SEHEMU-16
[emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3585][emoji3585]
Mzee Minja usiku wa kuamkia Jumapili, usiku ambao mtoto wake marehemu Josephu Minja amechakazwa risasi na majambazi alilala kwa shida. Alikuwa mahamumu kichwa kinamgonga barabara na maumivu ya mgongo. Usingizi wote ulimpaa usiku kucha akiugulia. Mkewe nae chango la uzazi likawa linamkata utasema mwanamke mjamzito anataka kujifungua. Uchungu wa mwana aujuaye mzazi, hiyo ilikuwa ni taarifa wanapewa ya msiba mzito wa nguzo yao katika maisha ya uzeeni Bosi Minja. Mtoto ambaye ndio pekee amefanikiwa kufika elimu ya Chuo kikuu,wamehangaika nae kwa kukopa, kulima buni ili mradi aweze kutimiza ndoto zake za kielimu. Sasa ndio ulikuwa wakati wao wa kula pensheni ya malezi toka kwa kijana wao, hata hawajaanza kufaidi vizuri, Malaika mtoa roho anawakatisha starehe yao.
Mpaka kufika majira ya alfajiri ndio akapatwa na usingizi mzito. Mama yake Bosi Minja ikabidi ajikaze kisabuni hivyo hivyo kama ujuavyo nani kama mama!. Mama ukimuona ameugua akalala kitandani basi tambua huo ugonjwa ni wa hatari sana lakini kwa kawaida mama anaweza kuugua na wala watu wasifahamu kama ni mahamumu. Atapika chakula, atafua nguo za watoto, atafanya usafi wa nyumba, ataosha vyombo na majukumu yake mbalimbali ya kila siku bila kuchoka, bila kuwa na likizo miaka nenda miaka rudi. Mama yake marehemu Bosi Minja ilipofika asubuhi akajikaza kisabuni kama vile ni mzima wa afya hana chochote kinachomsumbua mwilini akaandaa mtori wake kwa ajili ya mgonjwa, mkwewe mtarajiwa Recho aliyelazwa 'Huruma Dispensari', moja ya kituo cha afya kilichokuwa kinatoa huduma bora Jijini Arusha kikiwa kinamilikiwa na mwekezaji Mzungu mwenye uraia wa Kenya.
Asilimia kubwa ya Madaktari wake walikuwa ni Raia wa Kenya. Mpaka kufikia saa 12:15 asubuhi alikuwa tayari ameshawasili kwenye viunga vya dispensari hiyo. Moja kwa moja akapitiliza mapokezi na kwenda kumuulizia mgonjwa wake kalazwa wodi gani. Nesi wa zamu alikuwa ni Bibi mtu mzima kiumri aliyeonekana yupo makini na kazi yake. Alikuwa anawasikiliza kwa makini wateja wanaokuja dawatini kwake na lugha nzuri ya kujali wateja. Akaelekezwa aelekee wodi ya wazazi, ikabidi apatwe na mshtuko usiomithilika. Ikabidi aulizie tena kwa mara ya pili, maana mgonjwa Recho kweli ni mjamzito ila siku za kujifungua zilikuwa bado kabisa sasa alikuwa anashangaa iweje apelekwe wodi ya wazazi. Alipopata ufafanuzi kiufasaha toka kwa yule Nesi ndipo akaelewa kuwa Recho amejifungua majira ya jogoo la pili.
Akaanza kutembea kuelekea kwenye wodi ya wazazi kwa haraka huku akitamani apaishwe kwa furaha sheshe aliyokuwa nayo ya kupata mjukuu. Alipofika akabisha hodi chumba alichoelekezwa kisha akafungua mlango na kuingia. "Waooooh.....hongera mwanangu na pole kwa maumivu" aliongea kwa furaha mama yake Bosi Minja huku akilitua chini kapu lenye chupa iliyojazwa mtori. "Ahsante nashukuru mama.." alijibu Recho kwa ufupi huku macho yake yakiangalia chini kwa aibu akikwepesha kabisa kuangaliana nae uso kwa uso.
Dhamira moyoni ilikuwa inamsuta Recho hasa kwa kuwa alikuwa anajua kabisa kwa zaidi ya asilimia 100 kuwa mtoto aliyemzaa masaa machache yaliyopita sio wa Bosi Minja. "Umetuletea mtoto gani, ni mume wangu au mke mwenza wangu.." aliuliza kwa shauku Bibi yule akitaka kufahamu jinsia ya mjukuu wake aliyezaliwa. "Ni mumeo, mtoto wa kiume...." alijibu Recho huku akijilazimisha kutia utani kwa shida sana. "Muda wa kuona wagonjwa umekwisha, tupisheni sasa tuwahudumie ahsanteni sana kwa kuja kuwafariji wagonjwa wenu" lilikuwa ni tangazo la nesi anayepita kila wodi na kengele yake akiipiga kuwaondoa ndugu wa wagonjwa. Mama yake Bosi Minja ikabidi akusanye kila kilicho chake akitoe zake.
Recho alikuwa amejifungua mtoto njiti wa miezi 7, hivyo alitakiwa akae hapo kwenye kituo cha afya kwa siku kadhaa huku mtoto akiwa anatunzwa kwenye vifaa maalumu vya kuhifadhia watoto njiti. Hima hima akitembea mashimashi na kapu lake akielekea kwenye kituo cha daladala kurejea nyumbani kwake kumpa taarifa mumewe juu ujio wa mjukuu wa mtoto wao Joseph Minja.
[emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586]
Mzee Minja aliamka toka usingizini majira ya mafungulia ng'ombe akiwa kidogo amepata ahueni. Baada ya kupiga mswaki na kuoga akaamua achome utumbo wake kwa kahawa chungu ya moto sana, iliyochanganywa na samli bila sukari "Bullet Coffee" bila mchapalo wowote wa kitafunwa. Hapo akajisikia nafuu sana.
Akatoa kiti chake nje ya kibaraza huku pembeni ana redio yake kubwa maarufu kwa jina la 'Mkulima' anasikiliza 'Redio Tanzania Dar es Salaam' (RTD) kipindi cha muziki zilipendwa asubuhi hiyo. "Hureeeh....Hureeeeeeh.....Ripu... Ripu...mkwe wetu Recho katuletea mnangu" alilipuka kwa furaha mama yake marehemu Bosi Minja baada ya kumuona mumewe kibarazani kabla hata ya salamu yoyote. "Ooooh....usiniambie mama Jose huyo kichanga kampata lini? Mbona maajabu..!" Mzee Minja alilaki mazungumzo ya mkewe kwa shauku kubwa. "Huo ndio uhalisia, kumbe changolililokuwa linaniuma usiku kucha lilikuwa ni la kumpokea mjukuu wangu jamani, amejifungua ila mtoto ni njiti, hivyo mama na mtoto wataendelea kubakia hospitalini" alitoa maelezo ya kina Bibi Deborah yaliyomshibisha mumewe.
"Daaah.....mnangu wetu atakosa mambo mengi ya taratibu za kimila nilitamani aje leo leo" aliongea Babu Debora kwa sauti ya manung'uniko, hasa kutokana na ushabiki wake wa mambo ya kimila.
"Usijali kikubwa ni kuwaombea uzima wao, mie ngoja niingie jikoni nipike mlo wa mchana, itabidi nimtume kijana akapeleke taarifa kwa mama yake mzazi Recho, maana hata taarifa hizi ana mipango ya kupeleka chakula mchana hivyo ni bora azijue mapema!" aliongea Bibi Debora huku akijiandaa kufungua kitasa cha mlango wa kuingilia ndani. Mila zao Wachaga, mtoto akishazaliwa mkunga aliyemzalisha mama huagiza majani yaitwayo kwa kichaga masunzuku ambayo huyachovya ndani ya maji ya uvuguvugu na kisha kumfuta nayo mtoto mwili mzima na kumpaka siagi mwili mzima. Baada ya hapo mtoto hupewa dawa fulani ili akitumia maziwa ya mama yasimdhuru kisha hupewa maji ya chemuchemu au ndizi iitwayo mrarao iliyovumbikwa ndani ya majivu ya moto kabla ya kumenywa ili ipate kuiva vizuri na kuwa laini.
Ndizi hii ikishaiva hutafunwa na kutemewa mtoto kinywani aimeze. Chakula hiki cha kwanza anacholishwa mtoto mchanga 'mnangu' huitwa kelya ketocha mana ulaka maana yake, chakula cha kutoboa koo la mtoto. Pia Ilikuwa mwiko kumuona mtoto kabla ya kutimiza miezi mitatu kutokana na imani kadhaa zilizokuwepo. Alama ya kuonyesha nyumba au mahali palipofanywa marufuku ni kusimika mti uitwao kwa kichagga sale ulio na majani yaliyopigwa fundo na kusimikwa karibu na mlango wa nyumba ya mzazi.
Mila hizo zote Babu Debora alitamani zitumike kwa huyo mjukuu wake mpya, lakini mambo yalikuwa nje ya uwezo wake. Akaendelea kubakia pale kibarazani anasubiria mkewe apike 'machalari' huko jikoni, moja ya chakula cha asili alichokuwa anakipenda sana Babu Debora. Muda ukazidi kuyoyoma mpaka ikafika saa 7:00 za mchana, ikasomwa taarifa ya habari ya adhuhuri mara baada ya taarifa hiyo ya habari iliyochukua takribani dakika 5 kwisha yakaanza matangazo ya vifo. Ikasikika sauti "Booooooooommm....!" kutoka kwenye redio ikiashiria kuanza kwa matangazo ya vifo.
Tangazo la kwanza tu kuanza kutangazwa na mtangazaji lilikuwa ni la msiba wa Bosi Minja. "Shirika la Peace Corps-Tanzania linasikitika kutangaza kifo cha Mratibu wake kanda ya Kaskazini, Bwana Joseph Minja kilichotokea usiku wa kuamkia leo nyumbani kwake maeneo ya Philips kutokana na kupigwa risasi na majambazi. Habari ziwafikie Baba na Mama yake waliopo maeneno ya Boma Ng'ombe, Moshi, ndugu na jamaa zake waliopo Marangu, pia habari ziwafikie walimu wote wa Morogoro Sekondari mkoani Morogoro.Vikao vya maandalizi ya mazishi ya marehemu vinaendelea nyumbani kwake maeneo ya Philips. Mungu ailaze roho yake mahali pema peponi-Amiiin".
"Ooooh.....Oooh.....Yelewiiiiiiiii........Aaakh Aaakh.... Aaakh...!" alikuwa Babu Debora amepagawa anapiga kelele kama kama mtu aliyepandisha ruhani anahitaji kisomo cha ruqiya apate kutulia. Redio yake aliyokuwa muda wote ameikamatia mkononi aliiona kama kaa la moto, akaitupia kule na kupasuka vipandevipande. Mayowe yale yaliwavuta majirani, na mkewe nae ilibidi akurupuke toka jikoni ayaache machalari yake yanachemka na kwenda kuangalia mumewe kimemsibu nini.
Majirani wengi walikuwa tayari wamesharejea makanisani kwao, wanataka kupumzika na familia zao lakini ilibidi lazima waje kusikiliza kilio hicho hasa kama ujuavyo ukiona mtu mzima analia ujue kuna jambo sio bure. Ikabidi kwa shida sana awaeleze juu ya kifo cha Bosi Minja kilichotangazwa kwenye redio muda mfupi uliopita. Sasa eneo hilo likageuka kuwa msibani, vilio mtindo mmoja kila kona. Bosi Minja alikuwa ameshaondoka duniani amerejea jongomeo kwa Mola wake kwenda kuhesabiwa matendo yake ya duniani. Riziki zake za duniani tayari zilishakatika mali zake zote alizokusanya katika maisha yake ya dunia kwa njia ya halali au kwa dhuluma zilikuwa haziwezi kumfaa chochote huko jongomeo. Mpaka kufikia majira ya Alasiri maiti ya Bosi Minja ilifikishwa nyumbani ikiwa imesindikizwa na msururu wa magari ya kifahari ya waombolezaji kutokea Jijini Arusha.
Wazazi wa marehemu baada ya kujadiliana na kamati ya mazishi wakatoa tamko rasmi la familia kuwa mazishi yatafanyika siku ya Jumatano huko Marangu.
[emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586]