Riwaya: Matanga ya rohoni

Riwaya: Matanga ya rohoni

SEHEMU-46


Licha ya wafungwa wengi na vijiwe mitaani kulisifia gereza la Ukonga kwa sifa kemkem kuwa ni zuri lakini kwa mtazamo wake Mbweku Jr jela ilikuwa ni jela tu hata siku moja haiwezi kufanana na Hoteli ya nyota tano. Tamaa yake ilikuwa ni kufanya vyovyote awezavyo aweze kuwa huru uraiani. Sumu haionjwi kwa ulimi, ukitaka kujua mateso na bughudha za jela ombea siku moja uende huko ndio utajua tamu na chungu yake. Kulikuwa na watuhumiwa huko gerezani tokea walipokamatwa hadi kufikia miaka 3 kesi zao hazijawahi kusikilizwa Mahakamani, na wengine walikuwa wamebambikiziwa kesi na polisi wanahangaika nazo nenda rudi.

Mbweku Jr alipoletwa Ukonga, siku za mwanzoni alikuwa anachungwa kama mboni ya jicho ili mradi asilete rabsha na ghasia zozote. Ripoti zilizofikishwa pale Ukonga juu ya Mbweku Jr zilijaa chumvi, zikivumisha kuwa Mbweku Jr ni mahabusu hatari sana, hivyo jina lake lilivuma mithili ya papa baharini. Hii yote ilikuwa ni mbinu chafu za rafiki yake Timammy ili kumdhibiti Mbweku Jr asije kufanya mbinu za kutoroka. Masazo ya ndovu majani makavu, pesa za watu wakubwa kama Timammy zilikuwa zinaleta uharibifu katika jamii kwa kuwaonea watu wanyonge kama akina Mbweku Jr. Alikuwa anatengwa haruhusiwi katu kuchanganyika na mahabusu wenzake.

Akaanza kupelekwa kwenye chakula na pingu, chooni na pingu huku askari magereza mwenye mtutu mgongoni mwake. Pia kulala kwake nako shida tupu, analala na pingu mikononi, anafunguliwa pingu za miguuni peke yake. Mbweku Jr alishaanza kukata tamaa ya kutoroka nje ya gereza hilo lenye ulinzi madhubuti. Baada ya kupita miezi kadhaa ya uangalizi wakaanza kumpa uhuru wake kama watuhumiwa wengine. Alishangazwa sana na mabadiliko hayo ya ghafla asiyoyatarajia.

Baada ya kupita siku kadhaa akapata ugeni uliomtembelea gerezani. "Mimi ni Mwanasheria wa Bosi Timammy amenituma nije kumuombea msamaha kwa kukutelekeza gerezani. Ametoa ahadi kuanzia sasa ya kukuhudumia kwa hali na mali, pia ameniagiza niandae mkataba wa makabidhiano ya mali zako, na ameahidi kufanya juu chini utoke gerezani kwa haraka" yalikuwa ni maelezo ya mgeni yule kwa Mbweku Jr. "Mjumbe hauliwi, mwambie vitendo vyake ndio vitanijulisha kuwa kweli anataka suluhu na mimi" alijibu Mbweku Jr kwa ufupi huku akionyesha hana haja ya mazungumzo zaidi huku akinyanyuka na kumuacha mgeni amebaki amepigwa na butwaa kaachwa mdomo wazi, akimshangaa jinsi Mbweku Jr alivyokuwa masikini jeuri. Maana ilivyo ada ni kuwa mtu aliye kwenye shida, mazonge yamemsonga hana miiko wala makuu haja yake ni nafuu tu.

Maneno ya mwendawazimu hayana maana lakini ni maneno, majibu ya Mbweku Jr yalipomfikia Bwana Timammy kweli akayafanyia kazi kwa vitendo. Tokea siku ile mchana wake tu mabadiliko yakaanza mara moja. Mbweku Jr akaanza kuletewa chakula kilichopikwa nyumbani kikiwa kimewekwa kwenye vyombo maalumu vya thamani utasema yupo Hoteli ya nyota 5. Mchana akiletewa wali uliokolezwa nazi na mchuzi wa samaki uliotiwa nazi shatashata basi jioni ataletewa chai ya maziwa na chapati za maziwa ili mradi, Bosi Timammy alianza kuonyesha msamaha kwa vitendo.

Huko Mahakamani nako hali ya hewa ikabadilika kabisa, upepo ukaanza kuvuma upande wake, Jaji alikuwa amecharuka akitaka ushahidi wa kesi hiyo kukamilika ndani ya mwezi mmoja vinginevyo atamuachia huru mtuhumiwa Mbweku Jr. Sasa Mbweku Jr akaanza kuwa na imani na Timammy kuwa kweli ameamua kujirudi kwa vitendo. Akaamini moyoni mwake kuwa kweli shetani alizeeka hugeuka kuwa malaika. Akaanza kuhesabu siku tu za yeye kurejea uraiani akadake mali zake aanze maisha mapya ya raha mustarehe yasiyo na rabsharabsha.

Alipanga akipata mgao wake ni kwenda kujichimbia nje ya mji na kuanza maisha yake upya. Asichokijua Mbweku Jr ni kuwa Na iwapo akifanikiwa kumuangamiza basi dunia kwake itakuwa ndio kama pepo yake iliyoletwa ardhini kabla hajafika.

Timammy alibadilisha mbinu za mashambulizi dhidi yake, aliamua kumuweka karibu adui yake ili iwe rahisi kwake kumuangamiza. Na kweli Mbweku Jr akanusurika na kifo chupuchupu apelekwe jongomeo kwa usafiri wa jeneza usiotumia mafuta kama gari. Lilikuwa ni shambulio la mwisho toka kwa Timammy dhidi ya Mbweku Jr. Jaribio lake la mauaji lilikuwa kupitia chakula anacholetewa na Timammy. Mauti mamoja maziko mbalimbali, sio lazima umshambulie adui yako kwa njia chafu, unaweza kumshambulia kistaarabu na ukapata natija ile ile uliyoikusudia, huo ndio mpango wa Timammy aliousuka dhidi ya Mbweku Jr.

Timammy aliona kabisa, Mungu kampa neema zote za dunia lakini kuna kidudu mtu mmoja ndio anamnyima raha kutumbua kwa furaha neema hizo nae ni Mbweku Jr. Lakini kumbe Mbweku Jr hakuwa juhali, zumbukuku ulimwengu uko huku, katika vitu ambavyo Mbweku Jr alikuwa makini nacho basi ni chakula. Alikuwa anajaribu kuwa makini kila anapoletewa lazima ahakikishe mletaji yule amekionja ndio anakipokea.

Chambilecho maziwa ya ng'ombe wa kuazima hunywewa mnywaji amesimama, katu hakumpa imani ya asilimia 100% Timammy juu ya wema anaomfanyia hivyo kila kitu alikuwa anakiendea kwa tahadhari kubwa. Lakini siku ambayo chakula chake kiliwekwa sumu kilipokelewa na Askari magereza peke yake, tena ambaye alijiweka karibu nae sana kwa kila kitu, akaniambia, wakaaminiana kuwa kuna kaurafiki baina yao. "Leo chakula kimeletwa mapema sana, nikaona nisikusumbue nimeamua nikupokelee akakionja yule mletaji kipo fiti usiwe na wasiwasi" alisema yule Askari wakati anamkabidhi vyombo vyenye chakula Mbweku Jr huku anakwepesha kugonganisha macho baina yao. Mbweku Jr hakutia neno, lakini kajoto ka wasiwasi kikamvaa mwilini mwake, ila akapuuzia kutokana na yule askari aliyemkabidhi ni mtu wake sana hakuwa na chembe ya mashaka nae.

Mbweku Jr alishaumia tayari, alisahau kuwa mazoea papai kwa kijiko, yanakupunguzia uwezo wa kufikiri. Aliyemfaa Mbweku Jr na kumuepusha na kifo cha sumu ni askari mwenzake na yule askari rafiki yake ambaye alikuwa nae lindo moja. Alimkonyeza kwa kumpa ishara juu ya chakula kile. Hakushuhudia mwenzake anavyokionja hivyo akahisi kuna janja janja inataka kufanyika kutokana na uwongo anaosema mwenzake. Pia alimsoma mwenzake namna alivyojawa na hofu na wasiwasi mwingi kipindi chote anapokabidhi chakula kile kwa Mbweku Jr. Chakula kile Mbweku Jr akaenda moja kwa kukitupa chote kwenye pipa la taka kikawe kalamu ya wadudu na ndio ukawa mwisho wa chakula kuletewa toka uraiani kwa Timammy.

Walishanyoosha mikono kuwa Mbweku Jr ameshindikana, kama ni mchawi basi yeye ndio gwiji wao. Mbweku Jr baada ya kujifanya zuzu kwa muda mrefu na kuwaaminisha kuwa hana madhara tena, kiasi kwamba wakazidi kupunguza umakini dhidi yake ukafika wakati wa kuwaachia manyoya tu. Mbegu za leo haziwi miti keshoye, tayari alishatumia muda mrefu kuwasoma walinzi wa gereza na sehemu gani kwake rahisi kuitumia kutoroka Kilaini. Alijua mpango wake wa kutoroka ni wa hatari sana, kufa au kupona na daima mchele haukosi ndume hivyo alijitayarisha kwa chochote kile kitakachompata.
Mipango yake ilikuwa ni kutoroka kupitia Lori la kubebea takataka gerezani.

Utakumbuka siku Mbweku Jr anapewa taarifa za kuletwa Ukonga alikuwa na furaha sheshe kutokana na kufahamiana na mtu anayehusika na Lori la takataka. Lori hilo Mjomba wake alikuwa ndio utingo wake. Huyu ndio Mjomba aliyempa taarifa Mbweku Jr za baba yake kuhamishiwa gereza la Dar es Salaam kutokea Jijini Arusha walipogongana mtaani maeneo ya Manzese baada ya kupotea kitambo kirefu.

"Uncle...Uncle...mimi kijana wako Mbweku, tuongee kidogo nina shida...!" alinong'ona Mbweku Jr huku akimkaribia Mjomba wake aliyekuwa ametingwa na kazi ya kupakiza takataka ndani ya Lori hilo. Mbweku Jr alimfuata Mjomba wake baada ya kujihakikishia kuwa ndio yeye kwa kumchunguza kiumakini kwa muda mrefu tokea ahamishiwe gereza lile. Kuna baadhi ya siku alikuwa hata anamsaidia kupakiza taka kwenye gari, ila Mjomba mtu hamtambui Mbweku Jr kutokana na kupoteana kwa muda mrefu sana.

"Mjomba.... Mjomba.... siamini Mjomba kama ndio wewe Mjomba..!, umefikaje humu"? alijikuta anaropoka yule Mjomba wake Mbweku Jr huku akikiachia kifurushi cha takataka kikidondoka chini alichokuwa amekishikilia mkononi. Damu ni nzito kuliko maji, Mjomba mtu alipomuangalia kwa umakini sana, akagundua huyu kweli ni mtoto wa dada yake, ambaye taarifa walizonazo ni kuwa yupo nchini Afrika ya Kusini,hivyo alishangazwa na kumuona yupo mule gerezani. Ikabidi Mbweku Jr aanze kumfungulia kitabu cha maelezo Mjomba wake, akianzia tokea alipotorokea nchini Afrika ya Kusini mpaka kujikuta tena yupo gerezani.

Mjomba nae akampa taarifa kuwa baba yake mzazi Mbweku Sr ameachiwa huru kwa msamaha wa Rais, na sasa yupo Kijiji cha Kitomanga, Mkoani Lindi anajishughulisha na kilimo. Kisha mwishoni akamdokezea nia na madhumuni yake ya kutaka kutoroka ili kukwepa kifungo cha maisha au kunyongwa, na tumaini pekee lililobakia kwake la yeye kukwepa mkono wa dola ni yeye Mjomba wake kumsaidia kutoroka gerezani. Mjomba mtu mwanzoni alikuwa anasitasita kukubaliana na mipango hatari ya mpwa wake. Alikuwa anatafakari kwa kupima kwenye mizania ya usawa madhara na madhila yatakayomkabili iwapo atagundulika uhusika wake wa kumtorosha Mbweku Jr. Ikabidi Mbweku Jr afanye kazi ya ziada kumrai, kumlainisha na kumtongoza Mjomba wake mpaka wakaenda sawa. Wakakubaliana wiki ijayo ndio iwe wiki ya kutoroka.


Siku ya miadi ilipofika Lori hilo la kubeba takataka badala ya kuingia gerezani saa 9 alasiri kama ilivyo kawaida yake, likaingia saa 11 jioni. Kwa bahati nzuri siku hiyo Wafungwa karibia wote wazima kwa wagonjwa walikuwa wamejikongoja, wamekusanyika kwenye jengo moja wanaangalia mpira wa mechi ya miguu. Ilikuwa ni mpambano baina ya Yanga na Simba, mpambano ambao kwa kawaida huwa unateka hisia za washabiki na wapenzi wa soka, wake kwa waume katika nchi za Afrika Mashariki na Kati, habari hawana.

Mbweku Jr alikuwa amebakia Selo peke yake anapanga na kupangua mbinu mbalimbali za kuteleza toka gerezani. Lakini pia masikio yake yalikuwa yamemsimama dede kama dishi la televisheni linalosubiria kudaka mawimbi ya televisheni akiisikilizia Lori la takataka ujio wake. Muda wote Mbweku Jr alikuwa roho juu juu akilisubiria gari hilo lifike. Alipoona muda unayoyoma halitokei akaanza kukata tamaa, alishadhania Mjomba wake amebadilisha maamuzi yao waliyokubaliana. Sasa kabla hajaanza kuwaza kitu cha kufanya ili ajiokoe gerezani akasikia mlio wa Lori hilo la taka.

"Afandeee... Afandeee...!" aliitwa Askari Magereza pekee mwenye silaha na Mbweku Jr ili kumsikiliza shida yake, huku Askari wengine wote nao wakiwa wametekwa na laghwi ya mpira wa miguu, wamesahau kabisa jukumu lao la ulinzi walilokabidhiwa. Kilichopo fuatia hapo ni yule Askari kuja kuzindukia Muhimbili akiwa mahututi, hoi bin taabani. Alimfuata kizembe Mbweku Jr bila kuchukua tahadhari yoyote, hapo hapo akajikuta anapigwa ngwala moja matata sana na kulamba sakafu bila kupenda, kabla hajajua kinachoendelea akashtukiwa anapigwa kisogoni na kitako cha bunduk yakei na kujikuta analala fefefe usingizi wa kuzimia.

Mbweku Jr akamburuta askari yule mpaka ndani ya Selo hiyo iliyokuwa tupu bado.. Hima hima akachomoka zake kuelekea kwenye gari la taka. Baada ya hapo ilibakia historia tu kuwa mule gerezani kulikuwa na mtu anaitwa Mbweni Jr. Sakata la Mbweku Jr kutoroka lilizua kasheshe nzito gerezani.Mkuu wa gereza na baadhi ya Maaskari wake walijikuta wanapewa uhamisho wa kikazi bila kupenda kwa uzembe. Wafungwa na Mahabusu waliobakia gerezani walimlaani Mbweku Jr upeo wa juu wa kumlaani, kutokana na hali ngumu aliyowaachia.

Ile hali ya kudekezana na kuachiana ikatoweka kabisa. Mianya yote ya uzembe katika ulinzi ikatiwa Korokoroni, sasa ikawa kazi kazi tu hamna kuchekeana tena, Mbweku Jr alishawapa funzo kuwa ukimchekea nyani utayavuna mabua. Msako wa Mbweku Jr huko uraiani ukawa ni wa kimya kimya, ili kuhofia asije kugutuka kama anasakwa na pia kuhofia kuzua taharuki ndani ya nchi juu ya uzembe wa vyombo vya dola kwenye masuala ya ulinzi na usalama. Mbweku Jr tayari alishaenda kujichimbia kijiji kwao Kitomanga, huko Lindi kupata baraka za wazazi kabla hajarejea kudai haki zake zote kwa rafiki yake Timammy.

Msako wake ukawa kama moto wa kifuu, ilipopita miezi 3 tu wakaachana nae, maadamu alivyotoroka hakuua mtu, taratibu wakakubali matokeo kuwa Mbweku Jr amewazidi kete, maisha lazima yaendelee kama kawaida. Bosi Timammy nae kupitia vidinga popo vyake vya gerezani akapata taarifa juu ya utoro wa Mbweku Jr. Sasa nae akaanza kuishi kwa hofu na mashaka hana tena furaha ya maisha.

Siku za mwanzoni alikuwa anatumia muda mwingi wa mchana kujifungia ndani na kutoka usiku kama popo. Baadae alipoona mambo yake yatakwama ikabidi hana jinsi lazima atoke kama zamani kwa uangalizi maalumu. Kila alipokuwa anakwenda alikuwa anazungukwa na kikundi cha walinzi shupavu na makini wanaopenda kufa kuliko kuishi. Deborah bado alikuwa hajui chochote kinachoendelea kwa mumewe Timammy licha ya kuona mabadiliko yasiyo ya kawaida. Hakutaka kuhoji zaidi kutokana na hekaheka na misukosuko ya ujauzito wake.
[emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586]
HAYA BABA TIMAMMY USIYEMPENDA MBWEKU JR, KAJA URAIANI UTAKIONA CHA MTEMA KUNI LOFA WEWE...SIKUPENDI TIMAMMY SNITCH MKUBWA WEWE
[emoji24][emoji24][emoji24][emoji24][emoji24][emoji24][emoji24][emoji24][emoji125][emoji125][emoji125]
 
SEHEMU-47



️[emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586]
SURA YA ISHIRINI
Dr.Pesambili na mama Deborah walifikia katika Hoteli yenye hadhi ya nyota 4 inayoitwa 'Palace Hotel-Arusha' iliyopo katika barabara ya Makongoro. Ilikuwa ni Hoteli tulivu isiyo na fujo kama inavyokuwa nyumba ya wavuvi. Kutokana na uchovu wa safari walijikuta wanalala fefefe mpaka majira ya mafungulia ng'ombe, jua limeshachomoza vilivyo. Baada ya kujimwagia maji maliwatoni kila mmoja kivyake wakajikuta wanakutana kwenye Mkahawa kwa ajili ya staftahi ya asubuhi, hali ya kuwa miili yao imepata tahafifu dhidi ya uchovu.


Kilichofuatia baada ya kuonana asubuhi hiyo ni kupeana jambo sijambo kama ilivyo ada ya binadamu wote wenye akili timamu. " Shikamoo mama, umeamkaje mie nipo vizuri nashukuru...!" alisalimia Dr.Pesambili huku akiwa yupo mbele ya mama Deborah amekamatia sahani yake anachagua vyakula kwenye bufee iliyokuwa imesheheni anuwai mbalimbali za michapalo kuanzia mayai ya kuchemsha, ndizi mchemsho na za kukaanga, soseji, mikate, maharage, vipande vya kuku wa kukaanga. Ilikuwa ni bufee ambayo kama wewe ni mtu mlafi bora usisogelee kabisa yasije kukuta yale yaliyohadithiwa kwenye kitabu kuhusu Manenge na Mandawa.


"Marhaba mwanangu na mimi naendelea vyema namshukuru Bwana...tule haraka tuwahi huko Ofisini tusije kuwakosa wenyeji wetu...!" aliongea mama Deborah akiwa anajimiminia kwenye bakuli lake uji wa ulezi. Wakajongea kwenye meza yao wakaanza kukishambulia chakula chao. Kila mmoja alikuwa mkimya ametulizana kama maji mtungini, anakula huku anatafakari mustakabali wa matokeo ya ziara yao ya leo katika ofisi za 'Peace Corps-Tanzania'. Dr.Pesambili alikuwa anawaza jinsi atakavyomfahamu mama yake mzazi na kuonana nae kwa mara ya kwanza.


Tayari alishamsamehe kwa kitendo chake cha kumtelekeza kwenye kituo cha watoto yatima. Pia mawazoni mwake alijua itamchukua muda kusahau tukio hilo, hasa kutokana na kwamba katika maumbile ya mwanadamu, dhambi uliyowahi kuifanya huwa haisahauliki. Ukiwa mtu muovu kisha ukageuka na kuwa mtu swalihina, bado walimwengu watakumbukia maovu yako tu. Utawasikia wanasema "siku hizi amemrudia Mungu wake lakini zamani enzi zake alikuwa mwizi, mnyang'anyi, mlawiti na mengineyo mengi tu katika dhunubi zake mtu huyo alizowahi kufanya siku za nyuma". Mama Deborah nae nae alizama katka bahari ya luja kimawazo, akifikiria kama huyo mama yake Dr.Pesambili ndio mwanamke aliyempora mume wake halali wa ndoa takatifu ya kanisani na kisha kushiriki njama za kuondosha uhai wa mumewe kwa lengo la kujitajirisha kwa pesa za wizi na urithi na kwenda kula mbwende na hawara yake. Huyo mwanamke ndio aliyemsababishia awe mgonjwa mahututi kitandani kwa zaidi ya miaka 15 na kumpotezea kazi yake na familia yake kwa ujumla kwa kukomba mali zote za familia.

Kwa upande wa pili wa shilingi, Dr.Pesambili, mtoto wa huyo hasimu wake ndio kamrudishia tena matumaini ya uhai. Kamtoa kitandani ambako tayari alishakufa kimawazo na kimwili, akisubiria ahadi ya kifo cha kiroho ije kutekelezwa na Malaku mauti. Na bado kama haitoshi anamhudumia kama vile ni mama yake mzazi kwa kila kitu anachokihitaji. Alipofika hapo akajikuta machozi yanamtiririka na kulowanisha mashavu yake bila mwenyewe kupenda. "Mama nini tena kimekusibu mbona unalia tena kulikoni?" aliuliza Dr.Pesambili huku tayari akiwa ameshachomoa hanchifu yake kuanza kumfuta machozi yale kiupendo kabisa.

"Hamna shida, nimetafuna pilipili vibaya wakati nakunywa supu hii" alitunga uongo wa haraka kuzima maswali zaidi, huku nae akitoa kitambaa chake kupenga mafua. Dr.Pesambili kwa utaalamu wake wa saikolojia alielewa kinagaubaga kuwa anafichwa kitu na mama Deborah. Hakutaka kumghasi, alijua tu muda sio mrefu atang'amua kinachomsonga mama Deborah. Walipotoka hapo Mkahawani, roshani ya kwanza wakashuka mpaka nje ya Hoteli na kukodisha taksi ya kuwapelekea Ofisi za 'Peace Corps-Tanzania'.
[emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586]
Mama Deborah, Dr.Pesambili na dereva wao walikuwa ndani ya taksi ukimya umetawala, dereva anahangaika kuinyonga sukani ya gari lake na kukanyaga mafuta ipasavyo ili gari lielekee ueleleo wa sawa. Watu wema hawadumu Bwana, gari yangu ya kwanza niliinunua kupitia kazi za Bosi wa zamani wa Ofisi za 'Peace Corps-Tanzania', mimi ndio nilikuwa dereva wake kipenzi anapokuwa na safari binafsi nje ya saa za kazi" alisema yule dereva wao mtu mzima aliyeonekana ni mwingi wa habari, akivunja ukimya uliokuwa umetawala huku wakiwa wanakaribia Ofisi hizo wanakiona kibao chake kwa mbali. "Alikuwa anaitwa nani huyo Bosi....?" alidakia mazungumzo mama Deborah huku akiwa na wahaka wa kutaka kumfahamu, kwa jinsi umri wa dereva huyo ulivyo moja kwa moja mawazo yake yakamuelekeza huenda anayeongelewa hapo ni mumewe.

"Huyo Bosi alikuwa anaitwa Joseph Minja, Mungu amlaze mahali pema peponi, alikuwa na roho nzuri sana, ana nakidi ya pesa, watu wamejenga majumba hapa Arusha kwa ajili yake. Alikuwa akiingia Baa basi kila mtu anafurahia, ila Bwana akaenda kumvaa msichana mdogo, gubegube la Kimachame, chotara wa kizungu anaitwa 'Recho Miondoko', Katibu Muhtasi wake akamkamua pesa vilivyo na nasikia ndio alipanga njama za kifo Bosi Minja kupitia majambazi aliowatuma. Baada ya hapo nasikia yule msichana alikimbilia nchini Kenya huko kula maisha" alizidi kuropoka yule dereva bila kujua anaumiza hisia za abiria wake. Maelezo hayo ya dereva yalitosha kuuchanachana vipande moyo wa Dr.Pesambili na kupata picha halisi ya tabia za mama yake. Jina la mama yake alitajiwa anaitwa Recho ila ubini wa babu yake mzaa mama ndio alikuwa haujui, sasa haya maelezo yalikuwa yanazidi kumfikirisha, yakimpa mawazo tata.

Maelezo hayo ya dereva pia hayakumuacha salama mama Deborah, kwani dereva alikuwa anaanika hadharani maisha ya ulimbukeni ya mumewe Bosi Minja. Akaamini msemo wa masikini akipata, matako hulia mbwata hasa akikumbukia shida walizopitia wakati mumewe ni Mwalimu wa Morogoro Sekondari, anapokea mshahara mkia wa mbuzi kumbe maisha yalivyomnyookea akawa mtu wa kutapanya fedha zake kwa israfu kwenye Mabaa kwa kuzipiga shoka pesa zake. Kila mmoja katika wao, machozi yalikuwa yanamlengalenga ila anajitahidi kuyazuia kuepusha maswali toka kwa mwenzake.

Dr.Pesambili akamalizana nae dereva yule, akatimka zake na gari lake akiwaacha wateja wake wanaingia ofisini kupata huduma waliyoikusudia. Wakajitambulisha pale mapokezi kisha Dr.Pesambili akaelezea nia na madhumuni yake ya kuonana na Bosi Mkuu wa Ofisi. Wakaelekezwa sehemu ya kupumzikia wageni huku wakikaribishwa soda, chai na kahawa kavu kwa mwenye kuhitaji. Waliwekwa kwenye orodha ya mzunguko wa watu wanaosubiria kuonana na Mkurugenzi wa 'Peace Corps-Tanzania'. Ilipofika zamu yake Dr.Pesambili kuingia, wakaamua waingie wote wawili. Walipoingia, wakajitambulisha kisha Dr.Pesambili akaanza kueleza shida yake. Muda wote wakati Dr.Pesambili anajieleza, mama Deborah uso ulikuwa haubanduki kwenye moja ya ukuta uliokuwa na picha mbalimbali za Wakurugenzi waliopita katika Ofisi hiyo ya 'Peace Corps-Tanzania'.

Jicho lake likatuama kwenye picha ya marehemu mume wake Bosi Minja. Akiwa amevalia suti nyeusi na tai, akatabasamu. Akajikuta machozi yanamporomoka bila kupenda akikumbukia zama bora enzi za uhai wa mumewe. "Hapa kwenye huo mwaka unaotaja, mtumishi tunayemfahamu alikuwa anaitwa 'Rachel Francesco Gabriele'....na picha yake hii hapa...!" ilikuwa ni sauti ya Mkurugenzi Mkuu wa Peace Corps-Tanzania akimkabidhi picha ya Recho mkononi mwa Dr.Pesambili. "Whaaaaaat.......anaitwa nani?" aliuliza kwa sauti ya kugutuka Dr.Pesambili na kumfanya mama Deborah nae akae mkao wa kula kufuatilia mazungumzo baina ya Mkurugenzi na Dr.Pesambili. "Nimesema anaitwa 'Rachel Francesco Gabrielle', ila mara ya mwisho inaonyesha alipata urithi wa nyumba ya Bosi wake aliyezaa nae. Maeneo ya Moshi Mjini, maeneo ya Boma Ng'ombe, nyumba namba 32 Bloku B. Alipewa urithi yeye na mtoto wake mchanga anaitwa Pesambili Joseph Minja....!" maelezo hayo ya Mkurugenzi ilikuwa kama vile anapigilia msumari wa moto kwenye utosi wa mama Deborah baada ya kusikia kusikia huyu Dr.Pesambili ndio mtoto anayesadikiwa kuwa wa mumewe.

"Nttiiiiiiiiiiiiiiih......!" kilikuwa ni kishindo kizito cha kuanguka kwa mama Deborah kutoka juu ya kiti mpaka chini ya sakafu. Kisha akatulizana tuli bila kutikisika. Hamkani mambo yakawa si shwari tena Ofisini mule, hekaheka za kumkimbiza mama Deborah hospitalini. Mazungumzo kati ya Dr.Pesambili na Mkurugenzi yule ndio yalivurugikia hapo. Dr.Pesambili kila alipojitahidi kusikiliza mapigo ya moyo wa mama Deborah yalikuwa yameshuka sana yapo chini kuliko kawaida. Akawa muda wote amejishika kiunoni anatikisa kichwa kuonyesha ameshaanza kukata tamaa kama kweli mama Deborah atapona au atakufa fi.
[emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586]
"Mzee samaki wako wazuri sana, ukiwapata wazuri kama hawa wa leo usisite kuniletea nyumbani....! " alisema Bosi Timammy kumuambia mvuvi mmoja wapo aliyekuwa amejengeka kisawasawa misuli yake, kichwani ana msitu wa nywele zilizounguzwa na chumvi ya maji bahari. Pia alikuwa amefuga ndevu, masharafa na masharubu yake ameyasokota kama Karl Peters yule mkoloni wa Kijerumani. Viganja vyake vya mkono vilikuwa vigumu sana kama mbao ya Mninga na mikono yake imeshupaa kutokana na mazoezi ya kupiga makasia wakati anaendesha mtumbwi baharini.

Ngozi ya mwili ilikuwa imekaushwa vilivyo na maji chumvi ya bahari, ikiwa ngozi hiyo haijui bei ya rosheni dukani inauzwaje. "Ahsante Bosi wangu, mie Bosi mzigo wangu ni wa motomoto siuzagi samaki wa mochwari aliyevundikwa kwenye mabarafu nyumbani ni pale pale nilipopelekwa na dereva wako wiki iliyopita eeeeh...? " aliuliza mvuvi yule kiunyenyekevu. "Ndio pale pale, ukifika wewe jitambulishe tu kuwa umeleta samaki, nitaacha taarifa zako kwa mlinzi na mke wangu pia...!" huo ndio ukawa mwanzo wa mahusiano mapya baina ya Bosi Timammy na Mbweku Jr. Mahusiano yao yalianzia katika ufukwe wa Kunduchi kwenye mnada wa samaki.

Wateja wengi walikuwa wanampenda Mbweku Jr kutokana na ujuzi wake wa samaki wa baharini. Hamna samaki ambaye alikuwa hamjui jina kuanzia Changu doa, Perege, Fumi, Pono, Tasi, Kibua, Samsuli, Kolekole, Taa na wengineo lukuki tu katika anuwai za samaki. Na raha ya biashara ya samaki Bwana uwajue majina yao na namna ya kuwapika vizuri ili ufurahie mlo wako. Mfano umwambie mteja, ukitaka kumfaidi samaki Taa, umchanganye na futari ya muhogo wa nazi au umwambie kuwa huyu Samsuli ndio nyama ya ng'ombe ya baharini unaweza hata kupikia pilau.

Mbweku Jr alisharudi Jijini Dar es Salaam tayari akijiandaa kulipa kisasi kwa Timammy. Kipindi chote alichojichimbia kijijini alikuwa anajaribu kila Jumapili kuhudhuria kanisani na kuungama dhambi zake, huku akifunga nadhiri ya kumsamehe hasimu yake Timammy lakini juhudi zake hizo zikawa ni sawa na kutwanga maji kwenye kinu. Kwa ufupi alishindwa kabisa kumsamehe Timammy hasa akivikumbuka vimbwanga alivyomfanyia. Ikabidi lazima aje Jijini na kuanza kupeleleza nyendo za Bosi Timammy, ili kisasi kitibu majeraha yake ya moyo yanayovuja damu. Ndipo alipong'amua kuwa Bosi Timammy ni mpenzi mkubwa wa samaki na soko lake kubwa ni Kunduchi mnadani. Katika mahusiano hayo mapya, Mbweku Jr alikuwa anamtambua nje ndani Timammy lakini Timammy maskini ya Mungu hamtambui kabisa Mbweku Jr kutokana na kuchujuka kulikotokana na msoto wa maisha magumu.

Hawa mahasimu wapya walikuwa hawajatiana machoni kwa zaidi ya miaka 8, zaidi ya kuonana juu juu mara moja pale Mahakamani. Laiti Timammy angekuwa anamuangalia kwa umakini Mbweku Jr lazima angemtambua tu, kama ujuavyo mtu wako ni wako tu hawezi kukupotea machoni. Ila tatizo katika ulimwengu huu wa rakadha tunaoishi, ukiwa hohe hahe, kipato cha kijungu meko hakuna mtu anakuangalia kwa umakini. Wakikuangalia wanajua saa na wakati wowote utawabomu kwa kuwalalamikia shida zako.

Fursa ya kufanikiwa kufika nyumbani kwa Bosi Timammy bila kipingamizi ndio aliyokuwa anaivizia Mbweku Jr kwa udi na uvumba. Alijipanga aiteketeze familia yote ya Timammy kwa kutumia sumu atakayoiweka kwenye samaki. Tokea atoroke jela ilikuwa imeshapita nusu mwaka, Timammy alishaanza kupunguza umakini kwenye ulinzi wake, akijidanganya kuwa tayari Mbweku Jr ameshakubali matokeo kwa kushusha silaha chini kuwa yeye Timammy ni Taifa Kubwa haiwezekaniki. Hakujua kumbe simba mpole ndio mla watu, na daima mla kunde husahau lakini mtupa maganda kamwe hasahau. Mbweku Jr uhasama wake na Timamny aliona hauwezi kamwe kupata suluhu hapa duniani labda suluhu hiyo ikafanyike mbele ya Mola Mwenyezi kwenye mahakama iliyojaa uadilifu.

Hapa duniani kwenye mahakama zetu zilizojaa Mahakimu ,Majaji na Wazee wa baraza wapenda mlungula aliona kabisa hatoweza kumkabili Timammy mtu aliyejitengenezea naizesheni ya kutosha kwenye mihimili yote mitatu ya dola. Mfano huko bungeni kulikuwa na wabunge ambao pesa zao za kampeni kila kipenga kikipulizwa lilikuwa ni jukumu kake Bosi Timammy. Kulikuwa na Majaji nao baadhi yao amewatia mfukoni anagharamikia mpaka mapumziko yao na familia zao nje ya nchi kila inapofika mwishoni mwa mwaka.

Ni ununda tu na ujasiri wenye chembechembe za wehu wa Milembe usio mfanowe wa Mbweku Jr uliokuwa unamsukuma kuendeleza mapambano na Timammy, kubwa la maadui. Safari za kwenda na kurudi nyumbani kwa Timammy kukamfanya mpango wake wa kuiteketeza familia ya Timammy autie kapuni kimoja, na kuachana nao kabisa. Alifanikiwa kumuona mke wa Timammy ni Deborah, mwanamke wa ndoto yake, tena akiwa ameshajazwa mimba kubwa tu, tumbo limemuelemea kama mpiga ngoma kubwa wa bendi ya jeshi. Usicheze na nguvu ya mapenzi wewe, Samsoni wa kwenye biblia licha ya ubabe na maguvu yake dhidi ya Wafilisti lakini mbele ya penzi la Delila akajikuta nguvu zake zote zinayeyuka mithili ya siagi iliyowekwa kwenye kikaango kilichokolea moto.


Akamuona Deborah kwenye mavazi ya stara ya kiislamu tena akiitwa kwa jina la kiislamu la Faizah na masuria wake kochokocho wa kumhudumia. Mbweku Jr akazidi kumchukia Timammy hasa baada ya kugundua amemfunga bao la maudhi kwa kutumia kisigino cha mguu wake. Aliona ni dharau kubwa sana kumchukulia mwanamke wake ambaye alishampa tahadhari tokea siku ya kwanza anamtambulisha Deborah kwa Timammy, tena akasomeshwa kwa pesa za Mbweku Jr halafu hatimaye anakuja kumpokonya tonge mdomoni na mimba kamtilia kabisa.

Wakati bado akili yake inatafakari kitu cha kumfanyia akaona tukio linalojirudia pale nyumbani kwa Bosi Timammy ambalo akaona ni fursa kwake ya kwanza kujiweka vizuri kiuchumi apumzike maisha ya tabu kwa muda.
[emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586]
Kwa zaidi ya mara tatu mtawalia, Mbweku Jr alipokuwa anapeleka samaki hasa muda wa magharibi, lazima atakuta gari la kifahari la Mkurugenzi au Meneja wa mojawapo ya benki kubwa nchini limeegeshwa kwenye yadi nje ya nyumba ya Bosi Timammy. Mbweku Jr akahisi kuna kitu kibaya kitakuwa kinafanyika ndani ya nyumba ya Timammy na hawa Vigogo wa benki.

Kilichozidi kumpa wasiwasi ni kitendo cha Vigogo hao kuja nyumbani hapo bila madereva wao, kuonyesha kuna siri fulani wanataka kuificha. Kuna siku moja Mbweku Jr baada ya kuuza samaki wake alipotoka nje ya nyumba ya Timammy akatafuta sehemu na kujibanza ili kuchunguza kinachoendelea. Ilipofika majira ya saa 4:00 usiku akaona kitu kama mabegi mawili makubwa yanapandishwa ndani ya gari kisha likaondoka. Hisia zake zikamtuma kuwa hizo ni pesa zinasafirishwa kinyemela bila ulinzi wowote. Hisia za Mbweku Jr zilikuwa sahihi, kuna mchezo mchafu ulikuwa unafanyika kati ya Bosi Timammy na baadhi ya Maofisa wa benki wasio waaminifu. Baadhi ya Matajiri walikuwa wanacheza michezo na Maofisa wa benki, kwamba wanapewa pesa zIlizowekwa na wateja kama mkopo lakini sio mkopo rasmi. Wanapewa nje ya taratibu za kibenki wafanyie biashara halafu wanazirudisha kinyemela. Pesa hizo kwenye vitabu vya benki zinaonekana zimo ndani ya benki lakini kiuhalisia pesa hizo zinazungushwa mitaani na akina Timammy.

Mbweku Jr akaandaa shambulio takatifu namba moja kwa Timammy la kumshtua kuwa siku zote dhuluma hailipi, na mali ya dhuluma haina baraka kama ilivyo mali ya mtu bahili inavyoishia kuliwa na wadudu. Siku aliyoipanga ya tukio lao alitia bastola yake ya bandia, toi alilolinunua sokoni Kariakoo. Kila aliyemuona nalo toi hilo akiwa amelitia kwenye kikapu kule pwani kwenye samaki katika watu wake wa karibu akajitetea anampelekea mtoto wake ya kuchezea.

Ilipofika jioni kama kawaida yake akapeleka samaki kule nyumbani kwa Timammy na kupokewa na mke wake Timammy Bi.Faizah, ambaye ndio Deborah mwenyewe.
"Babu muuza samaki, kuanzia kesho usilete utapumzika kwanza, nategemea kusafiri na mume wangu tunaelekea nchini Afrika ya kusini siku zangu za kujifungua zimekaribia. Chukua hii namba yangu ya simu utanipigia baada ya wiki mbili kuniuliza kama tumerudi....!" aliongea Deborah akiwa amejitanda ushungi wa Manga wenyewe hamna hata unywele uliojitokeza nje sio ule wa kizushi wa kiswahili, utasema Mwarabu vile kama ungemuona. " Ahsante mama, hamna shida Mungu ni mwema panapo majaaliwa..!" alijibu Mbweku Jr huku anabonyeza batani za simu yake chakavu iliyofutikafutika baadhi ya namba zake akijitahidi kuingiza namba za simu alizopewa na Deborah.

Maumivu yalikuwa makali haswa ya kuitwa babu na mwanamke wa ndoto zake. Wakati kiumri Timammy alimzidi Mbweku Jr kwa zaidi ya miaka 5, ila ndio mambo ya pesa tena. Ukiwa na pesa kamwe huzeeki na ukizeeka bado utaitwa Mzee kijana. Akalipwa pesa zake za samaki, wakaagana. Kumbe Mbweku Jr siku hiyo alipanga kuwaadabisha kwa pigo namba moja. Moja kwa moja akapitiliza saluni akanyoa nywele vizuri, ghafla akageuka kijana. Baada ya hapo akakodisha chumba gesti bubu moja uswahili akaoga, alibadilisha nguo na kujiandaa kwa tukio.
[emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586]
 
Back
Top Bottom