mpasta
JF-Expert Member
- Jan 17, 2011
- 919
- 2,007
- Thread starter
- #41
SEHEMU-23
Mke wa Mjomba Kobelo akaapa kiapo cha Yasini Mkubwa cha kuanzisha mapambano ya kufa au kupona kuhakikisha wageni hao wanaondoka hapo nyumbani kwake. Deborah kwa umri wake wa miaka 5, akaanza kufanyishwa kazi kama trekta shambani bila kuchoka. Alikuwa anaamshwa saa 9 za usiku, jogoo la kwanza na kuanza kufanyishwa kazi za nyumbani. Kwanza ataanza kufulishwa nguo za mikojo za mama yake, akitoka hapo, apewe biwi la vyombo vya chakula cha usiku wake aoshe, akimaliza hapo aanze kufagia uwanja. Atapumzika kidogo, binamu zake wakiamka wafuatane nae mtoni kwenda kuchota maji ya matumizi ya nyumbani.
Mpaka ukifika muda wa kuelekea shuleni, alikuwa yupo hoi bin taabani mwili wake hautamaniki. Shangazi yake, mwili wa Debora ndio ulikuwa ngoma yake, kila akijisikia kuchapa, basi hasira zake zitamalizikia kwenye mwili wa Debora. Alikuwa anampiga mithili ya ngoma, kila anapozembea kutekeleza majukumu anayopewa kutokana na utoto wake. Mama Debora alikuwa anashuhudia vibweka vyote anavyofanyiwa binti yake, lakini alikuwa hawezi kuongea anabaki kulia machozi tu, lakini ni kilio cha samaki, macho yanasombwa na maji tu. Mateso hayo mazito kwa Deborah kuliko kipimo cha umri wake ukichanganya na tukio alilokutana nalo utotoni la kushuhudia kifo cha kikatili cha baba yake mzazi Bosi Minja, kikasababisha awe na ugonjwa wa wasiwasi wakati wote anaishi kwa hofu tu.
Pia ilikuwa kila ikifika usiku wa siku ya Jumamosi kuamkia Jumapili, sasa ile ile aliyopigwa risasi baba yake, lazima ajikojolee kitandani. Akiwa amelala fefefe kitandani, ikifika manane ya usiku tukio lile lote la mauaji huwa linajirudia kama mkanda wa video akiwa ndotoni mpaka anajikojolea chapachapa hapo hapo. Akishtuka usingizini tayari kashachafua mazingira. Hilo jambo la kujikojolea kitandani likawa ni doa kubwa katika maisha yake Debora pale nyumbani kwa Mjomba wake. Ilikuwa ni fedheha na soni kubwa kwa upande wake, Shangazi yake alikuwa anasubiria watoto wa kijijini wote wameshaamka vizuri, ndio anatwisha kichwani tandiko lake na shuka za mikojo huku anatoa amri wamuimbie nyimbo mbalimbali za kebehi kumsindikiza mtoni kwenda kufua nguo zake za mikojo. "Kikojozi Kikojozi....nguo zake tuzitie moto...! " huo ndio ulikuwa wimbo pendwa kwa watoto hao huku wanagonganisha vifuu, vyuma na ngoma, wananyimwa kwa kumsindikiza kikojozi Debora.
Sasa ikawa hata binamu zake, watoto wa Mjomba Kobelo ambao analala nao chumba kimoja, nao wakijikojolea kitandani msala wanamuangushia Debora kuwa ndio kajikojolea, hivyo mvua ya viboko mwilini inamshukia Deborah. Kazini kwa mama Debora ikafika barua ya kufukuzwa Chuo kutokana na kutoonekana kwa kitambo kirefu Chuoni. Wafanyakazi wenzake wa hospitali ya mkoa wakapanga ziara ya kumtembelea nyumbani kwake kujua kulikoni, Chuoni hayupo na kazini hayupo. Walichokipata nyumbani kwa Mjomba Kobelo hawatokuja kukisahau maishani mwao. Mjomba Kobelo aliwatimua kwa upanga wake akiwatuhumu kwa uchawi uliosababisha dada yake awe kitandani kwa muda wote. "Mmemroga dada yangu mkijua akimaliza masomo yake angewanyang'anya vyeo vyenu, nisiwaone tena kung'aza pua zenu nyumbani kwangu hapa wanga wakubwa, la sivyo nitawacharanga kama nyama ya buchani" alifoka Mjomba Kobelo huku yupo kidari nje hana shati mwilini. Watumishi wale wenzake mama Debora kila mmoja alijua namna alivyochomoka kwenye dhahama ile ya Mjomba Kobelo. Wapo waliopitia madirishani, wengine waliwahi kupita mlangoni na wengine walipenya kwenye uzio wa mabua ili mradi kila mmoja wapo alikuwa Yarabi Mola anasalimisha roho yake. Hawakukanyaga tena nyumbani pale, ndio ukawa mwisho wa ajira mama Debora, hakuwa tena na mtetezi.
[emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586]
Tarehe 1/09/1990 itakuwa ni siku ya kukumbukwa vizazi na vizazi kwa jamii ya Watanzania hasa kutokana na ugeni mzito walioupokea siku hiyo. Ilikuwa ni Jumamosi majira ya mchana, kadamnasi ya watu wa dini zote, makabila mbalimbali ya Tanzania na wa rika zote watoto, vijana kwa wakubwa walikuwa wamejipanga pande zote za barabara inayotokea Uwanja wa ndege wa Kimataifa wa Mwalimu Julius Kambarage Nyerere, wakiwa na majani, maua na bendera katika mikono yao huku wakiimba nyimbo mbali mbali, wakipiga shangwe na vigeregere wanapunga hewani. Walikuwa wanasubiria kumpokea Bwana Karol Joxef Wojtyla maarufu kwa jina la Papa John Paul II aliyekuwa katika ziara ya kuzitembelea nchi za Kiafrika zikiwemo Tanzania, Rwanda, Burundi na Ivory Coast. Alikuwa ndio kiongozi mkuu kabisa wa madhehebu ya kanisa katoliki duniani kipindi hicho akiwa ametokea nchini Vatican. Umati huo wa watu wapo walioanza kujikusanya barabarani kuanzia majira ya Alfajiri kwa kimuhemuhe, hamu na shauku ya kumuona mgeni huyo mukhtari. Papa huyo aliwasili uwanja wa ndege, aliposhuka tu moja kwa moja akaibusu ardhi ya Tanzania kisha akanyanyuka na kulakiwa na mwenyeji wake aliyekuwa Rais wa awamu ya pili, Mheshimiwa Rais Ally Hassan Mwinyi. Ilipofika majira ya saa 9 alasiri mvua kali ya kidindia ikanyesha sana lakini maajabu watu hawakuondoka barabarani mpaka alipopita Papa na kuwapungia mikono. Wapo wanaoamini kuwa rekodi yake ya umati uliojazana katika viwanja vya jangwani kusikiliza hotuba yake, haijavunjwa mpaka leo licha ya ujio wa marais watatu mfululizo wa Marekani, yaani Bill Clinton, George W. Bush pamoja na rais kijana mwenye asili ya Afrika, Barack Obama.
Ziara hiyo ya Papa huyo aliyetokea kuwa kipenzi cha wengi ilikuwa ni ziara iliyolenga zaidi katika Juhudi za Kupambana na gonjwa sugu la UKIMWI, pia hayati Yohane Paulo wa II alilenga zaidi Katika namna bora zaidi ya kuwahudumia wakimbizi. Pia aliambatana na timu nzito ya watendaji toka Vatican waliokuwa wanashiriki kuendesha mazungumzo mbalimbali ya kidiplomasia katika nchi mbalimbali walizotembelea na serikali husika. Pia walikuwa wanapata nafasi ya kufanya mazungumzo na asasi za kiraia zinazojihusisha na makundi muhimu katika jamii kama haki za watoto, mayatima, wanawake na mengineyo. Kwa kuwa Papa hakuwa na ratiba ya kutembelea nchini Kenya, hivyo Mkurugenzi wa kituo cha kulea yatima cha Cheryls Childrens Home and Learning Centre, Bwana 'Peter Ochieng' kituo ambacho mtoto mlemavu 'Pesambili Martin Tenga' ambaye ametelekezwa na wazazi wake alikuwa analelewa, hakulaza damu akaja kuvizia nafasi ya kuzungumza na ugeni huo mzito nchini Tanzania akitokea Kenya. Kama ilivyo pana nia pana njia na mgaa gaa na upwa hali wali mkavu akapata nafasi ya kuongea na ugeni ule toka Vatican. Akaeleza kinagaubaga mipango, malengo, maono na madhumuni ya uanzishwaji wa kituo chake katika malezi ya watoto yatima ambao wengi katika wazazi wao wamefariki kwa ugonjwa hatari wa UKIMWI. Kwa jinsi Bwana Ochieng alivyokuwa ametabahari katika kujieleza kwa ufasaha, wakapendezwa sana na kituo hicho, wakampa ofa ya fastafasta kuwachukua watoto yatima 10 kwenda nao nchini Italia kwenda kuwasomesha mpaka elimu ya Chuo Kikuu. Pia wakamuahidi misaada lukuki itakayokuwa inatumwa kwenye kituo chake ikiwemo gharama za chakula, malazi na mavazi.
Mungu si Athumani, Pesambili mtoto wa Recho alitelekezwa huko Kenya akaula nae akawekwa katika orodha ya watoto wanaotakiwa kuelekea nchini Italia. Ujio wa Papa John Paulo II nchini Tanzania ukawa ni neema kwake ya mwanzo wa kutoboa katika maisha yake. Uchaguzi wa watoto hao ulisimamiwa na wao wenyewe wazungu wa Vatican, kuhofia figisufigisu za Waafrika kuchaguana kindugu na kirafiki. Walikuwa wanajua nje ndani usanii wa vituo vingi vya watoto yatima, ofa kama hizo za kusomeshwa wanaweza kuchaguliwa watoto ambao sio yatima na hata wakati mwingine watoto wa vigogo serikalini. Wale mawakala wa viongozi toka Vatican waliotumwa Jijini Nairobi kuchagua watoto wa kuelekea Italia, walipomuona tu Pesambili pale kituoni wakavutiwa nae kutokana na upole wake na werevu wake wakamuweka katika orodha hiyo ya watoto 10, ya wanaotakiwa kusafirishwa hasa wakimuonea huruma kutokana na ulemavu wake.
Pesambili akarudishwa katika nchi ya asili ya Babu yake mzaa mama, baba yake Recho, Bwana 'Francesco Gabrielebila' bila kufahamu kuwa anarudishwa katika mizizi yake. Alisafirishwa akiwa hamjui baba wala mama yake, na wala hajui asili ya wazazi wake ni wapi katika nchi za Kiafrika. Alipofikishwa tu nchini Italia, moja kwa moja Pesambili akapelekwa katika moja hospitali kubwa Jijini Roma, Italia inayoitwa 'Policlinico Universitario Agostino Gemelli'. Hospitali ambayo inamilikwa na Chuo Kikuu cha "The Università Cattolica del Sacro Cuore" wakiitumia hospitali hiyo pia kama hospitali ya mafunzo kwa wanafunzi wake wa kitivo cha Utabibu. Ilikuwa ni hospitali kongwe na ya pili kwa ukubwa katika hospitali zote za nchi nzima ya Italia. Walipomfanyia vipimo vya uchunguzi vya kina chini ya jopo la madaktari bingwa, majibu yakatoka kuwa anaweza kufanyia upasuaji wa kurekebisha mifupa yake na ataweza kutembea kutokana na kuwa bado mifupa yake haijakomaa. Mara moja shauri likapitishwa la kufanyika kwa upasuaji huo, ambao kwa baraka za Mwenyezi Mungu, upasuaji ukafanikiwa.
Baada ya miezi 6 tokea upasuaji ule ufanyike, Pesambili akaanza kutembea vizuri kabisa kama vile hajawahi kuwa mlemavu, kiasi kwamba hata mama yake Recho angefanikiwa kumuona, basi angekataa katakata kuwa huyo sio Pesambili wake
Mke wa Mjomba Kobelo akaapa kiapo cha Yasini Mkubwa cha kuanzisha mapambano ya kufa au kupona kuhakikisha wageni hao wanaondoka hapo nyumbani kwake. Deborah kwa umri wake wa miaka 5, akaanza kufanyishwa kazi kama trekta shambani bila kuchoka. Alikuwa anaamshwa saa 9 za usiku, jogoo la kwanza na kuanza kufanyishwa kazi za nyumbani. Kwanza ataanza kufulishwa nguo za mikojo za mama yake, akitoka hapo, apewe biwi la vyombo vya chakula cha usiku wake aoshe, akimaliza hapo aanze kufagia uwanja. Atapumzika kidogo, binamu zake wakiamka wafuatane nae mtoni kwenda kuchota maji ya matumizi ya nyumbani.
Mpaka ukifika muda wa kuelekea shuleni, alikuwa yupo hoi bin taabani mwili wake hautamaniki. Shangazi yake, mwili wa Debora ndio ulikuwa ngoma yake, kila akijisikia kuchapa, basi hasira zake zitamalizikia kwenye mwili wa Debora. Alikuwa anampiga mithili ya ngoma, kila anapozembea kutekeleza majukumu anayopewa kutokana na utoto wake. Mama Debora alikuwa anashuhudia vibweka vyote anavyofanyiwa binti yake, lakini alikuwa hawezi kuongea anabaki kulia machozi tu, lakini ni kilio cha samaki, macho yanasombwa na maji tu. Mateso hayo mazito kwa Deborah kuliko kipimo cha umri wake ukichanganya na tukio alilokutana nalo utotoni la kushuhudia kifo cha kikatili cha baba yake mzazi Bosi Minja, kikasababisha awe na ugonjwa wa wasiwasi wakati wote anaishi kwa hofu tu.
Pia ilikuwa kila ikifika usiku wa siku ya Jumamosi kuamkia Jumapili, sasa ile ile aliyopigwa risasi baba yake, lazima ajikojolee kitandani. Akiwa amelala fefefe kitandani, ikifika manane ya usiku tukio lile lote la mauaji huwa linajirudia kama mkanda wa video akiwa ndotoni mpaka anajikojolea chapachapa hapo hapo. Akishtuka usingizini tayari kashachafua mazingira. Hilo jambo la kujikojolea kitandani likawa ni doa kubwa katika maisha yake Debora pale nyumbani kwa Mjomba wake. Ilikuwa ni fedheha na soni kubwa kwa upande wake, Shangazi yake alikuwa anasubiria watoto wa kijijini wote wameshaamka vizuri, ndio anatwisha kichwani tandiko lake na shuka za mikojo huku anatoa amri wamuimbie nyimbo mbalimbali za kebehi kumsindikiza mtoni kwenda kufua nguo zake za mikojo. "Kikojozi Kikojozi....nguo zake tuzitie moto...! " huo ndio ulikuwa wimbo pendwa kwa watoto hao huku wanagonganisha vifuu, vyuma na ngoma, wananyimwa kwa kumsindikiza kikojozi Debora.
Sasa ikawa hata binamu zake, watoto wa Mjomba Kobelo ambao analala nao chumba kimoja, nao wakijikojolea kitandani msala wanamuangushia Debora kuwa ndio kajikojolea, hivyo mvua ya viboko mwilini inamshukia Deborah. Kazini kwa mama Debora ikafika barua ya kufukuzwa Chuo kutokana na kutoonekana kwa kitambo kirefu Chuoni. Wafanyakazi wenzake wa hospitali ya mkoa wakapanga ziara ya kumtembelea nyumbani kwake kujua kulikoni, Chuoni hayupo na kazini hayupo. Walichokipata nyumbani kwa Mjomba Kobelo hawatokuja kukisahau maishani mwao. Mjomba Kobelo aliwatimua kwa upanga wake akiwatuhumu kwa uchawi uliosababisha dada yake awe kitandani kwa muda wote. "Mmemroga dada yangu mkijua akimaliza masomo yake angewanyang'anya vyeo vyenu, nisiwaone tena kung'aza pua zenu nyumbani kwangu hapa wanga wakubwa, la sivyo nitawacharanga kama nyama ya buchani" alifoka Mjomba Kobelo huku yupo kidari nje hana shati mwilini. Watumishi wale wenzake mama Debora kila mmoja alijua namna alivyochomoka kwenye dhahama ile ya Mjomba Kobelo. Wapo waliopitia madirishani, wengine waliwahi kupita mlangoni na wengine walipenya kwenye uzio wa mabua ili mradi kila mmoja wapo alikuwa Yarabi Mola anasalimisha roho yake. Hawakukanyaga tena nyumbani pale, ndio ukawa mwisho wa ajira mama Debora, hakuwa tena na mtetezi.
[emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586]
Tarehe 1/09/1990 itakuwa ni siku ya kukumbukwa vizazi na vizazi kwa jamii ya Watanzania hasa kutokana na ugeni mzito walioupokea siku hiyo. Ilikuwa ni Jumamosi majira ya mchana, kadamnasi ya watu wa dini zote, makabila mbalimbali ya Tanzania na wa rika zote watoto, vijana kwa wakubwa walikuwa wamejipanga pande zote za barabara inayotokea Uwanja wa ndege wa Kimataifa wa Mwalimu Julius Kambarage Nyerere, wakiwa na majani, maua na bendera katika mikono yao huku wakiimba nyimbo mbali mbali, wakipiga shangwe na vigeregere wanapunga hewani. Walikuwa wanasubiria kumpokea Bwana Karol Joxef Wojtyla maarufu kwa jina la Papa John Paul II aliyekuwa katika ziara ya kuzitembelea nchi za Kiafrika zikiwemo Tanzania, Rwanda, Burundi na Ivory Coast. Alikuwa ndio kiongozi mkuu kabisa wa madhehebu ya kanisa katoliki duniani kipindi hicho akiwa ametokea nchini Vatican. Umati huo wa watu wapo walioanza kujikusanya barabarani kuanzia majira ya Alfajiri kwa kimuhemuhe, hamu na shauku ya kumuona mgeni huyo mukhtari. Papa huyo aliwasili uwanja wa ndege, aliposhuka tu moja kwa moja akaibusu ardhi ya Tanzania kisha akanyanyuka na kulakiwa na mwenyeji wake aliyekuwa Rais wa awamu ya pili, Mheshimiwa Rais Ally Hassan Mwinyi. Ilipofika majira ya saa 9 alasiri mvua kali ya kidindia ikanyesha sana lakini maajabu watu hawakuondoka barabarani mpaka alipopita Papa na kuwapungia mikono. Wapo wanaoamini kuwa rekodi yake ya umati uliojazana katika viwanja vya jangwani kusikiliza hotuba yake, haijavunjwa mpaka leo licha ya ujio wa marais watatu mfululizo wa Marekani, yaani Bill Clinton, George W. Bush pamoja na rais kijana mwenye asili ya Afrika, Barack Obama.
Ziara hiyo ya Papa huyo aliyetokea kuwa kipenzi cha wengi ilikuwa ni ziara iliyolenga zaidi katika Juhudi za Kupambana na gonjwa sugu la UKIMWI, pia hayati Yohane Paulo wa II alilenga zaidi Katika namna bora zaidi ya kuwahudumia wakimbizi. Pia aliambatana na timu nzito ya watendaji toka Vatican waliokuwa wanashiriki kuendesha mazungumzo mbalimbali ya kidiplomasia katika nchi mbalimbali walizotembelea na serikali husika. Pia walikuwa wanapata nafasi ya kufanya mazungumzo na asasi za kiraia zinazojihusisha na makundi muhimu katika jamii kama haki za watoto, mayatima, wanawake na mengineyo. Kwa kuwa Papa hakuwa na ratiba ya kutembelea nchini Kenya, hivyo Mkurugenzi wa kituo cha kulea yatima cha Cheryls Childrens Home and Learning Centre, Bwana 'Peter Ochieng' kituo ambacho mtoto mlemavu 'Pesambili Martin Tenga' ambaye ametelekezwa na wazazi wake alikuwa analelewa, hakulaza damu akaja kuvizia nafasi ya kuzungumza na ugeni huo mzito nchini Tanzania akitokea Kenya. Kama ilivyo pana nia pana njia na mgaa gaa na upwa hali wali mkavu akapata nafasi ya kuongea na ugeni ule toka Vatican. Akaeleza kinagaubaga mipango, malengo, maono na madhumuni ya uanzishwaji wa kituo chake katika malezi ya watoto yatima ambao wengi katika wazazi wao wamefariki kwa ugonjwa hatari wa UKIMWI. Kwa jinsi Bwana Ochieng alivyokuwa ametabahari katika kujieleza kwa ufasaha, wakapendezwa sana na kituo hicho, wakampa ofa ya fastafasta kuwachukua watoto yatima 10 kwenda nao nchini Italia kwenda kuwasomesha mpaka elimu ya Chuo Kikuu. Pia wakamuahidi misaada lukuki itakayokuwa inatumwa kwenye kituo chake ikiwemo gharama za chakula, malazi na mavazi.
Mungu si Athumani, Pesambili mtoto wa Recho alitelekezwa huko Kenya akaula nae akawekwa katika orodha ya watoto wanaotakiwa kuelekea nchini Italia. Ujio wa Papa John Paulo II nchini Tanzania ukawa ni neema kwake ya mwanzo wa kutoboa katika maisha yake. Uchaguzi wa watoto hao ulisimamiwa na wao wenyewe wazungu wa Vatican, kuhofia figisufigisu za Waafrika kuchaguana kindugu na kirafiki. Walikuwa wanajua nje ndani usanii wa vituo vingi vya watoto yatima, ofa kama hizo za kusomeshwa wanaweza kuchaguliwa watoto ambao sio yatima na hata wakati mwingine watoto wa vigogo serikalini. Wale mawakala wa viongozi toka Vatican waliotumwa Jijini Nairobi kuchagua watoto wa kuelekea Italia, walipomuona tu Pesambili pale kituoni wakavutiwa nae kutokana na upole wake na werevu wake wakamuweka katika orodha hiyo ya watoto 10, ya wanaotakiwa kusafirishwa hasa wakimuonea huruma kutokana na ulemavu wake.
Pesambili akarudishwa katika nchi ya asili ya Babu yake mzaa mama, baba yake Recho, Bwana 'Francesco Gabrielebila' bila kufahamu kuwa anarudishwa katika mizizi yake. Alisafirishwa akiwa hamjui baba wala mama yake, na wala hajui asili ya wazazi wake ni wapi katika nchi za Kiafrika. Alipofikishwa tu nchini Italia, moja kwa moja Pesambili akapelekwa katika moja hospitali kubwa Jijini Roma, Italia inayoitwa 'Policlinico Universitario Agostino Gemelli'. Hospitali ambayo inamilikwa na Chuo Kikuu cha "The Università Cattolica del Sacro Cuore" wakiitumia hospitali hiyo pia kama hospitali ya mafunzo kwa wanafunzi wake wa kitivo cha Utabibu. Ilikuwa ni hospitali kongwe na ya pili kwa ukubwa katika hospitali zote za nchi nzima ya Italia. Walipomfanyia vipimo vya uchunguzi vya kina chini ya jopo la madaktari bingwa, majibu yakatoka kuwa anaweza kufanyia upasuaji wa kurekebisha mifupa yake na ataweza kutembea kutokana na kuwa bado mifupa yake haijakomaa. Mara moja shauri likapitishwa la kufanyika kwa upasuaji huo, ambao kwa baraka za Mwenyezi Mungu, upasuaji ukafanikiwa.
Baada ya miezi 6 tokea upasuaji ule ufanyike, Pesambili akaanza kutembea vizuri kabisa kama vile hajawahi kuwa mlemavu, kiasi kwamba hata mama yake Recho angefanikiwa kumuona, basi angekataa katakata kuwa huyo sio Pesambili wake