kiuchumi. Hivyo akajua atakapomaliza kidato cha 6 atakuwa hana pa kufikia hivyo atamnyakua kiulaini kama mwewe kwa kifaranga cha kuku. Lakini kumbe karata namba moja imeshafeli sasa alitakiwa achange upya karata zake, ndani ya Mji wa Morogoro, ajue wapi alipo Deborah amchomoe. "Sasa Bosi tunafanyaje, maana humo hata namba ya simu haipo, labda tuulizie hilo sanduku la posta lililoandikwa hapo mmiliki wake ni nani" aliongeleshwa Timammy na dereva wake baada ya kuonekana ametulia kimya muda mrefu anavusha mawazo. "Yap.. Yap..hapo umeongea jambo la msingi ndio maana nimekufanya uwe dereva wangu kwa sababu wewe ni mwerevu mno, sasa hiyo kazi nitamkabidhi wakala wangu mmoja anafanya kazi Shirika la Posta, makao makuu, akishaleta jibu sasa huyo aliyemchukua mpenzi wangu Deborah nitapambana nae kwa jasho na damu" alikuwa anaongea Timammy kwa msisitizo huku anapigapiga ngumi pembeni ya mlango wa siti ya abiria. Yule dereva bichwa lilivimba kwa misifa aliyomwagiwa, maana hiyo kazi ya ukuwadi kwa Mabosi wao ndio ilikuwa moja ya njia ya kuongeza kipato cha ziada kwa baadhi ya madereva wasiojitambua kama yeye. Baada ya muda mfupi, safari ya Timammy kurejea Jijini Dar es Salaam ikaanza, lakini akiwa ni mnyonge kupitiliza hasa kutokana na kuzidiwa kete. Walikuwa wamechoma mafuta kwenye gari toka Jijini Dar es Salaam mpaka Dodoma umbali wa zaidi kilometa 450 bila mafaniko yoyote. Ndio akakumbuka ule msemo wa vijana wa mitaani kuwa wakati unasubiri embe liive ndio uchume, wenzako wanalila hivyo hivyo likiwa bichi kwa kutumia chumvi. Ndio yaliyomtokea kwa Deborah, kamsubiria apevuke, wajanja wameshamdaka juu kwa juu. Usilolijua ni kama usiku wa giza, Alex alikuwa anaenda kutumbukia kwenye janga zito la kupambana na watu wenye pesa zao, kisa ni penzi la Deborah. Kibaya zaidi Timammy amekulia kwenye mfumo wa maisha ya kijiweni yaliyojaa kina aina ya uharamia, ghiriba na ukhabithi, yeye kwake suala la kumwaga damu ya mtu anapolitaka jambo lake ni dakika sifuri tu.
[emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586]
"Mtumiaji wa simu unayempigia hapatikani kwa sasa, jaribu tena baadae, ahsante" ilikuwa ni sauti ya mwanadada inayotoka kwenye mtandao wa simu ikimuelezea Alex kuwa simu ya Deborah imezimwa haipo hewani. Alex alizidi kuchanganyikiwa majira hayo ya akakiri akiwa ametulizana tuli sebuleni kwake kwa utulivu murua utasema anaaga maiti. Muonekano wa nje alikuwa anaonekana ametulia lakini ndani ya serikali ya kichwa chake kulikuwa na mkururu wa mawazo kinzani yanapita kama mkondo wa maji yanayotumika toka sehemu moja kwenda ingine. Chambilecho mwenye kupenda ni jura wala hana maarifa na mwenye kupenda hana usono asijapopata akitamanicho, hiyo ndio hali aliyokuwa amekumbwa nayo kijana Alex. Kilichokuwa kinampa mawazo zaidi si kingine bali ni mustakabali wake na Dendesha katika safari ya penzi lao jipya ambalo limeanza na mkosi. Hasa akikumbukia tukio la tishio la kutaka kupigwa risasi na mama mfadhili wa Deborah asubuhi asubuhi na mapema. Katika maisha yake Alex hajawahi hata kutishiwa maisha na kitu chochote hata mithili ya kuchanjwa na wembe achilia mbali risasi. Kisanga cha kuchomolewa mguu wa kuku hadharani na Mrs.Tonny kilimsababishia cheche za mkojo zilowanishe nguo yake ya ndani, na kumfanya akimbize gari lake kuelekea kusikojulikana kutokana na kiwewe. Fahamu zilikuja kumkaa sawa ma kujishtukia yupo Dakawa anaelekea Jijini Dodoma, wakati alitakiwa ashike uelekeo wa barabara ya Iringa ili aweze kufika kijijini Mzumbe anapoishi na kufanya kazi. Mpaka kufanya maamuzi ya kushika njia sahihi itakayompeleka nyumbani kwake tayari majira ya mafungulia ng'ombe yalishatimu na kipindi chake darasani kilishamkosa bila kutoa taarifa yoyote ofisini na kwa wanafunzi wake hali ambayo ilizusha taharuki kutaka kufahamu amepatwa na maswahibu gani. Alipopigiwa simu ikabidi adanganye kuwa hajisikii vizuri vizuri kuacha, ni mahamumu hivyo alijihimu Morogoro Mjini kupata vipimo kwa ajili ya kupatiwa matibabu. Moja kwa moja akapitiliza maskamoni kwake na kuanza kutuma meseji kwenye simu ya Deborah kutaka kufahamu mkasa wao umeishiaje. Lakini kitu cha kustaajabisha kwa upande wake meseji zote zaidi ya 8 alizotuma zilifikia, kuonyesha bado hazijapokelewa upande wa pili. Ndipo apofanya maamuzi ya kuanza kumpigia simu kujua kulikoni, jibu alilokuwa analipata kutoka kwenye simu yake ni sauti nyororo ya msichana inayosema "Mtumiaji wa simu unayempigia hapatikani kwa sasa, jaribu tena baadae, ahsante". Jibu ambalo lilikuwa linazidi kuvuruga na kuzalisha cheche za wahaka katika moyo wake. Kijasho chembamba cha uoga wa kuwa huenda penzi lao tamu la siku mbili tu ndio limefikia tamati. Penzi ambalo ndio kwanza limepandwa mbegu yake hata kuchipua bado, tayari limeshapigwa zongo na Mrs.Tonny, mfadhili wa muhibu wake Deborah. "Huenda Deborah kasikiliza ushauri wa mfadhili wake kuwa mimi ni bangai tu, mbabaishaji, tapeli wa Mjini wa mapenzi, hivyo kaungana nae, hivyo Deborah ameamua kuifukua mbegu ya penzi letu ili lisiote kabisa" alikuwa anawaza kijana Alex akiwa ameshika tama juu ya sofa lake pale sebuleni. Hali ya hewa ilikuwa ni baridi msimu huo wa kipupwe lakini jasho jekejeke lililokuwa linalomtiririka Alex utasema ni mtumishi wa tanuri la kuchoma mikate yupo jikoni anafanya mambo yake. "Huenda mfadhili wake kaamua kumpokonya simu yake na kuizima ili asiweze kamwe kuwasiliana na mimi kwa njia ya simu ya mkononi" alizidi kuwaza Alex dhana tofautitofauti dhana ambazo badala ya kumletea faraja ya moyoni zilizidi kumletea masumbuko yasiyo na mwisho. "Pia huenda ameamua kumpokonya simu na kumtimua kazi" aliwaza tena lakini dhana hii serikali ya kichwa cha Alex ikaipinga kwa nguvu zote, kwa hoja ya kwamba, kama Deborah angekuwa ametimuliwa kwa Mrs.Tonny basi kimbilio lake la pekee kwa Mjini Morogoro angekuwa ni yeye Alex kutokana na kutokufahamu wapi walipo ndugu zake mpaka sasa. "Ila anaweza kufukuzwa na mfadhili wake na kwangu asitie mguu kabisa, kutokana na kituko cha kujikojolea usiku wa kuamkia Jumapili niilipompisha alale kitandani kwangu na mimi kwenda kulala chumba cha wageni. Huenda tukio hilo limemsononesha sana na kuona ya kuwa limemvunjia hadhi na heshima yake, hivyo ameona bora ajihukumu mwenyewe kwa kuvunja penzi letu" aliendelea na mawazo yake kinzani. "Ila atakuwa wa ajabu basi kama ukikojozi wake ndio umemfanya avunje penzi letu, maana mimi nimemsamehe siku ile ile baada ya kunisimulia ni tatizo linalojirudia rudia kwake kutokana na kushuhudia sura ya mmoja wa Majambazi wauaji wa marehemu baba yake". Mawazo hayo yalikatishwa na kishindo kilichosikia kupitia mlango wa uani, kishindo mfano wa mtu aliyegonga mlango na kumfanya Alex akurupuke mbiombio toka sebuleni kwenda kujua kulikoni. "Huenda Deborah amefukuzwa, ameamua kuhamia rasmi nyumbani kwangu na mabegi yake, kaamua apite mlango wa uani kwa kuona aibu kwa watu kupitia mlango wa barazani" hizo ndio fikra za Alex wakati anachomeka funguo kufungua mlango wa uani. Alipofungua akabaki amepigwa na butwaa hana la kufanya, kumbe kIlikuwa ni kishindo cha paka wawili wa nyumba za jirani wanaogombania mabaki ya chakula cha usiku kwenye pipa la taka nje ya nyumba yake. Kinyonge akawa hana namna zaidi ya kuufunga tena mlango wake na kurejea sebuleni akiwa amekosa raha na buraha. Kabla hajakaa chini ndipo akakumbuka tumboni hajatia chochote tokea alivyoamka asubuhi na kuwahi kumkimbiza kazini kwake Deborah. Kabla hajakaa akageuka na kupitiliza uelekeo wa jikoni kwenda kuangalia chochote kitu kwenye jokofu lake la kuhifadhia vyakula anuwai mbalimbali. Alipofungua akakutana na maziwa freshi mabichi na robo tatu ya slesi za mkate ukiwa umefungwa vizuri. Akawasha jiko la gesi na kubandika sufuria la kuchemshia maziwa. Baada ya dakika takribani 3 maziwa yakawa tayari yamechemka. Akayamimina kwenye chupa ya kuhifadhia joto la vimiminika, akaweka mezani. Akachukua silesi 6 za mkate na kuanza kuzipaka siagi tayari kwa kula. Baada ya dakika kama 10 akawa tayari ameshashiba, alipotupia macho kwenye saa yake ya mkononi aliyoivaa akaona majira ya adhuhuri yameshatimu. Akakata shauri kuwa hicho kifungua kinywa alichokula ndio pia mlo wake wa mchana, hana haja tena ya kupika itakuwa ni ulafi kama akipika tena. Aliposhiba kidogo akili ikamtulia akaamua aende kujipumzish sha chumbani kwake na kukata shauri ya kuwa kama mpaka majira ya Alasiri atakuwa Deborah hapatikani kwenye simu ataenda kumsaka huko Mjini kwenye nyumba anayoishi aweze kupata jibu moja tu, kuwa bado mapenzi yao yapo au ndio yameshakufa ili ajue cha kufanya. Na kama akijua kuwa amezima simu makusudi kwa taadi yake tu basi ndipo atakubaliana na msemo wa wahenga wa unaosema usimjaribu mlevi na kutegemea shukrani abadani. Alikuwa hapajui wapi anapoishi Deborah kwa ufasaha ingawa alishamuelekeza lakini penye nia pana njia, liwalo na liwe hawezi kushindwa kufika.
[emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586]
 
Back
Top Bottom