Riwaya: Matanga ya rohoni

Riwaya: Matanga ya rohoni

SEHEMU-49


️[emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586]
SURA ISHIRINI YA MOJA
Mama Deborah alikuja kuzindukia hospitalini baada ya kupoteza fahamu kwa saa kadhaa. Alipopata nafuu akabakia kulia hana cha kuficha tena mbele ya Dr.Pesambili. Ikabidi aufunue ukweli aliokuwa ameuficha moyoni mwake kwa muda mrefu, kwa kumueleza Dr.Pesambili kuwa mama yake ndio aliyeivuruga ndoa yake mpaka kusababisha kifo cha mumewe, Bosi Joseph Minja. Kama haitoshi akamuelezea namna alivyomtumia yeye Dr.Pesambili akiwa mtoto mchanga kubeba urithi wa mumewe kwa kudanganya familia kuwa Dr.Pesambili ni mtoto wa Bosi Minja.

Alipotoka hospitalini mama Deborah, ikabidi wafuatane mguu kwa mguu na Dr.Pesambili mpaka Marangu kwa wazazi wake Bosi Minja kwenda kuanika ukweli kuwa yeye sio mtoto wa Bosi Minja. Ikabidi yafanyike matambiko ya asili kusaidia kuondosha mikosi kwa Recho, mama yake Dr.Pesambili kwa kuchafua ukoo wa Minja kwa kuleta mtoto asiye na nasaba nao ya damu. Baada ya wiki moja wakarejea Jijini Dar es Salaam kuendelea na maisha yao ya kawaida. Lakini Dr.Pesambili akiwa amelipia matangazo ya kumsaka mama yake mzazi kwenye magazeti, redio na televisheni. Siku zikawa zinayoyoma lakini mama yake hakujitokeza kama alivyotarajia, mpaka akaanza kuhisi huenda mama yake mzazi amefariki dunia.


Hata hivyo akamshukuru Mungu kwa hatua aliyoifikia ya kumtambua mama yake ingawa hajawahi kumtia machoni.
Dr.Pesambili ilibidi taarifa za kufanikiwa kumtambua mama yake azifikishe yeye mwenyewe Jijini Turin kwa babu yake mlezi. Ilibidi azifikishe hasa baada ya kuona mfanano wa ubini wa baba mzazi wa jina la mama, "Francesco Gabriele". Ikabidi Babu wa watu aungame ukweli kuwa Rachel, mama mzazi wa Dr.Pesambili ni mtoto wake ambaye alimtelekeza tokea akiwa mtoto mdogo bila kutoa huduma zozote. Hivyo ikabidi Dr.Pesambili aitwe Jijini Turin Italia, atambuliwe rasmi kama Mjukuu mkubwa wa Mzee Francesco Gabriele. Mzee wa watu kwa furaha yake ikabidi akate nusu ya utajiri wake ampatie Dr.Pesambili. Sasa rasmi Dr.Pesambili akageuka kuwa bilionea kijana. Utajiri ambao ulimtembelea katika wakati muafaka, wakati ambao alikuwa na ujenzi wa hospitali yake ya kisasa anayoijenga Jijini Dar es Salaam.


Lakini kwa upande wa pili taarifa ya kama Recho ndio mama mzazi wa Dr.Pesambili, iliibua simanzi na majonzi makubwa kwa baba mlezi wa Dr.Pesambili, Mr.Lorenzo. Mr.Lorenzo alishapata msamaha wa kifungo chake kutokana na mwenendo mwema aliouonyesha gerezani. Hivyo ujio wa taarifa hiyo ulimkuta Mr.Lorenzo yupo uraiani, alipoonyeshwa picha ya Recho na Dr.Pesambili akamtambua mara moja kuwa ndio mwanamke aliyemsababishia matatizo yote ya kufungwa jela. Akajilaumu kumbe alikuwa na mahusiano ya kimapenzi na dada yake wa damu kabisa kwa baba mmoja bila kujua. Ingawa lawama alizitupa pande zote, kwa baba yake mzazi kwa kuficha kama ana mtoto Tanzania. Pia lawama ziliangukia kwa Recho kwa kuamua kuficha ubini wake halisi, hali iliyosababisha wasifahamiane. Wote kwa pamoja wakazika tofauti zao kwenye kaburi la sahau, na kuamua kuwa yaliyopita si ndwele tugange yajayo.


Aliporejea Tanzania, Dr.Pesambili bila kuchelewa ndani ya wiki tatu tu hospitali yake ya kisasa, yenye roshani zaidi ya 20 ikawa imesimama. Hospitali hiyo akaipa jina la 'Huruma General Hospital'-(HGH). Akaajiri madaktari bora na vifaa vya kisasa, kiasi kwamba watu wakaipa hospitali hiyo lakabu ya "Muhimbili Ndogo". Mama Deborah nae akaula kwenye hospitali hiyo. Akawa ni mmoja wa Wakurugenzi wa hospitali hiyo anayesimamia rasilimali watu. Kutokana na uzoefu wake katika mambo ya hospitali, ndani ya muda mfupi kila Mfanyakazi wa afya Tanzania akawa anatamani akafanye kazi 'Huruma General Hospital'-( HGH). Madaktari wakongwe na wapya wote wakawa wanachuana kutafuta kazi kwenye hospitali ya Dr.Pesambili.

Wagonjwa nao, kimbilio lao likawa Huruma General Hospital-(HGH). Huko walikuwa wanapata tiba ya viwango vya juu, tena ya kiustaarabu bila kufokewa wala kutusiwa na watumishi wake. Mpango wake Dr.Pesambili sasa ukawa ni kufungua matawi kila kanda ya nchi ili kupunguza msongamano wa wagonjwa wanaofurika hospitalini hapo wakitokea Mikoani.
[emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586]
Kulipokucha gumzo la Jiji likagubikwa na kifo cha Meneja wa Benki maarufu nchini, aliyekutwa anaelea juu ya maji baharini. Yule Meneja aliamua kujihukumu mwenyewe kwa kujiua baharini ili kukwepa mkono wa sheria. Maana alijua tu lazima ataozea jela kwa kifungo atakachufungwa. Gari lake lilikutwa limetelekezwa katika makutano ya barabara za Dr.Barack Obama na Magogoni. Maafisa Usalama, walipofanya uchunguzi wao wakagundua mara ya mwisho alifanya sana mawasiliano ya simu ya kuonana na Bosi Timammy. Upelelezi ukaanzia kwa Bosi Timammy, akakamatwa na kuwekwa ndani kusaidia upelelezi. Katika nyaraka zilizofumwa nyumbani kwa Bosi Timammy ndio ikagundulika kuwa walikopeshana pesa za Benki milioni 500 kinyemela "offline" bila kufuata taratibu za kawaida za mikopo ya kibenki.

.Katika sekeseke hilo la mumewe kukamatwa, Deborah akashikwa na uchungu wa mimba wa ghafla kutokana na mshtuko wa kukamatwa kwa mumewe Bosi Timammy. Ikabidi akimbizwe katika hospitali ya 'Huruma General Hospital'-(HGH) ili kuokoa uhai wake na wa mtoto. Kama bahati tu, mama Deborah asubuhi moja akiwa kwenye harakati zake za ukaguzi wa shughuli za wodi ya wazazi ndipo akakutana na mtoto wake kwa mara ya kwanza baada ya kupoteana kwa zaidi ya miaka 12 lakini hawakutambuana. Mama Deborah alichoshangazwa ni kuona mgonjwa anayemdhania ni mtoto wake ana jina la kiarabu, anaitwa Bi. Faizah Timammy.


Mama Deborah akaamini kweli duniani wawili wawili na alishindwa hata kuongea nae kutokana hali mbaya aliyokuwa nayo Deborah na tayari mtoto wake mchanga alishafariki. Mchana wake Mama Deborah akakwea mwewe kuelekea Jijini Arusha kusimamisha ujenzi wa Huruma General Hospital-(HGH) tawi la kaskazini. Usiku wake alivyolala mama Deborah ndipo alipoanza kuona mauzauza ndotoni. Alikuwa amemuota mgonjwa aliyelazwa hospitalini kwao Bi.Faizah Timammy ndio Deborah wake wanacheka na kufurahi pamoja baada ya kupoteana kwa muda mrefu. Alipoamka akaipuuzia kuwa huenda ni ndoto tu haina maana yoyote. Usiku wake ndoto ile ile kama ya jana yake ikajirudia vile vile, ikabidi asiipuuzie tena arejee Jijini Dar es Salaam akampeleleze vizuri yule mgonjwa. Tahamaki mgonjwa kesharuhusiwa nyumbani. Namba za simu alizoziandikisha hospitalini ni za mumewe ambaye yupo korokoroni anapambana na hali yake ili akwepe kifungo kimagumashi.


Bahati nzuri Maabara kulikuwepo na sampuli ya vipimo vyake vya damu. Walivyoitumia kufanya vipimo vya DNA, majibu yakathibitisha pasina kuacha mashaka kuwa Bi. Faizah Timammy ndio Deborah Kunambi mtoto wa mama Deborah wa kumzaa. Kwanza akamshukuru Mungu kwa kumpa uhai mtoto wake na maisha mazuri mpaka wamefanikiwa kuonana bila kutambuana. Sasa ikawa mshikemshike kwa wote wawili, mchuzi moto ugali moto kwa kila mmoja, Dr.Pesambili anamsaka mama yake mzazi Recho na mama Deborah anamsaka binti yake Deborah.
[emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586]
Mbweku Jr pesa zake alizompora Meneja wa Benki akaamua kuwekeza kwenye kampuni ya usafirishaji majini. Aliamua kuwekeza kwenye kitu ambacho anakipenda. Utoto wake wote amecheza kwenye ufukwe wa bahari mpaka kuzamia kwake kwenda nchini Afrika ya Kusini alitokea ufukwe wa Kigamboni. Kampuni yake ilikuwa inaitwa "Express Boat Transport" (EBT)-Ltd, lakini hakuna mtu alikuwa anafahamu kama mmiliki ni Mbweku Jr.

Aliajiri vijana wasomi wa Chuo Kikuu wakawa wanamuendeshea kampuni, huku akiwa na timu ya wanasheria wanaoendesha mambo yake, yeye mwenyewe yupo pembeni anafanya shughuli zake binafsi. Bado alikuwa anajipanga kumpa pigo la mwisho Takatifu hasimu wake Timammy. Hakutaka kabisa kumuua tena alitaka ampe adhabu ambayo mwenyewe atajiona hastahili tena kuishi duniani. Alijua tu licha ya Timammy kuwekwa ndani hawezi kufungwa jela kutokana na mtandao wake wa uhalifu unaomlinda.


Alichokitabiri ni kweli kikaja kikatokea. Timammy hakufunguliwa kesi yoyote kutokana na shahidi mkuu, Meneja wa Benki kukosekana. Bosi Timammy akarudi uraiani huku amemkuta mkewe kapoteza ujauzito wake. Maisha ya Mbweku Jr yakawa yamejaa bashasha mpwitompwito wakati maisha ya Bosi Timammy yakawa mvangemvange hayana starehe tena. Wakati huo huo alishawaweka vijana wake wa upelelezi wanafuatilia nyendo za Bosi Timammy bila mwenyewe kujua kama anafuatiliwa. Baada ya miezi mitatu tu, Bosi Timammy akanasa kwenye mtego mwingine wa Mbweku Jr. Timammy alikuja kukodisha boti kwenye kampuni ya Express Boat Transport-(EBT) -Ltd.


Alikuwa anataka kupelekwa kwenye kisiwa cha Mbudya yeye na mke wake kwa kutumia boti ya kisasa, nambari wani kwa ubora. Walikuwa wanataka utulivu wa nafsi zao baada ya kila mmoja kutoka kwenye misukosuko. Bosi Timammy akiwa ametoka rumande, na Deborah ametoka kwenye kupoteza ujauzito wake. Waliweka oda wiki moja kabla ya tukio lenyewe, hali ambayo ilimpa uwanja mpana wa Mbweku Jr kujipanga kutekeleza tukio analolikusudia.


Siku ya siku ikawadia ya Bosi Timammy na mkewe Deborah kupelekwa kisiwa cha Mbudya. Msafara wa kuelekea kisiwani ulianzia katika Hoteli ya Whitesands kwa kutumia boti daraja la kwanza linalomilikiwa na kampuni ya Express Boat Transport-(EBT) -Ltd. Ilikuwa ni boti yenye kila kitu ambayo kuikodi kwa saa gharama yake ni milioni 5. Bosi Timammy aliikodi kwa kulipia saa 10. Boti ikang'oa nanga, ikiwa na abiria watano, nahodha wa boti na sarahange wake, Bosi Timammy, Deborah na khadimu wao mmoja wa kike. Nahodha, alikuwa mwili nyumba, amejengeka misuli utasema anakula sementi, huku kichwani alivalia kofia ya pama iliyoficha sehemu ya uso wake, huku akionekana yupo makini na kazi yake ya kulisongesha boti lifike linapotakiwa. Sarahange alikuwa kijana mdogo tu aliyemaliza Chuo Kikuu, aliyevalia mavazi nadhifu ya kibaharia. Alikuwa na jukumu la kuwapatia takrima ya kahawa na vinywaji mbalimbali wanavyohitaji abiria wao.

Nahodha alikuwa anaiendesha boti hiyo kwa mwendo wa kinyonga, ili kuwapa fursa maridhawa wateja wao ya kifurahia mandhari ya baharini. Kuna wakati alikuwa analeta mbwembwe za kulizima boti na kuliacha boti hilo lisukwesukwe na mawimbi ya bahari kwa kupelekwa pande za yamini na shimari. Huku nahodha huyo anazunguka kwenye boti anaongea na sarahange wake kisha safari inaendelea tena. Hayo yote yalikuwa ni madahiro na manjonjo ya kuwathibitishia kuwa kampuni ya Express Boat Transport-(EBT) -Ltd hawabahatishi katika fani, wana manahodha waliofurutu ada katika uendeshaji wa vyombo vya majini. Muda wote wa safari Bosi Timammy alikuwa amemkumbatia mkewe, kichwa cha Deborah kipo kifuani pake. Wanacheka, wananong'onezana, wanatabasamu pamoja ilimradi, waliweka pembeni shida zao zote na kuamua nuzuha hiyo ya kisiwani iwe ni ponyo na faraja kwa mazonge yote waliyoyapitia katika maisha yao.

Walipowasili Kisiwani walijikuta wametumia zaidi ya dakika 50, kwa safari ya takribani robo saa mpaka dakika 20. Yule khadimu wao aliposhuka tu, akaanza harakati za kuwasha majiko maalumu waliyokuwa wamekuja nayo kwenye boti. Majiko hayo yalikuwa ni kwa ajili ya kuchomea nyama ya mbuzi, kuku na samaki wabichi. Bosi Timammy na Nahodha wake wakapanda boti kwa mara ya pili kwa ajili ya kuvua samaki watakaowaleta kwa ajili ya kuchomwa kwenye jiko. Bosi Timammy ni katika vitu alikuwa anapenda katika maisha yake ni uvuvi wa samaki wa kitalii. Walipanga kwenda bahari kuu, hiyo ikiwa ni zaidi ya maili 12 kutoka pwani na sio chini ya himaya ya taifa lolote. Wakavaa nguo za kazi wakibeba na dhana za kazi za uvuvi wakajitoma baharini tayari kwa msafara wa mara ya pili. Hiyo ilikuwa ni majira ya mafungulia ng'ombe, jua bado halijachanganya vya kutosha. Wakatembea kwa zaidi ya maili 6 bila kuzungumzishana, kama kawaida yake Bosi Timammy akiweka mbele kiburi chake cha pesa. Ghafla bin vuu....Nahodha yule akazima injini ya boti.

"Huu ni ufala, nalipia pesa kochokocho halafu mnaweka mafuta kidebe, wewe una akili kweli au taahira..!" Bosi Timamny tayari alishajaa upepo kwa hasira baada ya kuona boti limezima tena wakiwa kina kirefu cha bahari. "Samahani Bosi tulijisahau, ngoja nifanye mawasiliano na wenzangu walete msaada wa haraka....!" alijibu Nahodha yule kinyonge sana huku akiendelea kuishindilia kofia yake kichwani kuzidi kuficha wajihi wake. "Nipe namba ya Meneja wako, wewe lazima ufukuzwe kazi leo mjinga mkubwa wewe...!" alifoka Bosi Timammy na bila kutarajia akamuezeka kibao cha nguvu shavuni yule Nahodha. Shambulio ambalo liliamsha chemchem ya hasira kwa Nahodha yule na kujibu mapigo kwa kumrushia teke la shingo Bosi Timammy, akaanguka mpaka chini kama gunia la mahindi.

"Mshenzi mkubwa wewe utanitambua leo, nitakuchakaza mpaka unitajie jando langu nilifanyiwa pori gani na ngariba wangu anaitwa nani..!" alisema kwa hasira yule Nahodha wa boti ambaye sasa alishatupa pembeni kofia yake na kuidhihirisha sura yake hali. "Khaaaaah....kumbe wewe ni best Mbweku Jr Shikamooo sana...!" Bosi Timammy kiherehere chote kilimuisha na kutumbukiwa na nyongo baada ya kugundua kuwa Nahodha wake aliyemchapa kibao ni Mbweku Jr.

."Ha.. ha.. ha....Mwanaharashi mkubwa wewe, pesa zangu zipo wapi? Deborah niliyekukabidhi akiwa na kizinda chake umsomeshe mpaka mwisho wa elimu yupo wapi? Baba yangu niliyekukabidhi umpelekee huduma Jela yupo wapi? Mbweku Jr rafiki yako aliyekuomba tu umlipie faini Mahakamani baada ya kukamatwa kwa uhamiaji haramu nchini Afrika ya Kusini yupo wapi? Au umeshamuua baada ya kumtumia jambazi jela na kumletea chakula cha sumu?" alikuwa Timammy anasomewa risala ya kifo wakati ameshakabwa koo yupo chini amelazwa kwenye ya boti.


"Ni...sa....me....he...... nipo....ta... yari.....kukupa....haki zako zote...!" aliongea kiunyonge kwa sauti ya kilio cha kwikwi chenye majuto ndani yake, huku boti iliyoitwa kutoa msaada na Mr.Mbweku Jr Nahodha feki ikiwasili eneo la tukio. Hofu ya Bosi Timammy ikazidi kuongezeka akijua fika hawa huenda ni maharamia wa Kisomali wenye michezo ya kuteka Meli kwenye bahari kuu. Wameitwa na hasimu wake wamchukue wakamtupe huko kwenye kina kirefu zaidi akaliwe na papa na nyangumi. Ghafla akaona timu ya watu wanashuka wakiambatana na baadhi ya Mameneja wake mwenyewe wa kampuni, pamoja na baadhi ya Watumishi wa Benki wakiwa na Brifkesi zao.

Bosi Timammy alizidi kunyong'onyea vilivyo wala hajui nini kinachotaka kufanyika mbele yake. Akajutia nafsini mwake kwa kuendekeza tamaa na uroho wa mali, ama kweli mbio za sakafuni huishia ukingoni. "Eheee....elezea hapa mbele ya mashahidi namna utakavyonilipa pesa zangu zote.....!" aliongea Mbweku Jr mbele ya watu wale waliokuwa wanafika idadi yao kama 6 hivi. Bosi Timammy alikuwa mnyonge kupitiliza, uso umemshuka kwa aibu utasema ni mzee wa miaka 80. "Usitake kunitibua nyongo, elezea mbele ya hadhira hii namna ulivyonidhulumu pesa zangu na kutaka kuniua ili nisije kudai mgao wangu, maana watu wasidhani ninakudhulumu, kwa kawaida mtenda akitendewa huona kaonewa.....!" alizidi kufoka Mbweku Jr ameshapandisha ruhani wake wa ugomvi huwezi kumuambia kitu akakuelewa.


Ikabidi Bosi Timammy ajikaze kisabuni, na kuanza kuelezea mkasa mzima wa chanzo cha utajiri wake na madhila mbalimbali aliyoyafanya juu ya swahibu wake Mbweku Jr. Baada ya kusikiliza maelezo ya pande zote mbili ikaamriwa, yafanyike makabidhiano ya mali zote za Bosi Timammy kwa Mbweku Jr kisheria. Timu ile ya Wanasheria sasa ukageuka uwanja wao wa kumsainisha nyaraka mbalimbali Bosi Timamu za makabidhiano ya mali. Uzuri tayari walishafanya speksheni ya mali zote anazomiliki Bosi Timammy na nyaraka zote za umiliki zililetwa na Watumishi wake waandamizi. Bosi Timammy bila pingamizi lolote akasaini nyaraka zote, na pesa zake zikahamishwa na Watumishi wa Benki pale pale kwa kutumia dhana zao za kazi na kuingizwa rasmi kwenye kampuni ya Express Boat Transport-(EBT)-Ltd. Baada ya kama muda wa kama saa 2 shughuli ile ikafikia tamati.

. Sasa rasmi baada ya kikao kile Bosi Timammy akageuka kuwa Mlalahoi na sio Mlalaheri tena. Mbweku Jr ili kuwachagiza wale Watumishi Waandamizi wa Bosi Timammy wasije kufanya hujuma kwenye Biashara, akawaahidi wote kutowafukuza kazi, waendelee na nyadhifa zao kama kawaida. Kilichobadilika kwao ni Mmiliki tu wa Kampuni. Ile timu ikaondoka zao, huku wakiisindikiza boti ya Mbweku Jr na Bosi Timammy mpaka ifike Kisiwa cha Mbudya.


"Tuondoke mke wangu sijisikii vizuri kiafya....." ilikuwa ni kauli ya Bosi Timammy baada ya boti kutia nanga ufukweni. Nyama za mbuzi na kuku walionona wenye kuchuruzika mafuta zikawa haziliki tena. Njia nzima wakati wanarudi hamna mtu aliyekuwa anamzungumzisha mwenzake mpaka Deborah alipovunja ukimya. "Mume wangu isije kuwa hii mikosi inatuandama kwa sababu hatuishi vizuri na ndugu, jamaa na rafiki zetu. Hivi yule rafiki yako Mbweku Jr aliyenihadithia kuwa alifia nchini Afrika ya Kusini kwa matumizi ya mihadarati, ndugu zake unawasaidia kweli? Tufanye walau tukawaone mie kwa upande wangu yule alikuwa kwako ni zaidi ndugu na kwangu yule ni zaidi ya kaka, Mungu amlaze mahali pema peponi......Ameeen! " Aliongea Deborah kwa hisia kali mpaka machozi yanamtiririka huku bila kujua anapiga bomu Ikulu, amelenga pale pale anapopata Mbweku Jr kuwa ukweli ujulikane kuwa mumewe ni mmoja wa Mafioso.

"Kumbe, mimi Mbweku Jr nimeshakufa tayari na kuzikwa...! Wewe mbwa koko hata aibu huna..! " alijikuta Mbweku Jr anaingilia mazungumzo hayo, huku akiwa tayari ameivua tena kofia yake hali ambayo ilimfanya Deborah sasa amtambue dhahiri shahiri. Kipindi hicho Boti ilikuwa inaendeshwa na Sarahange anapata uzoefu wa kuwa Nahodha kivitendo, hivyo Mbweku Jr alikuwa yupo jirani na Bosi Timammy, mkewe Deborah na khadimu wao.


"Khaaah....Kaka Mbweku Jr kumbe upo hai kaka? Kwanini lakini rafiki yako, mume wangu Timammy kanidanganya wewe ni marehemu, mmegombana nini haswa mpaka kufikia hatua hiyo ya kuleteana uchuro wa kifo jamani.....!" alilalama Deborah kwa uchungu mkubwa na kuangusha kilio kizito mpaka anajigaragaza chini. Fujaa akaonekana Bosi Timammy amekurupuka kwenye boti na kujitosa ndani ya bahari. Bosi Timammy alishindwa kuhimili vishindo vya aibu atakayoipata mbele ya mkewe pindi ukweli halisi ukianikwa hivyo, alifanya maamuzi ya kujiua majini.
[emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586]
 
Mmeona mke asomeshwi ukimsimesha imekula kwako Kama mwamba hapo
 
Kuna RIWAYA MPYA YA HUBA LA MISS TANZANIA,IFUATILIENI NAYO ITAFIKA MWISHO TU,BI BURUDANI BANDIKA BANDUA
[emoji1787][emoji1787][emoji1787][emoji125][emoji125]
 
Back
Top Bottom